Mkuu John tatizo kubwa linalotuumiza watanzania ni UJINGA. Siku zote watu wamekuwa wakisema lakini wanaonekana wana chuki dhidi ya serikali. Ila ukweli ni kwamba sisi tulikuwa na nafasi kubwa ya kupiga hatua kubwa sana kimaendeleo kuliko nchi yoyote ile barani Afrika.
Kamati ya haki ya mtoto ya Umoja wa Afrika (African Committee on Rights and Welfare of the Child) iliwahi kuchapisha taarifa yake ya mwaka na kutaja nchi ambazo zinatoa elimu bora yenye viwango kwa watoto barani Afrika. Rwanda ndiyo ilikuwa ya kwanza, na wataalamu wengi wakapinga. Timu maalumu (Special Rapporteur) walipelekwa Rwanda kuhakikisha hili na kuthibitisha yote ndani ya ripoti.
Kila mtoto ambaye anaanza elimu ya msingi nchini Rwanda anatumia Laptop/Ipad kusoma. Binafsi sikuamini lakini nikazungumza na watu wa kwenye kamati wakathibitisha hilo. Nikashangaa tena kusikia kule nchini Rwanda ni marufuku mtoto kupelekwa kwenye shule ya bweni mpaka afikishe miaka 14. Nikasema kama Raisi Paul Kagame ataendelea kufanya hivi, kuna siku tutaiangalia Rwanda kiutofauti sana.
Rwanda iko na madhaifu mengi kiutawala na kimfumo: UKABILA umeshamiri kwenye kila eneo na kama Raisi Kagame atabadilika na kukubali kuelewana na Wahutu bila kuweka masharti (Conditions) zozote zile kwenye amani, basi Rwanda itafika mbali sana. Maana taifa lolote lile ambalo linawekeza kwenye rasilimali watu ndiyo hufanikiwa kufika juu.
Ukweli mchungu ni lazima kukubali kwamba Tanzania tulijisahau sana, na hatupendi kukubali ukweli kwamba wananchi na viongozi wetu akili zetu ziko chini ya kiwango (Below Avarage). Tumewekeza rasilimali zetu nyingi kwenye mambo ambayo siyo sahihi: Tunatumia mabilioni ya pesa kwenye siasa, ulinzi (political surveillance), matumizi yasiyo na msingi na ubadhilifu.
Tangu aondoke Mzee Nyerere madarakani hakujawahi tokea Raisi wa nchi hii ambaye aliweza kutambua nini haswa kinatakiwa kuwa kipaumbele kwa taifa. Mzee Nyerere mbali na madhaifu yake yote, aliwekeza sana kwenye ELIMU ya watu wake. Vijana wa Nyerere japo wengi waliasi falsafa na wengi wao kuwa walafi, ndiyo wameisaidia Tanzania isitumbukie korongoni kwa spidi kubwa. Hivyo tunatumbukia kidogo kidogo (Gradually Disintegrating)...
Mzee Lowassa alivyosema ELIMU, ELIMU, ELIMU hakukosea kabisa. Kuikomboa Tanzania tunahitaji watu wenye uelewa mzuri kuhusu mazingira ya nchi yetu. Nchi hii inategemea kilimo, uvuvi na ufugaji kama shughuli asilia za kiuchumi, lakini tumefanya nini kwenye kuwawezesha wananchi kwenye kilimo, uvuvi na ufugaji ??? Tuna wataalamu wangapi ambao wanaweza kutusaidia ??? Sisi tumekazania siasa na katiba mpya: Ndiyo ni mambo ya muhimu sana, japo sidhani kama kila kitu kinaweza kutatuliwa kisiasa.
Nchi ndogo kama Uingereza na Japan ziliweza kuwa mataifa yenye nguvu sana duniani kwasababu walijua nini madhaifu yao na kufahamu vipaumbele vyao. Ingekuwa leo mtu anaenda Uingereza mwaka 1500 au Japani mwaka 1800 na akaambiwa hizi nchi zitakuja kuwa tajiri sana duniani asingeamini hata kidogo. Lakini nini kilifanya Waingereza na Wajapani wafike pale : Mapinduzi ya kifikra yaliyoletwa na ELIMU. (Meiji Revolution and Industrial Revolution)
Mfalme Meiji wa Japan baada ya kutambua kwamba dunia imebadilika sana na wao ni lazima wabadilike, mwaka 1868 alifanya mapinduzi makubwa sana nchini kwake. Alivunja kabisa mfumo wa Ukabaila (Feudalism) ambao uliwanyima watu wasio tabaka tawala elimu (hasahasa masikini na wanawake). Akaenda mbali zaidi kutafuta waalimu wa vyuo vikuu kutoka Ufaransa, Uingereza na Marekani ili kuja kufundisha sayansi nchini Japan.
