Simulizi: Harakati za Jason Sizya

Simulizi: Harakati za Jason Sizya

ufukweni mombasa.JPG

238

Nilimsindikiza kwa macho hadi alipotoka kabisa na kuelekea kwenye gari lake. Kisha nikasikia mlio wa milango ya gari kufunguka baada ya kubonyeza rimoti, halafu gari likawashwa na kuunguruma taratibu na baadaye mlango wa gari ukafungwa huku geti likifunguliwa na hatimaye gari likatoka na kutokomea barabarani.

Sikuchukua muda mrefu mawazo yangu yakarudi tena kwenye kazi iliyokuwa mbele yangu, kazi ya kutafuta taarifa za Zuena wa Mombasa, kuanzia kwenye mawasiliano yake ya simu hadi kwenye account zake za Tiktok, Facebook na Instagram. Nikazama kwenye kufuatilia kila taarifa aliyoichapisha kwa namna ya kiuchunguzi zaidi. Bado sikuweza kupata jambo lolote lililoonekana kunitia wasiwasi.

Nikiwa bado natafakari hatua zaidi za kuchukua simu yangu ya mkononi ikaanza kuita. Niliitazama nikaona namba ngeni, nikaipokea na kuisikiliza, nikagundua mpigaji alikuwa amekosea namba, nikaikata kwa kuwa haikuwa na kitu cha muhimu.

Sasa nikaamua kujipa mapumziko ili niweze kuendelea na mipango yangu ya safari ya kwenda Mombasa, mapumziko hayo yangekuwa ya muda na ningeuendeleza upelelezi wangu juu ya Rahma baada ya kutoka Mombasa nilikopanga kukaa kwa wiki moja na ushee. Hata hivyo mipango yangu hii haikuwa tuli (static), la! Nilikubaliana na nafsi yangu kuwa ingekuwa inabadilika kutokana na matukio yanavyokwenda, kutokana na mambo yanavyoenenda.

Huko Mombasa nilipanga kufikia katika hoteli ya Serena Beach Resort & Spa, na tayari nilikwisha wasiliana nao na kufanya malipo ya awali mtandaoni na kupewa chumba nambari 204. Nilivutiwa na hoteli ya Serena Beach Resort & Spa kutokana na maelezo niliyoyapata kupitia intaneti.

Ilikuwa hotel kubwa na tulivu zaidi yenye hadhi ya Nyota 4, ikiwa nje kabisa ya Jiji la Mombasa, katika ufukwe wa Bahari ya Hindi. Hoteli hii ilikuwa jirani na Mombasa Marine National Park, na pia ilikuwa rahisi kufika Shimba Hills National Reserve kutokea pale. Hayo ni maeneo ambayo nilipanga kuyatembelea nikiwa Jijini Mombasa.

* * *



Saa 5:15 usiku…

Ulikuwa usiku usio na furaha kwangu kwa mara ya kwanza tangu nimuoe Rehema. Ndiyo, nilikuwa nimelala na Rehema, tukiruhusu miili yetu kustareheshana kama kawaida, mikono ikijifariji kwa kugusa hapa na pale; miguu ikiburudika kwa mguso huo. Hata hivyo, faraja hiyo haikufikia kiwango cha kuzifuta chembechembe zisizoelezeka ambazo zilienea katika fikra zangu.

Sikujua kwa nini nilikuwa na fikra mbaya juu ya Rahma wa Singida! Sikuona kwa nini niendelee kuumizwa kifikra na mtu ambaye hakuwa na rekodi yoyote yenye kutia shaka. Rekodi ya uhalifu. Hata hivyo fikra mbaya juu yake zilishindwa kufutika akilini kwangu kila nilipokumbuka kuwa gari aina ya Range Rover walilokuwa wakitumia lilikuwa na namba za bandia, jambo lililomaanisha kuwa hawakuwa watu wa kuwaamini. Kuhusu Zuena wa Mombasa, ndiyo… alikuwa amenitia mashaka, pengine hata kuliko Rahma wa Singida, lakini hakunisumbua sana akili yangu.

Tukiwa kitandani Rehema alijua fika kuwa kulikuwa na jambo gumu lililonitatiza sana katika kazi yangu mpya na hakuthubutu kuniuliza kuhusu kile kilichonitatiza, alifahamu fika kuhusu utaratibu wa usiri (Compartmentation) kwenye kazi ya ushushushu hakujisumbua kuniuliza kwa kujua nisingeweza kumwambia kwa kuwa kwenye taalumu ya ujasusi kila mtu kwako ni adui na hutakiwi kumwamini yeyote, hata marehemu.

Alionekana kuyasoma mawazo yangu, akanihurumia sana na alijitahidi kufanya kila aliloweza kulifanya kwa dhamira ya kujaribu kunisahaulisha walau kwa muda. Alipoona vitendo vyake havitimizi wajibu alijaribu kutumia maneno, kwa sauti yake laini, iliyopenya katika mwanga hafifu mle chumbani baada ya kuzimwa taa na kisha kuwashwa taa yenye mwanga hafifu wa rangi ya bluu, Rehema aliniambia. “Baby, haya mambo yasikuvuruge, nadhani hakuna asiyejua kama wewe ni shujaa.”

Nilimtazama usoni katika mwanga ule hafifu, nikatabasamu huku mawazo yangu yakihama kutoka kuifikiria kazi yangu ya kumtafuta Rahma wa Singida na kuanza kumfikiria Rehema, ofisa kificho wa Idara ya Usalama wa Taifa. “Kama baba na mama ni mashushushu wasioaminiana sijui mtoto atakuwaje!’ niliwaza na hapo nikajikuta nikicheka.

“Unacheka nini? Ni kweli hakuna asiyejua kama wewe ni shujaa,” Rehema alisema huku akiupitisha mkono wake kwenye nywele zangu na kuanza kuzishikashika kwa namna ya kunitia mdadi.

“Shujaa!” niliuliza kwa sauti iliyokuwa na dalili ya uchovu. “Wanaonifikiria hivyo watakuwa wanakosea sana.”

“Japo sijui ugumu wa task uliyo nayo lakini inanishangaza kuona unavunjika moyo mapema kiasi hiki. Unautia dosari ushujaa wako,” Rehema aliniambia katika hali ya kunisimanga kisha akanikumbatia. Sikusema neno. Kisha kama aliyekumbuka jambo akaniuliza, “Kwa hiyo safari yako ya Mombasa bado ipo?”

“Ipo kama kawaida. Kesho lazima niondoke na nikirudi ndiyo nipite Kilosa nikamwone mtoto halafu niende Tabora kwa wazee,” nilisema kwa sauti tulivu. Kwa taarifa nilizokuwa nazo ni kwamba Zainabu alikuwa na mtoto wa kiume ambaye muda huo alikuwa na miezi minne.

“Jason!” Rehema alisema kwa sauti ya mshangao. Uso wake ulikuwa na dalili zote za mashaka. “Kwani ni lazima uende Mombasa kesho? Ingekuwa ni safari ya kikazi sawa lakini…”

“Lakini nini?” nilimuuliza Rehema bada ya kuona amesita kuongea.

“Nadhani kesho usifanye safari hiyo. Nenda kwanza ukamwone mtoto na kisha wazee upate na baraka zao halafu ndiyo uende safari yako,” Rehema alisisitiza.

“Kwa nini hutaki kesho niondoke?” nilimuuliza Rehema huku nikimtazama usoni kwa umakini.

“Hata sijui! Lakini… nina hisia mbaya,” Rehema alisema kwa kusita sita na kunifanya niangue kicheko.

“Huna sababu ya kuogopa chochote. Hakuna mtu atakayeniteka tena…” nilisema huku nikiwa bado nacheka. Kisha nikaongeza, “Sina njia nyingine zaidi ya kuondoka kesho. Nikiendelea kubaki Tanzania kuna mambo yatazidi kunitatiza akili yangu wakati nahitaji kuipumzisha.”

Rehema hakutia tena neno. Huenda aliamua kukubali yaishe kwa kubaki kimya baada ya kuona nilikuwa nimekusudia kuendelea na safari yangu siku iliyokuwa inafuata. Tayari nilikwisha fungasha vitu vyangu kwenye begi dogo la safari na nilishakata tiketi ya basi la kampuni ya Tahmeed.

Baada ya kitambo kirefu nikamwona Rehema akishusha pumzi na kuniambia kwa sauti ya unyonge, “Sawa, nakutakia safari njema…” kisha akageuka upande mwingine akinipa mgongo.

“Nashukuru, na nyinyi mbaki salama,” nami nilimwambia huku nikipeleka mkono wangu kwenye unywele zake na kuanza kuzipapasa kwa namna ya kuamsha ashki.

“Ila sielewi kwa nini umechagua kusafiri kwa basi hadi Mombasa badala ya usafiri wa ndege!” Rehema alisema kwa sauti tulivu, katika sauti yake kulikuwa na hali ya huruma na unyenyekevu huku masikitiko yakiwa yamejificha nafsini mwake.

“Usijali, mke wangu… nimeamua kutumia basi kama mojawapo ya kufanya utalii usio rasmi kwa sababu nitafanikiwa kuyaona vizuri mandhari ya kupendeza ya nchi yetu. Ila wakati wa kurudi nitapanda ndege,” nilisema huku nikimkumbatia kwa kupitisha mikono yangu kwenye kifua chake. Kisha nikafumba macho yangu nikijaribu kuutafuta usingizi.

* * *

Inaendelea...
 
ufukweni mombasa.JPG

239

Merina wa Mombasa…




Saa 11:20 alfajiri…

HALI ya hewa katika Jiji la Dar es Salaam ilikuwa tulivu na giza zito lilikuwa limetanda angani. Pamoja na umeme kutoa nuru lakini bado ulishindwa kuliondoa giza hili lililokuwa limetiwa nakshi na mawingu mazito na kusababisha Jiji la Dar es Salaam kuwa na kaubaridi ka aina yake! Giza hili lilikuwa limemudu kufifisha mwanga wa umeme uliothubutu kuangaza ukitoka katika baadhi ya nyumba na vyumba vya maghorofa na katika barabara za jiji hili, na kufanya mwanga huo wa umeme kuonekana kama kandili zisizo na mafuta ya kutosha.

Bado kilibaki kuwa kichekesho kwangu kwamba jiji kongwe kama hili katika Afrika ya Mashariki eti halikuwa na taa za barabarani! Hapana… taa zilikuwepo isipokuwa nyingi zilikuwa haziwaki kabisa, pengine tangu ziwekwe. Kwa nini? Majibu ya swali hilo walikuwa nayo maofisa wa Manispaa husika na Jiji au wale wa Tanesco.

Muda huo wa alfajiri nilikuwa barabarani ndani ya gari dogo la kukodi, teksi, nikielekea katika Kituo Kikuu cha Mabasi cha Magufuli, kilichopo eneo la Mbezi. Wakati huo barabarani kulikuwa na magari machache na hapakuwa na foleni za magari, hivyo mwendo wetu ulikuwa wa kasi sana na uliyafanya magurudumu ya gari nililopanda kuteleza kwenye barabara ile ya Morogoro kama nyoka atelezavyo kwenye nyasi.

Asubuhi hiyo nilikuwa nimevaa sweta jepesi la rangi ya maruni lililoungana na kofia iliyofunika kichwa changu na suruali ya bluu mpauko ya kitambaa kizito cha dengrizi. Miguuni nilivaa raba za Puma na kuweka miwani myeusi ya kuzia miale ya jua machoni, japokuwa hapakuwa na jua muda huo wa alfajiri.

Tulifika kituo kikuu cha mabasi cha Magufuli eneo la Mbezi mnamo saa 11:45 alfajiri, mara baada ya kuvuka geti la kuingilia kituoni hapo, dereva akaendesha gari lake taratibu huku akiyatembeza macho yake huku na kule akitafuta sehemu nzuri ya maegesho na baada ya muda mfupi hatimaye akawa amepata sehemu nzuri ya maegesho na kusimama.

Sikuwa na muda wa kupoteza kwani kwa mujibu wa ratiba iliyokuwa kwenye tiketi yangu ilionesha kuwa zilikuwa zimesalia dakika kumi na tano tu kabla ya basi letu kuanza safari yake ya kuelekea Mombasa. Hivyo bila kupoteza muda nikafyatua kabari ya mkanda wa kiti changu kisha nikachukua begi langu kutoka kwenye kiti cha nyuma na kushuka.

