Riwaya ya Kijasusi Mabaduni wa serikali

Riwaya ya Kijasusi Mabaduni wa serikali

TAMATI....Ngoma ya watoto haikeshi 🙆‍♀️
Hizi ni dalili tosha kuwa tuwe makini kwa kila zuri tulipatalo, maana wakaanga sumu kama huyu Jackal wapo wakipinga kila jema.
Ila yote yawezekana kwa mwenye Imani.
 
Riwaya hii ni ya kubuni, hivyo mfanano wa matukio wa ndani ya Riwaya na maisha halisi unayoyaishi ni shabaha tu ya fikra za Mtunzi.
karibuni nyote kwa wingi




MABADUNI WA SERIKALI



Utangulizi

Kila serikali ya taifa lolote hapa ulimwenguni ni lazima iwe na kikosi cha watu maalumu kwa ajili ya kutekeleza majukumu Fulani Fulani ambayo huwa ni magumu na ya siri sana.

Mara nyingi serikali hizi zimejikuta katika migongano mikubwa sana na hivi vikosi ambavyo vimesheheni watu wenye uwezo na ustadi wa hali ya juu sana katika mikakati mbali mbali kama vile hujuma na mauaji .

Hii hupelekea vifo vyenye utata kwa baadhi ya watu wenye nyadhifa serikalini na kuacha sintofahamu kwa jamii za watu wa taifa husika.



Sehemu ya 1



Pilika za uchaguzi wa viongozi mbali mbali nchini Songomo zilikuwa zimepamba moto.



Wagombea mbali mbali walikuwa wakijinadi ipasavyo kwa wananchi ili wapewe ridhaa ya ama kuendelea na nyadifa zao au kuingia kwa mara ya kwanza katika jopo la watawala.

Wagombea Uraisi nao walikuwa na shughuli pevu ya kulishawishi baraza la Seneti ili yapatikane majina mawili ya watu watakaochuwana vikali kukiwania kiti hicho.



Raisi Mwibale Moha ambae alikuwa anahitimisha ngwe yake nae alikuwa mgombea,

Japo hali ilionesha kuwa baadhi ya wajumbe katika seneti walikuwa hawamuhitaji kuendelea kutawala taifa hili lenye ukwasi wa kutisha, na ilionekana wazi angeanguka katika kura za wajumbe.



Lakini yeye aliamini ana karata ya ushindi ambayo ingempitisha na kufanikiwa kuwa Raisi tena .

Mbinu hii hakuwashirikisha hata watu wake wa karibu, ila mara kadhaa alisikika akisema kuwa kama atapoteza katika kura basi labda ni kwa wananchi lakini sio kwenye seneti.



Aliamini kuwa sehemu ambayo hatakiwi kuanguka ni kwenye kura za seneti, maana za wananchi hazimsumbui kamwe,

Ana uwezo wa kubadili nyeusi kuwa nyeupe. Mh!! Ogopa sana.





Basi siku zilikatika na kusalia majuma mawili kabla ya kikao cha baraza la Seneti kuwapigia kura wagombea.



***** ******* ******



Katika jengo moja kubwa sana la SHATOTO COMPLEX, mali ya kampuni ya MUKUNI INVESTMENT, kulikuwa na kikao cha siri sana.

Maana hata wageni waalikwa hawakutambua dhumuni la kikao hiki licha ya kupokea mualiko wenye muhuri wa Ikulu.



Saa mbili kamili asubuhi watu walianza kuwasili maeneo ya jengo hili na kuingia moja kwa moja kwenye hoteli moja kali sana iliyomo ndani ya jengo hili,

Niwaelezee kwa ufupi tu kuhusu hili jengo la SHATOTO COMPLEX.

Limejengwa likiwa na upana wa kilomita tano kuelekea kusini na kilomita kumi Mashariki,

Likiwa limejengwa kwenye eneo lenye ukubwa wa Kilomita 50 za mraba.



Lina mabwawa makubwa yasiyopungua themanini ya kisasa ya kuogelea,



Uwanja wa ndege wa kisasa wenye uwezo wa kutua ndege kubwa zaidi ya ishirini kwa wakati mmoja.

Hoteli za kisasa tano zenye ghorofa arobaini na tano kila moja zikiwa zimejengwa kwa maumbo ya tofauti kila moja



Kuna mitaa ishirini yenye barabara za wastani za kisasa,zilizotenganisha viunga vya hili jengo.

Kuna kumbi nyingi sana za kisasa za mikutano mbali mbali na kuna chemba za siri sana kwa ajili ya vikao nyeti zenye usalama na ulinzi wa mitambo ya kutisha sana.

Hivyo siku hii kikao hiki kiliikuwa kimeazimiwa kufanyika katika chemba moja yenye jina Black chamber 17.



Ni chemba isiyoweza kulipuliwa hata kwa bomu la aina yoyote ile,

na kuikodi hii chemba iligharimu pesa nyingi sana sio chini ya Dola millioni kumi, hivyo basi ilihitaji uwe na ukwasi wa kutisha ili uweze kuingia katika chemba hii.

Vyumba vya kulala vyenyewe viligarimu Dola laki moja kwa usiku mmoja tu.



Bila kusahau kulikuwa na utitiri wa maduka makubwa sana maarufu kama super markets zisizo na idadi,

Mandhari ya jengo hili yaliwavutia matajiri wazawa na wa kigeni kuja kuwekeza katika viunga hivi, ikiwa ni pamoja na mayadi makubwa na maduka yaliyojaa hapo.



Ndilo jengo kubwa na lenye hadhi nchini Songomo lenye mzunguko wa kila aina ya watu kutoka mataifa mbali mbali duniani.



Inakadiriwa kuwa idadi ya watu wanaofika katika jengo hili kwa mahitaji mbali mbali kwa siku inafika watu laki saba, maana kuna viwanja vya michezo ya aina zote.



Hata mechi muhimu nchini Songomo na matamasha makubwa ya kimataifa hufanyikia hapo.



** ** ** ** ** **

Kufikia saa tatu na nusu tayari wageni wote waalikwa walishafika na kuketi katika nafasi zao, na iliwashangaza maana kila meza ilikuwa na jina kamili la mhusika.



Utofauti mdogo tu ndio uliokuwepo hapo, viti viwili bado vilikuwa wazi.



Nafasi hizi mbili wengi walijua kuwa waliobaki ni Raisi mwibale moha, na nafasi nyingine ya mmiliki wa makampuni ya GIMONCHY GROUP OF COMPANIES.

Ambayo ndio baba wa makampuni ya,

Mukuni Investment,

Morigha Techs & media,

Junior Intelligence & security Agencies,

Super water Fishing & Marines,

P&G mining Company na

ONE OIL Refinery company.




Ambae alijulikana kama mkwasi wa hali ya juu sana nchini Songomo Bw. Fanton Mahal.

Baada ya ukimya wa sekunde kadhaa,

mara aliingia Rais Mwibale Moha na kwenda moja kwa moja mpaka kwenye nafasi yake, baada ya salamu fupi ya kunyanyua mkono wa kulia kwa wageni wote waliofika hapo ndani.



Baada ya Raisi kuketi tu, ndipo mlango uliokuwa ardhini ulifunguka kuja juu, akaonekana mtu wa mwisho, Bw. Fanton Mahal.

Aliingia akiwa na tabasamu pana usoni mwake,



Pesa ilimkubali sana mtu huyu, yaani hata tabasamu lake, kuna muda lilijenga hisia kama vile linataka kudondosha pesa.

Baada ya salamu na minong’ono ya hapa na pale, ukimya ulitanda kwa muda ili kuruhusu kikao kuanza, huku kila mmoja akiwa na shauku ya kujua lengo ama dhumuni la kikao hiki kizito.



Raisi Mwibale Moha akiwa ndiye mwenyekiti wa kikao hiki, alianza kuunguruma kwenye kipaza sauti, akiwakaribisha wageni wote waalikwa na kuwashukuru pia kwa muitikio wao juu ya hili.

“ Ninayo furaha kubwa na shukrani za dhati kwa nyote, maana muitikio wenu juu ya mualiko huu si tu kwamba unaonyesha umakini wenu, bali unadumisha umoja wetu tukiwa kama watu wenye maono na ndoto kubwa za pamoja katika kuhakikisha kuwa tuliyoyaazimia siku za nyuma yanabaki kuwa kipaumbele cha kwanza na muhimu Zaidi katika kupiga hatua itakayofanikisha malengo yetu ya pamoja.”



Kisha akapiga funda mbili za kinywaji kilichokuwa kwenye glasi nakutulia huku akiwatazama wenzake, ni kama alikuwa anajaribu kuyasoma mawazo yao,

lakini wengi walionekana kutaman aendelee ili wajue lengo la kikao kile. Baada ya kuona utulivu wao akaendelea.



“Hakuna asiejua hatua tulizopiga na imetugharimu juhudi nyingi na muda kuwa katika nafasi tulizopo.

Tumewekeza muda na pesa nyingi sana kufika hapa na sidhani kama kun ahata mmoja wetu anaetamani juhudi hizi zote kubaki kuwa hewa.

Kila mmoja hapa ndani ana mafanikio makubwa ambayo yametoka na utekelezwaji wa mipango kwa pamoja nah ii imezekana kutokana na undugu wetu tulioujenga wa kusaidiana ili kuhakikisha hakuna anaebaki nyuma.

Kuna jambo liko mbele yetu na ili tuweze kufikia malengo yetu ni muhimu kila mmoja wetu ahakikishe kuwa nafasi tulizonazo zinaendelea kubaki kwetu, tofauti na hivyo maana yake ni kuwa tutapoteza.

Mmoja wetu akipoteza maana yake wote tutakuwa tumepoteza, na hapo ndipo kutaibuka usaliti na hisia za chuki miongoni mwetu.



Nimewaalika hapa ili kuwakumbusha juu ya umuhimu wenu katika ushindi wangu ili kukitetea kiti changu ambacho pia ni msingi wa viti vyenu maana ninyi ndio wajumbe wa seneti.

Lakini kwa wale ambao hawahitaji kuendelea na mipango yetu ya awali sio vibaya pia wakaweka wazi nia yao juu ya hilo maana utawala wangu ni wa haki na uhuru kwa kila mwananchi wa Songomo, na ndio lengo la kuitana hapa leo.”


Alimaliza na kupiga funda tatu za kinywaji huku akiwatizama mmoja baada ya mwnine.

Kwa ufupi ni kama aliwaita kuwaambia kuwa mipango yao baadhi alikuwa akiitambua hivyo anawaonya wasifanye yale wanayoyafikiria wao bila kujali na kuangalia ni wapi wametoka wakiwa kama kikundi cha wanandugu hivyo kuwatishia pia kuwa kiti chake ni muhimu sana na ni kama jiwe kuu katika msingi way ale wanayotegemea kuyafanikisha mbeleni.

Hakika lilikuwa ni tishio kubwa sana kwa wajumbe hawa maana wengi wao walikuwa wafanyabiashara wakubwa nchini Songomo viongozi wakubwa wakiwemo mawaziri mbali mbali wakuu wote idara za usalama na vyombo vyote vya Dola kuanzia majaji wanasheria mbali mbali waliokwisha kustaafu mabalozi wa nchi tofauti Viongozi wa juu kabisa wa taasisi za kidini walikuwepo.

