Simulizi: Harakati za Jason Sizya

Simulizi: Harakati za Jason Sizya

I wish i was u ila subra ndo nimenyimwa everytime nakuja kuchungulia hola. Kuna namna mtu ukifaulu kusubiri iishe una faida sana maana wengine kususa tunatamani ila ndo hivo tena.....watunzi wazuri wanajua kutuweka roho juu honestly...
Ndo kwanza tupo season ya nne, hadi tufike ya kumi...
 
Mgeni mwema.jpg

195

Umenishtua sana!




Saa 3:15 usiku…

CHUMBANI ni eneo linalobaki kuwa la faragha kupita maeneo yote kwa wapenzi, hasa wale waliohalalishwa yaani wanandoa. Mimi na Rehema tulikuwa wapenzi tuliohalalishwa, japo baada ya kuhalalishwa ilipita miezi mingi tukiwa hatujapata faragha kama ambayo usiku huo tulikuwa tumeipata.

Humo chumbani Rehema alikuwa akinisimulia jinsi ilivyokuwa kwa upande wake kuhusiana na ile ajali tuliyoipata kule Makutupora miezi tisa iliyokuwa imepita, ajali iliyosababisha yote yaliyotokea hadi ikadhaniwa kuwa nilikuwa nimekufa.

Muda huo tukiwa chumbani, giza lilishatanda huko nje, mwanga wa umeme ndiyo uliotawala giza na kulipa nuru Jiji la Dodoma, watu wengi jijini Dodoma ama walikuwa wamefunga biashara zao na kurejea majumbani mwao au walikuwa wakijiandaa kufunga.

Pamoja na umeme kutoa nuru lakini giza hili lilikuwa na maana yake, halikuwa giza kama giza jingine. Hili lilikuwa limetiwa nakshi na mawingu mazito. Dalili tosha ya mvua kubwa katika jiji hilo kame lililokuwa katikati ya nchi ya Tanzania, na kusababisha mji kuwa na baridi kali la aina yake!

“…basi nilipotupwa nje nikaanza kusikia, kwa mbali, sauti za watu wakipiga kelele huku wakikimbilia kuja eneo lile… nilipotaka kuinua kichwa changu kikawa kizito mno, kisha ukungu ukatanda machoni kwangu, halafu ikawa kimya…” Rehema alisema kwa huzuni wakati akinisimulia kuhusu ile ajali.

“Nilipokuja kurudiwa na fahamu zangu ilishapita saa sita za usiku. Nilijikuta nipo wodini katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma nikiwa nimefungwa plasta ngumu kwenye mkono wangu wa kushoto uliokuwa umevunjika,” Rehema alisema huku akilengwalengwa na machozi kisha akaongeza, “Watu waliokuwa wamekizunguka kitanda changu wakati naamka walikuwa Mchungaji Ngelela, Mama Mchungaji pamoja na daktari…”

“Dah!” ndilo neno pekee nililoweza kusema kwa wakati huo.

“Basi sikutaka kujua kama nilikuwa nimeumia sana cha msingi nilikuwa hai hivyo nikataka kujua wewe ulikuwa wapi muda huo… kilichonishtua zaidi ni kuwaona Mchungaji na Mama Mchungaji wakiwa na huzuni kubwa, machozi yalikuwa yanawatoka, na mara walipogundua kuwa nimeamka walishtuka sana, na hapo Mama Mchungaji akatoka nje haraka,” Rehema alisema na kushusha pumzi.

Kisha alisema kuwa baada ya kugundua jambo hilo alimtazama Mchungaji kwa udadisi akitamani kujua kilichokuwa kinaendelea, alikuwa na mengi aliyotaka kumwuliza lakini kwa wakati ule alisita na kuamua kubaki kimya.

Siku tatu baadaye alipokuwa bado akiendelea na matibabu ndipo alipokuja kuambiwa kuwa nilikuwa nimekufa kwenye ile ajali na maiti yangu ilikuwa imeungua sana baada ya lile lori tulilogongana nalo kulipuka moto mkubwa uliosambaa na kuteketeza watu watatu. Eti waliweza kuitambua maiti yangu baada ya kuikuta jirani na tukio lile ambapo pia zilikutwa maiti za watu wengine wawili zilizotambuliwa kuwa za dereva wa lile lori na utingo wake…

“Basi tangu siku ile nilipoambiwa kuwa ulikuwa umekufa kwenye ile ajali basi maisha yangu yalibadilika, nilihisi dunia ikinielemea na nilihitaji sana msaidizi wa kuutua mzigo wa mawazo! Msaidizi huyo hakuwa mwingine bali ni kukurudisha wewe duniani kama ingewezekana…” Rehema aliniambia huku akiachia tabasamu laini.

“Kwa kweli kufiwa na mtu umpendaye si jambo dogo, hasa mume ambaye hujakaa naye hata mwezi tangu mfunge ndoa… nilihisi dunia imenidhulumu na kuninyang’anya furaha na faraja yote maishani mwangu. Hakuna mtu ambaye angeweza kuirejesha furaha hiyo isipokuwa wewe tu, mwanamume niliyekuwa nimekubebea mtoto tumboni mwangu!”

Aliendelea kusema kuwa siku ya tatu aliporuhusiwa kutoka hospitali alipelekwa nyumbani kwa Mchungaji Ngelela, hapo alikuta mazingira yakiwa ya majonzi sana, si kwa watu tu hata kuku na bata walikuwa katika hali ya taharuki. Hawakuranda randa huku na kule.

Nguvu zilimwishia na miguu ikafa ganzi. Ni kama aliuona umauti mbele yake. Hisia za maumivu makali zilijijenga ndani yake.
Akausikia uchungu bila kupigwa, hisia zilikuwa zinatesa kuliko maumivu ya kupigwa mwilini. Moyo nao ulikuwa unauma sana.

Kila alipojaribu kunyanyua miguu aliihisi ikiwa mizito, kisha ukungu mzito ukatanda machoni kwake, machozi yalikuwa yamemziba, halafu hakujua kilichoendelea hadi baada ya saa moja na nusu alipozinduka baada ya jitihada kubwa wa madaktari. Kisha jioni ya siku hiyo wakaelekea makaburini kuuzika mwili uliodhaniwa wangu.

Hata hivyo, Rehema alidai kuwa kuna wakati akili yake ilikataa kabisa kuamini kwamba nilikuwa nimekufa kwenye ile ajali, alijipa matumaini kuwa nilikuwa hai nikiwa sehemu fulani nimetulia na siku moja ningerejea nyumbani na maisha yakaendelea. Alikuwa akinihitaji sana kwa maisha yetu na hata maisha baada ya kifo! Hakunihitaji kimasihara!

Lakini kila alijikumbusha kuwa angeweza vipi kunirudisha katika maisha yake wakati tayari nilishazikwa? Hakika hakujua aanzie wapi! Alitamani asafiri huku na kule akanitafute kokote nilikokuwa na kunirudisha nyumbani lakini pia alijua hilo lisingewezekana.

Alikuwa anashinda akilia lakini baadaye akajiona mpumbavu kulia lia huku akiwa peke yake. Kilio kingemsaidia nini wakati nilikuwa nimeshakufa na kuzikwa na wala isingewezekana kurudi? Sasa akaamua kusimama imara, akajilazimisha ujasiri huku moyo wake ukiwa dhaifu na uliokufa ganzi!

Aliamini kuwa yeye hakuwa wa kwanza kufiwa na mume, wanadamu wengi walikuwa wanapatwa na mikasa mbalimbali ikiwemo maafa, na wengi wangeendelea kupatwa na mikasa hiyo kwani hiyo ilikuwa sehemu ya maisha ya mwanadamu.

Picha ya ajali ile ikawa inajirudia katika kichwa chake mara kwa mara. Ni kweli kwamba mara nyingi nilikuwa nikimuumiza kihisia lakini uwepo wangu ulikuwa kitu kingine kabisa. Msiba ule uliibadili kabisa historia, alibaki na ndugu zangu ambao wao muda mwingi walikuwa na familia zao. Akamwomba sana Mungu azidi kumpa nguvu kwani hakuwa tayari kukubali kushindwa.

Pia alijipa matumaini kuwa japo alishanizika lakini bado aliendelea kuishi na mimi kwa kuwa alikuwa amebeba damu yangu tumboni mwake na kwamba angejifungua mtoto wa kiume aliyekuwa anafanana na mimi kwa kila kitu.

Siku, wiki na hatimaye miezi ilisonga na hatimaye ikatimia miezi saba tangu anizike. Akaanza kujihisi mchovu sana, miguu ikawa inavimba na presha ya damu yake ikawa juu. Alipopimwa madaktari waligundua kuwa zilikuwa dalili za awali za kifafa cha mimba, kwa kitaalamu tatizo hilo liliitwa EPH Gestosis au Pre-Eclampsia.

Ni katika wakati huo ndipo Mchungaji Ngelela alipomtuma Mama Mchungaji kwenda Kahama kumfuata na kisha wakaenda Dodoma ambako walikaa naye na kumfanyia maombi maalumu ili kumwepusha na roho ya mauti.

Sasa ikaja siku ambayo akiwa chumbani kwake alfajiri alihisi maumivu makali ya tumbo, akajitahidi kuyavumilia akisubiri asubuhi ifike lakini hali ilizidi kuwa mbaya sana, akaanza kutapatapa.

Alijaribu kuinuka toka kitandani lakini alihisi kizunguzungu kikali na ukungu mzito ukitanda machoni kwake, akafinya macho yake huku akiyafumba. Zikapita dakika kadhaa akiwa katika hali ya kukosa matumaini. Hata hivyo, hakutaka kuruhusu hali ile ya kukata tamaa, akakusanya nguvu zake zote na kuinuka huku akipeleka mkono wake wa kushoto kushika ukuta alioutumia kujiegemeza ili asidondoke.

Na kwa kutumia mkono wake wa kulia alijikunja na kushika tumbo lake lililoendelea kuuma. Akiwa bado kafumba macho alikunja uso wake akizidiwa na maumivu makali ya tumbo yasiyokoma.

Endelea...
 
Mgeni mwema.jpg

196

Kisha alishusha pumzi ndefu za ndani kwa ndani na kujilazimisha kutembea akielekea mlangoni lakini akahisi miguu yake ikiishiwa nguvu na matone ya majimaji yalikuwa yakidondoka kwenye miguu yake. Alisimama na kuangalia miguu yake, akayaona matone ya damu yakidondoka sakafuni. Alishtuka sana na kufinya uso wake akiwa katika maumivu makali.

Tumbo lake sasa lilikuwa linauma sana kama vile kulikuwa na kitu kilikuwa kinalazimishwa kutoka, kwa kuwa hapakuwa na mtu mwingine mle chumbani alitamani kupiga kelele ili kuomba msaada lakini hakuweza. Moyo wake ulishikwa na mfadhaiko na ulianza kwenda mbio isivyo kawaida.

Kutokwa na damu kulimfanya ahisi kuwa alikuwa mbioni kumpoteza mtoto aliye tumboni kwake, na hivyo, kwa sekunde chache alijikuta akiyasahau maumivu yake na jasho jepesi lilianza kumtoka sehemu mbalimbali za mwili wake. Aliogopa sana. Alihisi pumzi zikimpaa na maumivu ya tumbo yakianza tena na kuzidi kuwa makali zaidi na zaidi. Maumivu yale yalianza kusambaa katika eneo lote la tumbo, kifuani hadi mgongoni.

