Simulizi: Harakati za Jason Sizya

Simulizi: Harakati za Jason Sizya

fungate.jpeg

154

Wewe ni lulu ya pekee…


Saa 5:00 usiku.

ULIKUWA usiku wa aina yake, usiku ambao nilihisi kama vile niko peponi. Hisia zangu zilikuwa zitendewa vyema kwa faraja kubwa iliyopenya hadi kwenye mishipa ya damu. Nje ya chumba tulichokuwemo mbalamwezi ilikuwa ikiangaza na kuifanya dunia ing’ae kwa nuru safi na adhimu ya mbalamwezi. Chumba chetu kilikuwa na mwanga hafifu uliotoka kwenye taa mbili za rangi ya bluu.

Kilikuwa chumba kizuri cha kifahari, taa mbili za rangi ya bluu zilikuwa zinatoa mwanga hafifu wenye mg’ao na kufanya nusu ya chumba kile kuwa kizani. Ndani ya chumba hicho kulikuwa na kitanda kikubwa cha samadari cha futi sita kwa sita, cha mbao ngumu za mninga na chenye droo mbili kila upande, na juu ya zile droo kulikuwa na zile taa mbili za rangi ya bluu.

Mbele ya kitanda kulikuwa na seti nzuri ya runinga pana ya inchi 52 na chini ya runinga hiyo kulikuwa na meza nzuri nyeusi ya kioo. Upande wa kushoto wa chumba, kwenye kona, kulikuwa na jokofu la vinywaji na hatua chache kutoka kwenye jokofu hilo kulikuwa na dirisha pana la kioo lililofunikwa kwa pazia zito na refu lenye nakshi za mchoro wa hifadhi ya taifa ya Serengeti uliodariziwa vizuri.

Upande mwingine wa chumba kulikuwa na kabati la ukutani la nguo na pembeni ya kabati kulikuwa na makochi mawili ya sofa na meza ndogo ya kioo. Kando ya sofa moja kulikuwa na meza fupi ya mbao iliyokuwa na simu ya mezani na kitabu kikubwa cha njano chenye orodha ya majina ya watu na kampuni zilizotumia huduma ya simu hiyo ya mezani.

Kwenye kona hiyo ya chumba upande wa kulia kulikuwa na mlango wa kuelekea kwenye chumba kidogo cha maliwato na bafu. Ukutani kulikuwa na picha kadhaa kubwa za michoro zilizotundikwa zikiwaonesha wanyama wa porini waliochorwa kwa ustadi wa hali ya juu. Picha zote ziliwekwa ndani ya fremu nzuri za kioo.

Mimi na mwanamke niliyempenda kuliko wanawake wote duniani, Rehema, tulikuwa tumejilaza kitandani. Rehema alikuwa amekilaza kichwa chake kifuani kwangu. Mguu wake mmoja ulikuwa katikati ya mapaja yangu huku mkono wake mmoja akiwa ameuzungusha shingoni kwangu na alikuwa anahema taratibu kwa sauti hafifu ya uchovu. Alikuwa ametulia mikononi mwangu na mimi nilikuwa nimemkumbatia kwa mahaba mazito.

Nilifumba macho yangu nikamshukuru Mungu kwa mara nyingine tena kwa zawadi hii aliyoniletea ya mwanamke mzuri pengine kupita wote duniani. Moyoni nilikuwa namsifu muumba kwa jinsi alivyolifinyanga umbo la Rehema kwa ufundi wa hali ya juu. Nilijihisi kama siko tena katika dunia hii iliyojaa kero na karaha za kila aina bali niko katika ulimwengu mwingine kabisa, ulimwengu wenye utulivu na mahaba mazito, ulimwengu usiokuwa na kero wala husuda za wanadamu.

Nilikuwa na kila sababu ya kufurahia kuwa na Rehema kwa sababu niliamini sasa ulikuwa wakati mwafaka wa kuwa na familia kwani umri nao ulikuwa unakwenda, aina ya maisha ya ubachela niliyokuwa nayaishi hayakupaswa kuwa sehemu ya maisha yangu tena. Mimi mwenyewe nilikwisha choshwa na maisha hayo.

Baada ya mateso makubwa niliyokuwa nimeyapata wakati Rehema alipopatwa na ugonjwa wa kiharusi kisha akaibuka mwanadada Olivia akijifanya mwekezaji na kisha nikaungana tena na Rehema kabla hatujawekeana ahadi ya kuwa pamoja katika shida na raha, sasa niliamini nimepata kitulizo cha moyo wangu. Rehema alikuwa kila kitu kwangu. Nilimpenda kuliko maelezo.

Mkono wangu mmoja ulikuwa unaichezea shingo laini ya Rehema. Ngozi ya mwanamke huyo ilikuwa laini kama sufu, nikapatwa na hisia kwamba huenda sikuwa nikiigusa ngozi ya binadamu wa kawaida. Nilihisi kuwa pengine nilikuwa naigusa ngozi ya malaika kwa jinsi ilivyokuwa laini na ya kung’aa hata katika mwangaza huu hafifu uliokuwemo chumbani kwetu.

Ilikuwa ni siku ya Jumapili, siku ya kwanza kabisa ya fungate ndani ya hoteli maarufu ya Singita Grumeti Reserves iliyopo kwenye hifadhi ya taifa ya Serengeti baada ya harusi yetu iliyoacha gumzo katika Mji wa Kahama, tukipeana ahadi mahususi ya kulizatiti pendo thabiti litakalovumilia raha na shida zote za ulimwengu kama chuma cha pua. Tukikubaliana kujenga pendo ambalo tungehakikisha halipwayi wala kupauka na kutiliana sahihi hati za mkataba wa milele usioweza kuvunjwa kwa kupwa na kujaa kwa bahari.

Kama ambavyo wazee wa zamani walisema; “Kawia ufike”, nami nilikuwa nimepigania kummiliki mrembo maridadi mwenye kila aina ya sifa ya uzuri, nikamtia mikononi mwangu na sasa tulitaraji kuishi maisha ya mume na mke.

Wazo la kwenda Serengeti lilikuja kama utani siku tatu tu kabla ya harusi yetu, mwanzoni tulikuwa tumepanga kwenda visiwa vya Mauritius kabla Rehema hajaja na wazo jingine.

“Hivi kwa nini tusitafakari upya wapi twende fungate?” Rehema alitoa wazo wakati tukiandikiana ujumbe kwa njia ya WhatsApp.

“Samahani mpenzi, wewe unafikiri twende wapi kwa ajili ya fungate yetu?” nilimuuliza nikaona ameweka ‘emoji’ za kushangaa kisha aliandika; “Unanirudishia swali, Jason!”

“Basi kama hupapendi Mauritius unaonaje twende Johannesburg, London, Paris au New York… sema wapi? Popote upendapo dear tutakwenda na hii ni zawadi ya pendo langu kwako…” nilimwandikia Rehema.

“Tuna haja gani ya kwenda nchi ya ugeni?” Rehema aliniandikia kisha akaendelea, “Kwa nini tusiende kwenye hifadhi ya taifa ya Serengeti na ikiwezekana tufike hadi bonde la Ngorongoro?”

“Wazo zuri sana, mpenzi…” nilimjibu Rehema. “Tutapata nafasi ya kuona wanyama na kupumzika vile vile. Leo leo nafanya mpango ili baada tu ya harusi yetu twende huko, wiki mbili zitatosha…”

Hivyo ndivyo tulivyojikuta tupo ndani ya Singita Grumeti Reserves katika hifadhi ya taifa ya Serengeti, hoteli ambayo sifa zake kwa nyakati tofauti ziliwavuta watu mashuhuri duniani wakiwemo marais wa Marekani wa 42 Bill Clinton na wa 43 na George W. Bush, kufikia kwenye hoteli hiyo.

Tulipanga kukaa Singita Grumeti Reserves kwa wiki mbili na kutembelea vivutio mbalimbali katika hifadhi ya taifa ya Serengeti kujionea idadi kubwa ya wanyamapori na uhamisho wa kila mwaka wa zaidi ya milioni moja ya nyumbu wanaovuka mto Mara na baadaye twende bonde la Ngorongoro.

Kwa dakika kadhaa macho yangu yalikuwa wazi kabisa yakikodolea dari ya chumba hicho tulichokuwemo. Kisha niliuvunja ukimya wa muda.

“Rehema Benard Mpogoro!” nililiita jina lake kwa ukamilifu kwa sauti tulivu na kumfanya Rehema ainue kichwa chake na kunitazama kwa udadisi.

“Abee!” Rehema aliitika huku akinitazama machoni kwa udadisi.

You are my wife now… u mke wangu sasa,” nilimwambia kwa Kiingereza na kisha kurudia kwa Kiswahili.

Rehema alicheka kidogo na kusema kwa sauti yake laini sana iliyoyafanya maungo yangu yasisimke, “Ndiyo, na wewe ni mume wangu sasa.”

“Kabisa! Am totally yours,” nilisema huku nikizishika shika nywele zake.

“Jason Sizya!” Rehema naye aliniita jina langu kwa ukamilifu huku akiendelea kunitazama usoni.

“Unasemaje malkia wangu?” nilisema huku nikimtazama machoni.

Do you really love me, Jason? Unanipenda kweli? Nataka kuondoa shaka iliyo moyoni mwangu,” Rehema aliniuliza maswali mfululizo huku akiendelea kunitazama machoni.

Maswali yake yaliufanya moyo wangu upige kite kwa nguvu. Nilimtazama kwa nukta kadhaa kisha nikashusha pumzi ndefu na kuminya midomo yangu.

“Shaka gani, Rehema?” nilimuuliza kwa sauti tulivu huku nikihisi hali fulani ya woga ikinitambaa mwilini kwangu. Ni kama aliyekuwa akiyasoma mawazo yangu, Rehema aliachia tabasamu.

“Unafahamu ninakupenda kiasi gani?” badala ya kujibu swali langu aliniuliza swali jingine huku akiwa bado amenikazia macho.

Nikatabasamu kidogo na kushusha pumzi za ahueni.

“Rehema, malkia wangu, nafahamu kwamba unanipenda sana, sioni kitu cha kulinganisha na upendo wako kwangu. Ni upendo ambao hauwezi kupimwa wala kulinganishwa na kitu chochote kile,” nilisema kwa sauti ya chini ya mahaba.

“Nashukuru kama unalifahamu hilo. Napenda kuongezea kwamba nakupenda kupita hata ninavyojipenda mimi mwenyewe. Nameamua kukabidhi moyo na mwili wangu uvilinde na kuvichunga kama unavyojipenda wewe mwenyewe. Wewe ndiyo kila kitu kwangu,” Rehema alisema kwa hisia kubwa.

Nikamkumbatia kwa nguvu zaidi na kumbusu katika paji la uso wake.

“Wewe ni lulu ya pekee na ya thamani kubwa katika maisha yangu. Nakosa hata neno la kukwambia ni namna gani nakupenda zaidi ya unavyoweza kufikiri. Naahidi kuwa siku zote nitakulinda, kukuheshimu na kukuthamini…” nilimwambia Rehema huku nikimtazama usoni, nikayaona machozi ya furaha yakimtoka na kukilowesha kifua changu.