“Hongera sana Bw. Mwibale Moha, kwa mafanikio na hatua uliyoifikia .

Sikuwahi kufikiri kwamba itauja siku ambayo utasimama na kututishia ili tubaki katika himaya yako,

Ni kweli mafanikio yetu yamejengwa juu ya umoja wetu, tukilindana na kusaidiana Kipesa pale inapohitajika. Lakini hii haimpi mtu yeyote yule kibali cha kuwa na mamlaka juu ya mwingine, ila tunategemeana.”


Kauli hii nzito na ya aina yake ilitoka kwenye kinywa cha Bw. Fanton Mahal.

Ni kauli iliyoleta mchafuko wa hali ya hewa ndani ya ukumbi ule.



Watu walionekana kuteta huku wakiwa kama wanaopingana maana misimamo ilianza kuonekana wazi wazi.

Raisi Mwibale Moha alionekana kuwa na nguvu na ushawishi mkubwa kwa wajumbe baadhi ambao walikuwa watiifu kwake.



Maana wengi ni wale ambao aliwapa madaraka kama zawadi ili kujiwekea kinga pindi kiti chake kinapokuwa hatarini

Lakini pia nguvu aliyokuwa nayo Bw Fanton Mahal haikuwa ya kawaida, maana wengi wa viongozi waliopo kwenye madaraka yeye pia alihusika kuwaweka kwenye nafasi zao kulingana na mafungamano yake na viongozi mbali mbali wa taifa waliokwisha kupita na baadhi waliokuwepo katika awamu ya Bw mwibale Moha.

Inasemekana hata Mwibale Moha mwenyewe kufikia kuwa Raisi ilitokana na sapoti ya Fanton Mahal.

Kwa ufupi kauli ya Bw Fanton Mahali iliibua wasi wasi mkubwa sana kwa watu wote waliokuwa mle ndani.

Hii ilileta picha kamili ya mpasuko ndani ya huu umoja,

Miongoni mwa watu ambao Raisi hakuwategemea kwenda kinyume ni Bw. Fanton Mahal,

Lakini baada ya kauli ile hata yeye kwa namna Fulani aliingiwa ganzi mwilini mwake, na aliona tishio la wazi juu ya nafasi yake.

Lakini hakutaka kuonesha hilo kwa watiifu wake, maana angewavunja moyo wa kuendelea kupambana na kwa wapinzani angewapa kete na asilimia za ushindi jambo ambalo hakuwa tayari kuliona likitokea, hivyo alitulia kimya akimtupia jicho la kiaina Bw. Fanton Mahal

Ni jicho lilobeba ujumbe ambao ungesomeka “ Hata wewe unanigeuka mtu muhimu kwangu leo unakuwa ngazi ya kunitelezesha kwenda chini?’”



Baada ya vurumai hii Raisi aliunguruma tena kwenye kipaza, awamu hakuwa na tabasamu wala kule kujiamini kama mwanzo, bali alikuwa na hasira iliyochanganyikana na hali ya maumivu ya kuhisi usaliti wa moja kwa moja.



Kuna muda inabidi wote tutambue kuwa, hakuna juhudi zinazopaswa kubezwa na hakuna haja ya kuwa na misuguano isiyojenga

Siku zote alieshiba hunyanyuka taratibu na kunawa kisha bila kuwabugudhi wengine wanaokula hutoka mahali pale”
Aliongea kwa mafumbo.



“Hatuwezi kuendelea kuumwagilizia maji mti wa kujinyongea na ingekuwa bora kama mti huo ungekauka tangu mwanzo kabla haujakomaa na kupeleka mizizi maana chaguo la mwisho ni kuung’oa ili usije ukachipua na kuacha mbegu za kumbu kumbu zitakazosumbua vizazi na vizazi” Ilimalizia sauti ya Fanton Mahali , kauli kinzani na ile ya Raisi mwibale Moha, awamu hii ikiwa imebeba taswira halisi juu ya maandalizi ya mapambano dhidi ya Raisi. Mmh!!! Ogopa sana.

Baada ya Fanton mahal kukaa kimya Raisi nae aliunguruma tena,

“Ndugu yangu Fanton Mahal, kumbuka nafasi uliyonayo kiuchumi imechangiwa na ulinzi kutoka kwangu. Maana mara kadhaa umehujumu Uchumi na kukwepa kodi bila Bughudha kutoka kwa vijana wangu na hata washirika wako wengi nimewalinda na unalitambua hili”

Alimalizia Rais awamu hii akimchimba Fanton juu ya utajiri wake kuwa na makando kando pia ikiwa ni kama onyo kuwa akivuka mipaka huenda akakutana na vikwazo vya kiuchumi na madhira ya aina nyingi pia.

Mwibale Moha Raisi mtukufu wa wanasongomo,

Unadhani unaimiliki serikali kwa asilimia ngapi? Aliuliza Bw. Fanton Mahal.

Asilimia themanini, alijibu Mwibale Moha kwa kujiamini ni kama vile alikuwa amefanya utafiti



Baada ya jibu lile la kujiamini aliambiwa na Fanton kauli ambayo ndiyo kwanza ilimzindua kutoka kwenye usingizi aliolala miaka mingi.



“Kwenye hizo asilimia zako toamo sitini na zile ishirini hata nikikuachia huwezi kushinda.

Sisi ndio msingi wa hili taifa tuondolee giza kwenye njia zetu, tulikubeba mgongoni haujui umbali wa safari tuliotoka hadi kufika hapa. Usituone tuko kwenye hivi viti ukadhani ilikuwa rahisi, hatukuamka usingizini na kujikuta hapa. Ni vyema ungekaa kimya na kuyaacha haya yapite, pengine huko mbeleni Mbingu zingekuwa upande wako, ungepata tena nafasi ya kuja kutawala.

Utailaani sana hii siku maishani mwako, lakini si ni mpaka tukupatie hiyo nafasi ya kuilaani?”




Alimalizia kwa swali Bwana Fanton Mahal, swali ambalo halikuhitaji kujibiwa.

Kisha akanyanyuka toka kwenye kiti chake na kuanza kupiga hatua kuondoka kwenye hii Black chamber 17 huku nyuma aliachia harufu ya mauti iliyozifikia pua za kila mmoja pale ndani kuonesha kuwa hakuwa mtu wa kawida kabisa,

Nyuma yake alifuatwa na wafuasi kama robo tatu ya wajumbe wote waliohudhuria kikao kile na kuyafanya maneno yake kuwa na maana aliposema Raisi aondoe asilimia sitini katika asilimia zake.



Raisi mwibale Moha aliangalia namna wajumbe wanavyoondoka kwa wingi wakimwacha akiwa amesimama huku mikono kaiweka mezani akiwa haamini, yaani ni kama alieandaa sherehe kisha watu wakaja wakala na kumwachia yeye aondoe vyonbo.

Alichukia sana, tena alichukia mchukio mpya.



Mara alipotupa macho yake katika skrini za mle ndani zilizokuwa zikionesha mazingira ya nje kwa chini kulizunguka lile jengo, aliona ghafla walinzi wake wanavyouawa kinyama na vikosi vya wauaji walioficha sura zao kwa vinyago .

Hapo ndipo alijua kuwa kumbe ni kweli ile miamba ilyoondoka ndio msingi wa hili taifa na hakuwa na cha kuwafanya,

Mwili wake uliishiwa nguvu na kujikuta akidondokea juu ya kiti chake mithili ya mtu ambae hakuwa tayari kuketi.

Akiwa amekata tamaa asijue nini cha kufanya maana hata akili yake haikuwa hapo ndani kwa wakati huo, mambo mengi yalikuwa yakipita kichwani mwake.



Kauli ya mwisho ya Fanton Mahal ilikuwa ikijirudia kichwani mwake, alichanganyikiwa na kufadhaika kwa wakati mmoja.

Ni kama mtu aliyezinduka kutoka usingizini,

Na hii ni baada ya kuhisi uwepo wa mtu mwingine pembeni yake maana anakumbuka alikuwa amebaki peke yake.

Baada ya kuinua sura yake ili amtazame ndipo alipopigwa na butwaa baada ya kumuona mtu aliekuwa amekaa pembeni yake bila wasi wasi wowote ule. Je ni nani huyo? Usikose sehemu inayofuata.

Sawa
 
Sehemu ya 4 ipo tayri Vipi mzigo ushuke jioni hii hii au tusubiri kwanza hadi ziishe zote mpaka sehemu ya 6??
Kura za watu 20 zinatosha.
 
Here We Go!!!!!

MABADUNI WA SERIKALI 4

N
je ya kasri kubwa la kifalme mjini Cadmon, kwenye bustani moja kubwa sana kulikuwa na meza kubwa ya duara ya kifahari nzuri sana. Yenye nakshi ya dhahabu, isiyohitaji kupambwa zaidi maana ilijitosheleza kimvuto.

Meza ilizungukwa na viti vitano tu. Na viti vitatu vilikuwa wazi. Kwa maaana kuwa kulikuwa na watu wawili tu hapo mezani na watu hawa ni mwanamke na mwanaume.

Walikuwa wamekaa kwa kutazamana yaani mkabala.

Na muda huu ndio Malone na Jiga Kinamba walifika eneo hili, Walimuona mwanamke vyema maana alikuwa amekaa kwa kutazama uelekeo wao. lakini mwanaume hakuonekana sura maana alikuwa kawapa mgongo na mavazi aliyovaa yalimfanya iwe ngumu kumtambua. Koti refu rangi ya kahawia na kofia pana nyeusi, maarufu kama pama mikononi alivalia glavu za kahawia pia.

Jiga Kinamba alishangaa baada ya kutambua kuwa mwanamke yule ni Mwana binti kutoka nyumba ile aliyopanga.

Anafanya nini hapa na yuko na nani yule,

Ni swali lililopita kichwani mwake bila majibu.

Kwa mbele zaidi waliona gari la mheshimiwa Raisi Mwibale Moha likifunguliwa na walinzi wa Raisi wakakaa imara, mara Raisi akashuka kutoka upande wa kushoto siti ya nyuma.

Haikuishia hapo upande huo huo siti ya mbele alishuka Team Leader wa PSU, mkononi akiwa na B&T APC9. Akiwa ameishika kwa mkono mmoja wa kushoto.

Hii ni bunduki moja ya kibabe sana, pia ni silaha nzito ya kivita.

Sio kawaida na ni nadra sana kumuona mtu huyu akiwa kashika silaha, ishara hii ilimaanisha kuna zaidi ya jambo lililowaleta hapa ikulu. Na haikueleweka muda huo walikokuwa wametoka maana ndio kwanza walikuwa wanawasili.

Upande wa kuume siti ya nyuma aliteremka mkwasi Fanton Mahal akiwa amevalia suti ya gharama ya kijivu iliyomkaa vyema mwilini.

Harufu yake ya marashi kutoka visiwa vya utuli vya mbali ilipenya vyema kwenye pua za watu wengi, na ilienda mbali zaidi kama mita arubaini kutoka alipo.

Nyuma ya gari hii kulisheheni gari nyingine tatu zenye wana usalama wa kutosha.

