Simulizi: Mimi na Mimi

Simulizi: Mimi na Mimi

MIMI NA MIMI 2

A Story by Elton Tonny

Familia, Urafiki, Mapenzi, Kazi, Siri, Tamaa, Hila, Usaliti, Ukatili, Mauaji, Mambo Yasiyotazamiwa

R-rated 18+

Enjoy!


★★★★★★★★★★★★★★

SEHEMU YA KUMI

★★★★★★★★★★★★★★


Jumanne ikakucha. Leo hii sikuamka mapema wala nini, yaani nililala katika maana ya kwamba ilikuwa siku ya mapumziko kwelikweli kwenye hizi siku za likizo, na moja ambayo ingeburudisha. Angalau leo ningetumia muda mwingi pamoja na binti Mariam na familia yake, na tena tungekwenda sehemu nzuri sana pamoja ili kufurahia mlo wa maana, hivyo kusingekuwa na mambo mengi mno ya kunivunja moyo ingawa najua hayakuwa yameisha.

Baada tu ya kumaliza usafi na kunywa chai pamoja na Ankia, nikawa nimeelekea kwa majirani zetu bila kukawia. Nilikuwa nimeshamwambia na Ankia pia kuhusu matembezi yetu ya baadaye niliyokuwa nimepanga kufanya pamoja nao, na yeye bila shaka alikuwa na utayari wa kuja, ila hakujua sana kama angeweza kuwahi kutoka kazini kwake ili ajiunge nasi.

Nikamsihi tu afunge duka lake ikifika mida ya saa saba au nane mchana ili aje tujiandae kwenda, na nikamtania kwa kusema ningelipia gharama yote ya wateja ambao angewakosa leo kwa wakati mzuri ambao angeupata pamoja nasi. Akawa ameridhia maana alikuwa na hamu pia ya kuja kupiga kisinia pamoja nasi, hivyo akaona awahi kuelekea dukani kwake kufungua kidogo mpaka hiyo saa saba, ndiyo angerudi kujiandaa.

Basi, baada ya kuwa nimefika hapo kwa kina Mariam, nikamkuta binti sebuleni, akiwa amekaa chini kabisa na kuonekana akiandika vitu fulani kwenye daftari. Alikuwa amevaa dera zuri lililoufunika mwili wake vyema pamoja na kinguo fulani kidogo cha kichwani kinachofunika nywele, na baada ya kuwa ameniona akaonyesha furaha yake na moja kwa moja kuniita nione alivyokuwa anaandika. Hapo sebuleni hakukuwa na mtu mwingine isipokuwa yeye, kwa hiyo nikamsogelea na kuchuchumaa, nikiangalia alivyokuwa akiandika.

"Dada ameanza kunionyesha... kutumia singyula na pluro..." akasema hivyo.

"Ahaaa... singular and plural?" nikamsemesha huku nikitabasamu.

"Eeeh. Wingii na umoja. Yaani nayaona mepesi sana," akasema hivyo.

"Na ni mepesi sana, safi. Ona... unaandika vizuri sana Mamu, eh! Yaani unanishinda hadi mimi!" nikampa sifa.

Akacheka kwa furaha na kusema, "Tena hapa ni kidogo. Yaani naandika vitu vingi sana. Kila zoezi dada akinipa, napata yote. Kila kitu rahisi yaani... sijui kwa nini zamani nilikuwa naona magumu!"

Nikamwangalia na kutabasamu kwa hisia kiasi, kwa sababu nilitambua kwamba akili yake ilikuwa ikifunguka zaidi, na aliongea kama vile hakujua kabisa kwamba alikuwa na shida kichwani.

"Ya kitoto sana haya, JC. Kiingereza naweza mbona? Uwe unanipa yale magumu ndiyo yenye challenge zaidi... dada ananiona kama yai tu! Nipe magumu magumu nimwonyeshe nayaweza," akasema hivyo.

"Ahah... kumbe unayajua eh?"

"Najua ndiyo!"

"Unasoma sana?"

