Riwaya: Mkimbizi

Riwaya: Mkimbizi

SEHEMU YA 35

“Siku moja nilitembelewa na watu nisiowafahamu ofisini kwangu, ambao walinitaka nifanye mambo kama yale niliyokuwa nikikufanyia wewe kule kwenye ile nyumba kwa mashinikizo ya Wagga Maingo...ila wao walinitaka nimfanyie rais....”
“Whaaat?” Nilishitushwa na taarifa ile na kumgeukia yule Dokta kwa mshangao.
“Mmmnh! Ndivyo walivyonitaka na nadhani unaweza kukisia ni jinsi gani nivyoshituka juu ya ombi lao hilo. Niliwakatalia katakata na kutishia kuwaripoti serikalini.”
“Lakini...kwa nini walitaka kitu kama hicho...”
“Walitaka kunitumia kumtia rais wazimu...kisha asiwe tena na uwezo wa kuongoza nchi... wenyewe walidai kuwa hiyo ilikuwa ni njia pekee ya amani ya kumtoa rais madarakani bila kumwaga damu...( alicheka kwa dharau na kutikisa kichwa kwa masikitiko) Yaani lilikuwa ni jambo la kipumbavu nililowahi kulisikia maishani mwangu”
Eh...jamani! Haya mapya kuliko!
Pale jirani na kile chuo cha ubaharia kulikuwa na geti dogo ambalo lilitokea kwenye ngazi ndefu za mbao na chuma zilizokuwa zikiteremka pwani, eneo ambalo zamani ilikuwa inaegeshwa boti kubwa ya kwenda Zanzibar iliyoitwa MS SEPIDEH. Dokta Kashushu alijitambulisha kwa mlinzi wa pale getini ambaye alionekana kumtambua vizuri na kumuambia kuwa tulikuwa tunaelekea kwenye boti lake huko chini, na kwamba mkewe atafika muda mfupi ujao. Tuliteremka zile ngazi huku nikimuuliza kuwa alikuwa anamiliki boti. Aliafiki kwa kichwa bila kuonesha kujali juu ya swala lile.
“Baada ya wale watu ambao baadaye nilikuja kuelewa kuwa walikuwa ni wawakilishi wa kundi moja la upinzani lililokuwa likiendesha vita vya msituni dhini ya majeshi ya serikali kuona kuwa nimezidi kuwa mkaidi katika kutekeleza matakwa yao, walianza vitisho kuwa nikithubutu tu kutoa taarifa serikalini, wataiteketeza familia yangu yote! Nilikuwa kwenye wakati mgumu sana Tigga, na nilipoendelea na msimamo wangu, waliwateka mke na watoto wangu. Wakinishinikiza nimfanyie rais vile wao walivyotaka, kwani ni mimi pekee ndiye niliyeidhinisha dawa aina yoyote anayopewa rais iwapo atakuwa mgonjwa, na jambo ambalo ulimwengu haukulijua ni kwamba kwa wakati ule rais alikuwa akisumbulia na ugonjwa wa kisukari ambao ulimlazimu awe anameza vidonge maalum kila mara. Nilichotakiwa kufanya ni kumchanganyia dawa zangu za kumharibu akili pamoja na zile dawa za kisukari.”
“Dokta Kashushu haya mambo unayonieleza ni mazito sana! Inawezekana vipi mambo kama haya?” Nilimuuliza kwa msahangao. Yule Dokta alitikisa kichwa kwa masikitiko.
“Ninachokueleza Tigga ni kweli kimetokea. Hatimaye nilimweleza rais ukweli wa jambo lote, na kujiuzulu nafasi yangu ya utabibu wa rais. Rais alianzisha msako mkali wa kuwasaka mke na watoto wangu waliotekwa na wale watu ambao niliwajua kwa sura lakini sikuyajua majina yao. Kitendo hicho kiliwaudhi sana wale watu na siku moja baada ya kujiuzulu nafasi yangu, miili ya mke na watoto wangu ilikutwa kando ya msitu mmoja wakiwa wameuawa...” Aliniambia kwa huzuni nami nikahuzunika pamoja naye.
“Siku ile ile wale watu walinitumia wauaji nyumbani kwangu kuja kuniangamiza. Lakini jambo walilosahau ni kwamba mimi nilisomea shahada yangu ya udaktari huko Urusi, ambapo pamoja na shahada hiyo nilisomea pia mbinu za kijasusi na mapambano, kwani wakati huo urusi ndio ilikuwa inaendekeza zile siasa zake za ujamaa na ilikuwa ikisomesha waafrika wengi bure na kuwatumia katika propaganda zake za kijamaa. Niliwateketeza wale wauaji wawili na kuiacha nyumba yangu ikiteketea kwa moto, nami nikakimbia ile nchi Tigga. Nchi yangu niliyozaliwa na kukulia. Nilikuwa nimeficha pesa nyingi nje ya nchi, hivyo haikuwa taabu kwangu kutoroka nchini. Na kuanzia hapo nikawa mkimbizi Tigga. Huku nyuma nikasikia ndege iliyokuwa imembeba rais wetu na yule wa Rwanda ilianguka na kuwaua wote, lakini nilijua kuwa ni lile kundi lililokuwa likinitaka nimharibu akili rais ndilo lilihusika na kuanguka kwa ndege ile.” Dokta Kashushu alimalizia maelezo yake taratibu. Tuliingia kwenye ile boti yake ambayo kwa kweli ilikuwa kubwa na ghali sana. Aliniambia kuwa alikuwa ameiandaa ile boti kwa ajili ya tukio kama hili, ingawa huwa anakuja na mkewe mara kwa mara na kuiendesha hadi katikati ya bahari, siku nyingine wakiishi kwenye ile boti kwa siku mbili au tatu kabla ya kurudi tena nyumbani kwao Mbezi bichi.
Dokta Kashushu aliniambia kuwa alikimbilia Senegal. Baadaye alimtambua mmoja wa wale watu waliomfuta na kumshurutisha kumharibu akili rais akiwa miongoni mwa mawaziri wapya wa Rwanda, nchi ambayo ilikuwa ikishirikiana na waasi waliokuwa wakiipinga serikali ya Burundi. Kisha uchunguzi wa kifo cha rais wa Burundi na yule wa Rwanda ulianza, kwamba ile ndege haikuanguka kwa hitilafu za kawaida, bali huenda ikawa ilitunguliwa. Hapo wale watu wakaanza kumsaka tena ili kummaliza, kwani walijua ni yeye tu ndiye anayeweza kuwatambua wale watu waliomfuata na kumshurutisha kumharibu akili rais. Walimuibukia Senegal. Akafanikiwa kuwatoroka na kwenda Botswana. Huko nako akaondoka baada ya miaka miwili na miaka sita iliyopita akaingia Tanzania kwa pasipoti ya bandia aliyomtambulisha kuwa yeye ni Mtanzania aliyejulikana kwa Jina la Dokta Mohammed Kashushu. Hapa alianza maisha mapya na alioa mwanamke aliyekuwa yatima, kwani alijua kuwa wale watu bado walikuwa wakimsaka na hakupenda kabisa kujihusisha na mwanamke mwenye familia. Akiwa Tanzania, yule mtu aliyemtambua kuwa ni mmoja wa wale waliokwenda kumshurutisha kufanya mambo ya ajabu kwa marehemu rais wa Burundi, ambaye baadaye alikuwa miongoni mwa mawaziri wapya wa Rwanda baada ya mauaji ya halaiki, alionekana kwenye Televisheni akiwa ni mmoja kati ya watu waliokamatwa na kuletwa kwenye mahakama ya kimataifa dhidi ya mauaji ya halaiki ya Rwanda na Burundi iliyopo Arusha, Tanzania. Kufikia hapo alianza kuona mashaka juu ya usalama na amani yake nchini Tanzania, hivyo alimweleza ukweli mkewe mtanzania. Mkewe huyo aliamua kuwa pamoja naye popote atakapoenda, na ndio maana tukawa pale tukimsubiri mkewe ili atoroke naye.
Haya maelezo yalikuwa mapya sana kwangu na nikaanza kufikiria upya mkasa wote ule. Nilikumbuka kusoma habari za mahakama ya kimataifa dhidi ya mauaji ya halaiki ya Rwanda na Burundi. Nilikumbuka kusoma habari juu ya mtanzania kuteuliwa kuwa jaji wa mahakama hiyo...
“Lakini Dokta Kashushu, ilikuwaje ukapata nafasi ya kufanya kazi hapa nchini kwani vyeti vyako vya shule, hizo digrii zako, zilikuwa zinakuonesha wewe kama Dokta Kashushu? Kwani hilo ndilo jina ulilokuwa ukilitumia wakati unasoma?” Nilimuuliza.
“Hapana Tigga. Ukumbuke kuwa nilikuwa na pesa nyingi. Nilipata digrii zangu Urusi. Lakini pia nilitengeneza vyeti vya digrii hiyo hiyo kutoka vyuo vingine viwili vya nchi za magharibi, kimoja Finland na kingine kutoka chuo kidogo sana kisichojulikana kabisa kilichokuwa nchini Austria. Hiki cheti cha Austria kilinitambulisha kwa jina la Mohammed Kashushu kutoka Tanzania. Na hiki ndicho cheti ninachokitumia hapa Tanzania. Kwa hiyo ingawa fani niliyosomea ni ya kweli kabisa kama inavyoonekana kwenye cheti, jina lililo kwenye cheti na chuo ambacho kinaonekana kwenye cheti kuwa nimesomea si vya kweli. Chuo cha kweli nilichosomea kiko Urusi na katika cheti cha chuo kile kuna jina langu halisi, ambalo siwezi kukutajia kwa sababu ambazo nadhani unazielewa kufikia sasa.” Dokta Kashushu alinifafanulia. Haya mambo kwangu yalizidi kuwa mazito.
“Sasa ina maana kuwa wale watu waliokuwa wakikusakama tangu Burundi, Senegal na Botswana ndio hawa akina Wagga Maingo?” Nilimuuliza Dokta Kashushu kwa mshangao, huku nikianza kupata hofu kubwa juu ya huu mkasa mzima ulioniangukia.
“Hapana...huenda hawa wakawa na uhusiano na wale, lakini sio wale walionifuata kule Burundi. Kilichotokea hapa Tanzania, ambapo kama ulivyoelewa, nilikuwa nikiishi kwa amani sana, lakini kama Burundi, siku nne tu zilizopita yule mtu niliyekuja kumtambua kama Wagga Maingo aliniijia ofisini kwangu na kuniambia kuwa anajua kuwa mimi si mtanzania na ninaishi kwa hati bandia, na nimepewa nafasi nzuri sana katika nchi hii iliyoniwezesha kuishi kwa raha. Na akanitaka nimfanyie kazi yake, ambayo nikiifanya bila matatizo, wataendelea kunitunzia siri yangu na kuniacha niendelee kuishi kwa amani hapa nchini...kinyume na hapo, wao wangepiga simu idara ya uhamiaji na maisha yangu yangesambaratika.”
“Oh, Mungu wangu...!”
“Ndio Tigga. Nilikuwa na wakati mgumu. Na wakati huu umri wangu umesogea, sikuwa tena na uwezo wa kujiingiza kwenye mikiki-mikiki kama hapo mwanzo. Kwa hiyo sikuwa na la kufanya, nikakubaliana na sharti lao, ingawa sikuwa na uhakika kuwa huu ndio ungekuwa mwisho...nadhani sasa unaelewa ni kwa nini nililazimika kufanya vile Tigga, na nataraji utapata nafasi katika moyo wako kunisamehe kwa hili....” Dokta Kashushu alimalizia huku akinitazama kwa huzuni. Sikuwa na la kusema. Nilibaki nikiwa nimeduwaa.
“Kwa hiyo hujui hawa watu...akina Wagga Maingo walikuwa wanataka nini hasa?” Nilimuuliza.
“Hapana. Ila nakuhakikishia kuwa hawa watu ni wabaya sana. Sasa kama wana uhusiano na lile kundi lililofanya mambo ya kule Burundi miaka ile, basi nchi yenu sasa iko hatarini, na kwa kuwa wewe unaonekana kuwa na kitu wanachokitaka, nakushauri na wewe ukimbie mdogo wangu. Hapa hapakufai tena. Ukiwapa wanachokitaka, sina shaka kuwa wataiangamiza nchi yenu...wataitia kwenye balaa fulani tu! Hawa ni watu wanaopenda kuvuruga amani ndani ya nchi Tigga...kwa namna fulani ili wao wawe na maisha mazuri, ni wajibu kusiwe na amani.Kama kuna amani si mahala pao...ndio maana nakushauri kuwa ukimbie Tigga...ukipenda tunaweza kukuchukua pamoja nasi...nitakupatia pasipoti ya nchi yoyote uitakayo ukakae huko...”
“Hapana! Hapana Dokta Kashushu...mimi hapa ndio kwetu! Nina ndugu na jamaa zangu hapa, siwezi kuwaacha...” Nilimjibu kwa hamasa. Na hapo mkewe akafika. Walikumbatiana kwa upendo huku yule dada, ambaye alikuwa kijana zaidi ya Dokta Kashushu, akibubujikwa na machozi. Alimtazama mumewe kwa upendo na huruma, kisha macho yake yakaangukia kwenye pingu iliyokuwa ikining’inia kwenye mkono wake wa kushoto na kumuuliza kwa woga kulikoni.
“Ni hadithi ndefu...nitakuelezea baadaye...” Dokta Kashushu alimjibu. Mkewe akaanza kumchunguza ule mkono uliojeruhiwa kwa risasi lakini Dokta Kashushu alimtoa wasi wasi kuwa halikuwa tatizo kubwa. Yule dada alikuwa amehamanika vibaya sana. Walikuwa na mtoto wa kike aliyapata miaka minne ambaye naye alikuwa akilia kwa kumuona tu mama yake akilia. Dokta Kashushu alinitazama huku akiwa amemkumbatia mkewe.
“Sisi hatuna muda wa kupoteza Tigga...inatupasa tuanze safari mara moja. Una hakika hutaki kuambatana nasi?” Aliniuliza. Nillimtazama yule Dokta mtu mzima kwa muda huku nikimhurumia kwa mikasa iliyompata. Nilitamani kuwa pamoja naye, lakini akilini mwangu nilikuwa na mambo mengi niliyotaka kuyafanyia kazi nikiwa hapa hapa nchini. Nilitaka kujua sababu ya yule mtu kuuawa kule msituni, nilitaka kumjua ni nani yule mtu kigulu aliyekuwa na akina Wagga Maingo kule msituni, nilitaka kujua nini hatma ya yule dada askari aliyekuwa akishirikiana na akina Wagga Maingo...nilitaka kujua juu ya yule mwanamke mwenye hijab, aliyetuvurumishia risasi na ambaye nadhani ndiye aliyehusika na kifo cha Dick Bwasha...na hatma ya John Vata.Masikini John...iliniwia vigumu sana kuamini kuwa amefariki.
“Mimi nitabaki hapa hapa Dokta Kashushu...hata kama nitauawa, ni bora nifie nchini kwangu.” Nilimjibu taratibu. Yule Dokta alinitazama kwa muda, kisha akafungua begi alilokuja nalo mkewe na kutoa funguo zipatazo tatu zilizokuwa zimefungwa pamoja na kunikabidhi.
“Basi nakuomba uchukue hizi funguo za nyumba yangu nyingine Tigga. Hakuna mtu yeyote anayeijua nyumba hii, na nimeaindikisha kwa jina la huyu binti yangu.Unaweza ukahitaji maficho...nadhani huko kutakufaa kwani nina imani ukiwa kule hutagundulika kirahisi...na vitu vyote utakavyovikuta humo ni mali yako kuanzia leo...hiyo ni namna yangu ya kukusaidia katika mtihani huu Tigga...”
“Ah! Dokta Kashushu...siwezi kukubali jambo kama hilo...mkeo....?” Nilimwambia yule Dokta huku nikimtazama mkewe. Yule mwanamke mwenye sura ya kuvutia na mwili uliojigawa vizuri aliniambia kuwa nisikatae amana ile. Kwani hata yeye hatarudi tena hapa nchini. Nilipokea kwa mikono iliyojaa kitetemeshi.
“Sa...sasa ni wapi huko, yaani nitapajuaje....?” Niliwauliza. Dokta Kashushu alimwambia mkewe anichoree ramani ya eneo ilipo ile nyumba na akanitajia maeneo ya kuulizia ili nifike hapo, halafu akatoa picha ya ile nyumba na kunikabidhi. Ilikuwa ni nyumba ndogo ambayo ilikuwa bado haijamaliziwa sawasawa kujengwa kwa maana kuwa haikuwa imepigwa plasta kwa nje, ingawa ilikuwa imeezekwa kwa vigae na ilikuwa imewekwa madirisha na milango na ilikuwa imewekewa “grill” madirishani na milangoni.
“Ahsante sana Dokta...na Mrs. Kashushu... Mungu awajaalie huko mwendako.” Niliwashukuru, na Dokta Kashushu alimwambia mkewe aandike barua ya kunitambulisha kwa mlinzi wao, akiniambia kuwa mkewe ndiye aliyekuwa akijulikana sana na yule mlinzi kuliko hata yeye. Yule dada aliandika na kusaini ile barua kisha akanikabidhi. Kisha yeye alinitoa nje ya ile boti nami nikateremka na kusimama kwenye ukingo wa bahari juu ya baraza. Dokta Kashushu alinitazama na kuniuliza.
“Yule mwanamke aliyekuwa akitutupia risasi...unamfahamu? Ulionekana kuwa uliwahi kukutana naye hapo mwanzo...”
“Aaah! Yule...hapana, ila kuna mtu aliuawa, na ikasemekana kuwa mtu wa mwisho kuonana naye alikuwa ni mwanamke aliyevaa baibui...hivyo nikahisi labda ni yeye. Kwani vipi?”
“Umeshawahi kumsikia mtu aitwaye ‘The Virus’?” Aliniuliza. Nikamjibu hapana, na kumuuliza huyo ni nani.
“Ni muuaji wa kukodiwa...kama Carlos the Jackal, kama uliwahi kumsikia, lakini yeye anajiita The Virus...yaani Kirusi...huwa anafanya kazi zake Afrika. Nadhani ndiye yule aliyekuwa akitushambulia pale...”
“Ah, lakini yule alikuwa mwanamke...!” Nilimjibu kwa hamasa.
“Ndio maana nakwambia hivyo...kwa sababu inasemekana kuwa huyo The Virus, ni mwanamke!” Dokta Kashushu alinijibu. Nilibaki mdomo wazi.
Muuaji wa kukodiwa! Tanzania hii? Hapana hii sasa imekuwa kazi kubwa!
“Kila la kheri Tigga, we have to go now (yatupasa twende sasa)” Aliniambia nami nikampungia mkono. Dokta Kashushu aliingia kwenye boti lake, na muda ule ile boti ikaanza kuondoka kwa mwendo mdogo.
Nilisimama pale nikilitazama lile boti likiondoka mpaka likapotea kwenye upeo wa macho yangu.
Goodbye Dokta Mohammed Kashushu....Mwenyezi Mungu akulinde huko uendako...

