Simulizi: Harakati za Jason Sizya

Simulizi: Harakati za Jason Sizya

Mgeni mwema.jpg

181

Kwa aibu nilianza kufuta mikono yangu iliyochafuka, tukaondoka na kuendelea na safari yetu ya kwenda nyumbani. Safari ilikuwa ya kimya kimya, hakuna aliyemsemesha mwenzake…

Tulipofika nyumbani Zainabu alinitazama machoni huku akionekana kuzuia machozi. Kabla sijamuuliza kulikoni akanikumbatia kwa nguvu na kuanza kunipiga mabusu uso mzima, mihemuko ya mwili wangu ilikuwa karibu kabisa na hisia zangu hivyo nilianza kulipiza mashambulizi, lakini kila nilipokuwa nikimshika Zainabu kuna picha ya msichana mwingine ilikuwa ikinijia. Msichana huyo alikuwa ni yule niliyemwona ndotoni.

Wakati tukiendelea kukumbatiana na kubusiana Zainabu akaniongoza hadi chumbani na kisha kazi ikaanza pale. Nilishangaa sana kwani siku hiyo Zainabu alikuwa mtundu sana kitandani, lakini kila alipojitahidi kunifanyia mambo fulani taswira ya yule msichana wa ndotoni ilikuwa inanijia.

Tuliendelea kusumbuana na kuchokozana hisia zetu na mwishowe tulikutanisha maungo yetu ya uzazi, nilipokuwa katikati ya mchezo wakati Zainabu akiwa juu kuongoza jahazi sura ya yule msichana ilijaa akilini kwangu na kunifanya nishtuke mno.

“Rehema!” nilijikuta nikilitamka jina hilo ambalo sikujua nililitoa wapi, na papo hapo Zainabu akaacha na kunitazama kwa mshangao mkubwa.

“Rehema kafanyaje?” Zainabu aliniuliza kwa mshangao huku akizidi kunikazia macho. Sikumjibu kwa kuwa sikujua namna ya kuelezea.

“Rehema ni nani?” Zainabu aliniuliza huku akinyanyuka vile vile akiwa uchi na kusimama kando, alinitazama kwa namna ambayo sikuweza kupata tafsiri ya haraka. Alikuwa amehuzunika sana.

Nilijivuta pale kitandani na kusimama, nikamsogelea na kutaka kumshika lakini hakuwa tayari kushikwa. Nilibaki nimetumbua macho na yeye hakuwa anaongea zaidi ya kunitazama huku machozi yakimlengalenga.

“Mgeni!” Zainabu aliniita huku akiketi kitandani. Niliitika huku nami nikiketi kitandani kando yake. Zainabu akanitazama kwa muda kisha akayahamisha macho yake na kutazama mbele huku akishusha pumzi, halafu akaongea bila hata kunitazama, “Naogopa sana… sitaki utoke mikononi mwangu.”

Sikusema kitu. Nilibaki kimya kana kwamba sikuwa nimemsikia.

“Umenisikia, Mgeni?” Zainabu aliniuliza huku akigeuza shingo yake kunitazama usoni.

“Nakusikia, Zai,” nilisema kwa sauti tulivu huku nami nikimtazama usoni.

“Niahidi kwamba hautaniacha,” Zainabu alinisihi huku akiendelea kunitazama usoni.

Kidogo nikawa kimya, nilizidi kushangazwa na kauli ya Zainabu. Sikujua alikuwa na nini na kwa nini alitaka nimhakikishie kwamba sitomwacha! Kwani alikuwa ameona nini? Nilibaki nikijiuliza pasipo kupata majibu. Alipoona nipo kimya akanitazama moja kwa moja machoni.

“Mgeni!” Zainabu aliniita tena.

“Zainabu, unajua mazingira yangu yalivyo, sikumbuki chochote na wala siwezi kutabiri kesho yangu,” nilimweleza huku nikimtazama usoni, nikamwona akivunjika kihisia.

“Sijui kwa nini unanisisitiza kuwa nisikuache, kwani umeona nini kwangu kinachoashiria kwamba nataka kukuacha?” nilimsaili Zainabu.

“Nataka tu kujua msimamo wako, nina wasiwasi endapo utarudiwa na kumbukumbu zako unaweza kuniacha,” Zainabu alisema kwa huzuni.

“Siwezi kujua lakini si kama hivyo unavyoweza kudhani,” nilisema na kuongeza, “ila nakuahidi siwezi kwenda mbali na wewe.”

“Unajua ukiniacha ulimwengu utakuwa tofauti kabisa! Ulimwengu utakuwa mkatili sana kwangu kupita kiasi. Sitaweza kuvumilia maisha haya bila wewe… tafadhali usiniache, Mgeni,” Zainabu alisema huku machozi yakizidi kumlengalenga. Kisha alinishika mkono wangu wa kuume kwa nguvu.

Nilishangazwa sana na hali ile, nikamfuta machozi na kumwahidi ningekuwa naye mpaka mwisho kwa kuwa nilikuwa nampenda sana, na sikupenda kumwona akigubikwa na huzuni. Nilimwambia ningefanya kila jambo lililo ndani ya uwezo wangu kuhakikisha anayafurahia maisha, na kwa nguvu zangu zote ningemwadabisha yeyote yule ambaye angemgusa au kumuumiza.

Hata hivyo nilimwona Zainabu akinitazama tu kama ambaye hakuwa akiyaamini yote niliyomwambia.

“Nakuahidi hilo kwa moyo wangu wote, Zai,” nilisisitiza kisha nikambusu kwenye paji la uso.

* * *



Saa 5:30 usiku…

“Una tatizo lolote, Zai? Naona leo kama hauko sawa kabisa!” nilimuuliza Zainabu baada ya kumwona hayuko sawa. Muda mwingi alikuwa mkimya akiwa anafikiria sana.

Muda huo tulikuwa kitandani. Zainabu alikuwa amenilalia kifuani akionekana mwenye mawazo mengi, lakini nilipomuuliza alinyanyuka na kuketi. Hii ilikuwa siku ile ile ambayo mchana wake nilijikuta nikiropoka jina la Rehema.

“Hapana, niko sawa,” Zainabu alinijibu huku akiachia tabasamu kama njia ya kunionesha kuwa yuko sawa. Hata hivyo nilijua kuwa tabasamu lile halikuwa halisi, lilikuwa limeficha huzuni ndani yake.

“Unakumbuka nimekuuliza maswali mangapi?” nilimuuliza huku nikimtazama usoni bila kupepesa macho yangu. Alionekana kuwaza kwa muda na kujibu japo nilimwona akiwa hana uhakika wa jibu.

“Mawili…” alinijibu na hapo akatazama kando kwa muda kisha aliyarudisha macho yake kwangu na kushusha pumzi za ndani kwa ndani na kuniuliza, “Rehema ni nani?”

“Hata simjui, nilijikuta nimeropoka tu,” nilimwambia Zainabu nikiwa nimeshtuka kidogo ingawa nilijitahidi kuumeza mshtuko wangu. Sikujua kumbe Zainabu alikuwa bado ana kinyongo!

Ukweli sikujua jina hilo nililitoa wapi, kwani lilinijia tu wakati tupo mchezoni baada ya sura ya msichana wa ndotoni kunijia akilini.

“Yaani uropoke tu jina la mwanamke pasipo sababu? Sijawahi kuona!” Zainabu alihoji huku akinikazia macho.

Nilihisi kuwa hata ningejielezaje bado nisingeeleweka, nikaanza kumshikashika Zainabu na kumbusu kila sehemu huku mikono yangu nikiipitisha kwenye ikulu yake. Zainabu aliusukuma mkono wangu na kujiondoa toka mikononi mwangu huku akiniambia kuwa hakuwa na hamu ya kufanya chochote. Nikamwacha.

“Najua hata nijieleze vipi huwezi kunielewa, naomba tu huniamini, mpenzi… hakyamungu simjui mwanamke yeyote mwenye jina hilo, lilinitoka tu,” nilijitetea huku nikihisi hatia imenikaba kooni. Zainabu aliendelea kubaki kimya kabisa akinikazia macho.

Please…” nilimsihi Zainabu, na bila kujua machozi yalianza kunidondoka. Nikamwona Zainabu akiingiwa na huruma.

“Nimekuelewa,” Zainabu alisema huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani. Kisha aliniita jina langu kikamilifu, “Mgeni Mwema!”

“Naam!” nilijikakamua kuitika.

“Naomba nikwambie kitu… kwangu wewe ni mwanaume wa kipekee…” alisema na taratibu akaanza kurudi katika hali yake ya kawaida ya ucheshi. “Sasa nimefikia uamuzi… nahitaji nikuzalie mtoto!”

Sikusema chochote. Nilibaki kimya nikimtumbulia macho. Zainabu akaniomba nisimame kisha akaniambia nimsogelee, nikamsogelea na kumkumbatia.