"Eeh. Nimekuta madaftari huko ndani, kumbe yalikuwaga yangu! Mambo mengi nimeandika, mengine siyaelewi, lakini nimekuta... ma-matiki, matiki, matiki. Tatizo mnanipa marahisi mno, nataka niyajue magumu zaidi na yenyewe yawe marahisi. Sawa JC?" akaongea kwa uhakika kabisa.

Nikatabasamu na kumwambia, "Sawa. Usijali. Kafate na daftari lako moja niyaone yanayokuchanganya."

"Yes!" akasema hivyo kwa sauti ya juu.

Kakanyanyuka kabisa na kukimbilia chumbani huko, na ni hapo ndiyo Bi Zawadi akawa ametoka ndani ya chumba chake. Nikasimama na kutabasamu kwa furaha.

"Mamu? Huyo vipi tena?" Bi Zawadi akanisemesha hivyo huku akija upande wangu.

"Amefurahi, nimemwambia afate daftari lake. Shikamoo?" nikasema hivyo

"Marahaba baba. Basi kanishtua, nikafikiri kuna mtu kavunja mtungi," akasema hivyo.

Nikacheka kidogo kwa pumzi na kusema, "Pole. Ulikuwa umelala?"

"Hapana, nilikuwa tu ndani nakunja nguo. Vipi, JC? Unaendeleaje?"

"Niko poa kabisa cheupe wangu. Jana nilichelewa kurudi nikakuta mmeshasinzia," nikamwambia.

"Kumbe? Basi haina shida. Tesha alituambia yote yaliyotokea ile Jumapili. Aisee, poleni," akasema hivyo.

"Ah, asante... na usijali. Yameshapita."

"Mmm. Niliongea na mzee Hamadi akasema uliwanyoosha waliomwonea Miryam. Hivyo ndiyo inavyotakiwa kijana wangu. Safi sana!" akasema hivyo.

Nikatabasamu kiasi na kusema, "Asante. Vipi hapa? Mnaendeleaje?"

"Tuko salama kabisa. Hofu kwako. Nasikia walikupiga na virungu ulipombutua yule mjinga aliyemchapa Miryam na waya..."

"Eee, yule jamaa si mjinga tu? Akafikiri tutaogopa. Nikampa dozi yake, hatathubutu tena," nikamwambia hivyo.

Bi Zawadi akacheka na kugongesha kiganja chake kwangu, naye akasema, "Ni vizuri sana. Endelea kuwapa dozi zao mbabe wetu."

"Ahahahah... haupingwi mama..."

Bi Zawadi akacheka kidogo.

"Vipi wengine? Wako wapi?" nikamuuliza.

"Tesha ameenda na mama yake mkubwa hapo sokoni Mzinga, na Jamila na yeye ananyoosha miguu kidogo," akasema hivyo.

"Okay, ni vizuri sana. Na Miryam? Kazini mapema?"

"Eeeh. Halafu naona kama vile hayuko sawa," akaniambia hivyo.

"Kwa nini unasema hivyo?" nikawa makini zaidi.

"Sijui tu. Nahisi kama vile anasumbuliwa na ki...."

"JC, hili hapa," Mariam akawa amerejea pamoja na daftari la somo la kiingereza, la kwake wakati yupo kidato cha nne.

"Ooh, safi. Haya... nenda sa' hapo mezani. Chukua na kalamu zako, nakuja unionyeshe, sawa?" nikamwambia hivyo.

Akatikisa kichwa kukubali na kuokota daftari lile lililokuwa chini na kalamu zake, naye akaelekea pale dining.

"Amechangamka sana sasa hivi, JC," Bi Zawadi akaniambia hivyo kwa sauti ya chini.

"Eeh, maendeleo," nikamwambia hivyo.

"Sawa, basi me niwaache mmalize..."

"Aa... ndiyo, ila... niambie... kwa nini umesema unahisi Miryam ana tatizo?" nikamuuliza hivyo kwa sauti ya chini.

"Ahaa... eee, yaani nimemsikia tu hii asubuhi anaongea kwenye simu sijui na nani... ila inaonekana ni kitu kimemshangaza kwa jinsi alivyokuwa anaongea. Ni kama vile nimemsikia anaongelea madeni, halafu... na kwamba haimhusu yeye sijui, yaani sikuelewa sana, alikuwa anaongelea huko chumbani..." akasema hivyo.