Aliyasikilizia mapigo ya moyo wake, ambayo kwa wakati huo yalionekana kwenda kasi zaidi. Akaanza kuona kizunguzungu na ukungu mzito kuanza kutanda machoni kwake. Alijaribu tena kufungua mdomo wake ili kuita lakini sauti yake ilikuwa haitoki. Akayakodoa macho yake lakini ukungu uliotanda kwenye macho yake ulimfanya kutoona chochote.

Sasa moyo wake ulikuwa unakwenda mbio na kuunguruma sana kama uliokuwa unapambana na kazi isiyo ya kiasi chake na hatimaye shughuli mbalimbali za mwili wake nazo alizihisi kuwa zilikuwa mbioni kusitisha utendaji wake. Alipojaribu kupiga hatua alijikuta mwili wake ukilegea na hapo akapiga mweleka na kuanguka sakafuni, akaanza kugaagaa kwa maumivu ya tumbo.

Lakini bado hakutaka kushindwa, alikusanya nguvu zake zote ili ainuke lakini alishindwa, alibaki kutapatapa huku akiwa hana msaada wowote. Alijaribu tena kutoa sauti ya kuomba msaada lakini haikutoka. Baadaye, kwa mbali, alisikia sauti ya Grace akigonga mlangoni. Hapo alijiwa na matumaini kidogo, akakusanya tena nguvu zake zote akitaka ajiinue na kusimama lakini hakuweza.

Alikusanya nguvu zake zote ili apige kelele lakini sauti yake haikutoka na badala yake aliishia kukoroma tu, na taratibu fahamu zake zilianza kumtoka taratibu. Sekunde chache baadaye hakuweza kufahamu kilichoendelea hadi siku ya pili alipojikuta akiwa wodini, katika wadi maalumu ya wajawazito walio katika hatari kubwa kwenye Hospitali ya Benjamin Mkapa.

Hapo hospitalini alikuwa amepewa matibabu ya awali na kutakiwa kupumzika muda wote hadi siku ya kujifungua, yaani ‘total bed rest’

Simulizi hiyo ya Rehema ilinifanya nihisi uchungu mkubwa sana ukinikaba kooni. Muda wote akisimulia nilikuwa namtazama kwa namna ambayo ilianza kumtisha yeye mwenyewe.

“Mbona unanitizama hivyo, Baba Junior?” kuna wakati Rehema aliniuliza kwa wasiwasi huku akinitazama machoni.

“Dah! hakika Mungu bado anatulinda sana, mke wangu,” nilisema kwa namna ya kumshukuru Mungu kisha nikashusha pumzi ndefu na kuongeza, “Katika kipindi cha miezi tisa wote wawili tumepitia mitihani mikubwa sana lakini tumeshinda.”

“Basi, wakati nikiwa wodini ikaja siku ambayo shangazi Mama Mchungaji alikuwa ananiandalia chakula kwenye sahani… ulikuwa mchemsho wa kuku wa kienyeji na ndizi za Bukoba, nakumbuka ilikuwa majira ya saa moja jioni…” Rehema alisema na kusita kidogo, akatazama juu kama aliyekuwa anavuta kumbukumbu.

“Kisha Mama Mchungaji alinikaribisha chakula na yeye kutoka nje, nilipoanza tu kula nikahisi maumivu makali sana ya tumbo na kiuno. Maumivu yale yalikuwa yameanza polepole tangu asubuhi ya siku hiyo na baadaye kuacha, na sasa yaliibuka tena na kuongezeka na kadri muda ulivyokuwa unaenda maumivu yalizidi kuwa makali zaidi, hasa kwenye tumbo na baadaye yalisambaa mpaka kiunoni,” Rehema alisema huku akiuma midomo yake.

Alisema kuwa maumivu yale yaliambatana na mkazo wa tumbo na ukali wake ulikuwa unaongezeka kadri muda ulivyozidi kwenda, kisha hali ile ya maumivu na mkazo ilianza kushuka kuelekea kiunoni. Na hapo akaanza kuugulia na kushindwa kula. Alifungua mdomo ili amwite Mama Mchungaji aliyekuwa ametoka kidogo lakini sauti ikagoma kabisa kutoka.

Aliinuka kutoka pale kitandani lakini aliishiwa na nguvu mwilini na kuanguka sakafuni, akaangukia tumbo pale sakafuni na kutoa yowe dogo kwa sauti dhaifu. Macho yake taratibu yalianza kupoteza nguvu ya kuona. Na hatimaye shughuli mbalimbali za mwili wake nazo alizihisi kuwa zilikuwa mbioni kusitisha utendaji wake.

Muda huo Mama Mchungaji na Grace walikuwa wanaingia ndani na walimkuta katika hali ile, Mama Mchungaji akapiga yowe la hofu na wakati huo Grace alikimbia kwenda kuwaita wauguzi ambao walifika pale haraka. Rehema aliniambia kuwa japo alishindwa kuongea lakini muda huo alikuwa anasikia kila kitu na alitamani sana kufumbua macho yake na kushuhudia kilichokuwa kinaendelea pale lakini hilo halikuwezekana, kwani macho yake yalikuwa mazito sana.

Wauguzi walimbeba na kumpandisha kitandani na alipompimwa alikutwa akiwa na shinikizo la juu la damu la 160/110 mmHg lililoashiria hali ya hatari kwake na hata kwa mtoto aliyekuwa tumboni. Akiwa pale kitandani hajielewi vizuri, alisikia kwa mbali sauti ya Mama Mchungaji akiomba kwa uchungu.

Kwa mara nyingine tena alitaka ajiinue pale kitandani lakini hakuweza kwani taratibu fahamu zake zilikuwa zinamtoka. Muda mfupi baadaye hakuweza tena kujua kilichoendelea hadi alipokuja kuamka kutoka kwenye usingizi mzito wa nusu kaputi siku ya pili tangu alipopoteza fahamu. Aligundua kuwa alikuwa bado yupo katika ile ile wadi maalumu ya wajawazito walio katika hatari na sasa alikuwa amevalishwa mipira maalumu ya kumsaidia kupumua.

Pia alikuwa amewekewa vifaa maalumu vya kumsaidia kuchunguza mwenendo wa utendaji kazi wa moyo wake, kifaa hicho kinaitwa ‘Cardiac monitors’ na kingine cha kumsaidia kula chakula kinachoitwa ‘Nasogastric tube’. Na pia kwenye mkono wake wa kulia kulichomekwa sindano yenye mrija uliokuwa unatoa maji maalumu yaliyochanganywa na dawa kwenye chupa na kupeleka kwenye mishipa ya damu.

Baadaye alikuja kugundua kuwa alikuwa amejifungua, kwa njia ya upasuaji yaani ‘caesarian section’, mtoto wa kiume mwenye afya njema. Siku mbili baadaye jopo la madaktari kadhaa walipita katika wadi ile ili kujua maendeleo yake, wakagundua kuwa hali yake ilikuwa inaimarika taratibu na mwenendo wa mapigo ya moyo wake uliridhisha.

Waliamua kuiondoa ile mashine ya kumsaidia kupumua na kuacha ile ya kuchunguza mwenendo wa utendaji kazi wa moyo na kifaa cha kusaidia kula chakula kwa njia ya mrija. Lakini waliporudi siku iliyofuata waliviondoa vile vifaa baada ya kuridhika kuwa hakuwa tena katika tishio la mashambulizi ya moyo au kushindwa kupumua.

“Hata hivyo jambo lililonishangaza mno, huwezi kuamini… ni kuwa siku niliyojifungua ilikuwa ni tarehe ile ile uliyozaliwa wewe, yaani Machi 26!” Rehema alisema na kuachia kicheko hafifu. Kisha akaongeza, “Hapo ndo nilipopata wazo la kumwita mtoto wangu Jason Junior.”

Endelea...
 
Mgeni mwema.jpg

197

Dah! Wakati wote nilipokuwa namsikiliza Rehema nilijikuta nasisimkwa mno mwili wangu na damu ilikuwa inaenda kasi kwenye mishipa yangu ya damu. Nilijikuta nikiwa najenga picha akili kwangu iliyojitokeza mfano wa sinema ya kusisimua sana ya mwanamke aliyekuwa akipitia kipindi kigumu sana cha mateso baada ya kufiwa na mumewe…

Hata hivyo nilijitahidi kuyafukuza mawazo hayo toka akili kwangu kwani hiyo haikuwa picha ya kupendeza. Ilikuwa picha ambayo ingeweza kumtoa machozi mtu yeyote.

* * *



Saa 3:30 asubuhi…

Asubuhi ya saa tatu na nusu siku iliyofuata ilinikuta nikiwa nimeketi kwenye bustani, nyumbani kwa Mchungaji Ngelela, nikiwa nimezama kwenye lindi la mawazo na mambo niliyokuwa nayawaza ni yale aliyokuwa amenisimulia Rehema usiku wakati tukiwa chumbani kwetu. Nilimsifu sana Rehema kwa ujasiri aliouonesha kwa kipindi chote cha miezi tisa ya kutokuwepo kwangu.

Hata hivyo, kwangu, mambo yote niliyosimuliwa na Rehema yalikuwa bado yanazunguka kichwani kwangu kama vile nilikuwa natazama sinema ya kusisimua ambayo kuna wakati fulani ilihuzunisha sana na wakati mwingine ilisisimua au kuogofya sana.

Katikati ya mawazo hayo mara yakaibuka mawazo mengine… mawazo ambayo yalinifanya nizame zaidi kwenye lindi la mawazo. Si hivyo tu, pia yalionekana kuniogofya mno. Yalikuwa mawazo juu ya Zainabu, mwanamke niliyeishi naye mjini Kilosa wakati nikiwa nimepoteza kumbukumbu zangu na kuishi katika uhusika mwingine.

Kilichonifikirisha zaidi asubuhi hiyo ni suala la ujauzito alioubeba Zainabu. Na kwa kweli, bado niliendelea kujishangaa sana niliwezaje kuishi maisha ambayo sasa sikuwa nayakumbuka kabisa?

Uamuzi wowote, uwe mzuri au mbaya, ni jambo ambalo huamua kesho ya mtu. Kuna uamuzi ambao mtu hufanya huku akiamini fika kuwa ni sahihi lakini kesho yake akajikuta katika wakati mgumu wa kujutia… mimi pia nilikuwa kwenye wakati mgumu sana wa kuamua hatma ya jambo hilo na niliogopa kuchukua uamuzi ambao ningekuja kuujutia baadaye.

Hadi muda huo sikuwa nimemwambia chochote Rehema kuhusu ujauzito wa Zainabu japo alikuwa anafahamu kuwa nilipokuwa nimepoteza kumbukumbu zangu nilikuwa naishi na mwanamke mwingine. Alimfahamu hadi jina.

Sasa nilitamani sana jambo hilo liwe ndoto tu na hata wakati mwingine nilifikiria kuukana ujauzito huo, au pengine nimwambie Zainabu akautoe, lakini nilipokumbuka kuwa kushika ujauzito huo halikuwa kosa lake wala langu basi nilijikuta nikiishiwa na nguvu. Niliamini kuwa hapa duniani hakuna jambo linalotokea kwa bahati mbaya kwenye maisha, kila jambo huja kwa kusudi la Mungu.