Kisha nilimshukuru dereva aliyenifikia hapo salama, tukaagana halafu nikaanza kutembea haraka haraka kuelekea lilipokuwa basi la Tahmeed, ilinichukua takriban dakika mbili hivi kuliona basi husika nililopaswa kuondoka nalo, nikatoa tiketi yangu na kumwonesha kondakta wa lile basi aliyekuwa amesimama mlangoni. Yule kondakta aliipokea ile tiketi na kwa kutumia mwanga wa simu aliihakiki na kisha akanukuu jina na namba ya tiketi kwenye fomu maalumu aliyoishika, halafu akanirudishia ile tiketi na kunitakia safari njema.

Nilipanda ndani ya basi nikakitafuta kiti changu, sikuchelewa kukiona kwani kilikuwa mwanzoni kabisa, kiti nambari tano kilichokuwa dirishani upande wa dereva. Ndani ya basi lile niliwakuta wasafiri wengine wakiwa wameketi kwa utulivu na wengine wachache waliendelea kuingia na kutafuta namba za viti vyao. Kwenye kiti nambari nne, jirani na kiti changu nilimkuta mwanadada mmoja akiwa ameketi kwa utulivu, macho kayafumba.

Alikuwa msichana mrefu na mwenye haiba ya kuvutia, alivaa fulana nyepesi nyeupe iliyoyaficha vyema matiti yake imara yenye ukubwa wa wastani na juu yake alikuwa amevaa shati zito la bluu la kitambaa cha dengrizi na chini pia alivaa suruali ya bluu ya kitambaa cha dengrizi. Miguuni alikuwa amevaa sandals ngumu za kike za ngozi.

Nilipomchunguza vizuri nikagundua kuwa alikuwa na nywele ndefu na laini zilizolalia mabegani na alikuwa amezifunika kwa mtandio laini mweusi ulioshindwa kuzificha nywele hizo zisionekane. Mdomo wake laini wenye kingo pana kiasi ulikuwa umepakwa rangi nzuri ya chocolate. Nikaliweka vizuri begi langu kwenye sehemu maalumu ya juu ya kuwekea mizigo ndani ya lile basi, halafu nikaketi kwenye kiti changu na kujiinamia nikiweka kichwa changu kwenye kiti cha mbele yangu na kukiegemeza juu ya mikono yangu niliyoikunja. Nikaanza kunyemelewa na usingizi.

Honi kali za basi la Kampuni ya Tahmeed zilinishtua sana kutoka kwenye lepe hafifu la usingizi ulioanza kunichukua, usingizi uliotokana na uchovu wa kutopata usingizi mzuri usiku wa kuamkia siku hiyo ya safari, nikainua kichwa changu na kuyatembeza macho yangu kutazama nje, nikaona vitu vikipita mbele ya macho yangu vikionekana kurudi nyuma. Na hapo nikatambua kuwa sasa basi lilikuwa linakiacha kituo cha mabasi cha Magufuli.

Nilipochoka kutazama nje nikashusha pumzi ndefu na kugeuza shingo yangu kutazama ndani, na hapo macho yangu yakaangukia kwenye sura ya yule abiria mwanamke aliyekuwa ameketi pembeni yangu, kwenye kiti nambari nne. Nikamwona akiwa amejiegemeza kwenye kiti chake na kuyafumba macho yake huku sauti hafifu ya mkoromo ikisikika kuashiria kuwa alikuwa amepitiwa na usingizi.

_____



Saa 2:15 asubuhi…

Sikujua ni muda gani usingizi ulinipitia tena, nilikuja kushtushwa na sauti za vijana wauza matunda na mahindi ya kuchoma, niliyapeleka macho yangu kutazama dirishani mara moja nikauona mwanga wa jua la asubuhi na miale yake ilikuwa inapenya kwenye vioo vya madirisha ya basi letu. Na hapo nikakumbuka kuitupia macho saa yangu ya mkononi. Nilipoona kuwai ilitimia saa mbili na robo asubuhi nikajua kuwa tulikuwa tumetumia muda wa saa mbili na dakika kumi na tano tangu tulipoanza safari yetu kutoka Mbezi jijini Dar es Salaam hadi hapo.

Nikapata shauku ya kutaka kufahamu tupo wapi, nikatazama vizuri kule nje na kugundua kuwa tulikuwa tumesimama katika kituo cha mabasi ya kwenda Arusha/Tanga cha Chalinze, njia panda inayoziunganisha barabara za Dar es Salaam, Morogoro na ile ya Arusha/Tanga. Eneo lile la Chalinze lilikuwa limetawaliwa na pilika pilika nyingi za kibinadamu zilizosababishwa na wachuuzi wa biashara ndogo ndogo.

Nilipochoka kuangalia pilika pilika za wachuuzi kule nje nikayarudisha macho yangu kutazama mle ndani ya basi na kuanza kuyatembeza taratibu nikiwatazama abiria wenzangu walioketi kwa utulivu kabla ya macho yangu kutua kwenye sura ya yule abiria aliyekuwa ameketi pembeni yangu, kwenye kiti nambari nne. Macho yetu yakagongana, nikajikuta nikishtuka sana japo nilijitahidi kuuficha mshtuko wangu.

Japokuwa tulikuwa tumeketi kwenye viti vilivyopakana muda wote lakini niligundua kuwa muda wote sikuwa nimemchanganyia vizuri macho. Nilikuwa natazamana na Zuena wa Mombasa. Asubuhi hiyo alikuwa anavutia mno. Licha ya urembo wake wa asili pia alikuwa amejiongezea kwa mapambo mengine ya gharama. Na kwa mara ya kwanza tangu niingie ndani ya lile basi nikaisikia harufu ya marashi ninayoyapenda - marashi ghali aina ya Dolce & Gabbana. Nikazidi kushangaa kimoyo moyo kwa nini vitu viwili; uwepo wa Zuena wa Mombasa karibu yangu na manukato yake, sikuvigundua mapema!

Nilipokuwa namtazama Zuena wa Mombasa yeye pia alikuwa ananitazama kama aliyekuwa akinifannanisha, lakini niligundua kuwa hadi muda huo hakuwa amenitambua, huenda ni kutokana na namna nilivyovaa ikiwa ni pamoja na miwani myeusi ya kuzuia miale ya jua iliyofanikiwa kuyaficha macho yangu. Mara nikamwona akisita na kunitazama kwa namna ya udadisi zaidi. Na bila ya kujijua ikamtoka “Oh!” kwa sauti yake laini.

Inaendelea...
 
ufukweni mombasa.JPG

240

Ni hapo alipoachia tabasamu la bashasha na kunyoosha mkono wake kunipa. Nikaupokea bila ajizi yoyote huku nikiachia tabasamu pana.

Slim! I didn’t expect to see you again!” Zuena alisema kwa sauti tulivu kuwa hakutarajia kuniona tena, huku akinitazama kwa umakini usoni. Kisha akaongeza, “Inasikitisha mno kuona kuwa hata wewe umekuwa Mswahili tofauti na mwonekano wako, halafu hukuniambia kama utasafiri.”

“Samahani ratiba za kazi zangu zilinibana mno nikashindwa hata kuwasiliana na wewe,” nilisema kwa sauti tulivu ya kuomba msamaha huku nikiuachia mkono wake.

“Haina shida. Yaliyopita si ndwele,” Zuena alisema kwa sauti tulivu iliyobeba kitu fulani ambacho nilishindwa kukitafsiri haraka, huku akiendelea kunitazama kwa namna ambayo sikuweza kuelewa mara moja. “Unaelekea Tanga au Mombasa?”

“Naelekea Mombasa,” nilijibu pasipo kusita.

“Mbona hukuniambia kama utakuwa na safari ya Mombasa?” Zuena aliniuliza na kabla sijajibu akaendelea kunisaili kwa maswali mfululizo. “Umeshawahi kufika au ndiyo mara yako ya kwanza?”

“Ni mara yangu ya kwanza kwenda huko. Nategemea utakuwa mwenyeji wangu,” nilisema huku nikiachia tabasamu pana.

Zuena alinitazama kidogo kwa utulivu huku uso wake ukishindwa kuonesha tashwishwi yoyote kisha akaniuliza tena, “Unaenda kwa shughuli gani?”

“Kuangalia fursa…” nilimjibu huku nikiendelea kumtazama machoni. Kisha nikamtupia swali, “Ni safari ya saa ngapi kwa basi kutoka Dar es Salaam hadi Mombasa maana mimi ni mvivu wa kusafiri na mabasi ya masafa marefu!”

“Mh! Sina uhakika ni mwendo wa saa ngapi kutoka Dar es Salaam, hii ni mara yangu ya kwanza kusafiri toka Dar es Salaam kwa basi, ingekuwa kutokea Tanga ningekuwa na jibu la uhakika,” Zuena alijibu baada ya kufikiria kidogo.

“Vipi kuhusu hali ya usalama Jijini Mombasa?” swali langu lilimfanya Zuena ashtuke kidogo japo alijitahidi kutokuonesha mshtuko, kisha akaachia tabasamu dogo, lakini tabasamu lake lilionekana kuficha kitu kama uchungu au hofu fulani, na mara tabasamu lake lilipokoma akavunja ukimya.

“Hali ni shwari. Siku hizi hakuna tena vitisho vya Al-Shabab kwa kuwa serikali imejitahidi sana kuimarisha ulinzi na usalama kwa raia wake na hata kwa wageni kama ninyi mnaofikia katika hoteli mbalimbali…”

“Wewe unaishi sehemu gani hapo Mombasa?” nilimtupia swali lingine haraka.

“Mikindani. Unataka kuja kunitembelea?” Zuena alisema huku akiachia kicheko cha chini chini. Nami nikacheka kidogo. Kisha Zuena akaongeza huku akiendelea kucheka, “Haata hivyo unakaribishwa sana.”

“Nitakaribia siku moja, tuombe Mungu,” nilimjibu Zuena huku nikijiweka vizuri kwenye kiti changu.

“Utafikia hoteli gani hapo Mombasa ili nije kukutembelea?” Zuena aliniuliza huku macho yake yakinitazama kiwiziwizi kwa namna ambayo sikuweza kupata tafsiri mara moja.

Nikataka kumtajia jina la hoteli ambayo ningefikia lakini kengele ya hatari ikalia kichwani kwangu. Nikajionya kuwa makini na kutomwamini yeyote katika safari yangu. Roho yangu ilisita sana kumwamini Zuena tangu nilipomwona mara ya kwanza kule Lamada Hotel jijini Dar es Salaam. “Bado sijajua hoteli gani itanifaa. Nikifika huko ndo ntajua,” nilimjibu na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.

Zuena alinitazama usoni kwa kitambo fulani, huenda alijaribu kuyasoma mawazo yangu kisha akaachia tabasamu. “Slim, you don’t trust me! I’m your friend, right?” (Slim, huniamini! Mimi ni rafiki yako, au sivyo?) alisema.

Nilipotaka kusema akanizuia kwa kuwekea kidole chake cha shahada kwenye mdomo wangu.

Don’t say anything, I can understand…” (Usiongee chochote, naelewa…) Zuena alisema na kuachia kicheko. “Nadhani hoteli kama CityBlue, Sarova Whitesands, Severin See Lodge, Travellers Beach Hotel can be nice to you. These are reasonable.”

Okay! Nitafikiria kati ya CityBlue na Sarova Whitesands, then nitakujulisha,” nilisema kisha nikabadilisha maongezi nikionesha kutaka kujua mengi kuhusu Jiji la Mombasa.

Bila hiyana Zuena alianza kuniambia mambo mengi kuhusu jiji hilo lililopo pwani ya Kenya, mambo ambayo kwa namna fulani yalikuwa msaada mkubwa kwangu kuufahamu mji wa Mombasa. Niligundua kuwa Zuena hakuwa mtu wa kukwazika kirahisi hata pale alipofahamu kuwa hukubaliani na jambo lake, alipenda stori na hivyo mazungumzo kati yetu yalinoga na kufanikiwa kuniondolea uchovu wa usingizi kwa kiasi fulani, tuliongea na kufurahia huku tukiifanya safari yetu kuwa ya kupendeza.

