Simulizi: Harakati za Jason Sizya

Simulizi: Harakati za Jason Sizya

taharuki..jpg

272

Kwa dakika kadhaa niliendelea kutulia pale dirishani huku nikiendelea kupiga picha za video kwa kila kilichokuwa kikiendelea pale chini ya lile jengo refu la Alpha Mall, na wakati huo huo nikichunguza kwa umakini kila kitu kwenye jengo lile kana kwamba niliambiwa kuna kitu kingetokea hapo!

Huku nikiendelea kupiga picha za video mara nikayaona magari mawili yakifika pale na kisha yakaegeshwa kando ya lile gari aina ya Toyota Prado TX la rangi ya fedha. Magari hayo yalikuwa ni gari dogo aina ya Toyota Vanguard la rangi nyeusi lililokuwa na namba za binafsi kutokana na utambulisho wa namba zake na Toyota Landcruiser GX V8 jeusi ambalo utambulisho wa namba zake ulionesha kuwa lilikuwa gari la Waziri wa Mambo ya Ndani.

Nikavutiwa zaidi kupiga picha za magari yale, na wakati nikiendelea kupiga picha nikashuhudia kwenye lile gari dogo aina ya Toyota Vanguard jeusi akishuka mwanamume mmoja ambaye ndiye alikuwa akiliendesha gari lile, alikuwa amevaa suti maridadi ya rangi ya kijivu na viatu vyeusi vya Ngozi. Kwa haraka tu niliweza kumtambua, alikuwa Octavian Lister, Ofisa Usalama wa Taifa ambaye alikuwa ni Katibu wa Waziri wa Mambo ya Ndani.

Nilikuwa nikimfahamu Octavian Lister japokuwa hatukuwa na ukaribu kivile, alikuwa mrefu na umri wake ulikuwa miaka 36, si mnene wala mwembamba lakini aliyeonekana kuwa mkakamavu na mwenye mikono imara iliyojengeka kwa misuli.

Katika lile gari aina ya Toyota Landcruiser GX V8 jeusi la Waziri wa Mambo ya Ndani, nilimshuhudia dereva wa Waziri, mtu mzima, mrefu na maji ya kunde aliyevaa suruali nyeusi ya kitambaa, shati la samawati la mikono mirefu, tai ya rangi ya bendera ya taifa na miwani myeusi ya jua, akishuka haraka kisha akaelekea kwenye mlango wa nyuma na kuufungua, na hapo akashuka mwanamama mmoja nadhifu sana na mrefu kiasi.

Mwanamama huyo alikuwa amevaa vazi zuri la kitambaa cha bazee lililoshonwa na kudariziwa vizuri kwa nyuzi za rangi ya dhahabu na kichwani alikuwa amevaa kilemba kikubwa kama wavaavyo wamama wa Kinaijeria. Nilimtambua vyema mama huyo kuwa ndiye Waziri wa Mambo ya Ndani, Bi Ummi Mrutu.

Mwanamama huyo alikuwa mnene wa wastani na mweupe kwa rangi ya ngozi yake. Hakuwa mwanamke wa kumtazama mara moja tu ukayaondoa macho yako kwake, kwani umbo lake lilisheheni vyema na kunesanesa huku likifanya kila jicho la mwanamume lililomwona kumtazama mara mbilimbili. Alikuwa na umri wa miaka 50 na watu wengi walijiuliza kuwa kama aliweza kuonekana bado mrembo katika umri ule, je, alikuwaje enzi za usichana wake?

Mbali na urembo, kikubwa zaidi kilichokamilisha haiba na mvuto pekee wa mama huyo ilikuwa ni machachari yake. Aliheshimika mno kwa uwezo wake mkubwa wa kusimamia operesheni dhidi ya ufisadi, uhujumu uchumi na nyingine kama hizo zikiwemo za kupambana na majambazi na wauza dawa za kulevya, na aliyafanya hayo akishirikiana na maofisa wa polisi makini wapambanaji kama Derick Mambo, Kamishna wa Taasisi ya kupambana na dawa za kulevya.

Mwanamama Ummi Mrutu alikuwa amefanikiwa mno endapo ungetaka kumlinganisha na mawaziri wa wizara hiyo waliokuwa wamemtangulia kwa kuwa alipenda kuwahamasisha maofisa waliokuwa chini yake kufanya kazi kwa bidii na kwa weledi, na alitoa ushauri bora kwa viongozi wa juu. Sifa hizo pamoja na nyingine nyingi ndizo zilizofanya akabidhiwe dhamana ya kusimamia wizara hiyo nyeti inayohusika na usalama wa ndani ya nchi, na ngumu kuliko wizara nyingi nchini.

Nikiwa bado napiga picha za video pale dirisha nikamwona Waziri Ummi Mrutu akiongozana na Katibu wake Octavian Lister, wakaingia ndani ya lile jengo la Alpha Mall. Mwanzoni nilidhani labda walikuwa wamefika pale kwa ajili ya manunuzi kwani ndani ya lile jengo kulikuwa na maduka mbalimbali kama duka la nguo maarufu la Kidoti boutique, duka kubwa la samani mbalimbali za ofisini na nyumbani na maduka ya bidhaa nyingine muhimu.

Kwa kumwona Waziri Ummi Mrutu pale shauku yangu ikazidi na kujikuta nikiachana na kupiga picha zilizohusu adha ya usafiri wa daladala katika kile kituo cha daladala cha Makumbusho na kujikuta nikivutiwa kupiga picha katika jengo lile la Alpha Mall, na sasa kamera yangu ilianza kupanda juu taratibu katika ghorofa za lile jengo na kutulia kwenye ghorofa ya kwanza ilipokuwepo supermarket kabla ya kuhamia kwenye vyumba vingine vya ofisi.

Madirisha mengi katika ghorofa ile ya kwanza yalikuwa yamefunikwa kwa mapazia mazito na hivyo vioo vyake viliakisi vizuri taswira ya vitu vya nje na kutomruhusu mtu yeyote kuona mle ndani kwa urahisi. Hata hivyo, katika ghorofa ya pili na ya tatu madirisha yake yalikuwa hayajafunikwa kwa mapazia na hivyo vioo vyake havikuwa vinaakisi kama ilivyokuwa kwa zile ghorofa zingine, na hivyo niliweza kuona kilichokuwa kikiendelea ndani ya vile vyumba.

Niliangalia vizuri katika ile ghorofa ya pili iliyokuwa na mgahawa wa kisasa lakini sikuona chochote cha maana kwani mbali na mgahawa huo kulikuwa na duka kubwa la samani za ofisini na nyumbani. Kamera yangu ikapanda juu zaidi hadi katika ghorofa ya tatu kulikokuwa na vyumba vya ofisi mbalimbali. Na hapo niliweza kuona vifaa vya ofisini kama meza na viti vyake, makabati ya kutunzia nyaraka, rafu za chuma, tarakilishi, mashine za kurudufu, printa pamoja na vitu vingine vidogo vidogo vya kiofisi.

Ndani ya vile vyumba vya ofisi niliweza kuwaona baadhi ya wafanyakazi wakiwa wanaendelea na shughuli zao. Wengine wakiwa wameinamia tarakilishi zao mezani na wengine wakipitia taarifa kwenye majalada ya ofisini. Kila mmoja alikuwa amezama kwenye hamsini zake na hakuna aliyekuwa akitazama pale dirishani ambapo nilikuwa nimesimama nikipiga picha, jambo ambalo lilinipa uhuru zaidi wa kuwapiga picha vizuri.

Wakati nikiendelea kupiga picha huku kamera yangu ikihama taratibu kutoka kwenye dirisha moja na kuhamia kwenye dirisha lingine katika ghorofa ile ya tatu hatimaye macho yangu yakaweka kituo kwenye chumba kimoja cha ofisi kilichokuwa kwenye kona ya kushoto ya ghorofa ile ya tatu ya lile jengo la Alpha Mall baada ya kuwaona watu watatu waliokuwa wameketi kwenye viti wakiwa wamezama kwenye mazungumzo ya kina.

Nilijikuta nikivutiwa mno na kile kilichokuwa kikiendelea humo ndani na kwa msaada wa lenzi kubwa ya kamera yangu yenye kuweza kuchukua vitu vilivyoko mbali, niliona vizuri ndani ya ile ofisi. Niliwatambua vyema wale watu watatu kwa kuwa pazia la dirisha la chumba kile cha ofisi lilikuwa limefunguliwa lote na kuachwa wazi. Watu hao walikuwa ni Waziri wa Mambo ya Ndani Bi Ummi Mrutu, Katibu wa Waziri Octavian Lister na mtu wa tatu alikuwa mpelelezi wa kujitegemea Daniel Kayera.

Huyu Daniel Kayera alikuwa amefungua kampuni binafsi ndani ya jengo lile la Alpha Mall, iliyohusika na upelelezi na iliitwa DanKay Private Detective Agent ili kutafuta ufumbuzi wa kesi tata zilizotingisha nchi zikionekana kuwayumbisha wanasheria na wapelelezi wa serikali. Kwa mfano kesi zilizohusu mauaji ya kutatanisha, ufisadi, uhujumu uchumi na dawa za kulevya.

Endelea...
 
taharuki..jpg

273

Kabla hajafungua kampuni binafsi Daniel Kayera alikuwa akilitumikia Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) akiwa katika Kikosi Namba 92 Ngerengere (92 KJ).

Daniel Kayera alikuwa mweusi na mrefu aliyekuwa amepanda hewani kisawa sawa akiwa na urefu wa futi sita na nusu na mwenye mwili ulioshiba. Akiwa na umri wa miaka 46 alikuwa na misuli imara ya mikononi iliyotuna kikamilifu vilimfanya aonekane kama bondia mkongwe. Alipenda sana kunyoa nywele zake mtindo wa bwenzi na uso wake ulikuwa mpana na uliotulia, huku miwani yake midogo ya macho ikiwa imeyahifadhi macho yake makubwa.

Nilimfahamu Daniel Kayera, alikuwa komando wa daraja la pili aliyekuwa amepata mafunzo maalumu ya mapigano ya ana kwa ana ya kiwango cha juu zaidi, namna ya kutumia karibia aina zote za silaha na milipuko ya jeshi, ufuatiliaji adui, kukabiliana na hali ngumu kwenye mazingira ya kawaida na nyikani, kumkwepa kumzuia na kumtoroka adui. Pia alikuwa msomi wa Shahada ya Sheria aliyoipata toka Chuo Kikuu cha Mzumbe.

Mafunzo ya ukomando yalimfanya kuwekwa katika kundi la maofisa wenye mbinu maalumu (specialized skills officers) na yalimsaidia sana katika kupata ufumbuzi wa maswali mengi yaliyowasumbua wataalamu na wakongwe wengine wa ujasusi si nchini tu bali katika Afrika Mashariki na ukanda wa SADC.