Raisi Mwibale Moha, Team Leader na Fanton Mahal walitembea uelekeo wa pale ilipo meza, lakini walipoifikia waliipita na kunyoosha moja kwa moja kuelekea kusini ambapo kulikuwa na jumba lingine kubwa. Na hapo ndipo lilionekana chopa moja la kisasa zuri aina ya MI-26, likiwa limepaki juu kabisa ya jengo lile lenye ghofa tatu.

Baada ya kuipita ile meza ndipo yule mtu aliyekaa na Mwana alisimama na kuunga tela kwa nyuma na kuufanya ule msafara kuwa wa watu wanne.

Walifika pale walipo Malone na Jiga Kinamba kisha Fanton Mahal alimpalaza Malone begani kwa kiganja cha kulia kisha Malone nae akaunga tela kwa nyuma lakini kuna kikaratasi kilipitishwa kwa ustadi sana kutoka kwa Fanton Mahal kwenda kwa Jiga Kinamba.

Ni wachache walilitambua jambo hili, yaani wale ambao waliona akiwemo Malone mwenyewe.

Jiga Kinamba yeye alibaki eneo lile akiwa anapiga hatua hafifu kuelekea mezani, ambapo alikuwa amebaki Mwana peke yake mithili ya kipepeo aliye bustanini.

Mara kwa nyuma gari waliyokuja nayo iliwapita ndani yake akiwemo Macka Shinea na jenerali wa majeshi ya Songomo akiwa bado hajitambui.

Macka alifuata msafara ule ulioishia chini ya lile jengo, kisha baada ya kuhakikisha idadi imetimia waliingia kwenye chemba ambayo iliwapaisha hadi floor ya juu ya hili jengo. General alikuwa akibebwa na watu wawili Malone na Macka Shinea.

Baada ya kufika juu waliingia kwenye chopa.

Chopa likatoweka mazingira haya ya Ikulu ya Cadmon.

Bustanini walibaki Jiga Kinamba na Mwana, wafanyakazi wengine wa ikulu walikuwa bize na majukumu yao kama ilivyo ada.

Jiga Kinamba baada ya kuketi, kwanza alikuwa na shauku ya kujua mambo mengi kumuhusu Mwana maana ni mara ya pili hii anamwona akiwa katika mazingira ambayo yanaashiria kuwa na uhusika wa juu kidogo katika mipango hii.

Baada ya kuketi Mwana alibabaika maana hakuwa akimfahamu mtu huyu,na hii ni kutokana na sura ya mtu huyu kuwa ngeni yeye aliizoea ile ya Seif na huyu wa sasa ni Jiga Kinamba, Yaani mwili mmoja sura nyingi.

Jiga Kinamba aliliona hilo kisha kwa upole sana alimuita Jina na kumsabahi Mwana

Kitendo kilichozidi kumchanganya Mwana baada ya hapo alimuambia Mimi ni Seif mpangaji mwenzako pale Gonza.

Mwana ndio kwanza akatumbua macho asielewe anayoambiwa na Jiga kinamba.

Mara akaja kijana mmoja akamkabidhi Jiga Kinamba Funguo za gari na kumuonesha gari lenyewe kwa ishara ya kidole, kisha akaondoka huyu ni mlinzi wa hapa Ikulu Cadmon.

Na muda huo huo baada ya kijana kuondoka simu ikaita, ni simu ya Jiga Kinamba. Akaiweka sikioni na kuanza kuzungumza kwa utulivu sana kisha akaikata simu hiyo na kumshika mkono mwana akimuashiria waondoke eneo hilo.

Mwana alitaka kugoma lakini nguvu iliyokuwa imemshikilia haikuashiria kupingwa.

Aliburutwa hivyo hivyo kibabe hadi lilipo gari kisha kwa kutumia skana ndogo mithili ya rimoti nyembamba gari ilikaguliwa na mtaalamu huyu wa kazi Jiga Kinamba. Ilikuwa salama kabisa.

Wakajitoma ndani, gari ikatekenywa ikatii amri ikaondoshwa eneo hilo kwa kasi ya kawaida tu na kuelekea kusikojulikana.

****** ****** *****



Makao makuu ya jeshi kwenye ofisi ya DCDF( Deputy Chief of Defence force)

Iliingia simu kutoka ofisi ya Wizara ya Ulinzi iliyokuwa na maelekezo ya kusitisha mipango yote ya awali na kutoendelea na mapambano.

Kwa maana nyingine ni kwamba amri zote walizokuwa wamepokea zilikuwa zinabatilishwa kuanzia muda huu.

Hivyo basi, vikosi vyote vilitakiwa kurudi katika maeneo yao ya kazi kulingana na kamandi zao.

***** ***** ******

Ndani ya Peak Ice Hotel kwenye Basements zilizo chini ya maji baharini kulikuwa na kikao nyeti cha watu wasiozidi hamsini.

Hawa ni wale watu wenye maamuzi ya mwisho juu ya mapendekezo ya nani anastahili kuliongoza taifa la Songomo. Waliitisha kikao hiki ikiwa ni dharula mara baada ya vurumai hii kuanza na taifa kuanza kuingia katika machafuko. Pia ilikuwa ni kwaajili ya kufahamu mwafaka wa nini kinatakiwa kabla baraza la seneti kukaa na kufanya utaratibu wao.

Hawa ndio DS wa taifa la Songomo yaani Deep State humu wamo watu wazito tu na wenye maamuzi ya mwisho hivyo ikiwa watu 26 wangependekeza Raisi Mwibale Moha kuendelea kutawala hakukuwa na namna zaidi ya kuwasikiliza na kama ingeenda tofauti pia ingebakia hivyo.

Mabaduni wa Serikali wote walikuwapo hapa isipokuwa kwa Jiga Kinamba tu. Pia kuna sababu ya kutokuwepo mahali hapa maana kwanza yeye huwa sio mpenzi sana wa mambo yanayohusu siasa.

Ukumbi ulikuwa umependeza na unavutia pia.

Heshima na adabu vilitawala, hakukuwa na ishara ya uvunjifu wa amani.

Ajabu ni kwamba hata team Leader naye alikuwa ni sehemu ya hili jopo tofauti na mafikirio ya Raisi na wengi kwamba pengine angekuwa nje akiratibu na kuangalia masuala yote ya ulinzi.

Lakini alikuwa kaketi kwenye siti inayotazamana na ile ya Raisi, mara chache alikuwa akiinua macho na kuwakagua baadhi ya watu kwa nukta kadhaa kisha angerudisha macho yake juu ya diary yake ambayo muda mwingi huwa anatembea nayo.

Muonekano wake ni kama mtu mwenye miaka 38 japo alishavuka umri huo zamani tu. Miwani yake na kipara kichwani vilimfanya aonekane mtu makini sana.

Ukumbi huu haukuwa na kamera wala vinasa sauti hii ni kutokana na unyeti wa vikao ambavyo hufanyika humu.

Baada ya salamu za heshima baina ya watu wote waliokutana humu ukumbini, kikao kilifunguliwa na Raisi mstaafu wa awamu ya kumi Mh. Wiza Marota, maana huyu wa sasa Mwibale Moha ni awamu ya kumi na mbili.

“Ahanteni na pongezi nyingi kwenu wote ambao mmeona mantiki kuu ya sisi kujumuika mahali hapa, Lengo la kikao hiki ni kupendekeza juu ya mtawala ajae ili taifa lizidi kusonga mbele.

Tunahitaji mtu ambae Imani ya wananchi itakuwa juu yake lakini zaidi ni yule atakaehakikisha kuwa anazilinda tunu za taifa letu kwa ajili ya Ustawi wa jamii yetu wote na mataifa jirani.”


Kama kuna kipindi ambacho viongozi huonesha kiwango cha juu cha unafiki ni kipindi kama hiki.

Hiki ndicho kipindi unaweza kushuhudia mtawala wa kada ya juu sana akipiga magoti kinafiki kwa wananchi ili kuwahadaa wakae upande wake, ilia pate kile anachohitaji lakini ni dhahiri kabisa akawa hawaoni wala kuwazingatia hao watu zaidi ya kuwatengenezea picha tu ambayo itaendana na fikra za walengwa.

Kwasababu, haya anayoyaongea Mh.Wiza ni tofauti na aliyoyafanya enzi za utawala wake.

Maana enzi yake ndio Mashirika mengi ya Umma yalibinafsishwa kwa wawekezaji wageni kutoka magharibi na mashariki.

Huduma za msingi kama usafirishaji na mawasiliano, ziliendeshwa na kutolewa na makampuni ya kigeni ambapo viongozi wachache walineemeka na gawio kidogo kutoka kwa makampuni hayo. Hii hali ya viongozi kujipatia vipato haramu vilivyotokana na mifumo ya kiunyonyaji na udhalimu kwa wananchi wa Songomo, ndio iliwafanya wawe na mioyo migumu mno na kutokuwa tayari kuona mtu kutoka nje ya mifumo hii akitawala taifa hili la Songomo.

Mifumo hii iliwapatia fedha nyingi sana, wakajisahau na kuanza kudhani kuwa wao ndio wenye haki ya kuendelea kukaa karibu na moto ilihali wengine wakifa kwa baridi kali.

Mfano ilipotokea mtu unataka kukiwania kiti cha Uraisi kwanza lilichunguzwa jina lako la mwisho, ili kuona kama una muunganiko na mfumo. Watu wachache tu ndio walikuwa na kibali cha kukikalia kiti cha uraisi.

Na zaidi ilionekana Jamii ya watu kutoka Songomo Mashariki walijipa zaidi haki juu ya nafasi nyeti, hivyo kupelekea watu kutoka pande zingine tatu kuona kama wanatengwa na kunyanyapaliwa na kikundi cha watu wachache.

Na mbaya zaidi ni pale watu kutoka katika familia ambazo zamani zilikuwa za kifalme walianza kuungana na kuaminishana kuwa wao walizaliwa wakiwa na kibali cha kuwatawala wengine, hivyo walikuwa wakienzi maisha ambayo familia zao zilizotangulia ziliyaishi. Yaani maisha ya Ufalme.

Na wengi ndio waliokuwa katika hii deep State, wakifanya yao ili kuyalinda maslahi yao.

Hivyo kwa mfano kama familia yenu ilitawa ufalme wa kusini, basi na wewe ulichukuliwa na kuingizwa kwenye mfumo.

lakini ni mfumo ambao ulikuwa na watu wengi kutoka familia za mashariki.

Na hata baadhi ya biashara nyingi za wazawa zilishikiliwa na watu kutoka mashariki. Na iwapo mtu kutoka nje ya ukanda huo angefungua biashara kiasi ikawa tishio kwa zile za wa mashariki basi vikwazo vilikuwa wazi ili tu njia za uchumaji wa pesa zibaki mikononi mwao.

Mfumo huu umekuwepo tangu enzi za utawala wa Awamu ya nane lakini ukashamiri zaidi na kuota mizizi kwenye utawala wa Mh. Wiza.

Na umeendelea na kuwa kama desturi mpaka sasa kwa Mwibale Moha.

Hali hii imepelekea wananchi wa Songomo kuuchukia utawala wa Raisi Mwibale Moha na kutamani hata radi impige mtu huyu, aliyejiziba masikio na kujifumbisha macho asione dhiki na tabu zinazotaabisha wananchi wake.

