Riwaya: Mkimbizi

Riwaya: Mkimbizi

SEHEMU YA KUMI NA NNE

Kwa nini watu wanapenda kumuamini Martin Lundi muongo?
“Hapana Tigga...hayo yote yamo katika fikira zako tu mwanangu...ni kutokana na...”
“Paranoid Schizophrenia?” Nilimkatisha mama yangu kwa uchungu, kabla hajamalizia ile kauli yake, na kuendelea; ”Hivyo ndivyo Dokta Lundi alivyokueleza mama? Kuwa hayo mambo ni fikira zilizojengeka bila msingi kichwani mwangu kutokana na huo ugonjwa unaosemekana kuwa ninao?”
“Tigga mwanangu, usiifanye hii hali iwe ngumu kuliko inavyohitajika...”
Nilitoa sauti ya kukata tamaa na kutikisa kichwa kwa masikitiko makubwa.
“Mama! Hivi kuna historia ya wazimu katika familia yetu? Kuna mtu yeyote...babu au bibi fulani huko nyuma, aidha upande wako au wa baba ambaye alipata kuugua wazimu?” Nilimuuliza kwa jazba. Mama alibaki akinitazama tu huku akivisogeza sogeza vile vyombo bila uelekeo maalum. Lile swali lilionekana kuwa lilimchanganya kidogo na niliona wazi kuwa wazo hilo halijawahi kumpitia kichwani mwake hata kidogo.
“Ennh, mama, hebu nieleze hilo...sijawahi kusikia hata siku moja...au mlituficha?” Nilizidi kumsukumia maswali.
“Hakuna Tigga, lakini...”
“Unaona? Mi’ najua magonjwa kama hayo yana namna ya kurithishwa katika familia, au nakosea?”
Mama hakunijibu. Niliona alikuwa amechanganyikiwa na nilimwonea huruma sana.
Nilihisi chuki ya hali ya juu kwa yule mjinga anayejiita Dokta Lundi kwa kutufikisha katika hatua hii mimi na mama yangu. Lakini kwa nini mama asiuone uongo huu? Mimi ni mwanae for God’s sake!
Nilimsogelea na kumuambia kwa kuomboleza: “Mama. Naomba uniamini mimi mwanao. Dokta Lundi ni muongo tena muongo mkubwa sana! Na wala sidhani kama ni dokta kweli yule. Anachofanya ni kupita akinipakazia uzushi wa ugonjwa huo wa uongo ili kuninyima nafasi ya kusikilizwa na kuaminika mahala popote nitakapokwenda. Na hiyo ni kutokana na mambo niliyoyaona kule msituni na ambayo nina ushahidi usiopingika...ushahidi ambao utamuathiri sana huyo Dokta Lundi na wenzake!”
Niliona kabisa kuwa hali ile ilikuwa ikimchanganya vibaya sana mama yangu, na nilizidi kumuonea huruma lakini ilibidi nimueleweshe.
“Mama, mi’ n’na ushahidi wa kuthibitisha kuwa Dokta Lundi si mtu mwema kama anavyotaka wewe umuone...”
“Amenionesha picha za kule msituni Tigga...watu wameuawa Tigga! Kama kuku...!Inatisha sana!” Alisema kwa sauti ya chini huku akilengwa na machozi.
“Na akakuambia kuwa ni mimi ndiye niliyewaua wale watu?” Nilimuuliza mama kwa uchungu. Hakunijibu, lakini katika macho yake niliona kuwa nilikuwa nimeuliza jibu. Iliniuma sana.
“Mama! How can you believe such rubbish?” Nilibwata huku nikitupa mikono yangu hewani,nikimuuliza ni vipi anaweza kuamini upuuzi kama ule, kisha nikaendelea kwa sauti ya chini huku nikisisitiza kauli yangu kwa mikono yangu.
“Mama...ni yeye pamoja na wenzake watatu ndio waliofanya yale mauaji kule msituni! Na hakuna mtu yeyote anayejua hilo isipokuwa mimi. Huoni kuwa anafanya kusudi kunipakazia ugonjwa huo ili taarifa nitakazotoa dhidi yake na wenzake zitiliwe mashaka na kila mtu? Si unaona jinsi wewe mwenyewe unavyoshindwa kuniamini? Hivi ndivyo anavyotaka, na ndivyo inavyokuwa kila mahali niendapo mama!How can you believe him mama?” Nilimueleza kwa hisia kali huku nikihoji uhalali wa mama yangu kuamini uongo wa Martin Lundi kirahisi namna ile.Na hata pale nilipokuwa nikiongea maneno yale, nilijihisi uchovu na usingizi mzito. Nilipiga mwayo mrefu na kujibwaga tena kwenye kiti. Mama alinisogelea na kunipapasa kichwani.
“Pole sana Tigga. Unaonekana una usingizi, kwa nini usijipumzishe kidogo halafu tutaongelea hili jambo baadaye?” Aliniambia kwa upole. Na hii ndio tabia ya mama yangu ambayo toka utotoni mwangu nilikuwa siipendi. Akiwa na jambo lake basi yuko radhi mliahirishe kwa muda kuliko kukubaliana na wazo jingine, akitumaini kuwa baada ya muda utakuwa umeelewa “ujinga” wako na kukubaliana na mawazo yake.
Sasa mimi sina muda wa kupoteza namna hiyo mama!
Nilimtazama mama yangu kwa kukata tamaa, na mwayo mwingine ukanitoka. Sikuwa nimepata usingizi wa kutosha usiku uliopita. Lakini huu sio wakati kulala!Dokta Lundi akitokea...
“Tafadhali usimruhusu Dokta Lundi anikamate mama...please!” Nilimwambia kwa sauti ya chini huku nikihisi macho yakiniwia mazito kuliko kawaida.
“Mi’ nakutakia yaliyo mema kwako mwanangu, na si vinginevyo.” Mama alijibu, lakini kauli ile haikunipa amani hata kidogo.Nilijilazimisha kuinuka na kwenda kujilaza kwenye kochi refu lililokuwa pale sebuleni huku nikiwa nimeukumbatia mkoba wangu. Mama alinishauri nikalale chumbani, lakini sikukubali, nilimwambia kuwa nataka kujipumzisha kwa dakika chache tu.
Nadhani nilisinzia kwa dakika chache sana, kisha nikahisi nikipambana na usingizi ule mzito, nikijitahidi usinielemee.
Lazima niamke! Lazima niamke!
Wazo hilo lilikuwa likinijia tena na tena ilhali usingizi ukizidi kunielemea.Kwa mbali nilisikia sauti ya mama yangu ikinisemesha. Niliinuka ghafla na kutazama kila upande, lakini nilikuwa peke yangu pale sebuleni. Ilikuwa ndoto? Hapana, nilisikia sauti ya mama ikitokea sehemu ndani ya nyumba ile. Alikuwa akiongea na nani? Aliniambia kuwa Koku alikuwa ameshaenda kazini, sasa huyo anayeongea naye ni nani? Niliinuka taratibu na kuelekea kule niliposikia sauti yake ikitokea.
Nilimkuta akiwa katika chumba cha kulia chakula. Alikuwa amekaa kwenye kiti akiwa amenigeuzia mgongo na alikuwa anaongea na simu, na alikuwa akimbembeleza kitu fulani huyo aliyekuwa akiongea naye. Nilisimama kando ya mlango wa kuingilia kule alipokuwepo na kujaribu kusikiliza maongezi yale huku moyo ukinienda mbio.
“...nataka nijue ni wapi hayo matibabu yatakapofanyika na mimi nataka niwepo...”
Usingizi ulinikauka mara moja, nikazidi kusikiliza.
“...yeye yupo hapa, lakini lazima na mimi niwepo...”
Moyo ulinilipuka na kuongeza mapigo.
Mama alikuwa anaongea na Dokta Martin Lundi!
Nilichanganyikiwa.
Haraka nilirudi kule sebuleni na kulinyakua lile begi langu dogo. Nilitembea haraka kuelekea mlango wa nyuma wa nyumba ile, na nilipopita tena kwenye ule mlango wa kuingia chumba cha kulia chakula, mama alikuwa ameshamaliza kuongea na simu.
“U...unaenda wapi Tigga...usingizi umeisha mara hii?” Aliniuliza huku akinisogelea. Moyo uliniuma kuliko kawaida. Sikuweza kumtazama.
“Na...naenda kulala chumbani...” Nilimjibu bila kumtazama na bila kupunguza mwendo wangu. Mwisho wa korido kabla ya kuufikia mlango wa nyuma wa nyumba ile kulikuwa kuna chumba cha wageni. Nilipokifikia nilisimama nje ya mlango wa chumba kile na kumgeukia mama yangu. Alikuwa amesimama akinitazama.
“Ennh...naomba uniamshe ifikapo saa saba...” Nilimwambia kwa sauti ya chini huku nikifungua mlango wa kile chumba.
“Sawa mama...” Alinijibu, kisha akanisogelea kwa hatua za haraka, nami nikamsubiri huku nikitazama sakafuni. Alinikumbatia kidogo na kunibusu kwenye paji la uso.
“Lala unono mwanangu...yote yatakwisha tu, muamini mama yako.”
Sikujua nimjibu nini, lakini machozi yalinitiririka nami nikageuza uso wangu ili asione jinsi nilivyoumia.Niliingia ndani ya kile chumba na kusimama nyuma ya mlango kwa ndani nikisikilizia mienendo ya kule nje huku moyo ukinipiga sana. Hakuna kilichotokea, kisha nikasikia maji yakimwagika jikoni na vyombo vikigongana. Nikahisi mama alikuwa akiosha vyombo jikoni.
No time to waste!
Nilitoka nje ya chumba kile taratibu na kufungua mlango wa kutokea nyuma ya nyumba ile taratibu mno. Nilitoka nyuma ya nyumba yetu na kuruka michongoma iliyofanya uzio wa kuizunguka nyumba ile na kutokea mtaa wa pili.
Huku nikitiririkwa na machozi, nilitembea kwa mwendo wa kasi kuelekea nisiKokujua.
Nilikimbilia kwa Kelvin, nikakutana na usaliti nisioutegemea na roho iliniuma sana. Lakini hili la kukuta usaliti kama ule kwa mama yangu liliniuma zaidi. Sasa nitakimbilia wapi? Kwa nini hawa akina Martin Lundi wanakuwa na uwezo wa kuwarubuni watu mpaka wanafikia hatua ya kunigeuka namna hii?
Au inawezekana ikawa ni kweli mimi nina huo ugonjwa ninaosemekana kuwa ninao na mambo yote ninayoamini kuwa nimeyaona ni fikara zangu tu zenye maradhi?
Lakini nilipopapasa begi langu na kuigusa ile kamera ya marehemu Gil, nilipata hakika kuwa niliyoyaona yalikuwa ni kweli tupu.
Sasa ni nini hii?
Hata mama yangu! Oh, My God!
Ama kwa hakika sasa nilikuwa peke yangu, nisiye na kimbilio.
Ili iweje sasa?
Nilijua kuwa mama alifanya vile akiwa na imani,kuwa ananisaidia, kwamba anafanya kwa faida yangu.
Lakini sivyo mama! Martin Lundi ni muongo na muuaji! Nitawezaje kusema hadi niaminike?
Nilikuwa nikiwaza mambo hayo na mengi mengine huku nikipotelea mitaa ya nyuma kutoka ule uliokuwamo nyumba yetu. Sikuwa na uelekeo maalum, na kwa wakati ule sikujali. Jambo pekee nililojali kwa wakati ule ni kujiweka mbali na mikono ya yule mtu mbaya anayejiita Martin Lundi, na kundi lake.
Bila ya kujua nilikuwa nimezunguka na kufuata mtaa uliotokea mwanzoni mwa ule mtaa ambao nyumba yetu ilikuwepo. Nikiwa nimesimama mwanzoni mwa mtaa ule, niligeuka kutazama upande ilipokuwepo nyumba yetu ambapo ni katikati ya ule mtaa. Nilishuhudia kwa kihoro magari matatu yakisimama kwa kasi na vishindo nje ya nyumba yetu na watu wakiremka na kukimbilia nyumbani kwetu, huku wengine wakiizingira nyumba ile kwa nje. Nilidhani nilimuona Dokta Lundi miongoni mwao. Lakini kwa umbali ule sikuweza kuwa na uhakika. Niliogeza hatua na kupotea eneo lile nikimwomba Mwenyezi Mungu amsaidie mama yangu.
iv.

S
iwezi kuelezea jinsi nilivyoumizwa na kitendo cha mama yangu kuamua kumuamini yule shetani anayejiita Martin Lundi na kupuuzia kabisa utetezi wangu. Kwa kweli hakuna maneno ambayo ninaweza kuyatumia hata yakatosha kuonesha ni kiasi gani jambo lile lilikuwa limeniumiza, kwani ilikuwa ni kupita kiasi. Ni kweli kuwa pale nilipogundua kuwa Kelvin aliamua kunisaliti kwa yule shetani Martin Lundi hata nilipompa maelezo yangu, niliumia hata nikahisi kama kuna ndoana iliyokuwa ikiuvuta moyo wangu kwa nguvu kubwa; lakini kuumia nilikoumia kutokana na hali iliyotokea pale kwa mama yangu, kulikuwa ni zaidi ya hivyo.
Lakini sikuwa na la kufanya, lililotokea lilikuwa limetokea, na aliyelifanya ni mama yangu.
Angalau kwa Kelvin niliweza kuamua kuvunja uchumba na kuachana naye, lakini huyu alikuwa mama yangu! Mama aliyenizaa kwa uchungu mwingi. Sasa vije mtu kama Dokta Lundi akaweza kumrubuni, kumlaghai na kumshawishi hata akaweza kumuamini yeye na akashindwa kuamini maelezo ya mwanae mwenyewe ambaye alipata uchungu usio mfano wakati akimzaa?
Nilishindwa kuelewa, na nilizidi kuchanganyikiwa iliponibainikia kuwa hata ningefanya nini, nisingeweza kumfuta asiwe mama yangu kama jinsi nilivyoweza kumfuta Kelvin kutoka katika maisha yangu (sijui naye yu hali gani huko aliko). Hivyo nilimwomba Mwenyezi Mungu amnusuru mama yangu na ghadhabu za Dokta Lundi baada ya kufika pale nyumbani na kukuta kuwa nimewatoroka kwa mara nyingine tena, wakati yeye aliwapigia simu na kuwahakikishia kuwa nilikuwepo pale nyumbani.
Baada ya kuwashuhudia kwa mbali akina Martin Lundi wakiizingira nyumba yetu, nilielekea moja kwa moja kituo cha basi na kupanda basi nililolikuta likipakia abiria pale kituoni bila ya kujali lilikuwa likielekea wapi, lengo likiwa ni kupotea kabisa eneo lile. Na njia nzima wakati basi lile likifanya safari yake ambayo nilikuja kuelewa baadaye kuwa lilikuwa likielekea posta, nilikuwa ni mtu niliyepigwa bumbuwazi. Woga ulinitawala kupita kiasi kwani sasa ilikuwa imenifunukia wazi wazi kichwani mwangu kuwa katika janga hili nilikuwa peke yangu.
Nilikwangua akili yangu nikijaribu kutafuta ni hatua ipi ifuate lakini niliambulia ukungu tu. Nilifikiria kumfuata dada yangu Koku kazini kwake, lakini nililifuta wazo hilo haraka, kwani nilijua kuwa asingeweza kunisaidia lolote katika mazingira yale. Nilijua iwapo mama ameamua kuchukua msimamo aliouchukua katika swala langu, hakuna shaka kabisa kuwa na yeye atakuwa na mtazamo ule ule.
Nilidhani kuwa Koku angeweza kusaidia kwa kumbana Dokta Lundi kwa maswali ya kitaalamu juu ya ule ugonjwa anaonipakazia na hatimye kubainisha uongo wake, lakini kama angefanya hivyo, basi hata mama angekuwa na mtazamo tofauti. Lakini pia nilikumbuka kuwa, dada yangu alikuwa ni nesi wa kawaida tu.Yumkini akawa hana uwezo na utaalamu wa kuuelewa ugonjwa ule kama jinsi alivyouelewa Dokta Martin Lundi muongo.
Sasa nifanye nini...?
Niliamua kwenda ofisini kwangu, katika jumba la Makumbusho ya Taifa. Huenda huko nikapata baadhi ya majibu ya maswali yangu. Kwani si huko ndipo iliposemekana kuwa ile barua ya uongo iliyopelekwa kwa mkuu wa wilaya ilikuwa imetokea? Sasa niliona kuwa iwapo nilikuwa nashutumiwa kwa mambo yasiyo na msingi, basi ni wajibu juu yangu kutafuta kiini cha shutuma hizo. Shutuma za kuwa nilikuwa mgonjwa wa akili zilikuwa ni nzito na mbaya sana. Nilijua kuwa ile barua ilikuwa imeghushiwa, na hata kule ofisini haijulikani kuwa kulikuwa kuna barua kama ile. Lakini sikuwa na namna ya kujithibishia hilo isipokuwa kwenda ofisini. Aidha nilijua kuwa kwa vyovyote iliniwajibikia kuripoti pale ofisini baada ya kutoka kwenye ile safari iliyozaa balaa niliyotumwa na ofisi. Sikujua ningekutana na nini huko nilipoazimia kwenda, lakini sikuona njia nyingine ya kuanza kutafuta ukweli wa mambo yale ya uongo niliyopakaziwa zaidi ya ile.
Niliingia ndani ya jengo la ofisi yetu na kuelekea moja kwa moja ofisini kwa afisa utumishi, ambaye ndiye muangalizi wa maswala yote ya wafanyakazi na ajira zao, lakini kabla sijaifikia ofisi yake niliwahiwa kwenye korido na baadhi ya wafanyakazi wenzangu ambao walinizingira kwa maswali kemkem kuhusu matukio ya huko msituni. Wapo walionipa pole, wapo walioulizia ilikuwaje hadi wenzangu wakaangamia kule porini, wengine walikuwa wakiniambia kuwa kwa kujipeleka pale ofisini nilikuwa nimejitia kwenye mtego na kunishauri niondoke haraka, huku wengine wakionesha wazi kuwa walikuwa wakiniogopa. Sikuweza kujibu swali hata moja, kwani yalikuwa yakija bila mpangilio maaluim, nami nilianza kuingiwa na woga na kujuta kwa nini niliamua kwenda pale ofisini. Niligundua kuwa habari zangu zilikuwa zimefika pale ofisini, na kwamba kwa ujumla ilieleweka kuwa Tigga si mtu salama tena kuwa karibu naye. Hili nililibaini kutokana na hali iliyojitokeza pindi nilipoingia pale ofisini, kwani wenzangu walikuwa wakiniuliza maswali yale na kunipa pole huku wakinitazama kwa wasiwasi, na muda wote walikuwa kikundi, hakuna hata mtu mmoja aliyekuwa tayari kukaa na mimi peke yake. Nikiwa nimezingirwa na wale wafayakazi wenzangu pale kwenye korido, nilimuona Mkurugenzi wa Idara ya Makumbusho akitoka ofisini kwake, iliyokuwa kwenye ghorofa ya kwanza, na kuchungulia pale chini nilipokuwa nimezongwa na wafanyakazi wenzangu. Tulitazamana kwa muda, kisha alirudi ofisini kwake na kufunga mlango.
Hatimaye nilifanikiwa kujichomoa kutoka kwenye lile kundi la wafanyakazi wenzangu na kuingia ofisini kwa afisa utumishi.
ITAENDELEA
Marylin.
Unachofanya si cha kiungwana. Hii ni kazi ya mtu yenye hatimiliki wewe unaiweka hapa bila ridhaa ya Mwandishi.Nakushauri usiendelee tena. Mod walishataarifiwa kuhusu hili.

Kama mtu anapenda kusoma vitabu vya Tuwa (pamoja na hiki) apakue app ya Uwaridi
Uwaridi - Apps on Google Play. Tuwape support waandishi wetu.
 
SEHEMU YA ISHIRINI NA MOJA

“Not so fast young lady!” Dick Bwasha alinikemea huku naye akisimama kutoka kwenye kiti chake na kunikunjia sura yake kwa ghadhabu, ile cheko yake ya kejeli na mchezo-mchezo ikiyeyuka kabisa usoni mwake, akimaanisha kuwa nisifanye haraka kuondoka.
“Hey! Niachie!” Nilimwambia kwa hasira huku nikijaribu kuunasua mkono wangu kutoka mkononi mwake. Dick Bwasha alizunguka ile meza kwa wepesi wa ajabu na kuja hadi pale kwenye kiti nilichokuwa nimekalia hapo awali na kunikalisha huku akiniinamia na kunisemea karibu sana na sikio langu.
“Unataka msaada, n’takusaidia. Lakini na wewe lazima ukubali kunisaidia bibie, unasemaje?”
Mwili ulinifa ganzi. Huyu bwana ana wazimu au kitu gani?
“Mista, mimi ni mtu mwenye heshima zangu. Naomba huo upuuzi wako uupeleke kwa wanaoweza kuuvumilia lakini sio kwangu! Naomba niende zangu.” Nilisema kwa utulivu wa hali ya juu huku nikitafuta kitu cha kumbamiza nacho ili niweze kutoka salama mle ndani. Nimekuja kujaribu kuchukua pesa kutoka kwenye akaunti yangu ili niweze kukabiliana na matatizo yangu, badala yake nakutana na mjinga mwenye mawazo ya ngono za kibeberu.
Haya mambo gani sasa.
Dick Bwasha alirudi nyuma ya meza yake na kutoa picha kutoka kwenye droo ya meza ile na kuitupia juu ya meza mbele yangu.
“Ukitazama hiyo picha utagundua kuwa sina shida kabisa na hicho ki----- chako mwanamke!” Aliniambia taratibu huku akinitazama kwa ghadhabu, akizitamka nyeti zangu kama anayetamka takataka fulani tu hivi.
Sikuamini macho yangu.
Nilitazama ile picha bila kuishika, ikiwa imelala pale mezani na nilihisi kudharaulika na kudhalilika kusiko kifani. Ile picha ilimuonesha Dick Bwasha akiwa uchi wa mnyama juu ya kitanda. Pamoja naye, ilikuwapo mijimama miwili ambayo nayo ilikuwa kama ilivyozaliwa, hakukuwa na shaka kuwa walikuwa wakifanya nini pale kitandani. Ilikuwa ni picha chafu sana na sikuelewa wale watu waliwezaje kupiga picha kama ile bila ya kuwa na wazimu kidogo. Na pia nilishindwa kabisa kumuelewa yule meneja wa tawi la ile benki niliyoiamini kunitunzia pesa zangu miaka yote ile.
Niliinua uso kwa mshangao na kumtazama yule jamaa, huku akilini mwangu nikijithibitishia kuwa jamaa hakuwa mzima.
“Kha! Sasa hii ndio nini?” Nilijikuta Nikimuuliza kwa mshangao huku ile hisia ya kudhalilika kusiko kifani ikizidi kunikolea.
“Hiyo ni kukuonesha ni jinsi gani mawazo yako yalivyo potofu. Niliposema na wewe inabidi unisaidie sikuwa na maana hiyo iliyojengeka kichwani mwako!” Aliniambia huku akibenua midomo yake kwa kiburi kikubwa kabisa.
Kwa kweli alinichosha!
“Sasa…” Nilianza kumuuliza, lakini Dick Bwasha alipiga meza kwa nguvu kwa kiganja chake na kunikatisha.
“We want the tape Tigga!” Aliniambia kwa sauti ya msisitizo huku akiinua mwili wake na kunisogezea uso karibu sana na wangu, akinitazama kwa macho makali yenye kuogofya, akimaanisha kuwa wanautaka ule mkanda wa video niliokuwa nao.
Duh! Hii sikuitegemea kabisa, na mshituko nilioupata naona ulikuwa mkubwa kuliko yote niliyowahi kukutana nayo tangu kinyang’anyiro hiki kinikute.
“Say whaaat!” Niliruka kwa mshituko huku nikiinuka kutoka kwenye kiti nilichokuwa nimekalia na kubaki nikiwa nimemkodolea macho yule mtu aliyekuwa mbele yangu huku nikishindwa kabisa kuuzuia mwili wangu usitetemeke. Dick Bwasha aliendelea kunitazama kwa hasira bila kutetereka.
“You give us the tape, we give your money back…and more.” Dick Bwasha aliongea taratibu huku akiendelea kunitazama, akimaanisha kuwa wataniruhusu kuchukua pesa zangu na hata na ziada, iwapo nitawapatia ule mkanda wa video wenye ushahidi dhidi ya akina Martin Lundi.
Niliinua mkono uliokuwa ukitetemeka na kumnyooshea kidole huku macho yakiwa yamenitoka pima.
“We…wewe…ni mmoja wao!” Nilisema kwa kitetemeshi. Dick Bwasha hakunjibu, badala yake aliketi vizuri kwenye kiti chake na kuirudisha ile picha yake chafu ndani ya droo ya meza yake.
“Mmoja wa akina nani Tigga?” Aliniuliza huku akiendelea kunitazama kwa makini. Sikuweza kujibu. Nilibaki nikimkodolea macho kwa kihoro.
Yaani hawa akina Martin Lundi wametanda kila mahali?
Inawezekana vipi hii lakini? Huyu mtu anahusikaje na swala zima la kule msituni? Mungu wangu! Sasa nitapambana na watu wangapi Tigga mie?
“Tunautaka huo mkanda Tigga, na tutakupa pesa zote uzitakazo.” Dick Bwasha alinizindua kutoka kwenye yale mawazo ya kuijutia nafsi yangu.
“Halafu hizo pesa nikazitumie ahera? Nyie ni wauaji! Sina mkanda mie!” Nilimropokea kwa jazba huku nikianza kusota ukutani kuuelekea mlango. Dick Bwasha aliendelea kuketi tu kwenye kiti chake bila hata kutetereka.
“Huwezi kutukimbia Tigga. Bora ukubali ofa hii. Tulijua tu kuwa utakuja hapa, nami nilikuwa nakusubiri muda wote. Toa mkanda huo halafu tutakusahau na hutatuona tena.”
“Ooh, Yeah? Sitawaona tena kwa sababu nitakuwa mfu sio?”
“Tukitaka kukuua Tigga tunakuua tu, wala hilo si tatizo kwetu lakini hilo si lengo letu…”
“Nyinyi ni akina nani? Mna lengo gani na nchi hii? Maana mnachokifanya kinaelekea kuathiri taifa zima sasa! Haiwezekani muwepo katika kila nyanja muhimu kama hizi halafu muwe na sera kama hizo….”
“Sio swala la nchi hili mwanamke!” Dick Bwasha alifoka kwa hasira kali kuliko nilivyotarajia, na akabaki akinitazama kwa hasira huku akihema kwa nguvu, kisha akaendelea; “Ni swala dogo tu la mkanda wa video Tigga, sasa sijui kwa nini unataka kulikuza bila sababu!”
“Khah! Hilo swala dogo limeacha watu wameuawa kama kuku kwenye msituni fulani ndani ya nchi hii, huku mimi nikitangaziwa wazimu!”
“Wewe ni mgonjwa wa akili Tigga, lazima ukubali hilo. Kuung’ang’ania kwako huo mkanda wa video ni sawa na kichaa kung’ang’ania bunduki. Ataua kila mtu, ndio maana sisi tunataka kukusaidia…”
Nilibaki nikimkodolea macho kwa mshangao yule jamaa. Hivi hawa jamaa ni kweli wanaamini kuwa mimi ni mwehu? Nilitaka kusema neno nikaghairi, sikuona sababu ya kuendelea kubishana na yule adui juu ya jambo lile.
“Siwezi kuendelea kusikiliza upuuzi huu. Mi’ naondoka, fanya utakalo!” Nilimwambia huku nikiuendea mlango kwa hatua za haraka.
“Nenda tu Tigga, na wala sitakuzuia. Lakini ujue kuwa tutayafanya maisha yako yawe magumu sana na utajuta kwa ubishi wako!” Dick Bwasha aliniambia huku akinitazama kwa hasira. Nilitoka nje ya ofisi yake na kupitiliza hadi pale kaunta ambako nilikuta watu wachache wakiwa wamepanga foleni wakiendelea kupata huduma kama kawaida, bila ya kujua mambo yaliyokuwa yakitokea nyuma ya zile kaunta, wala undani wa watendaji wakuu wa benki ile.
Ni wapi ambapo hawa watu hawapo?
Nilitoka nje ya ile benki nikipepesuka huku akili ikinizunguka. Nilivuka barabara bila ya kuangalia na nikashtukia nikipigiwa honi huku nikisikia msuguano wa tairi za gari na lami. Niliruka kwa mshituko huku nikikoswakoswa kugongwa na gari iliyokuwa inakuja kwa kasi. Nilichanganyikiwa nakurudi mbio kule nilipotokea, kumbe nako kulikuwa kuna gari nyingine inakuja, nayo ikanipigia honi kubwa huku ikiserereka na kunikwepa.
Dereva wa ile gari ya pili iliyonikwepa alitoa uso nje ya dirisha lakena kunipigia kelele kwa hasira.
“Anti umepewa talaka nini?” Kisha akamalizia na tusi zito la nguoni. Nilisikia kelele na mayowe ya watu wakizomea, lakini sikujali.
Nilizidi kuongeza mwendo, ingawa kwa wakati ule sikujua nilikuwa naenda wapi. Nilikuwa nimechanganyikiwa vibaya sana, na nilijiona kuwa sasa nilikuwa naelekea kabisa kwenye wazimu.
Nilipopata fahamu kidogo niligundua kuwa nilikuwa nimeshika usawa wa kuelekea kituo cha mabasi ya Kivukoni.
vi.

H
atua chache kutoka kwenye ile nyumba ya wageni niliyokuwa nimepanga kule Kigamboni nilipata na mshituko mwingine ambao sikuutegemea. Nikiwa kimya ndani ya teksi niliyokodi baada ya kuteremka kwenye pantoni baada ya kile kisanga cha kule benki kilichonivuruga akili, nilimuona mwanamke akitoka kwenye ile nyumba ya wageni na kuiendea gari iliyokuwa imepaki upande wa pili wa barabara nje ya nyumba ile. Moyo ulinilipuka na nikaketi wima kwenye kiti cha gari ile na kumtazama kwa makini huku ile tekis niliyoikodi ikizidi kuikaribia ile nyumba ya wageni na ile gari aliyoiendea yule mwanamke.
Moyo ukinipiga nilimtazama kwa makini yule mwanamke na kihoro kilichoanza kutulia baada ya mshituko nilioupata kule benki kilinirudia upya tena kwa kishindo kikubwa.
Alikuwa ni yule askari wa kike aliyeniachia kule kwenye nyumba ya wageni ya sinza nilipokimbilia baada ya vurumai iliyotokea nyumbani kwa Kelvin!
Mwili wote uliingia baridi na nikahisi nikishindwa kupumua vizuri. Nilibaki nikimkodolea macho yule mwanadada, ambaye alikuwa amevaa mavazi ya kiraia na alikuwa akiongea na mtu aliyekuwa ndani ya ile gari iliyokuwa imepaki mbele ya ile nyumba ya wageni, upande wa pili wa barabara. Na muda huo dereva wangu alianza kupunguza mwendo kwani tulikuwa tumeifikia kabisa ile nyumba ya wageni ambapo ndipo nilipomuelekeza anipeleke.
“Twende mbele tu! Usisimame hapa!” Niliropoka kwa hofu huku nikijishughulisha kutoa pesa kwenye mfuko wa suruali yangu.
“Lakini Anti, gesti si hii hapa?” Yule dereva aliniuliza kwa mshangao.
“Endesha bwana! Naenda...naenda saluni kwanza...kule mbele!” Nilimfokea yule dereva kwa kuchanganyikiwa, naye aliipita ile nyumba ya wageni kwa mwendo ule ule wa taratibu huku akinigeukia kwa mshangao. Wakati huo nilijitia kuangusha baadhi ya sarafu na kuinama kuziokota huku nikilaani kitendo kile, lakini nia yangu hasa ilikuwa kuinama ili yule mwanamke asinione wakati gari yetu ikipita pale walipokuwa wamesimama.
Nikiwa ndani ya ile teksi niligeuka na kupitia kwenye kioo cha nyuma cha ile teksi nilimuona yule mwanamke akiingia ndani ya ile gari nayo ikaondoka eneo lile kwa mwendo wa kasi.
“Shit!” Nililaani kitendo cha wale wauaji kugundua maficho yangu nikiwa nimechanganyikiwa na kutazama kule tulipokuwa tukielekea.
“Sasa nini tena Anti? Mbona hivyo?” Yule dereva alilalamika huku akinitazama kwa mshangao, akidhani nilikuwa nimemlaani yeye. Nilimtaka radhi kuwa si yeye niliyemkusudia na kumuambia aniteremshe mbele ya saluni moja ya akina mama, jambo ambalo alilifanya kwa faraja kubwa, kwani bila shaka alishaanza kuona kuwa nilikuwa kichaa.
“Heh! Sasa nitakimbilia wapi?” Nilijisemea mwenyewe huku nikizubaa nje ya ile saluni na kuelekea kwenye kiosk kimoja kilichokuwa jirani yake na kuketi nikiiangalia ile teksi ikitoweka.
Bila shaka utakuwa na hisia ni jinsi gani nilivyochanganyikiwa. Yaani baada ya msukosuko wa kule benki na vituko na vitisho vya yule mtu aliyeitwa Dick Bwasha, halafu nafika hapa kwenye maficho yangu nakuta kuwa kumbe yule mwanamke aliyeahidi kuyafanya maisha yangu yawe mabaya kabisa hapa duniani naye alikuwa amekwisha fika.
Ni wazi kuwa wale wauaji walifika pale kwenye ile nyumba ya wageni kunifuata mimi wakanikosa, sasa wameacha ujumbe gani pale kwenye ile nyumba ya wageni? Jambo la busara kuliko yote kwangu wakati ule lilikuwa ni kutokomea moja kwa moja, nisirudi tena kwenye ile nyumba ya wageni, kwani haikuwa na shaka kuwa ile nyumba sasa si salama tena kwangu, lakini nitafanyaje? Ni lazima niende tu nikajionee mwenyewe kilichoandaliwa kwa ajili yangu na wale wauaji wabaya. Pia kuna vitu vyangu kule kwenye ile nyumba ya wageni ambavyo nisingeweza kuondoka bila kuvichukua.
Hasa ule mkanda wa video.
Nilikaa kwa muda mrefu pale kwenye kiosk nikitafakari hatua ya kufanya, lakini kila nilivyotafakari, pamoja na woga ulionikumba katika kuingia tena kwenye ile nyumba ya wageni, sikupata wazo lolote zuri zaidi ya kwenda tu kwenye ile nyumba ya wageni na kukusanya vitu vyangu na kuondoka. Iwapo nitakuta kuwa yule askari wa kike anayeshirikiana na akina Martin Lundi ameacha wenzake wanisubiri, basi nitapambana nao huko huko. Si niliamua kuwa muda wa kuanza kuwawinda ulikuwa umefika? Sasa hii ndiyo ilikuwa nafasi yangu. Nilijipa moyo huku nikijiona kabisa kuwa ujasiri ulikuwa ukinipungua kwa kasi, kwani kasi ya maadui zangu kunizidi kete ilikuwa ni kubwa mno.
Kwanza Dick Bwasha, halafu yule mwanadada askari...kisha nani tena? (Niliguna).
Nililipia soda niliyoagiza na kuondoka kuelekea kwenye ile nyumba ya wageni huku nikiomba Mungu anijaalie uwezo wa kukabiliana na mambo nitakayokutana nayo.
Niliingia ndani ya ile nyumba ya wageni nikiwa na wasiwasi mkubwa. Nilichukua ufunguo wangu pale kaunta nikitarajia kusikia ujumbe wowote wa ajabu ajabu kutoka kwa yule mhudumu lakini haikuwa hivyo. Nilianza kuelekea chumbani kwangu taratibu, lakini nilirudi na kumuuliza yule mhudumu.
“Nilimuona dada mmoja akitoka huku ndani muda mfupi uliopita...ni nani yule?”
“Dada mmoja makini hivi mwenye shepu moja bomba sana?” Yule mhudumu aliniuliza, akielezea maumbile ya yule mwanadada. Nilimwambia ndio huyo huyo huku nikikumbuka jinsi hata mimi nilivyoisifia shepu yake siku ile nilipomuona kwa mara ya kwanza alipokuwa amevaa mavazi yake ya kiaskari.
“Yule ni mpangaji mpya, ameingia jana usiku, yuko na buzi lake chumba namba 16.” Yule mhudumu alinijibu bila ya kuonesha kutiwa wasiwasi na kuuliza kwangu juu ya yule mwanadada.
“Aaanh! Okay....” Nilimjibu huku nikigeuza na kuanza kuelekea chumbani kwangu huku uso wangu ukiwa umejikunja kwa kutafakari hali ile, kwani chumba namba 16 kilikuwa kinatazamana na chumba changu.
Na nilikumbuka kuwa usiku uliopita niliwasikia wahudumu wa ile nyumba ya wageni wakimkaribisha kwenye kile chumba yule “mpangaji” mpya, wakati nikiwa nimezongwa na mawazo juu ya kitendo cha rafiki yangu Aulelia Mushi kunikana wazi wazi hadharani na tatizo la pesa lililokuwa likielekea kunikabili.
Kumbe nilikuwa nimelala nyumba moja na adui yangu!
...ameingia jana usiku, yuko na buzi lake chumba namba 16.
Moja kwa moja nilijua kuwa wale watu watakuwa walinifuata nikitokea mjini siku iliyopita, kwani baada ya kuchanganywa na tabia ya Aulelia, sikuwa makini kabisa wakati narudi huku mafichoni kwangu. Hivyo iliwezekana sana wao kunifuatilia bila mimi kujua.
Shit!
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA ISHIRINI NA MBILI.

