Na. Makao makuu ya Polisi β Dodoma,
Jeshi la Polisi nchini limewatadhadharisha wananchi juu ya uwezekano wa kuibuka kwa matapeli baada ya Mkuu wa Jeshi la Polisi kutoa tangazo la ajira Disemba 1, 2022 kwa vijana wenye sifa za kuajiliwa na Jeshi hilo.
Hayo yalisemwa na Msemaji wa Jeshi la Polisi, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP), David Msime alipotoa taarifa kwa vyombo vya habari kufuatia kutangazwa kwa nafasi za ajira za Polisi.
Alisema kuwa vijana, wazazi ama walezi wasikubali kurubuniwa na mtu yeyote, awe anajiita mtumishi wa serikali wa aina yeyote au mwenye cheo chochote au mtu mwingine yeyote yule atakayewaambia kuwa anao uwezo wa kukusaidia au anafahamiana na kiongozi fulani ambaye anaweza kukusaidia kupata ajira hizo nje ya utaratibu uliotangazwa au utaratibu mwingine utakaotolewa baada ya Disemba 27, 2022 ambayo ni siku ya mwisho ya kuwasilisha maombi ya kuomba nafasi ya ajira.
Misime aliongeza kuwa Jeshi la Polisi linasisitiza kama kijana unazo sifa zilizoainishwa katika tangazo la ajira ni vema ukafuata maelekezo yaliyoambatana na tangazo hilo na si vinginevyo.
βUkikiuka na kufuata maneno ya ulaghai wa matapeli watakao kuambia toa kitu fulani ili usaidiwe, itakuwa ni hasara kwako na hatua stahiki zitachukuliwa dhidi yako kwa mujibu wa sheria pamoja na tapeli mhusika,pale itakapo bainikaβ alisema Misime.
Jeshi la Polisi linatoa wito kwa wananchi kutoa taarifa pale watakapo baini kuibuka kwa watu (matapeli) wa aina hiyo ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa.