KINACHOFUKUTA Zanzibar, kwa minong'ono kuwa yanahitajika mabadiliko kabla ya uchaguzi mkuu, kinaweza kuwa baraka kwa taifa hili kuliko balaa.
Hii ni kwa sababu, kuingia katika uchaguzi, wakati Zanzibar kunawaka moto, ni kumwaga petroli kwenye moto badala ya kutafuta juhudi za kuuzima kwanza.
Maangamizi ya aina ya 2001, ambako watu wapatao 40 walikufa, yaweza kurudiwa au kuwa makubwa zaidi.
Ni hivi: Visiwani Unguja na Pemba kunahitajika mwanzo mpya katika mambo mbalimbali ya kiutawala, kisheria na hata kiutaratibu. Haya bado hayajafanyika.
Ikibidi, siyo lazima kuongeza muda wa Rais Amani Abeid Karume wa kutawala kwa miaka mitatu; bali kipindi maalum cha kuweka mambo sawa kabla ya kuingia uchaguzi.
Kwa mfano, utaingiaje uchaguzi ikiwa matatizo ya msingi yaliyopo katika daftari la kudumu la wapigakura hayajapatiwa ufumbuzi?
Utaingiaje uchaguzi ikiwa sheria mbalimbali zikiwamo zile zinazotoa mamlaka kwa sheha (mtendaji wa kata) kuamuru nani aandikishwe na yupi aachwe, hazijabadilishwa?
Utaingiaje uchaguzi wakati vyombo vya dola vinavyotuhumiwa kuwa kiini cha mgogoro wa muda mrefu visiwani Zanzibar, bado vinaendelea kujiegemeza kwa chama kilichopo ikulu?
Utaingiaje uchaguzi wakati hakuna uhakika wa matakwa ya raia kuheshimiwa? Utaigiaje uchaguzi wakati Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) ikiwa inabebeshwa tuhuma za kuendeshwa kama kampuni binafsi?
Jibu liko wazi; kwamba haiwezekani. Kila anayetakia mema taifa hili, hawezi kutamani kufanyika uchaguzi kabla ya kupatiwa ufumbuzi kwa matatizo yaliyopo.
Si lazima hayo yafanyike kwa kuongezea muda Karume. Muhimu ni kule kutendeka, tena kwa moyo mmoja. Kutekeleza hayo kwa njia ya kulipua, huku wahusika wakitanguliza maslahi ya vyama kuliko taifa, hakuwezi kusaidia Zanzibar. Kutaangamiza taifa hilo na Tanzania kwa jumla.
Tukifika hapo atakayelaumiwa hatakuwa Karume pekee. Hata Rais wa Jamhuri, Jakaya Kikwete na viongozi waandamizi katika serikali na CCM. Wote watanyoshewa kidole, tena kila kona, ndani na nje ya nchi.
Hata nchi wahisani na jumuiya ya kimataifa, watapiga kelele na pengine kuchukua hatua kama ikibidi. Hoja ya kutaka Karume aongozewe kipindi kingine cha urais, imeibuka mara baada ya kiongozi huyo kukutana na Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Seif Shariff Hamad.
Hata hivyo, tayari umezuka upinzani ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) pande zote mbili za Muungano, zikipinga Karume kuongezewa muda zaidi ya kipindi kinachoruhusiwa kikatiba.
Ndani ya CCM na hata CUF, wanachama na viongozi wamegawanyika; hawa huku na wengine kule. Bali, kwa mtu anayepima mambo kabla ya kutenda, kuingiza Zanzibar katika uchaguzi mwingine bila ya kushunghulikia matatizo yaliyopo, ni kuhatarisha maisha ya raia.
Zogo la mgogoro visiwani Zanzibar lilianzia uchaguzi mkuu wa 1995. Vyama vyote viwili CCM na CUF, vilitangaza kugomea matokeo ya uchaguzi na kutuhumu ZEC kuwa imeendesha uchaguzi kinyume cha sheria.
Kabla ya matokeo kitangazwa, CCM iliamini na kukubali kuwa imeshindwa lakini kwa njama. Ilipeleka malalamiko kwa ZEC. Lakini baada ya kutumika kile walichoita teknolojia, Tume ikatangaza kuwa mshindi ni Dk. Salmin Amour (Komandoo) na siyo Maalim Seif.
Tangu hapo, Zanzibar hakujawa tena shwari. Utawala wa Komandoo uliendeleza chuki na uhasama miongoni mwa jamii. Ulikebehi hata jitihada za kuleta maelewano zilizofanywa na jumuiya ya kimataifa kupitia Jumuiya ya Madola.
Si mara moja wa mbili, Salmin na wapambe wake walikebehi majadiliano na mwafaka uliofikiwa kati ya chama chake na CUF mwaka 1999. Machafuko na mauaji ya Januari 25 na 26 mwaka 2001 yaliyofuatia huko Unguja na Pemba, yana kiini katika kutotekelezwa kwa mwafaka huo.
Sasa swali la kujiuliza ni hili: Nani anataka turudi tulikotoka? Bila shaka, hakuna atakaye. Je, kama hayupo, marekebisho yanayohitajika kabla uchaguzi mwingine, yawezekana katika kipindi kilichosalia?
Yapo yanayowezekana. Lakini mengi hayawezi kufikiwa. Kwa mfano, Karume aweza kuamrisha masheha kupunguza munkari na ukereketwa kwa CCM na hivyo wananchi walionyimwa haki ya kuandikishwa wakapata haki hiyo.