Nilipokuja kushtuka tayari tulikuwa tunaingia Pongwe, nje kidogo ya jiji la Tanga. Nikakumbuka kuitazama saa yangu ya mkononi na kugundua kuwa ilikwisha timia saa 6:05 mchana.

Tuliingia Tanga Mjini mnamo saa 6:35 mchana, basi letu likasimama kwenye kituo cha mabasi kwa ajili ya kushusha na kupakia abiria, na pia kutupa nafasi abiria ya kupata chakula cha mchana na tukatangaziwa kuwa tungekuwepo pale Tanga kwa muda wa dakika ishirini tu.

Wote tulishuka kwa ajili ya kujipatia chakula na mahitaji mengine. Nikaongozana na Zuena hadi ndani ya mgahawa mmoja uliokuwepo jirani na eneo lile kwa ajili ya chakula. Ule mgahawa ulikuwa mzuri wenye huduma zote muhimu ikiwemo aina mbalimbali ya vyakula vya kisasa na vya asili kwa watu wote hata watu wa mataifa tofauti na ulikuwa na utulivu wa kutosha.

Humo kwenye mgahawa mimi niliagiza wali kuku na saladi ya mboga za majani na Zuena aliagiza chipsi kuku, kisha tukatafuta meza moja iliyojitenga kwenye kona moja ya mgahawa ule na kuketi. Sehemu ile tuliyoketi ilituwezesha kuona nje ya mgahawa ule na kuliona basi letu, kupitia uwazi kwenye kuta zilizokuwa zikitazamana na kituo kile cha mabasi Jijini Tanga.

Tulipoketi tukaanza kuvishambulia vyakula vyetu huku kila mmoja wetu akionekana kuwa na njaa na wakati huo nikapata wasaa mzuri wa kumchunguza zaidi Zuena kwa jicho la wizi. Uchunguzi wangu ukanifanya kubaini kuwa hata yeye alikuwa akinitazama kwa jicho la wizi. Tena macho yake hayakuhama kwangu na badala yake yalikuwa makini kufuatilia kwa karibu kila hatua niliyokuwa nikiichukua.

“Chakula cha hapa kina ladha nzuri sana,” niliamua kuingiza maongezi kuhusu chakula ili kujaribu kumzuga Zuena.

“Ni kweli…” Zuena aliafiki huku akiachia tabasamu pana. Na huo ukawa mwanzo wa kufungulia maongezi baina yetu ndani ya ule mgahawa.

Tuliongea hili na lile kuhusu mapishi huku tukiendelea kupata mlo taratibu na wote tulionekana kufurahishwa sana na urafiki ule ulioanza ghafla kule Lamada Hotel, ukakoma siku hiyo hiyo na kuibuka tena siku sita baadaye baada ya kukutana ndani ya basi la Tahmeed, wote tukielekea jijini Mombasa.

Kisha kilipita kitambo fulani cha ukimya kabla ya Zuena hajaniuliza, “Slim, naomba unisamehe tafadhali, kabla sijakuuliza swali ambalo ni la kibinafsi kabisa.”

Nilimtazama Zuena kwa umakini sana usoni huku nikijaribu kubashiri swali alilotaka kuniuliza. Kisha nikamuuliza, “Ni swali gani hilo? Mbona unanitisha!”

“Usihofu kabisa…” Zuena alisema kwa sauti tulivu huku akiachia tabasamu la bashasha. “Swali lenyewe ni la kawaida sana lakini ni kwa watu wanaojuana, kwa wasiojuana kama sisi ni lazima tuombane radhi kwanza.”

“Sawa, niulize,” nilisema huku nikiwa makini kumsikiliza.

Inaendelea...
 
ufukweni mombasa.JPG

241

Nikamwona Zuena akitulia kidogo na kuinamisha uso wake chini kama vile alikuwa amesahau swali alilotaka kuniuliza, kisha aliinua uso wake na kunitazama moja kwa moja machoni, “Hivi umeoa? Au tusemee… una mke au labda mchumba?”

Nilishusha pumzi za ndani kwa ndani. Sikuwa nimelitegemea swali hili kwa sababu siku ya kwanza tulipoona kule Lamada Hotel aliniuliza habari za mke wangu. Hata hivyo ilionesha kama vile swali lilikuwa limekaa kimtego mtego.

“Hapana sijaoa na wala sina mchumba,” nilimjibu huku nikimtazama machoni.

Zuena alinitazama kwa sekunde kadhaa bila kusema neno. Kisha aliniuliza huku akinitazama kwa udadisi, “Unataka kuniambia hujaoa hadi sasa?”

“Sijabahatika,” nilimjibu kwa sauti tulivu.

“Kwa nini?” bado alikuwa ananitazama kwa udadisi.

“Kwa sababu Mungu hajanijaalia bado,” nilisema kwa kujiamini.

“Mh, inawezekanaje kwa mwanaume mtanashati kama wewe kusema kuwa hujaoa na huna mchumba?” Zuena aliuliza huku uso wake ukionesha mshangao wa wazi.

“Bado sijapata yule ambaye ataufanya moyo wangu usimame. Naamini mke mwema hupatikana kwa kusubiri, muda ukifika hakuna kitu ambacho kitanizuia kuoa,” nilisema na kuangua kicheko hafifu.

“Na vipi kuhusu hiyo pete?” Zuena aliniuliza huku akikiangalia kidole changu chenye pete ya ndoa. Sikuhangaika kukificha.

“Ni pete tu kama pete zingine zinazovaliwa kama urembo,” nilimjibu huku nikikitazama kidole changu chenye pete.

“Sawa, kama usemayo ni ya kweli!” Zuena alisema na kushusha pumzi.

“Vipi kuhusu wewe, umeolewa?” sikujali maneno yake nikampachika swali.

“Hapana, bado sijaolewa. Sina mume wala mwanaume na… pia sina mchumba,” Zuena alisema huku akitabasamu.

“Duh! Ina maana wanaume wote wa Mombasa wana maradhi ya upofu?” nilimuuliza kwa utani huku nikitabasamu.

“Kwa nini?” Zuena aliniuliza huku akiniangalia machoni kwa mshangao.

“Kwa jinsi ulivyo, umbo lako zuri, sura yako nzuri, haiyumkini msichana kama wewe kuwa huna mume, mwanaume wala mchumba mpaka wakati huu! Hawakuoni?” nilisema huku nikijitia kushangaa.

“Basi nisemayo ni ukweli mtupu. Kwa sasa sina uhusiano wa kimapenzi na mwanamume yeyote,” Zuena alisema na kushusha pumzi.

“Huna kwa kukosa au kwa kupenda?” nilimsaili tena.

“Kukosa ni vipi na kupenda ni vipi?” Zuena aliniuliza huku akitazama chini kwa aibu.

“Kukosa ni kuwa hakuna mtu anayekutaka kama mpenzi wake, na kupenda nako ni kuwa unatakiwa na wanaume lakini wewe huwataki,” nilisema na kumfanya Zuena aangue kicheko kilichowafanya watu wote ndani ya ule mgahawa wageuke kututazama kwa mshangao.

“Ninatakiwa na wanaume takriban kila siku ya maisha yangu tangu nipate fahamu, lakini wote wanaonitaka si kwa dhati ya mapenzi au kunioa bali dhamira zao kwangu ni kuchezeana tu jambo ambalo siko tayari nalo,” Zuena alisema kwa hisia. Kila neno lilisindikizwa na tabasamu.

Wakati akiongea nilikuwa namtazama moja kwa moja machoni nikijaribu kuoanisha kile alichokuwa akikiongea na mwonekano wake. Kumbukumbu ya kukutana kwetu siku ya kwanza pale Lamada Hotel ikanijia, nikakumbuka jinsi alivyokuwa akiongea kwa maneno na vitendo, mikono yake ikiruka na kutua hapa na pale katika mwili wangu, mara achezee vidole vyangu, mara mkono utue na kutulia juu ya paja langu.

“Siye huyu aliyekuwa anayafanya hayo pale Lamada Hotel? Anasemaje hapendi kuchezeana! Kama ni kuigiza basi ni mwigizaji mzuri. Uigizaji umo katika damu yake,” niliwaza kisha nikaachia tabasamu. Ni kweli alikuwa mwigizaji mzuri tatizo lake hakuwa na kumbukumbu!

“Mwombe sana Mungu akupatie mume bora mwenye mapenzi ya kweli,” nilimwambia huku nikitabasamu.

“Wewe pia unatakiwa kumwomba Mungu. True love is hard to find these days,” Zuena aliniambia.

It’s true… siku hizi watu wamekuwa wabinafsi sana,” nilisema na muda huo huo tukasikia tangazo kuwa abiria waliokuwa wanasafiri kwenda Mombasa kwa basi la Tahmeed walitakiwa kuingia kwenye basi tayari kwa safari. Tukainuka na kuelekea kwenye basi letu. Na huo ukawa mwisho wa maongezi kuhusu suala la mahusiano.

Tuliondoka pale Tanga mnamo saa 7:00 mchana na kuifuata Barabara ya Mombasa, baada ya mwendo wa dakika kama ishirini hivi tukaanza kupita katika eneo la mapango ya Amboni na hapo nikakumbuka kuhusu maajabu ya mapango hayo niliyoyashuhudia wakati fulani kwenye safari yangu niliyowahi kuifanya huko. Yalikuwa mapango yalivyohifadhi maajabu makubwa!

Pango langu la kwanza kuingia liliitwa ‘Pango la Jinsia’ ambalo ni pango dogo lakini lenye maajabu ya pekee, ambalo ni mzizi wa mti wavule uliochora alama ya “V” ama mshale ili kumwelekeza mtumiaji wa njia ya pango hilo kupata urahisi wa kutoka, ingawa utokaji wake si rahisi bila ya kuwa na mwongozaji.

Pia katika safari hiyo niliona taswira safi ya muundo wa Bara la Afrika ndani ya mapango likiwa limejichora katika maajabu ya kupendeza zaidi, huku pia nikiona muundo wa mshumaa ulioyeyuka ambao unazidi kufanya mapango hayo kuwa ya kustaajabisha zaidi hasa pale unapoupanda Mlima Kilimanjaro na kupenya katika njia nyembamba iliyopo ndani ya mapango hayo.

Si hivyo tu, ndani ya mapango ya Amboni niliona chumba mfano wa ukumbi wa sherehe ambao kwa juu kidogo kinaonekana chumba cha DJ wa sherehe huku upande wa kulia ikionekana njia ya kupanda kilele cha Mlima Kilimanjaro. Pia kuna kituo au pango ambalo limekuwa likitumika na wazee au watu wa kawaida kufanya matambiko au maombi yao ya kawaida na baada ya kumaliza maombi hayo watu hao hutoa sadaka mahali hapo.

Katika upande mwingine wa pango hilo niliona mfano au muundo wa kiti cha enzi ambacho kilikuwa kikitumika zamani kama kiti cha heshima kwa machifu ama watawala wa zamani. Pia niliyaona maficho ya Osale Otango na Paul Hamis. Hawa ni kati ya wapigania uhuru wa Tanganyika wa miaka ya 1950 waliochukuliwa kama wahalifu na serikali ya kikoloni.

Osale alikuwa na asili ya Kenya na inasemekana alikuwepo Tanga akifanya kazi katika mashamba ya mkonge ya wakoloni, na Paul Hamis alikuwa raia wa Tanzania mzaliwa wa Lushoto mkoani Tanga. Watu hawa walijulikana zaidi kwa matukio yao ya uhalifu kwa wakoloni hasa wizi na kisha walikimbilia mapangoni kujificha.

Na hapo niliweza kuona aina ya popo wajulikanao kama Fruit Bats wakiwa ndani ya pango hilo wakishiriki sana katika kuongeza michoro ya ajabu ya wanyama, na nyayo za binadamu ndani ya pango hilo kwa upande wa juu…

Tuliingia jijini Mombasa mnamo saa 11:40 jioni tukiwa tumechoka. Hali ya hewa ya joto la wastani yenye kiasi kikubwa cha unyevunyevu isiyotofautiana na ile ya Dar es Salaam kidogo inifanye nishindwe kubaini kuwa tayari nilikuwa nimeikanyaga ardhi ya Mombasa nchini Kenya.