“Mgeni, umekuwa nguzo kuu katika maisha yangu kuliko mtu yeyote maishani mwangu, umekuwa nuru mpya katika njia yangu. Na zaidi umekuwa mwanaume bora kati ya wanaume wote ninaowajua…” alisema kisha akasita kidogo na kunitazama usoni. Sikuwa na cha kusema zaidi ya kujibu, “ahsante”.

“Lakini kuna muda najikuta najuta kwa nini nimekufahamu, kwa nini umekuja katika maisha yangu,” Zainabu alisema na kushusha pumzi ndefu.

“Kwa nini unasema hivyo?” nilimuuliza huku nikimtazama usoni kwa umakini.

“Hata sijui lakini ukweli nitajiona mpweke sana siku utakapoamua kuniacha,” Zainabu alisema kwa huzuni.

“Mbona leo unaongea sana kuhusu kuachwa, kwani kuna nini umekiona kwangu?” nilimuuliza Zainabu kwa mshangao. Zainabu hakujibu, badala yake aliachia tabasamu lililobeba uchungu.

“Zai, naomba uniambie… una maana gani kusema hivyo? Huniamini?” nilimuuliza tena kwani maneno yake yalinichanganya kidogo.

“Hata sijui kama nakuamini au sikuamini, ila nimesukumwa tu kusema hivyo…” Zainabu alisema na kubetua mabega yake, “unajua ni vigumu kuwa wakili wa moyo wako.”

“Ninaweza kuwa nimekuelewa lakini huenda vile vile sijakuelewa! Kama shaka yako ni jina la Rehema ukweli hata simfahamu. Labda tu uniweke wazi una maana gani kama sivyo nifikiriavyo?" nilimuuliza Zainabu kwani maneno yake ya mafumbo yalizidi kuniweka njia panda.

Hakunijibu bali aliachia tabasamu na kunisogelea halafu akanikumbatia kwa nguvu na kuanza kunipa joto. Sikutaka kumhoji zaidi, nami nilimkumbatia. Muda huo Zainabu alikuwa anatetemeka kwa hisia kali za huba. Na muda mfupi baadaye tulijikuta tukimezwa na ulimwengu wa huba.

Ilikuwa kama tupo kwenye kisiwa cha maraha kilichoandaliwa maalumu kwa ajili yetu. Tukayasahau yote, tukajiona kama tuliozaliwa upya. Hatukuishiwa na hamu hadi tulipohisi kuchoka tukiwa hoi bin taabani, ndipo tukalala.

Haikuchukua muda nikamsikia Zainabu akikoroma taratibu. Lakini kwangu haikuwa hivyo, sikuupata usingizi na mawazo yangu yalikuwa juu ya Rehema. Nilijiuliza huyu Rehema ni nani? Kwa nini anijie akilini wakati nilikuwa simjui? Je, ni yule msichana wa kwenye ndoto?

Sasa mawazo juu ya Rehema yaliendelea kupita kichwani kwangu na kuninyima usingizi huku yakiufanya usiku kuwa mrefu sana kwangu. Niliishia kugaagaa tu pale kitandani.

* * *

Endelea kufuatilia...
 
woiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiii bishop pliz plz
 
woiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiiii bishop pliz plz
Tomorrow si ndo kesho?...
 
Mgeni mwema.jpg

182

Mimi si mwizi…




Saa 12:00 alfajiri…

MVUA ya rasharasha ilikuwa inanyesha. Hali ya hewa ilikuwa baridi ikiambatana na upepo wa wastani. Muda huo watu wachache walikuwa wanaonekana barabarani.

Kama kawaida yangu, nilikuwa nimedamka alfajiri na mapema na kufanya mazoezi ya viungo kisha nikaingia barabarani, katika barabara kuu ya kuelekea Morogoro, kufanya mazoezi ya kukimbia mbio za taratibu umbali wa kilomita zisizopungua tano. Nilikuwa nimevaa track suit maalumu za mazoezi na raba nyepesi nyeusi miguuni.

Wakati nakimbia nikawa nasikia sauti za watu zikiita “mwizi, mwizi!” zikitokea upande wa Chuo cha Maofisa Tabibu Kilosa (COTC). Kelele hizo zilianzwa na mama mmoja ambaye huenda alikuwa amekumbana na kibaka muda ule wa alfajiri.

Sikujali, niliendelea kukimbia taratibu nikiifuata barabara hiyo, mara nikamwona mtu mmoja akikimbia na kuingia kwenye kichochoro kimoja chembamba jirani na duka la dawa la Chigolo huku akitimua mbio zisizo za kawaida.

Wakati akiingia kwenye kile kichochoro nilimwona akigeuka nyuma kwa wasiwasi, na hapo nikawaona wanaume kadhaa wakimkimbiza, lakini kila sekunde kadhaa watu hao walikuwa wanaongezeka na mikononi walishika mawe, mapanga na marungu.

Kuna sauti ndani yangu ilinitaka nijiunge na watu hao kumkimbiza yule mwizi lakini nikaipuuzia na kuendelea na mbio zangu za taratibu. Haikuchukua muda mrefgu nikamwona tena yule mtu akiibuka, safari hii aliibukia mbele yangu na sasa akawa anakuja kwenye uelekeo wangu, hapo nikajiandaa kumkamata lakini aliponikaribia akapiga chenga na kuingia upande wa kushoto, akapotelea kwenye nyumba za jirani zilizokuwa zimezungukwa na miti mikubwa ya vivuli.

Nikampuuza na kuendelea na mazoezi yangu ya kukimbia. Lakini sikufika mbali, ghafla nilishtukia watu wakinivamia na kuanza kunishushia kipigo kikali kwa hasira, pengine walidhani labda ni yule mwizi waliyekuwa wakimkimbiza hasa ikizingatiwa kuwa kulikuwa bado na kiza na hivyo ilikuwa vigumu kunitambua. Kuona vile hofu ya kifo ikaanza kutambaa kwenye mwili wangu.

“Jamani mimi si mwizi mnayemtafuta!” nilijitetea huku nikipangua mawe na marungu kutoka kwa watu waliokuwa na hasira lakini hakukuwa na yeyote aliyeonekana kunisikiliza.

Kila nilipojaribu kujitetea ndivyo umati mkubwa wa watu ulivyozidi kunijia. Niliwashuhudia baadhi yao wakiwa wamebeba magongo, mawe, mapanga na hata silaha nyingine na walizidi kunijia na kunishushia kipigo. Kazi yangu ikawa kujihami zaidi kwa kupangua silaha zao huku nikijaribu kuwafahamisha kuwa sikuwa mwizi.

Hiyo yote haikusaidia, kwa kuwa watu walikuwa wengi vipigo vyao vilianza kunizidia na hapo nikaanza kuhisi harufu ya kifo. Nilihisi ujasiri ukianza kunipotea taratibu na moyo wangu ukipoteza utulivu, jasho jingi lilianza kunitoka sehemu zote za mwili wangu.

“Msinipige jamani mimi si mwizi… nipelekeni kituo cha Polisi… mimi si mwizi!” nilijitetea lakini haikusaidia kwani waliendelea kunishushia kipigo huku kelele na mayowe ya “Ua mwizi huyo!” zikizidi kutawala kwenye masikio yangu.

Sikuwa na namna nyingine isipokuwa kuipambania roho yangu maana kama ningejilegeza wangeweza kunidhuru au hata kuniua kabisa.

Wakati nikipangua rungu lililokuwa limerushwa nyuma usawa wa kichwa changu, nikashtukia nikipigwa na kitu kizito kwenye paji la uso wangu. Nilihisi damu ya moto ikinibubujika na kulowanisha nguo nilizovaa. Pigo hilo lilinipata barabara na kunipa kisulisuli lakini sikudondoka. Hata hivyo nilihisi nguvu zikianza kuniishia.

Ghafla kisogo changu kilipigwa na kitu kama rungu au pengine ulikuwa mpini wa jembe na kunifanya nianguke kifudifudi. Nilitaka kuinua mikono yangu kuonesha ishara ya amani lakini sikuweza. Nikashuhudia vipigo vya kila namna vikizidi kumiminika mwilini mwangu kama maji. Sasa mwili wangu wote ulikuwa unaniuma sana kama kidonda.

Kisha mtu mmoja alinipiga tekekwenye mbavu zangu lililonigeuza na kunilaza chali. Nilikuwa nimeishiwa na nguvu mwilini, na hata nilipojaribu kutoa yowe kutokana na maumivu niliyoyapata sauti yangu ilikuwa dhaifu sana. Sasa moyo wangu ulikuwa unanguruma sana kama uliokuwa ukipambana na kazi isiyo ya kiasi chake. Macho yangu nayo taratibu yalianza kupoteza nguvu ya kuona. Hatimaye shughuli mbalimbali za mwili wangu nazo nikazihisi kuwa zilikuwa mbioni kusitisha utendaji wake.

Kwa mbali nilianza kusikia kelele za mayowe kutoka kwa wanawake waliokuwa wakishuhudia kipigo kile waliokuwa wakilia kwa uchungu. Kisha nikamsikia mtu mmoja akitoa wazo, “Kabla hatujamchoma moto ni vizuri tukamtambua kwanza mwizi wetu.”