Kwa maana hiyo mimi pia nilijikuta kwenye mkondo huo huo wa maisha kwa sababu tu iliandikwa hivyo na pengine maisha ndiyo yaliamua kunichagulia namna ya kuishi na hatimaye nikakutana na Zainabu!

Sasa nilianza kumhurumia sana Zainabu maana alionekana kuwa na bahati mbaya, alitarajiwa kupata mtoto mwingine asiye na baba… hapana, baba wa mtoto huyu mtarajiwa nilikuwepo ila huenda Zainabu angelazimika kumlea mwenyewe pasipo uwepo wangu japo ningelazimika kuhakikisha anapata matunzo.

Ama kwa hakika watu wengi huikosa furaha kwa sababu hawatambui kuwa ili uipate furaha iliyokamilika huna budi kuwapa furaha watu wengine wanaoihitaji. Niliwaza kuwa ili nami niipate furaha niliyoihitaji nilipaswa kumpa furaha Zainabu… mbona yeye alikuwa amejitahidi kwa kadri awezavyo kunipatia furaha katika kipindi chote nilichoishi kama Mgeni Mwema? Kwa hiyo hakupaswa kabisa kulipwa huzuni!

Nikiwa katikati ya lindi la mawazo nilishtushwa sana na mkono ulionigusa kwenye bega langu la kulia ukitokea nyuma yangu, nikageuza shingo yangu haraka kutazama upande ambao mkono huo ulitokea na hapo nikamwona Rehema akiwa amesimama akiniangalia kwa wasiwasi na kwa udadisi, japo tabasamu laini lilikuwa limechanua usoni kwake.

“Oh!” nilisema huku nikijipiga kofi dogo kwenye paji langu la uso, “Umenishtua sana!”

Rehema alinitazama usoni kwa kitambo fulani kisha akasema, “Nini tatizo hadi unazongwa na mawazo kiasi hiki!”

“Wala sina tatizo lolote,” nilisema kisha nikashusha pumzi za ndani kwa ndani.

Kumbe Rehema alikuwa amefika hapo bustanini muda mrefu na alinikuta nikiwa nimezama kwenye lindi la mawazo. Aliniambia kuwa alijaribu kuniita zaidi ya mara mbili lakini sikuonesha kumsikia kutokana na kuzama kwenye lindi la mawazo hadi akalazimika kunisogelea na kunigusa begani ndipo nikashituka.

Rehema aliendelea kunitazama usoni kwa udadisi pasipo kusema neno, alionekana kama vile alijaribu kuyasoma mawazo yangu. Nikashusha pumzi ndefu huku nikiyakwepa macho yake. Nilijiona ninaelekea kumkwaza sana mke wangu, mtu ambaye alikuwa makini, alinipenda, akanivumilia na kuniheshimu sana.

Nilijisikia vibaya sana kwa jinsi nilivyoshindwa kupata ufumbuzi juu ya hatma ya ujauzito wa Zainabu ili niweze kuendelea na maisha yangu kama ilivyokuwa hapo nyuma. Nilijikuta nikitamani kumwambia Rehema ukweli hata kama ni kwa kufumba fumba lakini nikasita sana japo Olivia alikuwa amenishauri nimwambie ukweli kwa kuwa halikuwa kosa langu.

“Baba Junior, naona kama unatatizwa sana na kusumbuliwa na mambo, sijui ni yale yale yaliyokutokea au una mengine? Hata hivyo kama unahisi huwezi kuniambia basi mwombe sana Mungu akupe nguvu,” hatimaye Rehema aliniambia baada ya kupitisha sekunde kadhaa za ukimya akiniangalia usoni. Kisha aliniacha akaelekea ndani.

Nami niliingia ndani, kisha nikaelekea chumbani na kujilaza kitandani, kando ya mtoto Jason Junior. Sikuwa na shughuli maalumu ya kufanya asubuhi hiyo. Nililala hadi ilipotimia saa 7:15 mchana nikajumuika na watu wengine mezani kwa ajili ya chakula.

Wakati nikiwa hapo mezani kwa chakula, bado mawazo kuhusu Zainabu yaliendelea kutawala akilini kwangu hasa umbali uliokuwepo kati yetu. Niliona Dodoma na Kilosa ni kama kutoka bara moja hadi jingine! Bila shaka Zainabu muda huo alikuwa anaongea na mwanaume mwingine nisiyemfahamu. Pengine alikuwa bado hajala hadi muda huo au alikuwa ameketi chumbani kwake, katika hali ya upweke, akiwazia hatma yake baada ya mimi kumtosa… Au alikuwa akiniwaza miye!

Nilikula taratibu, muda mwingi nilikuwa nakikodolea macho chakula, mawazo yangu yakiwa mbali na moyo ukinienda mbio. Sikujua kwa nini sasa nilianza kuguswa sana na maisha ya Zainabu tofauti na hapo mwanzo! Moyo ulikuwa unaniuma sana kuwa mbali na Zainabu, sijui kama ilikuwa ni huruma juu ya kile nilichoamini kuwa bahati mbaya kwake, au ni mapenzi yalianza kuchipuka ndani yangu juu yake!

Lakini nilihisi kuwa ilikuwa sababu ya huruma na ilikuwa imezidi hasa nilipokumbuka siku ile nilipokwenda nyumbani kwake kumuaga baada ya kutoka hospitali, machozi yalimtoka hasa nilipomwambia kuwa hisia zangu kwake hazikuwepo tena na ziliyeyuka pamoja na jina la Mgeni mfano wa theluji ichemshwayo.

Zainabu alikuwa ameniambia kuwa ulimwengu umekuwa tofauti kabisa! Umekuwa mkatili sana kwake kupita kiasi. Na kwamba alikuwa anashindwa kuvumilia maisha bila ya uwepo wangu…

Dah! Hakuna jambo ambalo sasa lilinihuzunisha kama kumbukumbu za kumshika na kumlaza kwenye mapaja yangu. Zainabu alilala pasipo kupinga na kufumba macho yake huku akilia kilio cha kwikwi, kisha alisema kuwa alitamani sana iwe ndoto kwa kuwa siku zote tuliishi kama mke na mume, kwa upendo, iweje nimwache katika mazingira yale wakati alishanibebea mtoto tumboni mwake!

Endelea...
 
Mgeni mwema.jpg

198

Sasa nilikuwa kilometa nyingi mbali naye na sikujua hali yake ilikuwaje huko Kilosa nilikomwacha. Japo Olivia alikuwa amenihakikishia kuwa baada ya kurudi Kilosa angejitahidi kuwa karibu na Zainabu lakini bado niliamini kuwa uwepo wangu ungekuwa muhimu zaidi kwa afya yake na ya mtoto wetu aliyemo tumboni.

Vipi kama huko nyuma nilikomwacha angeamua kufanya jambo la kijinga kwa kuutoa ujauzito huo na hatimaye kupata matatizo makubwa? Swali hilo lilinijia bila ya kutazamia, likauchoma moyo wangu. Nilishindwa kuendelea kula, nikaisukuma kando sahani ya chakula kwa ncha ya vidole vyangu.

Sasa mawazo juu ya Zainabu yalinijaa kichwani mwangu, yakivunja kila mfupa wangu na kuutia ganzi kabisa mwili wangu. Akili ilinizunguka, na taratibu machozi yakaanza kunilengalenga machoni.

Sasa nilimwona Zainabu akiwa kasimama mbele yangu akilia kwa huzuni, na sikio langu la mawazo lilikisikia kilio chake. Nilishindwa kuvumilia, nikainuka na kuelekea chumbani. Sikujua kuwa wakati yote hayo yakiendelea kwenye ubongo wangu, watu wengine pale kwenye meza ya chakula walikuwa wananitazama kwa umakini.

Siku hiyo sikupenda kwenda kokote. Nilipenda kubaki chumbani, kitandani, ili kuepuka maswali. Nilikuja kushtuka wakati saa ya ukutani ikigonga kuashiria kuwa ilikuwa imetimia saa 12:00 jioni.

Nilikuwa najihisi mchovu sana, huenda ni kwa sababu nilikuwa nimelala mchana kutwa. Niliondoka hapo kitandani, nikaingia bafuni kujimwagia maji kisha nikatoka na kuelekea nje, halafu nikaenda kuketi bustanini. Nikaanza kujiuliza lipi la kufanya. Nitoke nikatembee mjini? Nimpigie simu Olivia ili kujua kama alikwena kuonana na Zainabu? Au nifanye nini?

Ilinishangaza sana, Zainabu niliyemkana pale hospitali alipokuja kuniona, nikimwambia kwamba simjui, iweje sasa alikuwa ametawala mawazo yangu? Nilipokuja kuzinduka kwenye mawazo yangu niliitazama saa yangu ya mkononi iliyonionesha kuwa ilishatimia saa 12:50 jioni. Nikawaza labda Olivia angenipigia simu muda wowote kwani alikuwa ameondoka asubuhi ya siku hiyo kwenda Kilosa.

Niliendelea kuitazama saa yangu mpaka mishale ifike kunako saa 1:00 jioni. Bila ya sababu, moyo wangu ulikuwa ukinidunda sana. Saa moja ilifika, na hatimaye dakika ya kwanza ilipita, ya pili… ya tatu! Sikujua nilichokuwa nikikisubiri. Simu ya Olivia? Hapana… huenda nilitamani zaidi kuisikia sauti ya Zainabu mwenyewe au pengine kumwona akiwa amesimama mbele yangu!

Moyo ulipasuka niliposikia simu ikiita mlio hafifu, nikaangalia lakini namba ilikuwa ngeni, niliipokea na kwa sauti ya kutetemeka nikasema, “Hallo!”

“Jason!” ilikuwa sauti ya mwanamume, nikashusha pumzi.

“Ndiyo… sijui nani mwenzangu?” niliuliza kwa shauku.

“Baba yako! Ndiyo kusema sauti yangu hauitambui? Au bado kumbukumbu zako hazijarudi sawa sawa!” Baba aliniuliza, sauti yake ilionesha kuwa alikuwa na wasiwasi.

“Oh! Baba! Samahani…” nilinyamaza kidogo kisha nikasalimia, “Shikamoo!”

“Marhaba!” Baba aliitikia. Kisha kikazuka kimya cha muda mfupi kabla hajauliza, sauti yake bado ilionesha kuwa alikuwa na wasiwasi, “Vipi, kwema huko?”

“Huku kwema tu, sijui huko Tabora?” niliitikia huku nikiuma midomo yangu.

“Una uhakika huko ni kwema? Mbona nimeambiwa kuwa tangu asubuhi hauko sawa! Umekuwa mkimya sana, siku nzima unajitenga tu na kuongea peke yako, na wakati mwingine unatokwa na machozi! Kwani una tatizo gani, mwanangu?” Baba aliniuliza.

“Sina tatizo lolote, Baba,” nilimjibu huku nikishusha pumzi.

“Niambie tu kama una tatizo nione namna ya kukusaidia, mimi ni zaidi ya baba yako… mimi ni rafiki yako,” Baba alisema.