Nilivutiwa sana kuwatazama watu hao watatu yaani Waziri Ummi Mrutu, Daniel Kayera na Octavian Lister walioonekana kuwa katika kikao nyeti mno wakipanga mambo fulani ambayo kwa vyovyote yalikuwa na unyeti fulani.

Nilifahamiana na Daniel Kayera na alikuwa rafiki yangu urafiki ulioanza baada ya kutoka Mombasa hasa ilipotokea kazi fulani ya kiuchunguzi kufuatia kifo cha Ofisa Mashtaka wa Mkoa wa Morogoro (RPO), Dk Devota Komba ambaye alidaiwa kujinyonga kwa kamba ya manila chumbani kwake katika eneo la Forest Hill Mjini Morogoro. Sababu ya kujinyonga ilitajwa kuwa alikuwa akisumbuliwa na tatizo la msongo wa mawazo. Ni kazi hii iliyonifanya niwe na ukaribu na Daniel Kayera na hivyo kujikuta tukijenga urafiki.

Wakati akipatwa na umauti huo Dk Devota Komba alikuwa peke yake chumbani kwa kuwa mumewe Dk David Komba alikuwa amekufa takriban miaka miwili kabla, kwa ajali ya gari iliyotokea katika eneo la Gairo wakati akitokea Jijini Dodoma akirudi nyumbani Morogoro.

Hata habari kutoka ndani ya Ofisi ya Mashtaka Mkoa wa Morogoro zilibainisha kuwa wiki chache kabla ya kifo chake, Dk Devota Komba alionekana kuwa mkimya sana akiwa na tatizo ambalo hakupenda kuliweka wazi, wengi walidhani kuwa huenda alikuwa na tatizo la kisaikolojia ambalo ndilo lililomfanya kufikia hatua ya kujiua.

Tukio la kifo cha mama huyo liliniingiza kazini, nikiwa na miezi mitatu tu tangu nitoke jijini Mombasa na wakati huo damu yangu ikiwa bado inachemka sana huku hamu ya kuendelea kupata misukosuko ikiniingia, sikutaka kukubaliana kirahisi na hoja kuwa mama huyo alijiua kwa sababu ya msongo wa mawazo, na hivyo mshawasha wa kutafuta taarifa za kiuchunguzi kuhusiana na kifo hicho ukanipanda na kunifanya nikose usingizi kabisa.

Nilijikuta nikiwa na mzigo mzito sana ndani yangu wa kutaka kujua kilichokuwa nyuma ya pazia na kumwomba mkuu wangu wa kazi, Bi Tunu Michael aniruhusu kufanya uchunguzi wa kifo cha mama huyo ili kujua kilichokuwa nyuma ya pazia la kifo chake.

Ni katika sakata hilo nilipokutana na kaka wa marehemu, Edward Lutego ambaye nilimkuta katika ofisi za DanKay Private Detective Agent alipokwenda ili kumwajiri mpelelezi huyo wa kujitegemea afuatilie ukweli wa kifo cha dada yake, kwani alidai kuwa dada yao aliuawa na wabaya wake kwa sababu wiki chache kabla ya kifo chake alikuwa amewaambia kuwa alikuwa akipokea jumbe za vitisho kutoka kwa watu wasiojulikana.

Mimi na Daniel Kayera tuliingia kazini, yeye kama mpelelezi binafsi na mimi kama mwandishi wa habari za uchunguzi na kwa nyakati tofauti tulifuatilia ripoti za madaktari walioufanyia uchunguzi mwili wa Dk Devota Komba na kugundua kuwa, mama huyo alikuwa amekufa kwa kuishiwa pumzi na si kwa kukosa hewa kwa sababu ya kujinyonga.

Hata hivyo binafsi nilijikuta nikilishangazwa na hali hiyo kwa kuwa historia ya mama huyo haikuonesha kama alikuwa na tatizo la pumu, au kuwepo sehemu isiyokuwa na hewa, na hivyo ulikuwepo uwezekano kuwa alibanwa na mto usoni kwa mkandamizo mkubwa ili kumkosesha pumzi na hatimaye kufa.

Taarifa ya kitaalamu ilibainisha kuwa endapo mtu akibanwa na mto usoni na kwa mkandamizo mkubwa kwa zaidi ya dakika tano kutamfanya mtu huyo kuishiwa pumzi na kukosa hewa na hivyo huharibu ubongo na mfumo wake wa taarifa na kusababisha mfumo wa hewa kuharibika kabisa na mwishowe kupoteza uhai.

Pia taarifa ya kitaalamu kuhusu kifo cha mama huyo ilibainika kuwa pingili mbili za uti wa mgongo za shingoni kwa Dk Komba zinazounganika na fuvu la kichwa chake hazikuwa sawa, hii ilikuwa na maana kuwa kulikuwa na kujitetea wakati mama huyo akizibwa pua na mdomo na kwa kuwa mkandamizo ulikuwa mkubwa zaidi ilisababisha shingo yake kucheza, na ndiyo moja ya vitu vilivyoharakisha kifo chake.

Katika harakati za kuhakikisha haki inatendeka, nilifanya uchunguzi makini zaidi kama mwandishi wa habari za uchunguzi niliyekuwa nikiandaa habari ya ki-uchunguzi kuhusiana sakata hilo na hivyo nikawa napata vitisho vingi kutoka kwa watu fulani, nilibaini kuwepo mawasiliano ya simu za vitisho baada ya kutumia programu maalumu ya TraverMark kufuatilia mawasiliano ya mama huyo aliyofanya ndani ya kipindi cha miezi mitatu kabla ya kifo chake.

Kitu ambacho huenda hawakukijua au walijisahau ni kwamba unapotuma ujumbe wako kwenye simu, nakala ya ujumbe huo hubakia katika hifadhi kwenye setelaiti kwa muda mrefu. Kumbukumbu ya simu iliyopigwa huweza kuhifadhiwa kwa kati ya miezi sita hadi miaka mitano kabla ya kuteketezwa. Hivyo, mtu yeyote mwenye nyenzo na utaalamu kama mimi akichimba katika msitu huo wa ‘meseji’ hupata kile anachokitafuta.

Haikuchukua muda ukweli ukabainika na watu wote waliofanya unyama huo, bila kujali nafasi zao katika jamii, walikamatwa na sheria ikachukua mkondo wake. Hadi kesi inakamilika, Daniel Kayera aliyekuwa amesimama kama mpelelezi binafsi aliyeajiriwa na familia ya marehemu alikuwa ametoa mchango mkubwa sana katika upatikanaji wa haki.

_____



Kumbukumbu za namna nilivyofahamiana na Daniel Kayera zilipita haraka kwenye kichwa changu, nikashusha pumzi na kuendelea kuwapiga picha watu wale watatu huku nikihisi kuwa kulikuwepo na jambo nyeti sana lililokuwa limemleta Waziri Ummi Mrutu kwenye ofisi za DanKay Private Detective Agent. Nilihisi huenda lilikuwa likihusiana na kifo cha kijana wake wa pekee, Fikiri Mrutu, ambaye alikufa kifo cha kutatanisha takriban wiki tatu zilizokuwa zimepita.

Kitu pekee nilichokikosa hapo na ambacho kiliniumiza mno akili yangu katika kutaka kujua kikao kile ndani ya ofisi ya DanKay Private Detective Agent kilihusu nini ni kushindwa kuzipata sauti zao japo niliweza kuwaona na kuzipata vizuri sura zao kwa kutumia kamera yangu.

Wakati macho yangu yakiwa bado yameweka kituo kuwatazama kwa umakini wale watu watatu ndani ya ofisi ya DanKay Private Detective Agent, taratibu fikra zangu zikazidi kuzama kwenye tafakuri ya kina nikijiuliza Waziri wa Mambo ya Ndani angekuwa akijadiliana nini na mpelelezi yule wa kujitegemea? Hii haikuwa mara ya kwanza kumwona pale Waziri Ummi Mrutu, ilikuwa ni mara ya pili ndani ya kipindi cha wiki mbili, ingawa mara ya kwanza sikushikwa na mshawasa wa kutaka kujua ni kipi kilichomleta pale.

Endelea...
 
taharuki..jpg

274

Sasa kichwa kilianza kuniuma na hali ya udadisi wa kutamani sana kujua kilichokuwa kikijadiliwa ndani ya ofisi ile ukanishika. Hata hivyo, nilihisi tu kuwa madhumuni ya kikao hicho hayakuwa mengine zaidi ya kutafuta taarifa fulani za kipelelezi au kupeana mikakati ya taarifa za kuhusu mambo fulani ambayo sikuyajua na nilitamani sana kuyajua. Niliendelea kuwaza, nikihisi kuwa pengine Waziri Ummi Mrutu alikuja kumpa kazi mpelelezi huyo wa kujitegemea ili aishughulikie!

Kwa kuwaza jambo hilo nikajikuta nikianza kupata maswali mengi kichwani kwangu, nilijiuliza ikiwa Waziri wa Mambo ya Ndani aliyekuwa akisifika kwa kufanya kazi kwa bidii na kwa weledi mkubwa kiasi cha kupewa dhamana ya kusimamia wizara hiyo nyeti iliyohusika na usalama wa ndani ya nchi, alikuja pale kwenye ofisi za DanKay Private Detective Agent kuongea na mpelelezi wa kujitegemea ili amfanyie kazi, hii ilikuwa na maana kuwa hakuwaamini Polisi aliokuwa akiwaongoza?

Hata hivyo, sikufika mbali kwenye maswali yaliyoanza kunijia kichwani kwangu kuhusu ujio wa Waziri Ummi Mrutu ndani ya ofisi za DanKay Private Detective Agent kwani mara moja mawazo yangu yalihamishwa haraka na tukio la pikipiki moja ya magurudumu matatu aina ya WANHOO ya rangi ya chanikiwiti iliyofika katika jengo lile la Alpha Mall.

Pikipiki hiyo ilikuwa ikiendeshwa na mwanamume mmoja mrefu mweupe kiasi mwenye ndevu nyingi aliyekuwa amevaa ovaroli la rangi ya samawati, kofia ya pama ya rangi ya samawati aliyoishusha hadi usawa wa macho ili kuficha paji la uso wake, miwani mikubwa myeusi iliyoyafunika macho yake na buti ngumu miguuni aina ya ‘safari boot’ za rangi ya hudhurungi.

Alikuwa mrefu niliyemkadiria kuwa na futi sita na ushee, mwenye mwili wa kimazoezi na mikono yenye misuli imara ya mikononi iliyotuna kikamilifu. Licha ya kofia ya pama alivyoivaa kwa mtindo wa kuficha paji la uso wake na miwani myeusi iliyofunika macho, lakini kwa mtu makini kama mimi asingeshindwa kutambua kuwa alikuwa na sura ndefu na macho yaliyoingia ndani.