Niliposikia hivyo nikataka niinuke lakini sikuweza, nikajikakamua kwa kutumia nguvu zangu zote ili niweze kuinuka lakini pia sikuweza na mara nikahisi fahamu zangu zikinitoka taratibu. Nilijaribu kupiga kelele za kuomba msaada lakini sauti yangu ilikuwa haitoki na badala yake niliisikia ikitengeneza mwangwi ndani ya kichwa changu.

Kisha nikaanza kuona nyota nyota na mara pazia la giza likatanda kwenye macho yangu huku mwili wangu ukilegea. Mapigo yangu ya moyo nayo yakaanza kudorora, mwishowe nikahisi roho yangu ikifika njia panda…

* * *

Endelea...
 
Mgeni mwema.jpg

183

Saa 10:30 jioni…

Giza liliendelea kutanda sehemu zote kiasi kwamba lilikuwa linanizuia kuona vizuri mbele japo nilikuwa limewasha taa. Nikiwa kwenye usukani ndani ya gari aina ya Toyota Lexus RX Hybrid la rangi ya maruni, nilijitahidi kuendesha kwa umakini sana, mara giza likatoweka na mwanga mkali wa mchana ukanipiga kwenye macho yangu, na hapo nikajikuta nikibabaika sana baada ya kuliona lori kubwa lenye tangi la dizeli likija kwa kasi mbele yangu.

Nilijitahidi kukanyaga breki kwa nguvu huku nikijaribu kuepuka mgongano na hatari lakini wapi! Lile lori lenye tangi la dizeli lilitupamia, likatuchota na kututupa kando kabisa ya barabara. Kisha likalipuka na moto mkubwa ukasambaa hadi kwenye gari letu na hata pale nilipokuwa nimeangukia.

Niliwahi kuinuka, na bila ya kujikung’uta vumbi nikataka nikawahi kumwokoa mwanamke niliyekuwa naye ndani ya gari lakini kabla sijafanya hivyo nilihisi akili yangu ikianza kuhama na hapo hapo nikaanza kupitiwa na usingizi mzito sana, usingizi uliokuwa mfano wa kifo!

Sikutaka kufa kizembe! Niliamua kujikakamua kwa nguvu huku nikiyafumbua macho yangu, mwanga mkali ukanipiga tena machoni… na hapo nikajikuta nipo kitandani! Nilipotazama vizuri nikagundua kuwa nilikuwa nimelala katika kitanda cheupe cha chuma. Kando ya kitanda hicho kulikuwa na kabati dogo na juu ya kabati hilo kulikuwa na sahani ndogo ya aluminium iliyokuwa na bandeji, dawa ya kukaushia vidonda, bomba la sindano, glavu na dawa za vidonge ambazo sikuzifahamu.

Dah! Kumbe ilikuwa ndoto! Nilijiuliza lakini nikajikuta nikipingana na mawazo yangu. Ndoto gani iliyonipeleka hadi kitandani, hospitali? Sasa sikuwa na uhakika kama ilikuwa ni ndoto au ni tukio la kweli la ajali lilikuwa limetokea.

Nilitaka kuhakikisha kama kweli nilikuwa katika kitanda cha hospitali, nikachunguza zaidi na kuona kando kidogo ya kitanda nilicholalia kulikuwa na stendi ndefu ya chuma ya kitabibu iliyokuwa imetundikiwa chupa ya maji yaliyoonekana kuchanganywa na aina fulani ya dawa. Sasa macho yangu yalipata uhai zaidi, nikauona mrija ukishuka kutoka kwenye ile chupa hadi kwenye mkono wangu wa kulia.

Niliiangalia ile chupa iliyotundikwa kwenye chuma kwa umakini na kushusha pumzi. Ni kweli nilikuwa hospitali lakini sikujua nilikuwa nimelazwa katika hospitali gani.

Nilipojichunguza zaidi nikagundua kuwa nilikuwa nimefungwa plasta ngumu (P.O.P) kwenye mkono wangu wa kushoto ambao bila shaka ulikuwa umevunjika. Niliyazungusha macho yangu kutazama huko na kule na kuwaona baadhi ya watu waliokuwa na majeraha mbalimbali kwenye miili yao na baadhi ya viungo vyao vilifungwa vyuma.

Nikagundua kuwa nilikuwa nimelazwa kwenye wadi maalumu ya majeruhi ingawa bado sikujua nililazwa katika hospitali gani na nilifikaje pale! Sikuwa na hakika kama nililetwa pale kwa gari, mkokoteni, machela au nilibebwa mgongoni kwa kuwa sikuwa na fahamu yoyote nilipokuwa naletwa hapo. Kwangu, hilo halikuwa la muhimu sana. Lililokuwa la muhimu ni kwamba nilikuwa hai.

Kisha niliyafumba macho yangu nikijaribu kutafakari na nilipoyafumba tena baada ya kitambo fulani nikajaribu kuipa utulivu akili yangu, ilinichukua takriban dakika nzima nikijiuliza kuhusu ajali ile niliyoishuhudia. Hata hivyo hisia zangu zilinitanabaisha kuwa nilikuwa nimetoka kwenye usingizi mzito sana mfano wa kifo na taswira fulani zilikuwa zinabadilika zikinitoa toka utambulisho mmoja kwenda utambulisho mwingine.

Nilijihisi kama vile nilikuwa nimo ndani ya tukio fulani la kisinema lioneshalo mambo yaliyopita ambalo hujulikana kama ‘flashback’, lakini tukio hili lilikuwa halisi na lilitokea katika maisha yangu halisi!

Picha mchanganyiko mfano wa matukio katika filamu zilizunguka kichwani kwangu, zilikuwa mchanganyiko wa taswira zilizomwonesha mwanamume mmoja aliyekuwa anapigwa na watu wenye hasira, na wakati huo huo ajili mbaya sana na magari kugongana na kisha moto mkubwa kulipuka zikipanda juu ya ile taswira ya kwanza!

Mara nikakumbuka jambo; nilimkumbuka mke wangu Rehema, sikujua alikuwa wapi muda ule! Je, yeye alikuwa amesalimika kwenye ile ajali niliyoishuhudia? Moyo wangu ulianza kupoteza kabisa utulivu pale nilipojikuta nikishindwa kupata majibu ya maswali yangu.

Nilishusha pumzi huku nikijitahidi kuupisha utulivu kichwani mwangu lakini bado akili yangu ilikuwa inasumbuka sana. Nilitafakari kuwa, kwa vyovyote mimi nilikuwa nimesalimika lakini vipi kuhusu Rehema?

Nilijikuta nikiwa na namna fulani ya mashaka juu ya kilichokuwa kimetokea baada ya ajali ile, na wakati wote nilipokuwa nimepoteza fahamu zangu. Sikujua nilikuwa nimepoteza fahamu hizo kwa muda gani! Saa kadhaa? Siku moja? Mbili? Tatu? Au majuma?

Nilitaka kujiinua toka pale kitandani lakini nikahisi kichwa changu kilikuwa kizito na pia nilihisi kizunguzungu kikali, na mwili wangu ulikuwa umedoofika sana mithili ya mlevi aliyeamka na uchovu mkali wa pombe.

Niliinua mkono wangu wa kulia wenye mrija wa maji na kuupeleka kichwani, mkono ukagusa bandeji iliyokuwa imefungwa kukizunguka kichwa changu. Hapo hapo nikagundua kuwa nilikuwa nimeumia kichwani.

Nikiwa bado natafakari nikashtushwa na sauti ya upole ya mwanamke aliyesema “Mgeni!”, nilihisi kuwa alikuwa kasimama kando ya kitanda changu ingawa sikujua alikuwa amefika pale muda gani. Hivyo niligeuza shingo kumtazama. Na hapo nikagundua kuwa alikuwa muuguzi wa ile wadi kutokana na aina ya mavazi aliyokuwa ameyavaa.

Kwa mwonekano tu alionekana kuwa na miaka kati ya therathini na therathini na tano. Umbo lake lilikuwa kubwa la kuvutia, mweupe kwa asili, lakini alionekana kujiongezea kwa vipodozi vilivyomfanya kuvutia zaidi. Hakuwa mwanamke wa kumtizama mara moja tu ukamwacha, kwani alivutia sana kutokana na umbo lake lililokuwa mfano wa umbo la nyigu. Alikuwa amebeba faili na kalamu.

“Vipi Mgeni, unajisikiaje?” yule muuguzi aliniuliza baada ya kugundua kuwa nilikuwa nimeamka, aliponiona nikimtazama kwa mshangao aliachia tabasamu la kunifariji usoni kwake.

“Unaongea na mimi?” nilimuuliza yule muuguzi kwa mshangao.

“Ndiyo kwani wewe si Mgeni?” yule muuguzi aliniuliza kwa mshangao huku akinikazia macho.

“Mgeni! Wa nani?” nilimuliza huku nikishindwa kuuficha mshangao wangu.

“Si mgeni wa mtu ila ndiyo jina lako… Mgeni Mwema au sivyo?” yule muuguzi aliuliza tena huku akionekana kunishangaa kidogo baada ya kuniona nikishangazwa na jina hilo.