Niliyazungusha macho yangu kutazama huku na kule ili kuona kama kulikuwa na mtu mwingine eneo lile ambaye angeweza kuyasikia mazungumzo yetu. Hakuwepo.

Nikamsimulia Baba kwa kifupi kile kilichokuwa kinaitatiza akili yangu siku hiyo hasa kuhusu ujauzito wa Zainabu. Baba alicheka kidogo na kunitoa wasiwasi kuwa jambo hilo halikupaswa kuniumiza kichwa, aliniambia kuwa mke wangu Rehema alikuwa mwanamke mwelewa sana na kwamba nitafute muda mwafaka nimwambie ukweli kwani ni ukweli pekee ambao ungeniweka huru. Kisha aliahidi kunipigia simu siku iliyofuata ili tuongee zaidi. Halafu akakata simu.

* * *



Saa 5:30 usiku…

“Hivi una tatizo gani, Baba Junior? Leo tangu asubuhi nakuona hauko sawa!” Rehema aliniuliza huku akinitazama usoni. Muda huo tulikuwa kitandani, chumbani kwetu. Rehema alikuwa amelala pembeni yangu.

Nilimtazama kwa sekunde kadhaa pasipo kumjibu, swali lake lilikuja baada ya muda mrefu tangu tulipopanda kitandani kulala. Muda mwingi alikuwa mkimya. Lakini hatimaye alishindwa kuvumilia. Lilianza kuwa saa moja, kisha likafuata la pili na zilipofika tatu subira yake ikawa imefikia kikomo.

Siku zote ukweli humweka mtu huru, lakini pia yapo mazingira ambayo ukiutanguliza ukweli basi unakuwa mwanzo wa kuwa mtumwa, na ukiuficha ukweli huo huo unakuangamiza kabisa! Je, kipi bora: kuwa mtumwa ama kuangamia? Nilijiuliza. Sasa sikuona kama lilikuwa jambo la busara sana kuendelea kukaa kimya, ilikuwa heri nimwambie ukweli Rehema. Lakini kabla sijaufungua mdomo wangu kusema Rehema akaniwahi.

“Jason Sizya!” sasa aliniita kwa jina langu.

“Naam!” niliitika huku nikimtazama kwa umakini.

“Wewe ni mwanamume wa kipekee maishani mwangu...” Rehema alisema huku akilazimisha tabasamu. “Tafadhali, ila kama utaona inafaa nieleze kuhusu kinachokusumbua.”

“Ndiyo nataka kukueleza,” nilimwambia. “Kwa kweli niliyopitia ni mengi sana… nakusihi ukubaliane tu na kile utakachokisikia kwa sababu hata nisipoyasema leo ndo tayari yameshatokea na hayawezi kubadilishwa!”

Rehema alinitazama tu pasipo kusema neno, alisubiri kusikia kile kilichonitatiza muda wote. Nikashusha pumzi na kumweleza kuhusu ujauzito wa Zainabu na jinsi nilivyotatizika na jambo hilo.

Nilitegemea kumwona Rehema akishtuka baada ya kusikia suala la ujauzito lakini hakuonesha kushtuka na badala yake alikaa kimya kwa kitambo kirefu pasipo kuonesha tashwishwi yoyote usoni, macho yake yaliangalia juu huku akiwa mtulivu sana. Sikujua alikuwa anawaza nini! Baada ya kitambo hicho cha ukimya nilimwona akinitazama na kuachia tabasamu laini.

“Hicho ndo kilikuwa kinakutatiza muda wote?” Rehema aliniuliza kwa sauti tulivu huku tabasamu likizidi kuchanua usoni kwake.

“Ndiyo,” nilijibu kwa kifupi.

Okay!” Rehema aliongea kwa utulivu na kuongeza, “Usijali… najua kila kitu ila usiniulize nimejuaje.”

Nilishtuka sana kugundua kuwa Rehema alikuwa anajua kila kitu. Zaidi ya mshtuko ule nilijikuta nikishangaa sana na nikajiuliza huyu Rehema alikuwa na nini hasa? Iweje siku zote alionekana kuwa hatua moja mbele yangu? Kila nilichodhani hakijui kumbe alikuwa anakijua na wala hakuonesha dalili yoyote ya kwamba alikijua! Uso wangu ulionesha maumivu makubwa, nilifungua mdomo wangu kutaka kusema neno lakini maneno yakawa hayatoki.

“Najua umepitia mengi magumu, na hili si kosa lako kwa hiyo hukuwa na sababu ya kuhofia chochote kilichotokea katika kipindi hicho, kama niliweza kuyavumilia yote wakati ule wa uhusiano wetu basi nipo tayari kumpokea mtoto atakayezaliwa kwa mikono miwili kwani ni zawadi toka kwa Mungu,” Rehema aliongeza huku tabasamu laini likiendelea kuchanua usoni kwake.

Nilibaki kimya nikiwa sijui niseme nini, nilianza kujiona mjinga sana.

* * *

Endelea kufuatilia hadi mwisho...
 
Mgeni mwema.jpg

199

Wewe wifi jamani…




Saa 3:15 asubuhi…

ZILIKUWA zimepita wiki tatu tangu nilipozungumza na Rehema kuhusu suala la ujauzito wa Zainabu, na Rehema alikuwa amenisihi niwe na subira kwani baada ya kutimiza siku arobaini tangu alijifungue, na kabla ya kurudi Kahama, tungesafiri pamoja kuelekea Kilosa ili kumwona Zainabu. Sasa nilikuwa mtu mwenye furaha na kila mtu pale nyumbani alilibaini hilo.

Asubuhi ya siku hii nilikuwa nimeamka mapema kama ilivyokuwa kawaida yangu, nikafanya mazoezi madogo madogo ya mwili, kisha… sikuwa na shughuli nyingine maalumu ya kufanya. Nilikwenda stoo nikachukua guduria la maji na kuelekea bustanini, nikamwagilia bustani.

Tangu siku nilipoliweka wazi suala la ujauzito wa Zainabu na kila mwanafamilia akajua, niliichukulia bustani hiyo kama sehemu ya majukumu yangu. Siku zote niliamka mapema nikimwacha Rehema bado amelala kitandani na kumwagilia maji japokuwa watu wengine walijaribu kunisaidia nyakati zingine, ila kwa kipindi chote hicho jukumu lote la utunzaji wa bustani hiyo ni kama lilikuwa mikononi mwangu.

Nilifanya hivyo kwa furaha kabisa, asubuhi na wakati mwingine hata jioni. Sasa bustani ilipendeza sana.

Kwenye saa 2:10 asubuhi nilirudisha guduria stoo, nikafunga mlango na kuelekea chumbani, niliichukua simu yangu iliyokuwepo juu ya meza ndogo ya vipodozi na kutazama kama kulikuwa na mtu yeyote aliyekuwa amenitafuta wakati nikishughulika na bustani.

Ni kweli, kulikuwa na miito miwili ya simu zilizopigwa pasipo kujibiwa yaani ‘missed calls’ kutoka kwenye namba moja ngeni, nilijaribu kuifikiria ile namba lakini sikuweza kuifahamu, nikashusha pumzi na kuirudisha simu juu meza nikipanga kumtafuta mtu huyo baadaye, kisha niliingia bafuni nikajimwagia maji. Nilipotoka humo nilijiandaa na kutoka huku nikiisahau ile simu pale pale juu ya meza ya vipodozi.

Wakati inatimu saa 3:15 asubuhi nilikuwa mezani nikinywa chai taratibu huku nikiongea mawili matatu na mjomba, Mchungaji Ngelela. Mara nikamwona Rehema akinijia haraka akiwa ameshika simu yangu na kunipa. Simu ilikuwa imetoa mlio ulioashiria kuwa ujumbe ulikuwa umeingia. Nilipoitazama vizuri nikagundua kuwa kulikuwa na miito mingine miwili ya simu zilizopigwa kutoka kwenye namba ile ile ngeni, na zaidi kulikuwa na alama ya ujumbe wa sauti (voicemail) iliyokuwa imetumwa kwenye simu yangu, ujumbe huo ulikuwa umetoka kwenye namba ile ile ngeni ambayo sikuifahamu.

Nikaamua kuufungua kwanza ule ujumbe na kuusikiliza kabla sijapiga simu. Ujumbe huo ukanifanya nihisi kichwa changu kikizunguka.

“Mgeni mume wangu, kwanza naombe radhi kwa sababu nitaendelea kukwita kwa jina la Mgeni…” Sauti ya Zainabu ilisikika ikizungumza kwenye ujumbe huo wa sauti, alikuwa analia. Nikamtupia jicho Rehema na kugundua kuwa hata yeye alikuwa makini kusikiliza huku akinitazama.

“Kumbuka nilikwambia kuwa ukiniacha ulimwengu utakuwa mkatili sana kwangu kupita kiasi. Nimeshindwa kuvumilia maisha haya bila wewe na sina imani tena kama nitakuona… ili nisiendelee kuwa chukizo machoni mwako, wacha nikawafuate wazazi wangu huko kaburini ili huu mzigo nilio nao usiubebe. Acha nife, Mgeni… acha nife kwa ujinga wangu…”

Ujumbe huo wa sauti haukunishtua mimi tu, ulimshtua kila mtu, ukabadili kila kitu, hapakuwa na mazungumzo tena. Nilijikuta nikipagawa, hata Rehema naye ujumbe huu ulionesha kumvuruga sana!

“Baba Junior, mpigie simu huyo mwanamke… mpigie simu tafadhali na umwambie asifanye hivyo, asijiue,” Rehema alinisisitiza huku akionesha kuchanganyikiwa.

Pasipo kujiuliza mara mbili niliipiga ile namba, nilijihisi nina hatia kubwa na iwapo ingetokea kwamba Zainabu angejiua kwa namna yoyote basi nilikuwa nahusika. Hata hivyo, baada ya kuipiga ile simu nilichokisikia kwenye simu kilinifanya niishiwe na nguvu. Namba ile iliyotuma ujumbe wa sauti ilikuwa haipatikani!

Nilijikuta naishiwa nguvu na kukaa sakafuni kama mtoto mdogo. Rehema na Mchungaji Ngelela walibaki kunikodolea macho huku wamepigwa na butwaa.

“Hebu mpigie simu Olivia umwambie awahi nyumbani kwa Zainabu,” Rehema alinishauri. Nikaipiga namba ya Olivia. Maajabu mengine… pia ilikuwa haipatikani!

“Jason, hapa hakuna kusubiri… jiandae tunaenda Kilosa,” Rehema alisema kijasiri.

* * *



Saa 6:16 mchana…

Tulikuwa ndani ya gari la kifahari aina ya Toyota Landcruiser GX V8 la rangi nyeusi tulilopewa na Mchungaji Ngelela. Tulikuwa tumeshakwenda zaidi ya umbali wa kilometa 130 kutoka Dodoma na tulishatumia zaidi ya saa moja na ushee tangu tuianze safari yetu. Muda huo tulikuwa tumefika Gairo na sasa tulianza kuitafuta Dumila.

Mwendo wangu ulikuwa wa kasi ila wa uhakika na nilikuwa makini huku nikishuka mabonde na kupanda milima katika baadhi ya maeneo na kukatisha kwenye sehemu zenye makazi ya watu. Kwa mwendo wangu, nilikuwa nimetenga fedha kwa ajili ya askari wa usalama barabarani iwapo wangetuzuia njiani.