Nilipomwona tu nikahisi kuwa ule uvaaji wa kofia wa kufunika sehemu ya juu ya uso wake na miwani yake mikubwa myeusi ilikuwa ni namna fulani ya kuficha sura yake ili asitambulike. Nilimwangalia kwa umakini mkubwa na kujikuta nikivutiwa zaidi.

Niliendelea kumpiga picha kwa kila kitu alichokuwa akikifanya pale chini ya jengo la Alpha Mall. Kilichonivutia zaidi ni kitendo cha mtu huyo kuonekana kubishana na mlinzi wa lile jengo la Alpha Mall, ilionekana kuwa alikuwa akilazimisha kuiegesha pikipiki yake kwenye nafasi finyu iliyokuwa katikati ya magari mawili, Toyota Landcruiser GX V8 jeusi la Waziri Ummi Mrutu na Toyota Prado TX la rangi ya fedha la mpelelezi Daniel Kayera, licha ya uwepo wa nafasi kubwa iliyokuwa wazi upande mwingine wa lile jengo!

Kisha mwanamume mwingine mtu mzima, mrefu na maji ya kunde aliyevaa suruali nyeusi ya kitambaa, shati la samawati la mikono mirefu, tai ya rangi ya bendera ya taifa, miwani myeusi ya jua na viatu vya ngozi vya gharama miguuni akatokea na kumkabili yule mwanamume aliyefika hapo na pikipiki ya magurudumu matatu. Mara moja nilimtambua yule mtu mzima mwenye shati la samawati la mikono mirefu kuwa alikuwa ni dereva wa Waziri Ummi Mrutu.

Walionekana kubishana kidogo. Nilianza kupatwa na hisia mbaya na hapo milango yangu ya fahamu ilifunguka zaidi na kunifanya kuwa makini zaidi huku nikijaribu kuishirikisha akili yangu kikamilifu katika kunitafsiria kile kilichokuwa kikiendelea pale kwenye jengo la Alpha Mall. Kwa mabishano yale nilianza kuhisi kuwepo kwa jambo lisilo la kawaida.

Kwa kutumia lenzi ya kamera yangu yenye uwezo wa kuchukua picha zilizo mbali sana na kuzisogeza karibu, nilimvuta zaidi yule mtu mrefu mwenye ovaroli na kumjaza kwenye kioo cha kamera yangu ili niweze kubaini nia yake. Kwa kufanya vile nikajikuta nikivutiwa zaidi na kile kilichokuwa nyuma ya pikipiki yake ya magurudumu matatu, sehemu ambayo kwa kawaida huwa na tera dogo la kubebea mizigo lakini nilichokiona ni kuwa kulikuwa kumetengenezwa kitu mfano wa tangi dongo la mafuta ambalo lilikuwa na ukubwa sawa na ule wa tera. Lile tangi lilikuwa limechomelewa kwa ufundi mkubwa.

Mara tu baada ya kulazimisha na kufanikiwa kuiegesha ile pikipiki ya magurudumu matatu katikati ya yale magari mawili yule mwanamume mrefu mwenye ovaroli alishuka haraka na kuinua mkono wake wa kushoto kutazama saa yake kabla hajaanza kuvuka barabara kwa mwendo wa haraka akielekea upande wa kituo cha daladala cha Makumbusho huku akionekana kuwasiliana na mtu mwingine kupitia kifaa fulani cha mawasiliano kilichokuwa kimepachikwa kwenye sikio lake la kushoto.

Nilimwona dereva wa Waziri wa Mambo ya Ndani na mlinzi wa jengo la Alpha Mall wakibaki wanamsindikiza yule mwanamume kwa macho ya mshangao, wakiwa hawana cha kufanya, wakati akiondoka haraka toka eneo lile. Muda wote yule mwanamume alionekana kuwa na wasiwasi mkubwa na alikuwa akizungusha macho yake kuangalia huku na kule.

Mlango wangu wa sita wa fahamu ulifunguka na kengele ya tahadhari ikalia kichwani kwangu na kunifanya nianze kuhisi jasho jepesi likianza kunitoka mwilini mwangu huku mapigo ya moyo wangu yakienda mbio isivyo kawaida. Bila kupoteza muda, nami niliinua mkono wangu wa kushoto kuitazama saa yangu ya mkononi. Mishale ya saa hiyo ilinionesha kuwa ilikuwa imetimia saa 11:05 jioni.

Kutazama saa ni mojawapo ya mambo muhimu anayopaswa kufanya ofisa usalama wa taifa au mtu aliyebobea kwenye kutafuta taarifa za kiuchunguzi anapokuwa kazini, inasaidia kujua na kutunza muda sahihi wa kila tukio linalotokea. Kufanya hivyo husaidia sana katika uchunguzi utakaofanywa baadaye hususan katika kuunganisha nukta, kujumlisha moja na moja ili kupata mbili, kupunguza idadi ya watuhumiwa, na hata kutambua sababu na lengo lililosababisha tukio husika kutokea au kufanywa katika muda huo.

Japokuwa watu wengi walionifahamu walijua nilikuwa mwandishi wa habari za uchunguzi lakini bado ule ‘u-Jason Sizya’ katika fikra zangu uliendelea kuwepo na ndiyo ulionifanya nisimame pale dirishani muda wote na kwa kupitia kioo cha dirisha lile nikawa nafuatilia kwa umakini sana nikimsoma kila mtu aliyekuwepo mahali hapo na kila kilichokuwa kikiendelea hapo.

Nikiwa bado natakafari tukio la mwanamume yule mwenye pikipiki ya magurudumu matatu kulazimisha kuegesha pikipiki yake katikati ya magari mawili huku kamera yangu ikiendelea kupiga picha za video za kila tukio lililokuwa likiendelea pale, mara nikaiona pikipiki moja aina ya Boxer BM 150 ya rangi nyekundu ikitokea upande wa kituo cha daladala cha Makumbusho ikiwa katika mwendo wa kasi na kuelekea kule alikokuwa akitokea yule mwanamume aliyekuja na pikipiki ya magurudumu matatu na ilipomkaribia ikapunguza mwendo kidogo.

Pikipiki ile ilikuwa ikiendeshwa na mwanamume mmoja mfupi, maji ya kunde ambaye pia alikuwa ana ndevu nyingi na alivaa ovaroli la rangi ya samawati, kofia ya pama ya rangi ya samawati aliyoishusha hadi usawa wa macho, miwani mikubwa myeusi iliyoyafunika macho yake na buti ngumu miguuni aina ya ‘safari boot’ za rangi hudhurungi.

Baada tu ya ile pikipiki aina ya Boxer BM 150 kupunguza kidogo mwendo huku ikimpita yule mwanamume aliyekuja na pikipiki ya magurudumu matatu, nikamwona akirukia nyuma ya ile pikipiki kwa namna ambayo ilinionesha kuwa alikuwa mtu wa mazoezi na kufikia kwenye kiti cha nyuma na muda huo huo ile pikipiki aina ya Boxer BM 150 ikaongeza mwendo na kutokomea mtaani kwa mwendo wa kasi ikielekea uelekeo wa Kijitonyama.

Endelea...
 
taharuki..jpg

275

Sikustaajabu sana kwa jinsi yule mwanamume alivyoweza kurukia juu ya pikipiki iliyokuwa katika mwendo bali akili yangu ilianza kusumbuka katika namna ya kutaka kufahamu kuhusu ile pikipiki ya magurumumu matatu iliyoachwa pale kwenye lile jengo la Alpha Mall.

Je, ilikuwa imebeba nini? Kwa nini yule mwanamume aliyekuja nayo alikuwa ameficha sura yake kwa kofia na miwani? Kwa nini alilazimisha kuiacha pikipiki yake katikati ya magari ya Waziri Ummi Mrutu na mpelelezi Daniel Kayera huku akionekana kuwa na wasiwasi na kisha akaondoka haraka? Kwa nini yule yule mwanamume mwingine mfupi aliyekuwa anaendesha pikipiki aina ya Boxer BM 150 naye alificha sura yake? Je, ni kweli walikuwa na ndevu nyingi au zilikuwa za bandia? Maswali hayo yalinifanya nihisi kukaukiwa ghafla na mate mdomoni na vinyweleo mwilini kwangu vikasisimka kwa hofu.

Hata hivyo, nilianza kujipa moyo kuwa hakukuwa na jambo lolote baya ambalo lingetokea bali zilikuwa hisia zangu tu za ‘U-Jason Sizya’. Lakini nilijiapiza kuwa endapo lingetokea jambo baya basi nilikuwa na ushaidi wote niliourekodi kwenye kamera yangu ukimwonesha yule mwanamume mrefu mweupe kiasi aliyevaa ovaroli la rangi ya samawati, kofia ya pama na miwani myeusi tangu akifika pale kwenye jengo la Alpha Mall akiwa na pikipiki yake ya magurudumu matatu, akalazimisha kuipachika katikati ya magari mawili japo kulikuwa na sehemu ya wazi kabisa upande mwingine na hadi alivyoondoka kwa kutumia pikipiki aina ya Boxer BM 150.

Wakati nikiendelea kujiuliza mara ghafla nilijikuta nikinyanyuliwa juu na kutupwa sakafuni kama mzigo huku nikishuhudia mlipuko mkubwa mno uliokuwa haufanani kabisa na kishindo cha kupasuka kwa tairi la gari, bunduki au muungurumo wa radi. Ule ulikuwa ni mshindo mkubwa na mzito kama muungurumo wa Rocket Propelled Grenade (RPG), silaha inayotumiwa na wanajeshi vitani kulipua vifaru vya adui.

Akili yangu iliyoonekana kushindwa kufanya kazi kwa kitambo kifupi na iliporudi katika hali yake ya kawaida nikawa kama mtu aliyezinduka, na bila kupoteza muda, niliinua tena mkono wangu wa kushoto kuitazama saa yangu ya mkononi. Mishale ya saa hiyo ilinionesha kuwa ilikuwa imeshatimia saa 11:10 jioni. Dakika tano tu tangu yule mwanamume aliyekuja hapo na pikipiki ya magurudumu matatu aitelekeze na kuondoka.

Huku nikiendelea kutafakari kuhusu mshindo ule, niliinuka haraka toka pale sakafuni nilipokuwa nimetupwa na kuzungusha macho yangu kutazama haraka haraka huku na kule, nikagundua kuwa lile jengo la ghorofa zaidi ya kumi la Alpha Mall lilikuwa limeporomoka na kubakia kama pagale lililotelekezwa. Muda huo hali ya mahala pale ilikuwa ya taharuki kubwa.

