189.-(1) Majukumu ya jumla ya Tume ya Maadili ya Uongozi na Uwajibikaji yatakuwa ni kufuatilia na kuchunguza tabia na mwenendo wa viongozi na watumishi wa umma kwa madhumuni ya kusimamia na kuhakikisha kuwa Maadili ya Uongozi wa Umma na Miiko ya Uongozi wa Umma inazingatiwa, inalindwa na kuheshimiwa katika utumishi wa Serikali, Bunge, Mahakama, taasisi na idara nyingine zote za umma.
(2) Bila ya kuathiri masharti ya jumla ya Ibara ndogo ya (1),majukumu mahsusi ya Tume yatakuwa ni:
(a) kusimamia maadili na uwajibikaji katika utumishi wa umma;
(b) kufanya upekuzi na kufuatilia kumbukumbu za wanaoomba nafasi za uongozi wa umma;
(c) kuchunguza tabia na mwenendo wa mtumishi au kiongozi wa umma na kuchukua hatua pale inapostahili, ikiwa ni pamoja na kuwafikisha watumishi watakaobainika, kuvunja maadili na miiko ya kazi katika vyombo vya sheria;
(d) kusimamia sheria itakayotungwa na Bunge kuhusu maadili na uwajibikaji wa viongozi na watumishi wa umma;
(e) kushughulikia masuala ya ubadhirifu wa fedha na mali za umma;
(f) kufanya uchambuzi yakinifu kwa viongozi wa umma wanaopewa dhamana kabla ya kuingia madarakani;
(g) kutoa elimu ya maadili kwa umma kuhusu miiko na maadili ya viongozi wa umma;
(h) kufanya uchunguzi kwa maamuzi yake yenyewe, au baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa mtu yeyote, kutokana na kutenda au kutokutenda kwa Kiongozi au mtumishi yeyote wa umma, au wakala wa Serikali, ikiwa kitendo kilichotendwa au kutokutendwa ni kinyume cha maadili ya umma;
(i) kumuelekeza, baada ya kupata malalamiko au itapoona inafaa, kiongozi au mtumishi wa umma au wakala wa Serikali au chombo chochote cha umma kufanya tendo lolote au jambo lolote linalotakiwa na sheria, au kuacha, kuzuia au kusahihisha utendaji mbaya au usiosahihi wa majukumu yake;
(j) kutoa maelekezo kuhusu kuchukuliwa hatua kiongozi au mtumishi yeyote wa umma;
(k) kumuelekeza kiongozi au mtumishi wa umma, kwa mujibu wa sheria, kutoa nyaraka zinazohusiana na matumizi ya ofisi,matumizi ya fedha au mali za umma, au kutoa taarifa ya
matumizi mabaya kwa Tume, kwa hatua stahiki.
(l) kuomba msaada au taarifa muhimu kutoka kwa mamlaka yoyote ya Serikali au binafsi katika kutekeleza wajibu wake,na kukagua, kama ni lazima, kumbukumbu muhimu na nyaraka husika;
(m) kwa kuzingatia sheria, kutangaza kwa umma, mambo yote yanayohusiana na uchunguzi iliyoufanya, iwapo mazingira yanaruhusu;
(n) kuchunguza jambo au mazingira yoyote yanayokiuka au kusababisha ukiukaji wa maadili; na
(o) kuandaa kanuni za taratibu na matumizi ya mamlaka au utekelezaji wa kazi na majukumu ya Tume kama itakavyoelekezwa na sheria.