Ndani ya gari hilo tulikuwa watu watatu; mimi, Grace aliyekuwa ameketi kiti cha mbele na Rehema aliyeketi kiti cha nyuma akiwa amempakata Junior. Lengo letu lilikuwa moja tu; kuokoa kwanza uhai wa Zainabu kisha tungepata uamuzi baada ya kufanya jambo hilo. Muda wote nilikuwa katika mduwao, sikuwa nimetegemea kupata habari hizo. Ni kama nilikuwa ndotoni. Ndoto ya mchana!

Rehema na Grace wakiwa wamefunga vyema mikanda walikuwa wanatetemeka. Roho mkononi. Niliwaona wakinitazama kwa macho yaliyokuwa yakinisihi nipunguze mwendo lakini nilihisi kila walipoikumbuka roho ya Zainabu wakaiona ni ya umuhimu zaidi.

Uzuri wa barabara ya kutoka Dodoma kuelekea Morogoro na kisha barabara ya Kilosa ilikuwa nzuri ikiwa na lami mwanzo mpaka mwisho. Nikiwa katika usukani nilijikita katika kutafuna bazoka, sikuwa na jingine nililofanya zaidi ya kuwa makini katika usukani. Barabara ililalamika kadri mwendo wa gari letu ulivyokuwa unaongezeka. magurudumu madhubuti yaliitesa lami ile.

Tulipofika katika mji mdogo wa Dumila tulipinda na kuingia kulia tukaifuata barabara ya Kilosa tukipita Magore Estate na Kitete, na wakati tukianza kuitafuta Msowelo tukapishana na basi la Mwendapole Express lililokuwa linafanya safari zake kati ya Kilosa na Gairo.

Hadi inatimu saa 7:50 mchana tulikuwa tunaingia Kilosa. Tulikuwa tumetumia takriban saa tatu na ushee kutoka Dodoma hadi Kilosa. Moja kwa moja tukaelekea eneo la Kichangani nyumbani kwa Zainabu. Uzuri barabara ya kuelekea huko nilikuwa naikumbuka. Ni hapo nyumbani kwake tuliamua kuanzia.

Hatimaye tuliifikia nyumba ya Zainabu. Nyumba ilikuwa imetulia sana ikiwa haina dalili za uwepo wa mtu. Nyumba ilinuka harufu ya ukiwa! Nilishuka haraka na kwenda kugonga mlango. Nyumba ilikuwa imefungwa. Nikaenda kwenye nyumba ya Jirani na kuwauliza majirani lakini hawakuwa na habari zozote za wapi alikoelekea Zainabu.

Nilibaki nimekodoa macho yangu nikimtazama yule jirani bila kujua nini cha kufanya. Nilitamani kusema lolote lakini sauti yangu ikakwama. Nilibaki nimeduwaa kama punguwani hadi pale nilipozinduliwa na mkono wa Grace ulionishika kwenye bega.

“Vipi, kuna taarifa gani?” Grace aliniuliza huku akiwa na wasiwasi.

“Hayupo nyumbani kwake na hakuna mwenye taarifa zake,” nilisema kisha tukaongozana hadi kwenye gari letu huku tukimwacha yule Jirani akitusindikiza kwa macho yaliyojaa wasiwasi.

Endelea...
 
Mgeni mwema.jpg

200

Sasa safari ikawa kuelekea nyumbani kwa Almasi. Sikuikumbuka vyema nyumba aliyoishi Almasi lakini uzuri nilifahamu aliishi eneo gani. Bahati nzuri Almasi alikuwa mtu maarufu eneo lile hivyo haikuwa tabu kuipata nyumba aliyokuwa akiishi.

Ilikuwa nyumba kubwa yenye wapangaji wanne. Nikaisogelea na kubisha hodi. Niligonga mara tatu pasipo kuitikiwa, nikaanza kukata tamaa na kugeuka kuwatazama Grace na Rehema waliokuwa wamesimama nyuma yangu wakiwa na wasiwasi.

“Nahisi hata hapa hakuna mtu ndani,” nilisema huku nikiwaashiria tuondoke ingawa sikujua tungeelekea wapi baada ya hapo.

“Habari zenu?” tuliisikia sauti ikitusalimia kutokea nyuma yetu. Tuligeuka na kumwona mwanamume mrefu aliyekuwa amevaa suruali ya dengrizi na shati la batiki, na hapo nikamtambua kuwa alikuwa ndiye Almasi. Alikuwa amebeba mfuko mweusi.

“Oh, Almasi! Afadhali umetokea maana tumegonga sana mlango bila mafanikio, tulikuwa karibu kukata tamaa,” nilisema kwa furaha.

Almasi alinitazama kwa umakini akaonekana kunitambua. Nikauona uso wake ukichanua tabasamu pana la furaha, na wakati huo huo mlango wa mbele wa ile nyumba ukafunguliwa, na msichana mmoja akachungulia nje, alipotuona tukiwa na Almasi akarudi ndani haraka.

“Daah! Mgeni!” Almasi aliita kwa mshangao huku akinitazama usoni kisha alinikumbatia kwa furaha.

“Aliyekuwa Mgeni ila kwa sasa ni Jason,” nilimjibu kwa utani huku nikiachia kicheko hafifu.

Almasi naye alicheka huku akigeuka kuwatazama Grace na Rehema kisha macho yake yakaelekea kwenye gari lililokuwa limeegeshwa kando ya barabara. Nikamtambulisha kwa Rehema na Grace, na hapo nikaona uso wake ukichanua kwa tabasamu pana huku akibetua kichwa chake.

I see…! Karibuni ndani,” Almasi alisema huku akiufungua mlango mkubwa wa kuingilia kwenye nyumba hiyo.

“Ahsante ila kwa leo sisi si wakaaji… tumekuja mara moja tunahitaji msaada wako,” nilisema na kushusha pumzi za ndani kwa ndani. kisha nikaongeza, “Tumekuja kwa dharula baada ya kupokea ujumbe wa sauti toka kwa Zainabu.”

Nilimwambia Almasi kisha nikaufungua ule ujumbe uliotumwa na Zainabu kwenye simu yangu, akausikiliza na kutaharuki sana.

“Basi ngoja niweke huu mzigo wangu ndani kisha twende tukamtafute,” Almasi alisema na kuingia ndani haraka pasipo kusubiri. Baada ya muda mfupi alitoka akiwa ameongozana na msichana mmoja ambaye nilimtambua mara moja. Alikuwa mchumba wake na aliitwa Sofia.

“Dah, hapa kuna maelezo nimeyapata, yanatatanisha kidogo, labda Sofia mwenyewe awaeleze,” Almasi alisema.

Kimya kilitanda, hakuna aliyesema neno bali tulisubiri kusikia toka kwa Sofia, akili zetu tuliziandaa kupokea taarifa yoyote, iwe nzuri au mbaya, kutoka kwa Sofia huku nikihisi mwili wangu ukifa ganzi.

Sofia alitueleza kwamba ni kweli Zainabu alikusudia kujiua kwa kuwa alikuwa amekata tamaa ya maisha na kwamba asingeweza kuishi na mtoto wake tumboni iwapo mwanaume aliyemtegemea aliamua kuwa mbali naye. Kwake, kuachwa si kioja kama angelipewa muda wa kusema na nafsi yake ila kumwacha katika mazingira yale ilikuwa sawa sawa na kuachwa na dunia nzima. Asingeweza kuishi.

Aliwafikiria wazazi wake, akamfikiria kaka yake na mwisho akamfikiria mama yake mlezi na kujikuta akiwaza kujumuika nao. Mawazo yakatulia, jeraha la hisia likachachamaa. Likaanza kumchokonoa katika namna inayokera. Machozi yakatiririka. Ni heri machozi hayo yangetiririka mashavuni huenda angeweza kuyafuta, lakini machozi hayo yalitiririka katika moyo wake mpweke.

Akajiuliza nani wa kumfuta machozi hayo wakati wa kumfuta alikuwa katika kifua cha mwanamke mwingine huku akimsahau yeye na mtoto aliyembeba tumboni? Hisia zilimtuma hivyo! Akajikuta akipagawa. Nyumba haikuwa inakalika tena.

Akawa na wazo moja tu kumpigia simu mwanaume ampendaye huku akipanga kueleza jinsi alivyokuwa akipitia maisha magumu pasipo uwepo wa mwanaume huyo, ambaye ni mimi. Alipopiga simu iliita, tofauti na matarajio yake kuwa simu ingepokelewa lakini hali haikuwa hivyo. Simu iliita hadi ikakata pasipo kupokelewa. Akapiga mara ya pili ikaita tena.

Zainabu akaanza kutokwa jasho, mshawasha wa kusikia sauti yangu au ya mke wangu Rehema ikiongea kwenye simu ile ukampanda lakini bado simu haikupokelewa.

Zainabu aliamua kuwa na subira sana, alipiga tena simu baada ya saa mbili lakini bado simu iliita tu pasipo kupokelewa, na sasa subira yake ilifikia kikomo baada ya kuhisi kuwa nilikuwa naitazama tu simu yake jinsi inavyoita na kuipuuzia bila kuipokea.

Sasa alikuwa amechanganyikiwa, alitembea huku na kule, na mwisho akaamua kutuma voicemail yaani ujumbe wa sauti, akaweka simu katika spika za nje na kurekodi ujumbe wa sauti alioutuma kwangu… katika ujumbe huo aliamua kusema kile ambacho nafsi yake ilimtuma kusema. Na baada ya ujumbe huo akajiona hana maana yoyote ya kuendelea kuishi duniani. Angeishi vipi iwapo nilikuwa sitaki kuwa naye? Angeishi vipi iwapo…

Sofia alitwambia kuwa aliyajua hayo baada ya kupita nyumbani kwa Zainabu na kumkuta akijiandaa kuondoka nyumbani kwake baada ya kuutuma ujumbe huo wa sauti akiwa na jambo moja tu, atoweke na kwenda kusikojulikana akiwa na wazo moja tu la kujiua. Alikuwa ameamua kujiweka mbali na dunia!

Sofia alimsihi sana asifanye hivyo, japo ilikuwa vigumu kukubaliana naye lakini hatimaye alifanikiwa kumshawishi. Mwishowe Zainabu alipata wazo la ghafla ambalo aliamua kulifanyia kazi, wazo ambalo pia lilikubaliwa na Sofia. Kwani nyumba yake haikuwa inakalika.

Sasa aliamua kusafiri kuelekea huko huko Dodoma aliko mwanamume wa maisha yake ili akajue mbivu na mbichi. Zainabu alianza kujiona mjinga sana kuwaza kujiua. Angejiua vipi amwachie mwanamke mwenzake mwanaume? Ingekuwa aibu ya karne!

Sasa aliamua kukipigania kile alichokipenda. Hakujali kama yeye alikuwa mwizi au mvamizi, aliamini anazo haki zote za msingi kwa kuwa alikuwa amebeba ujauzito wa mwanaume huyo, basi!

Safari yake ikaishia katika kituo cha mabasi cha Kilosa akisindikizwa na Sofia, hapo akabahatika kukuta basi la Mwendapole Express lililokuwa linaondoka muda huo kwenda Gairo. Aliamua apande Mwemdapole Express na kwenda kushuka Gairo ambako ingekuwa rahisi kupata mabasi ya kwenda Dodoma.