Ukubwa wa mshindo ule uliambatana na mtikisiko mkubwa wa majengo yote yaliyokuwa katika eneo lote lililo ndani ya mita 200 za mraba kutoka eneo la tukio na kuyaharibu huku ukiporomosha sehemu kubwa ya lile jengo la Alpha Mall.

Ukuta wote wa upande ule wa Mashariki wa lile jengo la Alpha Mall yalipokuwa yameegeshwa yale magari, sehemu ambayo pia ndiko kulikuwa na kikao Kizito kikiendelea ndani ya ofisi za DanKay Private Detective Agent kati ya mpelelezi wa kujitegemea Daniel Kayera na Waziri wa Mambo ya Ndani Bi Ummi Mrutu ulikuwa umeshuka wote na kulifanya jengo zima la Alpha Mall.

Chini ya lile jengo kwenye maegesho ya magari, yale magari yaliyokuwepo pamoja na ile pikipiki ya magurudumu matatu yalikuwa yameteketea kabisa na kubakia kama chuma chakavu na eneo lote palizagaa vipande vya vyuma, makaratasi na makorokoro mengine yalivyojaa vumbi jeusi.

Pia lile jengo la Makumbusho Plaza ambamo kulikuwa na ofisi zangu za Capital Media Inc. lilikuwa limepata uharibifu kidogo. Kioo cha upande mmoja cha dirisha la ofisini kwangu kilivunjika na kusambaa kila mahali huku meza ya kioo iliyokuwa na vitabu, nakala chache za magazeti ya siku za karibuni na majarida machache juu yake yaliyopangwa kwa ustadi ilikuwa imevunjika baada ya kuiangukia, na majarida hayo kusambaa kila mahali.

Magari yaliyokuwa yameegeshwa jirani na jengo ambalo zilikuwemo ofisi zangu la Makumbusho Plaza pia yalivunjwa vioo na kubondwa vibaya na vyuma. Sasa anga lote lilikuwa limefunikwa na rangi nyekundu iliyochanganyika na moshi mweusi, watu walipatwa na mshtuko mkubwa uliowafanya kwanza wasijue nini cha kufanya, kisha kama waliopandwa na wazimu walianza kutawanyika ovyo ili kunusuru roho zao.

Walitawanyika kuelekea huku na kule na mayowe ya hofu yakisikika kila upande, na wengine walionekana kutokea katika madirisha ya daladala walizokuwa wamepanda baada ya kuzisubiria kwa muda mrefu, ilimradi tu kila mmoja alijaribu kuokoa nafsi yake. Vilio vilisikika kila upande na watu waliumia sana huku wengine wakipoteza fahamu au kufa kabisa.

Daladala tatu zilizokuwa zikipita usawa wa lile jengo la Alpha Mall lililolipuliwa na bomu zilidaka moto huku zikibondeka vibaya kutokana na vipande vya hilo bomu kuruka na kisha zikaanza kuteketea kwa moto. Kwa tathmini ya haraka haraka magari mengi yalikuwa yameathirika. Kwa ujumla eneo lote lilionekana kama uwanja wa vita na hali ile ilikuwa imeleta mshituko mkubwa sana kwa kila mtu.

Oh my God!” niling’aka kwa mshtuko mkubwa kisha nilivuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu. Macho yangu yalikuwa yakitazama zile pilika pilika za watu zilizokuwa zikiendela kule chini kwa namna ya kupepesa macho kiufundi nikijaribu kubaini endapo ningeweza kuona jambo lolote lisiloeleweka.

Na hapo niliweza kugundua kuwa kumbe ni ile pikipiki ya magurudumu matatu ndiyo iliyokuwa imesababisha mlipuko ule kwa kuwa ilibeba bomu lililolipuka na kuathiri vibaya lile jengo la Alpha Mall na vilivyokuja kule kwenye majengo mengine likiwemo jengo letu la Makumbusho Plaza, ni vipande vya hilo bomu!

Pikipiki ile ya magurudumu matatu ilikuwa imerushwa juu na kuangukia katikati ya barabara ya mtaa huo ambao daladala zilikuwa zikipita kutoka kituo cha daladala cha Makumbusho ili kwenda kutokea kwenye Barabara ya Bagamoyo, na hivyo kusababisha moto mkubwa kwenye magari mengine.

Nilishusha tena pumzi, safari hii zilikuwa pumzi za ndani kwa ndani kisha nikaanza kuitafuta kamera yangu iliyoniponyoka wakati nilipopiga mwereka na kuangushwa sakafuni kutokana na ule mshindo mkubwa wa bomu. Katika kuitafuta niligundua kuwa ilikuwa imeanguka mita chache kutoka eneo nililokuwa nimesimama. Nikaifuata lakini nilipokuwa katika kuinama ili niiokote mlango wa ofisi yangu ukapigwa kumbo na kufunguka, nikashtuka sana na kuruka kando huku nikiichomoa haraka bastola yangu ndogo aina ya Glock 19M ambayo hutumiwa na wapelelezi wa Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI) toka kiunoni.

Kisha niliikoki na kuiruhusu risasi moja ichepuke toka kwenye magazine na kuingia kwenye chemba na wakati huo huo kidole changu cha shahada kilikuwa kimeshaifikia trigger tayari kufyatua risasi ikibidi. Nikiwa makini kutazama ni nani aliyepiga kumbo mlango wa ofisi yangu macho yangu yakatua kwa mwanadada mrembo Winifrida Kilomoni ambaye tulizoea kumwita Winnie, alikuwa mtaalamu wa kuandaa kurasa na picha (graphic designer) wa kampuni yangu.

Winnie alikuwa kwenye chumba cha uzalishaji cha ofisi zetu za Capital Media Inc. na aliingia mle ofisini kwangu, kwenye ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji haraka huku akiwa na uso uliojawa na wasiwasi mkubwa ingawa kwa kawaida alikuwa msichana mchangamfu sana na mtu makini sana kuliko hata simba jike.

Endelea...
 
taharuki..jpg

276

Alikuwa na umri wa miaka 26, mrefu wa wastani na mweupe kwa rangi ya ngozi mwenye umbo lililovutia mno. Alikuwa na mashavu mfano wa chungwa, nywele nyingi nyeusi fii na siku hiyo alikuwa amevaa gauni zuri la kitenge la mikono mirefu lililoshonwa kwa mtindo wa ‘Ankara midi tube’ likiishia juu kidogo ya magoti yake huku likiushika vyema mwili wake wenye umbo refu. Miguuni alikuwa amevaa viatu vyeusi vyenye vikanyagio virefu vya mchuchumio.

Aliponiona nikiwa nimeshika bastola na kidole changu kimoja kikiwa kwenye trigger huku nikiielekeza bastola hiyo kwake, alishikwa na butwaa! Ulikuwa ni mshangao zaidi ya woga!

Kwa kawaida mimi na Winnie tulikuwa watu tuliokuwa karibu mno kiasi cha rafiki zangu na hata wafanyakazi wangu wengine kudhani kuwa tulikuwa wapenzi, wengi waliamini kwamba nilikuwa nimeshabanjuka naye kimapenzi, japokuwa hali haikuwa hivyo kwa upande wetu. Hata hivyo, yeyote ambaye ungemwuliza asingebisha kuwa kulikuwa na hisia za mapenzi baina yetu, Winnie mwenyewe alilifahamu hili lakini kilichokuwa kikinishangaza sana ni kwamba sikuwa kabisa na ujasiri wa kumweleza bayana hisia zangu.

Hata nilipotambua kuwa ni Winnie aliyeingia ofisini kwangu bado nilibaki nikiwa nimeishika bastola huku nikimwangalia kwa macho makali kana kwamba niliambiwa kuwa yeye alikuwa na uhusiano na yule mwanamume aliyelipua jengo la Alpha Mall.

“Ni mimi jamani… vipi mbona hivyo?” Winnie aliniuliza kwa mshangao uliochanganyika na wasiwasi huku akiitazama bastola yangu.

“Unakwenda wapi?” nilimuuliza Winnie kwa ukali huku nikiendelea kumwelekezea bastola. Hata hivyo, kabla Winnie hajajibu nikaongeza, “Kwani huoni kuwa hali ni ya kutisha sana eneo hili!”

Maneno hayo niliyasema huku nikimtazama Winnie kwa mshangao uliochanganyika na wasiwasi kwani kwa hali ile iliyokuwa imetokea muda mfupi uliokuwa umepita nisingetegemea kumwona yeyote, achilia mbali mtoto wa kike kama Winnie, akijitokeza eneo lile bila wasiwasi wowote pasipo kujua mashambulizi yale yalitoka wapi!

Nilikuwa makini mno nikikumbuka katika mafunzo ya ujasusi tulifundishwa na kukumbushwa kila wakati suala la kutomwamini mtu yeyote anayejitokeza ghafla baada ya mashambulizi makubwa kama yale maana huwezi kujua adui atamtumia nani kuipenya ngome yenu.

Hata hivyo, badala ya kuogopa Winnie alishusha pumzi za ndani kwa ndani huku akiminya midomo yake yenye maki na kufanya visimo vidogo vijitokeze kwenye mashavu yake huku akiendelea kuniangalia kwa mshangao.

“Nilikuwa na wasiwasi na wewe, boss,” Winnie alijibu huku akiwa bado ana sura ya mshangao.

“Unawezaje kuja huku wakati hali ni ya hatari namna hii? Au huoni kama eneo hili limeshambuliwa kwa mabomu? Kwanza akina Evans wako wapi?” nilimuuliza Winnie maswali mfululizo huku nikiirudisha bastola yangu kiunoni.

“Kwani umesahau kuwa saa hizi tumebaki wawili tu mimi na wewe! Salma alikuomba ruhusa anauguliwa na mama yake, Evans yupo Dodoma na akina Mariam na Radhia wameshaondoka saa hizi!” Winnie aliniambia huku akiwa bado ananitazama kwa mshangao lakini macho yake yakizidisha udadisi. Nikajikuta nikianza kuwa na wasiwasi na binti huyu.

Kisha nilimwona Winnie akizungusha macho yake kutazama huku na kule, na mara macho yake yakatua kwenye lile jengo la ghorofa la Alpha Mall ambalo sasa lilikuwa limeporomoka na kubakia kama gofu lililotelekezwa kwa miaka mingi. Na hapo sura yake ikapambwa na mshangao mkubwa. Nilimsikia akiachia mguno huku akiikunja sura yake na kutengeneza matuta madogo usoni kisha akashusha pumzi za ndani kwa ndani.