Kazi yao asilia waliyokuwa wanaifanya ni kilimo na uvuvi: Mfalme Meiji akawekeza kwenye teknolojia ya kilimo na majini, ndiyo msingi mkubwa ambao ukaifanya Japani kuwa moja kati ya nchi zenye sekta bora kabisa duniani za ujenzi wa meli (Ship Building Industry) na uvuvi (Fishing Industry). Ikumbukwe kipindi chote kabla ya hapa Japani alikuwa anaishi kwa huruma za Uchina (The Ming + Qing Dynasties) ambao ndiyo lilikuwa taifa tajiri zaidi duniani mnamo karne za 18 na 19.
Uchina wao walibweteka wakiamini kabisa kwamba wao ni THE MIDDLE KINGDOM na wana haki kutoka mbinguni ya kuendelea kutawala biashara ya dunia. Uchina lilikuwa ndiyo taifa la kwanza kabisa kufika pwani ya Afrika Mashariki mnamo karne ya 14, miaka 90 kabla Vasco Da Gamma hajafika. Tena walikuja na manowari kubwa na za kisasa ambazo ndiyo zilikuwa bora duniani kote kwa wakati huo.
Walifungua ubalozi wao mjini Kilwa na kuanza kufanya biashara: Lakini bahati mbaya sana walifanya makosa kimaamuzi. Wafalme wa Uchina walianza kuchoma meli na kupiga marufuku safari na tafiti za baharini, huku wakianzisha matabaka ndani ya nchi. Ikumbukwe kipindi chote cha Ming Dynasty Uchina ulikuwa ni ufalme wenye uvumilivu sana wa dini, waislamu na dini zingine walipewa fursa kama watu wengine. Zeng He ambaye alikuwa nahonda towashi aliyefika Pwani ya Afrika Mashariki alikuwa ni Muislamu.
Lakini Uchina wakati yeye amelala na kujifungia (ISOLATIONISM) wenzake wa Ulaya wakawa wanapiga hatua kali sana. Siku waingereza wakaja mipakani mwake na manowari zenye injini ya mvuke (Steam Engine) walimtandika sana mchina na kumtawala kwa miaka mingi. Mfalme Meiji baada ya kuona Uchina kafanywa haya akaamua kuwa mjanja na kuanza kutumia elimu ya mzungu ili kufika mbele. Haikupita hata miaka 50 Ufalme wa Japani ukawafikia mataifa ya Ulaya kwenye teknolojia.
Siku moja mwaka 1904, Urusi akajichanganya akaingia kwenye kumi na nane za Japani akidhani kwamba ni nchi ileile ambayo walikuwa wanaionea miaka 50 nyuma. Russo-Japanese War (1904-1905) iliwaogopesha sana wazungu baada ya kuona teknolojia ya jeshi la Japan hasa ile ya manowari, kuwa bora kuliko nchi nyingi za Ulaya. Tokea pale kufika mwaka 1945 hadi leo hii Japan inaogopeka sana. ELIMU, ELIMU, ELIMU......
Lee Kuan Yew wa Singapore alifahamu hili, na mwaka 1965 alipokuwa akizungumza kwamba Singapore itafika mbali, cha msingi wawekeze kwenye ELIMU watu walicheka. Lakini ona leo hii wako wapi : Tena ikumbukwe Singapore ilikuwa kama Rwanda, kuna mchanganyiko wa watu (Diverse Ethnicities). Asilimia kubwa (70%) ni wachina na hizo zinazofuatioa ni wahindi, malaysia tena waislamu.
Baada ya kufahamu kwamba hawa watu hawampendi na kuna tatizo la ubaguzi Lee Kuan Yew akaamua kutumia ujanja. Akaanza kutumia Wachina na Wayahudi, kumsaidia huku akiwekeza sana kwenye Elimu. Aliita wanajeshi wa Israeli kufundisha jeshi na Idara zao za Kijasusi, alipofahamu kwamba Waislamu wasingependa kila kitendo kwasababu kipindi hicho Mashariki ya Kati kumewaka moto basi akaamua kusema wale ni wanajeshi wa Mexico.