* * *

Endelea kufuatilia...
 
fungate.jpeg

155

Simba dume…


Saa 4:15 asubuhi.

MVUA kubwa ilikuwa inanyesha katika barabara ya kutoka Arusha kwenda Babati, barabara hiyo ilikuwa ikikatisha katika eneo kubwa lenye misitu. Mvua hiyo ilinifanya wakati fulani nipunguze mwendo na kuongeza katika nyakati tofauti ili kujihami na ajali.

Hata hivyo mwendo wangu bado ulikuwa wa kasi mno lakini makini kweli kweli ila ulikuwa wa uhakika huku nikishuka mabonde na kupanda milima katika baadhi ya maeneo na kukatisha kwenye sehemu zenye misitu mizito iliyojitenga mbali na makazi ya watu.

Kuna wakati barabara ile ilikatisha katika vijiji vyenye nyumba duni za udongo, hata hivyo hatukusimama. Wakati wote tukiendelea na safari Rehema alikuwa kimya. Kila nilipokuwa nikiona kuwa ukimya ulikuwa ukizidi kushika hatamu mle ndani ya gari nilimchangamsha kwa maneno ya utani.

Nilimwambia nilitarajia watoto mapacha na nilikuwa mbioni kwenda kununua vitu na nguo za kisasa kwa ajili ya watoto hao ambao angewazaa pindi tu tukifika Kahama. Yeye alikuwa akitabasamu tu pasipo kusema chochote. Ajabu sana, sikujua kwa nini siku hiyo alikuwa mkimya sana jambo lililoanza kunishangaza.

Tukiwa tunarudi Kahama ili kuyaanza maisha rasmi ya ndoa, kutwa nzima ya siku ile, mimi na Rehema hatukuacha kutazamana kwa namna tofauti, mimi nilimtazama kwa namna ya mahaba na yeye alinitazama kwa namna ambayo sikuweza kupata tafsiri kabisa. Alionekana kama mtu mwenye wasiwasi hivi.

Nilikuwa namkumbatia kila baada ya dakika mbili ili kumfanya awe na furaha huku nikimweleza furaha yangu pindi akinizalia watoto lakini yeye aliishia kutabasamu au kuguna tu.

Tulikuwa ndani ya gari letu la kifahari aina ya Toyota Lexus RX Hybrid la rangi maruni tulilozawadiwa na baba mkwe siku ya harusi na tulikuwa tunatoka kwenye fungate yetu Serengeti na Ngorongoro na baadaye tukaenda kupumzika Jijini Arusha kwa siku mbili.

Hapo Arusha tulifikia katika hoteli ya kisasa ya Arusha Crown Hotel iliyopo barabara ya Makongoro jirani kabisa na Uwanja wa Mpira wa Sheikh Amri Abeid Kaluta. Tulikuwa tumekubaliana kuwa tukae hapo Arusha kwa siku mbili tu kisha siku zilizobaki za fungate yetu twende tukazimalizie Dodoma kwa mjomba, Mchungaji Edwin Ngelela, ndipo turejee Kahama.

Kwa siku tatu tulizokuwa kwenye hifadhi ya taifa ya Serengeti tulibahatika kutembelea vivutio mbalimbali na kujionea idadi kubwa ya wanyamapori ingawa hatukubahatika kushuhudia uhamisho wa kila mwaka wa zaidi ya milioni moja ya nyumbu wanaovuka Mto Grumeti na kisha Mto Mara na kuingia nchini Kenya, kwa sababu tuliambiwa kuwa tukio hilo hufanyika mwezi Juni.

Siku ya kwanza tu tukiwa ndani ya gari letu huku tukiongozwa na mwongoza watalii tulibahatika kuliona kundi la simba. Simba hao walikuwa majike wakiwa na watoto wao. Ngozi zao zilikuwa za rangi ya kahawia-njano na kwa mwonekano wa macho tu ungeweza kugundua kuwa zilikuwa laini, zenye kung’aa, zikipatana kwa umaridadi na nyasi ndefu zilizokauka.

Watoto wa simba walionekana machachari sana na wenye nguvu nyingi. Walikuwa wanaruka na kucheza wakiizunguka miili mikubwa ya simba majike, wasiojali vitendo vyao vya kuchekesha. Mara kundi hilo la simba lilitulia. Macho yao yakageuzwa kutazama sehemu fulani mbali.

Kutoka mahali tulipokuwa, kwenye mwinuko kidogo, sisi pia tulifuatilia mwelekeo wa macho ya simba hao, na mara moja tukagundua kile ambacho macho ya simba hao yalilenga.

Umbo lenye fahari la simba-dume mkubwa likajifichua na alikuwa anatusogelea. Macho yetu na ya yule simba dume yakakutana, akatukazia macho. Na hapo nikamwona Rehema akianza kutetemeka, si kutokana na ubaridi uliosababishwa na upepo wa mvua, bali kwa kutambua kuwa sisi ndio alitutazama na sikujua alituwazia nini. Nikamtoa hofu.

Yule mwongoza watalii alitwambia kuwa simba dume huyo alikuwa na uzito wa zaidi ya kilogramu 225. Na kwa jinsi alivyokuwa, alionekana mwenye kutia hofu, na maridadi vilevile.

Alikuwa na manyoya mengi mno ya rangi ya dhahabu yenye mistari myeusi yaliyokifanya kichwa chake kuonekana kikubwa kwa umbo. Macho yake yalikuwa makubwa yenye rangi ya kaharabu (mchanganyiko wa rangi ya njano na nyekundu) na yalikuwa makini sana.

Yule mwongoza watalii alitwambia kuwa, kati ya wanyama wote wa jamii ya paka, simba ndiyo mrefu (mabegani) na wa pili kwa uzito baada ya chui milia (tiger). Fuvu la kichwa la simba linafanana sana na lile la chui milia na kwamba tofauti ya taya zao za chini ndiyo pekee hutumika kuwatofautisha.

Tuliendelea kutazamana na yule simba dume na baada ya kitambo kifupi cha kutukazia macho, kundi lile la simba majike na watoto likavuta umakini wa yule simba dume, hivyo akawageuzia macho yake taratibu na kuwaendea. Nikamwona Rehema akishusha pumzi za ahueni.

Wakati yule simba dume alipokuwa akitembea, hatua zake zilikuwa za madaha na za kifalme. Na bila ya kututupia jicho mara ya pili, alipita karibu sana mbele ya gari letu na kuwaendea wale majike na watoto wao. Wote wakainuka ili kumlaki, mmoja baada ya mwingine, wakasukumiza nyuso zao dhidi ya domo lake kakamavu kwa kufuata mtindo wa jamii ya paka wa kuamkiana kwa kusuguana mashavu.

Yule simba dume akaingia katikati ya kundi, akajibwaga chini kana kwamba amechoka kwa kutembea, akajibingirisha kwa mgongo. Wale simba wengine wakauiga uchovu wake, na punde si punde kundi lote likalala usingizi wa kijuujuu.

Mbele ya macho yetu na watalii wengine tukaiona picha ya amani na uradhi iliyofanyizwa katikati ya nyasi za rangi ya dhahabu, zenye kupulizwa na upepo katika tambarare ile ya Serengeti iliyo wazi.

Yule mwongoza watalii akatwambia kuwa simba ni wanyama wa jamii ya paka wanaopenda kuishi kijamii zaidi. Hupenda kuwa katika makundi ya kifamilia, ambayo yaweza kuwa na idadi ya kuanzia washiriki wachache tu hadi kufikia zaidi ya 30.

Kundi la simba hufanyizwa na kikundi cha simba-majike ambao huenda wakawa wa jamaa za karibu. Wao huishi, huwinda, na kuzaa pamoja. Uhusiano huu wa karibu, ambao huenda ukadumu maisha yao yote, huandaa msingi wa familia ya simba na huisaidia isiangamie. Kila kundi la simba lina dume mmoja au zaidi waliokomaa na ambao hushika doria na kuweka alama ya mipaka ya eneo la kundi hilo la simba.

Kutoka kwenye ncha ya pua zao nyeusi hadi sehemu ya mwisho ya mikia yao yenye manyoya, wanyama hawa wenye fahari wanaweza kufikia urefu wa zaidi ya mita tatu, na uzito wa zaidi ya kilogramu 225. Kwa miguu yake yenye nguvu, taya imara, na meno yake chonge yenye urefu wa sentimita 8, simba anaweza akamwangusha na kumuua mnyama mkubwa.

Ingawa madume ndio hutawala kundi lakini ni majike ndio huongoza. Kwa kawaida simba-majike ndio huanzisha utendaji kama kwenda kwenye kivuli au kuanza kuwinda.

Baada ya kujionea maajabu ya simba tuliendelea na safari yetu ya kutazama wanyama wengine, na katika safari hiyo tuliliona kundi la tembo. Walikuwa na maumbo makubwa kupita wanyama wengine na walikuwa wanatembea kwa makundi. Tuliwaona wakila magome ya miti, majani na nyasi.

Mwongoza watalii alitwambia kwamba tembo wana uzito wa tani 6.6 kwa madume na tani 3.3 kwa majike na huishi miaka 60 hadi 70, na alituonesha tofauti ya tembo dume na tembo jike. Tembo dume wana miili mikubwa iliyojengeka na mapaji ya uso ni ya mviringo lakini tembo majike wana mapaji ya uso yaliyochongoka.

Endelea kufuatilia...
 
fungate.jpeg

156

Baada ya hapo tukawaona pundamilia, ni wanyama wanaofanana sana na farasi au punda wafugwao lakini wenyewe wana rangi ya pekee ya michirizi myeupe na myeusi. Michirizi yao ina mpangilio tofauti kwa kila pundamilia mmoja. Pia wana nywele shingoni kama farasi. Mwongoza watalii alitwambia kuwa pundamilia ni wanyama wenye kuchangamana sana na huonekana mara nyingi kwenye makundi.

Kisha tuliwaona nyani wakiambatana na swala na mwongoza watalii alitwambia kuwa nyani na swala hupenda kutembea pamoja hususan kwenye maeneo yenye miti na vichaka. Hii ina manufaa kwa wote; nyani na swala.

Alisema kuwa nyani anapokuwa juu ya mti anakuwa na uwezo wa kuona mbali na kutoa ishara kwa wengine kama hali ya usalama inaelekea kwenye dosari katika eneo walilopo. Hii inawasaidia swala nao kuweza kuiona hatari ikiwa mbali kabla haijawafikia.

Mwongoza watalii alisema kuwa si hivyo tu, kwani pia palipo na miti mingi nyani na ngedere hutupa chini maganda ya matunda wanayokula juu mtini, hii nayo huwa ni lishe kwa swala walio chini ambao kwa mazingira ya kawaida wasingeweza kuyafuata matunda au maganda hayo juu mtini.