***Heh, huyu muuaji The Virus ni nani? Dokta Kashushu ndio huyo ameenda zake na kumuacha Tigga katikati ya mashaka bila ya msaada wa Kamishna Vata...atawamudu vipi akina Martin Lundi muongo wakisaidiwa na huyu muuaji hatari, The Virus?
 
SEHEMU YA 36

Muuaji wa kukodiwa! Tanzania hii? Hapana hii sasa imekuwa kazi kubwa!
“Kila la kheri Tigga, we have to go now(yatupasa twende sasa)” Aliniambia nami nikampungia mkono. Dokta Kashushu aliingia kwenye boti lake, na muda ule ile boti ikaanza kuondoka kwa mwendo mdogo.
Nilisimama pale nikiitazama ile boti ikiondoka mpaka ikapotea kwenye upeo wa macho yangu.
Goodbye Dokta Mohammed Kashushu....Mwenyezi Mungu akulinde huko uendako...

--

Usiku ule ule nilirudi Uno Trabajo Bar nikiwa taabani. Nililiacha gari la Dokta Kashushu pale pale lilipokuwa limepaki, ingawa yule Dokta aliacha ufunguo ndani ya ile gari. Nilijua kuwa ile gari ilikuwa inajulikana na wale wauaji na hivyo sikutaka kabisa kulitumia. Akili yangu ilikuwa imechoka vibaya sana na nilikuwa nimejawa na simanzi kutokana na hatima ya John Vata. Kwangu ilikuwa ni ngumu sana kuamini kuwa yule afisa wa polisi kijana alikuwa amefariki. Nilipofika Uno Trabajo, Kachiki alinijia juu kwa mara nyingine kutokana na kupotea kwangu kazini kwa siku tatu mfululizo.
“Hivi Nuru una matatizo gani wewe! Unajua kuwa tayari umeshajifukuzisha kazi?” Kachiki aliniuliza kwa ukali tukiwa chumbani kwake, chumba changu tayari alishapewa msichana mwingine aliyepatikana kujaza nafasi yangu, na begi langu lilikuwa limehifadhiwa chumbani kwa Kachiki.
“Usijali Kachiki... ni hadithi ndefu...” Nilimjibu kwa unyonge.
“Nisijali gani? Nataka kujua ni nini kilichokufanya upotee namna hii!”Kachiki alinikemea huku akiwa amenishikia kiuno.
“Nilipata buzi...na kesho nahamia kwake, naomba leo tu nilale chumbani kwako, we’ si uko zamu mpaka karibu na alfajiri?” Nilimjibu kwa upole huku nikijishughulisha kupanga nguo zangu vizuri kwenye begi langu. Kachiki alinitazama kwa hasira, kisha akatoa mguno wa kukereka, halafu akatoka nje kwa hasira huku akilaani tabia ya akina dada kufanywa mabwege na wanaume “wasio na mpango hata kidogo”.
Nilienda kujimwagia maji na kurudi ndani huku nikiwa na mashaka makubwa na akili yangu. Madawa niliyomiminiwa mwilini na Dokta Kashushu kwa shinikizo la Wagga Maingo bado yalinitia wasiwasi. Sikuwa na uhakika kuwa kile kiasi kidogo kilichouingia mwili wangu hakitakuwa na madhara katika akili yangu. Usiku ule nilikaa kitandani kwa Kachiki na kuanza kuandika matukio ya mkasa wote huu ulionitokea mpaka kufikia siku ile, tangu nilipoanza safari ya kwenda Manyoni na mambo yote yaliyotokea baada ya hapo. Sikulala mpaka nilipohakikisha kuwa nimeyaweka kwenye maandishi matukio yote yaliyonitokea. Na nikaazimia kuendelea kuandika kila kitakachonitokea baada ya hapo mpaka nitakapoishia…au mpaka akili yangu itakapozimikia.
Labda siku moja kuna mtu atakuja kuyaona maelezo yangu haya na kusaidia kuielewesha jamii juu ya mambo haya na shutuma zilizotupwa dhidi yangu.
Ilinijia wazi kichwani mwangu kuwa bila John Vata, safari yangu kuelekea mwisho wa kisa hiki ilikuwa imebaki fupi sana…sikuwa tena na mategemeo ya kupata majibu ya maswali yaliyokuwa yakikisumbua kichwa changu tangu mkasa huu uanze kunikuta.
Wakati nilipopata nafasi ya kuweka ubavu kitandani, majogoo yalikuwa yakiwika huko nje. Na hata hivyo, sikupata hata lepe la usingizi. Badala yake nilijilaza kitandani na kubaki nikibubujikwa na machozi mfululizo, nikimlilia John Vata na kuijutia nafsi yangu. Moyo uliniuma kuliko kiasi. Akilini mwangu nikimfikiria yule askari kijana niliyekuwa nikimpa wakati mgumu kila alipojaribu kunishawishi nijitokeze ili anisaidie nami nimsaidie. Na pamoja na yote hayo, bado alijitolea kuja kuniokoa nilipokuwa nimenasa pasina ujanja wa kujiokoa.
Na sasa hayupo tena duniani…Mungu wangu!
Nilimfikiria Dokta Kashushu na mambo aliyonieleza juu ya watu ambao anahisi kuwa akina Wagga Maingo wanashirikiana nao. Nilimhurumia yule Dokta mtu mzima. Ilionekana kuwa maisha yake yalikuwa yamezingirwa na majonzi zaidi ya furaha, na sasa ataendelea kukimbia tu…Mungu amsaidie apate amani huko aendako. Yeye na mkewe na mwana wao. Lakini mimi siwezi kuwa mkimbizi milele…lazima nilifikishe mwisho swala hili. Lakini peke yangu nitaweza kweli?
Nilimfikiria yule mwanamke hatari aliyevaa hijab na kutushambulia kwa risasi mfululizo. The Virus…sikuwa na shaka kabisa kuwa yeye ndiye aliyemuua Dick Bwasha, na sasa nilikuwa na hakika kabisa kuwa ndiye mtu anayewajibika na kifo cha John Vata.
Oh, Mungu wangu! Laiti John Vata angekuwepo…!
Nililia! Nililia sana usiku ule. Nilimlilia John Vata. Nililia kwa uchungu na huzuni na hasira. Uchungu kutokana na kifo cha John Vata, huzuni juu ya maisha ya Dokta Kashushu na ambayo ndiyo yalielekea kunikuta na mimi, na hasira dhidi ya yule mwanamke baradhuli anayejiita The Virus…
Hatimaye nilipitiwa na usingizi mwepesi, lakini tayari kulikuwa kumepambazuka. Asubuhi ile niliagana na rafiki yangu Kachiki na kuondoka na begi langu begani kutoka katika ile baa ya Uno Trabajo ambayo ilinihifadhi kwa zile siku chache nilizokuwa nahitaji sehemu ya kujificha jijini. Mfukoni mwangu nilikuwa na ile ramani niliyochorewa na mke wa Dokta Kashushu ambayo ingenifikisha kwenye ile nyumba niliyoruhusiwa kuitumia na yule Dokta aliyezungukwa na huzuni maishani mwake. Sikuwa na pa kwenda na kwa kweli nilihitaji sehemu pweke. Nilipanda basi la Gongo La Mboto – Ubungo na safari ya kuelekea Kimara kwenye nyumba niliyoachiwa na Dokta Kashushu ikaanza. Kabla lile basi halijaanza safari niliwahi kununua magazeti kadhaa ya siku ile na kuanza kuyasoma kwa kiherehere, nikitarajia kuona habari za tukio la usiku uliopita kule Regent Estate. Habari za mlipuko wa bomu lililoteketeza nyumba huko maeneo ya Regent zilitawala vichwa vya habari katika magazeti mengi siku ile. Nilisoma gazeti mojawapo lililokuwa limeandika habari ile kwa mara ya tatu na kubaki nikiwa nimeduwaa. Habari ilieleza kuwa mlipuko ulitokana na bomu la mkono na kwamba miili ya watu wawili ilikutwa ikiwa imeteketea katika moto uliotokana na mlipuko ule. Mmoja kati ya miili ile ulikuwa ni wa mwanamke, ambaye sikuwa na shaka kuwa alikuwa ni nesi Tamala, na mwili wa pili haukuweza kutambulika kabisa.
Habari ziliendelea kupasha kuwa mara baada ya mlipuko ule kulizuka mapambano ya kutupiana risasi katika eneo lile baina ya makundi mawili yasiyojulikana na kwamba muda mfupi kabla ya polisi kufika eneo la tukio, mtu mmoja alionekana akitokomea kutoka eneo lile kwa pikipiki, wakati watu wengine wawili, mwanamke na mwanamume walionekana wakikimbia kutoka eneo la tukio na polisi wanaendelea na msako dhidi ya watu hao.
Mbona Kamishna John Vata hajatajwa kabisa katika habari ile?
Nini maana yake hii?
Ndio kusema ule mwili mwingine uliokuwa umeteketea kwa moto mle ndani ni wa John Vata? Inawezekana kweli? Hapana…It can’t be! (Haiwezekani!).
Oh, My God…sio John Vata tafadhali…John Vata hakustahili kufa kabisa Mungu wangu…
Lakini…mbona habari ile haikuelezea lolote juu ya gari ya Kamishna Msaidizi John Vata lililokuwa katika eneo la tukio? Kwa nini haikuandikwa habari juu ya simu iliyopigwa na Kamishna Msaidizi John Vata kutoka kwenye ile nyumba kwenda kituo cha polisi, bila shaka cha Oysterbay, kuwajulisha juu ya hujuma iliyokuwa ikifanyika ndani ya nyumba ile na kuwaelekeza namna ya kufika pale? Niliguna peke yangu na kutazama nje ya dirisha wakati lile basi likisafiri kwa kasi kuelekea Ubungo.
Angalau safari hii sikutajwa kuhusika au kushukiwa kuhusika na tukio lile. Lakini bado nilibaki na maswali mengi kichwani, na ikanijia kuwa maisha yangu sasa yalikuwa yamechukua uelekeo wa kwenda hatua tatu mbele na kurudi hatua tano nyuma.
Mungu nisaidie tafadhali...

--

Ubungo niliunganisha basi la Kimara ambalo kwa mujibu wa maelekezo ya mke wa Dokta Kashushu, nilitakiwa niteremkie kituo cha Suca, kisha nifuate ramani hadi eneo la ndani kidogo kutoka kituoni ambapo kulikuwa kuna bwawa kubwa. Ile nyumba niliyotakiwa kwenda ilikuwa kwenye kiji-mwinuko kidogo kando ya lile bwawa. Alinihakikishia kabisa kuwa nikilifikia lile bwawa tu sitapotea kabisa. Sikuwa nimewahi kufika maeneo ya Kimara hata siku moja maishani mwangu zaidi ya kupita tu kwa gari au basi nikiwa safarini kuelekea nje ya mkoa wa Dar es Salaam. Lile basi liliishia Kimara mwisho, na nilipomuuliza kondakta juu ya kituo cha Suca, aliniambia kuwa nilitakiwa nipande basi la Mbezi au Kibamba ndio niteremkie kituo hicho, kwani kile kituo kilikua mbele zaidi, na lile basi lilikuwa limefika mwisho wa safari. Sikubabaika. Niliwaendea madereva wa teksi bubu waliojazana pale kituoni na kuwauliza. Nilipowatajia bwawa tu wote walidai kuwa wanaifahamu sehemu ile, nami nikamkodi mmoja wao ili anipeleke. Tuliingia barabara ya zamani ya Morogoro na baada ya mwendo mfupi tuliingia ndani zaidi nami nikaanza kupata wasiwasi, lakini baada ya kuteremka kibonde kidogo na kupandisha mwinuko mmoja mkali kidogo, tuliteremka bonde jingine na mbele yangu nililiona bwawa kubwa. Yule dereva wa teksi aliniambia kuwa tumeshafika na akataka nimuoneshe ni nyumba gani hasa niliyotaka kwenda. Niliangaza kidogo na kweli kabisa, niliiona ile nyumba ikiwa kwenye kiji-mwinuko kidogo hatua kadhaa kando ya lile bwawa. Nilimwonesha yule dereva nyumba moja iliyokuwa jirani na pale tuliposimama huku nikiteremka na kumlipa pesa. Niliweka begi langu begani na kuiendea ile nyumba ambayo haikuwa ile niliyoitambua kuwa ni ya Dokta Kashushu huku yule dereva akihangaika kugeuza gari yake ili arudi kituoni kwake, nami nikabisha hodi kwenye ile nyumba. Mlango ulifunguliwa na binti ambaye nilihisi kuwa ni msaidizi wa ndani wa nyumba ile, na wakati huo yule dereva alikuwa ameshageuza gari yake na kuanza kuondoka. Nilimgeukia na tukapungiana mikono kuagana, kisha nikamgeukia yule binti aliyefungua mlango. Nilimtaka radhi na kumuomba maji ya kunywa. Hii ilikuwa ni njia ya kumpoteza yule dereva wa teksi ili aelewe kuwa safari yangu iliishia kwenye ile nyumba, sikutaka ajue kuwa nilikuwa naenda kwenye ile nyumba iliyokuwa juu ya kilima kando ya bwawa. Nilikunywa maji na kumshukuru yule binti, kisha nikaiendea ile nyumba ya Dokta Kashushu huku moyo ukinidunda kwa nguvu. Nisingeshangaa kabisa kama ningefika kwenye ile nyumba na kukuta mfuasi wa Wagga Maingo akinisubiri.
Maisha yangu sasa yalikuwa yamefikia hatua ya kuwa na wasiwasi kiasi hicho.
 
SEHEMU YA 37

. Nilimgeukia na tukapungiana mikono kuagana, kisha nikamgeukia yule binti aliyefungua mlango. Nilimtaka radhi na kumuomba maji ya kunywa. Hii ilikuwa ni njia ya kumpoteza yule dereva wa teksi ili aelewe kuwa safari yangu iliishia kwenye ile nyumba, sikutaka ajue kuwa nilikuwa naenda kwenye ile nyumba iliyokuwa juu ya kilima kando ya bwawa. Nilikunywa maji na kumshukuru yule binti, kisha nikaiendea ile nyumba ya Dokta Kashushu huku moyo ukinidunda kwa nguvu. Nisingeshangaa kabisa kama ningefika kwenye ile nyumba na kukuta mfuasi wa Wagga Maingo akinisubiri.
Maisha yangu sasa yalikuwa yamefikia hatua ya kuwa na wasiwasi kiasi hicho.
Nilimkuta mlinzi wa nyumba ile akilima-lima kwenye eneo la ile nyumba, ambayo kando yake kulikuwa na nyumba nyingine ndogo, kama banda la uani, ambalo nilielewa kuwa ilikuwa ndio nyumba ya yule mlinzi. Baada ya kusalimiana naye yule mlinzi aliyekuwa na asili ya kigogo, nilimpatia ile barua iliyoandikwa na mke wa Dokta Kashushu aliyeitwa Rukia huku nikijitambulisha kuwa mimi ni mdogo wa yule dada, kwani ndivyo ambavyo ile barua ya mke wa Dokta Kashushu ilivyonitambulisha. Kwamba mimi ni mdogo wake na kuanzia wakati ule nitakuwa nikiishi pale na yeye alitakiwa anipe ushirikiano wa kutosha. Kwa mujibu wa barua ile, yule dada alimfahamisha yule mlinzi kuwa yeye alikuwa anasafiri kwenda masomoni nje ya nchi na hivyo mimi ndiye nitakuwa naishi kwenye ile nyumba kwa muda wote ule amabao yeye hatakuweppo, ambao hakutaja ni muda gani. Yule mlinzi alinitazama kwa mashaka kidogo baada ya kusoma ile barua, lakini nilipotoa zile funguo za nyumba hakuwa tena na kipingamizi na alianza kuninyenyekea kwa heshima, akitambua kuwa sasa mimi ndio nilikuwa muajiri wake. Niliingia kwenye ile nyumba na kuanza kuikagua haraka haraka. Kwa hakika ilikuwa ni nyumba nzuri ya vyumba vitatu, sebule, sehemu ya kulia chakula na bafu na choo. Na kwenye chumba kikubwa cha kulala, Master bedroom, kulikuwa kuna bafu na choo humo humo ndani.
Kama jinsi ilivyokuwa nyumbani kwa Kelvin...
Lakini zaidi ya kitanda kimoja na godoro ambavyo bado havikuwa vimefungwa ipasavyo, hakukuwa na kitu kingine chochote mle ndani.
Sasa kwa nini Dokta Kashushu aliniambia kuwa vitu vyote nitakavyovikuta mle ndani ni mali yangu? Alimaanisha hiki kitanda...au...?
Niligundua kuwa mlango wa nyuma wa ile nyumba ulikuwa umefungwa kwa ndani na funguo zake zilikuwa zikining’inia kwenye tundu ya funguo ya mlango ule kwa ndani. Nilizitazama zile funguo tatu nilizopewa na Dokta Kashushu, ambapo moja ilifungua lile geti la chuma lililokuwa kwenye mlango wa mbele wa nyumba ile na ya pili ilifungua mlango wenyewe. Ile ya tatu ilikuwa tofauti sana na funguo za nyumba. Ilikuwa kama...lakini haileti maana...sasa kwa nini Dokta Kashushu alinipa ule ufunguo?
Nilitoka nje na kuitazama ile nyumba kwa umakini. Ilikuwa imejengwa kwenye mwinuko, na ile sehemu iliyokuwa imeinuka ilitumika kujengea gereji ya gari ambayo iliifanya ile nyumba ionekane kama ya ghorofa moja, ilhali ile sehemu ya chini ndipo kulipokuwa na ile gereji. Nilirudi ndani na kufungua mlango uliokuwa kando ya ule wa kuingilia bafuni na kuteremka ngazi zilizonifikisha kwenye ile gereji ambayo ilikuwa ina kiza kidogo. Nilipapasa ukutani na kuwasha taa na hapo nikatoa pumzi ya mshangao.
Kwenye ile gereji kulikuwa kuna gari ndogo ambayo ilikuwa imefunikwa kwa turubai maalum lililoificha kabisa. Niliisogelea ile gari na kulifunua lile turubai na pale nilibaki nikiwa nimesimama nikiitazama ile gari mpya na ya kifahari sana. Niliizunguka ile gari huku nikiitamani kwa uzuri wake. Ilikuwa ni gari aina ya Mitsubishi Diamante, ya rangi nyeusi metallic yenye vioo vya tinted. Ilikuwa mpya kabisa na hata namba ilikuwa haina. Sikuamini macho yangu na nikautazama tena ule ufunguo wa tatu uliokuwa pamoja na zile funguo mbili za nyumba ile nilizopewa na Dokta Kashushu, na nikatoa mguno wa mshangao na furaha kwani haikuwa na shaka kabisa kuwa ile funguo ilikuwa ni ya ile gari. Nilifungua mlango wa ile gari na kuipiga stati kwa kutumia ule ufunguo, na ile gari ilinguruma na kuwaka mara moja. Kwenye kiti cha nyuma cha ile gari kulikuwa kuna vibao vya namba za ile gari, ambazo zilikuwa ni mpya na za kisasa. Nilifungua sehemu ambayo madereva wengi hapa kwetu hutumia kuwekea kadi za gari pale mbele (Glove Compartment) na nikakuta kadi ya ile gari, ikiwa katika jina la mke wa Dokta Kashushu.
Rukia bint Mkiwa.
Nilikumbuka maneno ya Dokta Kashushu wakati akinikabidhi zile funguo.
“...na vitu vyote utakavyovikuta humo ni mali yako kuanzia leo...hiyo ni namna yangu ya kukusaidia katika mtihani huu Tigga...”
“Oh, Dokta Kashushu...yaani, Oh, Mungu wangu, yaani umeniachia hii gari?” Nilijisemea mwenyewe huku nikiizunguka na kuipapasa ile gari kwa kutoamini.
Duh! Dokta Kashushu! Wewe ni mtu wa aina gani lakini...? Ahsante sana huko uliko...!
Nilifurahi sana na kwa muda nilisahau matatizo yangu. Kwani kuwa na usafiri kungenirahisishia sana mienendo yangu iliyobakia katika kutafuta ukweli wa matukio haya ya ajabu yanayonikabili. Niliiacha ile gari ikiunguruma mle gereji nami nikarudi ndani ya ile nyumba na kuanza kufanya usafi. Kisha nilirudi na kuizima ile gari na kumuomba yule mlinzi wangu aje tusaidiane kukifunga kile kitanda kama inavyotakiwa.
Wakati tukifanya ile kazi nilikuwa nikimtupia maswali mbalimbali juu ya yule mke wa Dokta Kashushu ambaye yeye ndiye alimtambua kuwa ndiye mwenye nyumba, na nikagundua kuwa yule dada alimwambia yule mlinzi kuwa hakuwa na mume na alikuwa akijishughulisha na biashara zake binafsi ambazo hata yule mlinzi aliyeitwa Thonya hakuzijua. Naye alijaribu kunihoji juu ya maisha yangu na nikamwambia kuwa nimekuwa nikiishi Namibia kwa miaka mingi, na sasa nimerejea nchini kufanya kazi katika kampuni niliyokuwa nikiifanyia kazi huko Namibia, ambayo imefungua ofisi hapa nchini.
Alipotaka kujua jina langu nilimwambia kuwa nilikuwa naitwa Nuru bint Mkiwa.
Baada ya kumaliza shughuli hiyo nilioga na kujibwaga kitandani. Muda mfupi baadaye nilipitiwa na usingizi mzito, hasa kutokana na kwamba usiku uliopita sikulala vizuri.

--

Nilipoamka ilikuwa jioni na njaa ilikuwa ikiniuma sana. Nilibandika vile vibao vya namba kwenye ile gari na kutoka nayo nikimwambia Thonya kuwa nilikuwa naenda mjini mara moja. Niliingia kwenye kituo cha mafuta cha Suca na kuifanyia huduma muhimu (service) ile gari, kwani nilijua kuwa haikuwa imetembea kwa muda mrefu. Na wakati wale wataalamu wa kile kituo cha mafuta wakiifanyia marekebisho ya muhimu ile gari, nilikiendea kibanda cha simu kilichokuwa jirani na kupiga simu ile namba ya Kamishna Msaidizi John Vata. Ile simu haikuita kabisa, yaani ilikuwa kimya kabisa na moyo wangu ulizama kwenye simanzi. Bado iliniwia vigumu sana kuamini kuwa John Vata alikuwa amefikwa na umauti namna ile. Nilimpigia simu dada yangu Koku.
“Tigga? My God, uko wapi wewe...? Tuna wasiwasi sana juu yako! Yaani...hujajisalimisha kwa Kamishna Vata mpaka sasa? Sasa unadhani utaendelea kukimbia hovyo jijini mpaka lini mdogo wangu...mambo yametokea huku na hatujui uko wapi...!”
“Kamishna Vata...hajawasiliana na wewe...?” Nilimuuliza kwa wasiwasi.
“No! Angalau sio katika siku za hapa karibuni. Kuna wakati alinifuata ofisini na kuniambia kuwa ulikuwa ukimpa taabu...kwamba unampigia simu halafu hutaki kujitokeza...what’s the matter with you Tigga?”(...una tatizo gani Tigga?). Koku aliniuliza kwa hasira.
“Aaah, Koku...huu sio muda wa kulaumiana. Ni mambo gani hayo yaliyotokea tena...?”
“Kelvin is dead Tigga...(Kelvin amekufa Tigga)”
“Ke-Whaat? Mungu wangu, sasa...” Niliropoka kwa mshituko na nikahisi mbingu zikinishukia na pumzi zikinibana. Kelvin amekufa? Oh, Mungu wangu...kwanza John Vata...na sasa Kelvin...?
“Li...lini Koku? Amefariki lini...”
“Juzi. Hospitali. Na tumemzika mchana huu wa leo. Inasikitisha sana Tigga...ndugu zake, mama yake...wana simanzi kubwa, nao walitarajia wewe ungekuwepo kwenye mazishi, ingawa wanajua kuwa umekumbwa na matatizo...Kelvin aliwaeleza kwa kiasi fulani, nami nikawathibitishia.” Koku alinijibu haraka haraka. Ilinijia kumbukumbu ya Kelvin akiwa amelala sakafuni chumbani kwake huku akivuja damu. Akiniambia niondoke eneo lile kabla wale wauaji hawajanikuta. Na kuniomba samahani kwa kutoniamini hapo mwanzo. Niliumia sana na nikajitahidi kuzuia machozi yasinibubujike.
“Tigga...? Upo?” Koku aliniuliza kwenye simu.
“Ndiyo Koku nipo...hii habari imenishitua sana. Amezikwa wapi...?”
“Makaburi ya Kinondoni...Kulikuwa kuna askari kibao Tigga...na nadhani walikuwa wakikuvizia wewe. Ndio maana nakuambia kuwa jitahidi ujisalimishe kwa Kamishna Vata...he is the only one who can help you now Tigga (...kwa sasa ni yeye pekee ndiye anayeweza kukusaidia Tigga)” Koku aliniambia na moyo wangu uliumia kupita kiasi
“Kamishna Vata amekufa Koku...tulikuwa wote, ukatokea mlipuko...he is deadtoo...!(naye amekufa vile vile...!)”Nilimjibu kwa uchungu huku nikitoa mguno wa kilio.
“Whaaat?” Koku aliuliza kwenye simu nami sikuweza kuendelea na mjadala ule mchungu, nilikata simu na kurudi haraka kwenye gari yangu mpya. Niliendesha gari bila uelekeo maalum huku nikibubujikwa na machozi. Sikupenda kumkatia simu dada yangu namna ile lakini sikuwa na uwezo wa kuendelea kuongea naye hata neno moja zaidi baada ya habari zile.
Kelvin amekufa. John Vata amekufa. Moyo uliniuma na sikujua ni kipi kati ya vifo vile viwili kilichonisikitisha zaidi. Kelvin alishindwa kuniamini na nikamchukia kwa hilo, nikavunja uchumba wangu naye, lakini hakutakiwa kufa...na aligundua mapema kuwa alinikosea, ndio maana aliniomba msamaha na kunishauri niondoke haraka na nimuache yeye akiwa anavuja damu sakafuni.
John Vata alijitolea kuja kunisaidia hata baada ya kumpa taabu sana na kumfanyia vituko na kumjibu majibu ya mkato...na kwa kufanya hivyo akakutana na kifo...
...kwa sababu inaelekea kuwa kila unapopita unaacha kifo au vifo nyuma yako...
Maneno ya John Vata. Na inaelekea kuwa ni ya kweli tupu!
Oh, Mungu wangu...
Nilikuwa nikiendesha gari huku nikilia peke yangu. Njaa iliyokuwa ikiniuma iliyeyuka yenyewe na wala sikujisikia tena hamu ya kula kitu chochote. Na ilinijia akilini kuwa mambo yote haya, machungu yote haya, ni kwa sababu ya kushuhudia lile tukio la kutisha la kule msituni...na fitna za yule muongo aitwaye Wagga Maingo, natumai ile sindano niliyomchoma itakuwa imemuondoa duniani kufikia sasa.
Hatimaye niliishia kuegesha gari yangu kando ya bahari ya Hindi eneo la Ocean Road na kubaki mle ndani nikitazama bahari huku nikisononeka peke yangu juu ya misiba ile iliyoniangukia kwa kishindo. Sasa niliuona kabisa mwisho wangu ukinikaribia kwani sikuwa na shaka kabisa kuwa yule mwanamke mwenye hijab...The Virus...ataniua.
 