Mfukoni nilikuwa na kiasi fulani cha fedha za Kenya ambacho nilikuwa nimekipata baada ya kuvuka mpakani mwa Kenya na Tanzania na kubadilisha fedha za Tanzania katika duka moja la kubadilisha fedha za kigeni lililokuwa katika eneo la Horohoro, kwenye mpaka upande wa Kenya.

Inaendelea...
 
ufukweni mombasa.JPG

242

Hii haikuwa mara yangu ya kwanza kufika Kenya lakini ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kusafiri na basi na hasa safari ya Mombasa, lakini maelezo ya Zuena kwa kiasi fulani yalinifanya nisiwe mgeni kabisa wa mazingira ya Jiji la Mombasa.

Nilikuwa nimechoka sana kutokana na ukweli kwamba sikuwa nimepata usingizi mzuri usiku wa siku iliyokuwa imetangulia, halafu wakati tukiwa safarini baadhi ya maeneo, barabara ilionekana kuharibika, hasa barabara ya kutoka Lungalunga ukiivuka Ramisi, Ukunda hadi tulipoingia maeneo ya Likoni jijini Mombasa.

Baada ya kufika jijini Mombasa tulivuka katika kivuko maarufu cha Likoni (Likoni Ferry) na mara tu baada ya kuvuka nikashukia hapo Likoni na kuchukua begi langu dogo la safari huku nikiagana na Zuena wa Mombasa, tayari tukiwa tumeshapeana namba, Zuena alikuwa amenipa mawasiliano yake na niliahidi kumtafuta siku iliyokuwa inafuata baada ya kupata hoteli na kupumzika.

Niliposhuka yeye akaendelea na safari, alikuwa ameniambia kuwa angeshukia katika ofisi za kampuni hiyo ya mabasi ya Tahmeed zilizokuwa kwenye jengo moja Barabara ya Magongo kisha angerudi hadi Changamwe Roundabout kwenye mzunguko wa barabara za Mombasa na Magongo, halafu angeifuata Barabara ya Mombasa na kuelekea uelekeo wa Bangladesh hadi Mikindani alikokuwa akiishi.

Sasa hapo Likoni baada ya kushuka nikaenda mbele kidogo nikifuata uelekeo kituo cha Matatu huku nikitafuta teksi na hapo dereva mmoja wa teksi mjanja akaniwahi haraka kabla ya wenzake, baada ya kuhisi hitaji langu.

Mzee yule wa makamo, mrefu na mnene mwenye sura ya ucheshi alikuwa amevaa baragashia, shati jeupe, suruali ya kijivu na makubazi ya ngozi miguuni, aliwahi kuufungulia mlango wa teksi yake akinitaka niingine hata kabla sijaafikiana naye na kumweleza hitaji langu. Kwa ushawishi ule sikuwa na pingamizi hivyo nikaingia ndani na kuliweka begi langu la safari kwenye kiti cha nyuma, na mara tu nilipoketi kwenye kiti yule dereva wa teksi akaingia na kuketi kwenye usukani huku akinitupia swali, “Unaelekea wapi, bosi wangu?

“Nipeleke Serena Beach Resort,” nilimwambia yule dereva huku nikijiegemeza kwenye kiti changu kisha nikashusha pumzi ndefu.

Kitambo kifupi cha ukimya kikafuatia wakati mzee yule dereva wa teksi akiitoa teksi yake kwenye maegesho yale ya teksi karibu na kituo cha Matatu cha Likoni na kuifuata Barabara ya Likoni. Hakuwa mzee wa maneno mengi na badala yake akawasha redio ndogo iliyokuwemo kwenye gari lake na kuweka kituo cha burudani. Hapo nikawa nasikiliza nyimbo mbalimbali za wasanii wa Afrika Mashariki hususan nyimbo za Bongo Fleva.

Mbele kidogo tukaufikia mzunguko wa barabara maarufu kwa jina la Nakumatt Likoni Roundabout. Nilishuhudia tukiuvuka ule mzunguko wa barabara na kuendelea mbele zaidi tukiifuata Barabara ya Nyerere kisha tukayavuka majengo marefu yaliyojulikana kama Likoni Towers yakiwa upande wetu wa kulia.

Wakati tukiyavuka majengo ya Likoni Towers kwenye barabara ile ya Nyerere, nikakumbuka jambo na kumuuliza yule dereva wa teksi, “Ni shilingi ngapi kutoka hapo Likoni Ferry hadi Serena Beach Resort?”

“Shilingi elfu mbili tu, kijana wangu,” yule dereva wa teksi aliniambia bila ya kuniangalia, macho yake yalikuwa makini kutazama barabarani. Sikutia neno. Kwa nini nibishe wakati sikuwa hata najua nauli halisi ya teksi kutoka pale Likoni Ferry hadi Serena Beach Resort?

Tulizidi kwenda mbele zaidi kisha tukayavuka majengo mbalimbali makubwa ambayo kwa kuyaangalia tu nikagundua kuwa yalitumika kama ofisi za taasisi mbalimbali za serikali na binafsi, halafu tukavuka eneo la Uwanja wa Mpira wa Mamlaka ya Michezo ya Kenya, na mbele ya uwanja huo nikaliona Kanisa la Waadventista wa Sabato.

Gari lilizidi kukata upepo likiifuata barabara ile ya Nyerere hadi tulipozifikia barabara pacha za Nyerere na Dedan Kimath tukaendelea mbele zaidi tukiifuata barabara ile ya Nyerere huku tukikatiza katikati ya majengo ya ghorofa hadi tulipoufikia mzunguko wa barabara za Nyerere, Moi, Nkrumah na Abdel Nasser.

Hapo barabara ya Nyerere ikaonekana kukoma na hivyo dereva akaifuata Barabara ya Abdel Nasser hadi mbele tulipozikuta barabara pacha, tukaiacha barabara ile ya Abdel Nasser na kukata kushoto tukiifuata barabara ya Sheikh Abdullas F. Nilipoliona jina la Abdullas mara moja nikamkumbuka Leyla Slim Abdullas.

Ni wakati huo pia nikaona si vibaya kama ningetumia fursa hiyo kufanya utalii usio rasmi. Nilianza kuyatembeza macho yangu taratibu kutazama nje nikiyatathmini vizuri mandhari ya barabara ile ya Sheikh Abdullas F jijini Mombasa wakati gari letu likizidi kukata upepo. Kitu cha kwanza kilichokuwa kimenivutia ilikuwa ni juu ya mpangilio mzuri wa majengo mbalimbali, barabara nzuri na makazi ya watu katika jiji.

Kisha tulizipita Hosteli za Mzizima zilizokuwa upande wetu wa kulia na mbele kidogo tukaikuta Barabara ya Kisauni iliyokuwa inakatisha kutoka upande mmoja kuelekea upande mwingine wa eneo lile. Hapo nikamwona dereva akiongeza mwendo na kusonga mbele akiifuata barabara ile ya Sheikh Abdullas F hadi alipoyapita majengo ya Chuo Kikuu cha Tiba cha Aga Khan na Benki ya KCB Tawi la Nyali.

Eneo hilo tulikuta makutano ya barabara za Sheikh Abdullas F, Ronald Ngala na Nyali, nikamwona dereva wa ile teksi akikata kuelekea upande wa kulia akiifuata Barabara ya Nyali kisha akaongeza tena mwendo wakati tukilivuka daraja maarufu la New Nyali na kutokea upande wa pili wa mji kisha tukayapita majengo ya Best Western Plus Creekside Hotel na mbele yake tukayapita majengo mengine ya Lights Matatu Stage, Vipingo na Kituo cha Mafuta cha Shell.

Nikiwa bado nafanya utalii usio rasmi nikashuhudia tukiipita Fairdeal Plaza na mbele yetu tukaikuta Benki ya Gulf African. Safari yetu ikionekana bado inaendelea na kunifanya nishushe pumzi ndefu za ndani kwa ndani huku nikihisi njaa ikinisokota tumboni hasa nilipoyaona majengo ya Brookside Depot yaliyokuwa upande wetu wa kushoto, nilitambua kuwa majengo yale yalikuwa yanatumika kuhifadhi maziwa ya Brookside.

Mbele kidogo tukauvuka mgahawa maarufu wa Acapulco Club & Restaurant ambao ulikuwa upande wetu wa kulia, na kushoto kwetu kulikuwa na majengo ya Kituo cha Afya cha Kisimani. Kisha tukaipita Bombolulu Sports Stage na kisha Bombolulu Estate Stage.

Sasa nilihisi kuchoka zaidi maana niliona kama vile dereva aliamua kunichezea akili kwa kunizungusha tu katika barabara za mjini, kwani sikutegemea kama safari yetu ingelikuwa ndefu kiasi kile kutoka Likoni Ferry hadi Serena Beach Resort & Spa. Nikapiga miayo na kutoa msonyo mdogo wa uchovu huku nikijilaza kwenye kiti. Na hapo nikamwona yule dereva akinitupia jicho na kuachia tabasamu.

“Usichoke, kijana wangu, wewe bado una nguvu… hata hivyo tumeshakaribia Serena Beach Resort,” yule dereva wa teksi alisema.

Nilimtazama tu na kutabasamu bila kusema neno, kisha nikayapeleka macho yangu kuangalia nje na baada ya kitambo kifupi cha safari yetu hatimaye tukawa tumetokezea kwenye majengo ya Chuo cha Mafunzo ya Viwanda cha Mombasa yaliyokuwa upande wetu wa kulia na kushoto kwetu lilikuwa ni eneo la Haller Park Mombasa lililokuwa na miti mingi katika barabara ile ya Malindi.

Inaendelea...
 
ufukweni mombasa.JPG

243

Mara tu tulipoingia kwenye barabara ile ya Malindi tukashika uelekeo huo na mwendo wetu ukaongezeka tena huku dereva yule wa teksi akionekana kuwa makini zaidi na sheria zote za barabarani wakati alipokuwa akipishana na magari machache na watembea kwa miguu kando ya barabara ile.

Halafu tukayapita majengo ya Naivas Supermarket, Nakumatt Nyali Shopping Center, City Mall na CTM Mombasa. Safari yetu ikiwa inaendelea tukaanza kuyapita majengo mengine ya hoteli mbalimbali za kitalii upande wetu wa kulia, hoteli kama Mlele Beach, Bamburi Beach Villa na hoteli nyingine nyingi za aina ile zilizokuwa ufukweni mwa Bahari ya Hindi.

Tulipolizidi kwenda mbele dereva akazidi kukata kushoto na mbele tukalivuka Kanisa la AIC na majengo mengine yaliyoonekana kuwa ya makazi ya watu, ofisi na migahawa mbalimbali. Hapo tukaonekana kuzidi kuuacha Mji wa Mombasa tukielekea nje ya mji. Nikaanza kuingiwa na wasiwasi lakini nikakumbuka maelezo niliyosoma kwenye mtandao wa intaneti wakati nafanya mawasiliano na Serena Beach Resort kuwa ipo takriban kilomita 30 kutoka katikati ya Mji wa Mombasa.

Nikiwa bado nashangaa nikaona tukivuka jengo la White Cliff Villa na Shule ya Msingi ya Shimo la Tewa, kisha nikamwona dereva akipunguza mwendo na kuiacha Barabara ya Malindi halafu akakata kulia akiifuata Barabara ya Serena. Na hapo nikamwona akigeuza shingo yake kunitazama huku akiachia tabasamu kisha akazungumza katika namna ya kumtia moyo. “Sasa tumeingia katika Barabara ya Serena, hii inaelekea moja kwa moja hadi Serena Beach Resort.”

Kisha aliongeza tena mwendo akiifuata barabara hiyo ya Serena hadi mbele tulipozikuta barabara pacha, dereva akazidi kuifuata barabara ile ya Serena iliyokuwa inakunja kuelekea upande wa kulia huku akiyavuka majengo ya Sunset Paradise na mbele yake kulikuwa na Mgahawa wa Tavern Grill. Tulipoupita mgahawa ule wa Tavern Grill dereva akaanza kupunguza mwendo huku nikiendelea kufanya utalii wangu usio rasmi.