Halafu tuliwaona twiga, wanyama warefu wanaotembea kwa maringo, miguu yao mirefu sana na shingo zao pia ni ndefu sana, hata walipotembea walionekana kana kwamba walikuwa wakitembea pole pole. Muda huo mvua hafifu ilianza kunyesha, na hapo tukaliona kundi lingine la simba waliokuwa katika himaya yao wakipanda juu ya matawi ya miti ili kukwepa majimaji ya mvua iliyokuwa ikinyesha na kutotesha ardhi yenye udongo wa mfinyanzi.

Wanyama wengine wengi walikuwa wanakimbilia katika eneo la miombo ambako ungeweza kuwaona kutoka eneo la safu za milima. Mwongozaji alitwambia kuwa ni kutoka katika safu ya milima ungeweza kuyaona makundi makubwa ya nyati katika uwanda huo wa miombo.

Wakati mvua ikiendelea kunyesha idadi ya ndege ilizidi kuongezeka, yule mwongoza watalii alitwambia kuwa wakati wa mvua idadi ya ndege hufikia zaidi ya aina 300. Hii ilitokana na ukweli kwamba nyakati hizo kunakuwepo makundi ya ndege wahamiaji kutoka nchi za Ulaya na Asia ambayo huungana na makundi ya ndege wakazi kama vile chole.

Vile vile katika eneo hilo tuliweza kuona makundi makubwa ya pundamilia na nyumbu.

Baada ya kunyesha kwa dakika ishirini mvua ilianuka na kuliachia jua lenye kupunga la mchana likijitokeza tena kwenye mawingu mepesi na kuifanya miale yake kumemetesha majani yaliyolowa.

Baada ya siku tatu tulienda kutalii kwenye bonde la Ngorongoro, bonde maarufu sana duniani lenye urefu wa kilometa 20, kina cha mita 600 na ukubwa wa kilometa za mraba 300 na lina viashiria vyote vya bustani ya Eden kama ilivyoandikwa kwenye maandiko matakatifu kutokana na maajabu yaliyomo pamoja na historia ya binadamu wa mwanzo kuishi mule.

Ndani ya bonde hilo tuliona jinsi Wamaasai wanavyoishi pamoja na mifugo yao kwa amani na utulivu kabisa bila ya kuwabugudhi wanyamapori, ni kama masimulizi ya bustani ya Eden aliyoishi Adam na wanyama bila bughudha.

Tuliona alama za kale za miguu zilizovumbuliwa na Dk. Mary Leaky zikiwa zimehifadhiwa katika majivu ya volkano, wanasayansi wakiamini kwamba majivu hayo yanatokana na mlipuko wa volkano ya sadiman yenye urefu wa kilomita 20.

Kwa mujibu wa watafiti, mburuzo huo ni ushahidi usio kifani wa binadamu wa kale kutembea kwa miguu miwili zaidi ya miaka milioni 3.6 iliyopita.

Pia tulitembelea vivutio vingine kama Ziwa Ndutu na Masek; maziwa ambayo hayana kina kirefu lakini maji yake yana chumvi. Tuliambiwa kuwa Ziwa Ndutu hutumiwa zaidi na wanyama kama sehemu ya kunywa maji na kupumzika baada ya wanyama kuhama, na pia ni sehemu nzuri zenye wanyama kama kiboko na mamba, na tulitakiwa kutumia fursa hiyo kama sehemu ya kuwaona wanyama.

Kisha tulitembelea kwenye mlima pekee wenye volkeno hai, Oldonyo Lengai ambao unapatikana nje kidogo ya hifadhi ya Ngorongoro. Baada ya hapo tukashuhudia mchanga unaohama na unaosifika kwa kuwa na umbo kama la mwezi, ambapo safu ya mchanga huo ulitokana na majivu ya mlima wa Oldonyo Lengai.

Hapo tulijionea jinsi ambavyo umekuwa ukisukumwa taratibu kuelekea upande wa Magharibi wa hifadhi kwa kiwango cha mita 17 hadi 20 kwa mwaka. Mchanga huo una kimo cha mita 9 na mzingo wenye urefu wa mita 100, na unapatikana kaskazini mwa bonde la Olduvai.

Ndani ya Ngorongoro pia kuna bonde la Olkarien ambalo hutoa hifadhi kwa ndege tai aina ya Ruppell Griffon. Tuliambiwa kuwa tulifika kwa wakati kwani msimu mzuri wa kutembelea eneo hili ni miezi ya Machi mpaka Aprili ambapo tai huzaliana. Wanyama huja eneo hilo pale panapokuwa na malisho ya kutosha.

Kiukweli tuliifurahia sana fungate yetu na tulipanga kurudi tena Serengeti na Ngorongoro kwa safari maalumu ya kitalii.

Sasa tukiwa safarini, hadi tunafika katika Mji wa Babati saa yangu ya mkononi ilinionesha kuwa nilikuwa nimeendesha gari kwa muda wa saa mbili na robo tangu tulipoanza safari ya kutoka Arusha.

Muda mwingi macho yangu nilikuwa nimeyakaza barabarani lakini mawazo yangu yote yalikuwa kwa Rehema, mrembo wa shani anayeweza kumsahaulisha mwanamume yeyote machungu yote ya dunia. Rehema alikuwa ameketi kwa utulivu pembeni yangu. Kwangu, Rehema alikuwa ua waridi machoni mwangu, miski puani mwangu na pepo masikioni mwangu.

Kutoka Babati safari iliendelea tukipita barabara iliyopita vijiji vya Bonga, Bukulu na hatimaye Kolo (kwenye michoro ya Kondoa) na baadaye tukaingia katika Mji wa Kondoa kabla ya kuanza kuitafuta Wilaya Chemba. Bado mwendo wangu haukuwa wa kubahatisha.

Saa tisa na nusu alasiri gari letu lilikuwa likipita eneo la Makutupora, tulikuwa karibu kuzimaliza kilomita 442 za barabara kutoka Arusha kwenda Dodoma kwa kupitia Babati, na hapo nikakumbuka jambo nikachukua simu yangu na kumpigia simu mke wa mjomba, Mama Mchungaji, ili kumjulisha kuwa tulikuwa tumefika Makutupora, alitakiwa atuelekeze tuelekee upande upi baada ya kufika Dodoma Mjini kwa kuwa walisha hama kule walikokuwa wakikaa mwanzo.

Wakati naongea na simu Rehema alionekana kuwa na hamu ya kumsikia mke wa mjomba, na hivyo alijiegemeza kwenye bega langu kwa mahaba huku akisikiliza kwa makini maongezi yetu. Nilitabasamu na kumwambia Mama Mchungaji kuwa mkwe wake alitaka kuongea naye, kisha niliiweka simu kwenye sikio la Rehema huku nikimtazama kwa tabasamu.

Wakati nilipokuwa nafanya hivyo nilikosa umakini wa kuliona lori kubwa lenye tangi la dizeli lililokuwa likija kwa kasi mbele yetu wakati likilipita basi dogo aina ya Coaster, na wakati nayarudisha macho yangu tu barabarani nililishtukia lile lori tayari likiwa usoni.

Nikajitahidi kukanyaga breki kwa nguvu huku nikiung’ang’ania usukani barabara na wakati huo huo nikijaribu kupinda kushoto ili niweze kuepuka mgongano na hatari ambayo ingetokea, lakini wapi! Sauti kubwa ya mchuniko wa magurudumu ya gari yaliyokuwa yakisota juu ya lami ilisikika na sikuwa na shaka kwamba sauti hiyo ilimtia hofu na wasiwasi mkubwa kila aliyekuwepo eneo lile.

Ilikuwa kazi bure! Lile lori lenye tangi la dizeli lilitupamia, likatuchota na kututupa kando kabisa ya barabara hatua kadhaa. Nilijikuta nikitupwa nje ya gari na hapo, kwa mbali, niliisikia sauti ya Rehema akipiga yowe, huenda lilikuwa la hofu au maumivu, na wakati huo huo nilizisikia sauti za watu wengine wakipiga kelele nyingi za hofu. Niliponyanyua kichwa changu nikawaona wakikimbilia kuja eneo hilo.

Mara nikahisi kama vile akili yangu ilikuwa inabadilika na kisha ikaanza kuhama huku ikishindwa kufanya kazi sawa sawa. Na kuanzia hapo sikujua tena kilichokuwa kinaendelea…

Huu ni mwisho wa Msimu wa Tatu kwenye mfululizo wa mkasa wa Harakati za Jason Sizya. Usikose Msimu wa Nne katika mkasa uitwao “Mgeni Mwema”.
 
View attachment 2252867
156

Baada ya hapo tukawaona pundamilia, ni wanyama wanaofanana sana na farasi au punda wafugwao lakini wenyewe wana rangi ya pekee ya michirizi myeupe na myeusi. Michirizi yao ina mpangilio tofauti kwa kila pundamilia mmoja. Pia wana nywele shingoni kama farasi. Mwongoza watalii alitwambia kuwa pundamilia ni wanyama wenye kuchangamana sana na huonekana mara nyingi kwenye makundi.

Kisha tuliwaona nyani wakiambatana na swala na mwongoza watalii alitwambia kuwa nyani na swala hupenda kutembea pamoja hususan kwenye maeneo yenye miti na vichaka. Hii ina manufaa kwa wote; nyani na swala.

Alisema kuwa nyani anapokuwa juu ya mti anakuwa na uwezo wa kuona mbali na kutoa ishara kwa wengine kama hali ya usalama inaelekea kwenye dosari katika eneo walilopo. Hii inawasaidia swala nao kuweza kuiona hatari ikiwa mbali kabla haijawafikia.

Mwongoza watalii alisema kuwa si hivyo tu, kwani pia palipo na miti mingi nyani na ngedere hutupa chini maganda ya matunda wanayokula juu mtini, hii nayo huwa ni lishe kwa swala walio chini ambao kwa mazingira ya kawaida wasingeweza kuyafuata matunda au maganda hayo juu mtini.

Halafu tuliwaona twiga, wanyama warefu wanaotembea kwa maringo, miguu yao mirefu sana na shingo zao pia ni ndefu sana, hata walipotembea walionekana kana kwamba walikuwa wakitembea pole pole. Muda huo mvua hafifu ilianza kunyesha, na hapo tukaliona kundi lingine la simba waliokuwa katika himaya yao wakipanda juu ya matawi ya miti ili kukwepa majimaji ya mvua iliyokuwa ikinyesha na kutotesha ardhi yenye udongo wa mfinyanzi.

Wanyama wengine wengi walikuwa wanakimbilia katika eneo la miombo ambako ungeweza kuwaona kutoka eneo la safu za milima. Mwongozaji alitwambia kuwa ni kutoka katika safu ya milima ungeweza kuyaona makundi makubwa ya nyati katika uwanda huo wa miombo.

Wakati mvua ikiendelea kunyesha idadi ya ndege ilizidi kuongezeka, yule mwongoza watalii alitwambia kuwa wakati wa mvua idadi ya ndege hufikia zaidi ya aina 300. Hii ilitokana na ukweli kwamba nyakati hizo kunakuwepo makundi ya ndege wahamiaji kutoka nchi za Ulaya na Asia ambayo huungana na makundi ya ndege wakazi kama vile chole.