“Hapana!” nilimjibu kisha nikaongeza, “Naitwa Jason Sizya,” nilijibu huku nikimtazama yule muuguzi usoni kwa umakini.

“Mh! Tangu lini umeanza kuitwa jina hilo?” yule muuguzi aliuliza huku mshangao ukizidi kutawala usoni kwake. Alinitazama kwa namna ya kunionea huruma, pengine alidhani labda nilikuwa nimerukwa na akili zangu.

“Sikuelewi! Kulitumia tangu lini kivipi wakati hilo ndo jina langu miaka yote! Sijui hili jina jingine wewe umelitoa wapi?” nilihoji huku nikimkazia macho.

Endelea...
 
Mgeni mwema.jpg

184

“Mmh, makubwa!” yule muuguzi aliguna na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.

“Kwa vyovyote utakuwa umenichanganya na mtu mwingine, dada!” nilimwambia baada ya kumwona akiwa ameduwaa akinitazama kwa mshangao kama aliyeona kitu fulani cha kustaajabisha. Kisha nikaongeza, “Kwani hapa nipo wapi?”

“Upo hospitali, na mimi ni muuguzi wa wadi hii!” yule muuguzi aliniambia huku uso wake ukionesha wasiwasi kidogo.

“Najua kuwa nipo hospitali, wodini… ila nataka kujua nipo hospitali gani?” nilimuuliza tena huku nikiilamba midomo yangu iliyokuwa imekauka.

“Hospitali ya Wilaya ya Kilosa,” yule muuguzi alinijibu kwa sauti tulivu. Macho yake yalitulia kwenye uso wangu.

“Kilosa? Tangu lini nimelazwa hapa?” nilizidi kumsaili yule muuguzi huku mshangao wangu ukizidi.

“Leo ni siku ya tatu tangu uletwe hapa na jamaa zako ukiwa huna fahamu,” yule muuguzi alinijibu kwa utulivu huku akiendelea kunitazama kwa tuo.

“Kwa nini niletwe hapa Kilosa?” nilimuuliza tena kwa mshangao.

“Kumbe ulitaka upelekwe wapi! Kwani unajua nini kilikutokea hadi ukaletwa hapa?” yule muuguzi aliniuliza.

“Najua…!” nilimjibu kisha nikaongeza, “Tulikuwa tunatoka Arusha kwenye fungate na tunakwenda Dodoma, tukapata ajali eneo la Makutupora. Ninachoshangaa imekuwaje kutoka Makutupora niletwe huku Kilosa badala ya Dodoma au hata hospitali iliyo karibu na hapo?”

Na hapo nilimwona yule muuguzi akinitazama kwa mashaka mno, kwa namna ambayo sikuweza kupata tafsiri kabisa! Macho yake yaliongezeka ukubwa na kuwa ya duara na uso wake ulionesha kupambwa na mashaka makubwa. Sikujua alidhani labda nilikuwa nimerukwa na akili zangu!

“Samahani… kwani mke wangu yuko wapi?” nilimuuliza tena yule muuguzi na kumwona akishtuka kidogo, huenda nilikuwa nimemzindua toka kwenye mawazo yake.

“Alikuwepo hapa mchana alipoletea chakula akidhani labda umezinduka,” yule muuguzi alinijibu na kuitazama saa yake ya mkononi. “Hata hivyo bado dakika chache tu ufike muda wa kuona wagonjwa. Vuta subira huenda yeye akakufahamisha vizuri.”

Niliposikia hivyo nikapata matumaini nikiamini kuwa kumbe Rehema alikuwa mzima, nikaamua kujipa subira nikiamini kwamba angenifafanulia kila kitu.

“Kwa hiyo yeye ni mzima wa afya?” nilimuuliza yule muuguzi nikitaka kuhakikisha Rehema hakuwa na majeraha.

“Yeye hana shida ila mtoto ndiyo anaumwa,” yule muuguzi aliniambia jambo ambalo lilinifanya nijikute nikishangaa mno.

“Mtoto gani?” niliuliza kwa mshangao.

“Mtoto wenu, Mariam… kwani huna mtoto?” yule muuguzi alisema.

“Hatuna mtoto, ndiyo kwanza tumetoka kuoana,” nilimjibu huku nikianza kupata mashaka kuwa huenda alikuwa amenichanganya na mtu mwingine.

Kwa kusema hivyo nilimwona yule muuguzi akifungua mdomo wake kutaka kusema neno kisha akasita na kunitazama kwa mshangao mkubwa. Katikati ya mshangao wake alibetua midomo yake huku akinitazama kwa mashaka, “Daah! Basi kuna shida kubwa sana! Itabidi niongee na daktari wako.”

Sikusema neno, nilibaki na mshangao. Yule muuguzi akapiga kofi dogo la mshangao na kuongeza, “Mara sijui jina lako ni Jason nani, mara ooh nimepata ajali Makutupora, mara tumetoka kuoana! Dah… haya sasa makubwa!”

Nami nilimshangaa sana yule muuguzi, nilihisi kuwa kama ni kuchanganyikiwa basi ni yeye aliyekuwa amechanganyikiwa na si mimi. Nilimwona akishusha pumzi za ndani kwa ndani huku akiendelea kunitazama kwa namma ambayo ilinidhihirishia kuwa alikuwa kama anaona kitu cha kustaajabisha sana.

Huenda alidhani jeraha nililopata kichwani lilikuwa limeichanganya akili yangu. Kisha alitingisha kichwa chake na kuanza kuondoka.

“Nesi, samahani…” nilimwita yule muuguzi kabla hajatokomea na kumfanya ageuke kunitazama kwa wasiwasi, uso wake ulikuwa umejaa mashaka.

Alinitazama kwa kitambo akionekana kama aliyekuwa akijishauri iwapo arudi au aendelee na safari yake, kisha nikamwona akishusha pumzi na kusema, “Unasemaje, nisubiri nakuja sasa hivi.” Kisha aliondoka haraka na kuniacha nikiwa nimeshangaa sana. Nilimsindikiza kwa macho wakati akiondoka.

“Bila shaka watakuwa wamechanganya majina! Mgeni Mwema ndiyo nani?” nilijiuliza mwenyewe huku nikigeuza shingo yangu kuwatazama wagonjwa wengine mle wodini.

Hata hivyo, niliamua kuupisha utulivu kichwani mwangu huku nikiyazungusha macho kutazama mle wodini kisha nikayarudisha tena kule alikoelekea yule muuguzi. Na hapo fikra zangu zikahamia kutafakari juu ya Rehema na jamaa zangu.

Nilijiuliza kama kulikuwa na dosari yoyote juu yangu au pengine ni kweli nilikwisha anza kuchanganyikiwa! Na kwa nini yule muuguzi asisitize kuwa jina langu ni Mgeni wakati nilijua fika kuwa si langu? Hadi wakati huo nilikuwa na uhakika wa asilimia mia moja kwamba nilikuwa sahihi.

Swali jingine likawa; ni kweli Rehema alikuja pale hospitali akiwa na mtoto anayeitwa Mariam? Huyo Mariam alikuwa mtoto wa nani? Kila nilipojaribu kuwaza zaidi nilihisi kuchanganyikiwa mno. Sasa nilimwomba Mungu anipe unafuu haraka ili nitoke pale hospitali na kurudi nyumbani.

“Mgeni!” nilishtushwa na sauti ya mwanamume aliyeita kwa furaha huku akiharakisha kuja pale kitandani kwangu. “Mungu mkubwa, hatimaye umeamka?”

Nilishangaa sana na kumtazama yule mwanamume aliyeyasema hayo, kwa umakini, alikuwa mrefu na mwembamba akiwa amevaa suruali ya bluu ya dengrizi na shati la mikono mirefu la rangi ya samawati. Mkononi alikuwa amebeba mfuko mwekundu.

Mwanamume huyo alikuwa ameongozana na wasichana wawili, warembo ingawa walionekana wamechoka, mmoja wao alikuwa na mtoto wa miaka takriban mitatu. Wote walikuwa wakinitazama kwa furaha wakiwa hawaamini macho yao. Yule msichana aliyekuwa na mtoto alinyoosha mikono yake juu kumshukuru Mungu kisha akaharakisha kuja pale kitandani na kunikumbatia kwa furaha huku akitokwa na machozi ya furaha machoni.

Mwanzoni nilidhani labda walikuwa wamenifananisha na pindi wakigundua wangeniomba radhi na kuondoka lakini nilipomwona yule msichana mwenye mtoto akizidi kunikumbatia kwa nguvu na kuning’ang’ania huku akisema, “Jamani mume wangu…” nikamtazama kwa mshangao kisha nikayahamisha macho yangu kutoka kwa msichana huyo na kuwatazama wale wengine wawili. Nao walinitazama kwa furaha wakiwa hawana wasiwasi wowote.

“Nyinyi ni akina nani?” niliwauliza wale watu kwa mshangao huku hasira zikianza kuchipua ndani yangu, niliwakazia macho kwani nilihisi kitendo kile cha kuchangamkiwa na watu nisiowajua kilikuwa ni cha kutaka kucheza na akili yangu.