Nikakumbuka na kugeuza shingo yangu kutazama tena kule kwenye lile jengo la Alpha Mall huku picha ya yule mwanamume mrefu aliyevaa ovaroli la rangi ya samawati, kofia ya pama ya rangi ya samawati aliyoishusha hadi usawa wa macho, miwani mikubwa myeusi iliyoyafunika macho yake na buti ngumu miguuni za rangi ya hudhurungi ikinijia tena akilini kwangu.

Sasa nilitamani niondoke nikamsake kokote aliko nimkamate yeye na yule mwenzake mfupi mwenye pikipiki aina ya Boxer BM 150 ya rangi nyekundu aliyeondoka naye. Niliamini kabisa kuwa wale watu wawili walikuwa wanahusika na tukio lile la kigaidi. Na kama ningewatia mikononi basi ningewafinyanga kwa mikono yangu kwa kusababisha yale maafa makubwa. Nilijikuta nikikosa kabisa neno la kusema juu ya tukio hilo zaidi ya kutoa laana ya kimoyo moyo kuwalaani watu wale na vizazi vyao vyote.

Jambo hilo lilinifanya niikumbuke tena kamera yangu ambayo kabla sijaiokota Winnie akaingia mle ofisini. Niliinama nikaiokota na nilipoitazama vizuri nikagundua kuwa lenzi ya kamera ilikuwa imevunjika na sehemu ndogo ya kioo cha kamera kinachotumika kuangalia picha (LCD) wakati wa kurekodi pia palikuwa pameweka alama ya mpasuko.

Nilishusha pumzi za ndani kwa ndani na kusonya kwa hasira, kisha nilifungua kifuniko chake na kutoa kadi ya kutunzia picha zilizopigwa (memory card) kisha nikaiweka kwenye mfuko wa suruali yangu huku nikijikuta nikiropoka, “Hawana ujanja, watakamatika tu.”

Jambo hilo lilimfanya Winnie anitazame kwa udadisi zaidi na kisha alinitupia swali huku akiendelea kunitazama kwa udadisi. “Kina nani hao, boss?”

Nilijishtukia, nikamtazama Winnie na kuachia tabasamu la kumzuga, na hapo nikataka kusema neno lakini nikasita na wakati huo huo tukasikia sauti za ving’ora vya magari ya zimamoto, magari ya wagonjwa na yale ya polisi vikisogea kwa kasi kuelekea katika eneo lile la tukio (ground zero). Niligeuza shingo yangu kutazama upande ule zilikosikika sauti za ving’ora nikayaona magari mawili ya zimamoto, moja la wagonjwa na mengine mawili ya polisi kutoka Kituo cha Polisi cha Oysterbay.

Sikutaka kuzubaa, haraka nikafungua kabati la chuma lililokuwa pembeni kabisa ya ile ofisi yangu na kuiweka ile kamera aina ya Lumix SFX-20 kisha nikatoa kamera nyingine aina ya Canon EOS R, halafu nikachukua notebook pamoja na kalamu.

“Usitoke, ngoja mimi niende kwenye eneo la tukio kuona nini kinaendelea,” nilimwambia Winnie huku nikianza kutembea haraka kuelekea kwenye mlango wa kutokea. Mkononi nilikuwa nimebeba ile kamera.

“Boss, una uhakika utakuwa salama?” Winnie aliniuliza huku akiwa ananitazama kwa wasiwasi.

“Usijali! Kazi za hatari ndizo ninazozipenda, wewe endelea tu kuniombea,” nimlijibu na bila kusubiri kauli yake nilitoka kisha nikaufunga mlango nyuma yangu na kuanza kutimua mbio kuelekea kwenye ngazi za jengo halafu nikashuka na kuendelea kutimua mbio kuelekea kwenye eneo la tukio.

Ilinichukua dakika moja na nusu tu kutoka ofisini kwangu hadi kwenye jengo lile la Alpha Mall ambalo sasa lilikuwa limebakia gofu. Hapo niliwakuta maofisa wa usalama kadhaa, wanajeshi waliokuwa wamevaa mavazi ya kivita (combat gear) na kubeba bunduki za kivita aina ya Sub Machine Gun, na askari wa kikosi cha kutuliza ghasia (FFU) nao wakiwa wamebebelea bunduki aina ya Sub Machine Gun na vifua vyao vikiwa vimekingwa na mavazi maalumu yanayozuia risasi (bullet proof). Askari hao walikuwa na sura za kazi wakiwa tayari kwa mapambano.

Endelea...
 
taharuki..jpg

277

Baadhi ya askari walianza kuzungusha utepe maalumu wa njano maarufu kama ‘Barricade tape’ wenye maandishi ya “Police Line Do Not Cross” ukizuia watu kuvuka eneo lile la tukio, na pia kulikuwa na askari wa usalama barabarani waliokuwa wakiifunga Barabara ya Bagamoyo kuanzia eneo la Victoria mpaka Sayansi ili kuruhusu shughuli za uokoaji zifanyike bila bughudha. Magari pekee yaliyoruhusiwa kupita eneo lile ni yale ya Kikosi cha Zimamoto na Uokoaji, magari ya wagonjwa na ya watu wa usalama.

Moto mkubwa ulikuwa ukiwaka upande ule wa Mashariki ya jengo la Alpha Mall ambako yale magari matatu na ile pikipi ya magurudumu matatu yalikuwa yakiendelea kuteketea. Muda huo kazi ya kuuzima moto ilikuwa ikifanyika. Wafanyakazi wa kikosi cha zimamoto na uokoaji wakiwa na magari mawili makubwa walikuwa wakijitahidi kwa nguvu zote kuukabili moto huo bila mafanikio.

“Unaelekea wapi, si unaona eneo limefungwa na hakuna mtu anayeruhusiwa kupita eneo hili!” askari mmoja aliyeshika bunduki ya kivita aina ya Sub Machine Gun na kifuani akiwa amevaa vazi maalumu linalozuia risasi aliniuliza kwa ukali huku akinikazia macho yake kwa makini baada ya kuniona nikitembea kwa kasi kumfuata.

Alipoona bado nazidi kumfuata akaishika vizuri bunduki yake na kuuelekezea mtutu wa bunduki kifuani kwangu. Sikushtuka kwani nilikuwa nakitegemea kitu kama hicho kutokea. Nilikuwa nimepitia mafunzo ya kijeshi nilipojiunga na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kwa mujibu wa sheria baada ya kumaliza kidato cha sita, kisha nikapitia tena mafunzo ya kijeshi wakati nikichukua mafunzo ya ujasusi na baadaye kushiriki katika mapambano dhidi ya ugaidi jijini Mombasa.

Kwa hali hiyo niliweza kuhisi hatua anazoweza kuchukua mpiganaji katika hali ya hatari kama ilivyokuwapo muda huo, hivyo nilikuwa nimejiandaa ki-mwili na kisaikolojia. Huku moyo wangu ukizidisha mapigo yake na kwenda kasi, nikiwa umbali wa mita takriban kumi kumfikia yule askari nilinyoosha mkono wangu wa kulia kumwonesha yule askari kitambulisho changu cha uandishi wa habari (Press Card).

“Naitwa Jason Sizya, mwandishi kutoka Capital Media Inc.,” nilijitambulisha huku nikimtazama yule askari kwa umakini. Mara nikaliona tabasamu pana likichanua usoni kwa yule askari baada ya kuonekana kunitambua, kisha kwa ujasiri mkubwa nilimsogelea karibu yule askari huku nikiyazungusha macho yangu kutazama huku na kule halafu nikasogea mahali lilipotokea tukio (ground zero) ambako kulikuwa na wafanyakazi wa kikosi cha zimamoto na uokoaji waliokuwa wakiendelea kuukabili moto huo bila mafanikio.

Dakika chache zilizofuata eneo lote lilijaa magari ya Polisi, JWTZ, magari ya wagonjwa (Ambulance) na magari mengine ya zimamoto na uokoaji kutoka kampuni binafsi huku maofisa wa usalama wenye silaha za kivita wakishika doria kulinda eneo lile iwapo kungetokea uhalifu mwingine. Maofisa wale walikuwa makini sana wakizungusha macho yao pembe zote.

Miongoni mwa maofisa wa usalama waliokuwepo hapo niliwafahamu wawili, mmoja alikuwa mtaalamu wa uchunguzi wa eneo la tukio (Forensic experts) na mwingine alikuwa mtaalamu wa mabomu na milipuko wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania walioanza kukagua eneo lote ili kuona kama kulikuwa na masalia ya mabomu mengine ambayo yalikuwa hayajalipuka.

Polisi wa kikosi maalumu cha kutuliza ghasia walikuwa wametanda eneo lote wakikimbia huku na huku kuwadhibiti wananchi waliokuwa wakijaribu kusogea karibu zaidi ili waweze kuona vizuri. Waandishi kadhaa wa habari wa vyombo vya ndani na vya nje na wapiga picha binafsi nao walikuwa wameshawasili eneo lile na kuanza kupiga picha.

Muda huo huo magari matatu yalifika eneo hilo, gari mojawapo likiwa ni la Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI) Kamishina Zuberi Koba, gari lingine lilikuwa limemchukua Mkaguzi wa Polisi (Inspector) Aden Mkojela kutoka Makao Makuu ya Polisi, na gari la tatu lilikuwa la mkuu wa kituo cha Polisi cha Oysterbay, SSP Edwin Msimbe aliyekuwa amefuatana na maofisa wengine wa usalama. Wote waliteremka haraka na kuungana na maofisa wengine wa usalama waliokuwepo eneo lile ili kuokoa majeruhi na kuimarisha ulinzi.

Baada ya kuangalia hali ilivyokuwa, na kufanya tathmini ya haraka, DCI Kamishina Koba aliagiza askari wa ziada kutoka kikosi cha kutuliza ghasia kuja kuimarisha ulinzi kwenye eneo lote lililozunguka jengo la Alpha Mall ili kusaidia kuzuia kuvurugwa kwa ushahidi katika eneo lile la tukio.

Moto mkubwa uliendelea kuwaka kwa nguvu, ukiunguruma kwa utisho kadri ulivyoendelea kuteketeza magari na vitu vingine vya thamani. Muda huo sauti za vilio vya watu waliojeruhiwa vilisikika sambamba na kelele za watu waliokuwa wakihimizana kutoa msaada, wakati huo muungurumo wa moto mkubwa ulikuwa ukiongezeka kila dakika, vyote vilipafanya mahali hapo kuonekana kama uwanja wa vita.

Pamoja na hali ile ya eneo lile kuonekana kama uwanja wa vita lakini wasamaria wema waliokuwa wanamiminika katika eneo hilo hawakuacha kutoa msaada kwa majeruhi huku wakishirikiana na kikosi cha uokoaji. Wengi wa majeruhi waliotolewa walikuwa wameumia sana na walitapakaa damu mwili mzima. Nguo zao walizovaa zilikuwa hazitamaniki kutokana na damu, moshi, na uchafu mwingine uliotokana na vumbi la kifusi.