Vile vile katika eneo hilo tuliweza kuona makundi makubwa ya pundamilia na nyumbu.

Baada ya kunyesha kwa dakika ishirini mvua ilianuka na kuliachia jua lenye kupunga la mchana likijitokeza tena kwenye mawingu mepesi na kuifanya miale yake kumemetesha majani yaliyolowa.

Baada ya siku tatu tulienda kutalii kwenye bonde la Ngorongoro, bonde maarufu sana duniani lenye urefu wa kilometa 20, kina cha mita 600 na ukubwa wa kilometa za mraba 300 na lina viashiria vyote vya bustani ya Eden kama ilivyoandikwa kwenye maandiko matakatifu kutokana na maajabu yaliyomo pamoja na historia ya binadamu wa mwanzo kuishi mule.

Ndani ya bonde hilo tuliona jinsi Wamaasai wanavyoishi pamoja na mifugo yao kwa amani na utulivu kabisa bila ya kuwabugudhi wanyamapori, ni kama masimulizi ya bustani ya Eden aliyoishi Adam na wanyama bila bughudha.

Tuliona alama za kale za miguu zilizovumbuliwa na Dk. Mary Leaky zikiwa zimehifadhiwa katika majivu ya volkano, wanasayansi wakiamini kwamba majivu hayo yanatokana na mlipuko wa volkano ya sadiman yenye urefu wa kilomita 20.

Kwa mujibu wa watafiti, mburuzo huo ni ushahidi usio kifani wa binadamu wa kale kutembea kwa miguu miwili zaidi ya miaka milioni 3.6 iliyopita.

Pia tulitembelea vivutio vingine kama Ziwa Ndutu na Masek; maziwa ambayo hayana kina kirefu lakini maji yake yana chumvi. Tuliambiwa kuwa Ziwa Ndutu hutumiwa zaidi na wanyama kama sehemu ya kunywa maji na kupumzika baada ya wanyama kuhama, na pia ni sehemu nzuri zenye wanyama kama kiboko na mamba, na tulitakiwa kutumia fursa hiyo kama sehemu ya kuwaona wanyama.

Kisha tulitembelea kwenye mlima pekee wenye volkeno hai, Oldonyo Lengai ambao unapatikana nje kidogo ya hifadhi ya Ngorongoro. Baada ya hapo tukashuhudia mchanga unaohama na unaosifika kwa kuwa na umbo kama la mwezi, ambapo safu ya mchanga huo ulitokana na majivu ya mlima wa Oldonyo Lengai.

Hapo tulijionea jinsi ambavyo umekuwa ukisukumwa taratibu kuelekea upande wa Magharibi wa hifadhi kwa kiwango cha mita 17 hadi 20 kwa mwaka. Mchanga huo una kimo cha mita 9 na mzingo wenye urefu wa mita 100, na unapatikana kaskazini mwa bonde la Olduvai.

Ndani ya Ngorongoro pia kuna bonde la Olkarien ambalo hutoa hifadhi kwa ndege tai aina ya Ruppell Griffon. Tuliambiwa kuwa tulifika kwa wakati kwani msimu mzuri wa kutembelea eneo hili ni miezi ya Machi mpaka Aprili ambapo tai huzaliana. Wanyama huja eneo hilo pale panapokuwa na malisho ya kutosha.

Kiukweli tuliifurahia sana fungate yetu na tulipanga kurudi tena Serengeti na Ngorongoro kwa safari maalumu ya kitalii.

Sasa tukiwa safarini, hadi tunafika katika Mji wa Babati saa yangu ya mkononi ilinionesha kuwa nilikuwa nimeendesha gari kwa muda wa saa mbili na robo tangu tulipoanza safari ya kutoka Arusha.

Muda mwingi macho yangu nilikuwa nimeyakaza barabarani lakini mawazo yangu yote yalikuwa kwa Rehema, mrembo wa shani anayeweza kumsahaulisha mwanamume yeyote machungu yote ya dunia. Rehema alikuwa ameketi kwa utulivu pembeni yangu. Kwangu, Rehema alikuwa ua waridi machoni mwangu, miski puani mwangu na pepo masikioni mwangu.

Kutoka Babati safari iliendelea tukipita barabara iliyopita vijiji vya Bonga, Bukulu na hatimaye Kolo (kwenye michoro ya Kondoa) na baadaye tukaingia katika Mji wa Kondoa kabla ya kuanza kuitafuta Wilaya Chemba. Bado mwendo wangu haukuwa wa kubahatisha.

Saa tisa na nusu alasiri gari letu lilikuwa likipita eneo la Makutupora, tulikuwa karibu kuzimaliza kilomita 442 za barabara kutoka Arusha kwenda Dodoma kwa kupitia Babati, na hapo nikakumbuka jambo nikachukua simu yangu na kumpigia simu mke wa mjomba, Mama Mchungaji, ili kumjulisha kuwa tulikuwa tumefika Makutupora, alitakiwa atuelekeze tuelekee upande upi baada ya kufika Dodoma Mjini kwa kuwa walisha hama kule walikokuwa wakikaa mwanzo.

Wakati naongea na simu Rehema alionekana kuwa na hamu ya kumsikia mke wa mjomba, na hivyo alijiegemeza kwenye bega langu kwa mahaba huku akisikiliza kwa makini maongezi yetu. Nilitabasamu na kumwambia Mama Mchungaji kuwa mkwe wake alitaka kuongea naye, kisha niliiweka simu kwenye sikio la Rehema huku nikimtazama kwa tabasamu.

Wakati nilipokuwa nafanya hivyo nilikosa umakini wa kuliona lori kubwa lenye tangi la dizeli lililokuwa likija kwa kasi mbele yetu wakati likilipita basi dogo aina ya Coaster, na wakati nayarudisha macho yangu tu barabarani nililishtukia lile lori tayari likiwa usoni.

Nikajitahidi kukanyaga breki kwa nguvu huku nikiung’ang’ania usukani barabara na wakati huo huo nikijaribu kupinda kushoto ili niweze kuepuka mgongano na hatari ambayo ingetokea, lakini wapi! Sauti kubwa ya mchuniko wa magurudumu ya gari yaliyokuwa yakisota juu ya lami ilisikika na sikuwa na shaka kwamba sauti hiyo ilimtia hofu na wasiwasi mkubwa kila aliyekuwepo eneo lile.

Ilikuwa kazi bure! Lile lori lenye tangi la dizeli lilitupamia, likatuchota na kututupa kando kabisa ya barabara hatua kadhaa. Nilijikuta nikitupwa nje ya gari na hapo, kwa mbali, niliisikia sauti ya Rehema akipiga yowe, huenda lilikuwa la hofu au maumivu, na wakati huo huo nilizisikia sauti za watu wengine wakipiga kelele nyingi za hofu. Niliponyanyua kichwa changu nikawaona wakikimbilia kuja eneo hilo.

Mara nikahisi kama vile akili yangu ilikuwa inabadilika na kisha ikaanza kuhama huku ikishindwa kufanya kazi sawa sawa. Na kuanzia hapo sikujua tena kilichokuwa kinaendelea…

Huu ni mwisho wa Msimu wa Tatu kwenye mfululizo wa mkasa wa Harakati za Jason Sizya. Usikose Msimu wa Nne katika mkasa uitwao “Mgeni Mwema”.
Ahsante sana Bishop!
Naziona harakati za Jason.......anataka kumrudisha rehema kitandani tena
 
Asante sana Bishop, JS kila anapotaka kutulia mambo yanamchachia. Sijui hali ya mrembo wa shani mwenye ngozi nyororo na sura isiyochosha kuiangalia atakuwa na hali gan?
 
oooh jamani itakuaje Yarabi roh imeniuma saaana Bishop tupe tu hata kamuhtasari hata najipa moyo hii ni hadithi tu ila roho inauma kweli wasipatwe na mabaya please
 
oooh jamani itakuaje Yarabi roho imeniuma saaana Bishop tupe tu hata kamuhtasari hata najipa moyo hii ni hadithi tu ila roho inauma kweli wasipatwe na mabaya please
Usikonde, mambo bado ni moto sana...
 
Mgeni mwema.jpg

157

Labda uniite Mgeni…


Saa 4:30 asubuhi…

NDANI ya wadi ya watoto katika Hospitali ya Benjamin Mkapa, iliyojengwa katika eneo la Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) jijini humo, mtoto Mariam Mgeni mwenye umri wa miaka miwili na nusu, alikuwa amelala nusu mfu kwenye kitanda cheupe cha chuma chenye godoro nene la foronya laini na mto laini wa kuegemeza kichwa.

Hospitali ya Benjamin Mkapa ilionekana dhahiri kuwakilisha mapinduzi makubwa nchini katika sekta ya afya. Ilikuwa mojawapo ya hospitali za kisasa zenye ustaarabu, usafi na mandhari yenye kuvutia kiasi cha kutoa liwazo kwa wagonjwa hata kabla ya kupata tiba. Ilikuwa na mifumo ya kisasa kabisa ya teknolojia iliyokuwa inarahisisha utendaji kazi na utunzaji wa takwimu za hospitali ile.

Mfumo uliokuwepo ulikuwa ni ule wa kusafirisha sampuli ndani ya hospitali kwa njia ya ‘mawimbi hewa’ ambao ulisaidia sana katika kuharakisha usafirishaji wa sampuli na hivyo kuepusha ucheleweshaji wa vipimo.

Uwepo wa vifaa tiba vya kutosha na matumizi ya teknolojia katika hospitali ile uliwezesha pia utoaji wa mafunzo na huduma bora za matibabu, uchunguzi wa magonjwa na kufanya tafiti za fani za afya zilizo bora hapa nchini, lakini pia ulipunguza kwa kiasi kikubwa gharama zilizokuwa zinatumika kwa ajili ya matibabu nje ya nchi.

Pale kitandani mtoto Mariam alikuwa anapumua kwa shida sana kutokana na kusumbuliwa na tatizo la seli mundu lililokuwa likisababisha apungukiwe na damu mara kwa mara na hata kupata matatizo ya kupumua.

Kando ya kitanda chake kulikuwa na stendi ndefu ya chuma ya kitabibu iliyokuwa imetundikiwa chupa ndogo ya damu na mrija wake ukipeleka damu kwenye mshipa wa damu kichwani kwa Mariam.

Kando ya ile stendi ya chuma kulikuwa na meza ndogo na juu yake kulikuwa na trei ndogo ya chuma iliyokuwa na vifaa-tiba kama mikasi, plasta, bomba la sindano, glavu, chupa kubwa ya maji safi, bilauri, chupa ndogo ya dawa ya sindano na dawa za maji kwa ajili ya tatizo lake la seli mundu.

Baadhi ya vifaa hivyo vilikuwa vimefunguliwa na kuachwa wazi baada ya kutumika.

