Habari zenu wana jamvi,
Nimeacha ajira kwa hasira. Nimefanya maamuzi ya kipuuzi? sijui! Ngoja nianzie mbali kidogo kuwasimulia:
Nilihitimu Shahada yangu ya Uhandisi mwaka jana na baada ya kukaa mtaani kwa miezi mitatu tu nilifanikiwa kupata ajira. Nilipata ajira kama fundi mchundo (Technician) na sio Muhandisi kama nilivyotegemea. Kwa kweli nilivunjika moyo kwa hilo kwa kuwa wakati huo naingia kazini niliingia na jamaa mmoja naye akaajiriwa kama Technician ila yeye amesoma Veta Level 2.
Kilichoniuma mimi ni kwamba nina Stashahada Ya Uhandisi Pamoja na Shahada ya Uhandisi alafu bado nalipwa sawa sawa na mtu mwenye cheti cha Veta, tena kiuhalisia yeye analipwa kiasi kikubwa kwa kuwa yeye hana makato ya Bodi ya Mkopo ila mimi bodi wananinyoosha.
Wakati naanza kazi nilimuuliza bosi wangu kwa nini naajiriwa kama Technician na sio Engineer, akanijibu kwamba nitaweza kupandishwa huko mbeleni kulingana na utendaji. Basi mimi nikaanza kazi.
Kwa kweli kazi ilikuwa na changamoto kwa sababu nilikuwa na majukumu mengi. Nikiwa ofisini nilikuwa nikihusika katika usanifu na kuandaa mpango kazi na nikiienda site nilikuwa napigika zaidi maana nilikuwa nahusika kwenye kusimamia kazi, ununuzi wa materials, na pia nilikuwa nikihusika katika kazi za kufanya kwa mikono.
Yaani kwa ufupi nilikuwa nikifanya kazi za fundi mpaka za muhandisi mimi mwenyewe. Katika mradi wangu wa kwanza nikagundua hata dereva analipwa pesa nyingi kuliko mimi, nikazidi kuumia.
Sasa bwana mwezi uliopita, mwisho wa mkataba wangu ukafika, bosi akaniita akanikabidhi mkataba mpya, lakini baada ya kuupitia nikagundua mshahara ni ule ule na cheo ni kile kile. Basi mimi nikamuomba bosi anipe siku moja nikafikirie alafu nitakuja kusaini au la. Baada ya siku moja nilirudi na nikaamua kuweka dau la mshahara ninaloona mimi ni sahihi. Kwa kifupi bosi alikataa na mimi nilikataa na mimi nikaishia hapo kufanya kazi.
Sasa turudi kwenye kichwa cha uzi huu. Naomba mnishauri niazie wapi maisha ya biashara maana kazi nimeshaacha (na sijui kama lilikuwa wazo la busara), hapa nina 2 million ambayo nilifanikiwa kuikusanya kwa mwaka huo mmoja niliokuwa nikifanya kazi.
Sijawaambia wazazi wangu wala watu wangu wa karibu kwamba nimeacha kazi na ninafikiria kwenda mkoa ambao nitakuwa mbali nao nikaaendelee kujifunza maisha huko.
Nipo tayari kufanya biashara ya hali yoyote, nakaribisha ushauri.
Asanteni.