Kisha nikaona tukilipita jengo la Serena Mini na baada ya kitambo kifupi cha safari ile ndefu yenye mzunguko hatimaye nikamwona dereva akipunguza zaidi mwendo na kukata kona akiingia upande wa kulia. Kisha tukayavuka majengo ya Kenya Migros Shop, Safari Inn Bar & Restaurant, Sonia Hotels & Apartments na mbele yetu nikaanza kuyaona majengo ya Serena Beach Resort & Spa yaliyokuwa ufukweni kabisa mwa Bahari ya Hindi.

Dah… nilijikuta nikipata nguvu upya, nikainua kichwa changu kutazama mandhari ya kupendeza yaliyozunguka eneo la Serena Beach Resort & Spa, hoteli kubwa ya hadhi ya nyota 4 iliyokuwa kilomita 30 kutoka katikati ya Mji wa Mombasa.

Hoteli ile ilikuwa na eneo kubwa la mbele la maegesho ya magari lililokuwa limepandwa miti mirefu ya kivuli iliyozungukwa na bustani ya maua ya kupendeza yenye hewa safi ya upepo wa asili baina ya sehemu moja ya maegesho ya magari na sehemu nyingine. Kulikuwa na taa hafifu za ardhini zilizokuwa zikimulika eneo lile na hivyo kulifanya eneo lote lipendeze mno.

Nilibaki kimya nikilikodolea macho jengo la hoteli hiyo na kuyashuhudia magari kadhaa madogo yaliyokuwa yameegeshwa katika eneo la maegesho ya magari. Pia kulikuwa na malori mawili makubwa ya kubebea watalii wa masafa marefu yaliyokuwa yameegeshwa upande wa kushoto, mwisho wa majengo.

Upande mwingine wa eneo lile kulikuwa na bustani ya nyasi laini zilizokatwa vizuri na kupendeza na katika bustani ile kulikuwa na sehemu za kupumzika zenye viti na meza chini ya miamvuli mikubwa yenye rangi za kupendeza. Pia kulikuwa na mabwawa makubwa ya kuogelea, sehemu zenye viti maalumu vya kupumzikia chini ya miti mizuri aina ya coconut palms pamoja na vibanda vidogo vya faragha.

Nje ya ile hoteli niliona milingoti sita yenye bendera zilizokuwa zinazopepea taratibu. Kulikuwa na bendera ya Afrika Mashariki, Tanzania, Afrika Kusini, Uingereza, India na bendera iliyokuwa na nembo ya Serena Beach Resort. Kwa ujumla lile jengo la Serena Beach Resort lilikuwa limejengwa kwa ufanisi wa hali ya juu.

“Tumekwisha fika, kijana wangu,” sauti ya yule dereva wa teksi ilinishtua kutoka kwenye mawazo yaliyoanza kuniteka, nikainua uso wangu kumtazama na hapo nikakumbuka kuwa ile teksi ilikuwa imesimama mbele ya ile hoteli kubwa yenye mandhari tulivu ya kupendeza na nilisubiriwa mimi tu nishuke. Nikaachia tabasamu na kufungua mkanda kisha nikatoa pochi yangu na kutoa kiasi kilichotakiwa, nikamlipa yule dereva na kufungua mlango wa ile teksi halafu nikashuka.

Nikalichukua begi langu la safari na taratibu nikaanza kukatisha kwenye viunga vile vya maegesho ya magari nikielekea mbele ya lile jengo, sehemu ambayo kulikuwa na mlango mkubwa wa kioo kwenye varanda pana yenye ngazi iliyofunikwa kwa kofia nzuri ya zege.

Mbele ya jengo hilo kwenye varanda niliwaona vijana wawili na mara moja nikawatambua kuwa walikuwa wahudumu wa ile hoteli waliokuwa wamesimama kando ya ule mlango wa kuingilia kwa ndani. Vijana wale walivaa sare maalumu za kazi; suruali za rangi nyeusi, mashati meupe yenye kola za rangi ya bluu bahari na makoti ya suti ya rangi ya bluu. Wakanipokea kwa bashasha zote huku wakinionesha tabasamu la kirafiki kwenye nyuso zao.

“Habari za kazi?” niliwasalimia wale vijana huku nikiwatazama kwa tabasamu.

“Salama kaka, karibu sana Serena Beach Resort,” Wale vijana walinijibu huku wakichangamka kwa kuonesha bashasha zote za kirafiki. Muda huo huo nikaushuhudia ule mlango mkubwa wa kioo wa mbele ukifunguliwa na mfanyakazi mwingine mwanamume aliyekuwa amevaa sare akajitokeza na kunifuata halafu akapokea begi langu la safari kisha akaniongoza ndani.

Niliwashukuru vijana wale kwa ukaribisho wao na kumfuata yule mfanyakazi mwingine aliyebeba begi langu tukatembea juu ya kipande mstatili cha zulia jekundu kilichoanzia kwenye ngazi kikipanda samabamba na ngazi hizo hadi kwenye varanda ile yenye sakafu nzuri ya tarazo iliyoandikwa kwa ufundi mkubwa jina la hoteli ile na kuelekea sehemu ya mapokezi ya hoteli ile. Kisha yule mfanyakazi akausukuma ule mlango mkubwa wa kioo na kusimama kando akinipisha niingie ndani, nilipoingia na yeye akaingia.

Nikajikuta nimetokea katika sehemu ya mapokezi iliyokuwa na umbo la nusu duara ikizungukwa na meza nzuri ya kaunta ya mbao nzuri za mti wa mninga iliyokuwa ikitazamana na makochi meusi ya ngozi laini ya sofa. Pale mapokezi kulikuwa na watu wachache, wawili kati yao walikuwa wenye asili ya Somalia, Mswahili mmoja na Wazungu wawili ambao bila shaka walikuwa wanandoa kwa jinsi walivyoonekana.

Wale Wasomali na Mswahili walikuwa wameketi kwenye yale makochi ya sofa na Wazungu walikuwa wamesimama pale kaunta. Nikasogea pale sehemu ya mapokezi na kuwakuta wahudumu wawili, kaka na dada wakiwa katika sare zao nadhifu za kazi za mashati meupe yenye kola za rangi ya bluu bahari, suruali za rangi ya bluu na makoti ya suti ya rangi ya bluu huku shingoni wakiwa wamevaa tai ndogo nyeusi zilizowapendeza.

Yule mfanyakazi aliyekuwa amebeba begi langu aliponifikisha pale mapokezi akaniacha, nikasimama nikiwatazama wale wahudumu wawili niliowakuta hapo. Wakati huo yule mhudumu wa kiume alikuwa anazungumza na wale wazungu wawili.

Inaendelea...
 
ufukweni mombasa.JPG

244

Yule mhudumu wa kike alikuwa anajaza fomu fulani wakati niliposimama mbele ya ile kaunta ya mapokezi, hivyo haraka aliiacha ile fomu kisha uso wake ukiwa umefanikiwa kutengeneza tabasamu zuri la kirafiki alinitazama na kushusha pumzi ndefu za ndani kwa ndani.

Alikuwa msichana mrembo na kwa mtazamo wa haraka tu niliweza kubaini kuwa hakuwa amezidi miaka ishirini na tano, japokuwa alikuwa amevaa sare za kazi lakini bado uzuri wake haukuchujuka hata chembe. Nywele zake nyeusi za kibantu alikuwa amezisuka kwa mtindo wa mkia wa pweza hivyo kumfanya aonekane mzuri wa asili. Alikuwa na macho makubwa na meupe yaliyozungukwa na kope ndefu na nyeusi, pua yake ilikuwa ndogo, mdomo wake wa kike ulikuwa na kingo pana kiasi na vishimo vidogo mashavuni vinavyochomoza haraka kila anapotabasamu.

Nilipomchunguza vizuri yule mhudumu nikakiona kidani chenye herufi ‘M’ kikiwa kimenasa vyema kwenye shingo yake ndefu na kuning’inia katikati ya matiti yake madogo yenye chuchu imara zilizotuna na kuisumbua kidogo blauzi yake.

“Dada, habari za kazi?” niliwahi kumsalimia yule mhudumu wa kike huku usoni kwangu nikitengeneza tabasamu.

“Nzuri tu kaka, karibu sana Serena Beach Resort & Spa,” yule dada wa mapokezi aliitikia salamu yangu huku akiachia tabasamu pana la makaribisho kwa bashasha zote na kunikaribisha kwa sauti nyororo ya kike.

“Ahsante sana dada, nilifanya reservation nikiwa jijini Dar es Salaam siku tano zilizopita…” nilianza kujieleza, yule dada wa mapokezi akanidaka juu kwa juu kabla hata sijamaliza sentensi yangu, huku akinitazama kwa utulivu.

“Unaitwa nani vile?” aliniuliza huku akiyatuliza macho yake usoni kwangu.

“Jason Sizya,” nilisema huku nikikohoa kidogo kurekebisha sauti yangu. Na hapo yule dada wa mapokezi akanitazama kwa uyakinifu kama mtu anayejaribu kuvuta kumbukumbu zake kisha akakichukua kitabu kikubwa chenye taarifa za wageni wa ile hoteli kilichokuwa kando yake pale juu mezani.

Nikamwona akifunua kurasa kadhaa za kile kitabu kwa utulivu hadi pale alipoufikia ukurasa alioutaka, akaweka kituo na kuyapitia maelezo fulani yaliyokuwa kwenye ule ukurasa.

OkayJason Sizya from Dar es Salaam, Tanzania…” yule dada wa mapokezi alisema huku akiinua uso wake na kunitazama huku akibetua kichwa chake. Kisha akaongeza, “Room number 204. I hope you’ll like it.”

Aliposema hivyo akachukua kadi maalumu ya kielektroniki iliyokuwa mfano wa kadi ya benki, ambayo hutumika kufungua mlango wa chumba, halafu akaizunguka ile meza ya mapokezi na kunifuata pale nilipokuwa nimesimama na kuchukua lile begi langu, akanitaka nimfuate. Nikamfuata na hapo tukaliacha lile eneo la mapokezi na kushika uelekeo wa upande wa kushoto tukielekea sehemu kulipokuwa na chumba cha lifti ya lile jengo la hoteli ili kuelekea juu.

Mbele kidogo tukaingia upande wa kulia na kuupita mlango mkubwa wa kuelekea kwenye chumba cha mazoezi ambao juu yake kulikuwa na kibao cheusi chenye maandishi meupe yaliyokuwa yakisomeka ‘Gym’. Na upande wa kushoto kulikuwa na mlango uliokuwa unaelekea sehemu ya maliwato. Hatua chache mbele yetu mwisho kabisa wa ule ukumbi upande wa kushoto tukakifikia chumba cha lifti ya kuelekea orofa za juu za lile jengo la hoteli ya Serena Beach Resort & Spa.

Yule dada mhudumu akabonyeza kitufe cha kuita lifti kilichokuwa pembeni ya mlango wa chumba cha lifti. Kwa dakika nzima tulisimama pale tukisubiri kile chumba cha lifti kishuke chini kwa vile kulikuwa na watu ndani yake wakishuka chini kutoka orofa za juu za lile jengo. Kile chumba kilipofika chini na milango yake ikafunguka, wakatoka watu watatu, mwanaume mmoja Mwafrika na Wazungu wawili ambao kwa mtazama tu usingeshindwa kubaini kuwa walikuwa mke na mume.

Nasi tukapata nafasi ya kuingia ndani ya kile chumba cha lifti kisha yule dada wa mapokezi akabonyeza kitufe cha kuiamuru ile lifti itupeleke katika orofa ya pili ya lile jengo. Muda mfupi uliofuata kile chumba cha lifti kikaanza kukwea juu ya lile jengo hadi kwenye orofa ya pili. Kilipotia nanga na kugota katika orofa ile na milango yake kufunguka na kuturuhusu kutoka, nikatoka na kujikuta nikiwa katikati ya ukumbi mpana wenye utulivu wa hali ya juu.

Mandhari katika ile orofa ya pili ya jengo la Serena Beach Resort & Spa yalionesha vizuri kuwa ni kwa sababu gani hoteli ile ilikuwa imepewa hadhi ya nyota nne. Kulikuwa na hewa safi iliyokuwa ikisambazwa taratibu na viyoyozi viwili, kimoja kikiwa mwanzo wa ule ukumbi na kingine mwisho wa ukumbi. Sakafu katika ukumbi ule ilikuwa na tarazo maridadi zilizokuwa na nakshi za kupendeza na hapakuwa na kitu kingine cha ziada zaidi ya utulivu mkubwa.