Mwanadada Zainabu Pembe, mama wa Mariam alikuwa ameketi ukingoni mwa kitanda alicholala Mariam akiwa mwenye huzuni. Muda wote alikuwa mtulivu sana na alikuwa anamtazama Mariam katika namna ya kukata tamaa, alionekana kuwa mbali sana kimawazo na machozi yalikuwa yanamlengalenga machoni muda wote.

Zainabu alikuwa na umri wa miaka 22 na alikuwa amejaaliwa sura nzuri na umbo, alikuwa msichana mwenye mvuto sana na uzuri wa asili uliofichwa kutokana na hali duni ya maisha na hivyo ilikuwa vigumu kuuona. Alikuwa mrefu kiasi na mweupe.

Kiuno chake chembamba kilikuwa kimefinyangwa katika namna ya kulifanya umbo lake liweze kuitaabisha kila nafsi ya mwanamume yeyote asiyekuwa na msimamo.

Asubuhi hiyo alikuwa amevalia gauni zuri la kitenge lililoshonwa kwa mtindo wa ‘Ankara midi tube dress’ na alijifunga khanga kiunoni huku nguo zake zikiushika vyema mwili wake na kulichora umbo lake maridhawa, na miguuni alivaa makubazi ya kike.

Mimi, Mgeni, nilikuwa nimesimama kando ya kitanda nikimtazama mwanetu Mariam kwa huzuni. Sikuwa na raha, muda wote nilikuwa njia panda nikiwa na wasiwasi mwingi, si kutokana tu na hali ya Mariam bali pia kutokana na ukweli ambao uliendelea kuitesa akili yangu kwa takriban miezi saba sasa.

Nikiwa na umri wa kati ya miaka therathini na therathini na tano – kwa kuwa sikuujua umri wangu – nilikuwa mrefu na mwenye mwili wa kimazoezi. Asubuhi hiyo nilivaa suruali ya dengrizi ya rangi ya bluu mpauko, shati la mikono mirefu la rangi ya samawati, raba nyeusi na miwani myeusi ya jua niliyoipandisha kichwani juu ya uso wangu.

Huku nikimtazama Mariam sikuacha kutafakari kuhusu maisha yangu na hatma yangu. Nilikuwa nawazia kitu ambacho kilikuwa kikinitatiza sana na kukaribia kunitia uwendawazimu kwa takriban miezi saba, tangu nijifahamu. Nilijiuliza sana lakini bado sikuwa napata majibu: “Hivi mimi ni nani hasa?”; “Asili yangu ni wapi?”; “Jina langu nani?” n.k.

Hata hivyo, niliamini kuwa kujiuliza maswali hayo ni kupoteza muda tu maana nisingepata majibu abadani. Lakini si mimi tu, bali hakuna mtu yeyote kati ya watu walionizunguka aliyeijua asili yangu, jina langu, kabila langu, dini yangu wala jamaa zangu.

Jambo hili lilikuwa linaniumiza sana na hata kunitia hofu; kutokuijua asili yangu wala jina langu kulinifanya niishie kujiita “Mgeni” na Zainabu aliniongezea jina la “Mwema” baada ya kumnusuru kwenye kadhia fulani. Kwa maana hiyo nikawa najulikana kwa jina la Mgeni Mwema.

Maumivu makali yalikuwa yakiutesa moyo wangu hasa pale nilipotaka kukumbuka hata jina langu halisi lakini nikashindwa, sikukumbuka kitu chochote, niliishi maisha ya tabu sana, kila kitu kwenye maisha yangu kilikuwa kipya kabisa! Sikufahamu chochote kuhusu ulimwengu, kila kitu kilikuwa ni giza ndani ya maisha yangu.

Ilitokea tu siku moja, takriban miezi saba iliyokuwa imepita, nilipopata fahamu nikajikuta nipo katika Mji wa Kilosa, sikujua nilifikaje hapo Kilosa. Rafiki zangu walikuwa wananitania wakidai kuwa “eti” nilizuka tu kama kumbikumbi!

Sasa kumbukumbu zangu zilinirudisha miezi saba iliyokuwa imepita… siku ambayo nilizinduka toka kwenye usingizi mzito sana. Kilichonizindua ni baridi kali iliyoambatana na upepo wa kipupwe ambao ulinipiga mwili na kunifanya nijikute nikitetemeka na meno yangu yakigongana. Nilikuwa nimelala kwenye baraza ya jengo moja katikati ya mji, karibu na kituo cha mabasi, peke yangu. Jogoo waliokuwa wakiwika huko na huko waliniashiria kuwa ilikuwa alfajiri.

“Niko wapi?” nilijiluliza nikiinuka na kutazama huko na huko. Vidole vyangu vilikuwa vimekufa ganzi kutokana na baridi. Hata pale nilipojaribu kutembea miguu yangu ilinijulisha kwamba damu ilikuwa imeganda na hivyo ilikaribia ganzi kwa ajili ya baridi hiyo kali.

Nilijikaza na kuiburuza wakati inazidi kunyong’onyea, nikajikongoja hadi nilipomfikia mtu mmoja ambaye alikuwa anapita eneo lile akionekana mwenye haraka. Alikuwa mtu mzima wa makamo, mrefu na mwembamba mwenye sura ya ucheshi. Rangi ya ngozi yake ilikuwa maji ya kunde na macho yake yalikuwa makubwa yenye uchovu lakini yaliyokuwa makini. Kichwani alikuwa na upara uliokuwa unawaka na usiokuwa na unywele hata mmoja.

Alikuwa amevaa suruali ya kijivu, shati jeupe na sweta jeusi juu yake, kichwani alivaa kofia nyeusi ya pama na miguuni alivaa makubazi ya ngozi.

“Samahani, mzee. Habari za asubuhi!” nilimsalimia yule mtu kwa adabu.

“Nzuri, kijana!” yule mzee alijibu huku akinitazama usoni kwa makini.

“Samahani, sijui hapa nipo wapi?” nilimuuliza yule mzee huku nikimtazama kwa wasiwasi.

“Kwani wewe umetoka wapi hata uulize hapa ni wapi?” yule mzee aliniuliza huku akinitazama kwa mshangao kidogo.

“Hata sijui!” nilijibu kwa wasiwasi huku nikiangalia chini kuyakwepa macho ya yule mzee.

“Kwani umekuja na usafiri gani?” yule mzee aliniuliza tena huku akiendelea kunitazama kwa mshangao. Sikujua alinifikiria nini.

Sikuwa na jibu, jambo ambalo lilizidi kumshangaza yule mzee. Alinitazama kwa sekunde kadhaa kisha akaniuliza tena, “Ulikuwa umelewa au una matatizo… labda ya akili?”

Inaendelea...
 
Mgeni mwema.jpg

158

“Kwa kweli sijui, mimi nimejikuta nipo hapa tu,” nilisema na kumfanya aachie mguno wa mshangao.

“Sasa umewezaje kufika hapa Kilosa bila kujua umetoka wapi na umetumia usafiri gani?” yule mzee aliniuliza tena huku akinitazama kwa mashaka kidogo, huenda alidhani sikuwa timamu kiakili.

Sikuendelea kumuuliza wala kumsikiliza. Kilosa! Kumbe nilikuwa katika mji wa Kilosa! Niliwaza kwa mshangao huku nikiondoka eneo hilo nikamwacha yule mzee akinisindikiza kwa macho yaliyojaa mshangao.

Baridi kali ilikuwa ikinila mifupa. Hata mavazi ya watu wengi niliokutana nao mitaani yaliashiria kuwa ulikuwa msimu wa baridi: walivaa makoti, majaketi makubwa au masweta, kofia au vitambaa kichwani na viatu vizito miguuni.

Sasa baada ya kujikuta hapo Kilosa pasipo kujua wapi nilikotoka niliamua kutembea ndani ya mji huo uliokuwa mpya kabisa machoni mwangu, sikujua wapi pa kwenda wala pa kujipumzisha. Nilizunguka huku na huko kwa takriban saa tano kabla sijajikuta nipo kwenye eneo fulani lililokuwa na kambi, nje kabisa ya mji, nikiwa nimechoka.

Muda wote sikuwa nakumbuka kitu! Nilidhani ningekumbuka lolote kwa kutazama watu na majengo lakini haikuwa kama nilivyowaza. Sikukumbuka hata tone ya jambo! Niliwaza kuwa nitafute ilipo hospitali niende na kuwaelezea shida yangu ya kutokumbuka chochote pengine wangenisaidia lakini mfukoni sikuwa na fedha. Hivyo sikuona kama wangenielewa!

Nikataka nitafute chakula, na hapo ndipo nikakumbuka kwamba hata fedha ya chakula sikuwa nayo. Muda huo tumbo langu lilikuwa linanguruma kwa njaa! Nikaona nifanye stara kutafuta kazi yoyote ile ambayo ingenipatia fedha kabla jua halijazama na kiza kutawala.

Nilianza kazi ya kutafuta kazi kwa kupita huku na huko ila sikufanikiwa kupata, kila nilipoenda hata kuomba kazi ya kusafisha vyombo waliniambia kuwa hawahitaji mfanyakazi. Mpaka giza linaingia sikuwa nimepata kitu. Tumbo nalo lilikuwa linadai haki yake.

Sikuwa na namna ya kufanya bali kulala ndani ya jengo moja bovu lisilokaliwa na mtu. Niliazimia kulala mahali hapo nilipoamini pangenikinga kidogo na baridi la Kilosa. Nilijiegesha hapo nikijikunyata huku nikiwaza sana pasipo mafanikio. Mwishowe usingizi ukanichukua ila ulikuwa wa mang’amung’amu. Huenda ni sababu ya njaa na kuhisi kuwa sipo eneo salama.

Ulikuwa usiku mzito na mrefu sana, na ilipofika majira ya takriban saa sita hivi za usiku, nikiwa nimefumba macho yangu, nilihisi kusikia, mara moja tu, sauti ya mwanamke ikipiga kelele kuomba msaada, na wakati huo huo kulikuwa na sauti nyingine hafifu ya mtoto mdogo akilia.

Nilishtuka na kuinuka haraka, nikaketi huku nikisilikizia kwa umakini, nikasikia kama purukshani hivi huku sauti ya mwanamke ikiendelea kuugulia kwa maumivu na uchungu, na hivyo niliinuka na kutazama kushoto na kulia lakini sikuona kitu!

Niliamua nitoke nje ya lile jengo huku nikiangaza huku na kule maana sauti ile iliendelea kuugulia huku mwanamke huyo akiwa anasihi au kuomba msaada. Niliposikiliza vizuri nikatambua kuwa haikuwa inatokea mbali bali ilitoka upande wa Mashariki, katika mojawapo ya vyumba ndani ya lile lile jumba bovu nililokuwa nimelala. Haraka nikakimbilia upande huo nilioamini sauti hiyo ilikuwa inatokea, kwa pupa na kuangaza.

Kwa msaada wa mwanga hafifu uliotokana na nyota angani na mbalamwezi niliweza kuona kitu kilichoufanya moyo wangu upige kite kwa nguvu na nywele zangu kunisimama kwa hofu na hasira.