Pengo baina ya walionacho ambao wengi ni watawala na matajiri wachache wahuni wahuni na wale wasiokuwa nacho limekuwa kubwa sana. Kiasi inafikirisha ni kwa namna gani litaweza kupunguzwa.

Watawala wanajipangia mishahara na posho nono sana. ilihali mfanyakazi wa kada ya chini analipwa mshahara kiduchu.

Wafanyabiashara wa hali ya chini wanalipa kodi nyingi huku makampuni makubwa yakisamehewa kodi na kuingiza bidhaa bila tozo yoyote ile kwa kisingizio kuwa wanaisaidia Serikali kupambana na tatizo la ajira kwa watu wake.

Mifumo hii ya kishenzi ndio iliwasaidia watawala maana iliweza kuzifubaza akili za wananchi kwa umasikini na kuwafanya kuwa watu wenye fikra finyu.

Wakaishia kujikomba komba kwa watawala ilimradi watibu njaa zao.

Usingeshangaa kumuona mtu aliyeaminiwa na watu kama mtu mwenye msimamo thabiti na asiyeyumbishwa katika hoja yoyote inayoakisi ukweli, siku ikaja akatoa kauli ya ajabu na yenye kuwavunja moyo watu wale wanaomuamini na asijali kabisa.

Ilikuwa ni kawaida kwa wasomi waliotegemewa kuwa chachu ya kuleta mabadiliko kugeuka kuwa wezi na waongo wakubwa na wapotoshaji wa wazi bila hofu yoyote.

Yaani mtu yule yule anatoa kauli mwezi Januari kisha mwezi machi anatoa kauli kinzani na ile aliyotoa mwezi Januari, sio kwamba mtu huyu hana elimu au labda alighushi vyeti hapana, ni kwamba anajitahidi akae kwenye mfumo ambao anaamini akishakaa tu ataneemeka kwa kula jasho la wengi walio wanyonge. Maana sasa ni wazi kuwa kama Watawala hawashughuliki na matatizo ya wananchi na wananchi hao wanaendelea kulipa kodi basi usahihi ni kwamba wananchi hao ni wapumbavu tena wapumbavu sana.

Huwezi kulipia huduma ambayo haipo.

Na serikali yoyote ile inayolipa mishahara kwa watumishi hewa pia serikali hiyo inaongozwa na wapumbavu vile vile. Ni ujinga na kosa kubwa kumlipa mtu mshahara ilihali mtu huyo hakufanya kazi vile inavyotakiwa.

* ** ******

Leo hii Mh. Wiza anazungumzia suala la tunu za taifa ambazo ni uzalendo, utu,uwazi,uwajibikaji, uadilifu,Umoja na amani,

Tena bila aibu kabisa anasahau kuwa tunu hizo hazipo tena maana mifumo ya kihuni ilikwisha kushika hatamu.

Kikao kiliendelea kwa kila mmoja kuonesha msimamo wake huku wengi tu wakimpinga Raisi Mwibale Moha na wengi pia wakimuunga mkono ili aendelee kutawala. basi ilitokea mgongano wa misimamo baina ya hawa magwiji wa nchi

Ila hatimae waliokuwa wakimuunga mkono Raisi Mwibale Moha walishinda kwa wingi wao hivyo hii ilimaanisha kuwa Raisi mwibale amepata Baraka za Wazee kuendelea.

Fanton mahal alilifahamu hili sio leo tu tangu hapo awali alikuwa akijua ni wapi ambapo Raisi mwibale Moha anapata jeuri ya kuwananga wazi wazi wale wanaompinga.

Baada ya msimamo kuwa umeonekana wazi kuwa wengi walikuwa wakimuunga mkono Mh. Mwibale Moha ukumbi mzima sasa ulikuwa kimya, huku watu wakiendelea na mazungumzo ya chini chini wakisubiri chakula cha pamoja na vinywaji kama ilivyo ada kila mmoja akimtazama mwingine pale alipopata wasaa.

Raisi Mwibale Moha uso wake sasa ulianza kuonesha nuru tofauti na hapo awali na hii ni baada ya baadhi ya kauli zilizotolewa na wazee kwenda kwa Fanton Mahal kuwa asiiharibu nchi. Kwa kutaka kumuweka mtu ambae kwanza hana uzoefu na ambae hatoki katika mfumo wao baadae ikaja ikaleta madhara hivyo ugomvi wake na Mh. Mwibale Moha usifikie hatua ya kuvuruga utaratibu mzima uliopo.

Fanton Mahal awamu hii hakuongea hata kauli moja tofauti na awali ilivyokuwa kule Black chamber 17.

Leo hii alikuwa amekaa kimya tena kwa utulivu kabisa huku akiwa hana haraka yoyote ile, wengi wakihisi pengine ni kwasababu pia alikuwepo Mh. Murl Kamir, rafiki mkubwa wa marehemu baba yake Fanton. Mzee Mahal Abdul.

Mh. Murl Kamir alikuwa ni mtu mwenye muunganiko na wafanyabiashara wengi na wanasiasa mbali mbali duniani akiwa na urafiki wa karibu na tajiri mkubwa wa huko mashariki ya mbali Bwana Huang Feng.

Mh. Murl Kamir ndie anahusika na uagizaji wa bidhaa nyingi kutoka nje ya nchi, hususani sukari mafuta sabuni bidhaa za chuma na karatasi.

Huku akiwa anasafirisha baadhi ya malighafi kutoka Songomo kwenda nje kama vile makaa ya mawe, mazao ya misitu asili, ngozi za wanyama, pembe za ndovu na faru pamoja na meno ya tembo.

Murl Kamil alimfahamu vyema Fanton Mahal tangu ujana wake maana urafiki wake na Hayati Mahal ulianza siku nyingi enzi Mzee Mahal akiwa mjumbe wa bodi ya wawekezaji nchini Songomo. Ujumbe ambao baadae alikuja kujivua kutokana na utata mkubwa uliokuwepo kwenye bodi na kituo cha uwekezaji, kukiwa na uwalakini mkubwa katika namna walivyokuwa wakipitisha majina ya wawekezaji hasa wa kigeni.

Baadhi hawakuwa wakikidhi vigezo na wajumbe walikuwa wakikandamizwa na mamlaka yao kupokwa kwa nguvu kutoka juu huku wakipangiwa nani apewe kipaumbele na nani aachwe.

Hivyo uwepo wa Mh Mulr Kamir leo hii wengi walitafsiri kama ndio chanzo cha Fanton Mahal kukosa kauli lakini kitu ambacho wengi hawakujua, ni kile alichokuwa akiwaza Fanton Mahal kwa wakati huo. Na hawakujua kuwa mtu huyu alikuwa na mipango ipi mbeleni zikiwa zimesalia siku saba tu baraza kukaa na kupiga kura.

Ambapo baadhi ya watu kwenye Deep State walikuwa sehemu ya Baraza, iwe ni moja kwa moja au kupitia mashinikizo yao juu baadhi ya wajumbe hai.

Ajabu nyingine ni kwamba General alikuwa mzima kabisa tena akionekana mwenye nguvu tofauti na wakati ule anapandishwa chopa pale Cadmon.

Tofauti tu ni kwamba yeye alionekana mpole asie mchangiaji sana katika kikao hiki jambo ambalo Raisi alielewa ni kutokana na mshike mshike wa takribani siku tatu zilizopita, hivyo pengine alihitaji muda wa kutulia maana hata kuhudhuria kikao ni kwasababu tu nae alialikwa akiwa kama mtu muhimu kwenye masuala yanayolihusu taifa.

Hivyo mualiko huu wa ghafla ndio ulipelekea achomwe sindano za kutosha ili tu aweze kuwa katika hali ya kawaida lakini mara baada ya nguvu ya sindano hizo kuisha maumivu ya hapo hayaelezeki.

Kitu ambacho wengi hawakujua ni kwamba general alikutana na dhahma ya kutisha, na hakuwa amemwambia mtu yeyote kuwa mpaka hapo alikuwa chini ya ulinzi japo alikuwa akionekana kama yuko huru.

Kikao kiliisha na watu wote kuanza kuondoka ukumbini wakiingia kwenye meli moja ndogo ya kifahari iliyokuwa imeandaliwa rasmi kwa ajili ya matukio kama haya.

Meli ilikuwa na ulinzi mkali kutokana na aina ya watu waliokuwemo ndani ya hiyo meli Murl Kamir alikuwa amekaa na Fanton Mahal wakijadili jambo na mazungumzo yalikuwa kama Murl Kamir anamlaumu sana Fanton Mahal kwa kutaka kuingilia na kuharibu utaratibu wa wakubwa.

Murl Kamir alimwambia fanton Mahal, “Fanton sitarajii kusikia kwamba unapinga juhudi zetu wakati wewe mwenyewe unaneemeka kupitia mifumo hii hii ambayo unataka iondolewe je ni kwa faida ya nani? Ya kwako au kuna watu wengine unahisi unawapambania?”

Fanton alimwambia haoni vyema kuishi maisha ya kifahari ilihali wakati huo mamilioni ya watu wanakosa hata zile huduma za msingi, pili hawezi kuvumilia kuona watawala wakiingia mikataba ya ajabu na dunia ya mbali.

Mikataba ambayo inazidi kuudidimiza utu wa wanasongomo, wakati huo huo watawala wakineemeka na hongo kidogo wanazozipata kwenye hiyo mikataba.

Alipotaja kuhusu mikataba mara hiyo hiyo uso wa Murl Kamir ulisawijika na kumkatisha Fanton Mahal, “Wewe unawajua vizuri hao masikini unaowapambania? Je unadhani wao wakishika nafasi hizi watakufikiria kama hivyo unavyowafikiria? Acha kujidanganya Fanton, nimekufahamu tangu ukiwa mdogo. Kwanza nilidhani utakuwa na fikra tofauti na baba yako lakini sasa naona kumbe nyoka alizaa nyoka.

Mawazo na misimamo aliyokuwa nayo baba yako miaka ile sikutarajia kuviona kwako nilitamani nimuone mtu wa tofauti ndani yako Fanton. Masikini unaowapigania watakusaidia nini ? Unazungumzia suala la mikataba linakuhusu nini? Yale ni masuala ya wanasiasa na wewe ni mfanyabiashara kama mimi, ni bora ungekaa upande wetu tule mema ya nchi. Labda nikukumbushe tu kidogo, hapa duniani tupo kwa muda hivyo kuendelea kuipambania nchi hakutakupeleka popote na hautaweza. Maana huu ni mfumo wenye matokeo mazuri kwa aliyemo hivyo ni wachache watakaotongozwa na kuukataa huu mfumo.

Waliofanikiwa kuingiamo hawatamani hata kusikia tetesi za wao kupumzika walau hata mwezi sembuse mfumo kuondolewa?

Bwana mdogo, kama huwezi kutuunga mkono basi usitupinge. Hujui ni nguvu na pesa kiasi gani tumetumia kuyaandaa haya. kifupi ni kwamba unapotuambia tuachane na mipango yetu ni kwamba unatulazimisha tuchague hasara badala ya faida.

Wewe mwenyewe unamiliki makampuni mengi na unakwepa kodi, tukisema ufanyike ukaguzi wa makampuni yote tangu enzi za usimamizi wa baba yako mbona yatafutwa? Sioni sababu ya wewe kutunyooshea kidole maana wote tuko sawa kama ni uovu sisi na wewe wote ni waovu, kama wewe ni mwema mbona hulipi kodi vile inatakiwa?”
Alimalizia kwa swali.