Na nilikumbuka kuwa usiku uliopita niliwasikia wahudumu wa ile nyumba ya wageni wakimkaribisha kwenye kile chumba yule “mpangaji” mpya, wakati nikiwa nimezongwa na mawazo juu ya kitendo cha rafiki yangu Aulelia Mushi kunikana wazi wazi hadharani na tatizo la pesa lililokuwa likielekea kunikabili.
Kumbe nilikuwa nimelala nyumba moja na adui yangu!
...ameingia jana usiku, yuko na buzi lake chumba namba 16.
Moja kwa moja nilijua kuwa wale watu watakuwa walinifuata nikitokea mjini siku iliyopita, kwani baada ya kuchanganywa na tabia ya Aulelia, sikuwa makini kabisa wakati narudi huku mafichoni kwangu. Hivyo iliwezekana sana wao kunifuatilia bila mimi kujua.
Shit!
Nilifungua chumba changu nikiwa bado nimezongwa na wazo la kuwa wale watu wangeweza kunivamia usiku ule mle ndani na nisingekuwa na njia yoyote ya kujiokoa kwani sikuwa nimejiandaa kwa lolote, nikiwa na imani kabisa kuwa hakukuwa na mtu yeyote aliyejua kuwa nilikuwa nimejificha katika ile nyumba kule Kigamboni. Niliingia chumbani mwangu na kusimama ghafla huku nikitoa mguno wa mshituko mkubwa.
Chumba changu kilikuwa kimechakuriwa vibaya sana. Yaani ilikuwa ni kazi ya haraka na isiyojali mpangilio uliokuwamo mle ndani kabla. Mashuka yote yalikuwa yametolewa kitandani na kutupwa chini kwenye zulia. Makochi yalikuwa yamepinduliwa juu chini na kuraruriwa kwa ghadhabu, mito na godoro vilikuwa vimechanwa kwa kisu au wembe mkali sana. Kabati la nguo lilikuwa limefunguliwa na kuachwa wazi. Meza ndogo iliyokuwamo mle ndani ilikuwa imelalia ubavu kwenye kona moja ya kile chumba, madaftari na makaratasi yangu vikiwa vimesambaratishwa hovyo sakafuni. Zulia lilikuwa limefunuliwa baadhi ya sehemu na kuachwa likiwa hovyo kabisa.
Nilitazama mabegi yangu na nikaona kuwa yalikuwa yamepekuliwa kwa umakini wa hali ya juu. Nguo zangu zote zilikuwa zimetawanywa hovyo mle ndani na kutokana na mtawanyo ule wa vitu mle ndani, niliweza kuona hasira za wale waliokuwa wakiifanya hiyo kazi, na nikapata hisia ya hali ambavyo ingekuwa iwapo wangenikuta mimi mwenyewe.
Nilibaki nikiwa nimeduwaa huku hasira zikinipanda, kwani hakuna kitu kilichinokera kama mtu kuchezea nguo zangu za ndani. Na pale nilipokuwa nimesimama, niliziona nguo zangu za ndani zikiwa zimetupwa tupwa hovyo na hata zile pedi zangu za hedhi zikiwa zimechanwa chanwa kwa visu au viwembe na kutawanywa hovyo mle ndani.
Nikiilazimisha akili yangu ifanye kazi inavyotakiwa, nilianza kuisaka kamera yangu ambayo nilipoondoka niliiacha ndani ya kile kibegi chagu kidogo, ambacho nilikitumbukiza ndani ya lile begi langu jingine kubwa kidogo nililonunua wakati nilipotia mguu wangu kwa mara ya kwanza pale Kigamboni.
Niliikuta kamera yangu ikiwa chini ya kitanda, sehemu ya kuwekea mkanda ikiwa wazi.
Mkanda haukuwemo.
Nilitoka mbio na kuwaita wahudumu wa ile nyumba na kuwaonesha kituko kile, nikitaka kujua ni nani aliyehusika na tendo lile.
Kilichofuatia hapo ni vurumai ya hali ya juu, kila mhudumu akidai kuwa yeye hakuhusika na tukio lile. Waliuliza iwapo wakaite polisi, nikawauliza kuwa wanataka hao polisi waje wamkamate nani kati yao, na wote wakagwaya. Nilimuuliza yule mfagizi wa siku ile iwapo alipoingia kufagia chumba changu alikikuta katika hali ile, naye akaeleza kuwa hakikuwa kwenye hali ile na alikisafisha na kutandika kama kawaida na kukifunga, wakati huo mimi nilikuwa nimeshatoka.
“Ina maana hamkusikia kelele au vishindo vyovyote kutokea humu ndani?” Niliuliza kwa mshangao huku akili ikinichemka. Walinijibu kuwa hawakusikia chochote, na mara nyingi muda wa katikati ya asubuhi wakishafanya usafi wao huwa wanakaa upande wa mbele wa ile nyumba, hivyo inawezekana kabisa wasisikie lolote.
Niliwauliza iwapo waliwaona wale wapangaji wa chumba namba 16 wakitoka nje muda wowote katika siku ile baada ya mimi kutoka. Wakanijibu kuwa kwa mara ya kwanza wapangaji wa chumba namba 16 walitoka nje ya chumba chao muda mfupi kabla ya mimi kurejea, na kwamba hata usafi chumbani kwao hawakutaka ufanyike, wakidai kuwa walikuwa wanalala na chumba hakikuwa kichafu.
“Walipotoka muda mfupi uliopita, waliwaaga kuwa ndio wanaondoka moja kwa moja au walisema watarudi?” Niliwauliza, nao wakanijibu kuwa walikuwa wamelipia kwa muda wa siku mbili na kwamba walisema kuwa wangerudi.
Nilijua kuwa wale watu walikuwa ndio wameondoka na hawatarudi, lakini sikuwaambia hilo.
“Kwa hiyo Anti…kuna vitu vimeibiwa?” Mmoja wa wale wahudumu aliniuliza. Nilimgeukia kwa hasira na kumuuliza kwa ukali.
“We’ unaonaje, huu si wizi wa wazi tu?” Halafu nikaanza kuokota vitu vyangu huku nikilaani kwa sauti kuwa nilikuwa nimekaa kwenye nyumba ya wageni isiyo na usalama hata kidogo. Moyoni nilijua kuwa si kosa lao, kwani nilijua kuwa hata ningekuwa kwenye hoteli gani, au nyumba yoyote nyingine ya wageni, ilikuwa ni swala la wale wabaya wangu kujua niko wapi tu, halafu tukio kama lile lingetokea huko huko. Bahati yao mbaya ni kuwa nilikuwa nimeamua kuja kujificha kwenye nyumba yao ya wageni, na wale wabaya wangu wamenigundua. Ingawa walijitetea sana kuwa tukio kama lile halijawahi kabisa kutokea pale kwao, lakini niliamua kuzidi kulaumu ili wasizidi kuniuliza maswali zaidi, kwani kama ingewajia akilini kuwa ule haukuwa wizi bali wale watu walikuwa wakitafuta kitu fulani mle ndani mwangu, lazima wangekimbilia kuita polisi, jambo ambalo sikulitaka kabisa kwa sababu zinazoeleweka.
Mmoja wa akina dada wahudumu wa mle ndani alianza kunisaidia, lakini nilimzuia na kuwaomba wote wanipishe mle ndani nikiwaambia kuwa nilihitaji kuangalia vitu vyangu vizuri ili nijue ni vitu gani hasa vilivyoibiwa.
Walitoka huku wakibwabwaja maneno ya kunipa pole na wakiulizana wao kwa wao ni jinsi gani tukio lile liliweza kutokea.
Nilijifungia mle ndani na kuanza kukusanya vitu vyangu haraka haraka, nikijua kuwa muda wowote wale wauaji wangeweza kurudi na kunitembezea ubabe wao, kwani wakishindwa kuupata ule mkanda kwa njia moja, lazima watatumia nyingine. Kufikia sasa vitisho vimeshindwa, ndio kisa wakaamua kutumia njia hii ya wizi, na iwapo na hii haitafanikiwa, basi kwa vyovyote watatumia ubabe.
Baada ya kukusanya nguo na baadhi ya vitu vyangu ambavyo havikuathirika na ule upekuzi ambao kwangu niliuona kuwa ni kuingiliwa undani wangu kusikofaa kabisa, nililifungua tena lile begi langu kubwa na kuweka vitu vyangu vilivyonusurika kutoka kwenye upekuzi ule wa fujo, nikiitumbukiza na ile kamera ambayo likuwa imevunjika kidogo kwenye pembe yake moja, bila shaka baada ya kupigizwa chini katika ile pekua pekua yao, nikijua kuwa kama si kile chumba kuwa na zulia zito, basi bila shaka ile kamera ingevunjika vibaya sana.
Nilipokamilisha hili nilikimbia upesi kule bafuni na kuchukua mswaki na baadhi ya vipodozi vyangu na nilikuwa narudi tena kwenye kile chumba changu cha kulala wakati niliposikia simu ikiita. Nilipagawa, kwani sikuwa na simu na muda wote katika kuokota vitu vyangu mle ndani sikuona kuwa kulikuwa kuna simu.
Hii ni nini sasa?
Nilianza kuisaka ile simu nikifuatilia sauti ilipokuwa ikitokea huku moyo ukinipiga na akili ikinitembea kwa kasi sana. Ilikuwaje hata hii simu ikawa humu ndani? Ni kwamba imesahauliwa na wale wavamizi walioondoka muda si mrefu, au wameiacha makusudi ili wanipigie wakitaka kuongea na mimi? Na kama ni hivyo, ina maana walijua kuwa hivi sasa nilikuwamo mle ndani? Au walikuwa wanabahatisha tu?
Niliikuta simu kwenye ua la plastiki lililokuwamo mle ndani kama sehemu ya mapambo, ambapo simu ile iliwekwa kwenye kopo maalum lililobeba lile ua ambalo lilikuwa limesimamishwa kwenye kona moja ya kile chumba.
Nilipotoka mle ndani asubuhi ile, lile ua lilikuwa juu ya meza ndogo iliyokuwamo mle ndani, sehemu ambayo lilikuwa likiwekwa siku zote tangu nianze kuishi ndani ya chumba kile.
Ilikuwa ni ile simu yangu iliyotoweka kule msituni!
Niliichukua ile simu kwa mikono iliyojaa kitetemeshi na kuangalia namba iliyokuwa ikinipigia.
Hakukuwa na namba yoyote iliyoonekana kwenye ile simu zaidi ya neno “Private Number Calling”.
Huyu ni nani?
Nilizidi kuitazama ile simu kwa mshangao huku moyo ukinipiga kwa nguvu, nikijishauri iwapo niipokee ile simu au vinginevyo.
Vije iwapo ile simu ilikuwa imepigwa na wale wauaji kwa nia kwamba nikiipokea watajua kuwa nipo mle ndani ili wanivamie?
Au ni kweli kuwa wameisahau, na huyo alikuwa ni mwenzao akijaribu kuwasiliana nao? Kama ni hivi, basi labda nikiipokea angalau nitaweza kuongea na mmoja wa wabaya wangu na labda nitaweza kumlaghai kuwa mimi ni yule askari wa kike na kuweza kujua sehemu ya mikakati yao.
Lakini ni kweli ile simu ilikuwa imesahauliwa?
Kwa nini itokee leo ghafla tu baada ya kupotea muda wote huo?
Hapana,haikuwa imesahauliwa.
Niliona wazi kuwa ile simu ilikuwa imewekwa pale kusudi, kama jinsi lile ua lilivyosogezwa kusudi kwenye kona ya chumba kile na si kwa bahati mbaya; kwani kwa uharibifu uliofanywa mle ndani, ningetarajia na lile ua nalo lingekuwa limesambaratishwa vibaya sana.
Niliitupa kitandani ile simu na muda huo huo ikaacha kuita. Haraka niliinua ile meza iliyokuwa imelalia ubavu mle ndani na kuisimamisha usawa wa feni kubwa lililokuwa likining’inia kwenye dari la mle ndani. Nilikimbilia kule lilipokuwapo kabati la nguo, lakini nilijikwaa kwenye mabegi yangu na kupiga mwereka mzito mle ndani. Nilitoa tusi kubwa na kuinuka, nikachomoa droo ya kabati lile na wakati huo huo ile simu ikaanza kuita tena. Nilirudi na lile droo kubwa la kabati na kulilaza juu ya ile meza. Niliparamia na kusimama juu ya ile droo iliyokuwa juu ya ile meza na kupeleka mikono yangu kwenye moja ya panga tatu za ile feni na kuipapasa sehemu ya mgongo wake iliyokuwa imeelekea kwenye dari.
Hamna kitu.
Niliizungusha kidogo ile feni na kupapasa pangaboi jingine. Nako hali ikawa kama ile ya mwanzo na nikahisi kitu kikiuchoma moyo wangu na hofu ikanijaa. Niliizungusha tena ile feni na kukamata pangaboi la tatu la ile feni na kupapasa mgongo wake taratibu.
Vidole vyangu vilipapasa kitu nilichokitarajia.
Huku nikishusha pumzi ya faraja, niliushika ule mkanda mdogo wa video uliokuwa umeshikiliwa kwenye mgongo wa lile pangaboi kwa utepe wa gundi na kuibandua kutoka kwenye lile pangaboi.
Niliteremka na kuuweka ule mkanda ndani ya sidiria yangu, nikanyakua begi langu na kutoka haraka nje ya chumba kile nikiiacha ile simu ikiendelea kuita

“THE RICKSHAW”
vii.
K
oku alinijia juu vibaya sana. Aliponiona tu nimeingia ofisini kwake pale katika hospitali ya wilaya ya Temeke, aliangaza macho huku na huko, kisha aliinuka upesi, akachukua koti jeupe la manesi lililokuwa likining’inia nyuma ya mlango na kunitupia huku akiwa amekunja uso kwa hasira.
“Vaa hilo koti, upesi!” Aliniambia huku akiwa amekasirika. Nilishangaa, lakini nilifanya kama alivyoniagiza, huku naye akiukwapua mtandio mweusi niliokuwa nimejitanda kichwani mwangu, kisha akanishika mkono na kuniongozea maeneo ya vyoo vya wanawake, wote tukiwa tumevaa yale makoti meupe wanayovaa wahudumu wa hospitali yaliyofika hadi chini kidogo ya magoti, mimi nikiwa na ile miwani yangu ya jua usoni. Kando ya vyoo vya wanawake kulikuwa kuna chumba kimoja kidogo ambacho baadaye nilielewa kuwa kilikuwa kunatumika na manesi wa kike kubadilishia nguo.
Koku aliniingiza ndani ya chumba kile na kufunga mlango kwa ufunguo.
“What the matter with you Tigga, eenh? Kwa nini umekuja hapa? Hujui kuwa unajihatarishia maisha yako! Mi’ n’lidhani wewe ni smart kumbe bwege namna hii? Umekuja kufanya nini hapa? Ondoka! Tena ondoka upesi!” Alinikemea mfululizo kwa sauti kali ya kunong’ona huku nikiona kuwa alikuwa amechukia vibaya sana.
Nilibaki nikimkodolea macho dada yangu nisipate la kumweleza kwa wakati ule. Nilipotoka mbio kule Kigamboni, wazo lililonijia ni kwenda moja kwa moja hadi kazini kwa dada yangu. Sijui ni nini hasa kilichonipeleka kule, lakini nadhani nilihitaji sana kuonana na mtu yeyote kutoka kwenye jamii yangu, na sikuweza tena kwenda nyumbani kwa mama yangu. Pia nilihitaji msaada wa pesa kutoka kwake.
“Nilihitaji kukuona Koku! Nimekutwa na matatizo makubwa na nimekuwa nikikimbia na kujificha peke yangu kwa muda mrefu...”
“Na hilo ndio jambo la busara zaidi kwako!” Koku alinikatisha kwa ukali.
“Najua! Vipi mama, yu hali gani?”
“Ah! Yuko salama.Hajambo. Lakini amelichukulia vibaya sana swala lako.Linamuumiza.”
Nilimtazama dada yangu yule, na machozi yalinilengalenga usoni. Koku alikuwa akijitahidi kujikaza asiangue kilio na alipokuwa akinikemea niliona midomo ilikuwa ikimcheza. Tulibaki tukitazamana, kisha akanivuta na kunikumbatia kwa nguvu.
“Oooh! Tigga, pole sana mdogo wangu. Nimekuwa nikikuogopea sana kwa siku zote hizo ulizokuwa ukihangaika peke yako. Nina hamu sana ya kujua ni kipi kilichokutokea huko porini, lakini hapa mahala si salama kwako.”
“Ina maana unaamini kuwa mimi si mwehu? Siye niliyeua kule msituni?’ Nilimuuliza huku nikijitoa mikononi mwake na nikipangusa machozi. Koku alinitazama kwa huzuni kwa muda kabla ya kunijibu.
“Sio siri mdogo wangu, kwanza niliamini kabisa kuwa ulikuwa umefanya hayo mambo ya ajabu. Dr. Lundi ni mtu mwenye uwezo mkubwa wa kujieleza na akaaminika, lakini baadaye nikaja kuelewa kuwa wale si watu wazuri pale walipoanza kunihoji juu yako. Maswali waliyouliza...”
“Maswali gani?”
“Ah! Walianza kuuliza maswali ambayo nilidhani wao kama madaktari hawakutakiwa kuuliza. Maswali ambayo yangetakiwa yaulizwe na polisi.Maswali kuhusu mkanda wa video, jinsi nilivyokuelewa tabia zako, marafiki zako...lakini...lakini zaidi ya hapo ni baada ya kuongea na Kelvin...yeye ndiye aliyenihakikishia kuwa wale ni watu wabaya.”
”Kelvin? You talked to Kelvin?” Nilimuuliza kwa hamasa, nikaendelea,”Yu hali gani sasa?”
“Niliongea naye siku kadhaa baada ya lile tukio la pale nyumbani kwake, na hapo ni baada ya Dr. Lundi kuja kututembelea nyumbani na kutueleza juu ya habari zako. Baadaye nilipata habari za masahibu yaliyomkuta Kelvin na nikaenda kumtembelea hospitali ya Muhimbili. Akanieleza kila kitu, japo kwa taabu....”
“Ameumia sana?”
“Risasi ilimpata kifuani upande wa kulia, ikatokea mgongoni, na ndio salama yake, kwani ingeingilia upande wa kushoto tungezika.” Koku aliniambia lakini bado alionekana na wasiwasi mkubwa.
“Maskini Kelvin...sasa anaendeleaje?”
“Nilipoenda kumuona alikuwa na hali mbaya, lakini alijitahidi sana kunielezea yaliyomkuta na ndipo nilipoelewa kuwa Martin Lundi ni mtu mbaya na kwamba yote aliyotueleza juu yako ni uongo. Siku iliyofuatia tu hali yake ilibadilika ghafla, na sasa yuko chumba cha wagonjwa mahututi na hawezi hata kuongea, ni ajabu kabisa. Nilipoenda tena kumtembelea, Kelvin alishindwa kabisa kuongea, ila aliniashiria nimpe kalamu na karatasi, na nilipompa, kwa mkono uliotetemeka vibaya sana aliniandikia kitu ambacho kilinitisha sana, na kilifanya nisiende tena kumwona pale hospitali mpaka leo.” Koku alinieleza kwa kunong’ona nami nilipata msisimko mpya na moyo ukaanza kunipiga kwa nguvu.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA ISHIRINI NA TATU.

“Nilipoenda kumuona alikuwa na hali mbaya, lakini alijitahidi sana kunielezea yaliyomkuta na ndipo nilipoelewa kuwa Martin Lundi ni mtu mbaya na kwamba yote aliyotueleza juu yako ni uongo. Siku iliyofuatia tu hali yake ilibadilika ghafla, na sasa yuko chumba cha wagonjwa mahututi na hawezi hata kuongea, ni ajabu kabisa. Nilipoenda tena kumtembelea, Kelvin alishindwa kabisa kuongea, ila aliniashiria nimpe kalamu na karatasi, na nilipompa, kwa mkono uliotetemeka vibaya sana aliniandikia kitu ambacho kilinitisha sana, na kilifanya nisiende tena kumwona pale hospitali mpaka leo.” Koku alinieleza kwa kunong’ona nami nilipata msisimko mpya na moyo ukaanza kunipiga kwa nguvu.
“Alikuandikia nini Koku?” Nilimuuliza kwa jazba.
“Dr. Lundi. Ondoka upesi’!” Koku alinijibu.
Nilibaki mdomo wazi. “Yaani hayo ndio maneno aliyokuandikia?” Nilimuuliza.
Koku aliafiki kwa kichwa huku akizidi kuonesha wasiwasi mkubwa.
“Mungu wangu! Ina maana...”
“Nadhani Dr. Lundi alimfanya kitu kibaya Kelvin pale hospitali Tigga. Nadhani kuna sindano au dawa fulani amempa...inamuua Kelvin taratibu Tigga.” Koku aliniambia kwa huzuni kubwa.
Nilibaki hoi. Niliegemea ukuta na kujishika paji la uso. Akilini mwangu nilikumbuka wakati yule mtu aliyejiita Martin Lundi akipokea sindano kutoka kwa mmoja wa vibaraka wake kule katika ofisi ya mkuu wa wilaya na kujitia kuangalia kiwango cha dawa kilichowekwa ndani ya bomba la ile sindano.
Mungu wangu! Haya ni mambo gani sasa?
Lakini ilileta maana. Kama Kelvin ataishi na kuelezea juu ya tukio zima la kule nyumbani kwake siku ile, ingenitoa kabisa kwenye hizi shutuma za uongo, na wakati huo huo ingemuweka yule mtu anayejiita Dr. Lundi katika wakati mgumu.
“Kwa hiyo ni nini kilifuatia baada ya hapo?”
“Baada ya hapo ndio sijaenda tena kwa Kelvin, lakini akina Lundi walianza kunifuata fuata sana hadi hapa kazini, wakitaka kujua iwapo niliogea lolote na Kelvin. Niliwaeleza kuwa Kelvin hakuweza kuongea lolote na mimi, lakini naona hawakuniamini.” Koku alinijibu.
Hii kali. Sasa na dada yangu tena ametiwa katika mkumbo?
Nilimuuliza iwapo alimuelezea mama juu ya mambo haya, Koku akaniambia kuwa hakumueleza mama kabisa, kwa sababu mama alionekana kumuamini sana Martin Lundi, hivyo aliamua kumuacha hivyo hivyo.”
“Umefanya vizuri sana.”
“Na wewe umefanya kosa kubwa sana kuja hapa. Inabidi uondoke upesi sana.” Koku aliniambia kwa wasiwasi.
“Kwani bado wanaendelea kukufuata mpaka sasa?” Nilimuuliza. Koku alinishika mabega na kunitazama usoni kwa macho ya kuomboleza.
“Huelewi Tigga. Hawa watu wamo humu hospitalini!”
”Say Whaat?”
“Ndio Tigga. Watu wapya wamekuwa wakiletwa hapa ofisini kufanya kazi, na mmoja amewekwa moja kwa moja pale kwenye kitengo changu. Yaani kama leo ungewahi kufika kidogo tu ungemkuta na sijui ingekuwaje Tigga. Ondoka na usije tena hapa!” Koku aliniambia kwa jazba. Niliogopa kupita kiasi, na lile jambo nililiona haliwezekani.
“Sasa...sasa unajuaje kuwa ni miongoni mwao?” Nilimuuliza. Koku alitikisa kichwa kwa masikitiko na kukata tamaa.
“Yule mtu sio nesi Tigga. Hajui lolote juu ya unesi, kazi yake kukaa tu pale na kupokea simu, can you believe that? Jamaa kazi yake ni kupokea simu tu! Sasa pale kwangu ni ofisi ya maopareta pale?”
Nilikubaliana na Koku, huku kwa mara nyingine nikikubali kichwani mwangu kuwa hakika ule mtandao wa Dr. Martin Lundi ulikuwa mkali na ulizidi kunizingira. Lazima niondoke haraka iwezekanavyo. Kabla sijaongea neno lolote, Koku aliendelea kunipasha habari.
“Halafu na polisi nao wakaja na maswali juu yako.” Koku aliniambia kwa upole. Niliinua uso wangu na kumtazama kwa uso uliojaa maswali. Akili yangu ikienda kwa yule mwanadada askari aliyekichambua chumba changu kwa vurugu kubwa kule kwenye ile nyumba ya wageni muda mfupi tu uliopita, akitafuta mkanda wa video wenye ushahidi wa kumuangamiza Martin Lundi na wenzake.
“Na wao wako upande wa Martin Lundi.” Nilijibu kwa masikitiko huku nikitikisa kichwa.
“Hapana. Huyu aliyekuja ni polisi hasa, tena anaonekana wa ngazi ya juu tu, kutokana na mavazi yake. Na jinsi wale askari alioongozana nao walivyoonekana kumgwaya.”
Hapo nikawa makini sana.
“Yukoje huyo askari?” Nilimuuliza. Koku alimuelezea haraka haraka yule askari aliyemjia na maswali juu yangu, na aliposema kuwa alikuwa amekata ndevu zake katika mtindo wa Timberland, nilipata uhakika kuwa alikuwa ni yule askari niliyemtoroka pale ofisini kwangu, katika jumba la makumbusho.
“Alitaka nini?” Nilimuuliza.
Koku akaniambia kuwa yule askari aliwataka yeye na mama yangu waende kuutambua mwili wa mtu ambaye aliuawa akijaribu kunitorosha mimi kutoka mikononi mwa polisi, iwapo waliwahi kuniona naye mtu huyo wakati wowote hapo nyuma na katika mazingira gani.
“Mlienda? Mlimuona huyo mtu?” Niliuliza huku moyo ukinipiga sana, nikijua kuwa huyo mtu aliyetakiwa akatambuliwe alikuwa ni yule jambazi niliyempachika jina la Macho ya Nyoka.
“Tulipelekwa mpaka mochuari Muhimbili. Na tukamuona huyo mtu. Ni jambazi hasa, Tigga! Yaani hata katika kifo, unaona kabisa kuwa yule mtu alikuwa muuaji! Yale macho! Mama hakulala.”
“Kwa hiyo mlinuona kwa macho yenu kuwa amekufa?”
“Mimi ni nesi Tigga, na najua mtu akifa anakuwaje. Yule mtu alikuwa amekufa! Of course tulimwambia yule askari kuwa hatujawahi kukuona ukiwa na mtu yule hata siku moja, nasi hatukuwa tumepata kumwona yule mtu kabla ya pale kwenye sanduku la barafu la mochuari.”
“Kumbe kweli Macho ya Nyoka amekufa!” Nilijisemea mwenyewe kwa sauti, na Koku alinikazia macho.
“Unamjua yule mtu?”
“Hapana, ila nilikutana naye muda mfupi kabla yule askari hajamuua. Ni mfuasi wa Martin Lundi, na nilimuona kwa macho yangu akiua mtu kule msituni Koku. Ni mtu mbaya sana yule, bora alivyokufa.”
“Mungu wangu, Tigga!” Koku alistaajabia taarifa ile.
“Kwa hiyo yule askari akachukua hatua gani baada ya hapo?” Nilimuuliza. Koku aliguna kabla ya kunijibu.
“Achukue hatua gani nasi tulishamwambia kuwa yule mtu hatujawahi kumuona hata siku moja? Alichofanya ni kutueleza kuwa muda wowote utakapowasiliana na sisi tumjulishe, na tukushauri ujisalimishe. Akatuachia kadi yake yenye namba zake za simu ili tuwasiliane muda wowote tutakapopata habari kuhusu wewe.”
“Ooo? Kwa hiyo unadhani ni bora nijisalimishe? Au utamjulisha huyo askari kuwa nilikuja kuwasiliana na wewe?” Nilimuuliza dada yangu. Kauli yangu ilionekana kumuumiza sana.
“Wewe ni mdogo wangu Tigga. Najua mambo mengi yanayosemwa juu yako si ya kweli, na nilimueleza hata yule askari, pamoja na zile habari nilizozipata kutoka kwa Kelvin. Lakini siwezi kukusaliti hata kama ungekuwa umefanya hayo mambo. Lakini nadhani ni bora ujisalimishe Tigga, na katika kufanya hivyo inabidi uwe makini sana unajisalimisha kwa nani. Nadhani yule askari ni mtu safi...anaonekana ana uelewa fulani.” Koku alinieleza kwa kirefu. Niliyatafakari yale maneno ya Koku kwa muda. lngawa nilikubaliana kabisa na ushauri wake, bado nilikuwa na tatizo la kujua ni yupi hasa askari wa kumuendea. Je yule afisa aliyemuua Macho ya Nyoka alielekea kuwa muafaka? Sikuweza kupitisha uamuzi wowote kwa wakati ule, lakini hata mimi nilidhani kuwa labda ningeanza na yule askari katika kutafuta msaada wa kuaminika juu ya swala hili.
Tulibaki kimya kwa muda, kisha nikamwambia Koku shida yangu.
“Koku, nahitaji pesa. Unaweza kunipatia kiasi chochote? Nimeishiwa...” Nilimwambia dada yangu. Aliniambia nimsubiri mle mle ndani akanitazamie kwenye pochi yake pale ofisini kwake, kwenye kitengo cha madawa. Alitoka na kurudi muda mfupi baadaye akiwa amebeba maboksi matupu ambayo bila shaka yalikuwa yamewekewa chupa za dawa mbali mbali. Alinikabidhi kiasi cha pesa akiwa amekifumbata mkononi mwake, nami nilizipokea bila kuzihesabu na kuzishindilia mfukoni mwangu.
“Hiyo ni shilingi elfu hamsini. Samahani sina zaidi ya hapo.” Aliniambia. Nilimshukuru sana na kumwahidi kumlipa iwapo nitatoka salama katika msukosuko ulionikabili. Aliniambia nisijali na kunieleza kuwa yule mtu aliyekuwa akifanya kazi ya kupokea simu pale ofisini kwake ambaye alimhisi kuwa ni mfuasi wa Martin Lundi alikuwa amerudi. Hakukuwa na njia nyingine zaidi ya kutokea nje ya jengo lile isipokuwa kupita pale mbele ya dirisha la ofisi ya Koku. Koku alinibebesha yale maboksi, akitumbukiza lile begi langu ndani ya boksi moja na kuniambia kuwa nitoke nje nikiwa nimebeba yale maboksi na kuyatumia kuficha uso wangu nikipita mbele ya ofisi yake, labda nitafanikiwa kumpita yule mtu bila kutambulika, hasa kutokana na lile koti jeupe nililovaa juu ya nguo zangu. Nilimshukuru dada yangu kwa mara nyingine tena, naye alinikumbatia tena na kuniambia kuwa amefurahi kuniona hata hivyo.
Nikiwa nimebeba yale maboksi kama mmoja wa manesi wa hospitali ile, nilitembea haraka kuelekea nje ya jengo lile huku nikificha uso wangu nyuma ya yale maboksi. Nilipopita kwenye dirisha la ofisi ya Koku, nilichungulia juu ya uzio wa maboksi niliyokuwa nimeyabeba na kuzungusha macho yangu yaliyofichwa na ile miwani ya jua niliyovaa kuelekea ule upande ambao nilidhani ningeweza kumuona huyo mtu anayekaa kwa kazi ya kupokea simu tu mle ofisini kwa dada yangu.
Koku alikuwa sahihi.
Yule mtu alikuwa ni mmoja wa wale vibaraka wawili wa Martin Lundi alioniibukia nao kule ofisini kwa mkuu wa wilaya.
Nilitoka nje ya jengo huku nikiwa na woga mkubwa, lakini yule mtu hakunitambua wala hakunitilia shaka. Niliyatupa yale maboksi kando ya mapipa ya taka, huku nikitoa begi langu kutoka ndani ya moja yale maboksi. Nyuma ya jengo lile nililivua lile koti jeupe nililovaa juu ya nguo zangu na kulitupa nyuma ya maua.
Niliangaza kulia na kushoto, kabla ya kuvuka barabara na kutoweka eneo lile huku nikijifariji kuwa angalau nilikuwa nimepata mwanzo mzuri, kwani nilikuwa nimepata taarifa za muhimu sana kutoka kwa dada yangu Koku.
--
Saa yangu iliniambia kuwa muda ulikuwa ni saa sita na robo mchana. Nilisimamisha teksi na kumuelekeza dereva anipeleke Kijitonyama, nyumbani kwa aliyekuwa rafiki yangu Aulelia Mushi. Kwa kadiri nilivyoelewa, Aulelia bado alikuwa hajaolewa na alikuwa akiishi peke yake na msichana wa kazi tu. Aulelia alikuwa na tabia ya kurudi nyumbani kula chakula cha mchana na kurudi tena kazini. Nilitaka nimkabili ili nijue nini kiini cha tabia yake ya ajabu, na huenda kwa kufanya hivyo ningepata mwanga mwingine kuhusu wale watu wabaya wanaoniwinda.
Nilimkuta msichana wake wa kazi ambaye alinikaribisha kwa mashaka huku akinieleza kuwa tajiri yake amemzuia kukaribisha wageni asiowajua. Huyu alikuwa msaidizi tofauti na yule niliyemjua mimi, lakini kwa hapa jijini wasaidizi wa ndani huwa wanabadilika kila mara.Nilimwambia mimi ni dada ya tajiri yake na kwamba nimewasiliana naye kwa simu na kuwa yuko njiani anakuja. Nilikaribishwa sebuleni na kuketi nikisubiri huku moyo ukinipiga kwa nguvu.
“Samahani Aulelia, lakini ni muhimu kwangu kujua ukweli.” Nilinong’ona huku nikisubiri ujio wa Aulelia. Sikusubiri sana, kwani muda si mrefu nilisikia gari ya Aulelia ikisimama nje ya nyumba na Aulelia aliingia ndani huku akimpigia kelele msaidizi wake aende akashushe mizigo kutoka kwenye gari. Nilisimama kutoka kwenye kochi nililokuwa nimekalia na kumtazama. Aulelia alisimama ghafla na uso ulimbadilika mara moja, ukichukua mtazamo wa woga uliochanganyika na chuki kubwa. Tulitazamana.
“Toka nyumbani kwangu Tigga! Toka kabla sijakuitia polisi!” Hatimaye Aulelia alinifokea kwa chuki na ghadhabu. Nilimuinulia viganja vya mikono yangu kumwashiria kuwa sikuwa na silaha yoyote na kwamba sikuwa nikitaka shari.
“Nitaondoka Aulelia, lakini nataka maelezo ya kitendo chako cha kunikana vile mbele ya watu...kumbe unanifahamu kuwa mimi ni Tigga, sasa kwa nini ulisema hunijui?” Nilimuuliza huku nikimsogelea taratibu. Aulelia alinitazama kwa jeuri na kuniinulia kidevu kwa kiburi.
“Hilo ndilo lililokuleta au kuna jingine?” Aliniuliza. Nilimtazama na sikuamini kama ni yeye kweli anaweza kuniongelesha kwa kiburi namna hii.
“Aulelia! Ni nini lakini kinatokea? Mimi nimekutwa na matatizo makubwa sana rafiki yangu. Nimeshuhudia maiti za wenzangu zikiwa zimetawanywa kama mizoga ya wadudu tu huko porini, nimekuja hapa mjini kila mtu ananigeuka, kuanzia Kelvin hadi mama yangu....hadi wewe! Sijui ni nini kinatokea...”
“Kwa hiyo umekuja kunimalizia na mimi? Unataka kutafuna moyo wangu na kunywa damu yangu? Ndicho kilichokuleta?”
Nilishangaa.
“Nini? Mbona sikuelewi Aulelia? Ni vitu gani hivyo unaniambia?”
“Habari zako zote ninazo Tigga, na nakuhakikishia kuwa mimi hutanipata kirahisi...tutapambana!” Na baada ya kusema hivyo Aulelia aliruka kwa wepesi wa ajabu na kuchukua kisu kikubwa kilichokuwa kwenye kabati la vyombo lililokuwa pale sebuleni. Nilishangaa, lakini akili ilianza kufanya kazi haraka haraka. Aulelia alinijia akiwa na kisu mkononi. “Ondoka upesi nyumbani kwangu Tigga, Ondoka na usirudi tena!”
“Sitaondoka bila majibu Aulelia! Kama utaniua kwa hicho kisu basi uniue tu, lakini mimi sikuja kwa shari kwa sababu ushari si fani yangu, nawe unajua hilo.” Nilimwambia huku nikiwa bado nimemuinulia viganya vyangu na nikimsogelea. Aulelia aliduwaa kwa hatua yangu hii, kwani bila shaka alitaraji ningemjia juu na kujaribu kupambana naye.
“Tigga n’takuchoma kisu! Toka tafadhali...!”
“Nichome tu Aulelia! Mimi nimekikwepa kifo mara kadhaa tangu nikutwe na mkasa huu unaouendeleza hapa. Lakini huko nilifanikiwa kukikwepa kifo kwa sababu nilikuwa najua kuwa nilikuwa napambana na adui. Lakini wewe sio adui yangu Aulelia, wewe ni rafiki yangu. Natarajia msaada kutoka kwako na sio mapambano. Kwa hiyo kama unadhani kunichoma kisu ni salama zaidi kwangu Aulelia, nichome tu. Lakini mimi ninachotaka ni majibu tu kutoka kwako.” Nilimwambia kwa utaratibu huku nikizidi kumsogelea.Aulelia hakulitegemea hili na nikaona akitetereka katika msimamo wake na machozi yakimlengalenga.
“Umeongea na mtu anayejiita Dr. Martin Lundi?” Nilimuuliza kwa upole. Aulelia aliafiki kwa kichwa, na kutazama pembeni.
“Akakuambia kuwa mimi nina wazimu...Paranoid Schizophrenia?” Aulelia aliafiki tena kwa kichwa na akaketi kwenye kiti, akiachia kisu chake kikianguka sakafuni. Nami niliketi kando yake huku moyo ukinipiga. “Ulimuamini Aulelia? Uliamini kuwa mimi nina wazimu?”
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA ISHIRINI NA NNE.