Lilipotajwa basi la Mwendapole Express mimi na Grace tukatazamana. Nikakumbuka kuwa basi hilo tulipishana nalo katikati ya Kitete na Msowelo wakati tukielekea Kilosa. Kufikia hapo wote tulijikuta tumechoka. Sasa kazi ikawa ni kuwahi Gairo ambako tulipanga kubahatisha kama tungemwona na tukimkosa basi turudi Dodoma.

_____

Endelea...
 
Mgeni mwema.jpg

201

Saa 9:15 alasiri…

Nililiondoa gari, tukaingia barabarani tayari kwa safari ya kurudi Dodoma. Safari hii ndani ya gari aliongezeka mtu mwingine, Almasi, ambaye aliketi kiti cha mbele huku Grace na Rehema wakikaa viti vya nyuma.

Kabla hatujaianza rasmi safari yetu ya kurudi Dodoma nililiingiza kwanza gari katika kituo cha mafuta. Mafuta yakajazwa. Kisha nikaingia kwenye super market ya hapo hapo kwenye kituo cha mafuta, nikanunua maji, vitu vya kutafuna, soda za take away na Energy kadhaa. Pia sikusahau kuchukua Savanna tatu.

“Nipeni saa tatu tu tutakuwa Dodoma,” niliwaambia huku nikifunga mkanda.

“Ila angalia tu tusije tukaishia mortuary,” Grace alisema kwa utani.

“Wewe wifi jamani… maneno gani hayo lakini?” Rehema aling’aka huku uso wake ukionesha wasiwasi mkubwa.

Nililiondoa gari na kuliingiza barabarani. Mwendo wangu ulikuwa wa kasi ila wa uhakika na nilikuwa makini, bado sikuwa najali hata kidogo kuhusu askari wa usalama barabarani kwa kuwa nilikuwa nimetenga fedha kwa ajili yao.

Nikafanya kosa, tulipokuwa tunavuka Dumila tukielekea Dodoma, nje kidogo ya Dumila tuliwakuta askari watatu wa usalama barabarani, mmoja wao alijaribu kutusimamisha, nikamvuka bila kusimama. Hao tukaendelea na safari yetu huku nikijiona mshindi.

Tulipokuwa tukiingia Gairo ilikuwa imetimia saa 11:25 jioni, haraka nikapunguza mwendo wa gari baada ya kukiona kizuizi cha barabarani na kisha askari wawili wakajitokeza mbele yetu na kusimama katikati ya ile barabara huku wakituonesha ishara kwa mkono kuwa tusimame. Nilipowatazama vizuri nikaona kuwa mikono yao ilikuwa imekamata vyema bunduki aina ya SMG.

“Msala huo…” Almasi alisema huku akionekana mwenye wasiwasi.

Wakati nikipunguza zaidi mwendo na kujiandaa kusimama mara nikawaona askari wengine wawili wakijitokeza na kujongea katikati ya ile barabara kisha wakasimama nyuma ya kizuizi kilichokuwa katikati ya ile barabara.

Nililisimamisha gari letu kando kando ya barabara, nikawatazama vizuri wale askari huku roho yangu ikinidunda kwa nguvu. Sikushuka, niliamua kubaki ndani ya gari kisha nikashusha kioo cha dirishani kwangu huku nikijiandaa kutengeneza tabasamu la kirafiki pindi askari mmoja akinifikia.

“Unatoka wapi na unaelekea wapi?” askari mmoja ambaye alikuwa na cheo cha Koplo aliniuliza baada ya kunifikia huku akiwa amenikazia macho usoni.

“Natoka Kilosa naelekea Dodoma… Vipi kuna tatizo lolote?” nilimuuliza yule askari kwa kujiamini huku nami nikimkazia macho.

“Kwa nini hujasimama uliposimishwa huko Dumila?” aliniuliza huku akiendelea kunikazia macho yake pasipo kupepesa.

“Sijaona kama tulisimamishwa mahali. Kama ningesimamishwa kwa nini nisisimame?” nilisema kwa sauti tulivu huku nikimtazama yule askari usoni.

Wakati huo huo askari mwingine aliyekuwa na cheo cha Inspekta, akiwa na nyota mbili mabegani, alilifikia gari letu na kuzunguka akielekea upande wa nyuma wa gari huku akiwa analichunguza kwa jicho la hadhari.

“Nipe leseni yako ya udereva,” yule Koplo aliniambia kwa sauti kali ya kuamuru huku akiendelea kunikazia macho yake.

Nikatoa leseni yangu na kumpa huku nani nikimkazia macho bila kupepesa. Aliipokea ile leseni na kuanza kuikagua. Kitambo kifupi cha ukimya kikapita wakati yule askari akiendelea kuikagua ile leseni na wakati akifanya hivyo yule askari mwingine mwenye cheo cha Inspekta aliyekuwa amezunguka upande wa nyuma akawa anakuja mbele kwenye mlango wangu.

“Umebeba nini ndani ya gari yako?” yule Koplo aliniuliza tena kwa ukali akiwa bado kaishikilia mkononi leseni yangu.

Nilimtazama kwa umakini huku donge la hasira likianza kunikaba kooni maana niliona kuwa alikuwa anatuchelewesha kuendelea na safari yetu pasipo sababu za maana. Nilitafakari kidogo nikitafuta jibu la kumpa lakini kabla sijamjibu, yule Inspekta akanifikia na kunitazama kwa umakini usoni.

“Hey, Jason!” yule Inspekta alisema huku akiachia tabasamu pana usoni kwake.

Nilimtazama vizuri usoni na kumtambua. Aliitwa Ibrahim Ubwa, mtoto wa Mwalimu Musa Ubwa. Mimi na Ibrahim tuliishi mtaa mmoja huko Manispaa ya Tabora na tulikuwa marafiki wakubwa wakati tukisoma darasa moja kuanzia la kwanza hadi darasa la saba katika Shule ya Msingi Gongoni.

“Ooh, Inspekta Ubwa! Long time no see!” niliitikia huku nami nikiachia tabasamu pana usoni kwangu.

“Habari za siku, ndugu yangu,” Inspekta Ubwa alinisalimia kwa bashasha.

“Nzuri…” niliitikia huku nikitaka kumwambia aturuhusu kwani tulikuwa katika haraka za kumfuatilia mtu.

“Pole sana na matatizo… Mama aliniambia kilichokupata, na nilipompigia simu Eddy naye akanithibitishia! Pole sana mkuu,” Inspekta Ubwa alisema kwa huzuni.

“Ndo hivyo, yote ni mipango ya Mungu,” nilisema na kushusha pumzi.

“Daah… niliposikia sikuamini kabisa!” Inspekta Ubwa alisema na kuwatazama watu wengine niliokuwa nao ndani ya gari kisha akawasalimia, “Habari zenu jamani!”

“Nzuri,” waliitikia kwa pamoja.

“Enhe! Na huku mnatoka wapi tena?” Inspekta Ubwa aliniuliza huku akinitazama machoni.

“Kuna mtu tulimfuata Kilosa lakini bahati mbaya tumepishana naye, ameelekea Dodoma,” nilimwambia Inspekta Ubwa.

“Ooh!” Inspekta Ubwa alisema na kushusha pumzi.

Wakati huo yule Koplo alikuwa akitutazama mimi na Inspekta Ubwa kwa zamu na sasa alionekana kunywea, huenda ni baada ya kuona kuwa mtu aliyekuwa anataka kumkagua alikuwa anafahamiana na bosi wake. Sasa hakuwa na namna nyingine ya kufanya isipokuwa kunirudishia ile leseni yangu. Niliipokea na kushukuru.

Inspekta Ubwa akaturuhusu tuondoke na kuwapa ishara askari wengine waliokuwa wamesimama kwenye kile kizuizi kuondoa kile kizuizi. Askari hao walitii amri na kuondoa kile kizuizi cha barabarani, wakaturuhusu kupita.

“Tutafutane basi, namba yangu ni ile ile,” Inspekta Ubwa aliniambia na kutuashiria kuwa tunaweza kuondoka.

“N’takutafuta, ngoja kwanza nimalize haya mambo,” nilimwambia Inspekta Ubwa huku nikiachia tabasamu la kirafiki na kuwapungia mkono wale askari katika namna ya kuwaaga kisha nikatia moto gari na kuliondoka kutoka eneo lile nikiwaacha wale askari wakilisindikiza kwa macho.

Muda huo ilikuwa imetimia saa 11:45 jioni. Tulikuwa tumetumia takriban dakika ishirini katika kizuizi hicho cha barabarani.

Wakati tukiondoka nikakumbuka jambo, nilimwambia Almasi ajaribu kuipiga namba ya Zainabu, lakini bado ilikuwa haipatikani. Nikapata wazo la kumpigia simu mjomba, Mchungaji Ngelela na kumweleza kila kitu kisha tukakubaliana kuwa afuatilie katika kituo cha mabasi cha Nanenane, jijini Dodoma, pengine angeweza kumpata Zainabu.

Kisha nilimwomba Almasi amtumie mjomba picha ya Zainabu, kwa njia ya WhatsApp. Almasi alifanya hivyo.

Endelea...
 
Mgeni mwema.jpg

202

Safari ya kurudi Dodoma ikaendelea. Muda huo magari barabarani hayakuwa mengi jambo lililonifanya kuteleza kwa kasi. Ndani ya muda usiozidi saa mbili tukawa tumeingia jijini Dodoma. Mpaka hapo hatukuwa tumepata taarifa zozote kuhusiana na Zainabu.

Niliwasiliana na mjomba, akasema alikwisha ondoka kurudi nyumbani lakini aliacha maagizo kwa askari wawili aliofahamiana nao wa kituo cha mabasi cha Nanenane kumfuatilia Zainabu kwenye mabasi yaliyokuwa yakiendelea kufika yakitokea Morogoro na Dar es Salaam. Nikaamua kuliongoza gari hadi katika kituo cha mabasi.

Nilipoitazama saa ilinionesha kuwa ilishatimia saa 1:35 usiku. Tulikuwa tumechoka na njaa ilikuwa inauma, ndiyo kwanza nikagundua kuwa hatukuwa tumetia chakula tumboni zaidi ya vinywaji na vile vitafunwa tu tangu tulipokunywa chai asubuhi.

Wakati tukiinga katika kituo cha mabasi cha Nanenane tulikuta mabasi mawili yakiwa yameingia hapo muda mfupi uliokuwa umepita, na kulikuwa na pilika pilika za abiria kushuka na kutafuta usafiri mwingine wa kuwapeleka mjini. Niliegesha gari langu karibu na lango la kutokea kisha haraka haraka mimi na Almasi tukashuka kujaribu kumtafuta Zainabu.

Tulijitahidi kuangaza macho yetu kwenye ule mwanga wa taa za umeme huku na huko tukiwatazama watu, hasa wasichana waliokuwepo eneo lile bila mafanikio. Tukiwa tumeanza kukata tamaa na kutaka kurudi kwenye gari letu mara tukaona basi lingine la Kutoka Morogoro likiwasili eneo hilo.