Wale watu wakaonekana kushtuka kidogo baada ya swali lile na kunitazama kwa mshangao mkubwa, kisha wakatazamana.

“Mume wangu, inamaana umenisahau kama ni mimi Zainabu mkeo?” yule msichana mwenye mtoto ambaye sasa nilimtambua kwa jina la Zainabu aliniuliza kwa mshangao huku akijaribu kunishika begani lakini niliusukuma mkono wake.

Endelea...
 
Mgeni mwema.jpg

185

“Nani mumeo? We mwanamke vipi! Umechanganyikiwa!” nilimuuliza Zainabu huku nikianza kuchukizwa na mambo yaliyokuwa yakiendelea pale hospitali. Nilitamani ninyanyuke na kuondoka lakini haikuwezekana.

“Aah Mgeni, hebu acha masikhara yako bwana! Inamaana umetusahau? Au umeanza kuchanganyikiwa?” yule mwanamume aliniuliza huku akionekana kushangaa kidogo na kisha akaachia kicheko hafifu.

“Kwani na wewe ni nani?” nilimuuliza yule mwanamume huku nikimtazama kwa mshangao.

“Ni mimi Almasi, best wako…” alisema yule mwanamume, nikamkatisha kabla hajaendelea kuongea upuuzi wake.

“Hivi ninyi watu vipi, ni nani aliyewaambia mimi naitwa Mgeni? Mbona mnataka kunichanganya akili yangu!” nilifoka kwa hasira huku nikiwa nimedhamiria kuinuka lakini nikasita baada ya kumwona muuguzi akija haraka eneo lile huku akiwa ameongozana na daktari.

Yule daktari alikuwa mwanamume mfupi mnene na rangi ya ngozi yake ilikuwa ni maji ya kunde, akiwa na umri usiopungua miaka hamsini alionekana kuwa na misuli imara ya mikononi iliyotuna kikamilifu na kumfanya aonekane kama bondia mkongwe. Alikuwa na upara mpana uliokuwa unawaka na uso wake ulikuwa mpana, miwani yake mikubwa ilikuwa imeyahifadhi macho yake makubwa.

Alikuwa amevaa suruali nyeusi, shati la rangi ya dhahabu lililokuwa na mistari ya bluu na juu ya lile shati alivaa koti refu jeupe na kuning’iniza shingoni kwake kifaa cha kupimia ambacho nilikifahamu, kitaalamu kiliitwa stethoscope.

“Afadhali umekuja, daktari…” nilianza kusema baada ya yule daktari kunifikia.

"Pole sana kijana, kwani kuna nini?" yule daktari aliniuliza kwa sauti ya upole huku akinitazama kwa wasiwasi.

“Hawa watu siwaelewi kabisa, kuanzia huyu nesi wako. Naona kama wananichanganya akili yangu tu…” nililalamika huku nikielekeza macho yangu kwa wale wageni waliokuja kuniona.

“Ki vipi?” yule daktari aliuliza huku akiendelea kunitazama kwa wasiwasi.

“Wanajifanya kunifahamu na wanalazimisha kuniita jina lisilokuwa langu wakati siwajui na wala sijawahi kuwaona!” nilisema huku nikiwa nimekerwa sana.

“Una uhakika hujawahi kuwaona?” yule daktari aliniuliza kwa sauti tulivu. Alinitazama kwa tuo usoni na hakuwa anapepesa macho yake.

“Kweli siwajui kabisa!” nilisema huku nikiuinua mkono wangu wa kulia uliochomekwa mrija wa maji na kupitisha kidole changu cha shahada kwenye shingo yangu kama ishara ya kiapo.

“Hata huyu pia humjui?” yule daktari aliuniliza tena kwa mshangao huku akielekeza kidole chake kumwelekea Zainabu.

“Si yeye tu, hata huyu anayejiita Almasi simjui. Ndiyo kwanza leo nawaona!” nilisema kwa msisitizo.

“Dah!” yule daktari aliguna huku akinikazia macho, kisha alimtazama Zainabu kabla hajayahamishia macho yake kwa yule mtoto.

“Na huyu mtoto pia humfahamu?” yule daktari aliniuliza. Nikaanza kukereka.

“Daktari, kama mama yake simfahamu nitamfahamu vipi mtoto wake?” nilimuuliza yule daktari kwa sauti iliyoonesha wazi kuwa nimekerwa. Yule daktari alinitazama kwa kitambo fulani kisha akashusha pumzi na kuwageukia wale wageni.

“Eti jamani… kwani kuna nini kinaendelea hapa, mbona kama sielewi?” yule daktari aliuliza kwa mshangao.

“Hata mimi nashangaa, hata sijui niseme nini!” Zainabu alisema kwa mshangao uliochanganyika na huzuni, kisha akaongeza, “Inashangaza sana, mtu umeishi naye kwa takriban mwaka, mkisaidiana katika shida na raha leo anakukana mbele ya watu kwamba hakutambui, unadhani utafanyaje!”

“Ila mimi naamini kila kitu kitakuwa sawa, ni suala la muda tu!” alidakia Almasi huku akinitazama kwa namna ya kukata tamaa.

“Kwani wewe na huyu bwana uhusiano wenu ukoje?” daktari alimuuliza Almasi.

“Huyu ni best wangu sana, na pia ni mshauri wangu mkubwa…” Almasi alisema kwa kujiamini kisha akamgeukia Zainabu na kumgusa kwenye bega, “na huyu hapa ndiye mkewe.”

Sasa akili yangu ilianza kufanya kazi haraka haraka. Tukio la kuchangamkiwa na watu nisiowafahamu huku wakiniita jina lisilo langu ikanifanya kuikumbuka filamu moja ya kipelelezi inayoitwa “Jewel Thief” iliyotoka mwaka 1967 nchini India.

Kwenye filamu hiyo kijana Vinay anayeishi na wazazi wake jijini Bombay, baba yake akiwa Kamishna wa Polisi, aliondoka nyumbani na kwenda kutafuta kazi katika duka kubwa la vito la tajiri Vishamber Nath.

Muda mfupi tangu apate kazi watu mbalimbali wakaanza kumjia na kumwita kwa jina la Amar, alipolikana jina hilo wakamwambia kuwa alifanana sana na Amar, bosi mmoja aliyekuwa mwizi maarufu wa vito.

Katika muda huo mfupi wa kufananishwa na Amar, ikatokea binti wa tajiri Nath aliyeitwa Anju akavutiwa mno na Vinay eti akidhani ni Amar, na urafiki wao ukazaa mahaba.

Sasa watu wakaacha kumwita Vinay kwa jina lake na badala yake wakawa wanamwita Amar au “Prince Amar” huku jina lake halisi likifa kifo cha mende. Kabla hajakaa sawa akaibuka msichana mwingine Shalini na kudai Amar ni mchumba wake aliyemvalisha pete. Shalin alikuwa amefuatana na kaka yake.

Katikati ya mkanganyiko huo mambo yakajifunga zaidi baada ya Vinay kukutana na mwimbaji mrembo wa klabu ya usiku (Helen!) aliyeeleza kwamba anamjua Amar na kwamba anafanana sana na Vinay. Sasa wasichana wengi warembo wakaanza kumtaka huyu ‘shujaa Amar’. Muda wote warembo hawa wakawa wanamzunguka Vinay “eti” wakifikiri ndiye Amar!

Jeshi la polisi likiongozwa na baba wa Vinay, wakaanza kuhaha kumsaka Amar kila kona, na muda si mrefu utambulisho halisi wa Amar na Vinay ukageuka kuwa mkanganyiko. Kumbe yote haya yalipangwa na tajiri Nath, akiwaandaa watu, ili kuichanganya akili ya Vinay ajidhani yeye ni Amar (ambaye kimsingi hakuwepo) na baadaye amtumie kwenye mipango ya kihalifu...

Baada ya kumbukumbu za filamu hiyo kupita kichwani kwangu nikahisi kuwa hata mimi nilikuwa nachezewa akili kama ilivyokuwa kwenye kisa hicho cha filamu ya Jewel Thief. Sikutaka kabisa kuruhusu jambo kama hilo linitokee.

Doctor, I think they are f**king with a wrong guy, I don’t even know them!” (Daktari, nadhani wamekosea mtu wa kumfuata, hata siwajui!) nilisema kwa hasira na kuongeza, “Hapa kuna mchezo mnataka kuucheza ili kunichezea akili yangu, naapa hamtaweza…”

Calm down, Mister…” (Tulia, bwana…) yule daktari alijaribu kunituliza.

You must tell them, I’m not an idiot,” (Waambie kuwa mimi si zuzu) nilifoka.

“Lakini pia hawa si wajinga… hawawezi kutoka huko walikotoka wakaacha shughuli zao ili kuja kukuchezea akili zako. Kama hujui ni hawa hawa ambao wamekuwa wakikuhudumia siku zote tangu umeletwa hapa,” yule daktari alisema kwa sauti yenye utulivu huku akinikazia macho. Kisha akaniuliza, “kama wewe si Mgeni, basi jina lako ni nani?”