SEHEMU YA 38

Hatimaye niliishia kuegesha gari yangu kando ya bahari ya Hindi eneo la Ocean Road na kubaki mle ndani nikitazama bahari huku nikisononeka peke yangu juu ya misiba ile iliyoniangukia kwa kishindo. Sasa niliuona kabisa mwisho wangu ukinikaribia kwani sikuwa na shaka kabisa kuwa yule mwanamke mwenye hijab...The Virus...ataniua. Salama yangu ni kuendelea kuushikilia ule mkanda wa video wenye ushahidi dhidi ya akina Wagga Maingo na yule kigulu aliyekuwa nao kule msituni.
Kwanza yule kigulu ni nani? Kwa nini sijamuona tena tangu siku ile kule msituni?
Lakini swali kubwa kabisa lililokuwa likiusakama ubongo wangu sasa ni kwamba baada ya kifo cha John Vata, niupeleke kwa nani sasa ule mkanda?
Baada ya kuzubaa pale pwani kwa muda bila ya kupata uamuzi wa kufaa, niliamua kurudi kwenye makazi yangu mapya Kimara, na ndipo nilipopita tena kwenye ile barabara ambayo kando yake ilikuwako ile kasino maarufu jijini, La Dreamer, na nilipoiona tu sikufikiri zaidi. Nilitafuta sehemu muafaka nikaegesha gari yangu mpya kwenye maegesho ya ile kasino iliyoificha kasino nyingine ndani yake na kuingia mle ndani kwa mara nyingine tena. Huku moyo ukinipiga haraka haraka, nilipitiliza moja kwa moja hadi kwenye ule mlango wa vioo na kupanda lifti kuelekea kule ilipokuwa ile kasino iliyoitwa The Rickshaw. Niliteremka kutoka kwenye lifti na kujikuta tena kwenye ile korido ya vioo na ile hisia ya kuwa nimo ndani ya boksi kubwa la kioo ilinijia tena. Mlangoni niliwaona wale mabaunsa wawili nami niliwapita na kuingia ndani ya ile kasino niliyokuwa na hamu sana ya kuiingia tangu siku ile nilipoigundua. The Rickshaw ilikuwa tofauti sana na ile kasino ya kule chini, kwani hapa niliona wazi kuwa kulikuwa kuna mambo makubwa zaidi. Kwanza hakukuwa na mwanga wa kutosha, ambao nadhani uliwekwa vile kusudi ili kuficha mambo yaliyokuwa yakifanyika mle ndani,kwamba kila mtu awe huru kufanya lake bila kuwa na shaka ya kuonwa na wengine. Nilifinya macho na kuangaza mle ndani na baada ya muda, macho yangu yalizoea ule mwanga wa mle ndani na kwa kihoro kikubwa nilishuhudia wahudumu wa mle ndani wakiwa wamevaa nusu uchi! Yaani kama unavyoona kwenye makasino ya kule ulaya kwenye filamu. Walikuwa wamevaa vijikaptura vya jeans vifupi sana vilivyokatwa kama chupi, na sidiria za kitambaa cha jeans lakini chepesi zaidi. Kwa vile viji-kaptura walivyovaa akina dada wale, karibu nusu nzima ya makalio yao ilikuwa nje! Kivazi kingine kilichokuwa miilini mwao wahudumu wale baada ya hivyo nilivyovitaja ni viatu virefu. Wote walikuwa na shepu nzuri na za kuvutia. Sikuamini macho yangu.
Ina maana hivi ndivyo akina Kachiki wanavyovalishwa wakija kutoa huduma humu ndani?
Niliangaza mle ndani kwa muda, kisha nikaamua kwenda kuketi kwenye moja ya viti virefu vilivyokuwa kaunta, nikiacha meza na viti zilizokuwa kwenye ukumbi mkubwa uliokuwa umetapakaa wateja kadhaa waliokuja kujistarehesha mle ndani, na kuanza kuangaza mle ndani kwa utulivu, ingawa moyoni nilikuwa na wasiwasi mkubwa, kwani sikujua nitagundua nini humu ndani ambacho Mr.Q alitaka nikigundue. Kwa hakika TheRickshaw ilikuwa ni kasino ghali kuliko ile ya kule chini. Hili nililiona mara moja kutokana na watu waliokuwemo mle ndani. Wengi wao walikuwa ni watu wenye asili ya kihindi, kiarabu na wazungu, ingawa kulikuwa na watu weusi wachache. Kulikuwa kuna wanaocheza pool, kamari za kila aina na kwenye kona moja ya ule ukumbi kulikuwa kuna steji ambapo akina mama wawili walikuwa wakicheza muziki wa vyombo vitupu uliokuwa ukisikika kutoka kwenye spika zilizokuwemo mle ndani, na muziki uliokuwa ukitoka kwenye spika zile ulikuwa ni ambao nimewahi kuusikia kabla, lakini huu ulikuwa ni wa vyombo vitupu. Mhudumu wa kaunta aliniuliza nilihitaji kinywaji gani, nami bila kusita nikaagiza Red Bull. Niliwekewa kile kinywaji mbele yangu juu ya kaunta nami nikaendelea kuangaza mle ndani kwa udadisi wa hali ya juu.Macho yangu yalirudi kule kwenye steji walipokuwa wakicheza wale akina mama wawili, au niseme ilikuwa ni miji-mama. Walikuwa wakicheza ule wimbo wa sasambu-sasambu huku wakisasambua nguo zao moja moja na niliona walikuwa wamepata watazamaji wengi waliokuwa wakishangilia na kupiga mbinja kila kiwalo kilipotolewa huku wakitupa mapesa kule stejini ili kuwashawishi wale akina mama waendelee kutoa nguo zao na kuwaonesha miili yao. Nilibaki nikiwa nimeduwaa. Mambo waliyokuwa wakiyafanya wale akina mama ni sawa kabisa na yale ambayo huwa tunayaona kwenye “Kitchen Party”,cha ajabu hapa yalikuwa yanafanywa mbele ya midume ya kizungu, kihindi, kiarabu na baadhi ya waswahili. Nilitupa macho yangu upande mwingine wa ile kasino na nikaona kuwa kulikuwa kuna milango ya mninga iliyokuwa imejipanga katika upande ule, ambayo nilidhani ilikuwa ikifungukia kwenye vyumba. Na hata pale nilipokuwa nikiitazama ile milango, mmoja ulifunguliwa na mwanamme mmoja wa kiarabu alitoka na mwanadada mmoja wa kiswahili ambaye sikuhitaji kabisa kuambiwa kuwa alikuwa changudoa. Na kwa jinsi walivyokuwa wameshikana, sikuwa na shaka kuwa walikuwa wametoka kufanya ngono.
Mungu wangu! Yaani kuna danguro humu humu!
Na muda mfupi baadaye, jamaa mmoja wa kiswahili aliyekuwa akinyonyana na kupapasana na binti mwingine kwenye meza waliyokuwa wamekaa kwenye ule ukumbi, aliinuka na kuongozana na yule binti kuelekea kwenye vile vyumba.
“Uko peke yako?” Nilishitushwa na sauti ya kiume ya yule mhudumu wa kaunta aliyeniuliza huku akipangusa kaunta kwa kitambaa. Nilimtazama kwa muda na kumjibu kwa kichwa kuwa nilikuwa peke yangu.
“Ni nini unachokitaka hapa? Wanawake huwa hawaji peke yao hapa...” Aliniambia bila kunitazama huku akiendelea kupangusa kaunta yake kwa kitambaa.
“Kuna mtu namsubiri...tuna miadi tukutane hapa...kwani hairuhusiwi?” Nilimjibu na kumuuliza hapo hapo. Yule bwana alibetua mabega yake tu na kuendelea na shughuli zake bila kuongea zaidi. Sikuelewa nini maana ya kitendo kile, lakini nilielewa kuwa sikutakiwa nikae pale peke yangu kwa muda mrefu. Tayari nilikuwa nimeshaanza kuleta wasiwasi ndani ya nyumba. Nilivuta bakuli kubwa lililokuwa limejaa korosho na kuanza kuzitupia kinywani mwangu taratibu huku nikishushia kwa Red Bull yangu.
Nifanye nini sasa?
Muda huo aliingia mwanamume mmoja ndani ya ule ukumbi na kuketi kwenye kiti cha tatu kutoka kile nilichokalia nami sikumtilia maanani, nikiendelea kuangaza mle ndani, lakini baada ya muda niligundua kuwa yule mtu aliyeingia alikuwa akinitazama sana. Nilimgeukia kumtazama naye akaamua kutazama saa yake, kisha akainuka na bilauri yake ya kinywaji na kwenda kuketi kwenye meza iliyokuwa katikati ya ule ukumbi na kuanza kuangalia ile sasambu-sasambu iliyokuwa ikiendelea kule kwenye steji, sasa hivi ile miji-mama ikiwa imebaki na vibikini tu wakiwa wamejifunika vitambaa laini sana vilivyoonesha kila kitu, na ukumbi wote sasa ulikuwa ukizizima kwa vifijo na hoi hoi, wale mashabiki wakiwashawishi wale akina mama watoe kabisa zile nguo zilizobakia miilini mwao, nao wakitishia kuvua na kuvaa tena.
Nilimtazama yule jamaa aliyeingia mle ndani kwa makini. Alikuwa mwembamba na mfupi, rangi yake maji ya kunde, nywele za shombe, na alikuwa amevaa miwani myeusi usoni kwake. Sasa miwani myeusi ya nini humu ndani?
Ni nani huyu? Mbona ameonesha udadisi sana kwangu? Ni kwamba amenitamani tu kama kawaida ya matamanio ya wanaume, au kuna kitu kingine...?
Niliwatazama wale akina mama wenye maumbo makubwa yaliyojazia wakifanya yale mambo ya aibu na nikajihisi kudhalilika kusiko kifani. Na wakati nikiwatazama, nilipatwa na mshituko mkubwa sana na moyo ukaanza kunienda mbio. Niliteremka kwenye kile kiti kirefu na kusogea katikati ya ule ukumbi na kuwatazama kwa makini wale akina mama. Hususan mmoja kati yao, kwani ilinijia akilini mwangu kuwa nilishawahi kumwona sehemu kabla ya pale na akili yangu ilikuwa ikizunguka kujaribu kutafuta ni wapi hasa nilipomuona.
Nina hakika nimewahi kumuona huyu mwanamke sehemu...ni wapi...?
Na hata pale wazo hilo lilipokuwa likipita kichwani mwangu, yule mwanamke aliinama na kuwatazama wale wanaume wa makabila mchanganyiko huku akiwa ameinua makalio yake kuelekea ukutani na wale watu walikuwa wakimpigia kelele kumshawishi awageuzie wao, na yule mwanamke aliwatolea tabasamu fulani la tash-wishi, huku akiwa amerembua macho kwa namna ya kuchokoza hisia za wanaume. Na hapo ikanijia.
Lile tabasamu! Nimeshaliona mahali...
Oh, My God! Nilikumbuka! Nilikumbuka nilimuona wapi yule mwanamke na moyo wangu uliingia baridi na nikaanza kurudi pale kaunta nilipokuwa nimekaa hapo awali taratibu huku akili ikinitembea.
Yule mwanamke alikuwa ni mmoja kati ya ile mijimama miwili iliyokuwa kwenye picha niliyooneshwa na marehemu Dick Bwasha ofisini kwake siku ambayo baadaye alikutwa akiwa amefariki!
Ni yeye! Ni lile tabasami ndilo lililokuwa kwenye sura yake wakati anapigwa ile picha akiwa na mwenzake wote wakiwa utupu kabisa kitandani pamoja na yule meneja wa benki aliyekuwa mwingi wa jeuri na dharau.
Ah! Sasa nimemkuta “live” hapa The Rickshaw! Ama kwa hakika Mr. Q alijua kuwa hapa ndipo kwenye majibu ya maswali yangu. Nilimtazama yule mwanamke mwingine aliyekuwa akisasambua na yule niliyemtambua pale stejini, lakini yule hakuwa yule aliyekuwa kwenye ile picha niliyooneshwa na Dick Bwasha marehemu.
Na muda huo taa za pale ukumbini walipokuwa wakicheza wale akina mama zilizimika na nikashuhudia zile bikini zilizokuwa zimevaliwa na ile mijimama zikitupwa kule walipokuwa wamekaa wale wanaume waliokuwa wakiwashangalia. Ile midume ilizigombea zile bikini kama mijibwa inayogombea nofu la nyama, huku waliobahatika kuzitia mikononi mwao wakizibusu na kushangilia. Aibu iliyoje hii!
Taa zilipowashwa tena kule stejini, wale akina mama walikuwa wametoweka, wakiacha miguno na hoi hoi kutoka kwa wale wanaume waliojazana kushuhudia mchezo wao ule mchafu. Nilichoka! Yaani haya mambo ndio yako hivi! Niliagiza Red Bull nyingine na kubaki nikiangaza huku na huko mle ndani huku akili ikinitembea. Watakuwa wameenda wapi wale akina mama? Ni lazima niongee na yule mwanamke. Nimuulize kuhusika kwake na tafrani yote hii inayonikabili.
Lakini kaenda wapi sasa?
Niliinuka na kuelekea sehemu iliyokuwa na vyoo vya akina mama ndani ya ile kasino ambayo sikupata taabu kuiona, nikiwa na matarajio kuwa huko ndiko ningewakuta wale akina mama. Haswa yule mmoja niliyemtambua kutoka kwenye picha ya Dick Bwasha.
Kule chooni sikukuta mtu. Nilirudi tena kwenye kiti nilichokuwa nimekalia hapo mwanzo huku akili ikinizunguka.Kapotelea wapi tena?
 