Nikamshauri Almasi tuwahi kwenye basi hilo kabla abiria hawajaanza kushuka, lakini kabla hatujaelekea huko nikasita kidogo baada ya macho yangu kuvutwa kumtazama msichana mmoja aliyekuwa kwenye banda moja la chipsi, muda huo alikuwa amesimama akipokea chenji yake aliyokuwa anarudishiwa baada ya kulipia huduma ya chakula, kisha akatoka na kuanza kuondoka kwa madaha.

Msichana huyo alikuwa amevaa gauni zuri la kitenge la mikono mikono mirefu lililolichora vyema umbo lake zuri na alibeba begi dogo jeusi la mgongoni. Alikuwa anatembea mithili ya twiga akipenya katikati ya watu akielekea kwenye lango la kutokea la kituo kikuu cha mabasi cha Nanenane. Mara nikamwona akitoa simu yake toka kwenye mfuko wa pembeni wa begi lake na kuiwasha.

Nikamwonesha Almasi kule alikokuwa yule msichana, Almasi alipogeuka kutazama huko hakuchelewa kumtambua licha ya kiza kilichokuwa kimetanda kikishindana na mwanga wa umeme.

“Zainabu!” Almasi alisema na kuanza kupiga hatua za haraka akielekea kule alikokuwa yule msichana. Nami nikafuata haraka huku nikiwa makini zaidi kumtazama Zainabu ili asije akatupotea.

“Zainabu!” Almasi aliita huku akiongeza mwendo kumfuata yule msichana.

Sikuwa na hakika kama Zainabu alimsikia Almasi wakati akiitwa kwani aliendelea na safari yake huku akipiga simu yake na kisha kuiweka sikioni. Almasi akazidisha mwendo huku akiita kwa sauti kubwa zaidi, na hapo nikamwona Zainabu akigeuka haraka na kutazama nyuma yake kwa wasiwasi, nilihisi alimwona mtu akimjia haraka, akasita kidogo kabla hajamtambua Almasi na kuonesha mshangao.

“Ayi, Almasi!” Zainabu alisema kwa mshangao mkubwa huku akiachia mdomo wazi. Kisha akauliza, “Umefikaje huku?”

“Nimekufuata wewe, nimekuja na Mgeni…” Almasi alimwambia Zainabu mara tu alipomfikia, huku akigeuza shingo yake kunitazama, kisha akaongeza, “Alikufuata Kilosa lakini tukaambiwa na Sofia kuwa umekuja Dodoma.”

Muda huo nilikuwa nimeshawafikia na kusimama kando huku nikimtazama Zainabu kwa umakini. Zainabu aliinua uso wake kunitazama na hapo nikamwona akishtuka kidogo baada ya kunitambua. Alionekana kutahayari akiwa hajui aseme nini, machozi yakaanza kumlengalenga machoni.

“Zainabu, habari za siku?” nilimsalimia huku nikiendelea kumtazama kwa umakini. Nilishukuru Mungu kuwa alikuwa salama japo alikuwa amepungua sana, huenda ni kwa sababu ya mawazo.

Zainabu aliinamisha uso wake chini, akataka kusema neno lakini akasita. Mara akaanza kulia kwa uchungu, kilikuwa kilio cha kwikwi. Tulijaribu kumbembeleza lakini hatukuweza. Ilikuwa lazima alie kwa kuwa alikuwa amepitia mengi ya kusikitisha na mwanamume aliyemwona mbele yake alikuwa amemkumbusha upendo wa zamani.

Alilia huku akishindwa kunitazama usoni, macho yake yaling’ara kwa huba ya ajabu, midomo yake haikuzungumza lakini alikuwa anatangaza huzuni iliyopitiliza, katika uso wake. Ni kama vile alikuwa anasema, “nakupenda kupita wanaume wote duniani.”

Nilibaki kimya nikimtazama usoni pasipo kusema neno lolote. Hakika alikuwa katika hisia motomoto. Hisia za kukutana na mwanamume aliyekuwa akimpenda. Hisia za upendo uliodumu takriban mwaka. Baada ya kulia kwa muda aliyafuta machozi yake na kunitazama mara moja tu kisha akayahamisha macho yake na kutazama tena chini, bado alikuwa katika simanzi. Simanzi kuu!

Akiwa bado anatazama chini akaniambia, “Mgeni… naomba nisamehe sana kwa ujumbe wa maneno niliokutumia leo asubuhi, ni kwamba tangu siku ulipoondoka maishani kwangu sijawahi kuwa sawa kiakili.”

Kisha alishusha pumzi ndefu na kufuta machozi yaliyoendelea kumtoka na kuchuruzika mashavuni.

“Hata hivyo kila nikiukumbuka ujumbe nilioutuma kwako leo asubuhi najihisi mkosaji nisiyestahili hata kukuomba msamaha. Nimejikuta nikiumizwa zaidi na maneno hayo na hata dhamira yangu…” Zainabu alisema kisha akasita.

Mara zote, kama nilivyomfahamu japo kwa kitambo kifupi, Zainabu alikuwa jasiri sana ambaye hakuona haya kunitazama machoni, lakini safari hii hakuwa na ujasiri huo.

“Usijali… jambo la msingi ni kwamba nimekupata ukiwa hai…” nilisema huku nikiachia tabasamu. Kisha nikamtaka tuongozane hadi kwenye gari letu ambalo halikuwa mbali kutoka pale tulipokuwa tumesimama.

Hakupinga wala kusita. Tulielekea lilipo gari, tukalifikia gari letu na hapo nikamfungulia Zainabu mlango wa nyuma na kumtaka aingie huku nikiwataka Grace na Rehema waketi vizuri ili ipatikane nafasi. Zainabu akaingia na kuketi jirani na Rehema huku akiwatazama Grace na Rehema kwa wasiwasi. Nao wakamtazama kwa umakini.

Wote watatu wakabaki kuduwaa. Sasa Rehema, Grace na Zainabu walikuwa macho kwa macho. Macho manne yalikuwa yanatazamana na macho mawili ya Zainabu. Haikueleweka iwapo walikuwa katika hali ya taharuki ama tahamaki! Nilichobaini tu ni kwamba wote walikuwa kimya kabisa wakitazamana bila kusema chochote. Nani aanze kusema neno? Hili lilikuwa swali.

Nikaamua kutoa utambulisho, “Zainabu, kutana na dada yangu Grace…” nilisema huku nikimwonesha Grace aliyekuwa ameketi pembeni, kisha nikaendelea, “na huyo wa katikati ndiye mke wangu… na mtoto wetu, Jason Junior.”

Utambulisho ule ulionesha kumshtua sana Zainabu, alimtazama Rehema kwa jicho la wizi na kulegeza uso wake kwa tabasamu la kulazimisha, kisha kama ambaye alikuwa amebabaika akanyoosha mkono wake kumpa. “Nimefurahi kukufahamu, Mama Jason.”

“Nami nimefurahi kukufahamu, karibu sana Dodoma,” Rehema alisema huku akiachia tabasamu kisha alinitupia jicho mara moja na kuyarudisha macho yake kwa Zainabu.

Endelea...
 
Mgeni mwema.jpg

203

“Ahsante,” Zainabu alisema na kushusha pumzi, kisha kikazuka kitambo kifupi cha ukimya huku Zainabu akimtazama Rehema kiwiziwizi.

Nikakumbuka kuwa Zainabu alikuwa na mtoto aliyeitwa Mariam, lakini hapo sikuwa nimemwona na wala hakuna aliyekuwa amemwongelea. Sasa alikuwa peke yake. Je, mtoto wake alimwachia nani?

“Mbona uko peke yako, Mariam yuko wapi?” nilimuuliza Zainabu huku nikimtazama kwa umakini usoni.

Zainabu hakunijibu na badala yake kilio cha kwikwi kikaanza kuchukua nafasi yake taratibu, alilia kwa uchungu mno. Nikashtuka na kumtupia jicho Almasi. Ulikuwa mtazamo wa kuuliza ‘kulikoni?’

“Mariam amekufa… alizidiwa na kufariki dunia wiki mbili zilizopita,” Almasi alisema kwa huzuni huku akitingisha kichwa chake kwa huzuni. Moyo wangu uliingiwa na ganzi, na hapo nikajikuta nikipatwa na simanzi.

“Oh, pole sana! sikujua,” nilimpa pole Zainabu huku nikionesha huzuni yangu.

Na wakati huo huo Rehema alimkumbatia Zainabu kwa nguvu na upendo zaidi katika namna ya kumfariji huku akimpa pole. Wakakumbatiana. Kitu cha ajabu kilichoniacha katika mshangao ni ile hali ya Rehema kuanza kutoa machozi akilia na Zainabu badala ya kumbembeleza!

Vilio hivi vikanipa suluba ya ghafla. Nikahisi huruma zaidi lakini mara nikakumbwa na mshangao. Sikujua ni nani niliyekuwa namwonea huruma.

Baada ya muda walinyamaza na kufuta machozi huku Zainabu akishusha pumzi ndefu. Kisha kikapita tena kitambo kifupi cha ukimya. Muda wote nilikuwa nawatazama wote wawili kwa umakini.

“Tuondoke,” Grace alishauri na hapo nikakumbuka na kuwasha gari kisha nililiondoa taratibu na kuingia barabarani. Tukiwa sasa tumeishika barabara ya kuelekea mjini nikakumbuka kwamba hatukuwa tumempigia simu mjomba, nikamwomba Grace ampigie kumjulisha kwamba tumempata Zainabu na tulikuwa njiani kwenda nyumbani. Grace akafanya hivyo.

Muda huo nilikuwa katika mtihani mgumu sana. Japo ni Rehema aliyekuwa amenishauri tukamtafute Zainabu lakini ukweli ni kwamba hadi wakati huo sikuwa na uhakika wa kitu gani ambacho kingetokea baada ya kufika nyumbani na kisha kukaa na kuzungumza, mazungumzo ya watu watatu ili kuyaweka mambo sawa.

Niliamua kujiliwaza kwa kuweka muziki kwenye redio ya kisasa iliyofungwa katika gari, kisha nikawa nakitikisa kichwa changu kufuatisha midundo ya muziki.

Dakika therathini baadaye nilikuwa naegesha gari kwenye maegesho ya magari ndani ya jumba la kifahari la Mchungaji Ngelela.

* * *



Saa 3:45 usiku…

Watu watano tulikuwa tumeketi kwenye meza kubwa ya chakula kwa ajili ya chakula. Kwenye kiti cha kando yangu, upande wa kushoto aliketi Rehema na kwenye kiti cha upande wangu wa kulia aliketi Almasi. Grace na Zainabu walikuwa wameketi upande mwingine wa meza. Zainabu aliketi mkabala na kiti nilichokalia na alikuwa akitutazama mimi na Rehema kwa kuvizia vizia.

Meza ya chakula ilikuwa imejaa mapochopocho ya kila aina kama vile wali mweupe, mchuzi mzito wa kuku, bakuli lenye nyama za kuku, bakuli la maharage yaliyoungwa kwa karanga, bakuli la mboga za majani zilizoungwa kwa karanga, bakuli la saladi, matunda mchanganyiko kwenye sinia pamoja na jagi la maji ya kunywa na bilauri tano.