“Umeongea na mtu anayejiita Dr. Martin Lundi?” Nilimuuliza kwa upole. Aulelia aliafiki kwa kichwa, na kutazama pembeni.
“Akakuambia kuwa mimi nina wazimu...Paranoid Schizophrenia?” Aulelia aliafiki tena kwa kichwa na akaketi kwenye kiti, akiachia kisu chake kikianguka sakafuni. Nami niliketi kando yake huku moyo ukinipiga. “Ulimuamini Aulelia? Uliamini kuwa mimi nina wazimu?”
“What did you expect Tigga(Ulitegemea nini Tigga)? Yule ni daktari, mtaalamu...ananieleza mambo kama hayo unategemea nitaacha kumuamini?
“Yule sio mtaalamu lolote ni muuaji mkubwa! Nimeshuhudia kwa macho yangu akishirikiana na wenzake wawili kumtesa mtu na hatimaye kumuua!” Nilimkatisha Aulelia kwa jazba. Niliona Aulelia akichanganyikiwa, asijue iwapo aniamini au ndio aamini kuwa kweli mimi ni mwehu, kwani kwake Martin Lundi ni mtaalamu na mimi nasema ni muuaji.
“How could you believe him Aulelia? We’ unanijua mimi!”
“Sikumuamini wala sikumbishia Tigga! Nilichomuambia ni kuwa ni mimi ndiye nitakayeamua iwapo ni kweli Tigga ana wazimu au vinginevyo pale nitakapomuona kwa macho yangu mwenyewe! Ndivyo nilivyomwambia Tigga!” Alinijibu na kutazama pembeni huku akifuta machozi. Na hivyo ndivyo nilivyotegemea Aulelia angelichukulia swala lile.
“Sasa kama ulikuwa na mtazamo huo kwa nini ulinifanya vile pale tulipokutana?” Nilimuuliza.
“Habari zako zilizagaa kwenye magazeti Tigga, na hazikuwa habari nzuri. Halafu nikaanza kupokea meseji za simu...” Aliniambia
“Meseji za simu? What has that got to do with any of this?” Nilimuuliza kwa mshangao na kutoelewa, nikitaka kujua hizo meseji za simu zinahusika vipi na habari zile tulizokuwa tukiziongelea. Aulelia alinitazama kwa muda kisha akageuka pembeni na kutoa simu yake ya kiganjani kutoka kwenye mfuko wa koti lake la suti alilokuwa amevaa. Alibofya bofya kwa muda kwenye ile simu kisha alinikabidhi bila ya kusema neno. Niliipokea ile simu huku nikimtazama kwa macho ya kuuliza, lakini Aulelia aligeuka pembeni.
Niliitazama ile simu nikaona Aulelia alikuwa ameniwekea sehemu iliyoonesha ujumbe mfupi wa simu, nami nikaanza kuusoma. Ulikuwa ni ujumbe mbaya wa vitisho vikali sana, na matusi mazito ya nguoni ambao uliishia hivi:
Nina hamu na damu yako! Najisikia kukuua na kuutafuna moyo wako. Ole wako nikutie mikononi malaya mkubwa we!
Nilishangazwa na ujumbe ule na nikainua uso kumtazama Aulelia, nikaona alikuwa akinitazama kwa makini.
“Aulelia! Ni nini hii? Huu ujumbe umetoka wapi? Unahusu nini? Una ugomvi na huyu mtu? Ni nani huyu?” Nilimuuza lakini alizidi kunitazama kwa muda kisha alinijibu.
“Tazama mtumaji wa hiyo meseji ni nani” Nilimtazama kwa mshangao, lakini nilitekeleza na kwa kihoro kikubwa nikaona kuwa ule ujumbe ulikuwa umetumwa kutoka kwenye simu yangu!
Niliiweka kwenye kochi ile simu na kusimama nikimtazama Aulelia kwa mshangao mkubwa.
“Si..si..sikutuma mimi ujumbe huu!” Nilimwambia huku nikiinyooshea kidole ile simu. Aulelia alizidi kunitazama bila ya kusema neno. “Simu yangu ilipotea kule msituni...na hadi hivi niongeavyo sina simu! Nina hakika akina Martin Lundi waliichukua! Si nilikuambia? Hao ni watu wabaya sana!” Niliendelea kujieleza, lakini Aulelia aliichukua ile simu na kubofya tena kabla hajanikabidhi kwa mara nyingine. Niliipokea huku nikimtazama kwa mashaka na kusoma ujumbe mwingine uliotumwa kwa Aulelia kutoka kwenye simu yangu.
Nimeshaua watu wengi na sasa najisikia kuutafuna moyo wako! Kaa chonjo, nakuja kukumaliza! Changudoa mkubwa we!
Nilichoka! Mara moja nilielewa kuwa ile ilikuwa ni njama ya Dokta Lundi ya kutaka kunifarakanisha na watu wangu wa karibu ambao walielekea kuniamini. Na bila shaka yoyote nilielewa sababu ya Aulelia kufanya mambo aliyofanya siku ile nilipokutana naye pale katikati ya jiji. Machozi yalinibubujika bila kituo huku nikitikisa kichwa kwa masikitiko.
“Pole sana Aulelia, lakini mimi siye niliyetuma hizi meseji rafiki yangu. Why should I ? Ni wazi hii ni mbinu ya Dokta Lundi kutaka kunifanya mimi nionekane kichaa kwako!” Nilimwambia rafiki yangu huku nikitokwa na machozi.
“Ni kweli Tigga. Niliamini kuwa umepata wazimu baada ya kuanza kupata hizo meseji kutoka kwako...lakini nadhani sasa naelewa kilichotokea. Kama unachosema ni kweli...”
“Tangu lini nikaanza tabia ya uongo? Ninachokuambia ni kweli. Hawa watu wanataka kunichafua ili kila mtu apoteze imani na mimi...wewe ulitumiwa hizi meseji ili uamini kuwa mimi ni mwehu na upoteze kabisa imani na mimi! “
Aulelia aliniambia kuwa zile meseji zilikaribia kumtia yeye wazimu. Mara nyingine alikuwa akipigiwa simu usiku wa manane kwa ile simu yangu na akipokea hakuna anayeongea. Akanionesha ujumbe mwingine ambao ndio ulionichanganya zaidi.
Unatembea na mchumba wangu. Sasa nimegundua. Nimemuanza yeye halafu nakujia wewe! Nitainywa damu yako bila kuichemsha, Kimburu we!
Nilibaki mdomo wazi.
“Siku iliyofuata nilipata habari za mkasa uliomkuta Kelvin pale nyumbani kwake. Nilichanganyikiwa!” Aulelia aliniambia kwa huzuni.
Sikuwa na la kusema. Angalau nilikuwa nimeelewa ni nini kilichotokea kwa rafiki yangu Aulelia. Nilijenga chuki kubwa kwa yule mtu aliyejiita Martin Lundi, kwani mambo aliyokuwa akinifanyia yalikuwa hayavumiliki.
Tulikumbatiana na rafiki yangu Aulelia na kuombana radhi.
Nilimuelezea juu ya mkasa ulionikuta kule msituni kwa ufupi sana.Ingawa aliniomba sana niendelee kujificha pale kwake mpaka hapo mambo yatakapopoa, sikukubali. Nilimwambia kuwa ilikuwa ni salama zaidi kwake kama akiendelea kuwa mbali nami kwa kipindi hiki cha matatizo.
Nilichukua begi langu na kuagana na rafiki yangu Aulelia, nikimuacha akibubujikwa na machozi. Angalau nilikuwa nimefumbua ukweli fulani katika kitendawili hiki kilichonizunguka.

--

Nilikutana na Kachiki kwa bahati mbaya sana. Na nilipokutana naye sikuwa na hata chembe ya wazo kuwa yeye ndiye ambaye angenifunua macho kuhusu kile kitendawili cha pili nilichoachiwa na Mr.Q, The Rickshaw.
Niliondoka nyumbani kwa Aulelia pale Kijitonyama nikiwa mwingi wa furaha kuwa angalau nilikuwa nimefanikiwa kuzishinda fitna za Dokta Martin Lundi na kurudisha maelewano mazuri na rafiki yangu Aulelia. Aidha, nilikuwa nimefanikiwa kugundua njia aliyotumia yule mtu muongo,mfitinishaji na muuaji katika kunifarakanisha na watu wangu wa karibu, kama Aulelia.
Ndio maana walichukua simu yangu kule msituni!
Nilipanda basi la Kariakoo kutokea Mwenge nikiwa na nia ya kutafuta hoteli itakayoniridhisha katikati ya jiji na kuanza kupanga mikakati mipya ya kukabiliana na akina Martin Lundi, nikiwa na nia ya kutafuta namna ya kujisalimisha kwenye vyombo vya dola nikiwa na ule ushahidi wangu. Nilidhani kuwa kufikia sasa wale wabaya wangu walishajua kuwa huwa najificha kwenye nyumba za wageni zilizojiegesha nje kabisa ya jiji. Sasa mimi niliamua kuhamia kwenye hoteli na katikati ya jiji. Swala la pesa bado lilikuwa kikwazo, kwani nilijua elfu hamsini nilizoongezewa na dada yangu Koku, zingetosha kwa malazi ya siku nne tu hotelini. Nikiongezea na pesa zangu zilizobakia, labda ningeweza kuishi kwa siku tano zaidi. Baada ya hapo nisingekuwa na ujanja.
Lakini bado nilikuwa na jukumu la kukamilisha kazi niliyoachiwa na Mr. Q, na siwezi kuishi vema na nafsi yangu kama sijawafikisha kwenye mikono ya sheria wale wauaji wengine waliomfikisha yule mtu kwenye mauti dhalili kama yale kule msituni. Mauti yasiyo na maziko ya kueleweka na bila jamaa zake kujua kuwa amefikwa na mauti.
Hivyo nilikuwa naomba Mungu anisaidie katika wiki mbili ambazo nitaweza kuishi hotelini niwe nimetimiza azma yangu ya kumlipizia kisasi yule mtu na kuwafikisha kwenye sheria akina Martin Lundi.
Labda kufikia muda huo nitakuwa nimeshawasambaratisha akina Martin Lundi, au nikawa nimepata namna ya kujisalimisha kwenye mikono halali ya sheria na kuukabidhi ule mkanda wenye ushahidi katika mikono salama.
Lakini nitaweza?
Nikiwa nimezama kwenye mawazo yangu haya, ndipo niliposhitushwa na kelele za mabishano ndani ya daladala baina ya kondakta na dada mmoja aliyekuwa akidai kuwa ameibiwa pesa zake na hivyo hakuwa na nauli. Kutokana na mavazi yake yaliyoleta hisia kuwa alikuwa changudoa, hata abiria waliokuwamo mle ndani walianza kumshutumu na kumtetea kondakta kiasi yule dada alianza kuangua kilio. Basi nilijitolea kumlipia na safari ikaendelea kwa amani. Lakini nilipoteremka Kariakoo, yule dada alinifuata tena na kuniomba nimsaidie mia hamsini nyingine ili aendelee na safari yake ya Gongo la Mboto, kwani ni kweli kuwa alikuwa ameibiwa pesa zake zote.
Nikiwa na mashaka kuwa huenda yule dada alikuwa ni changudoa tu wa mjini anayetaka kunifanya bwege kwa kujitolea kwangu kumlipia nauli hapo mwanzo, nilianza kumhoji juu ya safari yake huku nikiendelea kutembea kuelekea kwenye maeneo niliyohisi yanaweza kuwa na hoteli ilhali yule dada akinifuata.
Ni hapo ndipo nilipogundua kuwa alikuwa anaitwa Kachiki, na kwamba alikuwa akifanya kazi ya uhudumu katika baa moja iliyoitwa Uno Trabajo iliyoko maeneo ya Gongo La Mboto. Nilikumbuka kuwa alipandia basi la Kariakoo maeneo ya Makumbusho, na nilipomuuliza kuwa ndipo alipokuwa akiishi, alinifahamisha kuwa yeye na wenzake wanaofanya kazi katika ile baa huwa wanalala palepale baa kwani mmiliki wa baa ile alikuwa amewajengea vyumba vya kulala, ila alienda kule Makumbusho kumfuatilia mwenzao ambaye aliondoka kazini siku mbili zilizopita na hakurejea, ambapo alipomkuta aligundua kuwa alikuwa ameamua kuacha kazi kienyeji tu kwani alikuwa amepata bwana wa kumweka ndani, kisha akaendelea kulaani tabia ile ya yule mwenzake ya kuamini wanaume wa mpito kiasi cha kuamua kuacha kazi, lakini kufikia hapa nikawa makini sana na ile taarifa yake.
“Mnapewa na malazi hapo hapo?” Nilimuuliza.
“Tena kila mtu na chumba chake bwana! Chakula tunakula hapo hapo, hata ukilipwa mshahara mdogo kuna tatizo gani? Kwa maisha ya hapa mjini Anti mtu ukipata pa kuweka ubavu bila kulipia kodi unataka nini tena zaidi?” Kachiki alisema kwa hamasa, nami nikawa nimeanza kulizungusha lile jambo kichwani mwangu.
Akina Martin Lundi sasa hivi lazima watakuwa wananitafuta kwenye nyumba za wageni, na muda si mrefu msako wao utahamia kwenye mahoteli. Muda si muda watanikamata, kama jinsi walivyoniibukia kule Kigamboni. Na pesa zilikuwa zinaniishia kwa kasi sana. Lakini hata siku moja wale watu wabaya hawatafikiria kunitafuta kwenye mabaa, labda nikutane nao kwa bahati mbaya tu wakiwa kwenye manywaji, jambo ambalo uwezekano wake ni moja kati ya mia moja.
Nilifanikiwa kumshawishi Kachiki anipeleke huko kwenye hiyo baa aliyokuwa akifanyia kazi na aniunganishie hicho kibarua alichokiacha huyo rafiki yake. Alinishangaa kupita kiasi, hakuamini kabisa kuwa mtu kama mimi naweza kuwa na shida ya kibarua tena cha hovyo kama jinsi yeye alivyokiona kama kile. Ilibidi niseme uongo wa kukata na shoka lakini nilifanikiwa, kwani nilimwambia kuwa pale nilikuwa naenda kutafuta nyumba ya wageni nilale kwani nilikuwa nimelaghaiwa na mwanaume aliyeniweka ndani kinyumba baada ya kunitorosha kwetu Kisiju, lakini sasa amepata bibi mwingine na ameamua kunitelekeza kwenye nyumba ya kupanga kwa wiki nzima bila taarifa wala matumizi yoyote. Nikimpigia simu anasema yuko bize. Nikaamua kuondoka lakini baada ya kuuona mji, sikuwa tena na haja ya kurudi kwetu Kisiju.
Kachiki aliipokea ile hadithi yangu ya uongo kwa masikitiko makubwa hasa akiioanisha na lile tukio la yule rafiki yake aliyetoka kumfuatilia kule maeneo ya Makumbusho. Moja kwa moja alikubali kunipeleka kwenye ile baa aliyokuwa akifanyia kazi kuchukua nafasi ya huyo mwenzao aliyeacha kazi kama namna ya yeye kulipa fadhila yangu.
Ingawa kwa wakati ule niliona kuwa ile ilikuwa ni njia ya kujipatia mahala pa kujihifadhi kwa muda na wakati huo huo kujipatia kipato kidogo, lakini umuhimu wa uamuzi wangu wa kumsaidia yule dada na hatimaye kuamua kwenda kuomba kibarua kwenye ile baa aliyokuwa akifanyia kazi nilikuja kuuona baadaye.

--

Uno Trabajo ilikuwa ni baa ya aina yake. Ilikuwa ni vigumu sana kuamini kuwa kule Gongo la Mboto kuliweza kuwa na baa kama ile, kwani ilikuwa katika kiwango cha kimataifa kabisa. Na kama alivyonieleza Kachiki, mmiliki wa ile baa aliwawekea wahudumu wake mazingira mazuri sana ya kazi, kwani pamoja na kuwapatia vyumba vya kulala nyuma ya ile baa, pia aliwapatia mahitaji kama sabuni, dawa za meno na matibabu.
Siku ile ile nilipata kibarua cha uhudumu wa baa kwa mshahara wa shilingi elfu ishirini kwa mwezi pamoja na mahitaji yote hayo muhimu,kwangu la msingi likiwa ni malazi na zile elfu ishirini. Nilipelekwa kwenye chumba changu kidogo lakini kisafi cha kuridhisha tu, kilichokuwa na kitanda kidogo cha futi tatu na mashuka yenye lebo ya ile baa.
Nilijifungia mle chumbani na kuanza kuweka vitu vyangu kwa mpangilio nilioutaka. Nilitoa lile burungutu la pesa nilizopewa na Koku na kuanza kuzipanga vizuri pamoja na pesa nyingine nilizokuwa nazo, na wakati nafanya hivyo niliona kitu kama kadi ndogo ikidondoka kutoka kwenye lile burungutu nililopewa na dada yangu. Niliiokota na kugundua kuwa ilikuwa ni kadi ya anuani, ambayo dada yangu aliifumbata pamoja na zile pesa wakati ananipa nami bila kuangalia nilizishindilia mfukoni mwangu pale hospitali ya wilaya ya Temeke. Niliisoma ile kadi na moyo ulinilipuka na kuanza kunienda mbio kwani ile kadi ilikuwa imeandikwa ifuatavyo:

John Vata
Assistant Commissioner of Police
Special Op.

Chini ya maelezo hayo zilifuatia namba za simu za waya, za kiganjani, anuani ya posta na anuani ya barua pepe. Nilikaa kitandani taratibu huku nikiendelea kuitazama ile kadi bila ya kuamini, nikijua wazi kuwa Koku alikuwa ameniwekea ile kadi makusudi, na kwa maana hiyo, lile jina nililoliona kwenye ile kadi ndilo lilikuwa la yule afisa wa polisi anayekata ndevu katika mtindo wa Timberland.
“Mungu wangu! Kumbe pale ofisini nilikuwa naongea na Kamishna msaidizi wa polisi!”
Nilijisemea mwenyewe na kutazama tena lile jina lililoandikwa kwenye ile kadi.
John Vata.*
 
SEHEMU YA ISHIRINI NA TANO.

Chini ya maelezo hayo zilifuatia namba za simu za waya, za kiganjani, anuani ya posta na anuani ya barua pepe. Nilikaa kitandani taratibu huku nikiendelea kuitazama ile kadi bila ya kuamini, nikijua wazi kuwa Koku alikuwa ameniwekea ile kadi makusudi, na kwa maana hiyo, lile jina nililoliona kwenye ile kadi ndilo lilikuwa la yule afisa wa polisi anayekata ndevu katika mtindo wa Timberland.
“Mungu wangu! Kumbe pale ofisini nilikuwa naongea na Kamishna msaidizi wa polisi!”
Nilijisemea mwenyewe na kutazama tena lile jina lililoandikwa kwenye ile kadi.
John Vata.*
Sikuwa nimepata kulisikia lile jina mahala popote kabla ya pale. Nilijikuta nikitikisa kichwa na kutabasamu nikistaajabia werevu wa dada yangu Koku, kwani nilijua kuwa alikuwa amefanya vile kusudi kwa sababu alitaka nijisalimishe kwa yule askari ambaye alimuona kuwa ni mstaarabu.
Lakini mimi naweza kukuamini John Vata?
Na kwa nini afisa mkubwa kama yule afuatilie swala lile yeye mwenyewe? Mtu mwenye wadhifa kama ule alitakiwa atume vijana wake wafuatilie, kisha yeye aletewe taarifa tu ya maendeleo. Vije aingie yeye mwenyewe kwenye upelelezi na hata kufikia hatua ya kupambana na muuaji kama Macho ya Nyoka namna ile?
Nilifikiria sana juu ya jambo lile, kisha nikapitisha uamuzi.
Baada ya kuweka vitu vyangu katika utaratibu nilioutaka mle ndani, nilitoka na kufunga mlango wa chumba changu kwa nje na kumfuata Kachiki aliyekuwa amejilaza chumbani mwake. Nilimuuliza ni muda gani tulikuwa tunaanza kazi akaniambia kuwa ni saa tisa mchana watu wakianza kutoka maofisini, ingawa kwa muda ule huduma ilikuwa ikitolewa lakini hakukuwa na wateja wengi hivyo tuliweza kupumzika tu na kwamba kuna zamu maalum huwa zinapangwa kwa kuhudumia muda ule wa kabla ya saa tisa. Basi nilitoka nikimuambia kuwa nilikuwa naenda kununua nguo za mitumba kwani niliona kuwa nguo zangu za kushindia zilikuwa haziendani kabisa na mazingira yale.
“Kweli shoga, maanake hizo suti zako na mazingira haya hata si mwake!” Kisha tukacheka nami nikatoka, nikiwa na ule mkanda wangu wa video ndani ya sidiria yangu. Nilienda mpaka Kariakoo, huko nikatafuta kibanda cha simu na kuipiga ile namba ya simu ya kiganjani ya Kamishna Msaidizi wa polisi John Vata na kuisikiliza ikiita huku moyo ukinienda mbio.
“John Vata!” Sauti niliyoikumbuka kuwa ni ya yule afisa wa polisi aliyenikamata pale ofisini kabla ya Macho ya Nyoka kutokea ilipokea ile simu.
“Tigga Mumba!”
Kimya kilitanda kwa muda, nikisikia yule afisa akihema upande wa pili wa ile simu.
“Uko wapi? Nahitaji kuongea na wewe...na ukumbuke kuwa bado uko chini ya ulinzi na...”
“Mimi ndiye niliyekupigia afande hivyo naomba unisikilize!”
“Unatakiwa ujisalimishe ndio uongee hayo unayotaka kuongea, sio kwenye simu namna hii...okay, unasemaje?”
“Niko tayari kujisalimisha afande, lakini nataka kwanza umtafute na umweke chini ya ulinzi mtu aitwaye Martin Lundi...Dokta Martin Lundi. Nitakapothibitisha kuwa huyo mtu
amewekwa chini ya ulinzi mimi nitajitokeza mahala popote utakapotaka, na nitakuja na ushahidi wa kukuonesha kuwa huyo ndiye mtu unayetakiwa umsake na sio mimi. Tena nisikie na nione kwenye vyombo vya habari kuwa amekamatwa...magazeti, redio na televisheni...sio uniletee stori tu kuwa...”
“Tigga...”
“Sikiliza bwana! Sio uniletee habari tu kuwa tayari amekamatwa bila mimi kuona ushahidi wa hilo. Bila hivyo sijitokezi ng’o!”

“Tigga, unafanya kosa kubwa. Ujue sisi hatushindwi kukutia mikononi, ni swala la muda tu. Na ujue kwamba sifanyi kazi kwa kupewa mashinikizo na watu wanaokimbia mikono ya sheria. Lakini nakuhakikishia kuwa hata usipojitokeza, mimi nitaendelea kukuwinda mpaka n’takutia mikononi tu...”
“Na ujue kuwa unaweza kuendelea kuniwinda na kujigamba namna hiyo kwa sababu mimi niliokoa maisha yako kutoka kwenye kifo kilichokuwa mikononi mwa yule muuaji aliyetaka kuniteka pale ofisini kwetu siku ile. Usisahau hilo kabisa!” Nilimjibu kwa hasira. John Vata alikuwa kimya kwa muda na nikahisi alikuwa amechomwa na ukweli wa maneno yangu.
“Sasa utafanya ninavyokuambia au hutafanya?” Nilimuuliza baada ya kuona amekuwa kimya kwa muda mrefu.
“Sitoweza kumkamata Dr. Martin Lundi kwa kusikiliza uzushi wako tu mwanamke, na kama huna la msingi kata simu na usubiri jinsi nitakavyokutia mbaroni!” Alinijibu kwa ile sauti yake ya utulivu mkubwa usioendana kabisa na mazingira ya mjadala ule, kwani pale alitakiwa awe mkali lakini yeye alikuwa mpole sana.
Kama jinsi alivyomjibu Macho ya Nyoka kwa upole wa hali ya juu kabla hajamshambulia kwa teke lililoipangusa bastola kutoka mikononi mwa yule muuaji.
Hapo nilijua kuwa John Vata alikuwa mtu hatari sana kupambana naye kwani anapochukia huwa anakuwa mpole. Nilianza kuogopa.
“Kwa nini unawahi kunishutumu kuwa ninazusha kabla hujafanya uchunguzi?”
“Martin Lundi unayemsema ni daktari bingwa wa magonjwa ya akili wa muda mrefu. Ni mzee wa miaka sabini na tano, na sasa ni mstaafu anayesumbuliwa na maradhi ya kiharusi. Anaishi kwenye nyumba aliyojenga shambani kwake Kibaha, hivyo hawezi kuwa ndiye mtu unayemsema wewe kuwa eti alikuwa na wauaji wengine huko porini, ambaye aliendesha helikopta baada ya mauaji ya kule msituni na kuwa ndiye anayekuwinda kwa nia ya kukuangamiza. Kwa hiyo kata huo upuuzi na ujisalimishe mara moja!”
Nilibaki mdomo wazi. Huyu askari ameyajuaje yote haya nami sijawasilisha maelezo yoyote kwenye vyombo vya dola? Yaani yule mtu sio Martin Lundi?
“We’ binti upo? Sema ulipo ili nije tuonane, sisi wawili tu.Nadhani tunaweza kusaidiana katika hili.”
Bado nilikuwa nimepigwa bumbuwazi.
“Um...Umejuaje yote hayo? Yule mtu sio Martin Lundi? Ina maana na nyie mlikuwa mnajua juu yake? Au na wewe ni mwenzao?”
“Habari zote hizo zilikuwa kwenye maelezo yako uliyoandika kwa muajiri wako pale ofisini. Ulitakiwa na mwajiri wako uandike yale maelezo kwa maelekezo yangu. Na baada ya kupata maelezo yale nilianza kuyafuatilia na ndio nikagundua hayo juu ya huyo Martin Lundi wako uliyemtaja kwenye maelezo yako.”
Nilikata simu.
Nilihisi dunia ikizunguka nami nikizunguka pamoja nayo. This is impossible!
Kwa hakika nilichanganyikiwa.
Nililipa pesa za muda nilioongea na kuondoka eneo lile haraka. Kwa mara nyingine tena Martin Lundi alikuwa amenizidi kete.
Alitumia jina la uongo lakini la mtaalamu wa kweli wa magonjwa ya akili, aliyestaafu kazi muda mrefu.
Ama kwa hakika yule ni Martin Lundi muongo!
Sasa kama Dokta Martin Lundi halisi ni mzee wa miaka sabini na tano na mgonjwa wa kiharusi, yule mtu aliyekuwa kule msituni anayejiita Dokta Martin Lundi ni nani?
Nilitazama saa yangu nikaona saa tisa ilikuwa inakaribia sana, na bado nilikuwa sijanunua hizo nguo nilizodai kuwa naenda kununua. Lakini nilijua nilipanga kulitatua vipi tatizo hilo, hivyo nikakamata teksi na kwa mara ya kwanza tangu niingie jijini kutoka kule Manyoni kilipoanzia hiki kizaazaa, nilimwamrisha dereva anipeleke nyumbani kwangu nilipopanga pale Upanga kwenye nyumba ya msajili.
Nilipanda ngazi kuelekea kwenye nyumba yangu iliyokuwa katika ghorofa ya pili ya jengo lile la msajili huku moyo ukinidunda na nikiwa makini sana. Wengi wa wapangaji wenzangu katika jumba lile walikuwa ni wahindi ambao sikuwa na mazoea nao, hivyo sikuwa na wasiwasi wa ule umbea wa mitaa yetu ya uswahilini, ambapo baada ya habari zangu kutangazwa kwenye redio na magazeti, muda huu ningekuwa natumbuliwa macho ya udaku na bila shaka baadhi ya majirani wangeanza kupiga simu polisi kuwaarifu kuwa nilikuwa nimerudi nyumbani kwangu.
Geti langu lilikuwa limefungwa vilevile kama nilivyoliacha.
Nilipanda kwenye ule mlango wa chuma uliozatiti usalama mbele ya mlango wangu wa mbele na kufungua tungi la kioo lilitakiwa liwe linaifunika taa iliyokuwa mbele ya mlango wangu ambalo ndani yake hakukuwa na taa yoyote hivyo lilibaki limefungwa pale kwenye dari kama urembo tu. Nililitoa lile tungi na kutumbukiza mkono wangu ndani yake nikatoa funguo zangu za nyumba, kisha nikalifunga tena pale kwenye dari.
Hii ilikuwa ni sehemu yangu ya kuficha funguo zangu miaka yote, na zaidi ya dada yangu Koku, hakuna mtu yeyote mwingine aliyeijua. Niliingia na kujifungia kwa ndani. Niliitazama nyumba yangu kwa upendo mkubwa kwani nilikuwa nimeipamba kwa namna nilivyotaka, na ilikuwa vile vile. Bila kupoteza muda nilienda moja kwa moja hadi kwenye runinga yangu iliyokuwapo pale sebuleni na kuigeuza kule nyuma...