Lakini Fanton alimwambia “ Nalipaje kodi ilihali najua kuwa haiendi kulisaidia taifa bali kuitunisha mifuko yenu ? Pili mimi kipato changu hakitokani na kukusanya kodi kwa wananchi, bali faida zinazotokana na biashara za makampuni.

Pia mimi sijaisaliti Imani ya wanasongomo kama mfanyavyo ninyi.

Labda nikuulize tu swali dogo, Je wewe ndiye uliehusika kumleta Bwana Huang Feng ili ainunue Lobeng
?”

Kitendo cha Fanton Mahal kuitaja Lobeng, kilimshitua vibaya sana Murl Kamir. Kiasi akakosa utulivu akabaki ametoa macho akiwa anajiuma uma midomo asijue cha kusema.

Mara akakurupuka na swali ambalo nahisi hakuwa amejipanga kuuliza, “ Ulitaka nimlete nani labda? Lakini pia nishakwambia yanayofanyika ni maswala ya utawala. Kama Serikali imeona fursa katika jambo Fulani ambapo nchi itapata matokeo chanya wewe ni nani hata upinge?

Na huwa nashangaa sana, Mh Raisi ameona aliletee taifa maendeleo ninyi watu mnaanza kupinga na kupotosha Umma juu ya jambo hilo. Ok kama nilivyokwambia Bwana mdogo fanya yanayokuhusu mengine waachie wenyewe.”

Mazungumzo haya yalikuwa yakifanyikia sehemu ya wazi lakini kulikuwa na sehemu iliyoandaliwa kama meza kukiwa na siti mbili zinazotazamana na huku viambaza hivi vikiwa vimeachana kama mita tano baina ya meza na meza lakini pia muziki ulikuwa ukisikika kwa mbali ni mziki aina ya country, wimbo wa No country music for old men ulikuwa ukirindima taratibu huku wakinywa wine za gharama. Meli ikizidi kuyakata mawimbi kuelekea ufukweni kutoka eneo la Peak Ice Hotel.

Fanton alimwambia Murl Kamir kwamba, “Najua unakaa upande huo kwasababu wewe ni miongoni mwa signatory wa Lobeng na ndio maana wewe na washirika wengine mnafanya State Indoctrination.”

Murl Kamir alimwambia Fanton Mahal kuwa masuala hayo hayamuhusu tena akae mbali kabisa maana sasa anavuka mipaka, na akijaribu kwenda mbele hatua moja zaidi atauawa.

Kauli hii aliitoa huku macho kayatoa akiwa kachafukwa roho. yaani alimaanisha kabisa hata mishipa shingoni ilimsimama. na alienda mbali zaidi kwa kupiga ngumi mezani kuoyesha msisitizo wa maneno yake.

Lakini tofauti na matarajio yake alishangaa kumuona Fanton akiwa anamtazama huku akitikisa kichwa kama anaemuonea huruma, kisha akaingiza mkono wa kushoto kwenye mfuko wa ndani wa koti lake la suti kama anaetaka kuchomoa silaha.

Murl Kamir akahamaki na kuingiwa na wasi wasi baada ya kudhani Fanton anataka kuchomoa bastola.

Badala yake mkono ulitoka na beji ya dhahabu yenye muhuri wa Ancient Guards of the nation. Akaiweka mezani bila kificho.

Mzee Murl Kamir alitoa macho, akaachama mdomo. Akawa anaikodolea macho ile beji asiamini aliyeitoa ni huyu huyu Fanton Mahal ambae amemfaham tangu akiwa kijana.

Hakuwahi kuiona kwa macho zaidi ya kuisikia tu kutoka kwa wakubwa wake, wengine walikwishakutangulia mbele za haki. Akawa akihisi ni hadithi tu za kusadikika zilizojaa uongo. lakini leo hii anaishuhudia mbele ya macho yake ikiwa imetolewa na mtu ambae ametoka kumpa vitisho sekunde chache tu zilizopita.

Murl Kamir alitetemeka mwili mzima na jasho jingi kuanza kumtoka hakujua hatima yake ni ipi.

Alijikuta akitamka kwa sauti ndogo “Mabaduni wa Serikali, kumbe ni kweli wapo?” Swali ambalo lilikosa wa kulijibu. Maana hakuwa na habari kama meli ilikwisha kufika na kutia nanga, kutokana na mawenge na sasa watu walikuwa wakishuka. Na alipotazama mezani tena hakuiona ile beji na sio beji tu, hata Fanton Mahal hakuwepo.

Alishangaa sana na kuogopa kwa wakati mmoja, akanyanyuka na kuanza kupiga hatua pole pole kutoka ndani ya meli. Alipofika nje aliangaza huku na huko kumtafuta Fanton mahal lakini hakumuona. Hivyo basi, kama watu wengine aliliendea gari lake lililokuwa limewashwa huku dereva wake akimsubiri waondoke. Alipofika mlango ulifunguliwa akajitoma ndani safari ikaanza.

******** ***** *******

General aliingia kwenye gari ambayo ilimleta mwanzoni mara tu alipoachiwa na mabaduni wa serikali ili ahudhurie kikao kwa sharti la kutoendelea na mipango yake. Na aliambiwa aache kushirikiana na Raisi kama anataka yeye awe salama na familia yake irudishwe ikiwa hai.

Hakuna kitu General anakipenda kama familia yake ya watoto wanne na mke mmoja ambao mpaka sasa hakujua walipo na wana hali gani.

Lakini kabla hajaachiwa kwenda kikaoni aliambiwa wako salama ila tu akae mbali na masuala yanayohusu wanasiasa.

Baada ya kufungua mlango wa gari, siti ya nyuma kulia alikutana na sura ya Malone akiwa amekaa siti ya kushoto ikimaanisha kuwa na yeye akae sambamba. Akasita kuingia akabaki amesimama, huku mlango ukiwa umefunguliwa vile vile.

Akatazama huku na huko mara akakutanisha macho na Fanton Mahal akiwa anamuangalia. Kisha Fanton akamuonyeshea kwa ishara ya kichwa tu kwamba aingie kwenye gari.

General akaingia , gari ikaondolewa eneo hilo kwa kasi na haikupita hata dakika General akagundua kuwa dereva hakuwa mwingine zaidi ya Macka Shinea. Pembeni ya dereva aliketi yule mzee aliyekuwa ameketi na Mwana kule bustanini na bado hatujamjua ni nani lakini nae alikuwepo kwenye kikao kilichomalizika punde tu.

Gari iliendeshwa kwa kasi ya ajabu kuelekea sehemu isiyojulikana. Wakiwa kwenye mwendo mkali kabisa kiasi General hili jambo likaanza kumpa wasi wasi akajikuta anauliza si mlisema mnaniacha…… hakumalizia sentensi yake alipigwa ngumi shingoni kwa nakozi ya kidole gumba pale pale akaona giza mbele yake kisha akasikia kitu cha baridi kilichochanganyika na maumivu kikiupenya mwili wake. Hapo fahamu zikamtoka kabisa akalala usingizi wa pono. Hatimaye safari illiishia eneo la Old Valley ambapo kulikuwa na kambi kubwa katikati ya msitu ambayo ilikuwa ikitumiwa na JISA( Junior Intelligence & Security Agencies). Eneo hili lilikuwa na miundombinu bora ikiwa ni pamoja na baadhi ya ndege za kivita Tanker aina mbali mbali kulikuwa na chuo cha mafunzo ya mapigano na ushushushu pia.

Baada ya kufika walikuta chopa kubwa imeshawashwa tayari kuanza safari wakajipakia na chopa likapaa likiwa na watu watano.

Safari iliishia katika mtaa mmoja uliokuwa kama mpaka kati ya mji wa Cadmon na mji wa Lobeng mtaa huu ulifahamika kwa jina la Soi.

General alizinduka na kushangaa akiwa katika eneo la Soi.

Pembeni yake kulikuwa na mtaalamu Malone, kwa mbali kidogo aliweza kuliona vumbi likitimka. Na hii ni kutokana na shughuli iliyokuwa inaendelea hapo.

Haikumchukua hata dakika kuweza kung’amua chanzo cha kuletwa mahali hapo maana kwa kumbu kumbu zake aliona ni wazi kuwa kulikuwa na tukio la kuchimbuliwa kwa baadhi ya mashimo ambayo ndani yake ilizikwa miili mingi sana ya halaiki waliouawa katika sakata moja la zamani kidogo.

Na hawa ni miongoni mwa wanaharakati waliokamatwa wakijaribu kuupinga ule mkataba wa Lobeng.

Tukio lenyewe lilikuwa hivi,: Mnamo tarehe 22 mwezi wa sita ikiwa imepita miaka mitatu tangu Raisi Mwibale Moha atwae kiti cha uraisi, taarifa zilianza kuenea kuwa Serikali kupitia kwa wawakilishi wachache ilikuwa inataka kuingia mkataba wa ajabu na kampuni moja kubwa kutoka Mashariki ya mbali jambo ambalo watu wengi waliliona kama ni ukiukwaji wa haki na utu wa Wanasongomo. Serikali kupitia wakuu wa taasisi mbali mbali ilikanusha vikali juu ya taarifa hiyo ikidai kwamba ni upotoshaji wa kiwango cha juu. Maana Serikali inatambua kuwa mali na ardhi ya Taifa la Songomo ni urithi wa vizazi na vizazi vya watu wa Songomo. Hivyo kutokana na Serikali kulitambua hilo haiwezi kushuhudia hatua yoyote ile inayoenda kinyume na maslahi ya Taifa ikichukuliwa kama ambavyo baadhi ya watu wanajaribu kuiaminisha jamii.

Lakini baadae Mwanaharakati Lozi Gozimbwe ambae alionekana kuwa mwiba sana kwa serikali alichapisha Preliminary Contract ya Lobeng na kuitolea maelezo ambayo wanaharakati mbali mbali walicharuka na kuungana na bwana Gozibwe katika ukososaji juu ya mkataba ule.

Mkatba ule ulikosolewa vikali sana na baadhi ya wanaharakati na wanauchumi wakidai kwamba Serikali imewakosea sana wananchi wa Songomo hivyo inabidi Raisi ajitokeze hadharani kutoa ufafanuzi juu ya Shutuma hizo.

Jambo ambalo Raisi alilitupilia mbali na kudai kuwa ni uzushi na propaganda za wanasiasa wenye tamaa ya kuingia Ikulu kupitia huruma za wananchi.

Wanaharakati waliwasilisha ombi la kufungua shauri mahakamani, ambapo ilichukua muda wa miezi mitatu hadi maamuzi ya mahakama yalipotoka.

Mahakama ya juu kabisa nchini Songomo iliamua kuwa Raisi anatakiwa aitishe mikutano mitano katika kanda zote tano, ili kuondoa sintofahamu hii. Lakini Raisi hakutii wito wa mahakama, kitendo ambacho kilimaanisha kuwa Muhimili wa juu wa baraza kuu unaukandamiza muhimili mwingine mkuu pia wa haki na maamuzi( Executive over Judiciary).