Ulikuwa ni mlo wa kimya kimya. Tangu alipomwona Zainabu kule kituo cha mabasi cha Nanenane, Rehema alionekana kupoa sana tofauti na kawaida yake, jambo lililonishangaza mno, sikujua kwa nini. Kuna muda alitaka kuniambia jambo lakini akaonekana kusita na kuendelea kula kimya kimya. Nilihisi kama alikuwa na donge fulani la fadhaa lililomkaba kooni.

Mara kwa mara nilimwona Grace akimtazama Rehema kwa udadisi na kuna wakati alitaka kuongea lakini akaonekana kujizuia na akabaki kuwa mtulivu muda wote. Kwa kawaida meza ya chakula hugeuka kijiwe cha soga wakati wa chakula lakini tofauti na siku nyingine, usiku huo meza ya chakula ilitanda ukimya mzito wakati wote wa chakula.

Ukiwatoa wageni wawili, Almasi na Zainabu, ambao walikuwa kimya kutokana na ugeni wao, sisi wengine watatu tulikuwa kimya, hakuna aliyeongea na kilichokuwa kikisikika muda wote kilikuwa ni mgongano wa vijiko na vyombo vingine vya mezani, wakati tukila.

* * *



Saa 4:30 usiku…

Tulipoingia chumbani baada ya mlo wa usiku hakuna hata mmoja aliyekuwa anamtazama mwenzake. Ni kweli tulikuwa tumechoka sana baada ya pilika pilika za kutwa nzima kwenda Kilosa na kurudi Dodoma, lakini ilionekana wazi kuwa Rehema alikuwa katika mawazo, sikujua mawazo hayo yalikuwa ya kufikiria hatma yetu baada ya ujio wa Zainabu au yalihusiana na nini.

Nilipojaribu kuyasoma mawazo yake kupitia uso wake nilishindwa kuelewa kwani uso wake haukuonesha tashwishwi yoyote. Hata hivyo sikuona kama kulikuwa na chochote cha kumfanya Rehema awe na wasiwasi au mawazo ya kiasi kile.

Nilibaki nimeketi kitandani nikiwa katika tafakari ya aina yake. Kwangu, nilimwona Rehema kama wanamke wa pekee aliyekuwa anajua kujali na hata akijua amekosa basi hakuwa mchoyo wa kujishusha na kuomba msamaha. Rehema alikuwa na sauti fulani inayoweza kubadili msimamo wa mtu hata kama hakuwa katika mpango huo. Alikuwa na kipaji cha ushawishi. Alikuwa mpiganaji kimaisha na kimapenzi.

Japokuwa ilionesha wazi kuwa kila mmoja wetu aliingia chumbani akiwa na lake kichwani, Rehema alionekana kuumizwa na jambo, sikujua ni jambo gani. Nilihisi kuwa huenda sasa alianza kufikiria tofauti, huenda sasa aliamini kuwa kitendo alichokifanya mchana cha kumpigania Zainabu ilikuwa sawa na kumkabidhi fisi bucha ili akuuzie nyama, na kwamba muda si mrefu mambo yangeweza kugeuka.

Nilihisi kuwa sasa alikuwa kafadhaika na kujikuta lile jeraha lake la kumpoteza mume kwa miezi tisa likirejea kuwa kidonda kibichi. Lakini angefanya nini wakati tayari ni yeye aliyekuwa ameamua iwe hivyo?

Sikujua… pengine ulikuwa wasiwasi wangu tu. Pengine Rehema hakuwa akiyawaza hayo na alikuwa na uchovu mwingi. Hizo zilikuwa hisia zangu… hisia mbaya! Hisia za ajabu kabisa!

Kwa nini mtu aruhusu hisia ziharibu uhusiano? Kwa nini hisia zichukue nafasi ya kufanya uamuzi katika nafsi? Siku zote jeraha la hisia hutibiwa kwa kuutambua ukweli na kuupa nafasi katika mioyo yetu. Basi!

Mimi na Rehema tulikuwa tumeanza maisha mapya kama wanandoa na kama wazazi wa mtoto Jason Junior. Tulikuwa wazazi na wanandoa ambao tulikuwa tumepitia mitafaruku mingi sana tangu kwenye uhusiano wetu na kisha tukajikuta tukitenganishwa kwa miezi tisa baada tu ya kutoka kufunga ndoa. Lakini kudra za Mungu na nguvu ya penzi la kweli vikasimama imara kupigana na vizingiti na hatimaye tukajikuta tumeungana tena.

Endelea...
 
Mgeni mwema.jpg

204

Sisi tukiwa chumbani kwetu muda huo Zainabu alikuwa chumbani kwa Grace, huenda na yeye alikuwa katika wakati mgumu kama wetu, akifikiria hatma yake…

“Jason…” Rehema alinizindua toka kwenye mawazo yaliyoanza kuiteka akili yangu.

Niligeuka kumtazama bila kusema neno lolote. Rehema hakuonesha kujali, alishusha pumzi na kusema kwa sauti tulivu isiyo na dalili zozote za ubaya, “She is a very good girl.”

Which one?” nilimuuliza kwa mshangao nikiwa sielewi alikuwa anamaanisha nini kusema ni msichana mzuri sana. Kisha nikajisahihisha haraka na kujibu, “Ooh, yeah… I think she is!

And she loves you very much, you know that?” Rehema alisema tena akiniuliza kama nilikuwa najua kuwa Zainabu alikuwa ananipenda sana, lakini safari hii sauti yake iliashiria kitu fulani, ni kama alikuwa na wivu hivi.

Na hapo nikaamua kumtazama moja kwa moja machoni nikiwa na lengo la kusoma mawazo yake kupitia macho na sura yake lakini sikuweza kusoma chochote kwani muda wote alikuwa anatabasamu. Nikashusha pumzi na kuangalia sakafuni.

“Sijui, lakini… hata kama ananipenda sana bado mimi na yeye hatuwezi kuwa pamoja,” nilimjibu Rehema kwa sauti tulivu.

Kisha kitambo kirefu cha ukimya kikapita na kunifanya nianze kuingiwa na wasiwasi, nikageuka tena kumtazama Rehema, nikakuta ametazama upande mwingine. Hata hivyo niligundua kuwa uso wake ulionesha kama macho ameyafinya hivi kuonesha kuna kitu alikuwa anakiwaza.

“Rehema…” niliita na kumfanya Rehema ageuke kunitazama huku akiachia tabasamu.

“Tangu siku niliporudiwa na kumbukumbu zangu na kugundua kuwa nilikuwa naishi na mwanamke mwingine, na mbaya zaidi nimempa ujauzito sijawahi kuwa sawa kiakili. Kila nikikumbuka najisikia mkosaji na nisiyestahili hata kukuomba msamaha…” nilijaribu kujieleza lakini Rehema akanikata kauli.

“Mbona sasa unafika mbali? Jambo hili si tulishaliongea na tukakubaliana kwa nini leo unataka uyarudie mambo haya?” Rehema aliniuliza huku akiwa amekunja sura yake. Ni Dhahiri alionekana kukerwa sana na maelezo yangu.

“Hata sijui niseme nini…” nilijaribu kujitetea kisha nikaongeza, “lakini naona kama umebadilika hivi baada ya kumwona Zainabu, nakuona huna raha pengine unadhani labda…”

“Jason!” kwa mara nyingine Rehema alinikata kauli. Safari hii alikuwa amechukia sana. “Kwa nini uwe na hisia mbaya juu yangu? Kwa nini udhani kuwa nimechukia baada ya kumwona Zainabu? Ni kweli nipo kimya tangu nimwone lakini unajua nawaza nini? Siwezi kumchukia, najua kukutana kwenu ulikuwa mpango wa Mungu, ambaye siku zote huwa hakosei katika kila jambo analolitenda. Aliwakutanisha kwa sababu anazozifahamu yeye mwenyewe? So please, acha kuwa na mawazo hasi juu yangu…”

Nilitaka kusema neno lakini nikajikuta nikisita maana sikujua niseme nini. Rehema alinitazama usoni.

“Kwa taarifa yako moyo wangu una furaha na amani sana tangu nilipomwona Zainabu… najua huwezi kuelewa haraka lakini nikwambie tu ukweli wewe huna kosa na wala Zainabu hana kosa lolote… after all she is a nice girl and she doesn’t deserve to be treated indifferently…” Rehema aliniambia na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.

Anyway, tuachane kwanza na hayo… nataka uniambie una mpango gani na binti wa watu?” Rehema alinitupia swali ambalo sikuwa nimelitarajia kwa muda huo, nikajikuta nikiingiwa na kigugumizi.

“Sijajua… labda… labda nifikirie kwanza,” nilisema kwa kusita sita.

“Kama mwanamke nafahamu ni jinsi gani Zainabu anajisikia. Najua alikuwa na matarajio makubwa sana ambayo sasa anaona ni kama yametoweka. Kwa kipindi hiki kifupi nimeyashuhudia hayo kupitia macho yake na ndiyo maana moyo wangu unaumia sana kumwona akiwa na fadhaa. Namwonea huruma sana…” Rehema alisema na kuminya midomo yake, akaangalia juu kwa sekunde kadhaa kisha akanitazama tena. “Naomba tumsaidie…”

Nilikosa kabisa cha kumjibu Rehema kwa usiku ule kwa kuwa sikujua nifanye nini, nilitamani kumshauri tulale kwanza huku nikifikiria nini cha kufanya. Nilijikuta nikiyatafakari maneno yake japo sikujua ni msaada upi aliotaka tumsaidie Zainabu.

“Kwa kuwa anakwenda kuwa mama wa mtoto wako, mtoto ambaye atakuwa ndugu wa Junior, sioni sababu ya kumwacha aishi maisha ya mashaka. Kwa sasa maisha yake na kila kitu chake vinapaswa kuwa jukumu lako… jukumu letu. Yapo mambo ninayoyafikiria tumfanyie…” Rehema alisema huku akinitazama usoni kwa umakini. Kisha alifunguka kila kitu alichokuwa akikiwaza.

Baada ya kunieleza niliinamisha kichwa changu nikatafakari kwa muda. Nilimshangaa sana Rehema kwa mawazo yake. Niliyatazama macho yake wakati akiongea na nilithibitisha kwamba alikuwa akimaanisha kile alichokisema.

“Rehema naweza kusema kwamba wewe ni mwanamke wa kipekee sana na nina bahati kubwa sana kuwa nawe. Una roho ya kipekee ambayo wengi hawana. Ndiyo maana thamani yako kwangu hailinganishwi na kitu chochote kile katika hii dunia….” Nilisema huku nikishindwa kuuficha mshangao wangu. kisha nikaongeza, “Kwa kifupi mimi sipingani na chochote ulichokiamua.”

Ama kweli ndoa ni tamu sana kama ukimpata mtu aliye sahihi lakini ukimpata ambaye si sahihi ndoa huchacha na hupoteza utamu wake wote na hutatamani kuisikia tena maishani mwako.

Rehema alikuwa ni maisha yangu. Alikuwa ni kila kitu kwangu. Alikuwa mwanamke wa tofauti sana mwenye moyo wa ajabu na wa kipekee kabisa! Alikuwa na upendo wa dhati na wa kweli. Upendo wake ulikuwa unatoka ndani kabisa ya moyo wake. Nilianza kumchukulia Rehema kama malaika anayeishi duniani!

* * *

Endelea kufuatilia hadi mwisho...
 
Back
Top Bottom