Alisomesha sana watu nje na kujenga vyuo vikuu vikubwa nchini humo: Alifahamu vizuri mazingira yake, na kutambua kwamba Singapore ni nchi ya bahari. Hivyo akawekeza kwenye bandari na biashara. Leo hii kila meli inayoenda Asia lazima ipite The Strait of Malacca kwenye bandari za Singapore na kulipa mamilioni ya fedha. Wasichofahamu watu wengi ni kwamba huyu jamaa ndiye aliyeiokoa Uchina baada ya kumshauri ndugu yake mtu wa kabila moja (The Hakkas) Deng-Xiaoping kuachana na ule upumbavu na UKOMUNISTI wa Mao Zedong.
Alimwambia afungue nchi, asomeshe sana watu nje na aruhusu uwekezaji: Deng baada ya kurudi Uchina akafanya vilevile huku akipeleka mamilioni ya wachina kusoma Marekani na Ulaya. Alimwambia wasomi wako ni bei rahisi (Cheap Labour) hivyo wakiwepo kwa wingi wazungu watawafuata tu nchini UCHINA.
NB 1 : Paul Kagame wengi tunamchukia sana, lakini ni lazima tukubali ukweli kwamba yule mtu ana akili sana. Ushirikiano mzuri alioujenga na mebeberu, pamoja na kufahamu vipaumbele vyake ndiyo vinamsaidia. Tusipokuwa macho atakuja kutushinda huyu mtu, japo wengi hasa wale ambao wako ndani ya CCM, TISS, MIT na TPDF wanakwambia wale wanyarwanda makolo tu (Kagame is Overrated), tunawamudu. Endeleeni kujidanganya mkidhani dunia inawasubiri ninyi na kwamba dunia ya leo kumtawala mtu lazima utumie vifaru...
NB 2: Nachokisema siyo msaafu, hivyo siyo lazima kitokee lakini katika kusoma kwangu na kufuatilia siasa za dunia kwa miaka mingi. Nina ujasiri wa kusema kabisa hadharani kama Rwanda wataendelea hivi, basi huko mbele watakuja kutusumbua hadi sisi watanzania ambao tunajihisi kama ulimwengu mzima unatuzunguka sisi. Leo hii kila kitu lazima kiwe siasa tu. Miradi mikubwa ni siasa, maendeleo ni siasa huku ELIMU na Maadili vikizidi kudorora.
Leo Raisi amepata nchi anaanza kucheza ngoma ile ile ya kufikiri Uchaguzi ujao atapitaje, badala ya kuliweka taifa mbele. Nadhani anakosea sana huyu MAMA, anaamini hela itapatikana. Lakini ukweli ni kwamba watanzania tunahitaji mabadiliko zaidi ya kuwa na pesa mifukoni. Tunataka watoto wetu waende shule, wekeza kwenye kilimo, uvuvi na ufugaji ili watanzania waweze kujiajiri wenyewe na kujikwamua.
Kuna kipindi huwa nawaza sana, naumia toka ndani, napata sana hasira, machozi yananilenga na navunjika moyo kuhusu mustakabali wa nchi yetu. Lakini ndiyo hivyo watanzania wamelala sana, siyo wanazuoni, siyo CHADEMA, siyo CCM. Kila siku ukienda mitandaoni habari ni zilezile MBOWE, FEMINISM, KATIKA MPYA, VUMBI LA MKONGO, DIAMOND PLATNUMZ, SIMBA NA YANGA: Haya ni mambo mazuri hata mimi nayapenda, lakini siyo ya msingi kuweza kugeuzwa mjadala wa kitaifa.
Sijawahi kusikia kule Twitter Space mtu anafanya mjadala au anatoa mkakati kuhusu jinsi gani tutainua kilimo, jinsi gani tutawekeza kwenye elimu, au tufanye maandamano kushinikiza elimu ya bure na usawa kama ambavyo wakina Martin Luther King Jr walifanya. Lakini siasa, siasa, siasa tu.
WACHA RWANDA IPIGE HATUA.....
Happy Nyerere Day to all....