Nikaweka uso makini zaidi.

"Sikujua ni nini... alipotoka chumbani nikamuuliza, akasema hamna shida. Ila, ameondoka kama vile hana raha. Itakuwa ni mambo ya kazi. Halafu... ametuambia unatutoa out leo. Ni kweli?" Bi Zawadi akasema hivyo.

Nikamtazama kishauku zaidi na kusema, "Eeeh. Tunaenda kula kisinia."

"Wow! JC wewe! Mamu... umesikia? Tunaenda kula kisinia leo," Bi Zawadi akasema hivyo kwa furaha.

Mariam akamwangalia na kuuliza, "Kwa nini tunaenda kula sinia?"

Mimi na Bi Zawadi tukaangaliana na kujitahidi kubana vicheko vyetu.

"Ni wapi?" Mariam akauliza.

"Usijali Mamu, nitawapeleka, utapaona. Pazuri. Utapenda sana kisinia," nikamwambia hivyo binti.

"Mi' sitaki kutafuna sinia," Mariam akasema hivyo huku akinyanyua bega kama vile mtoto.

Mimi na Bi Zawadi tukacheka kidogo.

"Njoo sasa JC unifundishe," kakaongea kwa msisitizo.

Bi Zawadi akasema, "Haya baba, kazi kwako."

"Ahah... sawa, asante cheupe wangu."

"Tunaanza kujiandaa saa ngapi sasa? Yaani, tuondoke saa ngapi?" Bi Zawadi akauliza.

"Tutaondoka kwenye saa tisa. Kuna usafiri nime..."

"JC!" Mamu akaniita kwa njia fulani ya lazima kwa kudeka.

"Eh, ngoja niwahi. Ila saa tisa tunaondoka..." nikamwambia hivyo Bi Zawadi huku nikimkimbia.

Akacheka kidogo wakati nilipokuwa nimemfikia Mariam hapo dining, nami nikakaa pembeni yake na kuanza kumwelekeza hivi na vile, na mama yake mkubwa akawa amerudi chumbani kwake.

★★

Nimekaa na Mariam hapo nikimfundisha mambo kadhaa kwenye lugha ya kiingereza, na niliona namna ambavyo akili yake ilizidi kuwa nyepesi kila dakika. Alishika vitu upesi, na najua hiyo ilikuwa kwa sababu tayari alikuwa anavijua, sema tu alikuwa amesahau. Sasa ndiyo tulikuwa kwenye daraja la kuvivusha zaidi hivyo vitu ili viingie kwenye ubongo wake kwa mara nyingine tena na kutomwondoka kabisa.

Tesha na Bi Jamila walikuwa wamesharudi kutoka kutembea kidogo, mama huyo akiwa amehitaji zoezi hilo dogo kwa ajili ya maandalizi ya kuondoka baadaye kwenda matembezi huko ambako ningewapeleka. Shadya hangeweza kuja nasi kutokana na kuwa sehemu nyingine kwa leo, ndiyo maana sikumkuta hata na hapa pia. Tesha alikuwa na hamu na haya matembezi maana alielewa ni namna gani Sinza ilivyokuwa na watoto wakali, kama kawaida akili yake ikiwa hapo tu, kwa hiyo eti alikuwa amepanga kupendeza haswa.

Nilikuwa bado nikifikiria kuhusu suala aliloniambia Bi Zawadi kuhusu Miryam. Inaonekana kulikuwa na kitu kipya kilichomsumbua bibie, labda kweli ingekuwa ni masuala ya kazi, lakini kitu tu kujua aliondoka akiwa hana raha kilininyima amani. Nikawa nataka kujua endapo kama ningeweza kusaidia kwa lolote lile, na labda ningempa hiyo ofa baadaye tukishakutana ikiwa bado angekuwa hajapata suluhisho kwa tatizo lake.