Nilichokiona ni mwanamume mmoja akiwa ameshika kisu kikubwa na kumbana chini msichana mmoja huku akiwa anaharakisha kufungua mkanda na zipu ya suruali yake kwa lengo la kutaka kumwingilia kwa nguvu msichana huyo ambaye muda huo alikuwa amelala juu ya sakafu chafu ya jengo hilo, akiwa uchi kama alivyozaliwa, mavazi yake yakiwa yamechanwa chanwa na kutupwa kando.

Kando ya msichana huyo nilimwona mtoto mdogo mwenye umri wa takriban miaka miwili ambaye alionekana dhaifu sana, na hata sauti yake wakati akilia kwa hofu ilikuwa hafifu na haikuweza kufika mbali.

Macho hayana pazia… macho yangu yalijikuta yakivutwa zaidi kuyatazama mapaja mazuri ya yule msichana yaliyonawiri vizuri na kulidhihirisha umbo lake zuri la nyigu lililoonekana kukosa matunzo bora, na uso wake ulikuwa unachuruzikwa na damu.

Kwa mtazamo wa haraka tu nilibaini kuwa msichana huyo alikuwa mzuri sana, mng’avu kwa rangi ya ngozi yake na alionekana mwenye haiba ya kuvutia ingawa alikuwa amechoka sana kutokana na hali duni ya maisha au ufukara uliokithiri.

Pia niliweza kubaini kuwa umri wake ulikuwa wa kati ya miaka ishirini na ishirini na tano, na nywele zake zilikuwa ndefu alizozisuka mtindo wa twende kilioni.

Macho yangu niliyarudisha tena kwa yule mwanamume aliyekuwa amembana yule msichana pale chini. Alikuwa mwanamume mrefu na mweusi mwenye mwili uliojengeka kwa misuli imara. Alikuwa amevaa fulana nyekundu ya mchinjo iliyoifanya misuli imara ya mikononi mwake iliyotuna kikamilifu kuonekana vizuri.

Alivaa uruali nyeusi ya dengrizi iliyochanwa chanwa kwa mbele usawa wa mapaja yake, kichwani alivaa kofia kubwa nyeusi aina ya mzula na miguuni alivaa raba nyeusi.

“Mwachie huyo mwanamke upesi!” nilimwamuru mwanamume huyo pasipo kujiuliza mara mbili, huku nikiwa namkodolea macho yaliyojaa hasira. Muda huo mapigo yangu ya moyo yalikuwa yanaenda mbio kwa hasira. Kwangu, mwanamume huyo alikuwa ni mnyama kabisa.

“Utanifanya nini nisipomwacha?” yule mwanamume alinijibu kwa jeuri huku akishusha pumzi ndefu.

Kabla sijajibu nilimwona yule msichana akipata nguvu mpya na kuanza kupambana ili ajinusuru kutoka kwenye kadhia ile ya kubakwa huku akionesha wazi kuwa alikuwa anahisi maumivu ya mwili, hilo lilionekana kwa namna alivyokuwa amekunja sura yake akiugulia na kugugumia.

“Usipomwacha nitakulazimisha kumwacha kwa kipigo ambacho hujawahi kupigwa tangu uzaliwe!” nilimwambia huku nikimnyooshea kidole.

Kwa dharau yule mwanamume alimwacha yule msichana na kumsukuma kando kisha alinifuata pasipo kujua nini nilikuwa nimempangia kichwani mwangu, laiti angejua nilikuwa nimempangia nini asingediriki kupiga hata hatua moja kunisogelea. Muda huo nilikuwa nimeng’ata meno yangu na kukunja ngumi, nikamwona akikishika vizuri kisu chake tayari kupambana na mimi.

“Nitakuua na hakuna mtu yeyote atakayekuja kuniuliza chochote!” yule mwanamume alibwata kwa ghadhabu, nami nisiseme kitu bali nilimngoja anifike ili nimfundishe adabu. Hadi muda huo sikujua kwa nini nilikuwa najiamini kiasi kile!

Aliponikaribia alirusha kisu chake ili anichome, nikaudaka mkono wenye kisu kwa namna iliyomshangaza hata yeye mwenyewe na kuutegua uachie silaha kisha nikamtwanga ngumi nzito chini ya kidevu chake. Akiwa anapepesuka, nikamsindikiza na teke zito lililonyanyua mwili wake mzito kwa kiasi chake na kisha kumbwaga chini.

Nilijishangaa sana maana sikujua niliupata wapi uwezo wa kupambana na mwanamume yule mwenye silaha na kumshinda kirahisi namna ile! Akiwa pale chini yule mwanamume aliinua uso wake kunitazama kwa mshangao, huenda hakuamini kama ningeweza kumpa kipigo cha aina ile ndani ya sekunde chache tu.

Kisha aliinuka na kujiweka sawa, pasipo kutarajia aliruka kama mkizi na kunikumba kisha wote wawili tukapiga mwereka chini. Nikawahi kusimama huku hasira zikiwa zimenipanda kichwani kama mbogo aliyejeruhiwa.

Yule mwanamume naye alisimama akiwa makini na kunitupia mapigo mawili ya kushtukiza ya ngumi kavu za tumbo, mapigo yale yalinikuta nikiwa bado sijakaa sawa na kunipata kisawasawa, nikaguna kwa maumivu makali niliyoyapata.

Kisha yule mwanamume alirusha teke lililonipata sawa sawa kwenye kinena na kunirusha likanitupa chini, nilihisi maumivu makali yasiyoelezeka.

Akiwa sasa amepandwa na hasira yule mwanamume alinifuata hapo hapo chini ili anifunze adabu lakini niliwahi kuinuka kwa kupiga samasoti na kisha nikajipanga tayari kwa mapambano huku nikionekana kujihami zaidi kwa kufanya mashambulizi ya nguvu.

Inaendelea...
 
Mgeni mwema.jpg

159

Niliruka na kumvaa, nikampiga kichwa kikavu kilichompata barabara mdomoni na kumng’oa meno kadhaa, pigo hilo likamfanya apepesuke huku akiweweseka kama mtu aliyepandwa na pepo.

Damu zilianza kumtoka mdomoni. Nilimwona akijishika mdomo wake, na kabla hajakaa sawa nilimrukia tena na kumkaba kabali ya nguvu iliyomfanya kukukuruka akitaka kujitoa kwenye ile kabali lakini nilizidisha kabali yangu na kumfanya yule mwanamume kuishiwa na nguvu. Nilipomwachia nikamwona akianguka chini kama mzigo na kutulia, akiwa hoi asiyejiweza.

“Dada, ondoka haraka, hapa si mahala salama!” nilimwambia yule msichana ambaye muda huo alikuwa amejikunyata kando na kumkumbatia mtoto wake kwa woga, tayari alikuwa amejisitiri kwa upande wa khanga yake baada ya gauni lake na nguo ya ndani kuchanwa.

Alikuwa anatetemeka kwa hofu. Nilimsogelea, nikamshika mkono wake kwa upole na kumsisitiza aondoke haraka eneo lile kwa kuwa haikuwa salama kwa msichana kama yeye na mtoto kuwepo eneo hilo muda huo.

Nilihisi kuwa alikuwa bado ana hofu kubwa na hakujua angeondokaje toka eneo hilo na hivyo niliamua kumsindikiza hadi tulipofika kwenye nyuma moja kubwa ya udongo yenye paa lililochoka sana. Akaniambia kuwa hapo ndipo alipokuwa amepanga chumba. Ulikuwa umbali wa takriban nusu kilomita kutoka eneo ambalo tukio la kutaka kabakwa lilitokea.

Nilimtakia usiku mwema na kisha nikaanza kupiga hatua ili niondoke lakini kabla sijaenda akaniita. Niligeuka kumtazama.

“Nakushukuru sana, kaka… lakini…” yule msichana alinishukuru lakini akaonesha kusita kidogo. Na kabla sijamuuliza chochote akaendelea, “mtu mwema kama wewe ulikuwa unafanya nini usiku huu ndani ya jumba lile bovu?”

Nilitabasamu kidogo kabla sijamwambia jibu ambalo kwa namna moja au nyingine lilionesha kumshangaza mno, “Hata sijui nikwambieje dada, kwa kifupi sina makazi.”

“Kweli?” yule mwanamke aliniuliza huku akinitazama machoni kwa huruma. Ni wazi alikuwa ameshangazwa sana na jibu langu.

“Ndiyo, nilikuwa nimelala humo kabla ya kusikia sauti yako ikiomba msaada,” nilimwambia kwa sauti tulivu lakini yenye majonzi.

Yule msichana alinitazama kwa namna ya kunikagua haraka haraka usoni mwangu kuona kama nilikuwa nasema ukweli kabla hajaachia tabasamu lililobeba uchungu.

“Kwani umetokea wapi?” alinisaili huku akiendelea kunitazama moja kwa moja machoni. Kabla sijajibu aliongeza swali jingine, “Na imekuaje hauna makazi?”

“Hata nikikueleza sijui kama utanielewa au kuniamini,” nilisema kwa huzuni na kutazama chini.

“Usijali, n’takuamini,” aliniambia kwa namna ya kunitoa hofu.

“Sijui kwa nini sina makazi,” nilimjibu, na kuongeza, “Sijui kwa nini nipo kwenye hali hii! Sikumbuki kitu chochote kwenye maisha yangu!” nilimweleza yule msichana kwa huzuni.

Nilimwona yule msichana akinikodolea macho kwa mshangao mkubwa, kisha mshangao wake ukapotea na kumezwa na kitu kama huzuni hivi, na wakati huo kukatokea kitambo kirefu cha ukimya.

“Na wewe ulikuwa unatoka wapi usiku huu na mtoto?” nilimuuliza yule msichana nikiuvunja ukimya huku nami nikimtazama machoni.

“Natoka hospitali, mwanangu anaumwa…” yule msichana aliniambia kwa sauti iliyojaa simanzi. Kisha aliongeza, “Hawezi kupumua vizuri kwa sababu ya kusumbuliwa na sickle cell inayomfanya mara kwa mara aishiwe na damu.”

Nilihisi fundo fulani la huzuni likikabaa kooni kwangu na kisha likasambaa hadi kifuani kwangu. Nilitaka kusema neno lakini nikashindwa na kubaki kimya nikimtumbulia macho, pasipo kusema neno lolote.

Akiwa bado ananitazama kwa umakini, aliniambia, “kama ningalikuwa na fedha ningekodi bodaboda na nisingalitembea kwa miguu. Hata hivyo Mungu ni wa ajabu sana, amemleta malaika wake kuja kuniokoa!”

Nilitabasamu tu nisiseme kitu. Kisha kwa mara nyingine tena nikaanza kupiga hatua ili kuondoka eneo hilo japo sikujua ni wapi nilikuwa naelekea.

“Kwa hiyo unakwenda wapi na wakati umesema kuwa huna makazi?” yule msichana aliniuliza kwa wasiwasi uliochanganyika na mshangao.

“Hata sijui!” nilimjibu huku nikinyanyua mabega yangu juu na kuyashusha.