--

Baada ya muda niliingia chumbani na kuchagua baadhi ya nguo zangu za kushindia ambazo niliona zingeendana na mazingira ya kule kwenye kibarua changu kipya na kuziweka kwenye mfuko wa nailoni nilioupata mle ndani. Niliiangalia nyumba yangu kwa mara ya mwisho na kufungua mlango ili niondoke,na hapo hapo nilisimama ghafla nikipatwa na mshituko mkubwa.
Nilikuwa natazamana uso kwa uso na yule askari wa kike niliyemtoroka kule kwenye ile nyumba ya wageni ya Kigamboni, safari hii akiwa katika mavazi yake ya kiaskari.
Niliguna kwa mshituko huku mfuko wangu wa nguo ukinidondoka na hapo hapo yule dada alinisukumia ndani kwa nguvu naye akaingia na kuufunga ule mlango kwa ndani.
Nilijiinua taratibu kutoka sakafuni nilipoangukia baada ya kusukumwa na yule dada na kumtazama kwa macho ya woga na wasiwasi mkubwa huku nikijiuliza ni jinsi gani alijua kuwa nitakuwa pale muda ule.
“Unaenda mahali Tigga?” Aliniuliza huku akinisogelea taratibu hali macho yake yakionesha ghadhabu za hali ya juu. Sikuweza kukusanya nguvu za kumjibu.
“Au ulidhani utaweza kutukimbia milele? Tulijua tu kuwa utakuja hapa kwako, kama tulivyojua kuwa ungekwenda kule ofisini kwako...ingawa kule ulitupotezea mwenzetu mmoja lakini bado tuko wengi na ni hatari kuliko hata yule uliyesababisha auawe.” Aliniambia kwa jeuri.
“Toka nyumbani kwangu! Huwezi kunitish-“ Nilianza kumkemea lakini yule dada alinirukia na kunichapa kofi kali la uso lililotawanya maumivu uso mzima. Kabla sijajua nijibu vipi pigo lile alinishindilia ngumi kama nne hivi za haraka haraka zilizotua bila mpangilio kuanzia kichwani hadi tumboni. Nilijibwaga kwenye moja ya masofa yaliyokuwa pale sebuleni nikitweta kwa mapigo yale. Yule dada alinijia kasi na kunikwida shati langu huku akiniinua na kunibamiza ukutani kabla ya kunishindilia ngumi nyingine ya tumbo. Niliguna kwa maumivu na nikahisi fahamu zikinihama. Huku nikiingiwa na wazo iweje mwanamke mwenzangu aninyanyase namna ile.
“Nilikuambia kuwa utajuta Tigga! Sasa wakati ndio umefika-“ Alisema kwa hasira lakini hapo nami nikawa nimezinduka kwani nilimtwanga kichwa cha uso naye akayumba pembeni huku akilalama kwa maumivu na akiniachia. Nilimuendea mbio nikamshindilia teke la tumbo huku nikimtukana naye akajipinda kwa uchungu. Sikuishia hapo, nikamtupia teke jingine lililokuwa linauendea uso wake, lakini alinidaka mguu wangu na kunitupa kwa nguvu nami nikajibwaga sakafuni nikipigiza kichwa changu kwenye upande wa sofa mojawapo mle ndani.
Kabla sijainuka yule askari alinijia na kuniwekea bastola usoni na kunikemea kwa hasira.
“Where is the tape Tigga?”
Badala ya kumjibu nilimtemea mate usoni naye akanichapa kofi kali la uso.Kisha alilichana shati langu kwa hasira kiasi cha kuniacha nikiwa na sidiria tu, na kutumia kipande cha shati langu kujifutia yale mate.
“Usinichezee mimi wewe! Lete huo mkanda!”
“Kwani kule gesti mlipochana chana mito na kuvuruga chumba kizima hamkuupata?” Nilimuuliza kwa jeuri. Akanipiga kichwani kwa kitako cha ile bastola yake na nikahisi maumivu makali.
“Na bahati yako hukuichukua ile simu tuliyokuachia kule gesti, kwani ungeichukua tungeweza kukufuata kila ulipoenda kwa kutumia mionzi maalum tuliyoitegesha kwenye ile simu.” (Akasonya).
“Hivi nyie mnadhani mimi ni mwehu kweli kama mlivyonipakazia?” Nilimuuliza kwa kujitutumua huku moyoni nikistaajabia jinsi wale watu walivyokuwa makini na maovu yao.
“Usilete ujeuri usio na msingi Tigga, nipe huo mkanda sasa hivi!”
“Nilishawaambia kuwa mkanda uko kwa wakili wangu! Kwa hiyo mimi mkanda sina jamani mbona mnanisumbua hivi?” Nilimuuliza kwa jazba. Alinichapa kofi jingine kali sana.
“Wacha uongo!”
“Sasa si uniue tu basi halafu uone jinsi mkanda utakavyooneshwa kwenye vyombo vya habari na wakili wangu?”
Yule dada alichanganyikiwa, alinitazama kwa hasira halafu akatazama pembeni. Nilimtazama kwa makini, nikaona kuwa kushindwa kwake kuupata ule mkanda kulikuwa kunamchanganya sana. Alinigeukia kwa hasira na kuanza kunipekua mwilini, akiutafuta ule mkanda. Alichana chana nguo zangu kwa hasira hadi ile sidiria yangu na kuniacha matiti nje.
Mkanda haukuwepo.
“Sasa hii ndio nini lakini wewe? Hivi ni kipengele gani cha neno ‘sina mkanda’ ambacho kinakuwia vigumu kuelewa?” Nilimuuliza huku nikishindana naye katika kunipekua kwake. Nilipoona hanisikii nilimpiga kofi la uso na alinisukumia kwenye sofa lilikuwapo pale sebuleni na kunibana juu ya sofa lile huku akiniwekea mdomo wa ile bastola yake usoni na kunitazama kwa macho makali na ya hasira huku akihema kwa ghadhabu. Kwa mara nyingine niliona kuwa yule dada alikuwa tayari kunilipua kwa ile bastola kama si kuhofia kuukosa kabisa ule mkanda wa video anaoutaka kwa kila hali. Yaani kwake kama kwamba kuupata ule mkanda lilikuwa ni jukumu binafsi.
Kwa nini?
“Hivi ilikuwaje hata askari mzuri kama wewe ukajihusisha na watu wabaya kama wale lakini?” Nilimuuliza yule dada nikiwa nimebanwa pale kwenye sofa.
“Si kazi yako kujua! Toa huo mkanda Tigga ama si hivyo mi’ n’takuua kweli!”
“Huwezi kuniua wewe!” Nilimbishia kwa jeuri huku nikimtazama usoni. Alianza kunisemesha kitu lakini hapo hapo nilijiinua kwa nguvu na kumsukumiza pembeni nami niliukikimbilia mlango ili nitoke mbio nimuache mle ndani, lakini alinirukia na kunidaka miguu na wote tukapiga mwereka mzito. Alinibana pale sakafuni na kuirudisha bastola yake kwenye mkoba wake uliokuwa ukining’inia kiunoni na kuanza kunishindilia mangumi na makofi mengi huku akinitukana na kunikemea kuwa alikuwa anautaka ule mkanda. Nilijitahidi kupambana naye lakini alinielemea vibaya sana na nikahisi nguvu zikiniishia.Nilijitutumua kwa nguvu zangu zote na kufanikiwa kumbwaga pembeni nami nikajiinua kujaribu kukimbia lakini alinirushia teke lililonisukima hadi kwenye friji langu lililokuwepo mle ndani nami nikaanguka tena sakafuni ilhali lile friji likifunguka na kuangusha chupa za maji ambazo zilipasuka na kumwaga maji sakafuni pamoja na baadhi ya vyakula vilivyokuwamo ndani ya ile friji. Maji ya baridi yakinimwagikia na kutapakaa mle ndani. Nilianguka chini nikiwa nimeishiwa nguvu kabisa.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA ISHIRINI NA SITA.

Nilijitahidi kupambana naye lakini alinielemea vibaya sana na nikahisi nguvu zikiniishia.Nilijitutumua kwa nguvu zangu zote na kufanikiwa kumbwaga pembeni nami nikajiinua kujaribu kukimbia lakini alinirushia teke lililonisukima hadi kwenye friji langu lililokuwepo mle ndani nami nikaanguka tena sakafuni ilhali lile friji likifunguka na kuangusha chupa za maji ambazo zilipasuka na kumwaga maji sakafuni pamoja na baadhi ya vyakula vilivyokuwamo ndani ya ile friji. Maji ya baridi yakinimwagikia na kutapakaa mle ndani. Nilianguka chini nikiwa nimeishiwa nguvu kabisa.
Yule askari wa kike aliniacha nikitweta pale sakafuni naye akauendea ule mfuko wangu wa nailoni niliokuwa nikijiandaa kutoka nao na kuanza kuupekua kwa vurugu, akitafuta ule mkanda wa video, bila ya kujali kuwa alikuwa amepiga magoti kwenye dimbwi la maji yaliyomwagika kutoka kwenye chupa zilizopasuka kutoka kwenye friji langu.
Nilipeleka mkono wangu na kukamata waya wa pasi uliokuwa umechomekwa kwenye swichi ya umeme ukutani hali ncha yake ya pili ikiwa kwenye pasi. Ile pasi ilikuwa imelegea sehemu ule waya ulipokuwa ukiingia kwenye ile pasi na mara kadhaa huwa inanitetemesha wakati nikiitumia. Niliung’oa ule waya kutoka kwenye ile pasi na huku nikiwa nimeushika hali zile ncha za kupitisha umeme zimetokeza nje, niliwasha ile swichi ya umeme na kuutupia ule waya pale kwenye lile dimbwi la maji hali mimi mwenyewe nikirukia juu ya kochi.
Yule dada alipigwa na shoti kubwa ya umeme ambayo hata mimi ilinitisha. Alitetemeshwa vibaya sana na ingawa alipanua kinywa kwa maumivu na kupiga ukelele, hakuna hata sauti iliyotoka. Alitupwa na ule umeme na kujipigiza kwenye mguu wa meza na kubaki akitupatupa miguu na mikono pale sakafuni. Nilikimbia na kuizima ile swichi na kubaki nikimtazama yule dada.
Alikuwa amenyooka kama gogo pale sakafuni akiwa ametoa macho bila ya fahamu.
Bila ya kujali iwapo nilikuwa nimemuua yule askari au la, nilikusanya vitu vyangu haraka haraka na kubadilisha zile nguo zangu zilizoraruriwa na yule askari mbaya. Nilijifuta uso wangu kwa nguo zile na wakati huo huo nilibadili na kuvaa nguo katika zile nilizochagua kwa ajili ya kwenda nazo kule Gongo la Mboto. Kisha nilimburura yule askari mpaka nje ya mlango wa nyumba yangu na kuangaza huku na huko.
Kama jinsi nilivyotarajia, hakukua na mtu. Muda kama ule pale kwetu huwa kunakuwa kimya sana. Nilifunga mlango wangu kwa ufunguo na kumalizia kwa kulifunga na lile geti langu la chuma na kuuficha ule ufunguo wangu mahala pale pale pa kila siku.
Niliuruka mwili wa yule askari na kuondoka haraka eneo lile. Nje ya lile jengo nilikodi teksi na kumwamrisha dereva anipeleke sokoni kariakoo. Huko nilimpigia tena simu yule afisa wa polisi aliyeitwa John Vata.
“John Vata.”
“Tigga...” Nilisema huku nikihema na kuangaza huku na kule.
“Tigga! Sasa mbona unakata simu kabla hatujamaliza kuongea? Uko wapi?”
“Sikiliza afande. Sasa hivi kuna askari mwenzenu ametaka kuniua nyumbani kwangu, na kama utawahi utamkuta pale nje ya nyumba yangu akiwa aidha hana fahamu au amekufa. Najua kufikia sasa utakuwa unapafahamu nyumbani kwangu.”
“Ndio, Upanga,...nilishafika lakini nyumba ilikuwa imefungwa..”
“Wahi eneo hilo upesi. Huyo askari ndiye atakayekupa undani wa mambo yote haya, na yuko upande wa yule mtu anayejiita Martin Lundi. Mi’ n’takupigia tena kesho..”
“No Tigga! Usikate! Nataka...”
Nilikata simu na kukodi teksi nyingine niliyoiamrisha inipeleke moja kwa moja hadi Uno Trabajo Bar kule Gongo la Mboto.
Nikiwa kwenye kiti cha nyuma ndani ya ile teksi, mwili wote ulianza kunitetemeka na woga usio kifani ulinitawala.
--
Usiku ule sikulala vizuri. Kwanza kutokana na kazi za uhudumu wa baa ambazo sikuwa nimepata kuzifanya hata siku moja, na sikutarajia kuwa ingefika siku ningelazimika kufanya kazi kama ile. Kachiki alinijia juu sana kwa kuchelewa kwangu lakini halikuwa jambo lililoleta matatizo makubwa kutoka kwenye uongozi wa ile baa. Nilipopata nafasi ya kuweka ubavu kitandani ilikuwa saa nane za usiku na badala ya kulala nilikuwa nikisumbuliwa na wazo la yule askari wa kike mshirika wa mtu anayejiita Martin Lundi.
Itakuwaje iwapo nitakuwa nimemuua? Je, yule mtu niliyetarajia anisaidie, Kamishna Msaidizi wa polisi John Vata atanielewa? Yaani huku kupambana na hawa wauaji kunanifanya na mimi sasa niwe muuaji? Kwa hiyo ndio tayari maisha yangu yamebadilika sasa, na sijui kama yatawezakurudi katika ile hali ya zamani...
Mawazo kama hayo yalinisumbua sana usiku ule na kulipokucha tu niliamka na kusubiri kupambazuke ili nikampigie simu John Vata nipate kujua hatma ya yule mwanadada, na mustak-bali wangu baada ya hapo.
“Yeah Hallow!”
“Eem-ah...Tigga hapa...”
“Sikiliza we’ binti, hivi unajua unaongea na kufanya mchezo na nani? Kwa nini hutaki kufanya...”
“Ulimkuta yule askari pale kwangu?”
“Unajua kuwa hakukuwa na mtu pale kwako, ndio maana nakuuliza kuwa unajua unafanya mchezo na nani?”
“Hakukuwa na mtu? Yaani hukumkuta nje ya mlango wangu?” Nilimuuliza huku nikifarijika moyoni kuwa kumbe yule dada hakufa. Ina maana alizinduka na kufanikiwa kuondoka kabla Kamishna Msaidizi John Vata hajamkuta.
“Hakukuwa na mtu na nyumba ilikuwa imefungwa vilevile!”
“Aaah....sasa basi...”
“Sasa mchezo basi! Hili swala la kusema kuna askari mwenzetu anashirikiana na huyo mtu anayejiita Martin Lundi sio la masihara, na nitahitaji uthibitishe hilo kwa ushahidi usiopingika, la si hivyo n’takutia kwenye matata mazito zaidi ya haya ambayo unayo hivi sasa!”
“Kwa hiyo huniamini Kamishna?”
“Siwezi kukuamini mpaka ujitokeze na nisikie maelezo yako!”
“Sasa basi nakutaka umweke chini ya ulinzi mtu aitwaye Dick Bwasha. Ni meneja wa tawi la benki moja hapa jijini. Huyu naye ni mmoja wa hao watu waliofanya mauaji kule msituni...”
“Tulishapitia mchezo huo na sasa hatuuchezi tena! Jitokeze utueleze unalojua juu ya watu wote hao ndipo sisi tutaamua iwapo tuwaweke chini ya ulinzi au la...”
Nilitaka sana kujitokeza kwake na kupata msaada na ulinzi kutoka kwake, lakini bado ilikuwa vigumu kwangu kumuamini moja kwa moja kwani kumbukumbu ya mambo yaliyonikuta mpaka sasa bado haikuniruhusu kuamini mtu yeyote kirahisi kama jinsi yule afisa wa polisi mtanashati alivyotaka.
“Fanya hivyo afande nami nitajitokeza. Nataka ujionee mwenyewe kuwa ni kweli hao watu ninaokutajia wapo, kisha tutaongea kwa undani zaidi na nitakupa vithibitisho vya kutosha.”
John Vata alibaki kimya kwa muda, kisha akauliza Dick Bwasha ni meneja wa tawi gani la benki nami nikamtajia, na kumsisitizia kuwa utaratibu ulikuwa ni ule ule. Nataka nihakikishe kwa yakini kabisa kuwa ni kweli huyo mtu amekamatwa.
“Kwa nini unafanya hivi wewe mwanamke?”
“Nataka kujua iwapo ninaweza kukuamini.”
“Unaitilia mashaka serikali?”
“Hata hao walionitumbukiza kwenye balaa hili nao walidai kuwa ni serikali.”
“Ni kina nani hao?”
“Kwa kweli sijui, ila ninachojua ni kwamba huyo mtu aliyejiita Martin Lundi ni mmoja wa viongozi wao na huyo Dick Bwasha niliyekutajia hivi punde ni mmoja wa vibaraka wao...mkamate Dick Bwasha afande, huenda akakufikisha kwa Martin Lundi muongo, nami nitajitokeza.” Nilimjibu na Kamishna Msaidiza John Vata alikaa kimya kwa muda kabla ya kuongea tena.
“We’ unanipigia simu kila unapotaka. Sasa mimi nikikuhitaji nitakupataje?”
“Nadhani ulisema kuwa utaniwinda mpaka utanitia mbaroni, sasa imekuwaje tena?” Nilimjibu na kukakata simu kabla hajaongea zaidi.
Nilirudi Uno Trabajo Bar na kuchapa usingizi mzito.
--
Baada ya kusubiri kusikia habari za kukamatwa kwa Dick Bwasha kwa siku mbili bila mafanikio nilimpigia tena simu Kamishna Msaidizi John Vata. Nikiwa nimejawa ghadhabu kutokana na kutotekelezwa kwa maagizo yangu, nilijitambulisha kwake na kuanza kumshutumu juu ya swala la kutokamatwa kwa yule meneja wa benki anayeshirikiana na kundi la Martin Lundi muongo, naye kwa utulivu mkubwa alinipa jibu ambalo sikulitarajia na lililonishitua kupita kiasi.
“Dick Bwasha is dead, Tigga!”
“Dick Bwasha is d-whaaaat?” Nilimuuliza kwa mshangao mkubwa.
“Huyo mtu uliyenielekeza nikamkamate kuwa ni mshirika wa mtu anayejiita Martin Lundi amekufa. Sasa nataka ujitokeze utoe maelezo juu ya mambo haya Tigga kwa sababu inaelekea kuwa kila unapopita unaacha kifo au vifo nyuma yako...halafu unasema mtu aitwaye Martin Lundi ndio muuaji!” John Vata aliniambia kwa upole wa hali ya juu, na nikajua kuwa alikuwa ameghadhibika kupita kiasi.
Ina maana sasa naonekana kuwa namsingizia tu huyu mtu aitwaye Martin Lundi, ambaye kiutaratibu ni kwamba hayupo kwani Martin Lundi halisi ni mstaafu wa miaka sabini na tano.
Sikujua niseme nini, nilipigwa na butwaa.
Kwa mara nyingine tena Martin Lundi muongo alikuwa amenizidi kete!
Hivi ni siri gani hiyo waliyonayo hawa watu ambayo njia pekee ya kuificha ni kifo?
“Tigga? Bado upo?”
“Yeah...lakini...Dick Bwasha? It can’t be! How...I mean... amekufaje?”
“Nadhani wewe ndiye unaweza kutueleza kwa ufasaha juu ya hilo Tigga, sasa aidha ujitokeze mara moja au uache kabisa kunipigia simu namna hii. Mimi ni Kamishna msaidizi wa polisi, sio mtu wa kufanyiwa mchezo namna hii!”
Niliogopa!
“Sifanyi mchezo afande! Lakini...lakini hizi taarifa zinanitatanisha! Itakuwaje Dick Bwasha Afe? Na kwa nini unasema kuwa mimi ninaweza kuwaeleza kwa ufasaha juu ya kifo chake?” Nilikuwa nakaribia kuangua kilio kwenye simu.
“Wewe ndiye unasemekana kuwa ni mtu wa mwisho kuonana naye kabla hajakutwa akiwa amekufa ofisini mwake siku chache zilizopita, na mezani kwake kulikuwa kuna fomu uliyoijaza ya kuchukulia pesa pale benki...”
Haya makubwa sasa!
“Niliondoka nikimwacha Dick Bwasha akiwa hai na jeuri kuliko kawaida afande! Kuna kitu kingine kimetokea baada ya mimi kutoka mle ofisini mwake...umewauliza vizuri wale wahudumu wa ile benki afande?” Nilipayuka kwa kihoro huku nikiogopa ile hali iliyokuwa ikijitokeza, na badala ya kunijibu John Vata alikata simu.
Khah! Yaani yule afisa wa polisi amenikatia simu! Sikuamini masikio yangu.
Ina maana ameniona kuwa mimi ni muongo na bila shaka muuaji na ninataka kumchezea kwa sababu zangu binafsi.
Oh! Mungu wangu hii ni mbaya sana! Hii ni mbaya sana!
Nilimpigia tena, lakini ile simu ilibaki ikiita tu bila kupokelewa hadi ikakatika yenyewe, nami nikazidi kuhamanika. Nikapiga tena, nayo ikawa inaita tu bila kupokelewa.
Please John Vata, pokea simu tafadhali!
Hatimaye ile simu ikakatika, na nilipopiga tena ile simu ikawa imefungwa.
Oh! My God! Nitafanyaje sasa...
Niliondoka nikiwa niliyevurugikiwa na niliyehamanika kupita kiasi. Nilienda moja kwa moja hadi kwenye mgahawa uliokuwa jirani na ile benki niliyohifadhia pesa zangu. Niliketi kwenye kiti kilichokuwa kwenye kona na kuelekea mlangoni ambapo niliweza kumuona kila aliyeingia na kuagiza chipsi kwa kuku na kusubiri kwa kufyonza juisi taratibu. Nilisubiri huku moyo ukinienda mbio na woga usio kifani ukinifanya nishindwe hata kuinua ile glasi ya juisi. Muda si mrefu niliona baadhi ya wafanyakazi wa ile benki wakianza kuingia mle mgahawani kupata mlo wa mchana nami nikawa makini sana nao. Hatimaye nilimuona yule dada niliyezoeana naye pale benki akiingia nami nikahama na juisi yangu hadi kwenye meza aliyoketi na kuketi mbele yake.
Tulitazamana.
“Ti...Unafanya nini hapa?” Aliniuliza kwa wasiwasi na kuanza kuangaza huku na huko ndani ya ule mgahawa.
“Nahitaji kuongea na wewe mara moja na naomba unisikilize kwanza halafu unijibu maswali yangu. Sina muda mrefu, itanilazimu niondoke mahala hapa.” Nilimwambia haraka, na kumtupia swali kabla hajasema neno lolote. “Ni kweli kuwa meneja Dick Bwasha amefariki?” Yule dada aliafiki kwa kichwa huku bado akionekana kuwa amepigwa na butwaa na ujio wangu.
“Amekufa lini na amekufaje?”
Yule dada alinitazama kwa muda kisha akameza funda kubwa la mate.
“Amekufa siku ile ulipokuja kujaribu kuchukua pesa pale benki...” Alinijibu na kuendelea kunitazama kwa mashaka. Niliendelea kumtazama nikitarajia maelezo zaidi kutoka kwake. “Tulichoambiwa ni kwamba amepatwa na mshituko wa moyo...stroke...amekutwa akiwa ameegemea kiti chake kama kwamba amelala.” Yule dada alinijibu huku akinitazama kwa mashaka nami nikiwa nimemkazia macho kwa umakini.
“Ninasemekana kuwa mimi ndiye nilikuwa mtu wa mwisho kuonana naye na polisi wananishutumu kwa kifo chake...unajua nini kuhusu swala hilo?” Nilimuuliza nikiwa makini sana. Akanieleza kuwa naye ndivyo alivyokuwa anajua na kwamba baada ya kuhojiwa na polisi amegundua kuwa kumbe nilikuwa nikitafutwa kwa mauaji ya kutisha tangu siku ile niliyokwenda pale benki na kujaribu kuchukua pesa kutoka kwenye akaunti yangu. Jambo alilodai kuwa nusura limtie na yeye kwenye matatizo kwa kushirikiana nami wakati akijua kuwa nilikuwa natafutwa kwa mauaji, ingawa ukweli ni kwamba yeye hakuwa akijua lolote juu ya hilo kwa wakati ule.
“Hayo yote sio ya kweli Anti, ila ni hadithi ndefu, muda hatuna na hapa sio mahala pake. Ni nani hasa aliyetoa hiyo taarifa kwa polisi kuwa mimi ndiye nilikuwa wa mwisho kuonana na meneja Dick Bwasha? Na kuna uhakika gani juu ya hilo?”
“Mimi nilikuacha naye mle ofisini, kisha ikaja amri kuwa asiruhusiwe mtu yeyote kuonana na meneja kwa siku ile...”
“Kwa hiyo wewe ndiye uliyewaeleza polisi kuwa mimi ndiye nilikuwa wa mwisho kuonana na Dick Bwasha?” Nilimuuliza kwa mshangao.
“Mi’ nilikuacha na Dick Bwasha ofisini, sijakuona ukitoka! Sasa ulitarajia niwaeleze nini polisi?” Yule dada aliniambia kwa msisitizo. Nilitaka kumtupia swali iwapo aliweza kuona kila aliyeingia na kutoka benki wakati akiwa anahudumia wateja, lakini niliona akipepesa macho kwa mashaka, kama kwamba hana imani na kauli yake.

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA ISHIRINI NA SABA.

“Kwa hiyo wewe ndiye uliyewaeleza polisi kuwa mimi ndiye nilikuwa wa mwisho kuonana na Dick Bwasha?” Nilimuuliza kwa mshangao.
“Mi’ nilikuacha na Dick Bwasha ofisini, sijakuona ukitoka! Sasa ulitarajia niwaeleze nini polisi?” Yule dada aliniambia kwa msisitizo. Nilitaka kumtupia swali iwapo aliweza kuona kila aliyeingia na kutoka benki wakati akiwa anahudumia wateja, lakini niliona akipepesa macho kwa mashaka, kama kwamba hana imani na kauli yake. Nilimkazia macho na kumsaili zaidi iwapo alikuwa na uhakika na maneno yake, akilini mwangu nikianza kupata mashaka iwapo naye hajarubuniwa na yule muongo ajiitaye Martin Lundi.
“Lakini walipokuja Agnes alikuwa ameshaondoka...na mi’ sikukumbuka kuwa siku iliyofuatia alikuwa anaanza likizo...” Yule dada alisema kwa wasiwasi, kama kwa kujitetea. Sikumuelewa, na nilipomuuliza zaidi aliniambia kuwa Agnes alikuwa ni yule dada mwingine aliyekuja kuniita na kunipeleka kule ofisini kwa Dick Bwasha na kutuacha naye mle ofisini. Yeye alikuwa ni sekretari wa meneja Dick Bwasha.
“Ah! Lakini nilipotoka Agnes alikuwepo pale kwenye meza yake nje ya ofisi ya Dick Bwasha!” Nilimwambia kwa msisitizo. Yule dada aliangalia pembeni, asijibu kitu.
“Sasa Agnes yuko wapi? Aliongea na polisi? Naye aliwaeleza nini?” Nilimuuliza kwa hamasa kubwa.
“Agnes hakuwepo wakati askari walipofika, siku ya tukio aliondoka mapema kwa sababu kesho yake alikuwa anaanza likizo...” Aliniambia. Nilimtazama kwa huzuni iliyochanganyika na mshangao. Yule dada aliona huzuni usoni mwangu, na aliendelea haraka. “ Mi’ niligundua kuwa kuna mwanamke mwingine aliyeingia ofisini kwa Dick Bwasha baada ya wewe kutoka nilipoongea na Agnes kwa simu akiwa nyumbani kwake kumpasha habari za kifo cha Dick, lakini wakati huo nilikuwa nimeshaongea na polisi...”
“Yaani kumbe kuna mwanamke mwingine aliye....” Nilidakia kwa mshangao.
“Kwa mujibu wa maelezo ya Agnes. Alikuja mwanamke aliyevaa baibui na hijab kama mzanzibari, akinukia manukato ya udi kama jinsi akina mama wa kizanzibari wanavyonukia....” Aliniambia nami nikawa nimezidiwa na jazba, nikadakia.
“Huyo mwanamke alionana na Dick Bwasha?”
“Aliomba kuonana naye lakini Agnes alimwambia kuwa meneja haonani na mtu yeyote. Yule dada alitoa simu yake ya kiganjani na kumpigia Dick palepale. Dick alitoka na kumkaribisha ndani yeye mwenyewe.”
“Kwa hiyo mpaka hapo tu Dick alikuwa hai baada ya mimi kuondoka siku ile...”
“Sasa mimi hayo sikuyajua wakati naongea na wale askari! Na kutokana na mshituko wa tukio lile, hakuna aliyekumbuka juu ya Agnes kwa kipindi kile!”
“Okay...nini kilitokea baada ya yule dada wa kizanzibari kuingia ofisini kwa Dick Bwasha?”
“Kwa mujibu wa maelezo ya Agnes, alikaa huko ndani kwa muda, kisha alitoka na kumuambia Agnes kuwa meneja amesema kuwa asisumbuliwe tena. Ni baada ya huyo dada kuondoka ndipo Agnes alipoenda kuchukua barua yake ya likizo na kuondoka kimya kimya bila kumuaga bosi. Kilichofuata ni wale wafagizi kumkuta Dick akiwa amekufa ofisini mwake. Muda huo benki ilikuwa imeshafungwa kwa siku ile kwa wateja na tulikuwa tumebaki sisi tu...”
Hizi taarifa zilikuwa kali sana na nisingeweza kuziacha hivi hivi tu bila kuzifanyia kazi.
“Sasa rafiki yangu mimi nazidi kuhisiwa uuaji huko na wewe unakaa na taarifa kama hizi?”
“Sasa mi’ sikujua nifanye nini baada ya hapo...na jambo hilo limekuwa likinitisha sana...”
Nilichukua simu yake ya mkononi na kuanza kupiga namba ya John Vata. Yule dada aliniuliza nilikuwa nafanya nini, nami nikamwambia kuwa nawapigia polisi ili wajue juu ya taarifa ile. Ingawa alijitahidi kupinga jambo lile, lakini sikujali. John Vata alipopokea ile simu nilijitambulisha na kumweleza juu ya ile taarifa kwa kifupi.
“We’ unajuaje mambo haya? Au bado unaendeleza mchezo wako wa kunitania? Nakuhakikishia kuwa....”
“Niko na huyo dada hapa niongeapo. Inaonekana hao vijana wako waliokuja kuchunguza juu ya kifo cha Dick Bwasha hawakuwa makini. Ndio maana hata mimi sina imani nao sana.”
“Nipe huyo dada niongee naye sasa hivi!”
“Sasa wewe ndio umpigie au umtembelee hapa benki, hii ni simu yake na tunammalizia dola zake!” Nilimjibu na kukata simu. Yule dada alikuwa ameogopa pasina kiasi, na alikuwa akilengwalengwa na machozi.
“Oh! Mungu wangu. Sasa itakuwaje...si nitaingia kwenye matatizo mimi?” Aliniuliza kwa wasiwasi mkubwa.
“Waeleze kama ulivyonieleza mimi. Usifiche chochote. Hutakuwa kwenye matatizo.” Nilimjibu na hapo hapo simu yake ikaanza kuita. Yule dada alishituka na kuruka kama aliyetekenywa kwenye mbavu na kuitazama ile simu ikiita kwa woga mkubwa.
“Pokea simu na uongee Anti...” Nilimwambia na nilipoona anazidi kuigwaya ile simu, niliipokea. Nilisikia sauti ya John Vata ikiongea nami nilimkabidhi yule dada ile simu. Aliiweka sikioni taratibu huku uso wake ukiwa na woga mkubwa. Niliondoka eneo lile haraka nikimwacha yule dada akiongea na Kamishna Msaidizi John Vata.