Muda wote nilikuwa makini sana kuchunguza mazingira ya eneo lile huku nikipiga picha kila nilichohisi kingeweza kunifikisha kwa watu waliofanya tukio hilo, mara macho yangu yalivutwa zaidi na mtoto mdogo wa miaka miwili aliyetolewa kwenye kifusi akiwa hai pasipo jeraha lolote ingawa nguo zake zilikuwa zimechafuliwa na vumbi la kifusi. Mtoto yule alikuwa na fahamu na alikuwa akilia kwa hofu huku hali yake kimwili ikionekana kuwa nzuri ila kisaikolojia alionekana kuathiriwa sana.

Na hapo nikajikuta nikisisimkwa mwili wote na nywele zangu kusimama wima kichwani. Nilijiluliza ikiwa mama wa mtoto huyo alikuwa hai au alikuwa ni mmoja wa watu waliokufa katika tukio hilo! Bila kupoteza muda utaratibu wa kuwakimbiza hospitalini majeruhi wote ulifanywa, walikimbizwa katika Hospitali ya Mwananyamala na wale walioonekana kuzidiwa zaidi walikimbizwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Hata wale watu ambao mwanzoni walikuwa wakigombea kupanda daladala katika kituo cha Makumbusho sasa walikuwa wamekusanyika kwa mbali katika eneo lile kushangaa na wengine walikuwa wakisimuliana jinsi walivyoweza kushuhudia mlipuko mkubwa ulioliangusha kabisa jengo lile la Alpha Mall na kuleta uharibifu mkubwa kwenye majengo mengine ya jirani na hata magari zikiwemo daladala.

Hata hivyo, hakuna yeyote kati yao aliyeonekana kuwa na fununu yoyote kuhusu mtu, au kikundi kilichohusika na tukio lile. Wapo waliolihusisha tukio lile na kundi la kigaidi la al-Shabab kutoka Somalia na wengine walidhani huenda ni kundi la Islamic State ambalo kwa wakati huo lilikuwa limeweka maskani yake katika Jimbo la Cabo Delgado, Kaskazini mwa nchi ya Msumbiji baada ya baadhi yao kudhaniwa kuwa ndio waliofurushwa maeneo ya Mkuranga na Kibiti.

Endelea...
 
taharuki..jpg

278

Kitu hicho kiliwapa wasiwasi maofisa wa usalama waliokuwa wakilinda eneo lile kutokana na kuwepo kwa uwezekano wa kutokea kwa shambulizi la pili. Jambo hilo walilipa uzito kwa kuelewa kuwa mara nyingi magaidi hupenda kufanya hivyo kwa lengo la kusababisha madhara makubwa, ili kutia hofu kubwa na kufikisha ujumbe wanaoutaka. Kwani kila wanapofanya tukio moja linalosababisha watu kukusanyika, kwao huwa ni fursa nyingine ya kufanya shambulio la pili, na ikiwezekana kubwa zaidi.

Hali hiyo iliwafanya maofisa wa usalama wazidishe ulinzi na umakini kwa kila mtu aliyekuwepo mahali pale. Hata mimi ambaye nilikuwa nimemshuhudia yule mwanamume mrefu mwenye ovaroli la rangi ya samawati akija pale na pikipiki yenye magurudumu matatu iliyobeba bomu na kisha kuondoka haraka kwa kutumia pikipiki aina ya Boxer BM 150 ya rangi nyekundu, sikuwa na uhakika kama mtu yule alitumiwa na Alshabab au Islamic State.

Kitu pekee nilichokuwa na uhakika nacho ni kuwa lile tangi lililokuwa mfano wa tangi la mafuta lililochomelewa nyuma ya ile pikipiki ya magurudumu matatu ndilo lililokuwa limehifadhi bomu ndani yake. Nilijitahidi kushirikiana na vikosi vya uokoaji na baadhi ya maofisa wa usalama kuwasaidia majeruhi na hapo hapo nikipiga picha na kukusanya taarifa za kiuchunguzi kwa kadri ya uwezo wangu.

Mpaka wakati huo maiti za watu kumi na nane zilikuwa zimeshapatikana ikiwemo miili ya Waziri wa Mambo ya Ndani Ummi Mrutu, dereva wake na Katibu wake Octavian Lister, huku mpelelezi wa kujitegemea Daniel Kayera na watu wengine kadhaa wakiwa katika hali mbaya, na hivyo ilitarajiwa kuwa idadi ya vifo ingeweza kuongezeka.

Daniel Kayera alikuwa ametolewa kwenye kifusi akiwa hoi, nguo zake zilikuwa zimelowa damu chapa chapa. Hakuwa na fahamu na hali yake ilionekana kuwa mbaya mno. Kwa kumwangalia tu, kungeufanya mwili wako wote usisimke na nywele zako kusimama wima. Bila kupoteza muda utaratibu wa kumkimbiza hospitalini ulifanywa, akakimbizwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Sasa vikosi vya uokoaji vilielekeza nguvu zote katika kufukua kifusi ili kuokoa watu waliokuwa bado wapo hai. Kila majeruhi aliyeokolewa ambaye alionekana kuwa na uwezo wa kuzungumza, maofisa wa usalama walichukua taarifa zake zote muhimu kama jina kamili, tarehe ya kuzaliwa, kabila, dini, anwani ya makazi, na taarifa nyingine muhimu walizoona zingesaidia kumpata muhusika kama angehitajika kusaidia upelelezi, au kuwapata ndugu zake kama mtu huyo angepoteza maisha.

Baadhi ya watu walikuwa wamejeruhiwa sana kiasi cha kutoweza kujitambua lakini wengine hawakuwa hata na mchubuko ingawa walikuwa hoi kisaikolojia kutokana na mshituko mkubwa walioupata; aidha kwa mshindo wa mlipuko, au ile hali ya kunusurika na kifo. Ni wachache tu kati yao waliokuwa na ujasiri wa kutoa maelezo mara moja, na kwa usahihi. Hawa ni wale waliotengenezewa utaratibu maalumu wa kuhojiwa wakati huo huo ili kupata dondoo za kuanzia uchunguzi.

Kila majeruhi aliyeokolewa alifanyiwa tathmini ya haraka kujua hali yake ya kiafya, kisha aliulizwa maswali machache ya kuwasaidia wanausalama mahali pa kuanzia uchunguzi, kisha walimwingiza katika gari na kumkimbiza hospitali. Hata wale walioonekana kutokuwa na majeraha makubwa bado ilisisitizwa kuwa waende hospitali kufanyiwa uchunguzi zaidi wa kitaalamu.

Kwa vile magari rasmi ya wagonjwa hayakutosheleza mahitaji ya majeruhi waliokuwepo, maofisa wa polisi walitumia magari binafsi yaliyokuwa jirani na eneo lile baada ya kuwaomba madereva au wamiliki wa magari hayo kusaidia kuwakimbiza majeruhi hospitali za Mwananyamala na Muhimbili.

Ili kujua hali halisi ilivyokuwa Kamishina Koba aliwaagiza askari wa upelelezi kufanya kazi ya kuchukua maelezo ya mmiliki, walinzi na wapangaji wote wa jengo la Alpha Mall waliosalimika, na watu wengine waliokuwepo katika eneo hilo wakati tukio likitokea. Hata hivyo, kutokana na mshituko uliowapata watu wengi, wengi wao hawakuweza kueleza kwa ufasaha mambo waliyoyashuhudia, na hata wengine walieleza mambo yaliyotofautiana kabisa na hali ilivyokuwa.

Nilishuhudia maofisa wa usalama wakijitahidi kufanya kazi kwa weledi ingawa hali ilikuwa ya kutisha sana. Kwa upande wangu huo ulikuwa ni wakati wa kukusanya taarifa za kiuchunguzi nikiendelea kujifanya mwandishi wa habari niliyekusudia kuihabarisha jamii. Nilichokifanya ni kuvizia wakati maofisa wa usalama wakiwahoji walioshuhudia tukio na mimi nilijitahidi kujiweka karibu ili kuwatambua watu wote walioelekea kuwa na taarifa za maana, kisha niliandika taarifa hizo kwenye notebook yangu.

Hata hivyo, hakuna kati yao aliyeonekana kuwa na taarifa za maana au kufahamu chochote juu ya ujio wa ile pikipiki yenye magurudumu matatu iliyokuwa na bomu au kuhusu yule mwanamume mrefu mwenye ndevu nyingi aliyeileta ile pikipiki na kisha kuitelekeza pale kabla hajaondoka na pikipiki nyingine nyekundu.

Kwa takribani dakika 35 ambazo nilikuwepo eneo hilo sikuwa nimeambua taarifa zaidi ya kiuchunguzi tofauti na zile nilizozifahamu lakini moyo wangu ulikuwa umeridhika sana kwa yale niliyokuwa nimeyafanya kushiriki kikamilifu katika shughuli nzima ya uokoaji na kuwa na taarifa muhimu za awali ambazo takriban maofisa wengine wote wa usalama hawakuwa nazo.

Ingawa niliamini kuwa taarifa nilizokuwa nazo bado zilikuwa zimefungwa katika fumbo gumu sana lililohitaji kazi ya ziada kulifumbua lakini nilijisikia vyema kwani nilikuwa mtu pekee niliyeshuhudia tukio zima tangu kufika kwa ile pikipiki yenye magurudumu matatu hadi pale mlipuko ulipotokea na nilikuwa nimefanikiwa kurekodi tukio zima kwenye kamera yangu. Zaidi ya yote niliamini kuwa huo ulikuwa mwanzo mzuri wa kupata taarifa zaidi ambazo zingesaidia kuwafichua wale wote waliofanya tukio hilo la kinyama.

Sasa niliamua kujichanganya katikati ya mvurugano wa wanausalama na watu waliokuwa wakisaidia katika uokoaji ili nipate mawili matatu, kwa kuwa nilikuwa nimejifunza mengi katika maisha yangu ya ujasusi na harakati zangu, niliamini katika kuliweka wazi sikio langu kumsikiliza kila mtu iwe anazungumza upuuzi ama anajenga hoja chanya na madhubuti na kisha ningeyafanyia kazi yale niliyoona ni muhimu kwangu. Niliamini kuwa hakuna gharama yoyote katika kusikiliza kila kitu ila kulikuwa na gharama katika kufanyia kazi hayo uliyoyasikiliza.