“Mji huu si rafiki sana wakati wa usiku, mimi ilinibidi tu kutembea kwa kuwa sikuwa na namna!” yule msichana aliniambia kwa wasiwasi. Nilimtumbulia macho nikiwa sijui niseme nini.

“Unajua…” yule msichana aliendelea kusema baada ya kusita kidogo, “Japo sikufahamu, sijui wapi unatokea na wala sijui jina lako ni nani… ila endapo utapatwa na matatizo usiku huu sitajisamehe na moyo wangu utakuwa shidani…” alisema na kuonekana kusita tena kisha akashusha pumzi.

Niliona macho yake yakiangalia chini. “…ndani kwangu si pazuri sana na unaweza usipafurahie lakini panaweza kukufaa japo kwa usiku huu tu. Naomba uje upumzike na kesho utaangalia cha kufanya,” alisema na kushusha tena pumzi huku akinitazama.

Niliona namna macho yake yalivyokuwa yamebeba dhamira kubwa ya kutaka kunisaidia ili kulipa fadhila na hakuwa anatania. Kwa namna moja ama nyingine nilihisi kukubaliana na nafsi yangu kuwa msichana huyo alikuwa ameguswa na hali yangu. Nilimkubalia kisha tuliongozana hadi ndani ya chumba chake kilichokuwa kwenye mabanda ya uani.

“Hapa ndo kwangu ninapolaza ubavu wangu na mwanangu!” yule msichana alisema wakati akinifungulia mlango.

Tuliingia ndani. Kilikuwa chumba kidogo chenye upana wa futi saba tu, chumba hicho kilibeba kitanda kidogo cha futi tatu chenye godoro lililochoka na majukumu yote ya jiko, sebule, ghala; na mengineyo.

“Karibu sana, japo hapastahili kuishi binadamu!” yule msichana aliniambia kwa huzuni huku akionesha meno yake meupe yaliyopangiliwa vizuri mdomoni huku yakiacha uwazi kwa mbele.

Muda huo alikuwa anamlaza mtoto wake juu ya kitanda na yeye kuketi kitako hapo hapo kitandani.

“Mbona panafaa sana, wala hapana tatizo lolote!” nilimtoa hofu huku nikiketi juu ya kochi dogo kuukuu lililokuwa na foronya iliyochoka sana.

“Sina hakika kama utapapenda lakini panaweza kusaidia japo kwa…” yule msichana alisema lakini nikamkatisha.

“Wala usijali. Kwanza nakushukuru sana, hadi hapa umenisaidia mno. Ni pazuri mara mia ukilinganisha na kwenye lile jumba bovu nilimokuwa nimejihifadhi,” nilimweleza huku nikimtazama. Hakusema neno bali aliachia tabasamu tu.

“Kwa kweli sikuwa na pa kulala. Na kama itawezekana naomba unisaidie niwepo hapa kwa kipindi kifupi, naamini kumbukumbu zangu zitarejea na kila kitu kitakuwa sawa,” niliongeza.

Inaendelea...
 
Mgeni mwema.jpg

160

“Usijali,” yule msichana aliniambia huku akibetua kichwa chake. “Utapumzika hapa kwa siku utakazotaka huku tukiangalia cha kufanya.”

Nilimtazama machoni na kutabasamu kwa mbali. Nikamshika bega lake na kumwahidi kuwa nami nitajitahidi kwa kadiri niwezavyo ili nimsaidie aweze kuondokana na aina ile ya maisha duni.

“Halafu nilisahau kukuuliza, kwani hapa waishi na nani?” nilikumbuka kumuuliza huku nikizungusha macho yangu ndani ya kile chumba.

“Nipo mwenyewe tu na mwanangu,” yule msichana aliniambia huku akinionesha yule mtoto mdogo aliyekuwa amemlaza juu ya kitanda.

“Kwani baba wa mtoto yuko wapi?” niliuliza kwa shauku nikitaka kujua kuhusu baba wa mtoto.

Nilimwona yule msichana akibadilika sura. Kwanza alitabasamu, lilikuwa tabasamu la uchungu… kisha tabasamu lake lilimezwa na uso uliojaa huzuni, na machozi yalianza kumlengalenga machoni.

“Vipi kwani?” nilimwuliza kwa mshangao.

Alibaki kimya akinitazama kwa kitambo fulani. Ilimchukua takriban dakika nzima akionekana kufikiria jibu la kunipa kisha alishusha pumzi huku akifuta machozi yaliyokuwa yakimlengalenga.

“Mh… yaani ninyi wanaume…!” yule msichana alisema kwa huzuni. Kauli yake ikanifanya nibaini jambo kubwa moyoni kwake, alikuwa na kovu la kutendwa.

Sikutia neno lolote bali nilibaki kimya nikimtazama kwa umakini. Ndipo aliponieleza kisa kilichonihuzunisha sana hata nikajikuta nikimwonea huruma sana.

Katika kisa cha maisha yake nilitambua kuwa aliitwa Zainabu Pembe na utoto wake ulikuwa umedhulumiwa na majukumu mazito aliyobebeshwa angali binti mdogo, asiyejua lila wala fila ya ulimwengu.

Hakuwa na elimu wala ujuzi wowote wa maana. Elimu ya kidato cha pili aliyofikia alifika hapo kwa mbinde kutokana na maisha yake kumpiga danadana hasa baada ya mlezi wake kufa kwa ugonjwa usioeleweka.

“Nimezaliwa katika familia ya kifukara, nilikuwa na kaka yangu ambaye tulipishana miaka kumi, alikuwa anasoma kidato cha tano katika Sekondari ya Mzumbe huko Morogoro kwa msaada wa serikali ya Kijiji cha Kitete. Kaka yangu huyo alikuwa ndiyo mboni ya jicho ya wazazi wangu hasa mama. Walimpenda mno, na ukizingatia alikuwa na akili nyingi. Kila mtu pale kijijini kwetu Kitete alimsifia. Kila siku wazazi wangu waliniusia nikazanie kusoma ili nifuate ndoto za kaka yangu…” Zainabu alisema kwa huzuni na kushusha pumzi.

“Maisha yalikuja kubadilika ghafla nilipokuwa darasa la tatu, nakumbuka nilipotoka shule nilikuta watu wamejikusanya nyumbani na kulikuwa na vilio. Nami nikaunga kilio pasipo kujua huku nikiwa naogopa kuuliza. Wakati wamama wananituliza wakaniambia kaka yangu aliugua ghafla shuleni na akafariki dunia siku hiyo hiyo. Ilituumiza sana kama familia,” Zainabu alinyamaza kidogo na kufuta machozi yaliyoanza kumtoka.

“Kuanzia hapo mama yangu alianza kusumbuliwa na sonona isiyoisha. Kila kitu kilibadilika pale nyumbani. Hata mawasiliano ya kawaida tu kati yangu na mama yalikuwa ya nadra sana. Kisha mama akaanza kuugua mara kwa mara. Mara alalamike mgongo, mara miguu, ama kichwa. Ili mradi hakuna machweo yaliyopita asiwe katika hali ya kunung’unikia maumivu…

“Akawa anatibiwa katika zahanati ya pale pale kijijini ila hakupata nafuu. Tabibu mmoja akagundua kinachomsumbua ni msongo mkali wa mawazo. Ikabidi aletwe huku Kilosa kwenye hospitali kubwa. Wakati wakija huku ikatokea ajali iliyosababisha wazazi wangu wote kufariki dunia hapo hapo,” Zainabu alisema na kuvuta pumzi ndefu kisha akazishusha taratibu.

Kisha kikatokea kitambo kifupi cha ukimya kabla hajaendelea kunisimulia kuwa; akiwa mtoto pekee aliyebaki kwa wazazi wake urithi pekee waliomwachia ilikuwa nyumba ndogo ya udongo na shamba huko kijijini Kitete. Hali hiyo ilimfanya kuyaona maisha machungu, mawio hadi machweo.

Kutokana na hali hiyo alichukuliwa na mama yake mkubwa ambaye hakuwa na mtoto na kuishi naye hapo Kilosa. Mama huyo alikuwa amepanga chumba katika eneo la Manzese B. Huko pia maisha hayakuwa mazuri ingawa kulikuwa na mabadiliko kidogo. Mama huyo alikuwa muuza pombe za kienyeji jambo lililomfanya Zainabu kila alipotoka shule kujiunga na mama huyo kumsaidia kuuza pombe, wakati mwingine mpaka usiku mnene. Muda mchache sana aliutumia kujisomea lakini akaishia kusinzia na aliposhtuka ilikuwa ni tayari alfajiri.

Mzunguko wa maisha yake ukawa hivyo kila iitwapo leo. Hakuyapenda yale maisha hata kidogo lakini ndiyo vile mtu hajichagulii pa kuzaliwa!

Hata hivyo mama huyo alimpenda sana Zainabu, alijitahidi kuifanya kazi yake ya kuuza pombe katika mazingira magumu mno, kazi ambayo ilimwondolea utu na heshima kwa jamii, ili tu Zainabu apate elimu.

Zainabu alisoma kwa bidii na aliyazingatia masomo akiamini elimu hiyo ingemkomboa toka katika lindi la ufukara, lakini akiwa kidato cha pili huyo mama naye akafariki dunia kwa ugonjwa ambao haukujulikana na hivyo kumwacha Zainabu akiwa hana tena pa kushika.

Urithi pekee alioachiwa na mama huyo ilikuwa kiwanja ambacho hakikuwa kimeendelezwa, katika eneo la Kichangani, hapo hapo Kilosa.

Zainabu aliendelea kusema kuwa kuna nyakati alisononeka sana na nyakati zingine alijiuliza kwa nini hakuzaliwa kwenye familia zenye ahueni kama wenzake! Hakukuwa na wa kumpa majibu au hata wa kumtia moyo kutokana na madhila yale. Hata hivyo, aliapa kutokata tamaa. Na hakutaka kujirahisi kwa wanaume ili apate ujira.

Alihangaika kutafuta kibarua, akifanya yote aliyoyafanya mjini, ili aweze kujikimu. Alifanya kazi dhalili katika mazingira magumu mno, kazi ngumu ambayo wakati mwingine iliyomwondolea utu na heshima kwa jamii ili tu ajikimu. Katika kuhangaika siku moja akajikuta akiangukia katika mtego wa kijana Deus Mkuro.

Ilitokea wakakutana mara moja tu na baada miezi miwili Zainabu akajigundua kuwa alikuwa ameshika ujauzito. Na alipomfuata Deus alimkuta akiwa na msichana mwingine chumbani kwake, walikuwa kitandani watupu kama walivyozaliwa.

Zainabu alishindwa kuvumilia hasa baada ya kugundua kuwa msichana huyo alikuwa shoga yake mkubwa, Maria Kikavu. Alilia kwa uchungu mkubwa mbele ya Deus lakini mwenzake akaukana ujauzito wake. Kuona hivyo, Zainabu hakutaka makuu, aligeuka akaondoka zake huku akilia kwa uchungu. Jambo moja lilimjia kichwani, atafute vidonge anywe ili afe yeye na mtoto wake tumboni.