--

Ni nani tena huyu mwanamke mwenye kuvaa baibui na kunukia udi?
Je, naye ni miongoni mwa wafuasi wa Martin Lundi muongo?(niliendelea kumwita hivyo kwa sababu sasa sikujua nimwite nani). Na kama ni mfuasi wa yule muuaji muongo, kwa nini amuue Dick Bwasha? Mimi sikuamini kabisa maelezo ya kuwa Dick Bwasha kafa kwa mlipuko wa moyo. Hilo kwangu nililiona ni uongo mtupu. Sikuwa na shaka kabisa kuwa wale akina Martin Lundi walikuwa wamemuua, kwamba walikuwa na namna za kumuua mtu kwa njia yoyote waitakayo. Nilikumbuka maelezo ya Koku juu ya mambo waliyomfanyia Kelvin, na sasa hawezi hata kuongea na inaelekea anakufa taratibu.
Ila kilichonishinda kuelewa ni kwa nini wamuue Dick Bwasha!
Au ndio adhabu yake kwa kushindwa kuuchukua ule mkanda wa video kutoka kwangu? Lakini kama ni hivyo mbona yule dada askari ameshindwa kuupata ule mkanda mara kadhaa na hajauawa?
Nilikuwa nimejilaza kitandani chumbani mwangu pale Uno Trabajo Bar nikitafakari mambo yaliyotokea siku ile.
“Yaani tayari Kamishna Msaidizi John Vata alishaniweka kwenye shutuma za kuhusika na kifo cha Dick Bwasha!” (Niliguna). Nilifikiria hali ingekuwaje kama nisingechukua jukumu la kumuendea yule dada wa pale benki na kuanza kumsaili juu ya kifo cha yule mtu jeuri aliyeitwa Dick Bwasha.
Na sasa huyu mwanamke anayevaa baibui....
Nilikumbuka maneno ya yule dada askari wakati aliponishtukiza pale nyumbani kwangu Upanga.
...ingawa kule ulitupotezea mwenzetu mmoja lakini bado tuko wengi na ni hatari kuliko hata yule uliyesababisha auawe.
Je, na huyu mwanamke mwenye baibui ndio miongoni mwa hao wenzao wengi na hatari kuliko yule muuaji niliyemwita Macho ya Nyoka?
Niliamua kwenda kumpigia tena simu Kamishna Msaidizi John Vata. Sikuwa na ujanja.
Nikiwa bado nasumbuliwa na haya mawazo, nilishitushwa na kishindo cha Kachiki aliyeingia chumbani mwangu kwa pupa akiwa amejawa hamasa kubwa.
“Nini wewe!” Nilimaka nikiwa nimeshituka sana.
“Mshikaji kuna dili la kwenda The Rickshaw, si mchezo!” Aliniambia huku akiwa ametoa macho na uso wake ukiwa umejawa matarajio makubwa.
The Rickshaw!
Niliinuka kutoka kitandani nikiwa makini mno na kumtazama kwa macho ya wasiwasi na kutoelewa.
“Umesema The Rickshaw?” Nilimuuliza nikiwa wima na nikimsogelea taratibu, akilini mwangu nikianza kumhisi kuwa kumbe na yeye anahusika na wale akina Martin Lundi.
“Yes! The Rickshaw mwanangu! Yiiiii-Hhaaa!” Alinijibu na kushangalia huku akiruka juu. Nilimkamata mabega kwa nguvu na kumkalisha kitandani.
“We’ unajua nini kuhusu hili neno The Rickshaw, eenh? Niambie upesi Kachiki na usinidanganye!” Nilimwambia kwa ukali huku nikimtikisa na moyo ukinienda mbio, akilini mwangu ikinijia picha ya yule mtu aliyeuawa kule msituni akinitamkia lile neno wakati akitapatapa katika dakika zake za mwisho za uhai wake.
Sasa leo Kachiki ananiambia kirahisi tu eti kuna dili la kwenda The Rickshaw! Tena kwa bashasha na furaha kubwa namna hii!.
Yaani mimi nililihusisha lile neno na kifo, tena kifo cha kutisha kilichoambatana na vifo vya watu wengine wasio na hatia, yeye analizungumzia kwa bashasha namna hii!
Nilihisi msisimko usio kifani.
Kachiki alinitazama kwa wasiwasi na mshangao kutokana na jinsi nilivyombadilikia ghafla baada ya kusikia neno lile.
“Aaah! Niachie bwana! Mbona hivyo?” Aliniambia huku akinikunjia uso na akiitoa mikono yangu kutoka mabegani mwake. Niliona kuwa nilikuwa nimekurupuka kwa jazba kubwa bila sababu, Kachiki angeshindwa kunielewesha juu ya neno lile kwa mtindo ule. Nilijitahidi kutulia na kumweleza kwa upole ingawa moyoni sikuwa na upole wowote.
“Samahani Kachiki, lakini nimekuwa nikiitafuta sehemu hiyo iitwayo The Rickshaw kwa muda mrefu bila mafanikio. Sasa leo unaponiambia kuna dili la kwenda The Rickshaw nimepatwa na kiherehere kikubwa...”
Kachiki alinicheka kwa kebehi.
“Huwezi kupajua The Rickshaw hivi hivi tu Nuru!(Yeye ananifahamu kwa jina la Nuru Bint Shaweji) Huko huwa tunapelekwa tu na tunajikuta tumefika, lakini wewe mwenyewe ukitaka kujiendea tu hivi hivi huwezi kufika...mpaka upelekwe.” Alinijibu nami nikazidi kuvurugikiwa kwa jibu lile.
Mbona inakuwa kama simulizi ya Alfu lela-u-lela? Vije nifike kwa kupelekwa tu na hata nikitaka kwenda mwenyewe nisipajue?
“Kachiki, huwa mnapelekwa? Mnapelekwa na nani? Na kwa nini kwenda huko kuwe ni “dili”? Kuna nini hapa Kachiki? Mbona sielewi?”
Kachiki alinicheka, kabla ya kujaribu kunifafanulia.
“Inasemekana Mzee Kazimoja ana hisa katika hiyo The Rickshaw, na mara moja moja...”
“Mzee Kazimoja? Ndio nani huyo tena Kachiki? Mbona unanichanganya?”
“Aaah Nuru nawe! Mzee Kazimoja si ndio mwenye hii baa tunayofanyia kazi? Sijakuambia?”
Nilibaki kinywa wazi. Sikuwa nimetilia maanani kumjua mmiliki wa ile baa hapo mwanzo, na hata nilipoanza kazi, sikuwa nimeonana na huyo mmiliki bali nilionana na muangalizi tu wa ile baa aliyekabidhiwa majukumu hayo. Lakini hapo pia nilipata jibu la swali langu, kwa sababu tangu niliposikia jina la ile baa, nililiona kuwa si la kawaida, kwani kwa lugha ya kihispania, neno “Uno Trabajo” lilimaanisha “Kazi Moja” kwa kiswahili. Kumbe yule mmiliki alikuwa ameiita baa ile kwa kufuatisha jina lake kwa lugha ya kihispania.
“Enhe, umesema Mzee Kazimoja ana hisa The Rickshaw...The Rickshaw ni nini?”
“Ndio...”
Kachiki alinieleza mambo ambayo sikuyatarajia kabisa, na kama nisingekutana naye na kuja kwenye hii baa, hakika nisingeyajua asilani!
Aliniambia kuwa The Rickshaw ilikuwa ni kasino moja ya hali ya juu sana jijini. Huko kuna kila aina ya starehe, kuanzia kamari hadi biashara ya ngono. Mara moja moja huwa wanakuja wafanyabiashara kutoka nchi mbali mbali za magharibi kwa ajili ya kujistarehesha katika ile kasino, na pindi wajapo hao wafanyabiashara, baadhi ya wahudumu wa ile baa ya Uno Trabajo huwa wanateuliwa na kupelekwa The Rickshaw kusaidia katika kutoa huduma kwani wahudumu wa huko huwa hawatoshi katika nyakati kama hizo. Na ni hapo ndipo kwenda huko inapokuwa dili, kwani wale wafanyabiashara wa kizungu huwa wanatoa bakshishi nyingi na kama ikiwa bahati yako unaweza kuchukuliwa na kuburudika na mmoja wao na kujipatia pesa nyingi. Kwa maelezo ya Kachiki, kuna mwenzao mmoja alifikia hatua ya kuchukuliwa kabisa na mmoja wa hao wafanya biashara na kwenda naye ulaya na mpaka muda ule alikuwa bado yuko huko.
Lakini kama hiyo haitoshi, mara tu wakirudi kutoka huko huwa wanapewa malipo maalum na uongozi wa ile baa ya Uno Trabajo, malipo ambayo hufikia kiasi cha laki mbili hadi tatu.
Hii taarifa ilikuwa mpya sana kwangu. Na hapo hapo niliamua kuwa ni lazima nifike huko The Rickshaw. Hii ilikuwa ni nafasi ambayo nisingeweza kuiachia hata kidogo.
“Mimi naujua sana mji wa Dar, Kachiki, lakini mbona hata siku moja sijawahi kuiona hiyo kasino iitwayo The Rickshaw?” Nilimuuliza.
“Sasa hapo ndipo hata mimi nilipochemsha, kwani mara ya kwanza nilipopelekwa huko, kesho yake nilitembela karibu mji mzima nikijaribu kuitafuta ile kasino ili nikatafute namna ya kuhamia huko moja kwa moja. Sikuiona kabisa Nuru. Na si mimi tu, hata wenzangu pia walijaribu lakini wapi!” Aliniambia kwa masikitiko.
Sikumuelewa.
“Lakini si mlipelekwa? Kwa nini sasa mshindwe kupajua baada ya hapo?”
“Tunapelekwa tukiwa kwenye gari kama ki-hiace hivi, ambalo huwa halina madirisha kabisa, lina kiyoyozi cha nguvu humo ndani. Hivyo huwa hatujui tunapelekwa wapi, na tukifika huko, ile gari huingia mpaka ndani, tukiteremka huwa tayari tuko ndani. Tunaona tu neno “The Rickshaw” mle ndani. Na mtindo huwa ni huo huo wakati wa kurudi. Tunateremkia kwenye mlango wa kuingizia vinywaji nyuma ya baa na kuingia ndani moja kwa moja” Kachiki alinieleza kwa kirefu.
Nilichoka!
Kwa vyovyote huko The Rickshaw kulikuwa kuna mambo mengi yasiyo sawa, ndio maana hata wale wahudumu wanaopelekwa huko walitakiwa wafike tu humo ndani bila ya kujua njia ya kufikia huko.
Kuna nini huko?
Ndio maana hata Mr. Q alikuwa amesisitiza sana eneo lile, ina maana alijua kuwa huko kuna jambo lisilo sawa...na huenda ndio lililosababisha kifo chake.
Je, huko ndio makao makuu ya lile kundi la akina Martin Lundi muongo?
“Sasa lini mnakwenda huko?” Nilimuuliza Kachiki kwa upole. Alinijibu kuwa siku iliyofuatia ndio walitakiwa wapelekwe The Rickshaw.
“Na mimi naweza kwenda? Nataka kwenda huko nami nikajionee!” Nilimwambia huku moyo ukinidunda, nikijua kuwa jibu lake ndilo lingekuwa mwanzo wa majibu mengi yaliyokizunguka kisa hiki cha kutisha kilichonizunguka. Kachiki alinicheka.
“Wewe huwezi kwenda Nuru. Lazima uelewe kuwa hata sisi tunaopelekwa huko kwanza huwa tunasisitiziwa kuwa tutakayoyaona huko ni siri na tunatakiwa tuyaache huko huko! Halafu tunachukuliwa wale tu tuliokuwa hapa baa kwa muda mrefu, wewe bado mgeni huwezi kuchukuliwa bwana!”
Akili ilinizunguka. Nifanyeje sasa? Nilizidi kumhoji Kachiki juu ya ile kasino iliyoitwa The Rickshaw lakini kufikia hapo alikuwa amechoka kujibu maswali yangu na kuamua kucheza muziki kwa furaha akisubiria hiyo siku ya kupelekwa huko The Rickshaw kasino. Nilimtazama kwa kukata tamaa, kisha nikamfukuza chumbani kwangu, nikimwambia nataka kulala.
“Usikonde shoga, nikirudi keshokutwa nitakukatia na wewe kidogo dogo, si unajua tena?” Aliniambia wakati akitoka. Nilimsukuma nje na kufunga mlango wangu.
Mungu wangu! Kumbe The Rickshaw ni kasino ya hapa hapa jijini!
Ee Mr. Q, ni kipi ulichokiona huko The Rickshaw hata ikabidi uuawe?

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA ISHIRINI NA NANE.

. Nilimtazama kwa kukata tamaa, kisha nikamfukuza chumbani kwangu, nikimwambia nataka kulala.
“Usikonde shoga, nikirudi keshokutwa nitakukatia na wewe kidogo dogo, si unajua tena?” Aliniambia wakati akitoka. Nilimsukuma nje na kufunga mlango wangu.
Mungu wangu! Kumbe The Rickshaw ni kasino ya hapa hapa jijini!
Ee Mr. Q, ni kipi ulichokiona huko The Rickshaw hata ikabidi uuawe?
Nilishindwa kulala. Nilikuwa nikizunguka mle ndani nikiwaza juu ya ile Kasino ya maajabu iitwayo The Rickshaw. Iko wapi? Kuna nini huko? Nitafikaje? Ina uhusiano gani na yale mauaji ya kule msituni na wale wauaji akina Martin Lundi muongo?.
Vyovyote iwavyo, nitahakikisha kuwa na mimi naingia kwenye huo msafara wa kwenda huko The Rickshaw hiyo kesho! Nilidhamiria.
Na nilisahau kabisa kumpigia simu Kamishna Msaidizi John Vata.

viii.
G
ari nyeusi isiyo na madirisha aina ya Nissan Serena Mini-Bus iliyokuwa imewabeba wasichana wanne wahudumu wa ile baa ya Uno Trabajo akiwemo Kachiki, ilitoka nje ya ua wa ile baa na kuingia barabarani. Nikiwa ndani ya teksi bubu iliyokuwa imepaki upande wa pili wa barabara nilimwamrisha dereva wa ile teksi aifuate ile gari mpaka itakapoishia. Ile teksi iliingia barabarani nyuma ya ile Nissan Serena ikiacha gari moja baina yetu.
Safari ya kuelekea The Rickshaw ilikuwa imeanza nami moyo ulikuwa ukinienda mbio kwa hamasa ya kuona mwisho wa safari ile ungenifumbulia kitu gani katika msukosuko huu ulioniangukia.
Awali nilitoka nje ya ile baa nikiwa nimevaa suruali yangu ya jeans iliyoukamata mwili wangu vizuri na fulana nyeupe nikiwa nimebeba mfuko wa nailoni. Niliwaaga wenzangu pale baa kuwa nilikuwa naenda kwa fundi cherehani kushona baadhi ya nguo zangu zilizochanika, nikiwaacha Kachiki na wale wasichana wengine watatu wakisubiri ile gari iliyotarajiwa kuwapeleka huko The Rickshaw, ambapo walitaarifiwa kuwa ingefika mnamo saa tisa za mchana. Nilipotoka na ule mfuko wangu nilipanda daladala na kuteremka kituo kimoja baada ya kile nilichopandia na kuelekea moja kwa moja hadi kwenye choo cha kulipia kilichokuwa karibu na kile kituo. Nilipotoka nilikuwa nimeongezea shati jekundu la mikono mirefu la kitambaa kizito cha drafti-drafti juu ya ile fulana, kichwani nilikuwa nimevaa kofia ya kapelo na usoni nikiwa nimevaa ile miwani yangu ya jua. Niliikodi ile teksi na kurudi nayo mpaka pale Uno Trabajo Bar na kumuambia dereva aegeshe upande wa pili wa barabara. Wakati tukisubiri huku nikiwa makini kuangalia kila gari iliyotoka kule baa, nilimweleza yule dereva kuwa nilikuwa namvizia mpenzi wangu ambaye nilishabonyezwa kuwa alikuwa ana uhusiano wa kimapenzi na mmoja wa wahudumu wa ile baa, nami nilikuwa nataka niwafuatilie mpaka watakapoishia ili niwafumanie.
Yule dereva aliniuliza swali moja tu; nilikuwa na pesa ya kutosha?
Nilitoa elfu kumi na kumkabidhi, nikimwahidi nyongeza pindi tutakapofika mwisho wa safari yetu naye akaona kuwa ile pesa haikutosheleza.
Tuliifuata ile gari wakati ikikata mitaa ya jiji kwa ustadi mkubwa, yule dereva akiamini kuwa ilikuwa ni gari ya mpenzi wangu iliyombeba mhudumu wa ile baa ya Uno Trabajo anayehusiana naye kimapenzi. Lakini kadiri tulivyoendelea kuifuata ile gari, niliona kuwa tulikuwa tukizunguka tu katika mitaa mbali mbali ya jijini bila ya uelekeo maalum, na nikaanza kupata mashaka kuwa huenda wale watu waliokuwa kwenye ile gari walikuwa wametugundua na kuamua kutuzungusha tu mjini ili watupoteze.
“Hawa jamaa zako vipi Anti, au wanatuchezesha...” Dereva naye alianza kupata wasiwasi lakini nilimkatisha.
“Endesha gari Anko! Kazi yako ni kuwafuata tu mpaka watakapoishia!”
“Sawa, lakini hii misele inakuwa mingi sasa! Tusije tukaanza kupigizana kelele kuhusu kulipana hapa, Oh-hoo!”
Bila ya kuongea nilitoa elfu tano na kumkabidhi. Jamaa aliipokea na kuendelea kuendesha bila kelele zaidi. Wakati tukiendelea kuifuata ile gari ikizunguka mitaani, nilipata wazo lililonielewesha ni kwa nini akina Kachiki, ingawa walishapelekwa mara kadhaa, bado walishindwa kujua ni wapi ilipo ile kasino ya The Rickshaw, kwani ilinijia akilini kuwa wale watu hawakuwa wametugundua, bali walikuwa wakiwazungusha hovyo mjini wale wasichana kabla ya kuwapeleka kulipokusudiwa ili wapoteze kabisa uelekeo wa safari yao ili wasiweze kurudi tena.
Kwa nini?
Sikupata jibu lakini hii ilizidi kunihamasisha kuwa uamuzi wangu wa kuifuata ile gari waliyopanda akina Kachiki ulikuwa wa busara sana, na kwamba Mr. Q alikuwa na sababu za msingi za kunisisitizia juu ya hiyo The Rickshaw kwani hapana shaka kabisa kuwa alijua kwamba The Rickshaw ndiko ambapo ningepata majibu ya kitendawili chote kilicholizunguka lile tukio la kutisha la kule msituni. Tuliendelea kuifuatilia safari ya ile Nissan Serena iliyokuwa mbele yetu, sasa hivi kukiwa kuna magari mawili baina yetu.
Baada ya kuzunguka bila uelekeo unaoeleweka kwa muda, ile gari iliingia maeneo ya katikati ya jiji, maeneo ambayo nilikuwa nimeyazoea sana na kwenda moja kwa moja hadi nje ya geti la nyuma la kasino maarufu jijini, Casino La Dreamer, na kupiga honi mara mbili. Tulisimamisha gari yetu hatua kadhaa nyuma, upande wa pili wa barabara nami nikawa natazama kinachoendelea kule kwenye lile geti huku maswali mengi yakianza kujijenga kichwani mwangu.
Casino La Dreamer ilikuwa ni sehemu maarufu tu ya starehe jijini na hakuna mwenyeji wa jiji hili lililojaa kila aina ya starehe asiyeijua kasino ile.
Sasa vije akina Kachiki waseme walikuwa wakipelekwa The Rickshaw wakati kumbe walikuwa wakiletwa Casino La Dreamer?
“Ee bwana ee...jamaa kamleta mtoto kasino! Si mchezo babaake...” Yule dereva alisema kwa kushabikia ile hali huku akinitupia jicho la pembeni na kukatisha mawazo yangu.
“Na sasa jasho litamtoka. Bado unahitaji pesa zaidi? Nimekupa elfu kumi na tano ukumbuke!.” Nilimwambia yule dereva huku nikishuhudia ile gari iliyowabeba akina Kachiki ikiingia ndani ya lile geti la nyuma la Casino La Dreamer, na lile geti likifungwa nyuma yake. Yule dereva alidai aongezwe elfu kumi zaidi, lakini baada ya mabishano mafupi, nilimuongezea shilingi elfu tatu na kuagana naye.
Kwa nini ile gari iliishia CasinoLa Dreamer? Hii kasino mimi nilikuwa nikiijua sana, kwani ingawa sikuwa nimewahi kuingia humo ndani hata siku moja, nilikuwa nikiiona mara kwa mara nilipokuwa katika pita pita zangu za mjini na hata katika matangazo mbali mbali ya barabarani na kwenye vyombo vya habari, hasa televisheni.
Lakini Casino La Dreamer sio The Rickshaw!
Sasa kwa nini akina Kachiki wasipelekwe huko The Rickshaw na badala yake waletwe hapa kwenye hii kasino?
Nilijipa moyo na kuingia ndani ya ile kasino, ikiwa ndio mara yangu ya kwanza kuingia katika kasino tangu nizaliwe. Niliangaza huku na huko kwa chati na kutafuta meza iliyokuwa pembeni na kuketi. Niliagiza kinywaji na chakula cha makaroni, huku moyoni nikiumia sana baada ya kutajiwa ile bei ya vyakula vile, na wakati nikisubiri nilianza kuangaza mle ndani. Hakukuwa na watu wengi, na niliona wengi wa waliokuwamo mle ndani walikuwa wakijishughulisha na michezo mbali mbali ya kamari, pool na kunywa pombe. Wengine walikuwa wamepakatana na mabinti waliokuwa nusu uchi, wakinyonyana ndimi na kufanya mambo ya aibu bila haya;na wala hakuna aliyeonekana kushangazwa na hali ile isipokuwa mimi.
Ni nini kinaendelea hapa? Wako wapi akina Kachiki?
Nilianza kula chakula changu taratibu sana, huku nikitembeza macho mle ndani kujaribu kuona iwapo kuna kitu chochote cha kuniwezesha kuelewa kinachoendelea mle ndani kuhusiana na tukio nililolishuhudia kule msituni siku kadhaa zilizopita, kwani kwa vyovyote ile sehemu iitwayo The Rickshaw ilikuwa na umuhimu mkubwa sana kwa yule mtu aliyeuawa kule msituni kiasi cha kuisisitizia sana kabla ya kifo chake. Sasa kama hii kasino iitwayo La Dreamer ilikuwa na uhusiano wowote na The Rickshaw, lazima kuwe na kitu cha kuniwezesha kujua...
Lakini ni kitu gani?
Mazingira yalionekana shwari kabisa. Hakukuwa na dalili ya hao wafanyabiashara kutoka nchi za magharibi, wala akina Kachiki...kulikoni?
Nilimwita mhudumu na kumuuliza uelekeo wa chooni. Aliponielekeza niliinuka na kuanza kuelekea usawa wa chooni huku nikiangaza kwa chati mle ndani nikijaribu kutafuta namna ya kuwaona akina Kachiki. Kabla ya kuvifikia vyoo, kulia kwangu niliona milango mipana ya kioo kisichoruhusu kuona upande wa pili, yaani tinted. Bila kujishauri zaidi na huku moyo ukinipiga kwa nguvu, niliacha ule uelekeo wa vyooni na kujaribu kusukuma ile milango, ambayo ilifunguka nami nilijitoma ndani haraka na kujikuta nikiwa kwenye korido fupi iliyokuwa na hewa safi ya viyoyozi visivyoonekana. Nilisimama kwenye ile korido na kuangaza mazingira niliyokuwamo. Kulia kwangu, hatua chache mbele yangu, kulikuwa na milango ya lifti za kupanda kwenye ghorofa ya juu, na hatua chache mbele zaidi, upande wa kushoto, kulikuwa kuna mlango mwingine mpana uliokuwa na kioo katika nusu yake ya juu ilhali nusu yake ya chini ikiwa ni mbao safi ya mninga. Niliunyatia ule mlango na kuchungulia kwenye kile kioo na kugundua kuwa ulikuwa ni mlango uliotokea jikoni, ambapo niliona wapishi wengi wake kwa waume wakiwa wamezama katika mapishi mbali mbali. Nilirudi hadi kwenye ile milango ya lifti na kubonyeza kitufe kimoja na pekee kilichokuwa kando ya ile milango nayo ikafunguka. Niliingia ndani ya ile lifti huku moyo ukiwa unanipiga kwa wasiwasi na ile milango ikajifunga. Ndani ya ile lifti nilibonyeza kitufe cha kwenda juu na ile lifti ilianza kupanda taratibu. Kufikia hapa moyo ulikuwa ukikimbia kwa kasi isiyo ya kawaida na ingawa kulikuwa kuna kiyoyozi cha nguvu ndani ya ile lifti, nilihisi jasho likinitoka.
Hatimaye ile lifti ilifika mwisho wa safari yake na ile milango ikafunguka nami nikatoka nje kwa mashaka, na kwa hakika sikuwa nimejiandaa kabisa na kile kilichokuwa kikinisubiri nje ya ile lifti.
Hatua zipatazo kumi na tano mbele yangu kulikuwa kuna lango kubwa lililonakshiwa kwa mbao na vioo kwa namna ya kupendeza kabisa, na juu yake kukiwa na maandishi yaliyowaka taa, herufi zake zikiwa zimerembwa kwa mtindo wa kuvutia nami nikabaki nikilitazama lile neno lililoandikwa juu ya mlango ule huku taa za rangi mbali mbali zikitembea ndani ya herufi zake.
THE RICKSHAW.
“Oh, My God...” Nilibaki nikiwa nimepigwa na butwaa huku nikiingiwa na msisimko mkubwa uliotokana na ufumbuzi wa fumbo lile la The Rickshaw nililoachiwa na Mr.Q, na uficho ulioizunguka sehemu hii kama jinsi nilivyoelezwa na Kachiki.
The Rickshaw ni kasino ndani ya kasino!
Niliangaza taratibu katika lile eneo nililokuwa nimeibukia. Sehemu yote ilikuwa na ukuta wa kioo, nami nilikuwa nimesimama kwenye korido pana iliyozungukwa na vioo kila upande, hadi kwenye dari. Kila nilipogeuka nilijiona mimi mwenyewe, na kiasi niliinigiwa na woga kutokana na hali ile. Ni kama nilikuwa ndani ya boksi la kioo. Sakafu ya ile korido ilikuwa ni ya marumaru, yaani ceramic tiles, na kushoto kwangu, mwisho wa ile korido kulikuwa kuna ngazi zilizoelekea juu ya jengo lile.
“Hakuna huduma leo Anti!” Nilishitushwa na sauti nzito ya kiume na kwa mara ya kwanza niliwatilia maanani wale mabaunsa wawili waliokuwa wamesimama kila upande wa lile lango kubwa la kuingilia ndani ya ile sehemu ya starehe iliyoitwa The Rickshaw.
Ingawa niliwaona wale watu wenye miraba minne wakiwa wametunisha vifua mbele ya ule mlango tangu nilipoteremka kutoka kwenye lifti, lakini akili yangu ilichotwa moja kwa moja na lile neno The Rickshaw lililokuwa juu ya ule mlango na yale mazingira ya vioo ya eneo lile kiasi kwamba sikuwatilia maanani kabisa.
Nilijikohoza kwa aibu na kuwauliza kulikoni leo kuwe hakuna huduma huku nikiwasogelea taratibu
“Leo ukumbi umekodiwa kwa siku nzima…labda uje kesho….” Mmoja wa wale mabaunsa aliniambia huku akisimama mbele ya ule mlango kunizuia nisijaribu kujipenyeza humo ndani. Moja kwa moja nilielewa kuwa huduma ilikuwa imefungwa kutokana na ule ugeni maalum wa wafanyabiashara kutoka nchi za mbali ambao akina Kachiki waliletwa kuja kuwahudumia. Nilijikohoza tena kwa kukosa jambo la kufanya na kumtazama kwa hofu yule baunsa na kujaribu kumuambia kitu lakini nilikosa la kusema. Nilirudi nyuma taratibu huku nikiwatazama wale watu kwa woga, huku nao wakinitazama kijeuri, kama kwamba walikuwa wakinitegea nibishane nao ili wanioneshe madhara ya kubishana na misuli yao.
Nilibonyeza kitufe, milango ya lifti ikafunguka nami nikaingia ndani. Niliendelea kutazamana na wale mabaunsa wakiwa mbele ya ule mlango wa The Rickshaw hadi ile milango ya lifti ilipojifunga nami nikateremshwa kule chini kwenye lile eneo la CasinoLa Dreamer.
Kwa nini ile kasino nyingine iitwayo The Rickshaw isitangazwe hadharani kama jinsi ilivyokuwa ikitangazwa ile kasino La Dreamer ambamo ndani yake ndio ilikuwamo ile kasino iliyoitwa The Rickshaw?
Nilitoka kwenye ile milango ya kioo na kukata kushoto haraka, nikijitia ndio nilikuwa natokea chooni, na kurudi kuketi mezani kwangu. Moyo ulikuwa ukinipiga kwa nguvu sana.
Ee, Mungu wangu! Yaani nimeigundua The Rickshaw!
Sikuamini, na kwa mara nyingine nilishukuru uamuzi wangu wa kumsaidia Kachiki siku nilipokutana naye kwa mara ya kwanza na kuomba kuambatana naye hadi kule Uno Trabajo Bar.
Ningeigundulia wapi The Rickshaw kwa jinsi ilivyokuwa imefichwa namna ile! Yaani ningezunguka mji mzima na ningeambulia patupu. Lakini sasa nilikuwa nimepagundua.
Hapana shaka pale ndio kwenye majibu yote ya mkasa huu niliotumbukizwa bila ya ridhaa yangu.
“Haya Mr.Q, nimeshafika The Rickshaw, ni kitu gani sasa ulichotaka nikione humu ndani?” Nilijinong’onea mwenyewe huku nikiendelea kushika shika chakula changu na nikiangaza-angaza mle ndani, nikitegemea kumuona yule muuaji muongo anayejiita Martin Lundi au yeyote katika wale wafuasi wake.
Lakini sikumuona yeyote kati yao.

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA ISHIRINI NA TISA.

Ningeigundulia wapi The Rickshaw kwa jinsi ilivyokuwa imefichwa namna ile! Yaani ningezunguka mji mzima na ningeambulia patupu. Lakini sasa nilikuwa nimepagundua.
Hapana shaka pale ndio kwenye majibu yote ya mkasa huu niliotumbukizwa bila ya ridhaa yangu.
“Haya Mr.Q, nimeshafika The Rickshaw, ni kitu gani sasa ulichotaka nikione humu ndani?” Nilijinong’onea mwenyewe huku nikiendelea kushika shika chakula changu na nikiangaza-angaza mle ndani, nikitegemea kumuona yule muuaji muongo anayejiita Martin Lundi au yeyote katika wale wafuasi wake.
Lakini sikumuona yeyote kati yao.
Baada ya kuzubaa mle ndani kwa muda, niliamua kuondoka. Nilijua kwa kuwa nimeshaigundua The Rickshaw ilipo, niliweza kurudi tena wakati wowote, jambo ambalo nilidhamiria kulifanya siku iliyofuata tu na kuendelea na uchunguzi wangu wa kutafuta majibu ya maswali yaliyotokana na lile tukio la msituni. Nililipia chakula na kinywaji changu na kutoka nje ya ile kasino na kuanza kukata mitaa kutafuta uelekeo wa kurudi Uno Trabajo Bar, huku kichwani mwangu nikiwa natafakari mtirirko wa matukio yaliyopelekea hadi mimi kulazimika kuitafuta ile kasino iliyoitwa The Rickshaw na kufanikiwa kuibaini. Mr. Q alikuwa ameniachia ile namba ambayo mpaka sasa sikuwa nimeweza kuing’amua ilikuwa inahusu nini, na lile neno The Rickshaw ambalo leo hii nimehakikisha kuwa ni jina la kasino iliyojificha ndani ya kasino nyingine katikati ya jiji. Sasa nilikuwa na kitendawili cha neno “Key”, neno lililotamkwa na yule marehemu aliyeuawa na marehemu Macho ya Nyoka kule msituni, likimaanisha “ufunguo”. Kwa kadiri mambo yalivyojitokeza hivi sasa, nilidhani kuwa yule mtu aliyeuawa kule msituni alikuwa akimaanisha kuwa nikiigundua The Rickshaw, nitakuwa nimepata ufunguo (key) wa ufumbuzi wa kile kizaazaa nilichokishuhudia kule msituni, ufunguo ambao ungeniwezesha kumtia mbaroni yule mwanaharamu aliyejiita Martin Lundi na wenzake. Nilidhani hivi ndivyo Mr.Q alivyomaanisha alipokuwa akinitajia yale maneno na kuniambia “find the bastard”, akimaanisha kuwa nimtafute mwanaharamu Martin Lundi muongo.
Nilikuwa nimefika eneo la posta mpya nikielekea kwenye kituo cha mabasi ya Gongo la Mboto, akilini mwangu bado nikiwa nimejawa na mawazo juu ya hatua ya kuchukua baada ya kuigundua ile kasino iliyoitwa The Rickshaw.
Sasa kitendawili pekee kilichobakia ni ile namba ambayo hapo mwanzo nilidhani kuwa ni ya simu na kugundua kuwa haikuwa hivyo.
Huyo “The Bastard” nilikuwa nimeshamjua, tatizo lilikuwa ni kumtia mbaroni tu. Na wakati nikiwa napishana na wimbi la watu waliokuwa wakipita na hamsini zao katika sehemu ile ya jiji iliyokuwa na msongamano mkubwa wa watu siku zote, nilifikiri kuwa ule ulikuwa ni wakati muafaka wa kumtafuta Kamishna Msaidizi John Vata na kujitokeza kwake nikiwa na zile taarifa muhimu dhidi ya kundi la akina Martin Lundi. Kwa vyovyote yeye angekuwa na namna nzuri ya kuingia The Rickshaw na kuvumbua kilichokuwemo.
Ghafla nilisikia nikichomwa na kitu kama sindano kwenye ubavu wangu wa kulia na hapo hapo nilihisi maumivu makali na mwili wangu ukinifa ganzi kutokea kiunoni kuelekea chini. Nilijishika eneo lililochomwa huku nikitoa yowe la uchungu na kuangaza huku na huko nikimtafuta aliyenichoma, lakini watu walikuwa wengi sana, na kila mtu alionekana akiwa na hamsini zake.
Au nimeumwa na nyuki…?
Nilihisi kichwa kikiniwia chepesi na miguu ilianza kugongana, ilhali kizunguzungu kikinigubika ghafla.
Imekuwaje tena Mungu wangu?
Nilitazama watu niliokuwa nikipishana nao huku nikijitahidi kutembea, lakini niliona watu wote sasa walikuwa wakitembea taratibu sana…kiminyato…kama kwenye slow motion ya kwenye sinema, na sura zao zikibadilika na kuwa za kutisha sana.
Naingiwa na wazimu au…?
Nilimpamia mama mmoja mnene sana naye akanigeukia kwa hasira na kunikemea, lakini sikusikia lolote katika maneno aliyokuwa akiniambia na badala yake nilisikia mvumo mzito masikioni mwangu na niliona midomo ya yule mama mnene sana ikifunguka na kufumba taratibu sana na meno yake yakiwa makubwa kupita kawaida ya meno ya binadamu.
Jamani…! Ni nini tena hii…?
Nilianza kuyumba huku nikiwatazama watu usoni, nikiona sura zao zikibadilika na kuwa kama za wanyama wa ajabu-ajabu. Mtu alinipamia kwa nyuma nami nikampamia mtu mwingine aliyenisukuma pembeni huku naye akitoa maneno ya kukereka na kitendo kile, lakini sikusikia neno lolote. Kwa mbali niliwaona makondakta wa madaladala na wapiga debe wakipanua midomo yao kwa nguvu na wakipiga kelele nyingi huku mishipa ya shingo zao ikiwatutumka ilhali macho yao yakiwa mekundu na makubwa sana. Lakini sikusikia sauti yoyote kutoka vinywani mwao. Ilikuwa ni taswira ya kutisha sana.
Mungu wangu…what is happening?(Ni nini kinatokea?)
Nilianza kusikia kichefuchefu na miguu ikiishiwa nguvu kabisa.Nilijiona nikianguka mzima mzima na sikuwa na lolote nililoweza kufanya kujiokoa. Nilipiga kelele kuomba msaada lakini hata sauti yangu sikuisikia. Nilijaribu kujizuia kuanguka kwa kujiegemeza kwenye meza ya mmoja wa wauza peremende waliokuwa pale kando ya kituo cha mabasi. Ile meza ilipinduka nami nilipiga mwereka mzito pamoja nayo mpaka chini. Hapo ndipo nilipoanza kusikia mayowe na sauti za wapita njia. Nilibaki nikiwa nimelala chali kando ya barabara nikitweta na nikiona maluweluwe matupu mbele ya macho yangu na mwili wangu ukiunguzwa na joto la jua lililoikaanga ile ardhi.
“Bila shaka ana kifafa! Mpeni nafasi! Apate hewa!”
Macho yalianza kuniwia mazito na nikaona watu wawili wawili wakiwa wameniinamia.
“Ana njaa huyo...mjini hapa, usimuone mrembo...”
Oh, Mungu wangu! Lazima niinuke..niondoke...nikampigie simu John Vata...
Nilijaribu kujiinua lakini mwili uliniwia mzito sana na nilihisi pumzi zikiniishia, watu walinizingira, na nikahisi mikono mingi ikinishikashika mwilini.
Wananiibia sasa…vibaka wananiibia! Wanajitia kunisaidia lakini wananiibia…wananiibia…
“Nipisheni! Nipisheni, mimi ni daktari...naweza kumsaidia!”
Naijua hii sauti! Naijua hii sauti... ni nani...?
“Jamani bahati kuna dokta...mpisheni, mpisheni...”
Nilijaribu kujiinua lakini nilishindwa na koo likaanza kunikauka. Niliona watu wakisogea pembeni na kuniacha peke yangu.
Jamani nisaidieni mwenzenu! Msiniache...!
“Jamani mimi ni daktari...I am a Doctor...naomba nimuangalie...tafuta gari haraka!”
Ile sauti! Ile sauti! Oh. My God...
Macho yalizidi kuniwia mazito, lakini nijitahidi kuyafumbua huku moyo ukinienda mbio kuliko kawaida.
Lazima nimuone mwenye hii sauti! Namjua! Ni nani...
Kwa kihoro nilimuona yule mtu anayejiita Martin Lundi akipiga goti kando yangu na kuniinamia wakati watu wote waliokuwa wamenizunguka hapo mwanzo wakikaa pembeni kumpisha.
Oh! Mungu wangu!
Nilijaribu kupiga kelele lakini sauti haikutoka. Niliinua mkono wangu na kumtandika kofi zito la uso, lakini hiyo ilikuwa mawazoni mwangu tu, kwani hata mkono wangu sikuweza kuuinua. Nilimuona Martin Lundi muongo akinitazama kwa makini, kama jinsi ambavyo daktari angeweza kumtazama mgonjwa katika mazingira kama yale, ingawa macho yake yalionesha mng’ao wa ushindi ambao watu wote waliokuwapo pale hawakuweza kuuelewa isipokuwa mimi.
Nilimtemea mate kwa ghadhabu, lakini niliambulia kujimwagia udenda mzito uliotiririka mashavuni mwangu na kumwagika mchangani kila upande wa shingo yangu.
Get away from me you bloody bastard!(Kaa mbali na mimi ewe muuaji mwanaharamu!)
Nilibaki nikimtazama yule mtu ajiitaye Martin Lundi kwa kukata tamaa huku nikishindana na macho yangu yaliyokuwa yanataka kufumba nami nikiyalazimisha yaendelee kutazama, lakini yaliniwia mazito kupita kiasi.
Martin Lundi aliniwekea mkono kwenye upande wa shingo yangu na kunifunua macho yangu kitaalamu.
Eti alikuwa akinichunguza kitabibu!
“Kaa mbali na mimi muuaji mkubwa we! Niache! Niache!” Lakini hizo kelele zote zilikuwa akilini mwangu tu, hakuna hata sauti moja iliyotoka kinywani mwangu. Mdomo uliniwia mzito kupita kawaida.
Oh! Mungu wangu, wameshanichoma sindano ya sumu...
Kisha kote kukawa kiza.