SEHEMU YA 39

Niliinuka na kuelekea sehemu iliyokuwa na vyoo vya akina mama ndani ya ile kasino ambayo sikupata taabu kuiona, nikiwa na matarajio kuwa huko ndiko ningewakuta wale akina mama. Haswa yule mmoja niliyemtambua kutoka kwenye picha ya Dick Bwasha.
Kule chooni sikukuta mtu. Nilirudi tena kwenye kiti nilichokuwa nimekalia hapo mwanzo huku akili ikinizunguka.Kapotelea wapi tena? Bila shaka kutakuwa kuna chumba cha kubadilishia nguo sehemu fulani mle ndani, naye atakuwa huko. Niliamua kuendelea kusubiri pale pale nikiamini kuwa mlango wa kutokea mle ndani ni ule ule mmoja tu.
Wakati nikisubiri huku nikinyonya Red Bull na kuendelea kuangaza mle ndani, nilipata mshituko wa hali ya juu baada ya kumuona yule jamaa mwenye nywele za shombe aliyevaa miwani ambaye hapo mwanzo nilimtilia mashaka kwa kunitazama sana akinyonyana ndimi na mwanaume mwingine aliyenyoa upara ambaye sikuweza kujua kwa urahisi iwapo alikuwa mmbantu au muasia kutokana na mwanga hafifu wa eneo lile.
Khah! Hii sasa dharau hii! Yaani...Ah!
Yaani sikuamini, na nikahisi kichefuchefu kuona midume mizima ikifanya mambo ya aibu namna ile. Na hata pale nilipokuwa nikistaajabia tukio lile, nilishuhudia yule jamaa mwenye upara akimpapasa yule shombe kama kwamba alikuwa mwanamke!.
Heh! Yaani kumbe huyu jamaa shoga! Mmnh! Mbona makubwa!
Nilimgeukia yule mhudumu wa pale kaunta ili nimuulize juu ya maajabu yale, lakini wakati huo huo nikamuona yule mama niliyekuwa nikimvizia akitokea sehemu nyuma ya ile steji waliyokuwa wakichezea na mwenzake na kuja pale kaunta. Alikuwa amevaa suruali ya skin tight iliyoonesha shepu yake kubwa ambayo sikuwa na shaka ilikuwa ikiwapagawisha wanaume kwa kadiri alivyotaka, na juu alikuwa amevaa shati fupi lililoishia juu kidogo ya kiuno chake ilhali mikono ya shati lile ikiiishia chini kidogo ya viwiko vyake. Chini alikuwa amevaa viatu vya chini kama vile vyangu vya kamba nilivyonunua mtumbani kule Manyoni katika hatua za mwanzo kabisa za mkasa huu , na kwapani kwake alikuwa amefumbata mkoba mzuri sana wa kike. Nilimkodolea macho yule mwanamke mtu mzima na nikastaajabia kitendo cha mama kama yule kujihusisha na mambo kama yale, hasa nikiikumbuka ile picha aliyopiga akiwa na Dick Bwasha. Alipita pale kaunta na kumsalimia yule mhudumu huku akimtolea tabasamu zuri sana na kuelekea kwenye mlango wa kutokea nje ya ule ukumbi wa starehe uliojaa madhambi. Bila kufikiri wala kujishauri nilimlipa yule mhudumu pesa yake na kuinuka kumfuata.
“Vipi, uliyekuwa ukimsubiri ameshafika? Au kakugandisha?” Yule mhudumu aliniuliza kwa kejeli. Niligeuka kumtazama na hapo nilimuona yule mwanamke mwingine aliyekuwa akifanya mambo ya unyago na yule mama pale stejini akitokea kule alipotokea mwenzake akiwa ameambatana na mwanaume wa kihindi ambaye alikuwa amemshika kiuno huku wakichezeana kwa mahaba, nami badala ya kumjibu yule mhudumu, nilimbetulia mabega kama jinsi yeye alivyonibetulia hapo mwanzo na kutoka nje ya ule ukumbi kumfuata yule mama.
Nilimuwahi kwenye lifti na nikajikuta nikiwa naye ndani ya ile lifti wakati ikiteremka kutoka kwenye ghorofa ya juu ya lile jengo lililohifadhi zile kasino mbili. Nilimtazama na kujikohoza kidogo kisha nikamsalimia kwa kumpa shikamoo. Yule mama alitabasamu na kuitikia salamu yangu. Nilimtazama naye alikuwa akinitazama huku akiwa amefanya tabasamu dogo.
“Anti...samahani. Nilikuwa na shida na wewe...sijui tunaweza kuongea kidogo...?” Nilimuuliza kwa mashaka. Yule mama alicheka.
“No, no, no....una shida na mimi Anti? Hapana, mi’ huwa sifanyi wanawake bwana! Kama unataka wanawake sema nitakuonesha wasagaji kibao hapo juu, lakini itabidi unilipe!” Yule mama aliniambia huku akicheka nami nikabaki mdomo wazi.
“Eti? Hapana Anti! Sio hivyo, sina nia hiyo, Loh!” Nilimjibu kwa kihoro huku nikimtazama kwa mshangao.
Mmnh! Yaani mambo ya The Rickshaw ni ufirauni mtupu! Sasa na mimi kwa kuja huku tayari nimeonekana ni miongoni mwao! Eh, Mungu wangu nisamehe mja wako! Mbona n’nazidi kutumbukia kwenye mambo ya ajabu?.
Ile lifti ilifika chini na yule mama alitoka na kuanza kuelekea kwenye ule mlango uliotokea kwenye ile kasino nyingine ya chini nami nikamfuata.
“Sasa ulikuwa na nia gani binti! Hii The Rickshaw bwana! Hakuna kinachotafutwa humu zaidi ya hilo...we vipi?” Alinisemesha bila kunitazama huku akiendelea na safari yake. Nilimshika mkono na kumsihi anisikilize. Aliuchomoa mkono wake na kunitazama kwa macho ya kuuliza.
“Anti, naomba dakika chache tu za muda wako. Labda tukae kidogo hapa tupate kinywaji...nina tatizo kidogo tu ambalo nadhani wewe utaweza kunisaidia...please!” Nilimwambia kwa kumsihi. Alinitazama kwa muda, kisha bila ya kusema neno alichagua meza iliyokuwa karibu pale kwenye ile kasino ya chini na tukaketi.
“Sema. Una shida gani, na sema upesi kwani sina muda wa kupoteza.” Aliniambia.
“Anti, ninaamini nimepata kukuona mahali. Na nilipokuona ulikuwa na mtu fulani. Nina hitaji taarifa za huyo mtu niliyekuona naye.” Nilimwambia kwa upole huku nikijiuliza iwapo ile ilikuwa ni njia nzuri ya kuanzisha mazungumzo na yule mama ambaye kila nilipomtazama, neno “shangingi” lilikuwa likipita kichwani mwangu. Alinitazama kwa namna ya kutoelewa.
“Sema kitu kinachoeleweka binti! Uliniona mahali, sasa mahali hapo ni wapi? Mimi natembea sehemu nyingi bwana!” Aliniambia kwa kukereka. Hapo mhudumu alifika, nikamwambia aagize atakacho.
“Castle ya kopo...mbili. Huyu atalipa!” Alimuagiza huku akinioneshea kidole, nami nikaafikiana naye kwa kichwa huku nikijiuliza kwa nini ameagiza Castle mbili. Mimi sikutaka kuagiza chochote.
“Actually, ni picha ambayo ulikuwa umepiga..ukiwa na mwenzako na mtu mwingine...” Nilianza kumuelezea, lakini hapo yule mama aliangua kicheko kikubwa sana. Nikashangaa ni nini kinachomchekesha, lakini kabla sijamuuliza alinijibu.
“Ah! We’ binti kweli juha. Mimi kupigwa picha ndio kazi yangu bwana! Nimepiga picha nyingi sana ambazo chache zinaonekana hapa nchini, lakini nyingi zinauzwa nje ya nchi na ninajipatia pesa nzuri tu. Hata mikanda ya video ipo niliyopiga. Sasa wewe kuona picha ndio inakuwa ajabu? Hiyo ni kazi yangu bwana!”
“No Anti. Sioni ajabu. Ila picha yenyewe...picha yenyewe ilikuwa ya utupu! Na ilikuonesha wewe na mwanamke mwingine mkiwa na mwanaume mmoja kitandani...sasa ni huyo mwanaume ndiye ninayetafuta habari zake.”
“Binti, kupiga picha za utupu kama unavyoziita, ni miongoni mwa kazi zangu. Si umeona mambo niliyokuwa nikiyafanya mle ndani sasa hivi? Nayo ni kazi yangu, na ndio inayoniweka mjini. Na wala sioni haya juu ya hilo. Sasa kuhusu huyo mtu niliyepiga naye picha, kama ni mumeo basi si swala langu. Ni yeye mwenyewe ndiye aliyeona kuwa anahitaji huduma ya watu kama sisi, kwani nina uhakika kabisa kuwa mambo tunayoweza kumfanyia watu kama sisi wewe usingeweza kumfanyia asilani!” Alinijibu kwa jeuri na muda huo vinywaji vilifika. Alifungua kopo moja la Castle na wakati huo huo akatumbukiza kwenye mkoba wake lile kopo la pili.
“Hapana Anti, yule si mume wangu, ila kuna mali alinidhulumu nami nilikuwa namtafuta kwa hilo...unadhani unaweza kunisaidia?” Nilimuuliza.
“Kwanza ni nani? Mimi hata sina kumbukumbu ya huyo mtu unayemsema wala hiyo picha unayoisema. Ninachojua ni kwamba mimi nikiambiwa na bosi wangu kwenda kumhudumia mteja naenda, nikirudi nachukua posho yangu naondoka. Sina haja kabisa ya kujua mteja ni nani au anatoka wapi!Ndio utaratibu tuliopangiana na bosi wetu!”
“Ah, sasa ina maana humfahamu mtu aitwaye Dick Bwasha?” Nilimuuliza huku nikimtazama kwa makini, nikijua kuwa Dick Bwasha ameshakufa na kwamba kama alikuwa anamfahamu, bila shaka angejua kuwa ameshakufa. Na kwa vyovyote angesema neno au angefanya jambo la kunijulisha kuwa alikuwa akimfahamu yule mtu.
Yule mama alitikisa kichwa kumaanisha kuwa hamfahamu huku akinywa kinywaji chake. Na wala haikuonesha kuwa alikuwa akimfahamu Dick Bwasha. Yaani kwake lile jina halikuwa likimaanisha chochote. Hii ilinipoteza muelekeo na sikujua niendelee vipi.
“Kwa hiyo sasa... bosi wako ndiye anayekuunganisha na hao wateja? Kwa hiyo ndiye aliyekuunganisha na Dick Bwasha?” Nilimuuliza. Aliafiki tena kwa kichwa kabla ya kuongea. “Nd’o maana’ake! Sasa kama huyo mtu uliyeniona naye kwenye picha alikuwa ndio huyo Dick-nani-sijui, au nani, hiyo mi’ sijui, lakini huo ndio utaratibu. Na naona nimekuwa nikikuongelea tu mambo yangu bila ya sababu ya msingi. Nashukuru kwa kinywaji na sasa naomba niende!”
Hakuonesha dalili ya kuondoka. Bado alikuwa akibugia ile bia niliyomnunulia.
“Hapana Anti! Naomba nikuulize swali la mwisho! Ni muhimu sana...!” Nilimwambia lakini alitikisa kichwa vikali kukana swala lile.
“Kama lingekuwa ni muhimu ningeona angalau elfu kumi mkononi mwako sasa hivi. Hapo ningeamini kuwa kweli ni muhimu! Sasa wewe hivi hivi tu...” Yule mama alisema kijanja huku akijitia kukusanya mkoba wake tayari kwa kuondoka. Nilijua alitaka nimpe pesa ili anipe ushirikiano zaidi.
Pumbavu!
Mara moja mkononi mwangu kukawa kuna noti ya elfu kumi, na nikamtupia swali.
“Sasa...huyo bosi wako ni nani...na nitampata wapi?” Nilimuuliza. Aliikodolea macho ile pesa.
“Aaa, sasa kwa hilo siwezi kukuambia! Sio taratibu...kama ungekuwa unamtafuta kwa biashara ningekuambia, lakini ni wazi sababu zako si za kibiashara...” Alinijibu kwa mashaka. Nilimwambia kuwa ndio maana kuna ile pesa mkononi mwangu, ili anitajie bosi wake ni nani, ingawa ni kinyume cha utaratibu. Alikaa kimya kwa muda, na nikaona alikuwa akijishauri kichwani mwake. Moyo ulianza kunienda mbio kwani nilijua kuwa akinitajia, huenda nikawa nimemjua mtu atakayenikurubisha kwenye chimbuko la lile genge la akina Wagga Maingo na yule mshirika wao hayati Dick Bwasha.
“Anti, nijibu tafadhali! Bado zipo nyingi huku nilipotoa hii noti...” Nilimwambia huku nikiongeza noti ya shilingi elfu tano mkononi mwangu. Yule mama alizikodolea macho zile noti zilizokuwa mkononi mwangu.
“Ni nani huyo bosi wako? Naahidi kuwa sitakutaja kuwa ni wewe ndiye uliyenitajia!” Nilizidi kumshawishi.
Alizichukua zile pesa taratibu kutoka mkononi mwangu, lakini nilizing’ang’ania naye akashindwa kuzichukua. Tulitazamani tukiwa tumeshikilia zile pesa, kila mmoja akijaribu kuvutia kwake. Huku akinitazama kwa makini yule mama aliniambia.
“Okay binti, umetaka jina la bosi wangu nami nitakutajia. Nipe hizo pesa kwanza!”
Nilimtazama kwa muda, kisha bila kusema neno niliziachia zile pesa naye akazizamisha ndani ya mkoba wake. Tukabaki tukitazamana.
 