Nikiwa bado nimejichanganya katikati ya mvurugano mkubwa wa watu kujaribu kupata mawili matatu huku nikitafakari hatua ya kuendelea nayo, simu yangu ya mkononi ikaanza kuita, nilipoitazama vizuri nikaliona jina la mke wangu Rehema kwenye kioo cha simu. Rehema alikuwa likizo na alisafiri kwenda nyumbani Tabora, hivyo baada ya kupata taarifa za mlipuko wa bomu jirani na ofisi yangu kwa vyovyote alitaka kujua kama nilikuwa nimesalimika.

Nikaipokea na kumjulisha kuwa nilikuwa katika harakati za uokoaji, hivyo ningewasiliana naye baadaye. Nikamsikia akishusha pumzi baada ya kujua kuwa nilikuwa mzima. Simu ikakatika.

Wakati nairudisha simu yangu mfukoni nikahisi mkono ukinigusa kwenye bega langu la kushoto huku sauti nzito ikinisemesha, “Hujambo, Jason?”

Nilishtuka na kugeuka haraka ili nimwone mtu aliyenitambua katika ule mvurugano mkubwa wa watu ingawa sikuona ajabu kwa mtu kunitambua kwa sababu kazi yangu bandia ya uandishi wa habari za kiuchunguzi ilinifanya kuwa mtu maarufu aliyefahamiana na watu wengi. Nilipomwona mtu yule aliyemsemesha sikuyaamini macho yangu, mwili wangu ulinisisimka na mapigo ya moyo wangu yalibadili mwendo wake na kuanza kwenda mbio isivyo kawaida!

Endelea kufuatilia...
 
taharuki..jpg

279

Nilikuwa nikitazamana na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI) Kamishina Zuberi Koba, ambaye wakati huo sura yake ilionekana kusawajika sana kwa mawazo na kujawa mikunjo ya hasira na uchungu.

“Shikamoo, Kamishina!” nilimwamkia Kamishina Koba kwa heshima.

“Marahaba, vipi umekuwepo hapa kwa muda mrefu kabla yangu?” Kamishina Koba aliniuliza kwa shauku.

Yeah, muda mfupi tu tangu bomu lilipuke na kuleta uharibifu,” nimlijibu kwa sauti tulivu huku nikishusha pumzi za ndani kwa ndani.

“Kwa kukuona tu hapa nahisi tayari kazi imeshampata mtu sahihi…” Kamishina Koba alisema kwa utani huku akiachia kicheko hafifu kisha akaongeza, “Tunaweza kuzungumza kidogo?” safari hii aliuliza huku akiwa na uso wa kazi na tabasamu lilikuwa limeshachukua likizo. Alikuwa akinitazama usoni kwa tuo.

Mwili wangu ulisisimka zaidi na moyo wangu ulipiga mshindo mkubwa, nilianza kuhisi damu yangu ikikimbia kwa kasi na nywele zangu kunisimama kichwani, sikujua Kamishina Koba alitaka tuzungumze kuhusu nini. Nilifahamu fika kuwa Kamishina Koba alinifahamu kama mwandishi wa habari za kiuchunguzi na hakujua kama nilikuwa ofisa wa usalama wa taifa, na hivyo nikajiuliza alitaka nini kutoka kwangu, au alishajua kuwa lile tukio nilikuwa nimelirekodi kwenye kamera yangu!

Hata hivyo, nilijitahidi kutabasamu ili nisioneshe hisia ya wasiwasi usoni kwangu kwani sikutaka kumpa nafasi yoyote Kamishina Koba ya kunishtukia. Nikabetua kichwa changu kukubali.

“Bila shaka yoyote,” nilisema huku nikijaribu kubashiri mazungumzo yangu na Kamishina Koba yangehusu nini.

“Sasa… naomba unikute pale kwenye kilima jirani na jengo la Jhpiego Tanzania kama unaelekea Victoria, baada ya dakika kumi kuanzia sasa. Nitakuwa nakusubiri hapo ndani ya gari langu…” Kamishina Koba alisema huku akiinua mkono wake kuangalia saa yake ya mkononi, kisha akaongeza akiongea kwa msisitizo, “Hakikisha saa kumi na mbili na robo juu ya alama uko pale.”

Mimi pia niliitazama saa yangu ya mkononi na kuafiki kwa kichwa. Bila kuongeza neno Kamishina Koba aligeuka na kutokomea kwenye umati wa watu waliokuwepo eneo lile. Nami nikajichanganya katikati ya makundi ya watu. Ilinilazimu kwanza kuangalia mazingira niliyokuwepo maana sikuwa nikijua nani angeweza kuwa mtu mbaya na nani mzuri kwani eneo zima lilikuwa kama uwanja wa vita.

Kama jasusi niliyejipa kazi ya uandishi wa habari hatari za kiuchunguzi, nilitambua kuhusu mbinu za kiusalama kwamba, huwa hatupaswi kuanza safari kwa kukurupuka hata kama hali ni shwari kiasi gani. Nilijua kuwa kila kachero hupaswa kujiandaa kabla ya kwenda mahali na hasa kama safari yenyewe ni ya kukutana na mtu muhimu, vinginevyo inaweza kumtia matatani yeye mwenyewe pamoja na mtu anayekwenda kukutana naye.

Kabla sijaanza kuondoka eneo lile nilitumia dakika tatu kuangalia watu huku nikijitahidi kumsoma kila mtu aliyekuwepo mahali hapo katika namna ya kujua kama yupo mtu aliyeonesha kuvutiwa na uwepo wangu eneo lile au hata kufuatilia nyendo zangu. Dakika tatu tu ziliniwezesha kuwatambua mashushushu wengi waliokuwa wamejichanganya katika umati uliosimama upande wa pili wa barabara, macho yao yakiwa yameelekezwa kwangu.

Na niliwaona waandishi wengi wa habari wa vyombo mbalimbali vya habari ambao pia walikuwa miongoni mwa umati wa watu uliosimama upande huo wa pili wa barabara. Sikushangaa, kwani nilijua kuwa waandishi hao hawakutegemea kuniona nikiwa nimejichanganya na maofisa wa usalama, polisi na wanajeshi namna ile wakati wao waliwekewa eneo maalumu la kusimama. walijua jinsi nilivyokuwa nimejenga uaminifu mkubwa, kwa muda mfupi, kwa wanausalama.

Niliweza kuwatambua waandishi wale, wengine walikuwa wa kutoka vyombo vya kimataifa kama CNN, BBC, DW na kadhalika. Wote walikuwa makini kufuatilia kila jambo lililokuwa linafanyika kwenye lile jengo la Alpha Mall lililoangushwa na bomu na wengine walikuwa wakipiga picha. Uwepo wa waandishi hao ulinithibitishia kuwepo kwa waandishi wengine wengi ambao sikuwafahamu ambao huenda sikuweza kuwaona kwa sababu walikuwa wamejichanganya.

Sikutaka kuendelea kuwepo eneo lile, nilifanya kama naelekea ofisini kwangu kwenye jengo la Makumbusho Plaza, niliufuata ule mtaa uliokuwa ukielekea kwenye jengo zilipo ofisi zangu na kupishana na mwanamume mmoja mfupi ambaye alikuwa akitafuna bubblish, alikuwa na macho ya kusinzia, mustachi mpana na uso wake ulikuwa serious, alikuwa akitazama mbele. Alikuwa amevaa shati la pundamilia la mikono mirefu, suruali nyeusi ya dengrizi, raba nyeusi za puma miguuni na miwani ya macho.

Kitu ambacho kingenifanya nimkumbuke mwanamume huyo ni namna ambavyo mustachi wake ulikuwa mpana na pengine macho yake ya kusinzia. Nilijikuta nikivutiwa sana kumtazama mwanamume yule huku hisia zangu zikiniambia kuwa nilitakiwa nifuatilie nyendo zake lakini bahati mbaya sikuwa na muda huo.

Kwa kuhesimu hisia zangu nikampiga picha mbili tatu za haraka haraka kwa kificho, wakati huo alikuwa akienda kujichanganya na watu wengine waliokuwa wamesimama kwa mbali, huku macho yake yakiwa makini sana yakilenga zaidi kumwangalia kila mtu aliyekuwa akibebwa kwenye machela na kuingizwa kwenye magari ya wagonjwa.

Niliridhika na kuendelea na safari yangu na nilipofika mwisho wa mtaa ule niligeuka kutazama nyuma nikiendelea kumsoma kila mtu niliyepishana naye ili kujua kama alikuwepo mtu au watu walioonesha kufuatilia nyendo zangu, niliporidhika kuwa hali ilikuwa bado shwari kwa upande wangu, haraka nikaingia upande wa kushoto nikiufuata mtaa wa Wakatibado.

Mtaa ule ulikuwa na watu wengi waliokuwa wakitembea kwa kasi, au kukimbia kuelekea kwenye eneo la tukio ili kujionea kinachoendelea. Kwa kuwaangalia tu jinsi walivyokuwa wanakwenda, niliweza kutambua kuwa asilimia kubwa ya watu wale, kama si wote, hawakuwa na ufahamu wowote wa mambo ya kiusalama. Walikuwa wanajiendea tu bila kuchukua tahadhari ya aina yoyote.

Nilitembea haraka kando ya ule mtaa ambapo ulikuwa ukikata zaidi kuelekea upande wa kushoto, nikazidi kuufuata na kwenda kutokea Barabara ya Bagamoyo, kulia kwangu kulikuwa na jengo la ofisi za Jhpiego Tanzania, nikaingia kulia kwangu kama naifuata barabara ile ya Bagamoyo, na mara nikaliona gari la Kamishina Koba aina ya Mercedes Benz jeusi lililokuwa na vioo vyeusi visivyomruhusu mtu kuona kilichokuwemo ndani ya gari likiwa limeegeshwa kando ya barabara.

Kamishina Koba alikuwa peke yake ndani ya gari lake na aliponiona akashusha kioo cha dirisha la upande ambao nilikuwepo na kuniashiria nipande ndani ya gari. Bila kujiuliza nilifungua mlango wa mbele na kukaa katika kiti cha abiria. Muda wote gari lilikuwa linaunguruma taratibu.

Kisha aliniambia nifunge mkanda, nikajiuliza alitaka kunipeleka wapi. hata hivyo niliamini kuwa hakuwa na nia mbaya na hivyo nikafunga mkanda wakati Kamishina Koba akitia gia na kuliondoa gari lake kwa kasi akaingia barabarani huku magurudumu ya gari lake yakichimba chini na kuyafanya yaserereke halafu akaifuata barabara hadi tulipofika usawa wa kituo cha daladala cha Victoria, kabla hatujalivuka jengo la Victoria kwenye ofisi za Knight Support Security, akaingia kulia akiufuata mtaa mmoja mfupi hadi alipoufikia mgahawa wa KFA, akaliegesha gari lake kando ya barabara, jirani na mgahawa huo.