“THE BASTARD"

H
ix.

arufu kali ya dawa ilizivamia pua zangu, nami nikajaribu kufumbua macho nikishindana na usingizi mzito. Mwanga mkali ulinipiga usoni na nikajikuta nikifumba tena macho yangu na nikaelewa kuwa nilikuwa nimelala chali kitandani, lakini sikujua nilikuwa wapi. Nilifumbua tena macho taratibu, na huku nikishindana na ule mwanga mkali wa taa uliokuwa ukinipiga usoni nilianza kuangaza yale mazingira niliyokuwamo na mara moja nilijua kuwa nilikuwa hospitali.
Nimefikaje hapa?
Sikuwa na kumbukumbu yoyote ya uhakika juu ya matukio yaliyopelekea mimi kuwa mahala pale, ila nilikuwa na kumbukumbu za mbali sana...kama ukungu tu, juu ya yaliyotokea. Moja kwa moja mbele yangu kulikuwa na mlango wa kioo kizito. Niligeuka taratibu kushoto kwangu huku nikisikia maumivu mwili mzima. Kulikuwa kuna ukuta uliopakwa rangi nyeupe na kalenda ikining’inia pale ukutani. Ile kalenda ilikuwa ikionesha kuwa ule ulikuwa ni mwezi wa julai mwaka 1999.
Nilikunja uso.
Eh! Hii nini sasa? Mwaka 99! Kwani huu si mwaka...mwaka...mwaka gani...! Mungu wangu, yaani nimesahau huu ni mwaka gani?
Niligeuza kichwa kulia kwangu ambako niliona mitambo kadhaa ya kitabibu, kitanda kirefu cha kufanyia uchunguzi wagonjwa na kando ya ule mlango kulikuwa kuna kabati refu lililojengewa ukutani ambalo milango yake ilikuwa imefungwa. Macho yangu yaliangukia tena pale mlangoni na kutokea pale nilipokuwa nimelala, niliweza kuona maandishi yaliyoandikwa kwa nje ya kioo cha mlango ule, ambayo yalisomeka kutokea kulia kwenda kushoto. Nilifinya macho na kujaribu kuyasoma yale maandishi kwa taabu, na nilipofanikiwa niliuhisi mwili wangu wote ukiingia baridi na moyo ukianza kunipiga kwa nguvu.
PSYCHIATRIC WARD 4
Psychiatric Ward?
Wodi ya wagonjwa wa akili!
Yaani niko kwenye wodi ya wagonjwa wa akili? Nini maana yake hii?
Na hapo hapo ilinijia taswira ya yule mama mkuu wa wilaya ya Manyoni akiniambia kuwa mimi nilikuwa mgonjwa wa akili.
“Wewe ni mgonjwa Sylvia…Paranoid Schizophrenia ni ugonjwa hatari sana, unaweza kuwaua wenzako bila kujijua halafu ukaamini kuwa watu walikuja kuwaua na wewe ukafanikiwa kutoroka…vitu hivi vipo…”
Eh, Mungu wangu! Sasa...
Kichwa kilianza kunigonga na ghafla niliuhisi ulimi wangu ukiwa mkavu kama msasa. Nilijaribu kwa mara nyingine kukumbuka matukio yaliyopelekea mimi kujikuta mle ndani lakini lile neno lililokuwa limeandikwa pale kwenye kioo cha ule mlango lilizidi kuikamata akili yangu.
Psychiatric Ward!
Ina maana mimi ni kichaa?
Kichwa changu kilikuwa kinazongwa na vitu vingi kwa wakati mmoja na hakuna hata kimoja katika hivyo kilichokuwa kimekamilika. Vitu vyote vilikuwa nusu-nusu.
Nikiwa nimeingiwa na woga mkubwa, nilijiinua kwenye kitanda kile na kuzungusha kichwa changu kulia zaidi ili nizidi kuona zaidi vilivyomo mle ndani na ndipo nilipomuona.
Mwanamke wa makamu aliyekuwa amevaa sare za nesi wa hospitali alikuwa amekaa kwenye kiti kilichokuwa kwenye kona ya chumba kile akisoma kitabu. Nilimtazama kwa wasiwasi, lakini yeye alikuwa amezama kwenye kitabu chake, akidhani bado nimelala.
Ni nani tena huwa anavaa nguo kama hizi...?
Nilimtazama yule mwanamke. Kifuani alikuwa amening’iniza simu nzuri ya kiganjani iliyokuwa ikining’inia kutoka kwenye kamba maalum iliyopitishwa shingoni mwake. Niliitazama ile simu, kisha nikageukia kule ukutani kwenye ile kalenda.
“Nitoe humu ndani upesi!” Nilimwambia yule mwanamke kwa sauti iliyokoroma na ingawa nilikuwa nimedhamiria kumkaripia, lakini ilitoka kwa udhaifu sana. Yule mwanamke alishituka na kuweka kitabu chake juu ya meza iliyokuwa kando ya kiti alichokuwa amekalia na kuja kando ya kitanda nilichokuwa nimelalia huku akitabasamu.
“Hatimaye ameamka! Unajisikiaje sasa kisura wangu?” Aliniuliza kwa sauti ya kuliwaza kama kwamba alikuwa anaongea na mtoto mdogo. Nilimtazama kwa mshangao. Sikuwa nimewahi kumuona hata siku moja kabla ya pale.
“Wewe ni nani...niko wapi hapa?” Nilimuuliza kwa wasiwasi.
“Mimi ni nesi...niite nesi Tamala...na hapa uko hospitali...Nellie Nightingale Memorial Hospital”
Sikuwa nimepata kuisikia hii hospitali hata siku moja na wala sikujali.
Kwa nini akili haizingatii mambo?
Niliitazama tena ile simu yake na kupeleka macho yangu kwenye ile kalenda, ambayo ilikuwa bado mpya.
“Leo ni siku gani...” Nilimuuliza taratibu, alisita kidogo.
“Emm...Alhamisi. Tarehe kumi na mbili Julai...”
“Mwaka gani...?”
“1999...Lakini usijitese kwa mawazo mengi...ni mbaya kwa afya yako.Unahitaji utulie...upumzike.” Yule mwanamke alinijibu haraka. Nilishindwa kuelewa, nikaigeukia tena ile simu yake. Nikakitazama na kile kitabu alichokuwa akisoma kilichokuwa juu ya meza kando ya kiti alichokuwa amekalia hapo mwanzo.
Mbona sielewi? Kuna kitu hakipo sawa hapa. Lakini ni nini? Na kwa nini najiona kama...kama...mjinga?
“Hii hospitali...Iko wapi? Na nimefikaje hapa?”
“Hapa hapa Dar es Salaam. Ulianguka njiani, wasamaria wema wakakuleta...lakini unahitaji upumzike Sylvia.Unahitaji kunywa dawa yako sasa....”
“Whaaat? Sylvia? Mimi sio Sylvia! Nani kakupa hilo jina? Mimi ni....mimi ni....” Oh, Mungu wangu mbona jina langu silijui? Wamenifanya nini hawa watu?
“Hapana binti, wewe ni Sylvia, ndio maana nakuambia kuwa unahitaji dawa na kila kitu kitakuwa sawa....”
Nilipata mlipuko mwingine wa kumbukumbu kichwani mwangu, safari hii nikiwa kule ofisini kwa mkuu wa wilaya na yule mwanamume aliyevaa mavazi ya kitabibu akinisogelea huku akitabasamu.
“Hallo Sylvia, unajisikiaje leo?”
Nilipiga ukelele mkubwa sana wa woga na hasira, kwani matukio yote yaliyotokea kule msituni hadi kwenye ofisi ya mkuu wa wilaya yalinirudia akilini mwangu haraka haraka na kuishia na sura ya yule mwanaume aliyekuwa amevaa mavazi ya kitabibu akinitolea tabasamu baya na la kuogofya.
“Waongo wakubwa! Wabaya sana nyinyi...! Nitoe humu ndani haraka sana! Nitoe! Nitoe! Nittt-toeeeeeeeeeeee!”
Nilijiinua kwa nguvu kutoka pale kitandani na kujaribu kuteremka lakini nilishindwa. Mikanda maalum iliyokuwa imefungwa kwenye kile kitanda ilikuwa imepita chini ya makwapa yangu na kubana kifua na sehemu ya mapaja yangu, na kadiri nilivyokuwa nikijikukurusha pale kitandani ndivyo ilivyozidi kujikaza na kunibana zaidi pale kitandani.
Ni nani yule mwanaume mwenye koti la kitabibu aliyeniita kwa jina la Sylvia? Nalijua jina lake, lakini kwa nini halinijii?
“Tulia Sylvia, utajiumiza bure kisura wangu! Tulia nikupe dawa! Usipotulia nitakuchoma sindano, lakini ukitulia nitakupa dawa ya vidonge tu umeze umesikia?” Nesi Tamala aliniambia kwa ukali nami nikabaki nikimtazama, nikishangaa kujisikia hamu kubwa sana ya kuangua kicheko.
Sasa kwa nini nicheke? Hii si hali ya kuchekesha! Nimekuwaje mimi?
Nilianza kububujikwa na machozi huku nikimtazama yule nesi kwa kukata tamaa.
Oh! Mungu wangu, sasa nimekuwa mwehu...

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 30.

“Tulia Sylvia, utajiumiza bure kisura wangu! Tulia nikupe dawa! Usipotulia nitakuchoma sindano, lakini ukitulia nitakupa dawa ya vidonge tu umeze umesikia?” Nesi Tamala aliniambia kwa ukali nami nikabaki nikimtazama, nikishangaa kujisikia hamu kubwa sana ya kuangua kicheko.
Sasa kwa nini nicheke? Hii si hali ya kuchekesha! Nimekuwaje mimi?
Nilianza kububujikwa na machozi huku nikimtazama yule nesi kwa kukata tamaa.
Oh! Mungu wangu, sasa nimekuwa mwehu...
“Ooo, sasa usilie kisura wangu eeenh....usilie anti utapona tu!” Nesi Tamala alinisemesha kwa kubembeleza huku akiwa ameshika bomba la sindano, tayari kunichoma. Niliitazama kwa woga ile sindano na nilihisi mwili ukinisisimka.
“Kwa...kwani ninaumwa nini nesi?” Nilimuuliza huku nikilia. Yule mwanamke alinitazama kwa muda kisha akaniambia kuwa nilikuwa ninaumwa sana. Nilikuwa ninaumwa sana kichwani.
“Una ugonjwa ndani ya kichwa chako Sylvia....ndio maana inabidi upatiwe hii dawa.”
“Lakini...lakini mimi sio Sylvia! Mimi ni...mimi ni....” Oh, Mungu wangu, jina langu ni nani tena? “Mimi ni....sio Sylvia!”
“Sasa kama sio Sylvia, jina lako ni nani basi?” Nesi Tamala aliniuliza taratibu huku akizidi kuiandaa ile sindano. Badala ya kumjibu, nilibaki nikiikodolea macho ile sindano.
“Naomba usinichome sindano tafadhali mama! Naomba usinichome sindano...” Nilibwabwaja kama mtoto huku nikilia. Eh! Mungu wangu, mambo gani tena haya! Mbona najiona nakuwa mjinga-mjinga tu?
Nesi Tamala alinitazama, kisha aliweka pembeni ile sindano na kutoa dawa za vidonge kutoka kwenye kichupa cheupe cha plastiki.
“Okay Sylvia...kwa kuwa umekuwa mpole nitakupa vidonge....”
“Mimi sio Sylvia! Kwa nini mnapenda kuniita hivyo?”
“Kwa sababu ndio jina lako, Sylvia!”
Nilishituka na kutazama kule mlangoni ilipotokea ile sauti nzito iliyonijibu kwa ukali. Na muda nilipomtazama tu yule mtu aliyenijibu akiingia mle ndani, nilipatwa na mlipuko mwingine wa kumbukumbu ya tukio lililotokea kabla ya kujikuta ndani ya ile hospitali.

Niliyumba na kupiga mweleka mzito barabarani, kisha nikasikia mayowe ya watu wengi, kila mtu akisema neno lake. Nikiona yule mtu akipiga goti kando yangu na kunishika shingoni, kisha akafunua macho yangu. Nikijaribu kumtemea mate na kuishia kujibubujia udenda. Kisha kiza kizito kilitanda...

Nilihamanika kuliko kawaida. Nilimgeukia yule nesi aliyekuwamo mle ndani kutaka msaada wake, lakini hapo hapo akili yangu ilikuwa kama iliyosimama. Nilibaki nikimkodolea yule nesi uso wake ukionesha woga mkubwa kwa yule mtu aliyeingia, na hiyo ilinikumbusha nesi mwingine aliyenitazama kwa woga kama ule...ni nani...?Lini...? Nilianza kumgeukia tena yule mwanaume aliyeingia na hapo nilipatwa na mlipuko mwingine wa kumbukumbu. Nilimuona dada yangu Koku akiwa katika mavazi kama ya yule nesi akinitazama kwa woga mkubwa sana kama ule niliouona usoni kwa yule nesi, akinisemesha kwa wasiwasi mkubwa.
“Huelewi Tigga. Hawa watu wamo humu hospitalini!”
Na hapo nilikumbuka.
Tigga! Jina langu ni Tigga...sio Sylvia!
Nilijiinua kwa nguvu kutoka pale kitandani nikijaribu kumrukia yule mtu kwa hasira huku nikimpigia kelele za ghadhabu.
“Wewe! Nimekumbuka! Mimi ni Tigga! Tigga Mumba...sio Sylvia, na wewe ni muuaji! Toka! Ondoka machoni mwangu! Usinisogelee! Muuaji!”
Martin Lundi muongo alishituka sana na nilishuhudia uso ukimbadilika na kwa muda hatua zake zilisita, kisha akajikaza na kunisogelea pale kando ya kitanda na kunitazama kwa ghadhabu bila ya kusema neno. Nami nilimrudishia mtazamo wa ghadhabu huku nikijitutumua nikijaribu kujiinua kutoka pale kitandani ilhali ile mikanda maalum iliyonibana pale kitandani ikizidi kukaza na kunibana zaidi.
“You are crazy Sylvia, and you know it!” Aliniambia kwa hasira, akimaanisha kuwa mimi nilikuwa kichaa na kwamba na mimi mwenyewe nilikuwa najua juu hilo, akizidi kuniita lile jina alilonibatiza kienyeji.
“I am not!” Nilimbishia kwa jeuri, kuwa sikuwa mwendawazimu.
“Then you soon will be, unless you give us what we want!” Alinijibu kwa jeuri, akimaanisha kuwa kama sikuwa na wazimu, basi nitakuwa na wazimu muda si mrefu, labda niwape walichokuwa wakikitaka.
Nilimkodolea macho kwa mshangao lakini kabla sijasema neno, mtu mwingine aliingia mle ndani, akiwa na mavazi ya kitabibu.
“Ni nini kinaendela hapa?” Aliuliza taratibu huku akisogea pale kando ya kitanda nilichokuwa nimelazwa. Huyu alikuwa mtu wa makamo, lakini aliyeonekana kujiweka katika afya nzuri na haikuwa na shaka kuwa alikuwa ni daktari. Alikuwa amevaa koti jeupe la kitabibu juu ya fulana nyeusi na suruali ya jeans. Martin Lundi muongo alimgeukia yule daktari na kumkemea kwa ukali.
“Naona dawa zako hazifanyi kazi inavyotakiwa Dokta!”
Yule daktari badala ya kumjibu aliniinamia na kuanza kuniuliza juu ya hali yangu. Nilimtazama kwa jeuri na kutazama pembeni bila kumjibu. Martin Lundi muongo alimkemea tena yule daktari.
“You said the medication will make her docile enough to tell us everything!” (Ulisema hizo dawa zitampumbaza na kumfanya awe mtiifu kiasi cha kutueleza kila kitu!) “Lakini bado akili yake inaonekana makini!”
Yule daktari alimgeukia Martin Lundi muongo na kumjibu taratibu, huku nikigundua kitetemeshi katika sauti yake.
“Yes, but I said after three days of medication. This is only the first day!” (Ndio, lakini nilisema baada ya kutumia dawa kwa siku tatu. Hii ndio siku ya kwanza!)
Eh! Ni nini kinatokea hapa?
“Nilishasema kuwa siwezi kusubiri muda wote huo! Nataka...”
“Then I can’t help you! Unless you want the poor girl to go completely mad...or even die!”
(Basi siwezi kukusaidia! Isipokuwa kama unataka huyu msichana awe mwehu kabisa...au hata afe!) Yule daktari alimkatisha Martin Lundi kwa ukali nami nikaingiwa woga mkubwa kwani yale maneno yalinielewesha kilichokuwa kikiendelea pale.
“Baada ya kupata ninachokitaka, hilo ndilo hasa ninalotaka litokee!” Martin Lundi muongo alijibu kwa hasira. Alienda kusimama nyuma ya dirisha na kukaa kimya kwa muda, kisha alimrudia yule daktari kwa mwendo wa haraka.
“Nakuambia nataka matokeo baada ya siku mbili, na usijitie kunitolea ukali mimi kwa sababu unajua ni nini ninachoweza kukufanyia na kukuharibia maisha yako! Don’t you ever forget that I can destroy your comfortable life by a single telephone call!” Alimwambia kwa sauti iliyojaa vitisho na hasira huku akimtomasa kwa kidole chake cha shahada kifuani, akimaanisha kwa yale maneno ya kimombo kuwa yule daktari asisahau hata siku moja kuwa yeye (Martin Lundi) anaweza kuyaharibu maisha yake mazuri kwa kupiga simu moja tu. Yule daktari alitahayari na kuingiwa na woga, lakini alijitahidi kujitutumua na kumjibu yule muuaji muongo.
“Na wewe usiingilie kazi yangu, kwani ujio wako unaingilia utendaji kazi wa dawa zangu. Huyu binti anakutambua na inaonekana taswira yako imejishindilia sana akilini mwake, hivyo ni vyema ukawa mbali naye kwa muda wote huo wa matibabu...”
Martin Lundi muongo alimtazama kwa hasira yule bwana, kisha akanitazama kwa hasira na alimjibu yule daktari huku bado akiendelea kunitazama mimi kwa ghadhabu.
“Okay Dokta! Nitafanya hivyo lakini nitakuwa humu humu ndani ya jengo! Kwani nimemuandalia mateso makali huyu dada baada ya kukamua taarifa zote nizitakazo kutoka kwake. Sasa ole wako baada ya siku mbili hizo dawa zisifanye kazi!” Kisha alitoka kwa hasira na kuniacha nikiwa na nesi Tamala na yule daktari aliyeshurutishwa kunipa dawa za kunichanganya akili na kunipumbaza.
Niliogopa kupita kawaida.
Yule dokta alimuuliza yule nesi iwapo alinipa dawa baada ya kuamka, akajibiwa kuwa ndio nilikuwa katika hatua ya kupewa hizo dawa wakati Martin Lundi alipoingia mle ndani. Yule daktari alitikisa kichwa kwa masikitiko bila ya kusema neno na kuanza kunichunguza mapigo ya moyo wangu kwa vipimo maalum vilivyokuwemo mle ndani huku akiniuliza maswali kuhusu jina langu, la mama yangu, umri wangu na kadhalika. Kwa maswali yake yote hayo sikutoa jibu hata moja. Hatimaye alimwambia yule nesi ampe sindano anichome. Hapo nilianza kujitutumua nikipinga ile hali.
“Mnataka kunivuruga akili yangu! Kwa nini?” Nilimuuliza kwa uchungu.
“Tulia binti, wala haitauma...” Alinijibu bila kunitazama. Niliona kuwa hakuwa akipenda kufanya jambo lile lakini ilikuwa wazi kuwa Martin Lundi alikuwa amemshurutisha kufanya vile kwa shinikizo fulani ambalo kama lingejulikana sehemu fulani, basi yule daktari angeingia matatani.
“Samahani binti...itauma kidogo tu halafu kila kitu kitakuwa shwari.” Aliniambia kwa upole huku akinichoma sindano.
“Unaonekana hupendi hii hali dokta...sasa kwa nini unafanya mambo haya?” Nilimuuliza huku nikiuma meno kutokana na uchungu wa sindano. Hakunijibu, badala yake alimgeukia yule nesi na kumpa maelekezo ya kunipa vidonge vitatu kila nitakapoamka kwa siku mbili zilizofuatia.
“Akiwa anaonesha upinzani ndio achomwe sindano, kwa sababu sindano ndio inafanya kazi haraka kuliko vidonge, ingawa zote zina nguvu sawa. Ila sindano zinaacha alama nyingi mwilini kiasi cha kuweza kuleta matatizo iwapo utafanyika uchunguzi baadaye.” Alimwambia yule nesi kwa sauti ya chini, nami nilimsikia kwa mbali. Nikianza kusikia macho yakiniwia mazito na masikio yakivuma.
Oh, Mungu wangu...jaalia hizi dawa zisifanye kazi...
Lakini niliona kuwa zilianza kufanya kazi nami nikaanza kujihisi hamu ya kuangua kicheko na kulia kwa wakati mmoja.
Oh, My God!
Nilimgeukia yule nesi na nikamuona akiyeyuka mbele ya macho yangu na kuwa mvuke. Nilitaka kupiga kelele lakini niliona mdomo wangu ukiwa mzito sana. Nilimtazama yule daktari aliyekuwa amesimama akinitazama na nikamuona akirefuka na kuwa mrefu sana. Nilitaka kupiga mayowe, lakini sasa niliuhisi ulimi wangu ukivimba na kujaa kinywa chote. Mama njoo unisaidie mwanao...nakufa....
Kiza kilitanda na kote kukawa kimya.
--

Nilipoamka sikuweza kujua kama ilikuwa usiku au mchana, kwani muda wote mle ndani kulikuwa kunawaka taa. Nilizungusha macho yangu huku nikihisi kichwa kikiniuma, lakini nikiwa na hisia kuwa kichwa changu kilikuwa kitupu kabisa! Yaani hakuna kitu chochote ndani ya ubongo wangu. Sijui inakuwaje hivyo, lakini kwa hakika hivyo ndivyo nilivyojihisi. Nilikuwa nimevalishwa gauni refu la kijani, kama yale ya hospitali,lakini lenyewe halikuwa limeandikwa jina la ile hospitali kama nilivyotajiwa na yule nesi, ambaye sikuwa na shaka kabisa kuwa alikuwa ni mfuasi wa yule mtu ajiitaye Martin Lundi. Nilitazama kule kwenye kabati refu lililokuwa ukutani kando ya mlango, nikahisi kuwa nguo zangu zilikuwa ndani ya kabati lile. Nilibaki kimya pale kitandani kwa muda mrefu na taratibu nilianza kuhisi akili yangu ikianza kufanya kazi. Nilikumbuka maagizo ya yule daktari aliyenichoma sindano kabla sijazama kwenye dimbwi la kiza kizito kuwa yule nesi anipe vidonge vitatu kila nitakapoamka kwa muda wa siku mbili mfululizo.
Kwa maana hiyo akili yangu haitapata muda wa kutulia na kufanya kazi sawasawa.
Niligeuka taratibu kule alipokuwa ameketi yule nesi akisoma kitabu chake, na kwa mara ya kwanza nikagundua kuwa yule nesi alikuwa amekaa mbele ya pazia maalum la hospitali, yale ambayo kama mtu akiwa anatakiwa kuchomwa sindano au kupatiwa tiba itakayomlazimu atoe baadhi ya nguo zake, huwa yanavutwa tu na kutoa faragha kwa mgonjwa na daktari. Hapo awali sikugundua hilo kutokana na rangi nyeupe ya lile pazia maalum kufanana sana na ile ya kuta za chumba kile.
Hawa watu walikuwa wameamua kunivuruga akili yangu kwa haya madawa yao, ambayo waliamini kuwa baada ya siku tatu yatanifanya nishindwe kabisa kubishana nao na badala yake nitawaeleza kila walilotaka...hasa juu ya ule mkanda wa video. Nilikuwa na hakika kabisa kuwa wakifanikiwa katika azma yao hiyo wataniua. Au wataniacha nikiwa mwehu kabisa, kama jinsi nilivyomsikia yule daktari akimuelezea Martin Lundi muongo juu ya athari ya zile dawa iwapo hazitawekwa kwa vipimo maalum.
Martin Lundi muongo angependa sana hali hiyo itokee, kwani ingenifanya kweli nionekane mwenda-wazimu na kwamba ndiye niliyefanya yale mauaji kule msituni, na hapo hakuna hata mtu mmoja ambaye angenisikiliza.
Mungu wangu!Hawa watu mbona wabaya hivi!
Nilimtazama nesi Tamala, nikaona alikuwa amekaa kwenye kile kiti chake akiwa anasoma kile kitabu chake cha hadithi, na kando yake juu ya meza kulikuwa na bilauri yenye soda ilhali kando ya ile bilauri kukiwa na chupa ya mirinda iliyokuwa imebakiwa na robo ya soda ndani yake.
Nilifinya macho na kukitazama tena kile kitabu.
Kilikuwa ni kitabu kipya kabisa cha Danielle Steel, ambaye hata mimi hupenda sana kusoma vitabu vyake.
Lakini kile kitabu ni cha karibuni sana na hakikutungwa mwaka 99!
Ndio maana nilikuwa nashindwa kuelewa juu ya ile kalenda ya mwaka 99 kuwamo mle ndani na yule nesi kuniambia kuwa ule ulikuwa ni mwaka 1999.
Shit! Mwaka 1999 mimi ndio nilikuwa naanza masomo Chuo Kikuu...!
Hata ile simu iliyokuwa ikining’inia shingoni kwa yule nesi haikuwa toleo la mwaka 99, kwani kwa kadiri nilivyoelewa, mwaka 99 simu aina ya Nokia 2100 ilikuwa bado haijatengenezwa.
Hawa watu wanataka kunifanya kichaa...ee mwenyezi mungu nisaidie kiumbe wako!
Kwa mara nyingine tena nilistaajabia umakini wa akina Martin Lundi katika kupanga maasi yao. Sasa nilielewa kabisa kuwa kuwekwa kwa ile kalenda mle ndani, na wale watu kuniita kwa jina lisilokuwa langu, ilikuwa ni mbinu yao ya kuzidi kunichanganya na kunivuruga akili. Mvurugiko huu ukichanganywa na hizi dawa wanazonishindilia akilini mwangu kwa hakika ungenifanya nishindwe kabisa kuelewa ukweli ni upi na uongo ni upi, hata nikiambiwa kuwa jina langu lilikuwa ni Jennifer Lopez mimi ningeamini tu, wachilia mbali hiyo kuambiwa kuwa eti mimi ni Sylvia vitu gani tu sijui huko...!(Nilisonya)
Bila shaka nesi Tamala alisikia jinsi nilivyosonya, naye akashusha kitabu chake na kuniangalia kwa makini.

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 31.

Hawa watu wanataka kunifanya kichaa...ee mwenyezi mungu nisaidie kiumbe wako!
Kwa mara nyingine tena nilistaajabia umakini wa akina Martin Lundi katika kupanga maasi yao. Sasa nilielewa kabisa kuwa kuwekwa kwa ile kalenda mle ndani, na wale watu kuniita kwa jina lisilokuwa langu, ilikuwa ni mbinu yao ya kuzidi kunichanganya na kunivuruga akili. Mvurugiko huu ukichanganywa na hizi dawa wanazonishindilia akilini mwangu kwa hakika ungenifanya nishindwe kabisa kuelewa ukweli ni upi na uongo ni upi, hata nikiambiwa kuwa jina langu lilikuwa ni Jennifer Lopez mimi ningeamini tu, wachilia mbali hiyo kuambiwa kuwa eti mimi ni Sylvia vitu gani tu sijui huko...!(Nilisonya)
Bila shaka nesi Tamala alisikia jinsi nilivyosonya, naye akashusha kitabu chake na kuniangalia kwa makini.
“Njaa...” Nilimwambia yule nesi kwa sauti iliyokoroma naye alinijia haraka na kuanza kunisemesha kinafiki kama kwamba ni nesi anayejali afya yangu, nami nikamnyamazia tu. Aliniandalia chakula ambacho nilikishambulia kwa nguvu kwani hakika njaa ilikuwa ikiniuma.
“Saa ngapi...?” Nilimuuliza. Alingalia saa kwenye simu yake na kuniarifu kuwa muda ulikuwa ni saa sita usiku. Nilijaribu kupiga hesabu kuona iwapo ilikuwa ni sawa au alikuwa akinidanganya. Sikupata jibu la haraka, na mara hiyo nesi Tamala akaniletea vidonge vitatu nimeze. Nilivipokea bila ubishi na kuvitupia kinywani mwangu huku nikipokea bilauri ya maji kutoka kwa yule nesi. Nilikunywa yale maji na kumrejeshea ile bilauri nami nikajilaza kitandani huku nikifumba macho. Nilisikia hatua za yule nesi zikielekea mezani kurudisha ile bilauri nami nikafumbua macho kumtazama na nilipoona amenigeuzia mgongo kuelekea kule kwenye meza, nilivitoa haraka sana vile vidonge kutoka chini ya ulimi na kuvitemea kiganjani mwangu. Nesi Tamala aliweka ile bilauri na kunigeukia, nami nikamtazama huku nikipeleka mkono wangu na kuviweka vile vidonge chini ya mto niliolalia bila yeye kuelewa kilichofanyika.
“Kulala sasa binti! Au unataka sindano?” Alinisemesha kama anayeongea na mgonjwa wa akili, nami nikamtukana tusi kali la nguoni kisha nikatema mate sakafuni kwa hasira. Yule nesi alitabasamu akiamini kuwa zile dawa zilikuwa zimeanza kufanya kazi, wakati mimi nilikuwa nimemtukana kwa dhati hasa kwani alinikera kupita kiasi na nilitema mate ili nisimeze mabaki ya zile dawa nilizokuwa nimezificha chini ya ulimi wangu.
Nilijilaza tena kitandani na kufumba macho, nikijitahidi kutafuta usingizi huku moyo ukinidunda, nikijua kuwa yule mtu anayejiita Martin Lundi alikuwamo ndani ya jengo lile, akisubiri kuja kunihoji baada ya zile dawa kufanya kazi...baada ya siku mbili.
Lazima nitoroke hapa kabla ya muda huo!
Nilibaki nikiwa nimejilaza pale kitandani huku nikiwa nimefumba macho kwa muda mrefu, nikijaribu kutafakari namna ya kujikwamua kutoka katika mtego ule. Kitu kilichonikosesha amani katika hali ile ni ile mikanda maalum iliyonibana pale kitandani,kwani nikiwa nimetulia haisumbui lakini muda nikianza kujikurupusha tu inakaza na kunibana kabisa pale kitandani.
Nitajitoaje hapa?
Hatimaye nilipitiwa na usingizi.