Kutokana na Raisi kuwa na moyo wa jiwe na kutotaka kulizungumzia jambo hili na kulitolea ufafanuzi, wanaharakati waliandaa maandamano ya kumtaka Raisi ajiuzulu na awajibishwe kwa kutumia madaraka vibaya. Maana amekaidi wito wa Mahakama na sauti za wananchi wake.

Maandamano yalipangwa kufanyika Tarehe 22 mwezi Oktoba tena maandamano hayo yalikuwa na kibali kutoka mahakama kuu, lakini baadhi ya wakuu wa majimbo kama Magavana walianza kuyapinga maandamano hayo huku wakisema kuwa yataleta uvunjifu wa amani nchini.

Lakini watu kutoka majimbo mengi nchini Songomo walikuwa tayari kuandamana ambapo maandamano yangedumu kwa takribani siku kumi kutokana na namna mazingira yalivyokuwa.

Tarehe 22 Oktoba mapema sana watu walianza kuandamana barabarani Jijini Homa bay, wakiongozwa na wanaharakati na wanasiasa wengi maarufu. Lakini ajabu polisi waliwavamia na kuanza kuwapiga waandamanaji kitendo ambacho kilizua vurugu na kupelekea jeshi la polisi kuzidiwa nguvu na ikawa ni kama vita.

Baadae wanajeshi waliingilia fujo hii na kuanza kupiga watu na kuwajeruhi.

Watu wengi walikimbia baada ya kuona kipigo kinazidi na wengi pia walipata vilema vya maisha huku wachache wakifariki katika vurumai ile.

Hatimaye takribani watu elfu tatu walikamatwa katika majimbo yote ya Songomo kutokana na sakata lile la maandamano na kupelekwa katika kambi ya Soi maana huko ndiko kulikuwa na kambi kubwa sana ya mateso tangu hapo zama za ukoloni inasemekana kambi hii ilikuwa na ukubwa wa Hekari elfu saba.

Na ndani ya kambi hii kulikuwa na mateso makali sana ikiwa ni pamoja na kunyimwa chakula kwa muda mrefu.

Inasemekana wale watu elfu tatu waliokamatwa watu elfu mbili mia tano kati yao waliuawa na miili yao kwenda kufukiwa nje ya kambi eneo la Soi huku wengine miili yao ikitupwa kwenye mto mkubwa wenye mamba ili wawe chakula cha mamba. Hivyo watu wengi waliuawa akiwemo mwanaharakati Lozi Gozibwe. Pia baadhi ya watu waliouawa wana undugu wa damu na baadhi ya Mabaduni wa Serikali.

Na Mauaji yale yalitekelezwa kijeshi chini ya amri ya Huyu General wakishirikana na Raisi Mwibale Moha.

Hivyo hata kama Deep State wangeimba vipi kuhusu huu uhasama kukoma, jawabu ni kwamba hakuna namna Mabaduni wangeweza kulifumbia macho hili swala lipite huku wao wakiwa kama walinzi wa taifa.

Mashimo yalifukuliwa na kutolewa mifupa na mafuvu ya watu

Wengi hesabu yao ilizidi elfu moja kwa maana kwamba kuna baadhi ya watu walikuwa wakipotea kimya kimya tena kwa kasi na mwisho wake ilikuwa ni mauti na kufukiwa Soi.

Hakika ilikuwa ni simanzi nzito kuitazama ile miili.

Haukupita muda aliingia Fanton Mahal akiwa na waandishi wa habari na baadhi ya Mawaziri na wafanyabiashara wa Songomo na msafara wa watu wengi ulianza kusogea eneo hili baada ya taarifa kuanza kurushwa live kwenye vituo mbali mbali ikiwa ni pamoja na mitandao mbali mbali.

Habari hii ilipewa Jina la (The Mystery of Soi Body Fossils)

Habari hii ilikuwa na wafuatiliaji wengi sana ulimwenguni kutokana na namna mashimo yale yalivyokuwa yanaonekana, kwanza ilitisha na kusisimua mno.

Nguli wa habari nchini Songomo alikuwepo eneo la tukio na huyu si mwingine bali Golo Zumba.

Zumba mara nyingi hutembea na meza na viti vitano kwenye gari lake ambavyo ni convetible. Zumba ndio yule mzee aliyekuwa amekaa kwenye bustani na Mwana. Na alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa kwenye helikopta iliyokuja na General. Baada ya msafara wa Fanton Mahali kuwasili vijana wa Zumba nao walitia timu kwenye gari ya ofisi.

Hivyo wakati hayo yakiendelea Zumba na vijana wake walikuwa wakiandaa mazingira ya mahojiano ikiwa ni meza na mitambo mbali mbali pamoja na vifaa kazi.

Haukupita muda msafara wa Raisi Mwibale Moha uliingia msafara huu ulikuwa na watu wazito sana nchini Songomo. Akiwemo Director General wa SIA( Songomo Intelligence Agency)Martin Kasoka, alikuwepo CMI (Chief of Military Intelligence) Bwana Kau Kamale. Mwnasheria mkuu wa Serikali, wote walikuwa kwenye huu msafara.

Baada ya gari kusimama alishuka Team leader akamfungulia Raisi mlango, Raisi alishuka huku akijiweka sawa kwa kulivuta koti lake kwa mbele kwa mikono miwili huku akinyanyua juu mabega na kuyashusha kama ishara ya kujiweka sawa na kaubabe kakiwemo ndani yake.

Baada ya Raisi kushuka tu kwenye gari wanausalama walipata kazi ya ziada ya kuwaengua waandishi wa habari waliokuwa wakimzonga Raisi muda wote wakitaka kumhoji.

Huku nyuma akifuatiwa na jopo kubwa la wanausalama na watu aliokuja nao.

Raisi alitembea huku akiongozwa na Team Leader kwa jicho la kawaida ni kama team Leader alikuwa akishughulika na usalama wa Raisi.

Lakini kwa jicho tofauti ungeweza kuhisi kuna namna tofauti katika uwajibikaji wa Team Leader.

Raisi aliongozwa mpaka sehemu ambayo kulikuwa na viti na meza, na mezani alikuwepo Zumba peke yake akiwa na Tablet yake.

Mezani kulikuwa na kamera kubwa mbili kwa juu urefu wa kama mita nne na mic tano zikiwa zimewekwa kulingana na idadi ya viti. Raisi baada ya kufika alipokelewa na Zumba aliyempa mkono baada ya kusimama kama ishara ya heshima kwa Kiongozi wa taifa kisha akamuashiria kuwa wakae.

Team leader alibaki amesimama hatua kadhaa nyuma huku majabali ya ulinzi yakiwa makini.

Punde tu General Floyd Balehl nae alisogea mezani na kuketi akiongozwa na Malone. Baada ya kuketi alimtazama Raisi Mwibale Moha kwa macho ambayo yalijaa lawama ni kama alikuwa akimuuliza kwanini umeniingiza katika mambo ya ajabu namna hii? Raisi kutokana na kutokuwa na uwezo mkubwa wa kijasusi hakuwa ameusoma mchezo huu kikamilifu tofauti na General ambaye pua zake zilikuwa na uwezo wa kunusa hatari iliyopo kilomita elfu moja.

Raisi yeye hakujua kuwa yeye tu ndie alikuwa akisubiriwa ili shughuli ianze. Mwanasheria mkuu wa Serikali nae alifika na kuketi.Idadi ikawa watu wanne, akisalia mmoja tu ili meza itimie, dakika kadhaa mbele aliingia Murl Kamir akiwa anaongozwa na Fanton Mahal.

Ujio wao ni kama baba na Mwanae jinsi walivyokuwa wameongozana, maana walikuwa wakizungumza vizuri ila ni mazungumzo ambayo hayakusikika kwa mtu wa tatu.

Ingawa kimuonekano yalionekana ni mazungumzo yaliyojaa amani, lakini uhalisia ni kwamba Murl Kamir alikuwa akimuomba sana na kumsihi Fanton Mahal asifanye haya anayofanya maana yatawagusa wengi na inaweza kupelekea taifa kutetereka na kuyumba.

Ni maneno ambayo Fanton aliyaona kama njia za mtu anaetapa tapa tu maana ni kama mzee alikuwa anajaribu kutumia turufu yake ya mwisho.

Hatimae Murl Kamir aliifikia meza na kuketi. Hapo ndipo mahojiano yalipoanza.

Mh Mwibale Moha alitarajia mahojiano yawe na mipaka yenye kuitambua nafasi yake katika taifa hili, lakini ikawa kinyume chake.

Aina ya mtindo wa maswali aliokuwa anautumia Mh Zumba ni ule uliokuwa ukiidhihirisha shutuma za wazi kwa hawa watu, kwa maana nyepesi ni kama mtu ambae alikuwa na uhakika mkubwa kuwa wao ndio walikuwa wahusika wakuu wa hili tukio.

Kitendo hiki kilipelekea Mh Mwibale Moha kuwa anamtazama Zumba jicho Fulani hivi ambalo sio la kheri kabisa.

Ni kama alikuwa anajaribu kumpa ujumbe wa hatari kuwa nikitoka hapa nitakufanya kitu kibaya usikae ukasahau maisha yako yote.

Hata General mwenyewe alishangazwa na ujasiri wa Zumba, maana Zumba alikuwa akiuliza maswali ambayo hayakuzingatia kabisa kinga za watu hawa, japo hakuwa akiwahoji kama vile mwizi wa simu mfukoni afanyiwavyo.

lakini wao waliona wazi nafasi zao hazikuwa zikiheshimiwa kabisa.

Mwanasheria Mkuu yeye alikuwa akijibu maswali vile anavyojisikia, maana kwanza aliamini kwa ubobevu wake katika sheria na mikataba ni vigumu sana kwa wao kuingizwa hatiani na hilo lilikuwa wazi usoni mwake maana alikuwa akimtazama Mh Zumba kwa kebehi mithili ya mtu anaesema Ndugu mwandishi unapoteza muda wako bure.

Kwanza wakati anawasili eneo hili alikuwa akimtazama Fanton Mahal kwa jicho la kejeli sana yaani aliwaona kama wanasesere Fulani.

Watu wengine walikuwa wamesimama mbali kama mita ishirini kutoka meza ilipo wakiwa wamefanya duara.

Baada ya mahojiano haya mazito ambayo yalikuwa yakifuatiliwa moja kwa moja kupitia vituo mbali mbali ulimwenguni na kadri muda ulivyokuwa unasonga idadi ya watazamaji ilikuwa inaongezeka kwa kasi sana maana mpaka ilikuwa imefikia watazamaji milioni miambili.

Wananchi mitaani walikuwa wakiandamana wazi huku wakiwa na mabango kuwa wahusika wajiuzulu na wakamatwe ili wawajibishwe kulingana na makossa yao.

Kutokana na kelele za wananchi kuwa juu kuliko kawaida na kuleta hofu ya machafuko ofisi ya Mkurugenzi wa makossa ya jinai ikishirikiana na ofisi ya Jaji mkuu ilitoa kibali cha kukamatwa kwa watu hawa na kufunguliwa mashitaka mara moja.

Baada ya hati ya kukamatwa kuwasili, kuliwasili watu kutoka Makao makuu ya jeshi wakiwa na ombi la kumchukua kiongozi wao kwa muda, Ili wakamhoji kwa kutumia utaratibu wa kijeshi ili wakijiridhisha juu ya tuhuma zinazomkabili waweze kutengua mamlaka yake.