“Naitwa Jason Sizya,” nilijibu kwa kujiamini.

Real?” yule daktari aliniuliza kutaka kupata uhakika wa kile nilichokuwa nikikisema.

Endelea...
 
Mgeni mwema.jpg

186

For sure! Kwa nini niongope? Naweza hata kuthibitisha kuwa mimi naitwa Jason Sizya!” nilisema kwa msisitizo huku nikishusha pumzi ndefu.

“Na unaishi wapi?” yule daktari aliniuliza tena.

“Makazi yangu yapo Kahama,” nilisema na kuwafanya watu wote kunishangaa.

“Sasa imekuwaje uko hapa?” yule daktari aliendelea kunisaili kwa sauti tulivu ya upole. Namna alivyokuwa akiniuliza ilikuwa kama vile alikuwa anaongea na mtoto wake mpendwa.

“Hapo ndiyo sielewi! Ninachokumbuka tulikuwa safarini mimi na mke wangu tukitoka kwenye fungate Serengeti, tukapata ajali eneo la Makutupora…” nilisema huku nikijaribu kukumbuka kilichotokea lakini sikukumbuka. “Baada ya hapo sikumbuki tena kilichoendelea hadi leo najikuta nipo hapa,” nilisema kwa huzuni.

Watu wote walipigwa na butwaa na walikuwa wananitazama kwa mshangao mkubwa kana kwamba nilikuwa kiumbe cha ajabu kutoka sayari ya mbali. Nikawaona yule daktari na Almasi wakitazamana kisha daktari akampa ishara fulani Almasi iliyomaanisha kuwa sikuwa katika akili yangu ya kawaida, kwamba huenda nilikuwa nimechanganyikiwa au kupata matatizo ya akili yaliyonifanya nijidhani kuwa mtu fulani tofauti, kumbe sivyo!

“Wala sijachanganyikiwa, daktari, nina akili timamu na nina uhakika na hiki ninachokisema,” nilimwambia yule daktari ili kumtoa shaka kwamba nilikuwa timamu na wala sikuwa nimechanganyikiwa.

Okay, nimekuelewa…” hatimaye yule daktari aliniambia na kushusha pumzi za ndani kwa ndani. Kisha kikatokea kimya kifupi, kila mmoja alionekana kuwaza.

“Umesema mlikuwa mnatoka fungate Serengeti na unaishi Kahama?” yule daktari aliniuliza huku akionekana kustaajabu kidogo kisha akaongeza kabla hata sijajibu swali lake, “na unaweza kuniambia mkeo anaitwa nani na yuko wapi ili tumjulishe?”

“Anaitwa Rehema Mpogoro ila sijui alipo kwa sasa… na tulikuwa tunakwenda Dodoma kwa mjomba wangu, Mchungaji Edwin Ngelela…” nilisema kisha nikanyamaza kidogo baada ya kukumbuka kuwa pale Kilosa ni nyumbani kwao rafiki yangu, Olivia Mkuro. “Pia nina jamaa yangu ambaye kwao ni hapa hapa Kilosa, huyu akipatikana anaweza kuthibitisha haya nisemayo, anaitwa Olivia Mkuro, ni daktari wa afya ya akili.”

Nilimtaja Olivia japo sikuwa na uhakika kama alikuwepo Kilosa. Ila nafsi yangu iliniambia kuwa kwa kumtaja Olivia ingesaidia kuwatafuta hata ndugu zake ambao wangethibitisha na hivyo kuondoa utata.

Na hapo nikamwona yule daktari akishtuka kidogo, aligeuka kuwatazama akina Almasi kisha akayarudisha macho yake kwangu, alinitazama kwa kitambo fulani huku akionekana kufikiria jambo kabla hajashusha pumzi ndefu.

“Inamaana… dah, hebu ngoja kwanza…” yule daktari alisita kidogo na kunitazama kwa umakini zaidi akionekana kutatizika mno na jambo ambalo sikulijua. “Inamaana… wewe na yule Mr. Sizya wa Kahama aliyekufa kwenye ajali miezi tisa iliyopita eneo la Makutupora mkoje?”

“Sizya yupi aliyekufa kwenye ajali miezi tisa iliyopita eneo la Makutupora? Mbona sielewi!” nilimuuliza yule daktari kwa mshangao mkubwa huku nikistaajabu kusikia habari hizo. Zilikuwa habari mpya kabisa kwangu.

“Kwani hujawahi kuwa na ndugu anayeitwa Sizya? Yeye pia alikuwa rafiki wa Dk. Mkuro na alikufa kwa ajili ya gari ajali eneo la Makutupora alipokuwa anatoka Serengeti kwenye fungate akiwa na mkewe Rehema…?” yule daktari alisema na kunifanya nishtuke sana.

Kwa nukta kadhaa nilihisi moyo wangu ulisahahu mapigo yake, na yalipoanza nilijikuta nikivuta pumzi ndefu, kwa tabu sana. Nilimtazama yule daktari nikijaribu kukumbuka kama Olivia aliwahi kuwa na rafiki mwingine aliyepata ajali eneo la Makutupora miezi tisa iliyokuwa imepita, aliyeitwa Sizya ambaye mkewe pia aliitwa Rehema. Ni Sizya yupi? Hata hivyo sikupata jibu.

“Mbona sielewi… Sizya aliyepata ajali eneo la Makutupora akiwa na mkewe wakati wanatoka Serengeti kwenye fungate ni mimi, na ajali yenyewe imetokea juzi tu na si miezi tisa iliyopita!” nilimwambia yule daktari, na hapo nikamwona akinitazama kwa namna ya ajabu kidogo. Sikuelewa!

Are you sure kwamba ajali hiyo imetokea juzi?” yule daktari aliniuliza huku akiwa bado ananitazama kwa namna ya ajabu.

“Kwani mimi nimeletwa hapa lini?” nilimuuliza yule daktari, lakini hakunijibu, na badala yake aliinamisha kichwa chake, akaonekana kutafakari sana.

Oh my God! It can’t be…” hatimaye yule daktari alisema huku akishusha pumzi.

“Kwani vipi, daktari! Mbona sielewi kinachoendelea hapa? Kwani unamfahamu Olivia?” nilimuuliza yule daktari kwa wasiwasi kidogo.

“Dk. Mkuro ni binamu yangu, mtoto wa mjomba. Na hata kwenye msiba wa huyo rafiki yake Sizya aliyekufa kwa ajali nilimsindikiza. Lakini wewe… hebu ngoja kwanza…” yule daktari alisita tena akionekana kubabaika kidogo na kushusha pumzi.

“Msiba huo ulikuwa wapi?” nilimuuliza yule daktari kwa wasiwasi. Midomo yangu ilikuwa inatetemeka kwa hofu kubwa.

“Msiba ulikuwa Dodoma, kwa Mchungaji Edwin Ngelela…” yule daktari alisema, nikamkata kauli.

“Lini?” nilimuuliza yule daktari kwa mshangao huku moyo wangu ukipiga kite kwa nguvu. Nilihisi koo langu likikauka ghafla.

“Miezi tisa iliyopita…” yule daktari alisema huku akitoa simu yake ya mkononi. “Anyway… ngoja nimpigie simu Dk. Mkuro nimjulishe mambo haya ili tuone nini cha kufanya maana mimi mambo haya yananikanganya zaidi.”

“Kwani Olivia yupo hapa Kilosa, au yupo Botswana?” nilimuuliza yule daktari.

“Yupo, alikuja juzi kwenye msiba wa mdogo wake, Lucky…” yule daktari alisema kwa huzuni na kunifanya nishtuke sana.

“Lucky amekufa? Lini?” nilimuuliza yule daktari huku nikihisi kuchanganyikiwa zaidi.

Nilimfahamu Lucky Mkuro, mdogo wake Olivia. Yeye alikuwa mwalimu katika Shule ya Sekondari Mazinyungu, hapo hapo Kilosa. Nilikumbuka kuwa mara ya mwisho kuonana naye ilikuwa siku ya harusi yangu, alikuja na Olivia.

“Amekufa siku tano zilizopita aligongwa na gari eneo la Uhindini, na jana ndiyo tumemzika,” yule daktari aliniambia kwa huzuni. Kisha aliwageukia akina Almasi akiwa bado amechanganyikiwa kidogo. “Naomba mnifuate, nitahitaji kuongea na nyinyi ofisini kwangu.”

Wale watu waliangaliana kisha wakanitazama huku wakiwa wamekata tamaa, na hapo nikamwona Zainabu akinitazama kwa huzuni huku akilengwalengwa na machozi. Kisha wakaondoka wakimfuata yule daktari. Nilibaki nikiwa nimepigwa na butwaa.

Sasa nilijikuta nikiwa katika hali ya upweke mno na mashaka makubwa, nilijitahidi kuupisha utulivu kichwani mwangu nikiamini mambo yangekuwa sawa. Sikujua ilikuwa imetimia saa ngapi ingawa niliamini kuwa ilikuwa jioni.