Lakini hakuna dalili kwamba aweza kuunda serikali ya umoja wa kitaifa kama ambavyo baadhi ya viongozi wa CCM na CUF wanavyopendekeza, ndani ya kipindi kifupi cha miezi mitatu.
Akiiunda haitamaliza tatizo. Kunahitajika muda wa majadiliano ili kuhakikisha serikali inayoundwa inadumu na kuwa imara. Vinginevyo, inaweza kuwa kama Zimbabwe.
Ni muhimu ifahamike mapema CUF wanapewa nafasi ngapi na zipi ndani ya serikali? CCM nao wanabaki na ngapi na zipi? Je, wanaishia katika baraza la mawaziri tu au wanashuka hadi chini kwa mawaziri na wakurugenzi?
Aidha, serikali ya umoja wa kitaifa, pamoja na kuhitaji kuwepo kwa sheria, ni sera ya chama kilichopo ikulu?
Sera ya sasa ya CCM haitaji serikali ya mseto Zanzibar. Kuiunda ni lazima utumie vikao halali vya chama chenyewe. Haya hayawezi kufanyika kwa mtindo wa kufumba na kufumbua.
Mpaka sasa inadaiwa Karume hajakiambia chama chake wamezungumza nini na Maalim Seif? Hajasema kipi kilichowafanya wazungumze, wakati ni yeye na wafuasi wake waliokwenda Butiama kwa lengo la kuzika mwafaka ulioandaliwa na chama chao?
Vinginevyo Karume atende kwa njia ya kuasi CCM. Abebe suala hili kwa njia ya kupeleka muswada kwenye Baraza la Wakikilishi la Zanzibar, ambapo kwa kutumia wingi wa wajumbe wa CUF na baadhi ya wafuasi wake, waweza kulipitisha.
Lakini ni vema kwenda ndani ya chama. Huko atapata nafasi ya kueleza kwa ufasaha alichojadili na Seif. Kueleza hata idadi ya ajenda zao na zililenga maeneo gani.
Je, ni kitu gani kimesababisha kushindwa kutekeleza hayo kwa miaka minne iliyopita? Kipindi kilichosalia hakitoshi kwa ajili ya kitu gani? Kitu gani kinahitaji muda zaidi? Hii ndiyo njia ya utekelezaji.
Akifanya hivyo, hakika atafanikiwa. Atajenga heshima kwa sasa na siku zijazo. Hata wanaaompinga wataishia kujifunika nyuso. Lakini hilo litawezekana iwapo atakuwa na dhamira ya dhati ya kumaliza tatizo, si kwa kutaka hayo kwa maslahi yake binafsi.
Matatizo ya Zanzibar ni mengi. Kwanza, kuna Katiba mbili na sheria mbili tofauti zinazosimamia chaguzi. Kuna Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 na sheria yake ya uchaguzi, pamoja na Katiba ya Jamhuri ya Muungano na sheria yake ya uchaguzi.
Katiba ya Zanzibar hailazimishi mtu kuwa na kitambulisho cha ukaazi. Inataja kitambulisho cha uraia. Si uraia wa Zanzibar kwa sababu Zanzibar si Jamhuri, ni uraia wa Jamhuri ya Muungano.
Kitambulisho hiki bado hakijapatikana mpaka sasa kutokana na kile kinachodaiwa kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Laurence Masha kuingilia mchakato wa zabuni kinyume cha taratibu na kusababisha ucheleweshaji.
Lakini katika sheria ya uchaguzi ya Jamhuri ya Muungano ambapo ZEC inasimamia upande wa Zanzibar, hakuna mahali panapotajwa kitambulisho cha ukaazi.
Yapo madai yanayoweza kuthibitishwa kwamba baadhi ya masheha wametumia vibaya madaraka yao. Wapo waliogomea kuandikishwa hata ndugu zao wa karibu wakwe zao, dada zao, shangazi zao na hata maimamu wa misikiti wanaowaswalisha asubuhi, mchana na jioni. Kisa? Wanaotaka kuandikishwa siyo wanachama wa CCM.
Mambo yote haya yanahitaji muda zaidi kuyarekebisha. Kingine kinachohitaji muda zaidi ni marekebisho katika ZEC ambayo kwa sasa imepoteza hadhi mbele ya wananchi.
Vinginevyo, katika mazingira ya sasa ambapo ZEC inatuhumiwa, vyombo vya dola vinashutumiwa, watendaji serikalini wananyoshewa kidole, kuitisha uchaguzi ni kujitafutia mgogoro usiokuwa na sababu.
Kuitisha uchaguzi kabla ya kutatua matatizo yaliyopo, ni kutaka nchi iandike historia nyingine badala ya ile ya mwaka 2001 ambapo Tanzania iliyokuwa kimbilio la wakimbizi, yenyewe ilizalisha wakimbizi.
Karume hawezi kukwepa lawama kwa kufikisha Zanzibar mahali ilipo. Ni serikali yake iliyogomea mwafaka mpya na CUF, badala yake ikaja na hoja ya kura ya maoni katika kile kilichoitwa kutaka kuipiku CUF.
Lakini Karume anajua siasa. Ajivunie nini baada ya kipindi cha miaka 10 ya utawala wake? Amani ya Zanzibar yaweza kuwa kitu pekee cha kujivunia kwa karne na karne. Atakayeachia fursa hii itoweke aweza kujuta maisha yake yote.
Chanzo:mwanahalisi