Kutokana na kanuni namba 329 kutoka sura ya kwanza kipengele namba nne ya makosa ya kijeshi chini ya (Songomo Penal Code).

General alitakiwa kufikishwa Songomo Superior Military Court.

Ilkuwa ni sawa kabisa kutokana na madai yao, lakini wasi wasi wa watu wengi ilikuwa ni je haki ingetendeka ipasavyo kutokana na cheo cha muhusika mwenyewe?

Lakini hakukuwa na karatasi ya kulipinga ombi kutoka kamandi kuu.

Basi General alikabidhishwa kwa wajumbe hawa wanne wenye insignia ya Brigedia General wakiwa wameambatana na military police saba wenye insignia ya sergent na corporal. Wakaingia kwenye chopa la kijeshi wakaondoka eneo hilo.

Waliobaki walichukuliwa na watu kutoka kitengo maalumu, kwaajili ya mahojiano zaidi kwa maana sasa ni kwamba Raisi Mwibale Moha, mwanasheria mkuu Mh. George Sobue na Mh Murl Kamir walikuwa chini ya ulinzi tena ulinzi mkali ili waweze kuhojiwa na hatimae kufikishwa katika Mahakama ya juu kabisa ya Songomo kujibu tuhuma mbali mbali ambazo ni Uhalifu dhidi ya ubinadamu, matumizi mabaya ya ofisi, na Uhaini.

Hatua hii ilifuatiwa na kushikiliwa kwa hati zote za kusafiria kwa wote na akaunti zao zote kuzuiliwa kuanzia zile zilizopo nje ya nchi mpaka za ndani.

Uchunguzi yakinifu ulianza kwenye miradi mbali mbali iliyokuwa ikimilikiwa na hawa watu, kiasi cha mali nyingi sana zilishikiliwa na serikali chini ya maelekezo ya Makamu wa Raisi ambaye alikaimu Madaraka hayo kwa muda mpaka hapo baadae.

Lakini kuna kiasi kikubwa hawa watu walikuwa wamekificha nje ya nchi na hakikuwa kwenye akaunti inasemekana ilikuwa ni pesa taslimu ikiwa imewekwa kwenye masanduku ya chuma na kuchimbiwa sehemu isiyojulikana. Wengi wakidai ni nje ya nchi wengine wakidai ni humo humo nchini Songomo ila eneo ndilo halikufahamika ni wapi hasa.

* *** ****

Kutokana na hofu ya baadhi ya washirika juu ya kutajwa na kuhusishwa na kashfa hiyo, basi baadhi ya ushahidi ulianza kufutwa kama vile watu wa karibu waliokuwa wakifahamu mafungamano ya hawa ambao hawajatajwa na wale ambao tayari wanatuhumiwa.

Wa kwanza ambae alitakiwa kuuawa ni Zurfa, huyu ni shangingi la mjini, anamiliki saluni moja kubwa sana jijini Homa bay. na mara nyingi makahaba wakubwa na wa bei ghali hushinda hapo na kupiga mdomo juu ya mikakati mbali mbali.

Makahaba hawa hutoa huduma kwa vibopa wa nchi, hivyo kuambulia baadhi ya siri za hawa watu ikiwa ni pamoja na kuwa na taarifa juu ya mienendo ya baadhi ya Viongozi.

Hivyo mara nyingi wanapokuwa Saluni kwa Zurfa, hujikuta wakimwaga mchele wote hata ule uliotakiwa kubaki kama akiba ya ugeni.

Zurfa pia huwakuwadia wanawake kwa viongozi mbali mbali na matajiri maana yeye mwenyewe alikuwa ni muuzaji wa mwili kwa gharama kubwa, mpaka pale alipokutana na mkwasi Fanton Mahal na kufanikiwa kuanzisha baadhi ya miradi kupitia mkwasi huyu, kama vile Hoteli moja kubwa ya nyota tatu pia ana kampuni kubwa ya upambaji na hii saluni kubwa ya kike achilia mbali mabasi madogo madogo ya usafirishaji yasiyopungua kumi.

Kifupi mwanamama huyu amefanikiwa kuitibu njaa na baadhi ya mahitaji ya msingi baada ya kukutana na Fanton mahal si unajua tena ukikaa karibu na uwaridi lazima unukie tu.

Ukimtazama Zurfa sura yake utamuona Mwana , tena mwingi tu.

Asubuhi yapata saa nne Zurfa alikuwa ashawasili ndani ya hoteli ya Crooven Hotel kwaajili ya kukagua maendeleo ya mradi huu pamoja na kuzungumza na baadhi ya wafanyakazi wa hapa ikiwa ni utaratibu wake kufika walau mara moja kwa kila juma. Wakati anasalimiana na mtu wa mapokezi ndani, kwa nje kuna gari moja ya kifahari aina ford ilipaki na waliokuwemo hawakuwa na haraka ya kushuka mpaka walipoona mlinzi aliekuwa zamu akiisogelea gari ndipo kioo upande wa dreva kilishushwa kidogo. Wakamuuliza mlinzi maswali machache kisha wakashuka na kuelekea mlango mkuu wakiwa idadi ya watu watatu huku dereva akibaki kwenye gari.

Ujio wao haukuwa na mashaka kutokana na namna walivyokuwa wamevalia nadhifu sana.

Waliingia mapokezi ambapo waliomba vyumba vitatu floor ya saba juu ambayo ilikuwa ni vyumba kwa wazito tu lakini pia kwenye hii floor ndio kulikuwa na chumba ambacho hukitumia Zurfa pindi awapo hapa.

Walilipia na kupewa kadi zao kama funguo kisha waliingia kwenye lifti iliyowapeleka hadi sehemu husika.

Mazingira na namna hoteli ya Crooven ilivyojengwa yalivutia sana na ilikuwa ni miongoni mwa hoteli nzuri sana jijini Homa bay.

***** ****** ****** ********

Jiga Kinamba baada ya kuondoka Cadmon akiwa na Mwana safari yake iliishia Jijini Homa bay, ambapo aliona atafute sehemu tulivu ili aweze kujipumzisha akiwa na mlimbwende wake ili apate pia kuzungumza nae vyema.

Safari ambayo iliishia Crooven Hotel, kwanza ni kwasababu kumbu kumbu zake zilikuwa vyema juu ya hii hotel kama sehemu iliyotulia. Maana ilikuwa imezungukwa na miti mingi ya matunda na maua mwitu mbali mbali ambayo ilitengeneza kajimsitu Fulani kalikoleta hewa safi na ya kipekee kwa watu waliokuwa wakibarizi katika viunga vya hii hoteli.

Vyumba vya hii hoteli vilikuwa vikubwa sana na vyenye madirisha makubwa ambayo yalipitisha hewa safi na kuingia vyumbani kulikuwa hakuna haja ya kuwasha kiyoyozi.

Baada ya kufika Crooven hotel, Mwana alimuuliza Jiga Kinamba “Unapafahamu hapa ?”

“Ndio napafahamu vipi kwani?”

“Hapana nimeuliza tu”.


Walipaki na kuingia ndani ambapo baada ya kufika mapokezi tu Kijana aliekuwa mapokezi alimsabahi Mwana kwa heshima na bashasha na kumpatia kadi maalum ( Stuff Card) ya chumba moja wapo floor namba saba.

Hii kidogo ilimfikirisha Jiga Kinamba lakini hakutaka kuwa na haraka alijua tu si muda atafahamu vyote asivyovijua kumuhusu huyu binti.

Basi baada ya kukabidhiwa kadi waliingia kwenye lifti iliyowapeleka floor husika wakajitoma chumbani. Kwakuwa walifika jioni basi uchovu wa safari ulikuwa wazi kwa wote kutokana na kukaa sana kwenye gari.

Waliingia bafuni ili kuoga.

Na hii ilikuwa ni mara ya kwanza kwa wawili hawa kuwa pamoja tena faragha basi ilikuwa ni furaha ya ajabu kwa wote maana kila mmoja alipata wasaa wa kuusaili mwili wa mwenzake ipasavyo hakika ilivutia hasa kuwa na kiumbe wa aina ya Mwana.

Jiga Kinamba aliutazama mwili na maungo ya huyu mwanamke mbichi kwa hamu kubwa sana na kadri maji yalivyokuwa yakiwamwagikia ndivyo ilileta raha zaidi huku vituko na uchokozi wa kushikana shikana vikiikoleza zaidi raha yah ii siku.

Ndimi zilinyonywa zikanyonyeka tena kwa hisia za kweli sio yale mapenzi ya kununua bali ni ile ashiki itokayo kwenye uvungu wa tamaa na hamu ya mioyo ya wote wawili.

Ulaini wa maungo ya huyu mwanamke na ulegevu wa macho vilizidi kumzamisha kihisia Jiga Kinamba na kujikuta wakizama ndani sana ya ulimwengu wa huba kiasi cha kubadili kasi ya kuhema na kubaki wakihemea jujuuu tu.

Haya yaliendelea kwa takribani dakika arubaini na tano mpaka walipoamua kumaliza kuoga na kurudi chumbani huku wakipokelewa na kitanda kikubwa kilichotandikwa vyema kama kilichokuwa kikitaraji yanayofuata juu yake.

Kitanda kiliwalaki na kuwaficha ambapo madoido mengi yaliendelea huku kila mmoja akijaribu kumuonesha mwenzake vile alivyotunukiwa maujuzi kunako ulingo wa wawili.

Burudani ya aina yake iliyosindikizwa na miguno ya hapa na pale iliendelea ilikuwa ni purukushani za patashika shuka kuchanika na kitanda kuvunjika Mikunjo ya ajabu na umafia wa Sanaa vilitumika kuhakikisha kila mtu anahitaji kuibuka kidedea.

Mitindo ya ajabu unayoijua na kuisikia ilitumika na ilikuwa ni ruksa maana hakukuwa na muamuzi wa kupuliza filimbi.

“She just had to ask for it. He gave it to her, treated and satisfied her like a Bitch.”

Moral of this part to all Realmen : “When fucking, https://jamii.app/JFUserGuide like you’ve never fucked and like you’ll never https://jamii.app/JFUserGuide, otherwise don’t https://jamii.app/JFUserGuide.”

Baada ya sanaa iliyochukua takribani masaa matatu na nusu, hatimaye wote walirudi maliwatoni, kila mmoja akimmwagia sifa kem kem mwenzake

Walipomaliza ilikuwa ni kujilaza, wala usingizi na uchovu havikuwaruhusu walau wazungumze maana ni punde tu wote walipotelea usingizini wakiwa wamekumbatiana Al-burrrrrdaaan!!.

Asubuhi ilikaribishwa kwa miale ya jua iliyokuwa ikipenya kupitia dirishani na kuingia chumbani ambamo wapenzi wawili walikuwa bado wamelala.

Mwanga wa jua ndio uliwaamsha na wa kwanza kuamka alikuwa ni Jiga Kinamba ambapo alitazama saa ya ukutani iliyoonesha kuwa tayari ilikwisha kutimu saa mbili na madakika yake.