Sasa fikra zangu zilihamia kutafakari juu ya habari za msiba wa Sizya uliokuwa umetokea miezi tisa nyuma kama nilivyoelezwa na yule daktari. Sikujua ni msiba upi aliokuwa akiuzungumzia kwani sikuwahi kuwa na ndugu aliyekufa kwa ajali miezi tisa nyuma eneo la Makutupora, na wala Olivia hajawahi kunieleza kama alikuwa na rafiki mwingine aliyeitwa Sizya. Au hii nayo ilikuwa drama nyingine?

Hata hivyo, kuna mambo yalizidi kunivuruga akili yangu, Iweje haya mambo yafananane? Yaani huyo Sizya na mimi wote tuwe marafiki wa Olivia! Wote tupate ajali eneo la Makutupora tukitokea Serengeti kwenye fungate! Wote tuwe na mke anayeitwa Rehema! Na wote tuwe na mjomba hapo Dodoma anayeitwa Edwin Ngelela!

Tofauti yetu iwe ni katika muda wa ajali tu, huyo Sizya nisiyemjua alipata ajali miezi tisa iliyopita eneo la Makutupora na kufa na mimi nikapata ajali eneo hilo hilo hivi juzi! Haya mambo yanakuwaje? Nilijiuliza sana pasipo kupata majibu!

Hata hivyo, nilijikuta nikimwomba Mungu anipe unafuu haraka ili nirudi nyumbani na maswali hayo yote ningeyapatia majibu yake baadaye. Lakini kwa muda huo nilihisi akili yangu ilikuwa haifanyi kazi sawa sawa na kwa namna fulani nilikuwa na mashaka juu ya habari nilizopewa na yule daktari. Kiwa vyovyote huu ulikuwa mchezo kama ule wa kwenye Jewel Thief!

Nikiwa pale kitandani moyo wangu uliendelea kupoteza utulivu lakini sikuwa na namna yoyote ya kufanya kwani chochote ambacho kilikuwa kimetokea nilipaswa kukubaliana nacho na pia ningekuwa tayari kukabiliana na chochote ambacho kingetishia usalama wangu.

Hata hivyo, kwa muda huo uzima wa afya yangu kilikuwa ni kipaumbele cha kwanza. Nilimeza funda kubwa la mate nikijitahidi kuyatowesha mawazo yale kichwani mwangu…

* * *

Endelea...
 
Mgeni mwema.jpg

187

Una mimba?




Saa 1:45 usiku…

“Jason!” nilisikia sauti ya mwanamke ikiniita, ikanishtua na kuniamsha toka usingizini. Sikuweza kufahamu ni wakati gani lepe hafifu la usingizi lilikuwa limefanikiwa kuziteka fikra zangu pale kitandani.

Niliyafumbua macho yangu na kugeuza taratibu shingo yangu, nikayapeleka macho kumtazama yule mtu aliyeniita. Na hapo nikakabiliana na macho ya watu wawili waliokuwa wamesimama mbele yangu wakinitazama kwa umakini.

Niliwatambua mara moja. Mmoja alikuwa ni yule daktari wa Hospitali ya Kilosa niliyeongea naye punde na mwingine alikuwa Olivia.

Olivia alikuwa amevaa gauni zuri la kitenge la mikono mirefu. Gauni hilo lilimbana kidogo na kulichora vyema umbo lake zuri lenye kiuno chembamba kilichoshikilia minofu laini ya mapaja yake. Shingoni alivaa kidani kilichozama katikati ya matiti yake ambayo yalikuwa bado yamesimama kama mkuki wa Kimasai. Miguuni alivaa sendoz ngumu za ngozi na begani alining’iniza mkoba mzuri wa kitambaa cha pundamilia.

Nilipomwona Olivia moyo wangu ulipata amani, na hapo nikajikuta nikiachia tabasamu la furaha. “Olivia!” nilimwita kwa mshangao uliochanganyika na furaha.

Oh my God! Jason!” Olivia alisema kwa mshangao huku akinitumbulia macho kama asiyeamini kuniona.

Nilihisi kuwa Olivia alikuwa amepatwa na mshtuko mkubwa baada ya kuniona. Alijishika kifua chake upande wa kushoto wa moyo akawa kama anayeyasikilizia mapigo ya moyo wake. Aliendelea kusimama pale pale pasipo kutingishika wala kupepesa macho yake kana kwamba alikuwa amepigiliwa misumali miguuni.

Nikajiambia kuwa huenda ni kweli yeye alikuwa mmoja wa walioamini kuwa nilikufa kwenye ajali na hivyo sasa alikuwa anatazamana na mzimu. Nilihisi nipo ndotoni na mara ningeamka kutoka usingizini ningekuta kila kitu kipo shwari.

Hata hivyo… akili yangu iliniambia kuwa ile haikuwa ndoto. Ni kweli mimi na Rehema tulipata ajali ya gari eneo la Makutupora wakati tukitoka Arusha. Moyo wangu ukazidisha mapigo yake na baridi nyepesi ikaanza kusafiri katika maungo yangu.

Yule daktari wa hospitali ile alitutazama kwa zamu, kwanza macho yake yalitulia kwenye uso wangu kisha akamtazama Olivia kwa umakini zaidi.

“Vipi daktari, mbona umeduwaa! Ni yeye, au?” yule daktari alimuuliza Olivia ili kupata uhakika.

Na hapo nikamwona Olivia akizinduka kutoka kwenye mshangao wake na kushusha pumzi. Alinisemesha kwa sauti yake tulivu huku akishindwa kuuficha mshangao wake, “Jason… I can’t believe it!

Kisha alinisogelea pale kitandani nilipokuwa nimelala na kunikumbatia kwa furaha. Hali ile ikanifanya nibabaishwe kidogo na harufu nzuri ya utuli aliojipulizia mwilini mwake.

Tulikumbatiana kwa takriban dakika nzima huku kila mmoja akionesha hisia za furaha kwa mwenzake. Olivia aliponiachia nilimtazama usoni nikajua kuwa alikuwa analia. Alikuwa anatokwa na machozi, huenda yalikuwa ni machozi ya furaha.

“Olivia, mbona umeshangaa sana kuniona!” nilimuuliza Olivia kwa mshangao.

Olivia alitingisha kichwa chake na kufuta machozi yaliyokuwa yanamtoka kisha nikamwona akimeza mate kutowesha koo lake ambalo nilihisi lilikuwa limekauka. Alibaki kimya pasipo kusema chochote.

“Rafiki yako Rehema yuko wapi?” nilimuuliza Olivia huku nikimkazia macho kwa umakini.

“Yupo…” Olivia alinijibu kwa kifupi huku akitazama kando.

“Yupo wapi, mbona hujaja naye ili nimwone?” nilidakia huku nikihisi moyo wangu ulikuwa umepatwa na tatizo la kiherehere.

“Yupo, utamwona muda mwafaka ukifika. Kuna mambo fulani kwanza nahitaji kuyaweka sawa,” Olivia alisema huku akionekana kuyakwepa macho yangu yaliyokuwa yanamtazama kwa umakini.

“Mambo gani?” nilimuuliza Olivia lakini hakunijibu na badala yake aliondoka eneo lile akijifanya kuongea na simu.

Baadaye nilikuja kugundua kuwa lengo la Olivia kuyakwepa maswali yangu lilikuwa kununua muda wa kutosha kutafakari kwanza kabla ya kunieleza chochote na pia aweze kuwasiliana na ndugu zangu kwani kila mtu aliamini nilikuwa nimekufa kwenye ile ajali na walishanizika na kusahau.

Ndiyo maana Olivia alipoambiwa habari zangu aliamua kuja peke yake kwanza pasipo kumshirikisha ndugu yangu yeyote ili ahakikishe kama ni kweli nilikuwa hai.

Baadaye nilikuja kuambiwa mkasa mzima kuwa ajali ile niliyodhani ilitokea siku tatu nyuma, ilikuwa imetokea zaidi ya miezi tisa nyuma na kila mtu aliamini kuwa nilikufa kwenye ile ajali. Na kwa kuwa sasa aligundua kuwa niko hai basi kulikuwa na uwezekano mkubwa kuwa nilikuwa nimepoteza kumbukumbu zangu kwa kipindi chote hicho cha miezi tisa.

Ndiyo maana habari za mimi kuwa hai zilikuwa zimemshtua sana Olivia. Niliposikia habari hizo nilichoka kabisa!

* * *



Kwa kuwa Olivia hakuwa daktari wa Hospitali ya Wilaya ya Kilosa hivyo aliuomba uongozi wa hospitali hiyo wamruhusu kunifanyia uchunguzi pale pale hospitalini, kuhusiana na madhara ambayo huenda nilikuwa nimeyapata kwenye ubongo wangu. Ulifanyika uchunguzi wa kina na baadaye iligundulika kuwa ile ajali ilikuwa imesababisha ubongo wangu kuhama kidogo toka katika sehemu yake ya kawaida.