Lakini aliahirisha kufanya hivyo kwa kuwa aliamini mtoto tumboni hakuwa na kosa lolote na hakustahili kufa, pia yeye hakutakiwa kukata tamaa kwani hakuwa wa kwanza kupatwa na madhila kama yale.

Mungu si Athumani, baada ya mahangaiko ya miezi tisa ya ujauzito wake hatimaye alijifungua mtoto mzuri wa kike aliyempa jina la Mariam, jina la mama yake. Mtoto ambaye badala ya kuwa faraja katika maisha yake akageuka kuwa mateso, kwani haupiti mwezi lazima wangejikuta wakilazwa hospitali kwa matatizo haya na yale.

“Ndo’ hivyo, Deus hakuishia kuukataa tu ujauzito bali pia alimuoa shoga yangu Maria na hadi leo sijui wanaishi wapi!” Zainabu alimalizia simulizi yake ya kuhuzunisha na kushusha pumzi.

Sikujua kilichotokea, nilijikuta nimesimama na kumkumbatia kwa namna ya kumfariji huku yeye pia akinikumbatia na kukilaza kichwa chake juu ya kifua changu huku akinong’ona maneno fulani ambayo sikuyasikia vizuri.

Inaendelea...
 
Mgeni mwema.jpg

161

“Pole sana!” nilimwambia huku nikiwa bado nimemkumbatia.

“Ndo’ hivyo. Naomba tuyaache, sipendi kuyakaumbuka,” alisema huku akijitoa kwenye mikono yangu.

Niliiheshimu kauli yake ila nilitaka kujua anafanya nini ili kujikimu kimaisha. Aliniambia kuwa alikuwa anafanya kazi ya kuwapikia chakula wafanyakazi wa kampuni ya kandarasi ya ujenzi ya Yapi Merkezi iliyokuwa inajenga reli ya kisasa (SGR) kutoka Morogoro hadi Makutupora Dodoma, ili kujipatia kipato na kukidhi mahitaji yake na mtoto wake asiye na baba.

“Mimi nimekwambia jina langu, na wewe waitwa nani?” kisha Zainabu alinitupia swali lililonifanya nishikwe na kigugumizi cha ghafla.

Nilisita kidogo huku nikifikiria nitaje jina gani maana sikujua naitwa nani! Nilimtazama usoni kwa huzuni. “Hata sijui nikwambieje, labda uniite Mgeni…” nikajisemea jina la kwanza kuja kichwani mwangu.

“Mgeni Mwema…” Zainabu alidakia huku akitabasamu, alikuwa ananitazama kwa namna ambayo sikuweka kupata tafsiri yake haraka, kisha aliyakwepa macho yangu na kutazama kando, alikuwa analengwalengwa na machozi.

Baada ya hapo tuliongea machache tu kisha alitaka tupumzike maana ulikuwa ni usiku mkubwa. Alikung’uta vumbi pale kitandani kisha akaniomba tulale wote pale kitandani, japo kwa kujibanabana, kwa kuwa hakukuwa na sehemu nyingine ambayo ningeweza kulaza ubavu wangu.

Nilipanda kitandani na nguo zangu. Zainabu alinipa kipande cha khanga nijifunike. Tukalala kwa kujibanabana, mimi nikilala mwanzo wa kitanda, yeye alilala ukutani huku yule mtoto akilala katikati yetu.

Ndiyo kwanza nikabaini kuwa godoro lilikuwa kuukuu, pengine ndiyo lile lile lililonunuliwa na mama yake mkubwa na halikupata kubadilishwa. Mbavu zangu zilikwenda moja kwa moja kukutana na chaga za mbao.

Si hilo tu, dakika mbili tu za kupumzika juu ya kitanda hicho, nilikaribishwa na kunguni walionitesa kwa kufyonza damu yangu kimyakimya na kunisababishia maumivu mengine. Nilifanikiwa kuwaua kunguni wawili watatu. Lakini harufu yao kali ilinitia kichefuchefu.

Japo godoro lilikuwa limechoka sana kiasi cha kuzihisi chaga za kitanda zikiumiza mbavu zangu na adha nyingine ya kunguni lakini nilipitiwa na usingizi hadi nilipokuja kushtuka alfajiri, sikujua ilikuwa saa ngapi! Hisia za kukumbatiwa na mtu pale kitandani zilinigutusha toka kwenye usingizi mzito, nilijigeuza kivivu na kukutana uso kwa uso na Zainabu.

Sura yake ya duara iliyopambwa na tabasamu maridadi kabisa la aibu ilinipumbaza kidogo. Na hapo pembe za midomo yake zikafinya na vishimo vidogo kwenye mashavu yake vikachomoza na kutishia kuzisulubu hisia zangu. Japo alinitazama kwa tabasamu usoni mwake lakini machoni bado usingizi ulikuwa umemjalia.

Nilishangaa kidogo kwani wakati tunalala usiku tulikuwa tumetenganishwa na mtoto katikati yetu lakini sasa mtoto alikuwa amelala ukutani.

“Umelalaje, Mgeni?” Zainabu aliniuliza huku akiendelea kutabasamu kwa aibu. Kisha alijiinua toka pale kitandani na kusimama huku akinitazama kwa aibu.

Alikuwa amejifunga khanga mbili, moja aliifungia kifuani na nyingine aliifunga kiunoni. Na hapo nikapata wasaa mzuri wa kuuona uzuri wake.

Alikuwa mzuri na mrembo lakini shida zilimkongoroa ingawa hazikuuficha uzuri wake wa asili. Katikati ya dhiki zake, ulimbwende wake uliwaka kama kandili hafifu gizani. Wala isingehitajika darubini kung’amua ni wapi uzuri wake ulikopotelea. Ni dhahiri, maisha yalimpigisha kwata. Ungeweza kudhani labda alikuwa anaikimbilia miaka arobaini tangu alione jua. Usichana wake ulikuwa umeshambuliwa na utu uzima uliomjia ukiwa umevikwa koti la umasikini.

Hata hivyo, nilijikuta nikikiri moyoni mwangu kuwa japo dunia ilifurika wasichana wazuri na warembo kupindukia na wengi wao wakiwa wameuongeza urembo wao wa asili maradufu kwa vipodozi lukuki, lakini Zainabu hakuwa wa kawaida kabisa machoni mwangu. Pamoja na kwamba uzuri wake haukuonekana waziwazi kutokana na hali duni ya maisha aliyoishi lakini alikuwa na ziada juu ya uzuri wake.

Ziada hiyo haikutokana na rangi yake nyeupe ya asili ya ngozi yake, la hasha! Haikutokana na lile tabasamu lake maridhawa lililotaka kuichanganya akili yangu, na wala haikutokana na macho yake malegevu yenye kushawishi. Lakini nilihisi kuwa alikuwa na ziada! Lakini ziada hiyo ilikuwa ipi? Ni swali lililoanza kunitesa.

“Nakusalimia,” sauti ya Zainabu ilinigutusha toka kwenye mawazo yangu.

“Salama. Vipi wewe?” nilijibu huku nami nikiachia tabasamu kisha nilijiinua na kukaa pale kitandani, miguu ikikanyaga chini, nikayafikicha macho yangu na kupiga miayo. Niliendelea kujiuliza kuhusu uzuri wa binti huyo.

“Salama tu,” Zainabu aliitikia huku akinitazama machoni kama aliyekuwa akijaribu kuyasoma mawazo yangu.

Macho yetu yalipogongana Zainabu aliyaondosha haraka macho yake na kutazama chini kwa aibu huku akizidi kuachia tabasamu maridhawa la aibu. Ni hapo ndipo nilipobaini ile ziada iliyonivutia kwa msichana huyo. Haya!

Nilijikuta nikivutiwa sana na jambo hilo! Niliamini kuwa katika karne hii kukutana na msichana mzuri wa aina hiyo mwenye haya lilikuwa jambo gumu mno, lakini Zainabu alikuwa mmoja tu kati ya wasichana wachache sana duniani waliobakia na haya.

“Twende nikakuoneshe lilipo bafu uoge ili kupunguza uchovu kisha nikupeleke kwa bosi mmoja wa kampuni inayojenga reli ya kisasa, huwenda ukapokelewa na kuanza kazi,” Zainabu alisema huku akinitazama machoni kwa upole.

Niliinuka pasipo kusema neno, nikamfuata kimya kimya hadi lilipo bafu.

“Ahsante sana kwa wema wako,” nilimwambia baada ya kuingia bafuni. Kumbe Zainabu alikuwa ameamka mapema zaidi na aliniandalia maji ya uvuguvugu kwenye ndoo.

“Ni mimi ambaye ninapaswa kukushukuru sana maana kama isingekuwa wewe jana hata sijui ingekuwaje kwangu na kwa mwanangu!” Zainabu alisema kwa huzuni huku akinitazama kwa macho ya shukurani.

“Jana au leo kabla hapajapambazuka?” nilimuuliza huku nikijaribu kuvuta picha ya kile kilichotokea usiku.

“Kweli ni leo…” Zainabu alijisahihisha huku akiangua kicheko cha aibu.

“Usijali, nisingekuwa mimi basi angetokea mtu mwingine wa kukuokoa. Kila kitu hupangwa na Mungu,” nilisema wakati nikilitengeneza vizuri pazia kuukuu lililowekwa kwenye mlango wa bafu ili kumsitiri mtu aliyemo bafuni.

Saa chache baadaye nilijikuta nipo ndani ya ile kambi niliyoiona siku iliyokuwa imetangulia. Nilikuwa naongea na msimamizi mmoja wa mradi wa ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) kutoka Morogoro hadi Makutupora Dodoma. Mwanzoni sikujua kuwa ile kambi ilikuwa ya kampuni ya kandarasi ya ujenzi ya Yapi Merkezi iliyokuwa inajenga reli hiyo ya kisasa.

Nilifanikiwa kupata kazi baada ya Zainabu kunikutanisha na msimamizi wa kampuni hiyo aliyeitwa Jerome Mloka, ambaye kwa mtazamo wa haraka haraka tu niliweza kubaini kuwa yeye na Zainabu hawakuwa tu wanafahamiana bali walikuwa na uhusiano wa kimapenzi, ndiyo maana Zainabu alinitambulisha kwa Jerome kama binamu yake.

“Umepata kazi moja kwa moja,” yule msimamizi aliniambia baada ya maongezi mafupi kati yake na Zainabu, huku akinitazama kwa huruma machoni, sikujua Zainabu alikuwa amemwambia nini kuhusu mimi.

Jerome alikuwa mrefu zaidi yangu mwenye mwili wa kimazoezi na mweupe mwenye sura ya tabasamu muda wote ingawa macho yake yalikuwa makini kama askari. Alikuwa na ndevu nyingi alizopenda kuzinyoa kwa mtindo wa “O” na alivaa suruali nyeusi ya dengrizi, shati zuri la rangi ya samawati, kizibao maalumu cha kazi chenye kung’aa na viatu vigumu vya ngozi.

Inaendelea...
 
Back
Top Bottom