Endelea kufuatilia...
 
taharuki..jpg

280

Kisha Kamishina Koba akanikabili huku akinitazama kwa umakini zaidi machoni kama aliyekuwa akijaribu kuyasoma mawazo yangu. Hii haikuwa mara yake ya kwanza kukutana faragha na mimi. Naam! Mkuu yeyote wa taasisi ya ulinzi na usalama ni mtu tofauti kabisa haijalishi unafahamiana naye au la, muda huo mapigo ya moyo wangu yalikuwa yakienda mbio isivyo kawaida, koo langu lilikauka ghafla na nywele zangu zilisimama kichwani kwa hofu.

Sasa nilikuwa ana kwa ana nikitazamana na mwanausalama huyo aliyekuwa amebobea katika medani za usalama kiasi cha kuaminiwa kupewa cheo cha Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai. Umri wake wa miaka 54 ulikuwa haujazipokonya nguvu zake mwilini. Macho yake makali yalinitazama kwa makini pasipo kupepesa wala kusema neno lolote, huku akionekana kuipa utulivu akili yake. Kisha alishusha pumzi za ndani kwa ndani na kujiegemeza kwenye kiti chake huku akivunja ukimya.

“Najua ofisi yako ipo jirani kabisa na eneo lilipotokea tukio na wewe ni mtu makini sana… je, una lolote la kuniambia?” Kamishina Koba aliniuliza kwa sauti nzito yenye mamlaka kana kwamba nilikuwa mtuhumiwa.

Moyo wangu ulipiga kite kwa nguvu! Nilishindwa kujibu swali lake na kumkodolea macho katika namna ya kuonesha kuwa sikuwa nimelielewa swali lake. Kamishina Koba aling’amua jambo hilo na kuachia tabasamu huku akivuta pumzi ndefu na kisha kuzishusha taratibu.

“Ninajua wewe ni mtu makini sana muhimu sana kwangu na kwa taifa… hata Jeshi la Polisi linauthamini sana mchango wako japo huna muda mrefu kwenye medani za uandishi… inawezekana kuwa ulimwona mtu au watu uliowatilia shaka kabla na baada ya mlipuko kutokea ndiyo maana ninajaribu kukuuliza kama una chochote ambacho kinaweza kutusaidia? Kumbuka mchango wako hautakuwa na msaada kwangu tu bali kwa taifa zima!” Kamishina Koba aliniambia kwa sauti tulivu huku akinikazia macho.

Mara tu niliposikia maneno hayo moyo wangu ukapoteza utulivu kabisa, kijasho chepesi kilianza kunitoka mwilini japo ndani ya lile gari kulikuwa na ubaridi mkali uliokuwa ukisambazwa na kiyoyozi.

Hata kama tulikuwa marafiki lakini sikuthubutu kumweleza chochote Kamishina Koba kuhusu yale yote niliyoyashuhudia, tangu yule mtu mrefu mwenye ndevu nyingi aliyevaa ovaroli la rangi ya samawati alivyofika pale na pikipiki aina ya WANHOO ya magurudumu matatu, alivyoiacha na kisha kuondoka haraka hadi kutokea kwa ule mlipuko.

Taaluma yangu ya ujasusi ilinionya kuwa makini na kuweka mipaka katika mazungumzo yoyote na mtu yeyote, hata mkuu wangu wa kazi. Katika mazungumzo yangu na Kamishina Koba nilipaswa kuwa makini sana maana kwa kusema kitu nilichokishuhudia ingeweza kuharibu mambo, akili yangu ilianza kusumbuka katika namna ya kutaka kufahamu kwa nini DCI Kamishina Koba alitaka kupata taarifa kutoka kwangu badala ya kuwauliza vijana wake waliokuwepo kwenye eneo la tukio!

Kwa hivyo, ili kutompa nafasi ya kugundua kuwa nilikuwa na jambo moyoni lakini sikuwa tayari kulisema kwake au kwa mtu mwingine yeyote hadi pale muda muafaka ukifika, nilijifanya kuangalia juu huku nikijitia kufikiria kwa kitambo fulani kisha niliminya midomo yangu na kushusha pumzi ndefu halafu nikatingisha kichwa changu taratibu kukataa.

Macho makali ya Kamishina Koba yalikuwa yananiangalia kwa makini na kwa kitambo fulani kukatokea ukimya wa kutisha ndani ya lile gari, kisha nilimwona akikohoa kidogo kusafisha koo lake. “Huenda ukawa umeshangazwa sana na swali langu…” aliniambia halafu akaweka kituo kidogo na kukohoa tena kabla ya kuendelea. “Naamini wewe ni mtu makini sana na una uwezo mkubwa mno wa kunusa hatari wakati wowote, ndiyo maana nilitarajia kusikia chochote toka kwako badala ya kuwauliza vijana wangu… sijajua kwa nini hukujiunga na Jeshi la Polisi au Usalama wa Taifa!”

Kamishina Koba aliposema hivyo nikatamani kucheka maana pamoja na kubobea kwenye medani za usalama lakini hakujua mimi ni nani hasa bali alinichukulia kama mwandishi tu wa habari. Akili yangu ikiwa imeanza kupoteza utulivu wake na mitupo ya mapigo ya moyo wangu ikiongezeka mara dufu, nilibaki kimya huku nikimtazama.

Kikazuka kitambo kingine cha ukimya huku kila mmoja wetu akiwaza lake. Nikiwa nimeanza kuzama kwenye tafakuri huku mawazo yangu yakihamia kwenye lile tukio la yule mwanamume mrefu mwenye ovaroli la rangi ya samawati aliyeleta pikipiki ya magurudumu matatu iliyobeba bomu, nilishtuliwa na sauti nzito ya Kamishina Koba.

“Naona kama una mashaka fulani, nimetaka tu kujua kama una chochote cha kuniambia ili nipime kama taarifa zako zinapaswa kutolewa hadharani kwa sasa au hazipaswi ili usije uka-expose mambo ambayo hayapaswi kutolewa kwa sasa kwani yanaweza kuingilia upelelezi…” Kamishina Koba alisema na kusita kidogo kisha akaendelea.

“Na kwa kuwa hili ni jambo linalohusu ugaidi, watakaohusika zaidi kuchunguza ni makachero wa kikosi cha Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Idara ya Usalama wa Taifa na Millitary Intelligence, shaka yangu ni kwamba kama unazo taarifa nyeti zisije zikawafikia watu wasio sahihi maana kwa aina ya shambulio lilivyotokea inaonekana kabisa kuna mkono wa watu kutoka katika majeshi yetu,” DCI Kamishina Koba alisema kwa sauti yake nzito na tulivu huku akiendelea kunitazama usoni kwa utulivu ingawa alionesha yupo mbali sana kimawazo.

Kitambo kingine cha ukimya kilipita baina yetu na kila mmoja wetu akionekana kuzama kwenye tafakuri nzito kichwani mwake, Kamishina Koba alikuwa katika hali ya simanzi huku akiviminyaminya vidole vyake vya mikononi taratibu katika hali ya kuupisha utulivu kichwani mwake.

“Nimekuelewa sana, Kamishina… endapo nikipata chochote nitawasiliana moja kwa moja na wewe kama ulivyoshauri,” niliongea kwa utulivu nikijitahidi kuonesha unyenyekevu mkubwa kwake huku nikiendelea kuyatafakari yale maelezo yake.

“Hili ni tukio baya sana linalotaka kutia doa jina letu la ‘Tanzania kisiwa cha amani’. Kwa hiyo ili kuhakikisha hawa watu wanapatikana tayari utaratibu wa haraka umeshafanyika kudhibiti mipaka yote ili watu waliofanya tukio hili wasiweze kuvuka kwa urahisi, pia tumeagiza kucheleweshwa kwa ndege za abiria katika viwanja vya ndege vyote nchini ili kuwapa maofisa wa Idara ya Usalama na Polisi muda wa kufanya upekuzi wa ziada kwa abiria wanaoondoka nchini,” Kamishina Koba aliendele kuongea kwa utulivu.

Nilimwangalia Kamishna Koba kwa macho yaliyobeba maswali lukuki ingawa nilijitahidi kuwa mtulivu sana. Sikujua kwa nini aliamua kunieleza mambo yale wakati akijua kuwa sikuwa polisi wala ofisa wa usalama bali nilikuwa mwanahabari tu wa kawaida!

Kama aliyekuwa akiyasoma mawazo yangu Kamishna Koba aliachia tabasamu na kusema, “Najua sipaswi kukueleza haya, lakini ukweli unabakia pale pale kuwa umekuwa source (mtoa habari) wetu muhimu sana… hata hivyo, naomba usimwambie mtu yeyote yule kuhusu haya tuliyoongea.”

Aliposema hayo aliweka tena kituo kidogo na kumeza mate ili kutowesha koo lake kabla ya kuendelea, “Sasa unaweza ukaendelea na taratibu zako zote za kiuandishi kama kawaida, baraka zangu unazo… Ila tafadhali, tafadhali…” alipokuwa akisema neno ‘tafadhali’ alikazia kwa kupiga piga ngumi juu ya usukani wa gari lake, “…nitakuomba unipe taarifa pale utakapogundua chochote kuhusu tukio hili. Sawa?”

Nilibetua kichwa changu kukubali. Kamishina Koba akaendelea kuongea kwa msisitizo huku macho yake makali yakiwa hayatoki usoni kwangu, “Unajua, Mr Sizya… sikio la mtu yeyote nje ya gari hili lisisikie chochote tulichoongea maana hujui yupi ni mwema kwako na yupi anaweza kukuuza. Nadhani umenielewa?”

“Nimekuelewa sana, Kamishina,” niliitikia kwa unyenyekevu na kisha nikashuka toka ndani ya gari lake. Kamishina Koba hakusubiri, alilitia moto gari lake na kuliondoa kwa kasi, akaingia mtaa wa Uporoto huku akiniacha nimeduwaa kwa muda nikilisindikiza kwa macho hadi lilipopotelea mtaani, halafu nikageuka na kuanza kutembea taratibu nikirudi zangu ofisini.

Muda huo jua lilikuwa limekwisha zama, na kwa mbali, kiza kikianza kuchukua nafasi yake huku anga la rangi nyekundu likinywea taratibu katika ukungu.

* * *

Mambo ndo kwanza yanaanza, endelea kuufuatilia mkasa huu wenye 'TAHARUKI'...
 
ila hapa kanisikitisha kidogo,hajafanya maamuzi ya haraka kuepusha maafa kutokea mara baada tu yakuona boma kwenye pikipiki
Sidhani kama alijua ni nini kilichokuwepo nyuma ya pikipiki, bila shaka hata yeye asingekaa pale akishangaashangaa[emoji16][emoji16]...
 
Asante sana Bishop, hii kweli ni Taharuki na hatujui kitakachotokea!
 
Back
Top Bottom