SEHEMU YA 40

Alizichukua zile pesa taratibu kutoka mkononi mwangu, lakini nilizing’ang’ania naye akashindwa kuzichukua. Tulitazamani tukiwa tumeshikilia zile pesa, kila mmoja akijaribu kuvutia kwake. Huku akinitazama kwa makini yule mama aliniambia.
“Okay binti, umetaka jina la bosi wangu nami nitakutajia. Nipe hizo pesa kwanza!”
Nilimtazama kwa muda, kisha bila kusema neno niliziachia zile pesa naye akazizamisha ndani ya mkoba wake. Tukabaki tukitazamana.
“Utahitaji kuongea na The Bastard...yeye ndiye bosi.” Alinijibu na nikapata mlipuko mkubwa wa moyo na hapo hapo ukaanza kunienda mbio.
“Eti Whaat?The Bastard...?” Niliropoka huku nikimkodolea macho yule mwanamke mtu mzima mwenye kupiga picha za utupu na kucheza unyago kwenye kasino. Nini maana yake hii? Yaani The Bastard ni mtu anayeishi? Ni jina la mtu? Ina maana yule mtu aliyeuawa na Macho ya Nyoka kule porini aliposema “Find The Bastard” alikuwa anamaanisha kuwa nimtafute mtu aitwaye The Bastrad!
Oh, My God...This is unbelievable!( hii ni ngumu kuamini!).
“He! We’ binti vipi? Mbona hivyo...?” Yule mama alinishitua kutoka kwenye mawazo yangu huku akinisukuma mikono yangu na ni hapo ndipo nilipogundua kuwa nilikuwa nimemkamata mabega kwa nguvu.
“Oh, Oh...samahani! Samahani...nilikuwa...nilikuwa...nime...umesema The Bastard ndiyo bosi wako? Ni nani yeye? Na nitampataje? Yuko wapi? Oh, My God! Nitamjuaje?” Nilibwabwaja kwa papara huku nikijitahidi kumzuia yule mama asiondoke, naye akiwa tayari ameshainuka na akipachika mkoba wake begani na akinitazama kama kwamba nilikuwa mwehu, au juha kama mwenyewe alivyoniita hapo awali.
“Binti. Mimi sijui wewe ni nani na kwa nini unamtafuta huyo Dick –nani-sijui. Umetaka kujua bosi wangu ni nani nimekutajia, na hapo ndipo biashara yetu ilipoishia.Mimi naondoka na nikiondoka hapa nitakuwa sijawahi kuonana na wewe hata siku moja, na wala wewe hujaonana na mimi hata siku moja. Kama kuna mtu aliyekutajia kuwa bosi wetu ni The Bastard basi mtu huyo sio mimi! Sawa?” Aliniambia na kutoka nje ya ile kasino, akiniacha nikiwa nimepigwa na butwaa pale kwenye ile meza. Nilipopata ufahamu, tayari yule mama alikuwa ameshatoka nje. Nilikurupuka kumfuata, lakini yule mhudumu alinisimamisha akidai pesa yake. Nilimpa noti ya shilingi elfu kumi na kumwabia kuwa nitarudi kuchukua chenji yangu na kuwahi kule nje alipopotelea yule mama. Nilimkuta akiongea na dereva wa teksi.
“Samahani Anti, lakini bado ninahitaji taarifa zaidi. Huyu The Bastard...hana jina jingine? Ni wapi anapofanyia shughuli zake?” Nilimuuliza. Yule mama alinitazama, na bila kunijibu aliingia ndani ya ile teksi, kisha alinijibu huku akinitazama kupitia dirisha la ile teksi.
“We’ binti mbona unakuwa juha hivi? Nimekwambia hilo ndilo jina lake! Na hiyo ndio ofisi yake!” Aliioneshea ile kasino kwa kichwa chake, kisha akamgeukia dereva wa teksi.”Lets Go!(Twende zetu!)”
Nilibaki nikiwa nimesimama pale nje ya ile kasino nikiishuhudia ile teksi ikiondoka eneo lile nikiwa sina la kufanya.
The Bastard ni jina la mtu!
Muda wote nimekuwa nikiamini kuwa Mr. Q aliposema yale maneno yaliyomaanisha nimtafute “The Bastard” alikuwa akimaanisha kuwa nimtafute yule mwanaharamu Wagga Maingo na wenzake ili niwafikishe mbele ya sheria.
Kumbe alikuwa anamaanisha mtu maalum! Mtu ambaye ndiye alikuwa akiendesha ile biashara ya ufuska na uhuni ndani ya ile Kasino iliyoitwa The Rickshaw.
Nimekuwa nikitafuta majibu ya tukio lile la kule msituni kwa muda mrefu. Na tangu mwanzo wa kizaazaa hiki niliambiwa na Mr. Q kuwa majibu nitayapata The Rickshaw, na leo ndio nimeambiwa kuwa The Bastard, ambaye ndiye alikuwa na majibu ya maswali yangu yuko ndani ya hii kasino The Rickshaw.
Lazima leo nipate majibu. Lakini nilijua kuwa huenda huu ukawa ndio mwisho wa safari yangu ya kutafuta ukweli juu ya mambo haya yaliyonikuta. Aidha niwafichue madhalimu waliofanya mauaji kule msituni, au wao waniangamize. Woga mkubwa ulinikumba na nikaanza kulitazama lile jengo lililokuwa na ile kasino The Rickshaw kwa mtazamo mpya.
I wish John Vata was here (Natamani John Vata angekuwepo).
Kwa vyovyote lazima nirudi tena mle ndani, hata kama ndio litakuwa jambo la mwisho kulifanya hapa duniani. Nilimfikiria dada yangu Koku na mama yangu.
Eh, Mungu wangu, huenda nisiwaone tena baada ya kuingia tena ndani ya hii kasino.
Na hata sijapata nafasi ya kwenda angalau kumwombea dua Kelvin kaburini kwake...
Nilivuka barabara na kukiendea kibanda cha simu kilichokuwa hatua chache upande wa pili wa ile kasino na kumpigia tena simu dada yangu. Alipopokea ile simu na kunitambua alianza kunifokea na kunilaumu kwa kumkatia simu wakati tulikuwa tukiongea mambo mazito namna ile. Nilimtaka radhi kuwa sikuweza kabisa kuendelea kuongelea mambo yale ya kuhuzunisha.
“Nilienda kumuulizia John Vata makao makuu ya polisi, lakini hakuna nililoelezwa, na nikashindwa kuwauliza iwapo ni kweli amefariki kwani ningejitia kwenye matatizo...” Koku alinieleza.
“John Vata amekufa Koku, mimi nilikuwepo wakati tukio lililopelekea kifo chake lilipotokea! Lakini hilo silo nililokupigia Koku...” Nilimjibu kisha nikamwomba anielekeze sehemu ambapo Kelvin alizikwa pale kwenye makaburi ya Kinondoni. Koku alinielekeza kisha akaniuliza nilikuwa nataka kufanya nini.
“Koku, naomba ujue kuwa mimi nakupenda sana dada yangu, na mama pia. Nimegundua sehemu ambayo nadhani ndio chimbuko la mkasa wote huu ulionikuta na sasa nataka kwenda. Huenda nisitoke salama huko niendako Koku...”
“Usiende Tigga! Achana na mambo hayo.Bora ujisalimishe polisi...” Koku alidakia kwa wasiwasi.
“Hapana Koku, wewe huelewi.Hili jambo ni zito na linawahusu wengi na siwezi kwenda kichwa kichwa kwa kila askari na kumueleza. Kama nitatoka salama huko niendako, nina nia ya kwenda kumwombea dua Kelvin, lakini kama nitatokewa na jambo lolote Koku, naomba ukaniombee kwa Kelvin kwa niaba yangu na ujue kuwa ninawapenda sana...wewe na mama...”
Koku alianza kulia.
“Kwa nini unaniambia mambo hayo mdogo wangu...?”
“Na kama nitatokewa na jambo lolote, nakuomba sana uchukue ile Televisheni yangu kule nyumbani kwangu. Nataka iwe yako Koku. Ina matatizo kidogo, lakini ukifungua kule nyuma, kuna kiji-waya kidogo huwa kinalegea. Ukikikaza itafanya kazi kama kawaida. Nakuomba sana Koku!” Nilimwambia bila ya kujali maneno yake. Koku alishindwa kunielewa na alizidi kulia kwa sauti.
“Kwa nini unanifanyia hivi mdogo wangu lakini...?” Alilalama.
“Zingatia maelezo yangu Koku! Televisheni iwe yako! Mimi yanipasa niende sasa. Kama nitatoka salama, ujue nitakuwa nimejikomboa kutoka kwenye mkasa huu, na nitakupigia simu kukufahamisha. Ila siku ya leo ikipita, na kesho ikapita bila kupata simu kutoka kwangu, basi ujue ndio...ndio...ukumbuke kuwa nawapenda sana...na uzingatie maelekezo yangu!” Nilimwabia nami nikihisi donge kubwa likinikaba kooni. Sasa Koku alikuwa akilia kwa kwikwi.
“Tigga...Tigga...”
“Koku, Kwa heri. Niombee kwa Mungu, na zingatia maelekezo yangu!”
Nilikata simu. Nilishusha pumzi ndefu, kisha nilijipa moyo na kuvuka tena barabara na kuelekea kule ilipokuwa ile kasino La Dreamer. Ndani yake kukiwa na ile kasino The Rickshaw.
Na mtu aitwaye The Bastard.
Niliingia ndani ya ile kasino na kuchukua chenji yangu kutoka kwa yule mhudumu wa La Dreamer. Kisha nilipanda tena ile lifti na kurudi ndani ya The Rickshaw.
Come what may.
Liwalo na liwe.

--

Nilipotokea tu kwenye ile korido ya vioo niliona wale mabaunsa wakitazamana na kujizatiti vizuri zaidi pale mlangoni. Mara moja nilijua kuwa sikuwa nikihitajika tena mle ndani, nilishajionesha kuwa si miongoni mwao. Nilisita kidogo pale kwenye korido nisijue nichukue uamuzi gani, lakini muda huo nikamuona binti moja akitokea mwisho kabisa wa ile korido, kushoto kwangu ambapo siku ile nilipokuja kwa mara ya mwanzo kabisa niliona kuwa kulikuwa kuna ngazi zilizokuwa zikielekea juu zaidi ya lile jengo. Bila kufikiri zaidi nilikunja na kuelekea kule alipokuwa akitokea yule binti ambaye alikuwa akihesabu pesa huku akitembea kwa mikogo. Nilimtazama kwa makini huku nikienda kule alipokuwa akitokea na nikamkumbuka kuwa ni yule binti wa kiswahili niliyemuona akiingia kwenye vile vyumba nilivyohisi kuwa ni vya kufanyia ngono mle The Rickshaw akiwa na mwanamume wa kiswahili.
Nilipomfikia karibu niliona yule binti akinitazama kutoka chini mpaka utosini na kunishusha, kisha akabetua midomo yake kwa dharau. Nilimtazama kwa mshangao.
Inahusu nini tena? Kwa nini ananitazama namna hii? Sikuelewa, na sikujali. Mwisho wa ile korido nilikunja kulia na kuzifikia zile ngazi. Nilizipanda taratibu huku nikijitahidi nisigeuke nyuma kutazama iwapo wale mabaunsa walikuwa wakinifuata. Mwisho wa zile ngazi nilikuta mlango mzito wa mninga ambao ulikuwa umezatitiwa na geti la chuma mbele yake. Ule mlango ulikuwa ukiingia kwenye nyumba ndogo iliyokuwa juu ya ile kasino ya The Rickshaw, yaani Penthouse. Kwa uelewa wangu mara nyingi nyumba za aina hii huwa hazina vyumba vingi. Nilisimama nje ya ule mlango nikijishauri nifanye nini huku nikigeuka nyuma kutazama iwapo wale mabaunsa walikuwa wameamua kunifuata, na nikaona nilikuwa peke yangu. Lile geti la chuma lilikuwa wazi. Niliujaribu ule mlango nao ulifunguka bila taabu. Sidhani kama nina haja ya kukuambia ni jinsi gani moyo wangu ulivyokuwa ukipiga kufikia hapa, lakini ndani kabisa ya moyo wangu kulikuwa kuna msukumo uliokuwa ukinizuia kabisa kurudi nyuma.
Hapa ndipo nilipoambiwa kuwa majibu yatapatikana, na sikuwa na namna nyingine ya kuyapata majibu hayo bila mimi mwenyewe kujitosa. Niliingia ndani.
Nilijikuta nikiwa ndani ya sebule moja nzuri sana, kuta zake zikiwa zimepambwa na mapicha ya akina dada wa kila kabila wakiwa utupu katika mitindo mbalimbali. Hewa ndani ya sebule ile ilikuwa ikipozwa kwa kiyoyozi mwanana. Zulia lililotandikwa sakafuni lilikuwa zuri na ghali sana.
Chumba chote kilikuwa kikinukia harufu ya manukato fulani ambayo sikuweza kuyajua mara moja, lakini ilikuwa ni harufu iliyoleta hisia fulani ya mapenzi. Yaani hata mimi niliyekuwa kwenye matatizo mazito kama haya niliyonayo nilipata hisia hiyo, sasa sijui kwa mtu anayekuja hapa kwa nia ya kutafuta burudisho la mapenzi. Muziki laini wenye mahadhi ya kiarabu ulikuwa ukisikika kutoka kwenye spika zilizokuwa zimening’inizwa kwenye kila kona ya chumba kile kwa juu. Kufikia hapa tayari nilikuwa nimeshapata hisia kuwa hapa ndipo haswa mahala nilipotakiwa kuja, kwani kulionekana wazi kuwa ndipo mipango yote ya ngono za kule ndani ya kasino ilipokuwa ikifanyikia. Kulikuwa kuna masofa mazuri sana pale sebuleni nami nilianza kutembea mle ndani kwa hatua zisizo na uhakika huku nikijikohoza ili kama kuna mtu anisikie na kuja kunisikiliza shida yangu.
Kulia kwangu kulikuwa kuna mlango mwingine ambao sikuwa na shaka kuwa ulikuwa ukiingia chumbani. Mlango ule ulikuwa wazi na pazia laini ilikuwa ikidhibiti macho ya mtu aliye sebuleni kuona kilichokuwa kikitendeka ndani.
“Karibu mrembo, karibu! Pita ndani!”
 