--

Asubuhi baada ya kunipatia chai, na yule nesi alinipa tena vidonge vitatu vya ile dawa. Nilifanikiwa kutumia mbinu ile ile ya kuvificha chini ya ulimi na kupitisha maji juu ya ulimi wangu na kuyameza nikiacha zile dawa chini ya ulimi bila yule nesi kugundua. Muda mfupi baadaye yule daktari alikuja na kunifanyia uchunguzi katika mapigo yangu ya moyo, na kuniwekea kipimo maalum kichwani huku akisikiliza mienendo ya ubongo wangu kwa kuweka visikilizio maalum masikioni mwake. Moyo ulikuwa ukinienda mbio sana kwani nilijua kuwa yule mtaalam atagundua kuwa sikuwa nimemeza dawa yoyote tangu alipoondoka siku iliyopita. Nilimuona akikunja uso kwa kutafakari matokeo ya uchunguzi wake.
“You are very resistant young lady(U-msichana mbishi sana)...itabidi nikuongezee dozi, ingawa nisingependa kabisa kufanya hivyo.” Alisema kwa sauti ya chini kuniambia, akimaanisha kuwa mwili wangu ulikuwa unatoa upinzani mkubwa kwa zile dawa, hivyo itabidi aniongezee dozi. Niliona wazi kuwa alikuwa akijisemea mwenyewe, kwani kwa uelewa wake, mimi nisingeweza kuelewa chochote katika yale aliyoyasema.
We’ ongeza dozi kadiri utakavyo, lakini ujue mi’ simezi hata kidonge kimoja katika hizo dawa zako!
Nilizidi kumtazama tu bila ya kusema neno. Yule daktari alinitazama kwa muda mrefu.
“Kwa nini usiwape tu hicho wanachotaka msichana? Inaweza kukupunguzia matatizo mengi tu!” Aliniambia kwa upole huku akiamini kuwa ingawa nilikuwa nikimtazama, akili yangu ilikuwa haielewi chochote katika maneno yale. Yaani ilikuwa kama anaendelea kujisemea mwenyewe.
Oh, Yeah? Una hakika kuwa kaburini huwa hakuna matatizo? Unadhani Martin Lundi ataniachia nitembee huru mitaani baada ya kumpatia hicho anachotaka?
Badala ya kumjibu nilifumba macho na kugeuza uso pembeni, nikimsikia yule daktari akimwambia yule nesi kuwa nikiamka aongeze kidonge kimoja katika dozi zangu zilizobaki.
Sawa. Vyote hivyo vitaenda chini ya mto.
Yule dokta alitoka na kutuacha na nesi Tamala nami nikajitia nimelala, lakini akili yangu ilikuwa ikifanya kazi haraka sana. Nilijua kuwa ni lazima nitoke mle ndani, lakini kila nilipojaribu kutafuta namna ya kutoka nilishindwa kupata jibu. Nilijiuliza iwapo ile hospitali ilikuwa na yule mhudumu mmoja tu na daktari wake, kwani nilitegemea kuona manesi wakibadilishana, lakini tangu nimekuja nilikuwa na nesi yule yule na hata pale nilipokuwa nimejilaza kitandani nikimtupia jicho la wizi, yule nesi hakuwa na dalili za kuondoka. Je, hana mume na watoto? Kwa nini asirudi kwa familia yake na kumuachia nesi mwingine akae na mimi?
Baada ya kupata mlo wa mchana, nilimuomba yule nesi anipeleke chooni, nikitarajia kutolewa nje ya chumba kile, lakini badala yake, yule nesi alinifungua kutoka pale kitandani na kunipeleka nyuma ya lile pazia maalum, kama yale yanayopatikana katika mahospitali mengi, ambako huko kulikuwa kuna mlango mwingine wa kioo na kando ya mlango ule kulikuwa kuna meza iliyokuwa na vifaa vingi vya upasuaji pamoja na chupa kadhaa za dawa. Lakini kilichoyavutia macho yangu zaidi ilikuwa ni simu iliyokuwa juu ya ile meza pamoja na vile vitu vingine. Nesi Tamala aliniingiza chooni na kunisimamia wakati nikijisaidia, kisha alinirudisha tena kitandani na kunifunga na ile mikanda, lakini wakati huu nilishajua ni jinsi gani ya kuifungua bila ile mikanda kunibana zaidi.
Alinipa vidonge vinne nami nikatumia ujanja ule ule na kuvificha chini ya mto, kisha nikajilaza kitandani wakati nesi Tamala akifungua soda nyingine ya mirinda na kuanza kusoma kitabu chake.
Nilipokisia kuwa muda ulikuwa umefikia saa kumi na moja za jioni nilijitia kuamka. Nesi Tamala kuona hivyo alinishindilia tena vidonge vingine vinne, nami nikavificha chini ya mto. Nilikuwa nimepata muda wa kutafakari mustak-bali wangu kwani nilijua kuwa Martin Lundi angenijia siku iliyofuata kupata majibu ya maswali yake, akiamini kuwa zile dawa zitakuwa zimenilevya na kunipumbaza kiasi cha kum-miminia majibu kwa kila swali atakaloniuliza, kubwa likiwa ni wapi nilipouficha ule mkanda wa video.
Sasa ole wake yule daktari atakapokuta kuwa zile dawa hazijafanya kazi ipasavyo, na nilitamani sana kuona jinsi nesi Tamala atakavyohamanika pindi ikigundulika kuwa kumbe sikuwa nikimeza vile vidonge alivyokuwa akinipa.
Lakini la muhimu kuliko vyote lilikuwa ni namna ya kutoka mle ndani.
Nilimuomba tena yule nesi anipeleke chooni, naye alinifungua kutoka pale kitandani huku akinisimanga kwa tabia yangu ya kubugia “mimaji mingi” wakati wa kumeza dawa halafu naanza kumsumbua kwenda chooni kila mara.
Nilikuwa natembea kwa taabu kidogo ili kumfanya nesi Tamala aone kuwa nilikuwa nayumba kutokana na dawa nilizomeza, naye alinishika mkono kuniongoza chooni. Tulipofika usawa wa ile meza yake ambapo alikuwa ameweka kile kitabu chake na bilauri yake ya soda, niliachia mkojo ukinipita hadi sakafuni na kujitia kushangaa kibwege huku nikiinama kuangalia jinsi nilivyojikojolea.
“Aaaah! Unaona sasa! Yaani umeshindwa kujikaza we binti...?” Nesi Tamala alinikemea kwa kero huku naye akiinama kutazama jinsi nilivyojikojolea. Na huo ndio wasaa niliokuwa nikiusubiri, kwani haraka sana nilitumbukiza vidonge vyote nilivyovitoa chini ya mto wangu, ambavyo muda wote nilikuwa nimevifumbata kwenye kiganja cha mkono wangu, ndani ya ile bilauri yake ya soda.
“Hebu sogea huko sasa! Na ukianza kunipa kazi za kupiga-piga deki humu tutakorofishana sasa hivi!” Alinikemea huku akinisogeza pembeni nami nikabaki nikiwa namtazama tu, nikijitia bwege niliyepumbazwa na madawa aliyokuwa akinimezesha, moyoni nikiombea asiinuke kabla zile dawa hazijayeyuka vizuri ndani ya ile soda yake.
“Kubwa zima kazi kujikojolea tu...kama mtoto bwana! Sasa bado kujinyea tu!” Alizidi kunikemea kwa hasira nami nilishindwa kujizuia, nikaanza kumcheka huku moyoni nikiona raha kumsumbua namna ile. Alinitupia jicho la hasira kwa muda, lakini hiyo ilinifanya nizidi kumcheka, naye akaona kuwa tayari nilikuwa nimesharukwa na akili kutokana na zile dawa.
“Lione kwanza, na utabaki hivyo hivyo! Hebu vua hilo gauni huko nikutafutie jingine!” Alinikemea huku akifuta ile mikojo kwa ufagio maalum wa kupigia deki. Niliacha kucheka na kuanza kuvua lile gauni taratibu bila ya kusema neno, safari hii nikijitahidi kujifanya bwege kadiri nilivyoweza huku moyo ukinienda mbio sana, kwani vile vidonge vilikuwa vinakawia kuyeyuka.
Itakuwaje iwapo atagundua nilichokifanya?
Nesi Tamala aliweka pembeni lile fagio na kwenda moja kwa moja hadi kwenye lile kabati la nguo la ukutani na kulifungua nami nilitumia muda aliokuwa amenigeuzia mgongo kuichukua ile bilauri yake ya soda na kuitikisa kidogo ili vile vidonge viyeyuke haraka. Nesi Tamala aligeuka kutoka kule kabatini akiwa na gauni jingine kama lile wakati nikirudisha mkono wangu baada ya kuitikisa ile bilauri. Aliona kitendo cha mkono wangu na alianza kupata wasiwasi, akinitazama usoni na kunitazama mkononi mwangu, akidhani kuwa nilikuwa nimechukua kitu fulani kutoka pale mezani, nami hapo hapo nilijitia kuingiwa na kizunguzungu na kujiyumbisha huku nikirembua macho kama ninayetaka kupiga mwereka nikipeleka ule mkono alioutilia mashaka kwenye paji langu la uso. Haraka sana alinikimbilia na kunidaka, kisha akaniburuza hadi kitandani huku mimi nikiwa nimejilegeza kabisa. Huku akigumia kwa taabu, yule nesi alinivika lile gauni jingine na kunilaza kitandani, ambapo nilijitia kupitiwa na usingizi moja kwa moja, huku nikisikilizia jinsi hatua zake zilivyokuwa zikitembea mle ndani na kwenda tena hadi pale kabatini kwani nilisikia milango ya lile kabati ikifungwa, kisha nikasikia hatua zake zikitembea na kusikia mlango wa kule chooni ukifunguliwa na maji yakitiririka kutoka bombani.
Kaa basi unywe hiyo soda!
Moyo ulikuwa ukinipiga kwa nguvu sana na nilitamani kufumbua macho nimtazame harakati zake, lakini nilijilazimisha kujitia nimelala ili yule nesi asiwe na shaka kabisa. Hatimaye nilisikia hatua za yule nesi zikiishia pale kwenye kiti chake naye akijibwaga juu yake. Kimya kilitawala ndani ya kile chumba. Nilifumbua jicho kwa chati na kumuona nesi Tamala akiwa kwenye kiti chake akisoma kitabu ilhali ile bilauri yake ya Mirinda ikiwa pale pale juu ya meza.
Hebu kunywa hiyo soda basi we’ mwanamke!
Nililala nikimchungulia namna ile kwa muda mrefu, lakini ilionekana kama kwamba yule nesi alikuwa amesahau kabisa juu ya ile soda. Nikaanza kupata wasiwasi, kwani nilijua kuwa muda wowote yule daktari angekuja kuangalia maendeleo yangu na huenda yule nesi akaona kuwa ile soda imekaa sana na kuimwaga.
Nilipokuwa nimekata tamaa kabisa, Nesi Tamala aliinua ile bilauri na kubugia soda yote iliyobaki na kuijaza tena ile bilauri kwa kumimina kiasi cha soda kilichokuwa kimebaki kwenye chupa. Aliiweka ile bilauri mezani naye akarudia kusoma kitabu chake, akiachia mbwewe kubwa. Nilishusha pumzi za faraja na kujilaza kimya nikisubiri matokeo, kwani nilijua jinsi zile dawa zilivyokuwa zikifanya kazi, lakini kwa idadi ya vile vidonge nilivyommiminia yule nesi, sikujua nitarajie kitu gani.
Nesi Tamala alikuwa amebugia zaidi ya vidonge kumi kwa mpigo!
Nilibaki nikiwa nimelala pale kitandani nikimkodolea yule mwanamke aliyebugia vidonge vingi vya kupumbaza akili huku nikikumbuka maneno ya yule daktari alipokuwa akimuelezea madhara ya kutumia zile dawa kinyume na maelekezo.
... Unless you want the poor girl to go completely mad...or even die! (...Isipokuwa kama unataka huyu msichana awe mwehu kabisa...au hata afe!).
Mungu wangu! Anaweza kufa huyu mama...
Mara yule nesi aliinuka ghafla, kitabu kikimtoka mikononi na kuanza kumanga manga mle mdani bila uelekeo maalum. Alitumbua macho na kuanza kukoroma huku akinitazama kwa macho ya woga, akijishika koo na kuanza kuyumba huku akinijia pale kitandani nilipokuwa nimelala nikimkodolea macho kwa woga huku moyo ukinienda mbio.
“We..we! Umeni...fanya ni-ni?” Alinikemea kwa taabu huku akizidi kunisogelea, miguu yake ikigongana na povu likianza kumtoka kinywani. Alipiga yowe kubwa huku akinitumbulia macho na akinyoosha mbele mikono yake yote miwili kuielekeza pale nilipokuwa nimelala.
Oh! My God, anakuja kunikaba sasa! Na mimi nimefungwa hapa kitandani...amewehuka nini ?
Nilianza kuhangaika kujifungua lakini mikono ilikuwa ikitetemeka vibaya sana, na ghafla nilimuona nesi Tamala akisimama wima na kukauka kama gogo huku akiwa ametumbua macho akitazama moja kwa moja kule ukutani kulipokuwa na kalenda ya mwaka 1999. Kwa jinsi alivyokuwa ametumbua yale macho,ni wazi alikuwa haoni chochote. Kisha alijibwaga mzima mzima sakafuni kwa kishindo kikubwa.
Kimya kilitawala.
Nilibaki nikiwa pale kitandani kwa muda mfupi tu, kisha nilijikurupusha kutoka kwenye ile mikanda na kuliendea lile kabati lililokuwa ukutani, nikiuruka mwili uliokauka wa yule nesi pale sakafuni. Nilitoa nguo zangu na kuanza kuzivaa haraka haraka. Kisha nilikimbia kule nyuma ya pazia na kuikamata ile simu na bila kufikiri zaidi, nilianza kuipiga namba ya John Vata huku mikono ikinitetemeka na moyo ukinienda mbio.
“John Vata!” Niliisikia sauti yake ikijibu simu upande wa pili na moyo wangu uliyeyuka kwa faraja.
“Oh! Kamishna! Oh...thank God! Msaada Kamishna!. Nisaidie! Niko matatani... nimetekwa!” Nilipayuka haraka haraka kwenye ile simu huku nikipeleka macho kwa yule nesi aliyelala pale sakafuni bila fahamu.
“Nani...Tigga...?”
“Ndio Kamishna..ni mimi Tigga. Wameniteka! Na sasa wananilisha dawa za kunivuruga akili ili nichanganyikiwe! Oh! Mungu wangu sijui nitafanyaje...
“Tigga, hebu tulia kwan...”
“Naomba uje uniokoe Kamishna! Naogopa sana...mambo haya ni magumu sana kwangu...”
“Hebu tulia basi, ebbo!Ni nani waliokuteka na uko wapi?” John Vata alinikemea, nikajilazimisha kutulia na kuongea kwa utulivu.
“Nimetekwa na nimeletwa kwenye hospitali fulani...Nightingale Memorial Hospital...sijui iko wapi...”
“Hakuna hospitali ya jina hilo hapa jijini. Ni nani waliokuteka, unawafahamu?”
“Martin Lundi! Na mwenzake daktari...”
“Tigga! Tulishapitia huo mchezo wa Martin Lundi! Nimeshakwambia kuwa Dr. Martin Lundi ni mzee wa miaka sabini na nilikwambia uache kabisa kunifanyia mchezo mimi...”
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 32

“Hebu tulia basi, ebbo!Ni nani waliokuteka na uko wapi?” John Vata alinikemea, nikajilazimisha kutulia na kuongea kwa utulivu.
“Nimetekwa na nimeletwa kwenye hospitali fulani...Nightingale Memorial Hospital...sijui iko wapi...”
“Hakuna hospitali ya jina hilo hapa jijini. Ni nani waliokuteka, unawafahamu?”
“Martin Lundi! Na mwenzake daktari...”
“Tigga! Tulishapitia huo mchezo wa Martin Lundi! Nimeshakwambia kuwa Dr. Martin Lundi ni mzee wa miaka sabini na nilikwambia uache kabisa kunifanyia mchezo mimi...”
“Lakini sio mchezo Kamishna Vata! Ni kweli huyu mtu anayejiita Martin Lundi ameniteka na hivi niongeavyo wanafanaya bidii ya kunimezesha vidonge vya...”
“Sasa mbona unaongea na simu...wao wako wapi?”
“John Vata naomba unielewe! Hapa nimefanikiwa kumdhibiti nesi anayenisimamia humu ndani ya wodi,naomba unisaidie kabla yule mtu anayejiita Martin Lundi na yule daktari mwingine hawajanikuta humu ndani!” Nilimjibu kwa kiherehere huku nikibubujikwa machozi.
“Kwa mwenendo wa tabia uliyoonesha kwangu Tigga, inaniwia vigumu sana kukuamini.”
“Tafadhali naomba uniamini Kamishna na unisaidie! Please!” Nilimwambia na hapo hapo niliangua kilio. Nililia kwenye simu, nikimlilia John Vata aje anisaidie. Huwezi kuamini.
“Okay..Okay! Sasa...unaweza kujua hapo ulipo ni wapi?” Aliniuliza kwa sauti ya upole lakini iliyojaa uharaka ulioonesha kuwa alikuwa amelitilia umuhimu ombi langu. Sikujua niko wapi, na nikamweleza hivyo huku nikipeleka macho kule mlangoni. Bado kulionekana shwari.
“Okay, Tigga. Unaweza kuchungulia dirishani na kuniambia hiyo hospitali iko jirani na jengo au eneo gani?” Aliniuliza, nami nilimjibu kuwa niliweza na kuivuta ile simu kuliendea dirisha, lakini waya wa ile simu ulikuwa mfupi. Nilimwambia asubiri na nikaiweka sakafuni ile simu na kukimbilia dirishani. Niliangaza nje lakini kulikuwa kuna ukuta mrefu tu ulioizunguka ile nyumba, na nje ya ukuta ule kulikuwa kuna miti mirefu ya mi-Ashok, ambayo ilinizuia kuona kitu chochote nje ya ukuta wa ile hospitali.
“Shit!” Nililaani jambo lile na kuangaza mle ndani kwa fadhaa. Hakukuwa na dirisha jingine zaidi ya lile. Nilirudi kwenye simu na kumueleza Kamishna Msaidizi John Vata.
John Vata alionekana kutilia mashaka jibu lile.
“Dah! Sasa...Lakini Tigga, are you sure about all this? Isn’t this one of your tricks?” (...una uhakika na yote haya unayonieleza? Je hii si moja kati ya laghai zako?)
“Oooh Kamishna Vata! Mimi sina laghai zozote! Ninachokuambia ni kweli tupu! Naomba ujaribu kuniamini, kwani kama wakifanikiwa kunivuruga akili, hata wewe hutaweza kufanyia kazi ushahidi nitakaokupa kuhusiana na mauaji ya kule msituni...na wauaji wa kweli watabaki wakitembea tu mitaani na bila shaka kuua tena na tena. Is that what you want?” (...Je, hilo ndilo unalotaka litokee?)
“Of Course not! Lakini wewe umekuwa na tabia ya kunichengachenga sana kila nilipokuwa nikikutaka ujitokeze...sasa leo ghafla unanitafuta eti nije kukusaidia, halafu wewe mwenyewe hujui uko wapi! Unategemea mimi nielewe vipi?” John Vata aliniuliza kwa sauti ya utulivu mkubwa, nami nikajua kuwa alikuwa amechukia.
Nilizidi kuogopa.
“Please Kamishna Vata. Hatuna muda wa kubishana...tayari niko kwenye wakati mgumu bila ya hizo shutuma zako. Wewe ni afisa wa jeshi la polisi, tena wa ngazi ya juu kabisa. Nimekuletea ombi langu la kuomba msaada wa kuokoa maisha yangu. Sasa hata kama huniamini, naomba tu utimize wajibu wako kama afisa wa usalama...hata sio lazima uje wewe mwenyewe. Unaweza hata kutuma askari walio chini yako waje wanisaidie, kwa sababu najua kuwa hawa watu wabaya wakifanikiwa kujua wanachokitaka kutoka kwangu...they will kill me!” (...wataniua!) Nilimjibu kwa kirefu huku nikitiririkwa na machozi.
“Kwa hiyo unataka kuniambia nini Tigga?” Aliniuliza kwa utulivu mkubwa sana, nami nikajua amezidi kuchukia, lakini sikujali. Shit! Yeye ni afisa wa polisi, na ni wajibu wake kunilinda mimi kama raia, hata kama hanipendi au hataki.
“Wakiniua, damu yangu itakuwa mikononi mwako John Vata!” Nilimwambia kwa hasira.
“Unanitishia?” John Vata aliniuliza kwa hasira. Niliamua kurudi chini.
“Nakuomba Kamishna John Vata! Nakuomba unisaidie. Kwa sasa sina mtu yeyote wa kunisaidia hapa duniani isipokuwa wewe...niamini tafadhali!” Nililia huku nikimbembeleza yule afisa wa polisi ambaye hapo mwanzo sikuweza kumuamini kabisa. Kimya kilitawala kutoka upande wa John Vata.
“Kamishna? Bado upo...? hatuna muda, nisaidie tafadhali!”
“Okay...lakini nitakusaidiaje Tigga? Hatujui uko wapi! Hatujui ni watu gani waliokuteka...”
“Wewe ni askari John Vata! Tafuta namna ya kunisaidia...mimi akili yangu inashindwa hata kufikiri sawasawa sasa!” Nilibwabwaja huku nikilia.
“Okay...nimeshaipata namba yako. Nitakupigia. Just...you wait right there!” (...wewe subiri tu hapo hapo!)
“Lakini muda sasa, Kamishna...!” Nilimwambia kwa kiherehere, lakini alikuwa ameshakata simu.
Kilichofuata kilikuwa ni kipindi kigumu miongoni mwa nyakati ngumu nilizowahi kukabiliana nazo maishani mwangu. Niliona kuwa Kamishna John Vata aliamua kunitosa katika swala lile. Vije aseme nisubiri anipigie simu katika mazingira kama yale? Ana mpango gani? Vije itakuwa iwapo ataamua kupiga simu ile wakati wale wauaji wamo mle ndani? Na kwa nini apige simu? Swala lile lilikuwa halihitaji simu! Lilihitaji askari kuvamia ile hospitali na kufanya msako wa wodi mpaka wodi hadi wanikute na wanitoe mle ndani na kuwaweka chini ya ulinzi wahudumu wote wa ile hospitali na viongozi wao, akiwemo Martin Lundi muongo. Sasa yeye anasema nisubiri anipigie simu...huyu ni Kamishna kweli au naye ndio wale makamishna wa kubebwa bebwa tu?(Nilisonya).
Siwezi kukaa tu kiwete wete hapa nikisubiri Kamishna wa Polisi aitwaye John Vata anipigie simu!
Nilikurupuka mpaka pale mlangoni na kujaribu kuufungua lakini ulikuwa umefungwa kwa funguo, na nje ya ule mlango wa kioo niligundua kwa mara ya kwanza kuwa kulikuwa kuna mlango mwingine wa chuma. Nilitoa sauti ya ghadhabu, kisha nikarudi kwa yule nesi aliyelala pale sakafuni. Nilianza kumpekua mwili wake nikitafuta funguo za ile milango. Nilikuta funguo mbili zilizobanwa pamoja ndani ya sidiria yake.
“Yes!” Nilijisemea kwa ushindi na kurudi tena pale mlangoni na kuanza kuingiza moja ya zile funguo kwenye tundu ya funguo pale mlangoni, lakini nilibaki nikiwa nimeduwaa.
Kile kitasa kilikuwa na tundu mbili zilizofanana za kuingizia funguo! Nilitazama zile funguo zilizokuwa mkononi mwangu. Zilikuwa ni funguo aina mbili tofauti! Nini maana yake hii? Niliingiza funguo moja ikagoma, nilipojaribu nyingine ikakubali kufungua kitasa cha moja kati ya zile tundu mbili. Ile nyingine ikagoma kabisa kuingia kwenye ile tundu nyingine. Nilijaribu kufungua ule mlango, lakini hata haukutikisika. Mungu wangu! Sasa nitafanyaje? Nilihamanika kuliko kawaida. Nilichungulia kule kwenye ule mlango mwingine wa chuma, nao nikaona kuwa ulikuwa na tundu mbili za kuingizia funguo.
“Pumbavu! Sasa hii ndio nini...?” Nilifoka kwa hasira, huku nikielewa ile hali iliyojitokeza. Ilimaanisha kuwa nesi Tamala alikuwa na ufunguo mmoja tu kwa kila mlango, na ili aweze kufungua ile milango, ilibidi na mtu mwingine, aidha yule daktari mtu mzima au Martin Lundi muongo, naye afungue kwa funguo nyingine katika zile tundu za pili zilizokuwa katika kila mlango. Hii ilinionesha ni jinsi gani Martin Lundi muongo alivyodhamiria kutofanya makosa kabisa katika kuupata ule mkanda wenye ushahidi dhidi yao kutoka kwangu. Na kwa kufanya hivyo alikuwa amenizidi kete kwa mara nyingine tena.
“Aaah! Jamani! Sasa...sasa...” Nililia kwa uchungu na maneno yakanikaba kooni, sikuweza hata kuendelea kusema. Nilirudi tena kwa yule nesi na kumpekua upya, lakini hakukuwa na funguo nyingine. Nikaenda kule nyuma ya ile pazia na kupekua kwenye droo za ile meza iliyokuwako kule lakini nako hakukuwa na kitu. Nilikuwa nimenasa.
Sasa nifanye nini?
Nilirudi na kumtazama yule nesi aliyelala pale sakafuni. Niliona alikuwa akipumua kwa taabu sana, na nikaona kuwa kwa pale alipokuwa ameangukia, mtu yeyote akichungulia tu kwenye ule mlango wa kioo angeweza kumuona moja kwa moja. Nilianza kumuinua na kumburuzia pale kitandani, lakini alikuwa mzito sana kwangu. Nilikiendea kile kitanda na kufyatua vizuio maalum kutoka kwenye matairi yaliyokuwa kwenye miguu ya kile kitanda na kukisukumia pale alipokuwa ameangukia yule mwanamke. Kwa taabu sana nilifanikiwa kumlaza chali pale kitandani. Nilimfunga kwa ile mikanda maalum iliyokuwa kwenye kile kitanda na kumfunika kwa shuka mpaka usoni, nikiacha sehemu ya pua tu ili asikose hewa. Nilisimama kando ya kile kitanda nikimtazama huku nikitweta.
Na wewe uonje adha uliyokuwa ukinitia! (Nilimsonya)
Nilirudi kuchungulia kwenye kioo cha ule mlango. Kote kulikuwa kimya kabisa. Hakukuwa hata na pirika pirika za kawaida katika mahospitali. Hii hospitali gani? Kwanza ni hospitali kweli hii? Nilishitushwa kutoka kwenye mawazo yale na mlio mkali wa simu. Niliruka huku nikiropoka yowe la mshituko na kuikimbiia ile simu huku nikihisi kuwa ule mlio ungeweza kuwashitua watu wote waliokuwemo ndani ya jengo lile, hususan Martin Lundi muongo. Ilikuwa inaita muito wake wa tatu wakati nilipoifikia na kuikwapua.
“Hello...?” Nilisikia sauti ya John Vata ikiongea upande wa pili wa ile simu na kwa mara ya pili katika siku ile niliuhisi moyo wangu ukiyeyuka kwa faraja.
“Kamishna! Oh, Kamishna umenipigia kweli? Ahsante sana! Yaani nilikuwa...”
“Tulia Tigga, nilikuwa nataka kuhakikisha hiyo namba kama inakuja hapo unaposema kuwa upo. Endelea kusubiri.”
“Kamishna No! Usiniache....” Alikuwa ameshakata simu.
Nilijiona kuwa ninaelekea kupata wazimu. Hapo hapo nilianza kuipiga ile namba yake. Iliita mara kadhaa kisha ikakatwa bila kupokelewa.
“Shit! Shit! Shit!” Niliipiga tena ile namba, lakini safari hii ikawa imefungwa. Nilijibwaga sakafuni na kuagua kilio cha uchungu na kukata tamaa.
John Vata, una mpango gani na mimi? Kwa nini unanifanya hivi?
Nilikaa kule nyuma ya pazia kwa muda mrefu nikibubujikwa na machozi. Na hata machozi yaliponikauka, niliendelea kukaa kule nyuma ya pazia nikisubiri ujio wa yule daktari na hatima yangu, kwani nilikuwa na hakika kabisa yule daktari alikuwa na uwezo wa kuingia mle ndani bila hata ya kuhitaji funguo za nesi Tamala.
Baada ya muda ambao sikuweza kujua ulikuwa mrefu kiasi gani, nilisikia ule mlango ukifunguliwa. Nilihamanika na kuanza kutapa tapa nikiangaza huku na huko katika lile eneo nililokuwa nimejibanza. Nilikamata kisu kikubwa na kikali sana cha upasuaji kilichokua miongoni mwa vingi vilivyotapakaa juu ya meza iliyokuwa nyuma ya ile pazia. Huku Moyo ukinipiga kwa kasi sana nilichungulia kutokea kule nyuma ya pazia na niliona mlango ukifunguka na yule daktari mtu mzima akiingia mle ndani, macho yake yakienda moja kwa moja pale kitandani ambapo mwili wa nesi Tamala ulikuwa umefungwa na ile mikanda maalum naye akiwa hana fahamu, kisha akageukia ule upande kilipokuwa kiti cha nesi Tamala, na niliona uso wake ukitoa mikunjo ya mshangao.
“Eeee...Tamala! Tamala...?” Yule daktari aliita kwa sauti ya chini huku akianza kupiga hatua kuelekea ule upande niliokuwapo. Nilijizatiti nikiwa nimekishika kile kisu kwa mikono yangu yote miwili huku moyo ukinipiga kwa nguvu na woga ukinielemea.
Sasa nitamfanya nini na hiki kisu...nitamchoma kweli au...?
Alizidi kukaribia. “Nesi Tamala? Uko chooni...?”
Alitokeza nyuma ya ile pazia nami niliruka huku nikipiga ukelele wa mashambulizi, mikono yangu iliyokamata kile kisu ikiwa imeinuliwa juu tayari kuteremsha pigo la hatari. Yule daktari alitoa pumzi ya mshituko na hapo hapo aligeuka, na aliponiona uso wake uliingiwa na woga mkubwa. Haraka sana alijigeuza na kunikwepa, lakini wakati huo huo akiipiga ile mikono yangu kwa mikono yake yenye nguvu na kunisukuma pembeni. Ingawa alionekana mtu mzima, yule mtu alikuwa na nguvu za ajabu, kwani nguvu ya msukumo wake ilinitupa mbali naye kama unyoya. Nilipepesuka na kujipigiza ukutani huku nikitoa yowe la woga. Niliteleza na ule ukuta na kujibwaga sakafuni nikiwa nimekalia matako na kuinua uso wangu kwa woga kumtazama yule daktari.
Nilibaki nikiwa nimepigwa na butwaa nilipomuona yule daktari mtu mzima akiwa amesimama kishujaa ilhali kile kisu kirefu kilichokuwa mikononi mwangu kikiwa mikononi mwake. Sijui kilitokaje mikononi mwangu na kuhamia kwake, lakini nilijua kuwa katika ile sekunde aliyoipangusa mikono yangu kama unyoya, alinipokonya kile kisu kitaalamu sana!
“That was very foolish Tigga!(Huo ulikuwa ni ujinga mkubwa sana Tigga!). Ningeweza kukuua bure!” Alinikemea nami nilibaki nikiwa nimejikunyata pale sakafuni nikimtazama kwa woga mkubwa, akilini mwangu nikiamini kabisa maneno yake, kwani kama yule mtu ameweza kufanya kitendo cha haraka na ajabu namna ile, hakika asingeshindwa kuniua. Nilimeza funda la mate na kujaribu kujiinua kutoka pale sakafuni lakini yule daktari alipiga hatua moja kubwa na kuninyooshea kile kisu huku akinikemea tena kwa ukali.
“Kaa chini!”
Nilikaa huku nikitoa mguno wa woga. Yule Daktari alinitazama kwa mshangao uliochanganyika na hasira, macho yake yakielekea pale kitandani alipolala nesi Tamala na kunirudia.
“Umefanya nini we’ mtoto, umefanya nini?” Aliniuliza kwa hasira. Sikumjibu, badala yake niliendelea kumtazama kwa woga, moyo ukinienda mbio. Alimtazama nesi Tamala aliyelala pale kitandani bila fahamu. Alitukana tusi zito sana la nguoni, kisha alitikisa kichwa kwa kuchanganyikiwa na kunigeukia.
“Nijibu wewe binti! Ni nini ulichofanya na utarajia ufanywe nini sasa baada ya hapo eenh?” Aliendelea kunikemea, nami nikaamua kujitutumua na kuinuka taratibu kutoka pale sakafuni, nikimtazama kwa jeuri.
“Unajua ulichofanya wewe binti? Unajua...?
“Ndio! Ndio!” Nilimjibu kwa jazba, kisha nikaendelea. “Nimemshindilia huyo nesi wenu vidonge zaidi ya kumi vya ile midawa mliyokuwa mnatarajia mimi niibugie! Now do you have a problem with that?”(Sasa wewe una tatizo lolote juu ya hilo?)
Nilisikia sauti kwanza, halafu ndio nikaelewa kuwa nilikuwa nimezabwa kofi kali la shavu na yule daktari lililonipeleka na kunibamiza ukutani. Yaani sikupata hata nafasi ya kupiga yowe.
“Don’t talk to me like that young lady!(Usinijibu namna hiyo bi mdogo!) Hujui ni kitu gani ulichofanya wewe! Huyu mama anaweza kufa! Vidonge kumi? Oh, My God, wamekutoa wapi we’ mwanamke?” Alinikema huku akimnyooshea nesi Tamala. Nilijishika shavu langu huku nikihisi machozi yakinichonyota na shavu likinifukuta.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 33.