Hangekuwa mgumu mno kukubali msaada wangu kama ilivyokuwa kipindi kile, kwa sababu sasa hivi aliniona kama rafiki, na mimi hisia zangu kumwelekea ndiyo zingenifanya nijitoe kwa lolote kwa ajili yake mpaka afanikiwe kutatua shida zake. Kwa hiyo matembezi haya niliyokuwa nimepanga tayari yangeifanya siku yetu iishie pazuri sana, na hivyo mikazo yoyote ambayo malkia wa moyo wangu alikuwa akiipitia ingeweza kupungua uzito kwa furaha ambayo angepata akiwa pamoja nasi. Napenda kumwita hivyo!

Ikiwa ndiyo imeshafika mida ya saa saba mchana, nikawa nimepigiwa simu na rafiki yangu Bobo. Bobo bwana alikuwa anataka kuniona, akisema kuna kitu cha muhimu alihitaji kuzungumza nami maana kilikuwa kinamsumbua, na alikuwa hapo Masai tu ametulia hivyo niende kumwona. Nikaweka wazi kwamba sikuwa na muda mrefu sana maana nilihitaji kuwa sehemu nyingine, na yeye akasema haingechukua muda mrefu; maongezi mafupi tu.

Kwa muda huu, mama wakubwa walikuwa wakijiandaa huko pamoja na Mariam pia, na mimi na Tesha tulikuwa sebuleni tu. Baada ya Bobo kukata simu nikamwambia Tesha kuwa naenda hapo nje kukutana na jamaa maana amesema kuna ishu ya muhimu alitaka kuzungumza pamoja nami, naye akasema haina shida, yeye pia angetumia huo muda kuanza kujiandaa. Nilikuwa nimewaambia kwamba nimekodi usafiri ambao ungetupeleka moja kwa moja mpaka huko Sinza, na ungefika huku kwenye saa tisa, ndiyo sababu wote walikuwa wanachangamka.

Hivyo nikatoka hapo na kwenda mpaka Masai, jua likiwa kali kinoma, na nilipofika, hawakuwa wameanza shughuli zao bado. Hakukuwa na watu zaidi ya wahusika wa kuendesha biashara katika maandalizi yao, na Bobo alikuwa amekaa pale pale ambapo tulikaa ile juzi kwenye mechi ya Simba na Yanga pamoja na wakina Miryam. Alikuwa amevaa T-shirt ya kijivu na suruali nyeusi ya jeans, huku kofia nyeupe ikificha uso wake kiasi.

Nikaenda mpaka hapo na kusalimiana naye kirafiki, kisha nikakaa pembeni yake na kusema, "Uko poa mwanetu?"

"Eeh, kwa nini nisiwe poa?" akauliza pia.

"Simu yako ya ghafla imenifanya nihisi labda umevurugwa, nimekuja nakimbia."

Akacheka na kusema, "Mbona sioni jasho?"

"Ah, sitokagi jasho..."

"Hah... hakuna mtu wa hivyo bana, unazingua."

"Nambie mtu wangu. Mishe niaje?"

"Fresh. Mwanetu na wewe una michongo ya ukweli siku hizi, hutulii sehemu moja..."

"Eeh, michongo lazima. Nitaishije mjini sa' nisipo-hustle, we' vipi?"

"Ahahahah... hata me naona. Bado unamla Bertha?" akauliza.

"Well... sijui hata nikwambiaje. Analika, lakini..."

"Siyo kwamba ni wa kumeza?"

Akanifanya nicheke kidogo na kusema,"Kidogo umeelekea kwenyewe, maana siyo kwamba anatemwa."

"Ahah... sawa. Uko vizuri mwanangu," akasema hivyo kwa njia fulani ya huzuni hivi.

"Vipi wewe? Salome wako amekutema au?" nikamuuliza.

"Aa, kale kademu? Me ndo' nimekatema," akasema hivyo.

"Ih? Lini tena?"

"Hiyo hiyo Jumapili, kabla ya mechi."

"Eh! Yaani umemtambulisha kwangu Jumamosi, halafu Jumapili ukamtema? We' kweli Bobo!" nikamwambia hivyo.

Akacheka sana na kugonga kiganja chake kwenye changu, naye akasema, "Kijinga tu kile. Kilikuwa kinanipotezea time... unajua huwa havitulii."

"We' umetulia kwani?" nikampa suto.