SEHEMU YA 41

. Kufikia hapa tayari nilikuwa nimeshapata hisia kuwa hapa ndipo haswa mahala nilipotakiwa kuja, kwani kulionekana wazi kuwa ndipo mipango yote ya ngono za kule ndani ya kasino ilipokuwa ikifanyikia. Kulikuwa kuna masofa mazuri sana pale sebuleni nami nilianza kutembea mle ndani kwa hatua zisizo na uhakika huku nikijikohoza ili kama kuna mtu anisikie na kuja kunisikiliza shida yangu.
Kulia kwangu kulikuwa kuna mlango mwingine ambao sikuwa na shaka kuwa ulikuwa ukiingia chumbani. Mlango ule ulikuwa wazi na pazia laini ilikuwa ikidhibiti macho ya mtu aliye sebuleni kuona kilichokuwa kikitendeka ndani.
“Karibu mrembo, karibu! Pita ndani!” Sauti ya kike ilinikaribisha kwa pozi za madaha ya hali ya juu na nikashituka kusikia ile sauti ikitokea kule chumbani. Niliangaza huku na huko mle ndani lakini nilikuwa peke yangu.
Sasa huyo mtu wa huko ndani amenionaje?
Sikuwa nimetegemea kukuta mwanamke humu ndani, lakini mara baada ya kuisikia ile sauti, nilijua kuwa kwa mazingira ya pale ni mwanamke pekee ndiye ambaye nilitakiwa nimtarajie humu ndani. Niliusogelea ule mlango wa kile chumba taratibu huku moyoni nikiwa nimejawa na woga juu ya nitakayokutana nayo humo ndani.
Je, huyu mwanamke atanitajia The Bastard ni nani?
Niliingia chumbani. Na nikabaki nikiwa nimepigwa na butwaa.
Kilikuwa ni chumba kipana sana, na katikati ya chumba kile kulikuwa kuna kitanda kikubwa kiasi cha kuwa zaidi ya futi sita kwa sita. Upande mmoja wa chumba kile pamoja na dari lake vilikuwa ni kioo kitupu, kiasi kwamba kama ukilala chali pale kitandani utakuwa ukijiona kutokea kwenye dari la chumba kile. Upande wa pili kulikuwa kuna mlango wa kioo kizito ambao sikuwa na shaka kuwa ulikuwa ukielekea chooni. Upande mwingine wa kile chumba, kulikuwa kuna kabati kubwa kabisa la nguo lililotambaa upana wote wa chumba kile, na kutoka chini hadi juu. Na kwa ule upande ambao mlango ulikuwako, kando ya ule mlango, kulikuwa kuna meza kubwa na safi ya kiofisi ambayo juu yake kulikuwa kuna viji-runinga vidogo vipatavyo vinne au vitano hivi, na kiti kizuri cha kiofisi kikiwa nyuma ya ile meza. Hapo nilielewa kuwa yule mwanamke aliweza kuona kila kilichokuwa kikitendeka pale sebuleni kwake kupitia kwenye moja ya zile runinga, na ndio maana aliweza kuniona nikiwa pale sebuleni kabla mimi sijamuona.
Nilizungusha macho yangu mle ndani. Zaidi ya kuonesha matukio ya pale sebuleni, pia zile runinga zilikuwa nikionesha matukio mbali mbali yaliyokuwa yakitokea kule ndani ya ile kasino The Rickshaw, kwani niliweza kuiona ile steji waliyokuwa wakichezea michezo ya ajabu wale wanawake wawili muda mfupi uliopita, sasa hivi kukiwa kuna binti mmoja akitumbuiza kwa kuimba wimbo ambao sikuuelewa. Zile runinga nyingine zilikuwa zikionesha matukio ya aibu kabisa ya watu wakifanya ngono bila shaka ndani ya vile vyumba nilivyoviona kule ndani ya ile kasino. Yote haya niliyaona ndani ya mkupuo mmoja tu wa kuzungusha macho yangu mle ndani.
Lakini yote haya hayakunifanya nipigwe na butwaa kama jinsi nilivyopigwa na butwaa na kile nilichokiona pale juu ya kitanda.
Mimi ni mwanamke na ninajiamini sana kwa jinsi nilivyoumbika. Ninaamini kuwa Mwenyezi Mungu ameniumba mrembo wa kuvutia, nina shepu nzuri tu na ninajua kuwa huwa inawapagawisha wanaume ipasavyo.
Lakini huyu kiumbe aliyelala pale kitandani akinitazama huku akiwa ameshikilia sigara kwa pozi za hali ya juu kwa mkono wake mmoja alikuwa ni zaidi ya mrembo. Alikuwa amejilaza kitandani ilhali akiwa ameegemeza uzito wa mwili wake kwenye kiwiko cha mkono wake mmoja wakati ule mwingine ukiwa umeshikilia sigara, na alikuwa akinitazama huku mdomo wake ukiwa umefanya tabasamu dogo na akinitazama kwa macho ya kutegea, kama kwamba alijua fika kuwa nitababaishwa sana na urembo wake, naye alikuwa anataka kuona ni kwa kiasi gani nitakuwa nimebabaishwa.
Na sio siri, nilibabaishwa vilivyo. Na mimi ni mwanamke mwenzake...
Miguu yake mirefu ilikuwa imejazia kwa namna ambayo ningeweza kuamni kuwa labda huyu alipewa nafasi ya kujichagulia mwenyewe miguu yake iwe namna gani na Muumba, halafu naye hakufanya makosa katika hilo. Ngozi yake nyororo ilikuwa na rangi ya weusi ulioelekea kwenye kahawia na nywele zake ndefu zilikuwa nyeusi na za kuvutia. Macho yake sasa! Ama kwa hakika huyu mwanamke ameumbika na nilibaki nikimkodolea nisijue la kusema, huku akilini mwangu nikimkumbuka yule mwanamke niliyewahi kusikia tu simulizi za urembo wake hapo zamani, Cleopatra.
Mungu wangu! Huyu ni mtu au jini....?
“Nimeumbika eenh?” Yule mwanamke aliniuliza kwa maskhara huku akiinuka kutoka kitandani na kusimama mbele yangu na akinitazama kwa makini, mdomo wake ukifanya tabasamu dogo la kupendeza. Alikuwa amevaa nguo ndefu iliyotoka shingoni hadi chini kabisa miguuni mwake, na hapo niliona kuwa alikuwa amejaaliwa shepu ya ajabu. Makalio yake makubwa yalikuwa yamejikamata vizuri sana mwilini kwake na hips zake zilikuwa zimejizungusha kwa namna ya kuvutia haswa. Ile nguo aliyovaa ilikuwa imetengenezwa kwa kitambaa cha mfano wa chandarua, na chini ya nguo ile hakuwa amevaa kitu chochote! Hata pale nilipokuwa nimesimama, niliziona chuchu za matiti yake ya wastani ambayo nilijua wasichana wengi walikuwa wakitamani kuwa nayo.
“Sa...sam...mahani Anti, Shika...moo!” Nilijitahidi kusema kitu na kuishia kumpa shikamoo, kwani pamoja na urembo wake ule uliotukuka, yule mwanamke alikuwa na umri mkubwa kuliko mimi, na nilimhisi kuwa kati ya miaka thelathini na saba au na nane, lakini bado hajafikia miaka Arobaini. Na bado alikuwa na mvuto wa hali ya juu!
Yule mwanamke alicheka sana na hapo hapo alinisogelea na kunitazama mwili mzima huku akinizunguka. Alinikamata makalio yangu na kuyatomasa-tomasa nami nilijisogeza mbali naye huku nikiingiwa na woga mkubwa. Lakini yule mwanamke alizidi kunichumguza kwa makini na kunikamata matiti yangu nami nikalazimika kurudi nyuma huku nikijiziba matiti yangu.
“Anti vipi...?”
Alinitazama na kuvuta sigara yake kwa utulivu, kisha akanipulizia moshi mwingi usoni kabla ya kunijibu.
“Vipi kivipi mrembo? Kwani si umekuja kutafuta kazi? Nitakwambia neno moja tu kuwa na wewe si mbaya hata kidogo.Unafaa. Na hapa nikikutazama tu tayari nimeshaona wateja kama saba hivi ambao nikikupeleka kwao tutafanya biashara nzuri sana na wewe utanufaika...what’s your name (Jina lako nani?)” Yule mwanamke aliongea taratibu nami nikashikwa na kihoro.
“Kazi...?” Nilimuuliza, halafu hapo hapo nilielewa. Yule mwanamke alikuwa akidhani kuwa nimeenda pale kuomba kazi ya ukahaba. Je, yeye ndiye mtendaji wa TheBastard? Haraka sana nilidakia.”Oh,kazi...ndiyo lakini....” Mungu wangu nifanye kazi ya ukahaba mimi?
“Lakini nini? Hujiamini...? Usiwe na wasiwasi, hapa utatulia tu. Jina lako nani?”
“Ti...Nuru. Naitwa Nuru...lakini wewe ni nani? Nataka kuongea na muhusika mkuu. Mwenyewe hasa....” Nilimjibu huku nikiwa sina hakika iwapo huu mwelekeo niliochukua ulikuwa sahihi. Yule mwanamke aliangua kicheko kikubwa na kujibwaga kitandani. Alikuwa ana kicheko kizuri.
“Mnnh! Kwanza hilo jina si la kweli. Kwani kama lingekuwa la kweli usingesita. Labda jina lako ni Tina au Tindikali au kitu chochote kinachoanzia na Ti, lakini sio Nuru. Lakini hilo si tatizo, kwa sasa nitaenda na jina hilo hilo.” Aliniambia huku akitabasamu. Nilijiona mjinga sana, lakini sikuwa na ujanja.
“Sawa...lakini nataka kuonana na mwenyewe...yaani muhusika mkuu...”
“Mimi ndio mwenyewe. Mimi ndiyo muhusika mkuu na wala usiwe na wasi wasi wowote. Mimi ndiyo Kemirembe Wairema!” Alinijibu kwa utaratibu lakini kwa msisitizo, nami nikabaki nikimtazama nisijue niseme nini. Alinitazama kwa macho ya kuuliza.
“Hujawahi kunisikia?” Aliniuliza nami nikamjibu kwa kichwa kuwa sijawahi kumsikia.
“Basi mimi ndio Kemirembe Wairema a.k.a PCD...Principal ChanguDoa, Mkuu wa Machangu Doa jijini, a.k.a The Bastard...”
Nilihisi chumba kikididimia nami nikididimia pamoja nacho. Moyo ulinilipuka na akili ilinifa ganzi, nikahisi kama niko ndotoni. Yule mwanamke alikuwa akiendelea kuongea maneno mengine lakini inaelekea usikivu wangu ulikomea pale pale kwenye lile neno “The Bastard” alilolitamka na sikusikia chochote alikichosema baada ya neno lile.
“YOU ARE THE BASTARD....??” Nilibwata kumuuliza huku nikiwa nimemkodolea macho na nikimnyooshea kidole. Mambo yakiwa hayapangiki kabisa akilini mwangu. Sasa huyu mwanamke muongoza danguro ndani ya kasino hapa mjini atahusika vipi na mauaji ya kule msituni hata yule mtu aliyeuawa anisisitizie nimtafute kiasi kile?
This is too much!(Hii sasa imezidi!).
Yule mwanamke aliuona mshituko wangu juu ya lile neno ambalo yeye alijitambulisha kuwa ni jina lake na hapo akawa makini kuliko kawaida.
“The one and only pretty one(Ni mimi pekee mrembo). Ni nini hasa kilichokuleta hapa we’ binti, kwani naanza kuhisi kuwa ujio wako ni zaidi ya jinsi nilivyodhani mimi hapo mwanzo.” Alijibu kwa ukali na kuachana kabisa na maskhara. Na hata alipokunja sura kwa hasira yule mwanamke alizidi kuonekna mrembo.
“We..wewe...ndiye The Bastard...? Jina lako...unaitwa The Bastard...?” Nilimuuliza taratibu huku nikimkodolea macho. Akilini mwangu ilinijia ile taswira ya yule mtu aliyeuawa kule msituni niliyempachika jina la Mr.Q akinisisitizia kwa taabu kuwa nimtafute mtu aitwaye The Bastard...

“Watakuua...wacha nijaribu kukusaidia”
“I don’t care...you go find the bastard!”

Na hata sikumuelewa. Kwa wakati ule nilielewa alikuwa akimaanisha kitu tofauti kabisa. Mungu wangu...
Yule mwanamke alinitazama kwa muda mrefu, kisha alinijibu taratibu.
“Ndiyo. Mimi ndiye The Bastard... and what exactly brought you here?(...na ni nini hasa kilichokuleta hapa?)”
Oh, My God...! Oh, My God...

“MR. Q”

x.

S
ekunde kadhaa zilipita bila ya mimi kujua nifanye nini. Bila shaka miguu iliniishia nguvu, kwani nilipokuja kupata akili ya kuamua nifanye nini, nilikuwa nimeketi kwenye kile kitanda kikubwa nikimtazama yule mwanamke mzuri aliyejinadi kuwa yeye ni The Bastard. Na katika sekunde zile nilizokuwa kama nimepigwa bumbuwazi, yule mwanamke alikuwa amewahi kufunga mlango wa kile chumba naye akawa amenishikia bastola huku akiwa ameketi kwenye kile kiti chake kilichokuwa mbele ya ile meza iliyokuwa na runinga kadhaa huku akiwa amekunja nne.
“Wewe ni nani na unataka nini hapa?” Yule mwanamke aliniuliza tena alipoona kuwa nilikuwa nikimkodolea macho bila ya kusema neno. Nilimtazama na akilini yakanijia yale matukio ya kutisha ya kule msituni.Nilikumbuka matukio ya ndani ya ofisi ya mkuu wa wilaya kule Manyoni na hapo woga wangu ukawekwa pembeni na badala yake hasira kubwa ilinitawala.
“Nataka majibu...na nimekuwa nikikusaka kwa muda mrefu ili unipe majibu na maelezo...Bastard!” Nilimjibu kwa hasira huku nikilitilia mkazo lile neno “Bastard”. Yule mwanamke alinitazama kwa mshangao.
“Majibu? Majibu ya nini? Maelezo juu ya nini? We’ mtoto mwehu? Yaani we’ umekuja kwenye anga zangu halafu unajitia jeuri? Kwa jinsi hali ilivyo ni kwamba wewe ndiye unayetakiwa kutoa maelezo na si mie!” Alinikemea kwa hasira, lakini bado sura yake haikupoteza ule urembo wake.
“Come on The Bastard, unajua ni nini ninachozungumzia. Nataka kujua ni nini kilichotokea kule msituni...” Nilimkemea huku nikionesha kukerwa kwa hali ya juu na majibu yake, lakini yule mwanamke alizidi kunishangaa.
“Mbona sikuelewi wewe mtoto? Kama una wazimu...na huelekei kuwa una wazimu... nitakuitia mabaunsa sasa hivi waje wakutupe nje. Lakini kama una sababu za msingi za kunijia humu ndani na kuanza kunisemea mambo nisiyoyaelewa, basi nakuomba uziseme hizo sababu haraka sana kabla sijachukua uamuzi mwingine. Mimi nina kazi za kufanya hapa...” Aliniambia kwa ukali.
 
Barikiwa sana mkulu....Ila tunaomba episode ya 19
SEHEMU YA KUMI NA NANE.

Baada ya matukio ya kule kwa mkuu wa wilaya nilipokimbilia kutafuta msaada, na yale ya kule kwa Kelvin na nyumbani kwa mama yangu, nilikuwa nimejitosheleza fika akilini mwangu kuwa sehemu pekee yenye usalama kwangu ni pale nitakapokuwa peke yangu. Na kwamba kila nitakayemdhania kuwa huenda akawa na msaada kwangu, anaondokea kuwa upande wao.
Wao.
Wao ni akina nani?
Na yule afisa wa polisi naye...
Macho ya Nyoka alikuwa tayari kabisa kumuua yule askari...sasa amekufa yeye!
Kwa hakika nilijua kuwa kama sikuchukua uamuzi wa haraka na kumbamiza Macho ya Nyoka na ile ndoo, bila shaka ningeshuhudia yule askari akiuawa mbele ya macho yangu.
Kadiri nilivyolitafakari tukio lile, nilijishawishi kuwa kwa wakati ule, nilikuwa nimechukua uamuzi wa busara sana kukimbia kutoka eneo lile, kwani kwa mambo niliyoyashuhudia kutoka kwa akina Martin Lundi, isingekuwa ajabu kabisa kukuta kuwa yule askari na Macho ya Nyoka walikuwa kitu kimoja, na walikuwa wanajifanya kutupiana mateke mbele yangu ili nijenge imani kwa yule askari wapate kunichukua kirahisi.
Lakini sasa nilielewa vinginevyo.
Kwa hakika yule alikuwa ni askari wa kweli, lakini hata kama ningebaki pale ofisini kama alivyoamrisha, angenielewa na kunisaidia? Au ndio ingekuwa kama yale ya kule kwa Mkuu wa Wilaya?
Kadiri nilivyoitafakari ile hali huku nikiendelea kuzifumua zile rasta, ilinijia wazi kuwa ingawa kifo cha Macho ya Nyoka kilitakiwa kiwe faraja kwangu, bado hakikuleta unafuu wowote katika hali yangu, kwani bado nilikuwa natafutwa na Dokta Martin Lundi na wenzake waliobaki. Tena sasa baada ya kifo cha mwenzao na kuelezwa gazetini kwa mazingira yaliyopelekea kifo chake, nilikuwa na hakika kabisa kuwa watazidisha bidii za kunisaka kwani nilikuwa na hakika kabisa wao hawakutaka kabisa nitiwe mbaroni na polisi wasio upande wao ili waweze kupata na kupoteza ule ushahidi ambao ulikuwa na madhara makubwa sana kwao. Lakini kama hiyo haitoshi, na polisi nao kwa upande wao walikuwa wanaendelea kunisaka. Sasa sijui kwa nini gazeti liliandika kuwa Macho ya Nyoka alikuwa amekuja kunitorosha, wakati yule afisa aliona wazi kuwa yule muuaji hakuwa na nia ya kunitorosha kwa urafiki baina yetu bali kwa sababu nyingine tu. Vyovyote itakavyokuwa, mbele ya yule afisa wa polisi na jeshin lake, bado nilikuwa mkimbizi kutoka kwenye mikono ya sheria, tena niliyekaidi amri ya kutotoroka niliyopewa na yule afisa wakati akimfukuza yule muuaji.
Lakini yule afisa wa polisi akiendelea kuniwinda ajue kuwa anaweza kuendelea kuniwinda kwa sababu niliokoa maisha yake...
Kwa siku mbili mfululizo sikutoka nje ya chumba changu zaidi ya kwenda kula na kurudi tena chumbani. Uzuri wa mambo ni kuwa pale pale kwenye ile nyumba ya wageni kulikuwa kuna sehemu ya mgahawa, hivyo sikupata taabu ya kutembea umbali mrefu kutafuta chakula. Kwangu, hizo zilikuwa ni siku mbili za tathmini ya matukio yote yaliyonitokea na jinsi nitakavyokabiliana nayo.
Siku yangu ya kuondoka pale kwenye ile nyumba ya wageni, niliongeza siku nyingine tatu, nikidai kuwa nilikuwa bado nina kazi za kuandika. Wakati huu nilikuwa nimeshanunua madaftari na makaratasi pamoja na kalamu kadhaa ili kweli nionekane mwanafunzi niliye kwenye utafiti. Na ili nisijiletee mashaka, nilikuwa nikitoka nje na kwenda kuzubaa pwani iliyokuwa karibu na ile nyumba ya wageni, na mara nyingine nikitembea tu mle mjini. Na mara zote nilizotoka, nilihakikisha kuwa nilikuwa na madaftari yakionekana wazi kwenye mkoba wangu.
Katika kipindi hiki, nilitumia muda wangu mwingi kadiri nilivyoweza kuangalia televisheni iliyokuwamo mle chumbani, hasa taarifa za habari ili nijue iwapo kuna habari zaidi juu yangu katika vyombo vya habari na kama zipo, zimetolewa kwa mtazamo gani. Aidha nilikuwa nikinunua magazeti kila siku nilipotoka kwenda kupata kiamsha kinywa asubuhi na kuyasoma kwa makini kutafuta habari zozote zilizohusiana na matukio niliyokumbana nayo. Lakini katika siku zilizofuatia, habari zile zilionekana kufifia kabisa.
Kama mvua iliyonyesha ghafla wakati wa kiangazi, halafu ikapotea na kukiacha kiangazi kiendelee kutawala.