Nilisikia sauti kwanza, halafu ndio nikaelewa kuwa nilikuwa nimezabwa kofi kali la shavu na yule daktari lililonipeleka na kunibamiza ukutani. Yaani sikupata hata nafasi ya kupiga yowe.
“Don’t talk to me like that young lady!(Usinijibu namna hiyo bi mdogo!) Hujui ni kitu gani ulichofanya wewe! Huyu mama anaweza kufa! Vidonge kumi? Oh, My God, wamekutoa wapi we’ mwanamke?” Alinikema huku akimnyooshea nesi Tamala. Nilijishika shavu langu huku nikihisi machozi yakinichonyota na shavu likinifukuta.
“Oh, Yeah? Kwa hiyo mimi kufa ni sawa, ila huyo mama hapo si sawa, sivyo?” Nilimkemea huku nikibubujikwa na machozi.
“Ningekuwa na nia ya kukuua usingekuwa ukibishana na mimi hapa sasa hivi binti! Nia si kukuua, na ndio maana hukupewa vidonge kumi kwa mpigo mwanamke!”
“Sikutakiwa kupewa kidonge hata kimoja, Dokta! Na wala sikutakiwa kuwa hapa sasa hivi, Okay? Sasa kama wewe ungekuwa Daktari anayejali maadili ya kazi yake, usingeshiriki kabisa katika zoezi lote hili!” Nilimjibu kwa hasira. Yale maneno yalionekana kumchoma sana yule daktari mtu mzima. Alinitazama na kujaribu kusema neno, akaghairi. Akamgeukia yule nesi aliyelala pale kitandani, kisha akanigeukia.
“Hujui ulisemalo na wala huwezi kuelewa. Sasa Wagga akija hapa sijui itakuwaje...”
“Wagga...?”
Yule daktari alitikisa kichwa kwa masikitiko bila kusema neno. Nilibaki nikimtazama kwa utashi wa kupata habari zaidi.
“Wagga...ni nani? Ndio yule mtu unayemuogopa sana anayelazimisha nilishwe hizo dawa...?” Nilimuuliza.
“Kelele!” Alinikemea kwa hasira huku akininyooshea kile kisu kilichokuwa mkononi mwake.
“Don’t Move!”
Wote tuligeukia kule mlangoni ilipotokea ile sauti nyingine ambayo kwangu haikuwa ngeni. Kamishna Msaidizi John Vata alikuwa amesimama ndani ya kile chumba akiwa amekamata bastola mkononi mwake nami sikuamini kabisa macho yangu! Alikuwa amevaa suruali nyeusi na fulana nyeusi ya mikono mirefu. Miguuni alikuwa amevaa viatu vyeusi vya buti vilivyokuwa na soli za mpira. Yaani kumuona vile alivyokuwa akitusogelea taratibu huku akiwa amemuelekezea bastola yule daktari ilikuwa ni kama ndoto kwangu. Kwa mara ya tatu katika siku ile John Vata aliuyeyusha moyo wangu kwa faraja isiyo kifani. Chozi la furaha lilinitoka.
“Kamishna!” Nilipiga kelele huku nikikimbilia ule upande aliokuwepo na kumuacha yule daktari mtu mzima akiwa ameduwaa, akimtazama Kamishna John Vata kwa mshangao huku akiangusha kile kisu sakafuni. “Oooh Kamishna umekuja kuniokoa! Hukuniacha! Umewezaje kuigundua sehemu hii...? Oh! Mungu wangu...” Niliropoka kwa sauti iliyozongwa na kitetemeshi cha furaha.
“Namba ya simu. Nilifuatilia kumbukumbu za ile namba ya simu uliyotumia kunipigia huko Kampuni ya simu. Nikapata anuani kamili ya sehemu ilipo hii nyumba, utashangaa kutambua kuwa hii nyumba si hospitali wala nini!” John Vata alinijibu taratibu huku akiwa amemkazia macho na kuendelea kumnyooshea bastola yule daktari aliyekuwa ameduwaa, na alivyokuwa akiongea na kumtazama, niliona kuwa John Vata alikuwa amemtambua.
“Dokta Kashushu?” Alimwita huku akimsogelea taratibu, nikihisi mshangao katika sauti yake.
“U...unanifahamu mimi?” Yule Daktari alimuuliza kwa kitetemeshi huku akiinua mikono yake juu kujisalimisha.
“Yeah...Nakufahamu wewe ni nani! Wewe ni daktari bingwa wa magonjwa ya akili nchini baada ya kustaafu kwa Dokta Martin Lundi. Mimi ni Kamishna Msaidizi wa Polisi John Vata na kuanzia sasa uko chini ya ulinzi!” John Vata alimjibu kwa sauti ya utulivu sana, nami nikajua kuwa alikuwa amechukia kwa kiasi kikubwa. Nilimtazama yule daktari mtu mzima kwa mshangao.
Dokta Kashushu! Yaani kumbe huyu mtu ni Daktari bingwa wa magonjwa ya akili!Sasa inakuwaje akina Martin Lundi...Wagga...kama mwenyewe alivyomwita wakawa na uwezo wa kumshurutisha mambo kama haya namna hii?
Bila kusubiri zaidi Kamishna Msaidizi John Vata alichomoa pingu kutoka kwenye mfuko wa suruali yake na kunikabidhi, akiniamrisha nikamfunge zile pingu yule daktari. Nilimuendea yule daktari ambaye alikuwa amefadhaika ghafla na kuwa mnyonge sana. John Vata alikisogelea kile kitanda na kufunua ile shuka iliyomfunika nesi Tamala usoni huku bado bastola yake ikiwa imemuelekea Dokta Kashushu, nami nilimkamata mkono mmoja yule daktari na kumfunga ile pingu.
“Umenikatisha tamaa kabisa Dokta Kashushu! Sikutegemea kabisa kukuta mtu kama wewe sehemu kama hii!” John Vata alisema kwa uchungu, nami niliukamata mkono wa pili wa yule daktari ili niufunge sehemu ya pili ya ile pingu.
“I am not the bad guy Commissioner!” (Mimi sio mtu mbaya unayemtafuta Kamishna!) Dokta Kashushu alimjibu kwa upole huku akitia msisitizo maneno yake kwa mikono, na ule mkono wake wa pili nilioushika ukanitoka.
“Alaa! I had no idea! (Sikujua!) Wewe ni mtu mzuri sana, ulichofanya ni kumteka tu nyara huyu binti na kumtishia kwa kisu na kumfanyia vitu gani tu vingine, au sio?” John Vata alimjibu kwa kebehi iliyochanganyika na hasira. Niliuchukua tena ule mkono wa yule dokta kwa ajili ya kuufunga pingu.
“You don’t understand Commissioner...” (Wewe huelewi Kamishna..)
“Na ndio maana nakuweka chini ya ulinzi ili tukaeleweshane vizuri huko mbele ya safari...” John Vata alimkemea kwa hasira huku akichungulia kule nyuma ya ile pazia, ilhali bado akiwa amemuelekezea Dokta Kashushu bastola yake, lakini yule dokta hakuwa na dalili ya kutoa kipingamizi chochote. Mimi nilikuwa nimeugeuzia mgongo mlango na yule daktari alikuwa akielekea kule mlangoni, wakati Kamishna Msaidizi John Vata alikuwa amemuelekea Dokta Kashushu na akitembeza macho mle ndani.
Mambo yote yalitokea haraka sana.
Ghafla nilisikia kishindo kikubwa kikitokea nyuma yangu, na wakati huo huo nilimuona Dokta Kashushu akitoa macho akitazama kule mlangoni nami nikaanza kugeuka, lakini hapo hapo yule daktari bingwa aliuchomoa mkono wake kutoka kwenye himaya yangu na kunisukumia mgongoni kwake kwa mkono wake huku yeye akijisukuma mbele na akipiga kelele.
“Wagga Noooooo!”
Hapo hapo nilisikia milipuko mfululizo ya bastola na Dokta Kashushu akinikumba kwa nguvu na sote tukasambaratika sakafuni huku akitoa yowe la uchungu. Nilimsikia John Vata ikitoa ukelele wa ghadhabu nami nikajigeuza haraka pale sakafuni kushuhudia kilichokuwa kikitokea huku nikipiga kelele kwa woga. Na hata pale nilipogeuka, nilimuona yule mtu niliyekuwa nikimtambua kwa jina la Martin Lundi akiwa anamimina risasi kwa bastola mbili zilizokuwa mikononi mwake kuelekea kule alipokuwapo Kamishna Vata, na katika nukta ile nilipolitia lile tukio akilini mwangu, nilimuona John Vata akikisukuma kwa nguvu kile kitanda alicholalia nesi Tamala na kumbabatiza nacho Martin Lundi ukutani, ambaye alitoa yowe la maumivu huku bastola moja ikimtoka mkononi. Muda huo huo John Vata alirukia juu ya kile kitanda na akiwa amesimama juu ya kile kitanda bila kujali kama alikuwa akimkanyaga nesi Tamala, aliipiga teke bastola iliyobaki mkononi mwa yule muuaji muongo nayo ikatupwa pembeni, na hapo hapo Martin Lundi alimdaka mguu na kumvuta kwa nguvu. Wote wawili walipiga mweleka mzito hadi sakafuni, bastola ikimtoka John Vata mkononi. Wakati yote haya yakitokea nilikuwa nikipiga kelele kama mwehu, huku nikimsikia Dokta Kashushu akigumia kwa uchungu.
Nilimgeukia Dokta Kashushu aliyekuwa akigaragara sakafuni na kuona alikuwa amepigwa risasi ya bega la kulia na damu nyingi ilikuwa imemtapaka eneo la kifuani na begani mwake.
Ile risasi ilikuwa inipate mimi, na Dokta Kashushu alikuwa akijaribu kuniokoa na badala yake ikampata yeye!
“Oh, Dokta Kashushu! Umeni...yaani umepigwa kwa ajili yangu...!” Nilibwabaja huku nikijaribu kumsaidia kujiweka sawa pale sakafuni.
“Sikutaka mtu yeyote afe... na we’ unajua hilo! I am just sorry that things got out ofhand!” (Nasikitika tu kuwa mambo yamevurugika!).
“Aaah, Pole sana Dokta Kashushu..lakini kwa nini ulilazimika kushirikiana na Martin Lundi...?”
“Sio Martin Lundi yule! Dokta Martin Lundi ni mtu mzuri na aliyejitolea sehemu kubwa ya umri na ujuzi wake kwa ajili ya taifa hili! Huyu mshenzi sio Martin Lundi! Yeye ni Wagga Maingo! And he is a very bad guy!”(Na ni mtu mbaya sana!) Dokta Kashushu aliongea kwa hasira huku akiuma meno kwa maumivu ya jeraha lile, nyuma yangu purukushani za mpambano baina ya John Vata na Wagga Maingo ulikuwa ukiendelea.
Hii ilikuwa ni taarifa mpya kwangu. Kumbe yule muuaji anaitwa Wagga Maingo! “Sasa...sasa lile tukio la kule msituni lilikuwa linahusu nini Dokta...” Nilimuuliza yule daktari kwa kiherehere, lakini alinibadilishia mazungumzo.
“Sijui lolote juu ya hilo...Chana hii fulana msichana...tuangalie! Nadhani risasi imepita kwenye nyama, haikupiga mfupa...” Yule daktari bingwa aliongea kwa taabu, na wala hakuonesha kutilia maanani maneno yangu. Nyuma yangu niliendelea kusikia vishindo na mikiki mikiki ya mapambano baina ya John Vata na yule muuaji aliyeitwa Wagga Maingo, ambaye hapo mwanzo nilikuwa nikimtambua kama Dokta Martin Lundi. Hali hii ilinichanganya sana. Niligeuka na kutazama kilichokuwa kikiendelea nyuma yangu, na nilimuona John Vata akimshindilia Wagga teke la kifuani lililompeleka yule muuaji hadi ukutani ambapo alijibamiza kwa nguvu, yowe la uchungu likimtoka na niliona uso wake tayari ulikuwa umeshachakazwa kwa kipigo, kwani ulikuwa umetapakaa damu na umevimba. Mungu wangu John vata ni mtu hatari namna hii? Na hata pale nilipokuwa nikipitiwa na wazo lile, John Vata alimrukia kwa teke la kushindilia ili ambabatize zaidi pale ukutani, lakini Wagga aliwahi kujitupa pembeni na John Vata akautimba ukuta badala yake. Hapo hapo Wagga alimchota ngwara ule mguu wake uliobakia na Kamishna John Vata akaenda chini mzima mzima. Oh, Mungu wangu... Wagga alimrukia pale chini na kuanza kumkaba na hapo hapo Dokta Kashushu akanipigia kelele kwa hasira.
“Hebu chana hii fulana msichana, ebbo!”
Nilikurupuka na kujitahidi kuichana ile fulana nikashindwa. Nikachukua kile kisu kilichotupwa pale sakafuni na yule daktari na kuirarua ile fulana yake na kutazama lile jeraha. Ni kweli risasi ilikuwa imepita kwenye msuli wa bega lake na kutokea upande wa pili, ikiacha tundu baya lililokuwa likivuja damu iliyoniogopesha. Huku akitweta na kuuma meno kwa uchungu, Dokta Kashushu aliniagiza nikachukue vichupa vyote vya dawa nitakavyovikuta kwenye droo ya meza iliyokuwa nyuma ya ile pazia maalum iliyoigawa ile sehemu ya mwisho ya kile chumba, pamoja na bomba la sindano. Huku nikiwa bado nasumbuliwa akili yangu na mpambano baina ya Wagga Maingo na John Vata, nilifuata maagizo yake na kurudi pale alipokuwapo na vichupa vipatavyo vinne vya dawa ambazo sikuzitambua na kuviweka sakafuni kando ya Dokta Kashushu. Wakati huo nilimuona John Vata akimtupa pembeni Wagga Maingo na kujiinua kutoka pale chini walipokuwa wakigaragarazana. Wagga Maingo alijiinua haraka lakini John Vata alimwahi kwa teke kali la uso. Yowe lilimtoka Wagga Maingo naye akajipigiza kwenye kitanda alicholalia nesi Tamala na kupepesuka huku akijitahidi kusimama wima. John Vata hakumpa nafasi. Alimrukia teke jingine lililompata chini ya kidevu ambalo lilimrusha nyuma mzima mzima, sehemu ya nyuma ya magoti yake ikijipigiza kwenye kile kitanda naye akapinduka na kile kitanda mpaka sakafuni kwa kishindo kikubwa. John Vata alikuwa kama mbogo aliyejeruhiwa. Alikiruka kile kitanda na kumshukia Wagga Maingo kifuani aliyekuwa akijiinua kwa taabu kutoka pale sakafuni alipoangukia kwa miguu yake yote miwili.
“Msichana!” Dokta Kashushu aliniita kwa hasira, nami nikashituka na kumgeukia. “Hebu nisaidie hapa, huoni nashindwa...?” Alikuwa anajaribu kuweka dawa kwenye bomba la sindano bila mafanikio kwani mkono wake wa kulia ulikuwa hauwezi kufanya kazi kabisa. Nilichukua kichupa kimoja kati ya vile vilivyokuwa pale sakafuni na kuvuta dawa iliyokuwamo mle ndani kwenye lile bomba la sindano nikifuata maelekezo ya Dokta Kashushu kwamba ile dawa ijae kwenye lile bomba hadi kwenye namba tano iliyoandikwa nje ya lile bomba.
“Choma hiyo sindano kando ya hicho kidonda!” Aliniambia.
“Mimi?”
“Sasa kuna nani mwingine hapa? Hebu fanya upesi!”
Niliinua ile sindano na Dokta Kashushu alinizuia kwa mkono wake wa kushoto na kuitazama ile dawa iliyokuwa ndani ya lile bomba la sindano kwa makini.
“Umeitoa wapi hii dawa wewe?” Aliniuliza kwa wasiwasi mkubwa. Nilimshangaa, kwani sikuelewa maana ya swali lile, lakini aliniuliza tena. Nilimwonesha kile kichupa kilichokuwa na ile dawa. Dokta Kashushu alitikisa kichwa kwa fadhaa na woga.
“Si...sio hii wewe! Hii dawa ni hatari sana!” Aliniambia huku akiusukumia pembeni mkono wangu taratibu, na kunionesha kichupa kingine kilichokuwa pale sakafuni.
“Dawa ninayohitaji ni hii, fanya haraka!”Aliniambia. Niliweka pembeni lile bomba la sindano na kuchukkua kile kichupa kingine, ambacho ingawa hapo mwanzo nilikiona ni sawa na vile vingine, lakini kilikuwa tofauti kabisa. Niliinuka haraka na kwenda tena kuchukua bomba jingine la sindano huku kwa mara ya kwanza ikiniingia akilini kuwa mle ndani kulikuwa kimya, purukushani za John Vata na Wagga Maingo zilikuwa zimekwisha.
John Vata alikuwa amesimama akiwa amejishika kiuno, akimtazama yule mtu aliyenipa taabu sana maishani, aliyejitia kujiita Martin Lundi, ambaye sasa nimembaini kuwa anaitwa Wagga Maingo. Alikuwa amejitawanya sakafuni akiwa hana fahamu, kipondo alichopokea kutoka kwa John Vata kilikuwa si cha mchezo.
“Bastard!” John Vata alisema kwa hasira kumuambia yule muuaji aliyezirai pale sakafuni na moyoni mwangu nilifarijika kupita kiasi. Nilitaka kumsemesha yule afisa wa polisi kijana lakini kwa mara nyingine Dokta Kashushu alinihimiza.
Niliweka ile dawa nyingine niliyoelekezwa kwa kufuata kipimo kile kile na kumchoma yule daktari kwenye eneo alilonielekeza kando ya lile jeraha. Yule daktari alijiegemeza ukutani na kuonekana kama aliyepoteza fahamu nami nikamgeukia John Vata, ambaye alikuwa akimfungua nesi Tamala kutoka kwenye ile mikanda iliyombana pale kitandani. Wakati huu alikuwa ameshaamka, lakini alikuwa ameduwaa tu akitumbua macho ukutani, akionekana wazi kuwa akili yake ilikuwa imezimika.
Mungu wangu! Nimefanya nini sasa...?
“Tuondoke haraka eneo hili!” John Vata alisema baada ya kumfungua yule nesi aliyerukwa akili na kumwacha akiwa amejilaza sakafuni naye kuiendea ile simu na kuanza kupiga kituo cha polisi kuwaarifu juu ya tukio lile, akiwapa maelekezo jinsi ya kufika pale.
Kitendo kilichofuatia kilikuwa ni cha haraka na si mimi wala Kamishna Msaidizi John Vata aliyekitarajia. Wagga Maingo alikurupuka kutoka pale chini na kukikwapua kile kisu kikali cha upasuaji kilichokuwa kimetupwa sakafuni hapo awali na kumuendea John Vata kwa kasi.

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 34

“Tuondoke haraka eneo hili!” John Vata alisema baada ya kumfungua yule nesi aliyerukwa akili na kumwacha akiwa amejilaza sakafuni naye kuiendea ile simu na kuanza kupiga kituo cha polisi kuwaarifu juu ya tukio lile, akiwapa maelekezo jinsi ya kufika pale.
Kitendo kilichofuatia kilikuwa ni cha haraka na si mimi wala Kamishna Msaidizi John Vata aliyekitarajia. Wagga Maingo alikurupuka kutoka pale chini na kukikwapua kile kisu kikali cha upasuaji kilichokuwa kimetupwa sakafuni hapo awali na kumuendea John Vata kwa kasi. Wote tulisikia vishindo vya miguu yake kwa wakati mmoja na nilipoona jambo alilokuwa anataka kulifanya, nilibaki nikiwa mdomo wazi. John Vata aligeuka haraka na kuona Wagga Maingo akimwendea kasi ilhali kile kisu kikiwa kimeinuliwa juu kwa mkono wake wa kulia, akiwa amekenua meno na amekunja uso kwa ghadhabu. Kwa pale alipokuwapo sikuona ni jinsi gani John Vata angeweza kujiokoa, lakini alifanya jambo ambalo hata Wagga Maingo hakulitarajia.
John Vata alitupa chini ile simu na haraka sana aliruka hatua moja kubwa kumuendea yule muuaji na hivyo kumfaya awe karibu zaidi naye kuliko yule muuaji alivyotarajia na ili aweze kumchoma kile kisu, ilimbidi yeye arudi nyuma kidogo, lakini hakukuwa na muda wa kufanya hivyo, matokeo yake alijaribu kushusha kile kisu kwa nguvu ili abahatishe tu kumchoma John Vata kwa ukaribu ule ule, na hapo John Vata aliwahi kuinua mikono yake na kumkamata ule mkono wenye kisu kwa mkono mmoja ilhali kwa mkono wake mwingine akiukamata mkono mwingine wa yule muuaji.
Na hapo ndipo nilipopata nafasi ya kupiga kelele.
Wale wanaume walikuwa wakishindana nguvu, Wagga Maingo akitaka kukishindilia kile kisu kwenye mwili wa John Vata, na John akishindana naye katika hilo. Walijibamiza ukutani huku wakitoa miguno na bado wakiwa wameshikana vile vile. John Vata alimgeuza Wagga Maingo na kumbamiza ukutani, lakini ilioneka Wagga alikuwa amekishika vizuri kile kisu. Nilikuwa nikiwazunguka huku nikipiga kelele hovyo, na wakati nikifanya hivyo, niliweza kuona kwa kihoro kuwa John Vata alikuwa anaelekea kushindwa kuendelea kuishikilia ile mikono ya Wagga Maingo kwa muda mrefu kutokana na jasho lililokuwa limetapakaa mikononi mwa yule muuaji na kufanya vidole vyake viteleze. Kwa pale walipokuwa wameshikana, nilikuwa nauona uso wa Wagga Maingo aliyebanwa ukutani, John Vata alikuwa amenigeuzia mgongo wake, na niliona uso wa Wagga Maingo ukitoa lile tabasamu lake baya la ushindi.
Bloody fool!
Nilimtupia jicho Dokta Kashushu pale chini alipokuwa amelala na nikaona bado hajitambui. Sikufikiri wala kusubiri zaidi. Nilikurupuka na kunyakua lile bomba la sindano nililotaka kumchoma Dokta Kashushu kwa makosa hapo mwanzo na kuwaendea kwa kasi pale walipokuwa wakivutana. Wagga Maingo alitumbua macho kwa woga alipoona nawaendea kwa kasi nikiwa nimeinua juu lile bomba la sindano yenye ile dawa ambayo Dokta Kashushu aliniambia kuwa ni hatari sana, lakini kwa kuwa alikuwa ameshikwa na John Vata hakuwa na la kufanya, na badala yake alianza kunipigia kelele.
“Tigga Noooooo! Noooooo! Aaaaaaaaaagh....”
Nilipitisha mkono wangu wa kushoto ubavuni kwa John Vata na kumkamata Wagga Maingo kiuno, kisha kwa nguvu zangu zote niliishindilia ile sindano kifuani kwa yule muuaji, na kuishindilia ile dawa mwilini mwake.
“Ayyyaaaa Tiggaaaaa! You Bitch!(Malaya we!)....Aiiii....” Wagga Maingo alipiga kelele huku akifurukuta ilhali mimi na John Vata tukiwa tumemshika na kumbana kwa nguvu, mimi nikiwa nimekandamiza kifua changu mgongoni kwa John Vata ambaye aliendelea kuikata ile mikono ya yule muuaji muongo. Tulitazamana na yule muuaji wakati akihangaika kushindana na ile dawa na wakati huo huo akijaribu kujikwamua kutoka mikononi mwetu bila mafanikio.
“Tulia wewe! Bastard...! John Vata alimkemea kwa sauti ya kugumia, lakini yule muuaji alikuwa na mimi tu. Alinitazama kwa macho ya hasira na kunitukana tusi zito la nguoni.
“Mwenyewe, Wagga Maingo! Na wewe uonje ladha ya ufidhuli wako!” Nilimjibu kwa hasira huku nikijisikia furaha isiyo kifani moyoni mwangu kwa kumfikisha pale yule mtu aliyenisumbua na kunifitinisha na watu wangu wa karibu.
Nilizidi kumkandamiza kifuani na ile sindano hata baada ya ile dawa yote kuuingia mwili wake. Alijitutumua kwa nguvu sana na ile sindano ikakatikia mwilini kwake, lakini niliendelea kumkandamiza ukutani kwa mkono wangu wa kulia huku ule wa kushoto bado ukiwa umemkamata kiuno. Alipiga yowe kubwa la uchungu na kukata tamaa na niliona uso wake ukimbadilika na kuingiwa na woga mkubwa. Chozi lilimbubujika Wagga Maingo na niliona akianza kuishiwa na nguvu.
Kisu kilimtoka mkononi na ghafla alikuwa mzito sana. Macho yalimrembuka na povu likaanza kumtoka kinywani huku akitoa sauti za mikoromo, miguu ikamlegea na akaangusha kichwa kifuani kwake.
Wagga Maingo, zamani Martin Lundi, alipoteza fahamu.
Nilimwachia na kurudi nyuma huku John Vata akimlaza chini taratibu nami nikitazama hali ile kwa hali ya kutoamini.
Nimemweza Wagga Maingo! Nimemtoa machozi Wagga Maingo! Atie adabu, pumbavu zake...kama ataishi!
John Vata alinigeukia.
“Safi sana Tigga...safi sanna!” Alinipongeza kwa kitendo changu cha kumshindilia yule muuaji kwa ile sindano na kummaliza nguvu.
“Mi’ nakushukuru wewe afande, kwa kuja kuniokoa...”
“Whaaa...? Aaauw! Nini kimetokea...?” Dokta Kashushu alizinduka na kuuliza huku akiangaza mle ndani. Tulimtazama lakini hatukuona umuhimu wa kumjibu, naye akabaki akiwa ameduwaa tu. John Vata alinigeukia.
“Sasa tukubaliane hapa hapa. Utanitoroka tena au nikutie pingu na wewe? “ Aliniuliza huku akimfunga Wagga Maingo pingu miguuni na mikononi.
“No! No afande! Sina tena sababu ya kukutoroka! Mi’ nitakuwa bega kwa bega na wewe...nahitaji sana msaada wako.”
“Vizuri. Sasa tufanye hima tuondoke, maana niko peke yangu na sina hakika iwapo wenzao hawa watu hawako mbali na hapa...”John Vata aliongea huku akimuinua Dokta Kashushu, nami nikamuuliza vipi alikuja peke yake.
“Nilitaka kuchunguza eneo lenyewe kwanza...bado nilikuwa na mashaka na maelezo yako, na nilipolifikia eneo hili na kuona kuwa nyumba yenyewe haikuwa hata na dalili ya uhai, nikaamua kuingia kupeleleza...ndio nikawakuta na Dokta Kashushu.” Alinijibu.
Tulitoka mle ndani tukiwa tumembeba Dokta Kashushu aliyeonekana kuishiwa nguvu. Na nilipotoka kule nje niligundua kuwa ni kweli ile nyumba haikuwa Hospitali, badala yake ni kile chumba kimoja tu nilichokuwa nimefungiwa ndicho kilichotengenezwa kionekane kama wodi ya hospitali. Ilikuwa ni nyumba ya kawaida sana iliyokuwa maeneo ya Reagent Estate jijini. Kiza kilikuwa kimeingia na lile eneo, kama kawaida yake, lilikuwa kimya, hata baada ya milio ya bastola. Tuliiendea gari aina ya Land Rover Discovery aliyokuja nayo John Vata na kumweka Dokta Kashushu katika kiti cha nyuma cha ile gari. John Vata aliniagiza nibaki na Dokta Kashushu pale kwenye gari naye akakimbia kurudi tena mle ndani kumchukua Wagga Maingo na ghafla, muda mfupi baada ya John Vata kuingia mle ndani, tulisikia mlio wa bastola na muda huo huo mlipuko mkubwa ulilitikisa jiji na ile nyumba ikalipuka moto mkubwa.
“Jooohn!” Nilipiga kelele kwa kihoro na kuanza kutimua mbio kukimbilia kule kwenye ile nyumba, lakini Dokta Kashushu alinikamata kiuno na kunizuia.
“Usiende huko Mwanamke! Huna utakachofanya...ni hatari!’
“No!No! John Vata! Lazima tukamsaidie!”
“Huna cha kumsaidia hapo! Hilo ni bomu. Lets go!(Tuondoke!)” Dokta Kashushu alinikemea nami nikajitutumua ili aniachie, na hapo hapo nilishuhudia kioo cha dirisha la ile Landrover Discovery kikipasuka sambamba na mlio wa bunduki. Dokta Kashushu alinirukia na kunikandamiza chini huku akipiga kelele.
“Tunashambuliwa kwa risasi...Take cover!(Jifiche!)”
Nilipiga kelele kwa kuchanganyikiwa, na nikiwa nimekandamizwa na Dokta Kashushu pale chini nilisikia mlio mwingine wa bunduki na mchanga ukatifuka hatua chache kutoka pale tulipokuwa tumejilaza na Dokta Kashushu alijiingiza chini ya uvungu wa ile gari huku akinihimiza nami nifanye hivyo hivyo. Nilipeleka macho kule nilipohisi kuwa zile risasi zilikuwa zikitokea huku nikijisokomeza chini ya lile gari na nikipiga mayowe. Na hapo, kwa kusaidiwa na mwanga uliotokana na ule moto uliokuwa ukiwaka kutoka kwenye ile nyumba, nilimuona mwanamke mwembamba na mfupi akiwa amevaa joho la kike kama la baibui hivi, ambalo lilikuwa wazi sehemu ya mbele na kuonesha suruali na fulana ya mikono mirefu na kichwani akiwa amejitanda mtandio uliofunika sura yake yote na kuacha sehemu ya macho tu, akitutupia risasi kwa bunduki fupi aliyoishika kwa mikono yake yote miwili.
“Aah! Ndio yule mwanamke...!” Nilipiga kelele wakati akilini mwangu nikikumbuka maelezo juu ya yule mwanamke aliyeenda kuonana na hayati Dick Bwasha kule benki baada ya mimi kutoka.
Yule mwanamke alikuwa amesimama kwenye pikipiki kubwa, na katika ile sehemu ya mbele ya ile pikipiki, karibu na tanki la mafuta, niliuona mwili wa Wagga Maingo ukiwa umelazwa kifudi fudi kwenye ile pikipiki, sehemu ya juu ya mwili wake ikiwa upande mmoja wa ile pikipiki, na sehemu ya miguu yake ikiwa upande mwingine.
Mambo yote haya niliyaona ndani ya sekunde moja tu na hapo hapo tukatupiwa risasi nyingine na nikapata mshituko mkubwa niliposikia mlipuko wa bastola karibu na sikio langu. Dokta Kashushu alikuwa anajibu mashambulizi kwa kutumia bastola aliyokuwa ameishika kwa mkono wake wa kushoto.
“Wanataka kuniua mimi! Lakini siuawi kibwege...nitapambana!” Alikuwa akisema huku akifyatua risasi mfululizo kumuelekea yule mwanamke, na kwa mbali nilianza kusikia ving’ora vya gari za polisi. Yule mwanamke alitia moto pikipiki yake na kutokomea kwa kasi kutoka eneo lile akiwa ameubeba mwili wa muuaji Wagga Maingo kwenye ile pikipiki yake.
“Twen’zetu!” Dokta Kashushu aliniambia huku akitoka uvunguni mwa ile gari na kuanza kutimua mbio kukiendea kichochoro cha jirani.
“No! John Vata...”
“Huna unachoweza kufanya kumuokoa yule, mwanamke...! Bila shaka amekufa!” Aliniambia huku akizidi kukimbia kwa taabu. Nilibaki nikiwa nimeduwaa, nikiiangalia ile nyumba ikiteketea na kuona kuwa hakuna hata dalili ya John Vata kutokea. Na ving’ora vya polisi vilizidi kukaribia na baadhi ya majirani wa eneo lile wakianza kutoka nje ya nyumba zao.
Oh, My God...sasa...
Sikujishauri zaidi. Nilitoka mbio kumfuata Dokta Kashushu huku nikilia kwa sauti na bila ya kujua naye atanifikisha wapi, ilhali moyoni nikiwa nimeumia kupita kiasi, nikishindana na nafsi yangu juu ya kukubali ukweli kuwa Kamishna Msaidizi John Vata amefariki katika mlipuko ule.
Kwa ajili ya kuja kuniokoa mimi...
Kichochoro alichoingia Dokta Kashushu kilitokea kwenye mtaa uliokuwa nyuma ya ile nyumba iliyokuwa ikiwaka moto, na nilikuta yule dokta akihangaika kufungua mlango wa gari ndogo ambayo niliihisi kuwa ni Toyota Mark II nyeusi, au buluu. Nilipomfikia aliniuliza iwapo nilikuwa najua kuendesha gari huku akinikabidhi ufunguo na kuniambia nifungue mlango wa ile gari. Haraka bila ya kujisumbua kumjibu nilifungua mlango wa ile gari na kujitumbukiza ndani huku nikimfungulia na yeye mlango wa abiria, naye akjitupa ndani.
“Tunaenda wapi sasa?” Nilimuuliza yule dokta huku nikiiondoa ile gari kwa kasi kutoka eneo lile.
“Endesha kwa mwendo wa kawaida! Vinginevyo tutaanza kufukuzwa na mapolisi sasa hivi! Just Relax...Okay?” Dokta Kashushu alinikemea, kisha alinielekeza njia za vichochoroni ambazo zilitufikisha eneo la Drive Inn, kisha tukakamata barabara ya Kawawa hadi Magomeni Mapipa, hapo akaniambia nielekee maeneo ya feri.
“Dokta Kashushu...ni nini kinaendelea hapa? Wagga Maingo anataka nini hasa?” Nilimuuliza yule daktari bingwa huku nikiendesha ile gari na nikitiririkwa na machozi. Badaya ya kunijibu, yule dokta alikuwa akijifunga kidonda chake kwa kipande cha fulana yake huku akigumia kwa maumivu. Kisha alitoa simu na kuanza kuongea na mtu ambaye nilielewa kuwa ni mkewe.
“Rukia! Rukia nisikilize kwa makini...limetokea! Nimeshagundulika...we have to go! Kama bado uko na msimamo wako basi mchukue mtoto na begi letu uondoke sasa hivi!’ Aliongea kwa kiherehere, nami nikazidi kujawa na udadisi na kutoelewa.
“Muondoke kwenda wapi dokta? Na mimi itakuwaje...”
“Ndio, Rukia! Acha kila kitu kama kilivyo. Ukichelewa wanaweze kukuta hapo, tukutane kwenye boti sasa hivi! Utanikuta...”
“Dokta Kashushu! Mbona sielewi?”
“Si kazi yako! Lakini labda nitakuelezea kiasi cha kukuwezesha kuelewa, na labda ukishaelewa na wewe utaamua kuondoka kama mimi!” Dokta Kashushu alinikemea, kisha akaendelea kuongea na simu yake.
“Niko na mtu ananiuliza maswali tu hapa...ah, fanya hima Rukia! Okay!” Alimaliza kuongea na simu na kuirudisha ile simu mfukoni mwake.
“Dokta Kashushu...ni nini kinaendelea? Mimi sielewi...!” Nilimwambia huku nikiendelea kuendesha ile gari nzuri.
“Nitakueleza Tigga. Na Labda nikishakueleza utaweza kuelewa kwa nini nililazimika kufanya mambo yale niliyokuwa nikikufanyia ingawa hata wewe uliona kuwa sikuwa nikipendelea kufanya vile...lakini...I had no choice (Sikuwa na la kufanya). Na sasa, maisha yangu hapa nchini yamefikia mwisho. I have to be on the run again(Yanipasa nianze kukimbia tena)” Dokta Kashushu aliniambia kwa upole huku akigumia kwa maumivu, nami nikazidi kushangaa.
“Uanze kukimbia tena? Ni nini kilichotokea Dokta...Oh, Mungu wangu, mbona mnanichanganya hivi?”
Hapo Dokta Kashushu alianza kunieleza mambo yaliyopelekea hata yeye na mimi tukakutana katika mazingira yale, na kufikia hatua ile ya kukimbia pamoja baada ya ule mlipuko uliopoteza maisha ya Kamishna Msaidizi John Vata.

--

“Miaka kadhaa iliyopita, nilikuwa daktari wa rais wa Burundi. Ingawa fani yangu ilikuwa ni magonjwa ya akili, niliteuliwa kuwa daktari mkuu wa rais na baadhi ya majukumu yangu ilikuwa ni kuhakikisha kuwa rais na familia yake wanapatiwa matibabu yanayofaa ndani na nje ya nchi...” Dokta Kashushu alianza kunielezea kisa chake nami nikabaki nimepigwa na butwaa, kwani kama alikuwa daktari wa rais wa Burundi, vije awe Tanzania hivisasa?
“Sasa kwa nini uliteuliwa wewe wakati fani yako ilikuwa tofauti?’ Nilimuuliza.
“Sio siri Tigga...kwa wakati ule ilikuwa kila anayechukua madaraka anawaweka watu anaowaamini...na hilo nadhani ndilo tatizo kubwa la siasa za Afrika ya kati...” Dokta Kashushu alinijibu. Kisha akaendelea.
“Nilikuwa na mke wangu na watoto wawili niliowapenda sana...kama utakumbuka, kwa miaka mingi hali ya kisiasa ya Burundi haikuwa shwari. Kulikuwa kuna vikundi vilivyokuwa vikipingana na serikali, vikundi ambavyo vilikuwa vinapata msaada kutoka vikundi vya upinzani vya nchi za jirani hasa Rwanda, ambako uhasama wa kikabila ulikuwa umekithiri...”
Tulikuwa tunakaribia eneo la pwani na Dokta Kashushu alinielekeza niegeshe gari kando ya barabara katika eneo la kituo cha mabasi cha posta ya zamani, kisha tukaanza kutembea kwa miguu hadi kwenye eneo jirani na chuo cha ubaharia.
Wakati tukielekea eneo lile Dokta Kashushu aliendelea kunielezea huku bado akionekana kuwa na wasiwasi sana juu ya usalama wa mkewe.
“Siku moja nilitembelewa na watu nisiowafahamu ofisini kwangu, ambao walinitaka nifanye mambo kama yale niliyokuwa nikikufanyia wewe kule kwenye ile nyumba kwa mashinikizo ya Wagga Maingo...ila wao walinitaka nimfanyie rais....”
ITAENDELEA
 
Back
Top Bottom