"Ah... ndo' nilichokuitia mwanangu," akasema hivyo.

"Nini? Unataka nikutafutie wa kukutuliza?"

Akasema, "Nimeshampata. Oya, JC... huyu mwanamke nimemwelewa sana. Sana yaani mwanangu."

"Wee! Usiniambie... dem mama, nini?" nikamsemesha kizembe.

"Siyo mchezo kaka, niko serious yaani. Hawa watoto wadogo-wadogo, sitafika popote. Nahitaji mwanamke wa kutulia naye... na ndo' huyu nimeshamwona atakayefaa. Perfect yaani," akaniambia hivyo.

"Okay. Fresh kaka, mawazo kuntu. Na... nadhani unaniambia hivyo kwa sababu huyo mwanamke namjua, si ndiyo?"

"Ee, unamjua. Ndiyo maana nataka tuchonge... maana nakuwa naona kama ashanipiga chini..."

"Ni... ahah, ashakupigaje chini wakati hata hujamtokea? We'... ni nani kwanza?"

"Ankia."

"Wewee! Hahahah..." nikajikuta nacheka tu.

"Si umeona? Lazima ucheke..." akasema hivyo.

"Ahahah... hamna, nimefurahi tu. Yaani... umemwelewa Ankia kihivyo kweli, ama unataka kula tu?"

"Nimempenda, JC. Sikutanii yaani," akaniambia hivyo kwa hisia.

"Dah! Mwambie sasa... mtoe hata anywe bia na nini, mwanamke independent yule, kwa hiyo uongee naye na kumtendea kama mwanaume independent pia."

"Hiyo siyo shida. Nataka tu mwanga halisi..."

"Mwanga wa nini?"

"Uliniambiaga ulishamla," akasema hivyo.

"Eh! Ahee. Well... ile ilikuwa tu... si unajua yaani..."

"Naelewa, ila hiyo ndiyo point yangu. Nataka kujua kama yuko easy kihivyo, kiasi kwamba atatoka na mwanaume yeyote kama JC tu ulivyokuja ukampagawisha, mkalala..."

"Siyo hivyo..."

"... ama kama, yaani anaweza kuwa mwaminifu ama vipi? Maana sikutanii bro, natafuta kutulia sa'hivi," akaniambia hivyo.

Niliona yuko serious, kwa hiyo nikamwambia, "Sawa. Nimekuelewa. Yaani... Ankia ni mwanamke aliyetulia. Sana. Sawa? Anajua kutulia. La muhimu awe amekupenda. Akikupenda, we' mwenyewe utafurahia. Yaani ni kimoja. Mimi nilikuwa yule mtu wa kurukaruka sana, si unajua? Nikaona anataka tuzame, kwa hiyo nikamwambia sipo hivyo, mapema kabisa ili asije kuumia. Yaani ni mwanamke ambaye akikupenda, amekupenda, kamaliza. Kitakachobaki yaani itakuwa labda ni wewe tu ndiyo umuumize..."

"Kumbe?"

"Uhakika. Kwa hiyo Bobo... me sa'hivi nimeshapigilia msumari uhusiano wangu pamoja naye iwe kama kaka na dada yaani, na toka hapo, katulia zake mwenyewe yaani kama hana mpango. Kwa hiyo inabidi uwahi, halafu... uende na swaga za uhakika aone upo serious... kuna majamaa yameshaanza kummendea," nikamwambia hivyo.

"Dah! Basi kaka, me kweli nataka nimsemeshe. Nimefikiria sana yaani..." akaniambia hivyo.

"Jaribu. Ongea naye... bangi weka pembeni yaani, najua atataka mwanaume anayejielewa..."

"Uliniona lini navuta, we' fala nini?" akanisemesha hivyo na kucheka kidogo.

"Ahahahah... haya kazi kwako. Ila... kwanza umeanza kumwangalia kama hivyo kutokea lini?" nikamuuliza.

"Ile siku, juzi, wale wajinga walipotukamata..."

"Aaaa... ile juzi..."

"Eeeh. Alivyokuwa anawatolea mapovu yaani nilimwelewa sana."