Hali ile ya ubongo kuhama kutoka katika sehemu yake ya kawaida ilinisababishia tatizo la kupoteza kumbukumbu ambalo kitaalamu niliambiwa kuwa lilijulikana kama ‘retrograde amnesia’, yaani hali ya kutokuwa na uwezo wa kukumbuka taarifa zozote za kabla ya siku husika ya kutokea tatizo.

Katika hali nyingine niliambiwa kuwa wakati mwingine tatizo lile husababisha kukosa kumbukumbu za kurudi nyuma miongo kadhaa, na kwa wengine mtu anaweza kupoteza kumbukumbu miezi michache tu baada ya tukio.

Kwa upande wangu ilionekana kuwa baada ya ile ajali nilipoteza kabisa kumbukumbu na hivyo nikajikuta nikianza maisha mapya kabisa nikiwa katika utambulisho mpya huku taarifa zote za kabla ya ile ajali zikitoweka! Ndiyo maana niliishi kama mtu mwingine kabisa kwa kipindi chote cha miezi tisa, nikitumia utambulisho mpya na jina jipya!

Endelea...
 
Mgeni mwema.jpg

188

Hakuishia hapo, pia aliniambia kuwa kipindi chote hicho nilikuwa naishi na msichana aliyeitwa Zainabu, kama mke wangu.

Ilipotokea siku nikadhaniwa mwizi na kupigwa, kipigo kile kilisababisha kuurudisha ubongo wangu katika sehemu yake ya kawaida na kumbukumbu zangu za awali zikarejea tena zikianzia siku ambayo tulipata ajali eneo la Makutupora, na hivyo kufuta kabisa kumbukumbu za maisha mapya niliyoishi kama Mgeni Mwema kwa miezi tisa.

Taarifa zile za uchunguzi wa kitabibu zilinifanya nibaki mdomo wazi kwa mshangao, sikuamini kabisa kile nilichokisikia. Nilihisi hatia ikinikaba kooni hasa baada ya kugundua kuwa nilikuwa nimewakana watu wangu wa karibu niliokuwa nikiishi nao hapo Kilosa kwa miezi yote tisa wakati nikiwa katika uhusika wa Mgeni!

Hata hivyo, maswali kemkem yaliendelea kuzunguka kichwani mwangu; Ni nani aliyekuwa amezikwa kule Dodoma akidhaniwa kuwa ni mimi wakati kumbe nilikuwa hai? Kwa mazingira ya ajali kama ambavyo kumbukumbu zangu sasa zilinijia, iliwezekanaje tukapona wakati watu wengine watatu walikufa? Je, yule mtu wa tatu alikuwa nani?

Taarifa nilizokuwa nimepewa na Olivia ni kwamba; ilisemekana kuwa nilikufa kwenye ile ajali baada ya kukutwa maiti za wanaume watatu katika eneo la tukio zilizokuwa zimeungua. Wakati maiti za dereva wa lile lori na utingo wake zilikuwa na uafadhali na ziliweza kutambulika kirahisi, maiti ya tatu ilikuwa imeungua sana kiasi cha kutoweza kutambulika, na hivyo ikadhaniwa kuwa ni yangu…

Dah! pamoja na taarifa hizo nilitamani sana kumwona Rehema ili nijiridhishe kwamba ni kweli alikuwa hai na hiyo haikuwa ndoto, maana hadi wakati huo sikuamini zaidi ya kuambiwa tu. Kwa kipindi chote nilichokuwa nafanyiwa uchunguzi, Olivia alikuwa amenishauri kupumzika wakati yeye akitafuta namna ya kuwajulisha jamaa zangu kwani aliamini habari ile ingewashtua sana.

Uchunguzi wa kina wa kitabibu ulikamilika baada ya siku tatu na ndipo nilipomwomba Olivia anikutanishe na Zainabu pamoja na Almasi ili niwaombe msamaha kwa kuwa sikupaswa kuwakwaza kiasi kile hasa baada ya kugundua kuwa walikuwa watu wangu wa karibu sana, niliishi nao vizuri sana huku tukishirikiana kwa mambo mengi.

Olivia alikubali haraka. Kumbe muda wote nilipokuwa kwenye uchunguzi wa kitabibu Olivia alikuwa anawasiliana nao na alikuwa akiwaeleza kila kitu kilichokuwa kinaendelea.

* * *



Saa 9:30 alasiri…

“Kuna kitu nataka kukwambia, Zainabu…” nilimwambia Zainabu wakati tulipobaki peke yetu ndani ya nyumba yake ndogo ambayo niliambiwa kuwa nilikuwa nimeijenga kwa nguvu zangu baada ya kupata kibarua kwenye kampuni ya kandarasi ya ujenzi ya Yapi Merkezi iliyokuwa ikijenga reli ya kisasa (SGR) kutoka Dar es Salaam hadi Makutupora, Dodoma.

Muda wote Zainabu alikuwa mkimya sana, alikuwa akinitazama huku uso wake ukiwa na huzuni na machozi yalikuwa yanamlengalenga machoni.

“Naamini hakuna jambo linalotokea kwa bahati mbaya kwenye maisha, kila jambo huja kwa kusudi la Mungu. Pia kwenye maisha kuna muda kila mtu hufanya mambo fulani kwa kuwa hujikuta katika mkondo fulani kwa sababu tu iliandikwa hivyo au wakati mwingine maisha yalimchagulia namna ya kuishi,” nilimwambia Zainabu kwa sauti tulivu huku nikimtazama kwa tuo. Zainabu aliendelea kuwa mkimya sana.

“Lakini hayo yote huwa ni matokeo ya bahati au bahati mbaya ambayo kuna muda hutokea kwa kusudi la Mungu au kwa uzembe wetu… nimegundua kuwa niliwakosea sana pale nilipowakana hospitali japokuwa wakati huo sikuyajua haya yote. Kama nilivyosema mwanzoni, nimekuja kukuomba msamaha, na pia nitawaomba msamaha Almasi na Sofia, kwani ninataka nirudi kwenye maisha yangu halisi,” nilisema na kushusha pumzi.

“Daah! Nilijua tu… na tangu siku nilipogundua kuwa umerudiwa na kumbukumbu zako niliona ulimwengu umekuwa tofauti kabisa! Umekuwa mkatili sana kwangu kupita kiasi. Ukweli nashindwa kuvumilia maisha haya bila uwepo wako, Mgeni…” Zainabu alisema huku machozi yakimtoka. Nami nilihisi machozi yalikuwa yananilengalenga.

“Sina namna ya kufanya, Zainabu. Hisia zangu kwako hazipo au pengine zimeyeyuka pamoja na kumbukumbu ya jina la Mgeni mfano wa theluji ichemshwayo, siwezi kukupa matumaini yoyote kwa kuwa tayari nina mke na nampenda sana,” nilimwambia Zainabu kisha nikamshika na kumlaza kwenye mapaja yangu. Zainabu hakuonesha upinzani, alilala na kufumba macho yake huku akilia kilio cha kwikwi.

“Siamini kinachotokea, natamani iwe ndoto… siku zote tumekuwa pamoja kama mke na mume, tumeishi kwa upendo eti leo hii unaniacha katika mazingira kama haya ambayo tayari nimekubebea mtoto wako tumboni mwangu!” Zainabu alisema na kunifanya nishtuke sana.

“Una mimba?” nilimuuliza huku nikimtazama kwa wasiwasi. Mwili wangu ulikufa ganzi, nilihisi kama vile nimepatwa na ugonjwa mbaya wa kiharusi.

“Ndiyo, nina mimba yako… sasa sijui ni nini unataka nifanye na hali hii? Ni nini unataka na mimi nitafanya! Niambie tafadhali,” Zainabu aliongea kwa uchungu huku akilia kama mtoto.

Nilimwonea huruma sana lakini sikuwa na namna yoyote ya kufanya. Hata hivyo suala la kwamba alikuwa na mimba yangu lilianza kunitesa sana.

“Dah, nimeambiwa ulikuwa mtu mzuri sana kwangu, ulinipokea na kuishi nami, ukanitafutia kazi na kisha ukanionesha mapenzi ya kweli… nashukuru sana kwa hilo lakini kwa sasa nipo njia panda kwa kuwa ninaye mke, ila kwa suala la ujauzito nitaongea na Olivia tuone namna ya kukusaidia,” nilimweleza kwa kujikaza kwani hata sikujua niseme nini wakati huo.

“Kwa hiyo wewe huwezi kujihusisha na ujauzito huu hadi uongee na Olivia? Daah, haya bwana…!” Zainabu alisema kwa kukata tamaa.

“Sina maana hivyo…” nilisema lakini akanikata kauli.

“Kumbe una maana gani?” Zainabu aliuliza huku akiinuka, akanitazama usoni kwa mashaka kidogo.

“Olivia ndiye mtu wangu wa karibu, isitoshe hapa Kilosa ndo nyumbani kwao na hivyo itakuwa rahisi,” nilisema huku nikiwa na mashaka.

Zainabu alibaki kimya akinitazama pasipo kusema neno. Macho yake yaliendelea kulengwalengwa na machozi.

* * *

Endelea kufuatilia...
 
Back
Top Bottom