Tulitembea taratibu tukikatisha katikati ya ule ukumbi, yule dada mhudumu akiwa mbele na mimi nyuma huku nikiyatembeza macho yangu kutazama upande huu na ule nikizisoma namba zilizokuwa juu ya milango mikubwa na imara ya mbao ngumu iliyokuwa ikitazamana na ule ukumbi, wakati tukitembea tukapishana na mwanamume mmoja mrefu wa Kisomali aliyetoka katika chumba jirani na eneo lile.

Wakati tukipishana akatusalimia, tukaitikia kisha akashika hamsini zake akielekea kwenye lifti. Wakati tunatazamana niliona kitu fulani katika macho yake ambacho si rahisi kwa mtu wa kawaida, asiye na taaluma ya ujasusi kukiona. Kulikuwa na dalili zote za ukatili, dharau, unyama na dhihaka ya hali ya juu kwenye macho yake. Nikajikuta nikivutiwa zaidi kumtazama kwa umakini, na hivyo nikageuka kumtazama. Ni wakati huo huo yeye pia alikuwa anageuka kunitazama na macho yetu yakagongana. Nikamtambua.

“Abshir!” nilitamka kwa sauti ya chini ambayo haikuweza kusikiwa na yule dada wa mapokezi. Nilihisi kusisimkwa mwili wangu na damu ikaanza kunichemka na kukimbia kwenye mishipa yangu ya damu, vinyweleo mwilini na nywele kichwani zikanisisimka. Na hali ile ikasababisha mapigo yangu ya moyo yaende mbio huku jasho jepesi likianza kunitoka sehemu mbalimbali za mwili wangu! Sasa hamu yangu ya kutaka kumfuatilia ikaibuka tena ndani yangu lakini nikasita kufanya hivyo kwa muda huo.

Ndiyo, alikuwa Abshir, mwanamume wa Kisomali aliyeambatana na Rahma wa Singida pale Lamada Hotel baada ya kushuka toka kwenye gari aina ya Range Rover SV Autobiography LWB la rangi nyeusi nililolifuatilia tangu Posta.

Donge la hasira lilinikaba kooni na kunifanya nipumue kwa nguvu, na wakati huo huo kengele ya hatari ikalia kichwani kwangu. Kwa mara ya kwanza nikawa nimepata jibu la kwa nini hisia zangu ziliniambia kuwa Rahma wa Singida alikuwa na mambo yaliyojificha nyuma ya pazia.

Nikatambua kuwa kumbe walipoondoka pale Lamada Hotel walikimbilia Mombasa, sasa nikawa na hamu ya kutaka kukutana na Rahma wa Singida. Wakati nikiwa bado namtazama Abshir huku nikitafakari nikamwona akikifikia chumba cha lifti na kubonyeza kitufe cha kuita lifti kisha akageuka kunitazama na kuachia tabasamu ambalo niliona kuwa lilibeba dharau. Milango ya ile lifti ilipofunguka nikamwona akiingia huku akinitupia macho yaliyoongea, “See you soon!” (Tutaona hivi karibuni).

Nami nikamtazama kwa macho yaliyonena, “You go to hell!” (Nenda kuzimu!) huku hasira zikichemka ndani yangu.

Wakati huo huo milango ya ile lifti ikawa inajifunga, nikahisi kama alikuwa ananiambia “You’ll see how hell looks like…” (Utaiona kuzimu inavyofanana…) Kisha milango ya lifti ikajifunga na lifti kuanza kushusha chini.

Inaendelea...
 
ufukweni mombasa.JPG

245

“Chumba chako ni hiki hapa, kaka,” nilishtuliwa na sauti ya yule dada wa mapokezi aliyekuwa amesimama mbele ya mlango uliokuwa umeandikwa nambari 204 juu yake. Alikuwa ananitazama kwa mshangao huku akiwa ameshika ile kadi ya kielektroniki akijiandaa kuipitisha juu ya kitasa cha mlango.

Nilimfuata haraka wakati akiipitisha ile kadi ya kielektroniki juu ya kitasa kisha akakishika na kukinyonga taratibu huku akiusukuma ule mlango kwa ndani, mlango ukafunguka na kuturuhusu kuingia. Tulipoingia nikajikuta nimo ndani ya chumba kikubwa cha kisasa. Nikasimama katikati ya kile chumba nikikitazama kwa namna ya kukitathmini vizuri. Nilikuwa nakitazama kwa kukikagua ili kuhakikisha usalama wangu kwanza. Ilikuwa ada yetu kuhakiki usalama kila mahala tunapokuwa.

Kilikuwa chumba kikubwa chenye nafasi ya kutosha kikiwa na kitanda kikubwa cha sofa chenye godoro la foronya laini ambalo lilikuwa limefunikwa kwa shuka safi za rangi ya bluu bahari. Kando ya kile kitanda kulikuwa na mlango wa kuelekea kwenye chumba kidogo cha maliwato.

Pia kulikuwa na makochi mawili ya sofa nyuma ya meza ndogo fupi ya mbao yenye kibakuli kidogo cha majivu ya sigara juu yake na pembeni yake kulikuwa na kabati zuri la nguo la ukutani, likiwa pembeni ya dirisha kubwa la kile chumba. Dirisha ambalo lilifunikwa kwa mapazia marefu na mepesi yaliyokuwa yanaruhusu hewa safi kutoka nje ipenye na kuingia mle ndani.

Kwa upande mwingine kulikuwa na seti moja kubwa ya runinga pana aina ya Sumsung iliyokuwa imefungwa vizuri ukutani na kuunganishwa na kisimbuzi cha DSTv chenye chaneli nyingi za kimataifa. Chini ya ile runinga kulikuwa na meza ndogo nyeusi na juu ya ile meza kulikuwa na simu ya mezani. Pembeni ya simu ile kulikuwa na kitabu kikubwa cha rangi ya njano chenye orodha ya majina na namba za simu za watu na kampuni mbalimbali za nchini Kenya. Pia kulikuwa na jokofu lililokuwa limesheheni vinywaji mbalimbali ndani yake.

Yule dada wa mapokezi aliliweka lile begi langu juu ya meza ndogo fupi ya mbao iliyokuwa mbele ya yale makochi mawili ya sofa kisha akaziendea swichi zilizokuwa ukutani na kuzibonyeza kwa pamoja mara taa za mle chumbani zikatoa mwanga wa kutosha na hapo hapo kiyoyozi kilichokuwa sehemu fulani kwenye kona ya kile chumba, kikaanza kusambaza hewa safi ya ubaridi mle chumbani.

Baada ya hapo akanimpa maelekezo kuhusu ile simu ya mezani na taratibu zingine za pale hotelini na kuniaga akiwa tayari kuondoka, lakini kabla hajaondoka kabisa nikakohoa kidogo kama ishara ya kutaka kuongea neno. Yule dada wa mapokezi akageuza shingo yake kunitazama kwa shauku. Nikashusha pumzi za ndani kwa ndani huku nikiachia tabasamu.

“Nashukuru sana kwa ukarimu wenu lakini napenda kufahamu hiyo herufi ‘M’ kwenye kidani chako ina maana gani?” nilimtupia swali yule dada wa mapokezi, swali hilo likamfanya aachie tabasamu pana.

“M inasimama badala ya jina langu,” yule dada wa mapokezi alisema huku akiinamisha uso wake kutazama eneo la kifuani kilipokuwa kinaning’inia kile kidani, akakishika kisha akainua uso wake kunitazama huku akiwa bado anatabasamu.

“Miriam, Mary, Monica, Mercy...” nilijaribu kubashiri jina huku nikimkazia macho.

“Merina…” yule dada wa mapokezi alinikatisha kabla sijamaliza ubashiri wangu huku akiangua kicheko hafifu kilichofanya vishimo vidogo vya mashavuni mwake vijitokeze na kuonekana waziwazi bila kificho.

“Ooh… Merina wa Mombasa!” nilisema kwa sauti tulivu huku uso wangu ukipambwa na tabasamu.

“Merina Ndambuki,” Merina alinisahihisha huku akitazama kando kuyakwepa macho yangu yaliyokuwa yakimtazama kwa makini usoni.

“Niruhusu nikuite Merina wa Mombasa…” nilisema kwa utani huku nami nikiangua kicheko hafifu kisha nikaongeza, “Afterall, una jina zuri sana kama ulivyo wewe mwenyewe.”

“Mmh! Ya kweli hayo?” Merina aliuliza huku akiona aibu. “Hata hivyo nashukuru, sijui na wewe unaitwa nani?”

“Duh! Yaani mara hii tu tayari umeshasahau jina langu?” nilimuuliza Merina kwa mshangao. Na hapo nikamwona akijipiga kofi dogo kwenye paji la uso wake kwa kiganja cha mkono wake wa kulia huku akijisonya kwa usahaulifu.

Oh shit! Your name is Jason Sizya from Dar es Salaam, right?” Merina alisema na kuangua kicheko hafifu kisha akanitupia swali, “Hii ni mara yako ya kwanza kufika hapa Serena Beach Resort & Spa?”

“Si hapa Serena Beach Resort & Spa pekee bali ni mara yangu ya kwanza kufika Mombasa,” nilisema huku nikiketi juu ya kile kitanda kikubwa.

“Ooh! Karibu sana Mombasa, I hope you’ll enjoy a lot…” Merina alisema huku akiangua kicheko. Na hapo nikagundua kuwa alipenda sana kucheka.

I hope too…” nilisema kwa sauti tulivu kisha nikamtupia swali huku nikiwa nimemtazam usoni, “Vipi shemeji yangu hajambo?”

Swali langu likamfanya Merina anitupie jicho la hisia huku akiachia tabasamu la aibu kisha taratibu akatikisa kichwa chake kuonesha kuikataa hoja ile huku tabasamu lake likiwa bado linachanua usoni mwake.

“Unakaa wapi hapa jijini Mombasa?” nikamtupia swali jingine huku nikiwa makini kumtazama machoni.

“Nakaa eneo la Utange barabara ya Old Malindi karibu na Kanisa la Agape Fellowship Center,” Merina akaniambia huku akiitazama saa yake ya mkononi.

“Leo unatoka saa ngapi kazini?” nilimsaili tena, nikamwona ameshtuka kidogo na kunitazama usoni kwa udadisi, nikaachia tabasamu la kumlainisha. Na kweli akaonekana kulainika.

“Natoka saa mbili usiku baada ya wenzetu kuja kutupokea zamu,” Merina akaniambia kwa sauti tulivu huku akionesha jitihada za kutaka kuondoka ili arudi mapokezi.

“Nikija kukutembelea kuna shida yoyote?” nilimsaili tena kwa sauti tulivu huku nikiumba tabasamu usoni, muda wote nilikuwa namtazama machoni katika namna ya kutaka kupata hakika na jibu ambalo lingemtoka mdomoni.

Merina alibaki kimya akiwa ameinamisha uso wake chini kama mtu anayefikiria jibu, kisha akainua uso wake kunitazama, “Dah, nyumbani kuna mbwa mkali.”

“Basi naomba namba yako ya simu,” nilimwambia. Hakusita badala yake akaanza kuzitaja namba zake za simu taratibu katika namna ya kuhakikisha kuwa nazinakili bila usumbufu.

“Kesho utakuwa na ratiba gani?” nilimuuliza tena baada ya kuzikariri zile namba kichwani.

“Kesho ninapumzika hadi keshokutwa ndiyo nitaingia kazini asubuhi,” Merina alisema kwa utulivu huku akifikiria jambo.

“Basi tutawasiliana,” nilimwambia.

“Ondoa shaka,” Merina alisema kisha akaniaga kwa tabasamu maridhawa lililojaa aibu na kuondoka zake. Nikashusha pumzi na hapo nikakumbuka kumpigia simu Rehema ili nimjulishe kuwa nilikuwa nimefika Mombasa salama.