"Unapenda hivyo?"

"Eeh, yaani... mwanamke anayejua ku-fight kutetea haki hata kama anapigana na askari... ni mzuri sana. Napenda niwe na mwanamke wa hivyo maana atapambania familia yetu kwa ujasiri kama huo," Bobo akafunguka namna hiyo.

Nikampiga ngumi kiasi begani na kusema, "Hapo ndo' umeondoa bangi sasa. Ongea na Ankia kwa njia hiyo hiyo aone kile unachotaka na unachoweza kumpa pia, na atakachoamua, chochote kile... uwe tayari kukipokea yaani."

"Fact mwanangu," akasema hivyo.

"Na ikitokea akakukubali usije ukafanya ujinga! Kaka zake tuko hapa," nikamtania.

"Eheh... eti kaka yake, 'akati ushamlamba lile shundu!"

"Ahahah... na ni la ukweli!" nikamwambia hivyo.

"Fala wewe!" akasema hivyo.

Sote tukacheka kidogo na utani mwingine kuendeleza, mpaka inaingia saa nane bado nikawa hapo Masai, ndiyo nikamuaga jamaa na kuelekea kwa Ankia sasa ili nijiandae pia. Inaonekana na Ankia angekuwa na jambo jipya la kufikiria kuanzia sasa ikiwa Bobo angemtokea, na nisingemwambia chochote mpaka wakati ambao jamaa angepiga hatua kwake. Kwa hiyo mimi na mwana tukawa kwenye usawa wa kutaka kuwafikishia hisia zetu wanawake tuliowapenda, ilisisimua mno!

★★

Maandalizi yakakamilika bwana. Mzee mzima nikavaa zangu T-shirt jeusi lenye mikono mirefu, lililokuwa jipya na hii ikiwa ndiyo mara ya kwanza kulivaa. Rangi nyeusi iliendana vizuri sana na rangi ya ngozi yangu, kwa hiyo nilihakikisha najiweka fresh zaidi kimwonekano kuanzia utosini mpaka vidoleni. Suruali ya jeans ya samawati pamoja na sneaker nyeupe chini zilikamilisha mwonekano wangu, bila kusahau saa yangu maridadi mkononi. Bastola isingenihusu kwa leo. Nilihisi amani.

Ankia alikuwa amesharejea pia na kwenda kuoga fasta utadhani alikuwa ameambiwa anaachwa na treni. Akavalia nguo nyepesi kwa juu, kama T-shirt ya kijani laini lenye maneno "Supreme" kifuani (zile zinazokuwa ndefu, halafu pembeni kwenye hips zinakuwa kama zimechanwa na kuunganikia kiunoni), suruali nyeusi ya skinny iliyomchora huko nyuma, wee! Akavaa na ndala nyeupe za kike huku akibebelea pochi ndogo mkononi, na nywele zake alikuwa amezichana kabisa na kuwekea tiara yenye rangi ya njano kwa mbele kichwani. Alipendeza.

Tukatoka, tukafunga nyumba, kisha tukaelekea kwa kina Tesha. Tayari jamaa, mama wakubwa, na Mariam walikuwa wameshajivika mavazi mazuri yaliyowapendezesha, mama wakubwa wakivaa kimama zaidi, Tesha kisharobaro zaidi kwa Manga nyeupe na suruali ya jeans iliyo na mtindo wa kuchanika-chanika, huku Mariam akivalia gauni safi na refu la blue mchanganyiko na nyeupe, na nywele zake laini akiwa amesukwa kwa mkono njia tano sijui sita na kuvaa kitambaa mbele ya paji la uso wake mpaka nyuma ya kichwa.

Mariam alionekana kweli kuwa mwanadada zaidi ya jinsi ambavyo alikuwa mtoto kwa ndani, na kutoka kwake leo ingekuwa rudio la kuwafanya wenye kumtazama wamtazame haswa. Alikuwa mzuri kama Miryam yaani, na najua muda si mrefu angeweza tena kuitafuta njia yake katikati ya ulimwengu wa nje uliomzunguka. Matembezi haya yalikuwa sehemu nzuri ya kuanzisha hilo na kuliendeleza zaidi.