Kisha akatupa macho kando kuusaili mwili wa mlimbwende aliyekuwa bado amelala, alimtazama namna alivyovimba na kujaa vyema sehemu za nyuma zilizojishikiza vyema kwenye kiuno chembamba, akakitazama na kifua cha huyu mwanamke kilivyobeba tunu za maana.

Akiwa bado anamuangalia, mara Mwana alifumbua macho taratibu na kuyafikicha ili aweze kuona vyema.

Jiga Kinamba alikwepesha macho yake kwa haraka ili kuepuka kujulikana kama alikuwa akimtazama mrembo huyu, lakini alichelewa maana tayari Mwana alikuwa ameng’amua hilo, ambapo hali hii ilizua tabasamu la kicheko kutoka kwa Mwana.

Baada ya hapo mwanaume alihamishia fikra zake kwenye simu na kuanza kuperuzi taarifa mbali mbali nyingi zikiwa zinaelezea kuhusu Mwibale Moha kushikiliwa na hiyo ilimaanisha kuwa alikosa sifa ya kuendelea kugombea nafasi ya Uraisi.

ILipotimu saa tatu Mwana alivuta simu ya mezani na kuagiza stafutahi kisha wakaendelea na maongezi ya hapa,na pale ikiwamo kujitambulisha kwa wawili hawa na hapo ndipo Jiga Kinamba alifahamu kuwa kumbe hoteli hii ni ya mama yake Mwana, Bi Zurfa. Na juu ya hilo ni kwamba huyu Mwana ni binti wa kuzaliwa kabisa na Mkwasi Fanton Mahaal.

Wakati mazungumzo yakiendelea ilisika kengere ya mlangoni ambapo Mwana alisimama na kwenda kufungua mlango, akakutana na muhudumu akiwa na vifurushi kadhaa vya chakula akapokea na kuurudishia mlango ambao baada ya sekunde tano ulijilock.

Baada ya kifungua kinywa walioga na kuvaa wakatoka wakiwa na lengo la kwenda floor ya chini ambapo kulikuwa na maduka, walihitaji mavazi hasa wakiwa hapa.

Basi walishuka chini na kuingia dukani na kufanya manunuzi ya nguo na mahitaji mengine kisha wakatoka nje, wakashika korido ndefu iliyokuwa inaelekea kwenye lifti na ngazi za kuelekea chini lakini pembeni kabisa kulikuwa na mlango mzito ambao muda mwingi huwa umefungwa.

Kwa uzoefu wa Jiga Kinamba alijua kuwa ile ni vent ya kuelekea chini kwenye basement za hii hoteli ikiwa kuna dharula inayohitaji kufanya hivyo.

Lakini wakati wakiwa bado hapo nje ya duka Jiga Kinamba alizitazama gari zilizokuwa zimepaki pale nje akaitilia mashaka gari moja, maana plate number yake ilikuwa na kasoro ambayo ilihitaji umakini ili kuweza kulitambua hilo.

Namba moja ilikuwa imefutwa nusu, hivyo kupelekea kutoonekana vyema yaani huwezi kuelewa kama ni nane ama tatu au ni tisa.

Kengele ya hatari ikagonga kichwani, wakaiendea lifti huku Mwana akiwa hana hili wala lile lifti ilpofika floor ya saba ikagoma kufunguka, kila wakibofya kitufe inagoma lakini ilpofika floor ya nane ikafunguka na hapo ndipo Jiga Kinamba akatambua kuwa eneo lililo kwenye hatari ni floor namba saba.

Muda huu wote tangu walipowasili hapa alikuwa ameivaa ile sura ya Seif maana wakati wanaondoka Cadmon alikuwa na sura yake halisi ya Jiga Kinamba lakini baada ya kuwa wameuacha ule mji kama kilomita nne ndipo aliivaa sura ya Seif.

Baada ya kutoka kwenye lifti walilazimika kutumia ngazi kushuka. Jiga Kinamba alimwambia Mwana akae nyuma yake na awe makini maana anahisi hali tofauti hapo hotelini hivyo kuna ugeni usiokuwa wa kawaida hotelini hapo.

Mwana ikabidi tu atii sharti japo hakuelewa maana ya maneno ya Jiga Kinamba.

Wakiwa wanamalizia ngazi ili waishike korido ya vyumbani wakakutana na mtu alievalia suti nyeusi akiwa na bastola yenye kiwambo akawazuia na kuwaamuru warudi walikotoka na kuwaambia kuwa floor namba saba iko katika hali ya dharula kidogo.

Jiga Kinamba alizidi kupiga hatua zenye hesabu kali ndani yake kama anaetaka kulazimisha kupita maana kwanza alimuaminisha huyu mtu kuwa yeye ni goi goi tu asieweza wala kujua lolote muda wote huu macho ya huyu mtu yalikuwa yamemakinika kwa Jiga Kinamba.

Ile sasa anayapeleka kwa Mwana akagundua kuwa binti huyu anafanana kabisa na yule Mwanamama walietumwa kumuua.

Hapo ndipo akagundua kitu lakini kabla hajafanya chochote alizungushiwa vidole shingoni kwa kasi ya ajabu na mtu ambaye yeye alimchukulia kama mluga luga tu.

Ni kitendo kilichoacha jeraha jembamba ila lililochimba kwenda ndani zaidi na kuifanya nyama za kuta za jeraha kuonekana namna zinavyokusanya damu na kuitemea nje.

Alidondoka chini huku roho ikiuacha mwili kifupi alichinjwa ghafla kwa kisu chembamba na kuuawa kinyama.

Mwana sasa alianza kumtazama huyu mtu kwa sura na mtazamo tofauti hakuwa akijua kama yule Seif aliezoea kumuona mpole anaweza akawa kiumbe wa ajabu namna hii hakuamini alianza kurudi nyuma kwa uoga ambapo Jiga Kinamba alimfuata na kumshika mkono huku akimvuta kwa nguvu na kumkokota kuelekea koridoni ambapo alikutana na mtu mwingine wa pili akiwa na mavazi kama yale yale yaani suti nyeusi.

Mtu huyu baada ya kuwaona tu aliwaambia huku akipiga kelele kuwatahadharisha “Hakuna njia huku hakuna njia huku”.

Lakini ndio kwanza walizidi kumfuata alipoona hawamsikilizi alivuta bastola ambayo haikutumika. Maana uhai wa mwenye bastola ulikatishwa na risasi iliyotoka kwenye bastola ndogo sana ya Jiga Kinamba mithili ya pochi ya kiume ya kubebea pesa.

Risasi hii moja ilitua vyema katikati ya paji la uso na kufumua sehemu ya nyuma ya kichwa na kuufanya ubongo kumwagika sakafuni.

Walipoufikia mlango wao waliuona ukiwa umefungwa vile vile, lakini chumba cha mbele yaani mlango wa nne ukihesabu kuanzia kwenye chumba chao walisikia kelele za mtu akiomba msaada na sauti ikiwa ya kike.

Sauti ambayo mwana aliitambua vyema maana hata angekuwa ndotoni asingeshindwa kuitambua sauti ya mama yake.

Baada ya kuisikia sauti ya mama yake akiomba msaada alimwambia Jiga Kinamba kuwa sauti hiyo ni ya mama yake.

Basi walifanya upesi kuufikia mlango huo ambao ulikuwa wazi ukiwa umeacha upenyo wa mtu kupita kwa kujipenyeza kiubavu ubavu.

Basi waliingia ndani na kushudia mwili wa mwanamke ukiwa kwenye dimbwi la damu akiwa na hali mbaya kutokana na majeraha ya kisu tumboni muuaji alijitosa toka floor ya saba kwenda chini. Alipitia dirishani kutokana na uwazi wa kioo kusukumwa kidogo uliokuwa unaonekana, Jiga kinamba alijaribu kuchungulia kupitia dirishani kwenda chini akamuona mtu yule akitembea kuelekea kwenye ile gari aliyoitilia mashaka.

Uwezo wa huyu muuaji kidogo ulimpa mashaka maana hakuwa sawa na wale aliowaua pale koridoni. Inaonekana huyu alikuwa ni mamluki wa kukodiwa aliebobea maana hata urukaji wa kutoka floor ya saba kwenda chini iliwezekana kwa watu wachache sana tena walioiva sana kimafunzo, yaani sio mtu wa kawaida kabisa.

Wakati ile gari inataka kutoka getini tu kuna gari nyingine ya gharama ilifika na kuweka zuio hapo getini, kisha kwenye gari alishuka Shetani mwenyewe “Fanton Mahal”

Kitendo cha Fanton Mahal kushuka na ile gari kuendelea kuweka zuio pale kiliwafanya wale watu wawili kushuka yaani dereva na yule muuaji.

Walishuka ili kumshikisha adabu huyu mjinga alieegesha gari mbele yao.

Hawakujua kuwa huyu kiumbe hakuwa wa level yao kabisa. kwanza ogopa mtu anatembea na walinzi lakini kawaacha kwenye gari na kushuka akiwa peke yake.

Watu hawa walizipiga hatua kumwendea Fanton Mahal wakijiamini sana kuwa wanammudu mtu huyu, lakini ukweli halisi hawakuujua.

Walipomkaribia walichomoa visu wakiwa tayari kushambulia.

Wakiwa wamejiandaa vyema kabisa, ndipo walipoona kitu kilichowashitua sana tena sana.

******* ******** *********

General akiwa ameshikiliwa katika jengo moja lililopo Makao makuu ya Jeshi, alikuwa na furaha maana alijua vijana walicheza vyema ili waweze kumtengenezea mazingira ya kutoroka nchi. Wakati huo akiwa ameshafunguliwa mashitaka makama kuu akiwa kama Absentia.

Aliona wazi hatia itawaangukia kulingana na watu walio nyuma ya hilo suala japo Mwanasheria Mkuu alikwisha kuwaaminisha kuwa watabaki salama hawataweza kuinngia hatiani, lakini yeye aliamini nguvu ya watu walioko nyuma ya hilo jambo inaweza kuwaangamiza kabisa huku yeye akiwa amepewa mgao kiduchu tu na hawa wanasiasa.

Aliona ni bora afanye mpango atoroke nchi na kwenda kuishi mafichoni mpaka hapo baadae. Japo alijua kuwa familia yake anaiacha katika mikono ya hao watu.

Ila Imani ya familia yake kubaki salama ilikuwa kubwa maana watu hao wasingeweza kuidhuru familia yake kwaajili ya makosa yake maana kama ni kuidhuru wangeshafanya hivyo tangu hapo awali.

Kwasasa jambo ambalo alilitaka ni kutoroka kwanza, asalimishe maisha yake na aibu iliyokuwa mbele yake hakuwa tayari kuona mabadiliko ya muda mfupi eti akitoka kuwa kiongozi aliheshimiwa na kufanyiwa mambo mengi, leo akigeuka kuwa mfungwa asie na thamani kabisa tena ndani ya majuma mawili tu.

Kutoroka ilikuwa ni lazima kwake kwa namna yoyote ile hata kama ingegharimu kupoteza mkono ila atoroke tu, alikuwa tayari kwa hilo.



Je unadhani general atafanikiwa kutoroka?

Nini hatma ya wauaji kule Croveen Hotel?

Je Zurfa hatma yake itakuwaje?

Tukutane sehemu ya tano, wenu katika utunzi Sonko Bibo.
 
Back
Top Bottom