Nilichukua simu yangu na kupiga lakini simu ya Rehema ilikuwa haipatikani, nikapiga tena lakini hali ilikuwa ni ile ile. Nikataka kupiga namba ya mfanyakazi wa nyumbani lakini nikakumbuka kuwa sikuwa nimechukua namba yake. Nikashusha pumzi huku nikipanga kumpiga tena baadaye na kama hali ingeendelea kuwa ile ile ya kutopatikana basi ningempigia Pamela nikimtaka aende nyumbani akajue kulikuwa na tatizo gani.

Kisha nilijilaza chali juu ya kile kitanda huku miguu yangu ikiwa inaning’inia sakafuni. Simu yangu niliiweka kando yangu na kutazama juu ya dari halafu nikaanza kuzama kwenye bahari ya mawazo yaliyonirudishia kumbukumbu za Rahma wa Singida na Abshir. Picha nzima ya tukio la siku nilipowafungia mkia kuwafuata tangu Benki ya NBC kule Posta hadi Lamada Hotel pale Ilala ikajengeka akilini kwangu.

* * *

Inaendelea...
 
ufukweni-mombasa-jpg.2332085

246

Macho ya nyoka…




Saa 12:30 asubuhi…

NILISHTUSHWA kutoka usingizini na mlio wa kengele uliokuwa unasikika kwa fujo masikioni mwangu na kugeuka kuwa kero. Niliyafumbua macho yangu taratibu nikayatembeza mle ndani kutazama huku na kule na hapo nikakutana na mwanga mkali wa taa machoni mwangu.

Hali ile ikanifanya niyatulize vizuri mawazo yangu huku nikijaribu kufikiria vizuri kuwa pale nilikuwa wapi! Sikupata jibu la haraka na hivyo nikapeleka mikono yangu huku na kule kupapasa. Kwa kufanya vile taratibu fahamu zangu zikaanza kurejewa na uhai. Nikakumbuka kuwa nilikuwa nimelala kitandani kwenye chumba nambari 204 cha hoteli ya Serena Beach Resort & Spa na ile sauti niliyodhani ilikuwa ya kengele ilikuwa ni simu yangu ya mkononi ikiita.

Sikuweza kukumbuka haraka ni wakati gani usingizi ulifanikiwa kunichukua, nilichokumbuka tu ni wakati nilipopiga simu kutaka kumjulisha Rehema kuwa nilikuwa nimewasili salama Mombasa. Kisha nikajilaza kitandani na kuanza kutafakari juu ya Rahma wa Singida na yule mwanamume wake wa Kisomali, basi. Baada ya hapo sikukumbuka kitu kingine.

Kutokana na uchovu wa kutopata usingizi usiku uliokuwa umetangulia, ukijumlisha na safari ndefu ya kutoka Dar es Salaam hadi Mombasa kwa basi nikajikuta nimelala bila kula, bila kuoga na wala sikuwa nimevua nguo zangu! Nikashangaa sana na kuitupia jicho saa yangu ya mkononi ambayo ilionesha kuwa ilikuwa imetimia saa kumi na mbili na nusu. Nikajiuliza, ilikuwa ya jioni au asubuhi?

Nikiwa naanza kutafakari huku nikitazama nje kupitia ukuta msafi wa kioo cha dirisha nikajikuta napata jibu kuwa ilikuwa saa kumi na mbili na nusu ya asubuhi. Nikakurupuka kutoka pale kitandani na kusimama wima huku nikiikodolea macho saa yangu nikiwa siamini macho yangu. Saa kumi na mbili na nusu asubuhi! Hii ilimaanisha kuwa nilikuwa nimelala usingizi mzito, usingizi wa kifo, hadi asubuhi! Niliitazama tena saa yangu na kuminya midomo yangu, nikajikuta nikianza kuwaza mbali. Sikuamini kabisa kile nilichokuwa nikikiona kwenye ile saa.

Laiti ingekuwa ni saa ya kawaida labda ningesema ina kasoro, lakini ile ilikuwa ni saa ghali sana iliyonigharimu fedha nyingi. Haijawahi kudanganya hata siku moja! Nikahisi koo langu likinikauka ghafla na jasho jepesi likaanza kunitoka mwilini huku mapigo ya moyo wangu yakienda mbio isivyo kawaida.

Ile simu juu ya kitanda ilikuwa imekatika muda na kisha ikaanza kuita tena kwa fujo, niligeuka kuitazama na wakati huo huo nikipiga mwayo hafifu wa uchovu na kuanza kuvinyoosha viungo vyangu vya mwili, kisha nikajikongoja kivivu vivu kwenda pale kitandani nikiifuata ile simu. Nikaichukua lakini ikakatika kabla hata sijaangalia mpigaji alikuwa nani.

Niliitazama namba ya mpigaji wa simu na kushtuka baada ya kukutana na jina la Rehema. Nikakumbuka kwamba tangu nifike Mombasa jioni ya siku iliyotangulia sikuwa nimewasiliana naye, japo nilikuwa nimejaribu kumpigia kwenye simu yake mara mbili lakini haikuwa inapatikana. Nilibaki kuikodolea macho ile simu kama vile nilikuwa nimeshika kitu cha hatari sana huku akili yangu taratibu ikianza kuzama kwenye tafakuri nikiwaza jinsi ambavyo Rehema angeanza kulalamika kwa kutowasiliana naye tangu nifike Mombasa.

Wakati nikifikiria kumpigia mara simu ikaanza kuita tena. Sikusubiri, nikaipokea haraka na kuiweka sikioni huku nikiipa akili yangu utulivu wa hali ya juu.

“Hello!” sauti ya upande wa pili ikanitanabaisha kuwa mzungumzaji alikuwa mke wangu Rehema. Aliongea kwa sauti ya upole yenye utulivu mkubwa na hakuanza kulalamika kama nilivyodhani. “Vipi Baba Junior, bado umelala?”

“Ndiyo baby, bado nipo usingizini,” nilimjibu kwa utani huku nikiachia kicheko hafifu.

Sauti ya Rehema ikasikika kutoka upande wa pili wa simu wakati alipoangua kicheko cha ghafla na kicheko kile kilipokoma akasema, “Tangu lini mtu aliyeko usingizini akapokea simu na kujinadi kuwa yupo usingizini? Hebu acha vituko bwana…”

“Sawa mama, lakini tangu lini umeanza kuniuliza kama nimelala wakati unaona kuwa nimeipokea simu yako?” nilisema tena kwa utani huku nikimfanya Rehema aangue tena kicheko. Tukacheka kwa pamoja.

“Haya baba… Nitakuweza wapi maana siku zote huwa hukosi cha kuongea,” Rehema alisema baada ya kicheko kukatika. Kisha akaongeza, “Mbona umekuwa kimya tangu uondoke! Nimeshindwa kujua kama umefika salama au umepatwa na tatizo! Nimepiga simu tangu jana usiku hadi asubuhi hii lakini ikawa haipokelewi hadi nikaanza kupatwa na wasiwasi!”

Nilikunja sura yangu na kuitazama simu yangu kwa umakini huku nikijaribu kuvuta kumbukumbu ya kilichotokea usiku wa kuamkia siku hiyo, ni kweli kulikuwa na miito mingi ya simu ambayo haikuwa imepokelewa (missed calls). Nikashusha pumzi ndefu za ndani kwa ndani.

“Dah… usinilaumu na badala yake nihurumie tu, mke wangu. Jana nilichoka sana na nilijaribu kutafuta ukawa hupatikani, nikasema ningekupigia baadaye… lakini unajua nini kikatokea?” nilijaribu kujitetea huku nikipiga mwayo hafifu wa uchovu.

“Kulitokea nini, Al Shabab walivamia hoteli?” Rehema aliniuliza kwa utani huku akiachia kicheko hafifu.

“Aah… utani wa Al Shabab si mzuri…” nami nilisema kwa utani huku nikicheka. Kisha nikaongeza, “Nilichoka mno nikapitiwa na usingizi mzito! Nikasahau hata kula wala kuoga, na nguo nilizovaa tangu natoka Dar es Salaam bado zipo mwilini. Ndo kwanza simu yako imenishtua kutoka usingizini!” nilisema huku nikivinyoosha viungo vyangu vya mwili kwa mazoezi mepesi.

“Duh!” Rehema alisema kwa mshangao.

“We acha tu. Sikumbuki mara ya mwisho ilikuwa lini kulala usingizi wa namna hii,” nikasema huku nikishusha pumzi za ndani kwa ndani.

“Si nilikwambia usafiri kwa ndege ukang’ang’ania kwenda na basi, umeona sasa matokeo yake!” Rehema alisema katika namna ya kuninanga.

“Si mbaya kwani safari yangu imekuwa ni bonge la adventure ambayo huwezi kuipata ukisafiri na ndege,” nilisema huku nikipiga tena mwayo hafifu wa uchovu.

“Ni adventure sawa lakini na wewe umeipata fresh,” Rehema alisema kwa utani huku akiangua kicheko.

“Hapo ndo ngoma droo…” nilisema huku nikiitupia jicho saa yangu ya mkononi. “Basi ngoja nikajimwagie maji chapchap nitoe uchovu maana hapa napiga miayo mfululizo utadhani teja.”

Okay, take care!” Rehema aliniambia na kukata simu.

Niliirusha simu juu ya kitanda kisha nikafungua begi langu na kutoa mswaki na dawa ya meno halafu nikachukua taulo na kuelekea bafuni huku nikipepesuka. Mle bafuni nilijimwagia maji na kupiga mswaki, na dakika kumi na tano baadaye nilitoka nikiwa nimechangamka kweli kweli. Ama kweli maji ni dawa nzuri ya uchovu kwani nilikuwa najisikia safi kabisa.

Kisha nilijifuta vizuri maji, nikavaa suruali ya dengrizi ya rangi ya samawati, fulana nyepesi nyeupe na juu yake nilivaa shati la dengrizi la mikono mirefu, pia la rangi ya samawati. Kichwani nilivaa kofia ya bluu ya kapelo na miwani myeusi ya jua niliyoitumia kunikinga na macho ya watu. Halafu nikajipulizia marashi na kujitazama kwenye kioo kirefu kilichokuwemo mle chumbani, nikaona niko safi.

Inaendelea...
 
ufukweni mombasa.JPG

247

Sasa nilikuwa nimeingia rasmi Jijini Mombasa, jiji ambalo nilidhani nimekuja kupumzisha akili yangu na kufurahia mapumziko yangu na mwanadada mrembo Leyla Slim Abdullas, lakini uwepo Abshir, pengine na Rahma wa Singida, pale Mombasa ulikuwa umeamsha ari yangu ya kutaka kuyajua yaliyojificha nyuma ya pazia.

Baada ya hapo nikatoka chumbani na kuelekea ukumbi wa maakuli. Ulikuwa ukumbi mkubwa wa kisasa wenye madirisha makubwa ya vioo yaliyofunikwa na mapazia marefu yaliyosogezwa kando kidogo kuruhusu mwanga wa jua kupenya kwa urahisi kutoka nje na kuangaza mle ndani. Humo ukumbini nilikuta watu wengi kiasi na nyuso nyingi nilizoziona zilikuwa za wageni yaani watu kutoka nje ya bara la Afrika.

Mandhari yake yalikuwa mazuri na tulivu na ukumbi ule ukiwa na eneo kubwa lililotengenezwa kwa ustadi wa hali juu likiwekwa nakshi zilizochorwa na kutengenezwa kwa ustadi kuashiria mila na tamaduni za makabila yaliyopo Kenya. Ndani ya ukumbi wa chakula kulikuwa na meza ndefu za kisasa zilizozungukwa na viti vizuri vya sofa vyenye foronya laini.

Nilipoingia nikaanza kuzitupa hatua zangu kwa utulivu hadi kwenye meza moja ndefu iliyokuwa upande wa kulia kwenye kona moja ya ukumbi jirani na mlango wa kuelekea jikoni. Chakula kilikuwa kimeandaliwa kwa mtindo wa buffet (au kama tulivyozoea kuita bufee) ambapo unatakiwa ujipakulie mwenyewe na unaweza kurudia kuchukua chakula kadiri utakavyo.

Hivyo nilichukua sahani kubwa na kujipakulia chakula; nusu kuku wa kienyeji, chapati mbili za kumimina, vipande viwili vya muhogo, soseji pamoja na saladi nyingi ya mboga mboga. Kisha nikachukua chupa ya maji ya Dasani na bilauri ya sharubati ya parachichi.