--

Ukimya uliotawala baada ya habari ya kuuawa kwa Macho ya Nyoka ulinitia wasiwasi sana. Haikuniingia akilini kabisa kuwa baada ya taarifa kama ile, na taarifa zangu zikiambatana na picha yangu kutolewa gazetini, mambo yawe kimya kiasi kile. Nami nilizidi kuchoka kukaa katika ile hali ya wasiwasi na kujificha nikipita nikijibandika majina yasiyo yangu kwa woga wa kukutwa na watu wa Dokta Lundi au wana usalama.
Na kadiri nilivyokuwa nikiendelea kujificha katika ile nyumba ya wageni, nilikuwa nazidiwa na hamu na duku duku la kutaka kujua hali ya mama yangu ikoje hasa baada ya kukutana na dokta Lundi siku ile nilipowatoroka pale nyumbani. Nilitamani pia kumpigia simu dada yangu labda angenipa habari zozote lakini nilishindwa kutokana na woga kuwa huenda namba ya simu nitakayotumia ikafuatiliwa na kugundulika kuwa nimepiga kutokea Kigamboni halafu wakaniibukia kule kule Kigamboni. Nilishindwa pia kutafuta habari za Kelvin kwa sababu hiyo hiyo, ingawa naye nilikuwa na shauku kubwa ya kujua ni nini ilikuwa hatima yake.
“Lakini kwa nini niendelee kuishi maisha haya ya kikimbizi namna hii?” Nilijisemea peke yangu nikiwa chumbani mwangu pale kwenye ile nyumba ya wageni na kusonya kwa hasira na kuchanganyikiwa. Niliinuka kutoka kitandani nilipokuwa nimejilaza na kwenda kusimama nikiegemea ukuta huku nikiwa nimetumbukiza mikono yangu kwenye mifuko ya suruali ya michezo niliyokuwa nimeivaa.
“Na nitaendelea kuwindwa namna hii mpaka lini?” Nilijisemea tena kwa hasira na kutoa msonyo mkali. Nilitembea mle ndani huku nikiwa nimezamisha mikono yangu mifukoni nikitafakari ile hali niliyokuwa nayo.
“Halafu kibaya ni kwamba hao wanaoniwinda wananijua fika, lakini mimi siwajui…naona watu wananikimbiza, wanaua watu, wanawarubuni ndugu na jamaa zangu nao wanigeuke…lakini wao ni akina nani hasa sijui!” Niliguna na kujibwaga tena kitandani kwa kukata tamaa.
Muda ulikuwa ni kama saa kumi na mbili za jioni na kwa mbali nilisikia sauti ya adhana ikiwakumbusha waislamu kwenda msikitini kwa swala ya jioni.
“Lakini tatizo hasa ni nini…? Kwa nini yale mauaji yalitokea kule msituni? Kwa nini ilikuwa muhimu kwa Dokta Lundi kunipakazia mambo ya uongo namna ile…?”
Niliinuka na kuliendea begi langu na kuitoa ile kamera ya Gil, na kwa mara ya kwanza tangu nitoke kule Manyoni nilikaa chini na kuutazama upya ule mkanda tangu mwanzo hadi mwisho. Nikilirudia upya lile tukio la kule msituni. Nilipomaliza kutazama yale mambo ya ajabu niliyoyarekodi kule msituni nilijikuta nikibubujikwa na machozi bila kupenda. Lakini pia kulitazama tena lile tukio kuliniletea mwanga mpya katika uelewa wangu wa tukio lile na nikajikuta nikiurudisha tena nyuma ule mkanda na kuuangalia upya kutokea mwanzo hadi mwisho huku nikitafakari matukio mengine yaliyonitokea ambayo hayakuwamo mle kwenye ule mkanda.
Niligundua kuwa kumbe wale wauaji, akina Martin Lundi, wote walikuwa wamevaa glovu mikononi mwao, kitu ambacho sikuwa nimekiona hapo mwanzo.
Ina maana walikuwa wamedhamiria kuwa wasiache ushahidi wowote wa kuhusika kwao aidha na kifo cha yule mtu, au tukio zima la pale msituni.
Nilirudia ile sehemu nilipokuwa naongea na yule mtu asiye na jina kule msituni, ambapo hapa nadhani nilirekodi bila ya kujijua, kwani ile kamera ilikuwa imeelekea ardhini kwenye mchanga, na ilichorekodi kilikuwa ni yale mazungumzo yaliyotokea baina yetu pale mchangani. Na nilipokuwa nikitazama ule mkanda ukionesha michanga tu ya pale alipokuwa amelala yule mtu na sehemu kidogo ya bega na mkono wake, nilikuwa nayasikia upya yale maongezi kutoka kwenye ile kamera.
“Usiongee! Tulia, nitakusaidia”
Halafu nilisikia miguno ya yule mtu kisha nikaona zile namba ambazo yule mtu aliziandika mchangani na kunisistizia nizitazame.
Niliusimamisha ule mkanda na kukimbilia kalamu na kijitabu kidogo kilichokuwa mezani, nikarudi pale nilipoiacha ile kamera na kuinakili ile namba huku moyo ukinienda mbio.
Nikaendelea kuangalia ule mkanda.
“Sawa...nimeshaona! Hizi namba ni za nini? Na wewe ni nani...kwa nini wale watu wamekufanya hivi? Umewafanya nini? Ni nani wale?”Ilifuatia sauti ya yule mtu akikohoa kwa taabu, ikifuatiwa na pumzi zake akitweta kama mtu aliyemaliza mbio ndefu.
“Find the Bastard!”
“Yes! Usiwe na wasiwasi nitahakikisha wanafikishwa mbele ya sheri...’
“...at the Rickshaw...!”.
“Rickshaw? Rickshaw iko wapi ?”
Niliisimamisha tena ile kaseti na kuandika tena kwenye kijitabu changu:
Bastard.
Rickshaw.
Nikaendelea kuutazama tena ule mkanda.
Zilifuatia sauti za yule mtu akigumia kwa taabu, nami kumbukumbu zangu zikanionesha picha ya yule mtu alipokuwa akitapatapa huku akitupa kichwa chake huku na huko na nikakumbuka jinsi nilivyopandwa na woga nilipodhani kuwa yule mtu ndio alikuwa anakata roho.
“Wewe ni nani...ndugu zako ni nani?”
Niliusimamisha ule mkanda na kuandika kwenye kijitabu changu:
Wewe ni nani? – No answer. Mr. Who?Mr. Nani? Question Mark! =Mr. Q?
Nikabonyeza sehemu inayotakiwa na ule mkanda ukaendelea.
“Get the key....the bastard!”
“Key…? What key…?”
Niliisimamisha ile kaseti na kuandika tena kwenye kijitabu changu:
Key – Ufunguo. ???
Nikaendelea kuutazama ule mkanda.
“At the Rickshaw…!”
“I don’t understand!”
“Please…Go now!”
“Lakini bado sijaelewa…nataka kukusaidia! Au hujui Kiswahili…? Can’t you speak Swahili?”
“Find the bastard!”
Niliisimamisha tena na kuandika kwenye kijitabu changu:
Find the Bastard! – Mtafute Mwanaharamu? (M. Lundi&wenzake???)
Nilibaki kimya kwa muda mrefu huku nikitafakari wakati picha ya siku ile msituni ikinijia akilini na nikakumbuka jinsi yule mtu alivyonitazama huku akitoa kitu kama tabasamu dogo sana baada ya kuniambia yale maneno.
“Now why did you smile like that Mr. Q, eenh?” Nilijisemea mwenyewe kwa sauti ya chini, nikimuuliza yule marehemu huko aliko kwa nini alitabasamu namna ile baada ya kunieleza maneno yale. Nilikaa nikitafakari kwa muda mrefu sana, huku nikichorachora vitu visivyoeleweka katika kile kijitabu changu. Kisha niliamua kuendelea kuuangalila ule mkanda.
“Okay...I can speak english....who are you? Who are those people…? Do you have any relatives….? I can help you…I want to help you!”
“Please Go...watakukuta!”.
“Watakuua...wacha nijaribu kukusaidia”
“I don’t care...you go find the bastard!”
Hapa niliusimamisha tena ule mkanda na kuandika kwenye kijitabu changu:
Mr.Q hajali kama angeuawa?? Anachojali = Find the Bastard!!!!
Who is the Bastard? – M. Lundi, Kigulu,Macho ya Nyoka(Dead?) Au kuna kitu kingine?
Hapa nilitafakari tena kwa muda mrefu, na ingawa sehemu hii yote ya mkanda nilikuwa nimerekodi sauti tu, wakati picha ikionesha michanga tu ya pale mchangani alipokuwa amelala yule mtu asiye na jina(nilishampachika jina la Mr.Q), bado niliikumbuka vizuri sana sura yake ilivyokuwa pale alipomaliza kusema yale maneno na jinsi alivyojitahidi kutabasamu tena halafu akazidiwa na kikohozi kikali na damu ikaanza kumtoka mdomoni. Hapa mkanda ulisimama kabisa kurekodi na hakukuwa na picha wala sauti yoyote, nami nikakumbuka kuwa ni wakati huu ndipo nilipomwinua kichwa chake ili damu isimpalie na kuanza kumfuta ile damu kwa mkono wa shati langu. Nilikumbuka waziwazi kuwa nilipofanya hivi, yule mtu alinishika mkono kwa nguvu na kunitolea macho huku akinisisitizia kuwa niondoke eneo lile haraka kabla wale wauaji hawajanikuta na kuniua.
Na kweli masikini, nilipoondoka na kumwacha pale, wale wauaji walirudi na kumkuta akiwa anagaa gaa pale mchangani.
Nililia kwa uchungu baada ya kuona ni jinsi gani yule mtu alivyonisisitiza niokoe maisha yangu ingawa alijua kuwa yeye angekufa muda wowote.
“Lakini kwa nini uliniita? Hukutaka nikuokoe, bali ulitaka kunieleza kitu…?” Nilimuuliza yule marehemu huko aliko kwa fadhaa huku nikibubujikwa machozi na nikihisi donge kubwa likinikaba kooni.
“Sasa mbona hukunieleza kitu chochote cha maana, Mr. Q?” Nilimuuliza tena kwa uchungu huku nikibubujikwa na machozi. Nilitazama vitu nilivyoandika kwenye kile kijitabu changu. Hakukuwa na kitu chochote kilichokamilika ambacho kiliniwezesha kujua ni nini yule mtu alitaka kunieleza. Kwa muda mrefu nilibaki nikikodolea macho vitu nilivyoandika kwenye ule ukurasa wa kile kijitabu changu, na bado sikupata jibu la moja kwa moja.

456718
Bastard.
Rickshaw.
Wewe ni nani? – No answer. Mr. Who? Mr. Nani? Question Mark! = Mr. Q?
Key – Ufunguo.???
Find the Bastard! – Mtafute Mwanaharamu?(M. Lundi&wenzake???)
Mr. Q hajali kama angeuawa?? Anachojali = Find the Bastard!!!!
Who is the Bastard? – M. Lundi, Kigulu, Macho ya Nyoka (Dead?) Au kuna kitu kingine?

Nilidhani ningeweza kupata mwelekeo fulani kutoka kwenye ule mlolongo wa vitu nilivyoandika kutoka kwenye kauli za yule mtu aliyeuawa msituni. Nilihitaji kutafakari zaidi.
Hatimaye niliamua kuendelea kuutazama ule mkanda na nilipofikia katika sehemu ambapo yule mtu niliyembatiza jina la Mr. Q alimrukia Macho ya Nyoka na kuanza kupambana, niliusimamisha tena ule mkanda na kubaki nikikodoa macho kwa mshangao mkubwa huku akili ikinizunguka. Kitu nilichokiona pale, ingawa nilishakiona kwa macho yangu kule msituni, na nikakiona tena kwenye ule mkanda mara ya kwanza, kilinishitua na kuniletea mtazamo mpya kabisa katika swala zima la mkasa huu ulioniangukia.
Ilikuwa ni vigumu kuamini, lakini ndivyo ilivyoelekea.
Niliirudisha tena ile sehemu na kuiangalia upya.
Ni kweli kabisa nilichogundua, na hata pale ugunduzi ule uliponiangukia, nilijikuta nikishikwa na butwaa nisijue la kusema.
Mr. Q alimrukia Macho ya Nyoka kusudi ili auawe!
Naam! Ndivyo haswa.
Nilihisi mwili ukinisisimka na hapo hapo vipele vya baridi vilinitoka mwilini.
Kwa nini Mr. Q aamue kufanya vile? Kwani bila shaka na yeye alijua kuwa katika wale watu watatu, Macho ya Nyoka ndiye aliyekuwa anaelekea kuua bila hata ya sababu, hivyo akaamua kumpa sababu ya kumuua na ndivyo ilivyotokea!
Nilifikiria maana ya kitendo hiki huku maswali yakinielemea.
Kwa nini aamue vile? Kwa nini aamue vile wakati ule, na si wakati wowote kabla ya hapo?
Kutokana na tukio lile kama jinsi nilivyojikumbusha kwa kuutazama tena ule mkanda, ni kwamba yule mtu aliteswa sana kabla ya kuletwa pale msituni, na kama aliteswa, lazima kuna sababu ya kuteswa huko.
Nilikumbuka kuwa kuna wakati kabla ya yule mtu kumrukia Macho ya Nyoka na hatimaye kuuawa, alimtemea mate Kigulu ambaye alikuwa akimuuliza kitu fulani, na kisha akamtupia mchanga usoni, na wakati kigulu anajipangusa mchanga, yeye alimrukia Macho ya Nyoka.
Ambaye wakati huo alikuwa pembeni kabisa tena na bastola yake alikuwa ameiweka mfukoni baada ya kukemewa na wenzake alipokuwa akimtishia Mr. Q kwa bastola ile.
Hii ilimaanisha kitu kimoja tu...
Yule mtu alikuwa anawachokoza kusudi ili wamuue!
ITAENDELEA .

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Back
Top Bottom