Halafu nikaanza kuzitupa hatua zangu kwa utulivu nikitafuta sehemu nzuri ya kuketi mle ndani. Kwa kufanya vile nikaiona meza moja iliyokuwa imejitenga kwenye kona ya ukumbi ule na kuifuata halafu nikavuta kiti na kuketi. Sikuwa na muda wa kupoteza, nikaanza kujipatia mlo. Kwa kuwa nilikuwa na njaa sana niliufakamia ule mlo na muda mfupi baadaye nilikuwa nimemaliza.

Nikasubiri kidogo ule mlo ushuke vizuri tumboni kisha taratibu nikawa nashushia na ile sharubati na wakati ikishuka taratibu kooni mwangu akili yangu nayo ikaanza kuchangamka na kuanza kufikiria nini cha kufanya baada ya hapo. Nikiwa natafakari nikaanza kuwatazama watu waliokuwa wameketi katika meza zao wakiendelea kupata staftahi, kila mmoja alikuwa katika hali ya utulivu kama ambaye hakuwa na wasiwasi wowote duniani.

Katika uchunguzi wangu baadhi ya watu hawakunishawishi sana kuwatazama. Macho yangu yalihama haraka toka kwao hadi kwenye meza nyingine. Sikupata tabu kugundua baadhi yao walionekana kama si wafanyabiashara wakubwa basi viongozi na vigogo wa kiserikali. Pia wapo ambao kwa kuwatazama tu nilifahamu wazi kuwa ni mafisadi na wapiga dili wazuri na hapo walikuwa wanapanga harakati zao kwa sauti ya mnong’ono.

Kisha macho yangu yaliangukia kwenye meza moja iliyokuwa pembeni kabisa karibu na mlango wa kutokea, ambapo kulikuwa na mwanamke mmoja, peke yake kama yeye, alikuwa anakunywa sharubati ya pesheni taratibu bila haraka.

Alikuwa mrefu kiasi, si mnene wala mwembamba na alikuwa amevaa niqab, vazi la baibui lililomfunika mwili wote na kumbakisha macho tu na wakati akila alikuwa anapata tabu kufunua kitambaa chepesi kilichofunika uso wake ili kupitisha chakula kwenye mdomo. Miguuni alivaa soksi na sendoz nzuri za kike za ngozi halisi, mkononi alikuwa amevaa saa ghali ya kike na juu ya meza yake kulikuwa na simu aina ya Iphone 13 Promax na mkoba mzuri wa nguo ya pundamilia ambao bila shaka yoyote ulimgharimu fedha nyingi.

Pamoja na kuvaa mavazi yaliyomficha sura na umbo bado niliweza kubaini kuwa mwanamke huyo alikuwa mzuri wa sura na umbo la kuvutia ila hakuonekana kuwa na furaha, ni kama aliyekuwa anahofia jambo fulani. Pia nilitambua kuwa alikuwa mwanamke wa Kiarabu. Halafu… mbona kama tumewahi kukutana sehemu nyingine kabla ya hapa? Nilijiuliza huku nikimtazama vizuri. Tulikutana wapi na lini? Na tulikuwa tunafanya nini? Nikamtazama kwa umakini huku nikijaribu kuwaza. Nilikuwa na uhakika niliwahi kumwona sehemu, si tu kwamba nilimwona bali tulionana.

Kufikia hapo nikajikuta nikishindwa kabisa kuyaondosha macho yangu kutoka kwa yule mwanamke. Uvaaji wake wa ile niqab iliyofunika uso ulinifanya nipate maswali, nilijiuliza ya nini kupata tabu yote kwa kuvaa nguo kama ile wakati wa kula? Hata hivyo nikapatwa na hisia kuwa hakufanya hivyo kwa bahati mbaya bali alikusudia kuficha uso wake ili asitambulike kwa urahisi.

Asitambuliwe kwa urahisi na nani? Na kwa nini hakutaka kutambulika? Maswali mengine yalinijia na hapo hapo kengele ya hatari ikalia kichwani kwangu na kunifanya nihisi ubaridi wa aina yake ukinitambaa mwilini huku mapigo ya moyo wangu yakianza kwenda mbio isivyo kawaida! Nikabaki mdomo wazi nikimkodolea macho.

Nikamwona akiinamisha uso wake kutazama ndani ya bilauri yake ya sharubati kama aliyeona kitu, alitazama kwa kitambo kisha aliinua uso wake taratibu kwa madaha kana kwamba alikuwa anaigiza filamu na kutazama upande wangu, macho yetu yakakutana. Kwa takriban sekunde therathini macho yetu yalitulia yakitizamana kama ambao tulikuwa tukisomana fikra zetu.

Kisha aliyahamisha macho yake toka kwangu na kutazama kando. Muda huo huo simu yake ya mkononi ikaanza kuita. Yule mwanamke aliitazama kwa kitambo kama aliyekuwa akijishauri iwapo aipokee au aipotezee, kisha aliipokea na kuipeleka moja kwa moja sikioni. Alionekana kuwa mtulivu sana alipokuwa anaongea na simu, na muda wote alikuwa akinitupia jicho kwa namna ambayo sikuweza kufahamu haraka na baada ya mazungumzo ya takriban dakika mbili alikata simu yake na akaonekana kushusha pumzi.

Sasa alionekana kukosa zaidi furaha, akaitazama saa yake na kuinamisha uso wake chini, akawa anawaza. Nikiwa bado nimetulia kwenye kiti changu nilijifanya kutoona kilichokuwa kinaendelea kwa yule mwanamke mwenye niqab. Hisia zangu ziliniambia kuwa lilikuwepo jambo lisilo la kawaida, nikapanga nimfuate pale kwenye meza yake ili nijue nini kilikuwa kinamsumbua.

Kabla sijafanya hivyo nikamwona mwanamume mmoja mrefu akiisogelea meza yake na kuketi huku akinigeuzia mgongo. Sikuweza kumtambua mara moja lakini nilitambua kuwa alikuwa ana asili ya Kihabeshi au Kisomali, na niliamini kuwa alikuwa anacho kila kitu ambacho angeweza kukihitaji duniani kwani alionekana kunuka fedha kwa mavazi yake. Mkononi alikuwa ameshika funguo za gari akizungusha kwenye kidole chake cha shahada.

Alionekana kuongea na yule mwanamke mwenye vazi la niqab kwa muda mfupi, alikuwa kama vile akimpa maelekezo, na kisha akainuka na kuondoka haraka eneo lile akielekea kwenye mlango mwingine ambao nilihisi nao ulikuwa wa kutokea nje. Wakati anaondoka aligeuza shingo yake kunitazama, macho yetu yakakutana. Sikuweza kumtambua lakini nilijikuta nikiangaliana na macho ambayo sijapata kuyaona maishani mwangu. Yalikuwa kama ya nyoka aliyeghadhabika. Ni kama yanatoa cheche za moto.

“Duh!” niling’aka kwa mshangao. Sasa nilianza kupata hisia tofauti zilizoanza kuumbika kichwani mwangu, moyo wangu ulipiga kite kwa nguvu, hata hivyo niliendelea kutulia kwenye kiti changu.

Muda huo huo nikamwona yule mwanamke mwenye vazi la niqab akinyanyua mkono wake kuitazama saa yake ya mkononi na kisha akageuka na kutazama katika ule mlango aliopitia yule mwanamume mwenye macho ya nyoka.

Hakuendelea kukaa, akanyanyuka na kuanza kuondoka huku akionekana mwenye hofu fulani, alipofika mlangoni, kabla hajatokomea akageuka kunitazama. Macho yetu yakagongana. Nikamtambua.

Rahma! Oh my God!” nilijikuta nikimaka kwa mshituko mkubwa baada ya kumtambua Rahma wa Singida. Nikajikuta nikinyanyuka. Muda huo watu wengine nao walianza kutoka.

Niliamua kuelekea kule kule alikoelekea Rahma wa Singida lakini nikiwa na tahadhari kichwani kwangu. Nilipofika mlangoni sikutoka moja kwa moja, nilisimama kwa muda huku nikipima hali ya usalama, na baada ya kuhakikisha hali ilikuwa shwari nikatoka na kujikuta nimetokea kwenye ukumbi mpana uliokuwa unatokea eneo la mapokezi. Nikaangaza macho yangu huku na kule lakini sikuona dalili yoyote ya uwepo wa Rahma.

Mlango wa sita wa fahamu ukafungua na hisia zangu zikaniambia kuwa huenda alikuwa ametoka nje kabisa ya hoteli, nikatoka mbio na nikiwa sitaki kumpoteza na kujikuta nimetokea kwenye eneo pana la mbele la maegesho ya magari lililokuwa limepandwa miti mirefu ya kivuli iliyozungukwa na bustani ya maua ya kupendeza yenye hewa safi ya upepo wa asili baina ya sehemu moja ya maegesho ya magari na sehemu nyingine. Nikaangaza eneo lote lakini sikumwona.

Pale nje kulikuwa na magari kadhaa yaliyokuwa yameegeshwa. Nikaamua nielekee upande mwingine kwenye bustani ya nyasi laini zilizokatwa vizuri iliyokuwa na mabwawa makubwa ya kuogelea, sehemu zenye viti maalumu vya kupumzikia chini ya miti mizuri aina ya coconut palms pamoja na vibanda vidogo vya faragha, na sehemu za kupumzika zenye viti na meza chini ya miamvuli mikubwa yenye rangi za kupendeza.

Wakati nikitembea kuelekea huko nikaipapasa bastola yangu kiunoni na kuikuta imetulia mahala pake, mwili ukanisisimka na damu kuchemka. Sikuridhika, nikaichomoa na kuishika vizuri kwa uficho nikiwa tayari kwa lolote.

Mara nikamwona Rahma nje kabisa ya uzio wa Serena Beach Resort, ng’ambo ya pili ya Barabara ya Serena. Alikuwa anatembea haraka na alionekana mwenye wasiwasi mwingi. Sikutaka kupoteza muda, nikaanza kumfuatilia lakini nikiwa makini kumchunguza kila mtu niliyemwona kuona kama kulikuwa na mtego wowote niliotegewa. Nilikuwa najua namna ya kutembea na nilikuwa mwangalifu sana katika nyendo zangu.

Muda huo huo gari dogo aina ya Toyota Crown jeusi lenye vioo vyeusi visivyomwonesha mtu aliyemo ndani lilionekana likitoka kwenye viunga vya maegesho ya magari ya Serena Beach Resort na kuelekea barabarani nje ya uzio wa ile hoteli. Kengele ya hatari ikalia kichwani kwangu wakati lile gari likinikaribia, na hapo nikashuhudia kioo cha nyuma cha upande wangu kikishushwa haraka. Mwili ukanisisimka na kijasho chepesi kikanitoka mwilini.

Sikujiuliza mara mbili, kitendo cha kufumba na kufumbua tayari nilishajitupa chini na kubiringika kwenye maua yaliyopandwa baina ya sehemu moja ya maegesho ya magari na sehemu nyingine, na wakati huo huo nikausikia mvumo wa risasi kutoka kwenye bastola iliyofungwa kiwambo cha kuzuia sauti ukipita sentimita chache tu kutoka kwenye kichwa changu.

Pamoja na ujasiri wangu lakini niliogopeshwa sana na tukio lile lililotokea ndani ya sekunde mbili tu. Nikajificha nyuma ya moja ya miti mirefu ya kivuli iliyozungukwa na ile bustani ya maua huku nikisikia mivumo mingine miwili ya risasi ikipita karibu na ule mti niliokuwa nimejificha.

Kisha nikashuhudia lile gari likiongeza kasi na lilipofika hatua chache kutoka alipokuwa Rahma mlango wa nyuma ukafunguliwa na Rahma akaingia ndani ya gari, na hapo lile gari likaondoka kwa kasi. Lilikuwa ni tukio la haraka ambalo sikulitarajia kabisa. Mambo yote yalikuwa ya haraka sana na yalitokea ndani ya sekunde zisizozidi kumi!


Mambo yanazidi kupamba moto, endelea kufuatilia ili kujua mwisho wake...
Bio
 
Dah! Mambo ni mengi na muda mchache. Wacha nami nikahesabiwe...
 
Back
Top Bottom