Hivyo kila kitu kikiwa kimeachwa kimpangilio hapo, sote kwa pamoja tukaondoka. Ilikuwa rahisi kwa wengi waliofahamiana na akina Bi Zawadi hapo mtaani kuwasemesha na kuwasifia kuwa wamependeza na wao kuwajibu vizuri, lakini mimi na Tesha tulitembea mbele ya wanawake kama vile hatuwajali. Sikutaka niwe na shobo kwa wengi bado hata kama nilikuwa pamoja na hawa marafiki zangu, yaani ndiyo uliokuwa mtindo wangu. Mwendo wa taratibu tu, mpaka tukawa tumefika hapo Mzinga barabarani, na angalau jua lilikuwa limefunikwa kwa mawingu wakati huu.

Gari ambalo nilikuwa nimekodi tayari lilikuwa hapo likitusubiri, na mama wakubwa hawakuwa wametarajia ingekuwa ni Noah nzuri sana, wakiwa wamefikiri nilikodi taxi labda. Kwa hiyo wakaingia, mimi nikikaa na Mariam, mama wakubwa, pamoja na Ankia huku siti za nyuma, naye Tesha akakaa huko mbele na dereva.

Hii ilikuwa kama Uber tu, ingawa niliiagiza kutokea huko huko Sinza maana huyu dereva nilimfahamu, kwa hiyo ilikuwa rahisi kwake kuja mpaka huku kwa kuwa alijua sikuwa mbabaishi; angelipwa vizuri. Mariam alionekana kuwa tayari kutalii mazingira ya sehemu nyingine ya mbali baada ya kipindi kirefu kuwa kimepita akiwa nyumbani tu, na safari ya kuelekea Sinza ikaanza.

★★

Safari ya kuelekea huko Sinza bwana ikawa imetufikisha maeneo hayo kupita hadi Makumbusho na kusonga mbele zaidi. Wapendwa wangu hawa walifurahia sana kuwa nje kama hivi, maeneo yenye majengo maridadi na mifumo iliyoonekana kuwa ya hali ya juu kwa nchi yetu, na Mariam ndiye aliyefurahia zaidi na kuulizia hicho ni nini, kile ni nini, karibia kila mara. Binti hakuwahi kufika huku kabla, ama labda aliwahi lakini hakukumbuka, kwa hiyo ilikuwa nafasi nzuri kumwonyesha vitu vingi na kumwelekeza kwa mengi pia.

Imefika saa kumi dakika za mapema, tukawa tumeingia eneo fulani ukiwa unaelekea Mbezi ama Tegeta hapo kati, wanapaita Mbezi Jogoo, na ndiko kulipokuwa na hiyo sehemu niliyopanga kuwapeleka marafiki zangu. Dereva akaliingiza gari eneo la maegesho nje ya hoteli nzuri ya kitalii (resort), isiyokuwa ghorofa wala nini, kawaida tu ingawa ilisambaa kwa eneo kubwa, nasi ndiyo tukashuka hapo. Nikawa nimemlipa jamaa ya kwanza na kumruhusu aondoke, kisha wakati ambao tungemaliza ishu zetu ningemwita tena. Akasepa.

Hoteli hii iliitwa Viva, ikiwa na mwonekano mzuri kwa kujengewa mbao nene kuizunguka zaidi ya matofali hapa au kule, ikiwa na yale madari ya nyasi ngumu na vijumba vidogo-vidogo vya aina hiyo hiyo kwa ajili ya wageni au wateja, sehemu pana ya ndani yenye meza na viti vingi, bar na kaunta refu huko mbele, sehemu yenye swimming pool mbele zaidi, na ndiyo lingefata jengo lililobeba vyumba vya kulala wageni.

Ilikuwa maridadi, wengi waliofika hapo walikuwa watu wenye pesa, na kwa leo hakukuwa na watu wengi sana kwa muda huo tuliofika kwa hiyo palitulia, na ndiyo maana niliamua kuwaleta hawa huku. Palitulia sana. Tukapata meza ndefu ya kukaa kutoshea "familia" nzima, na hatukusahau kumtunzia siti bibie Miryam pia, kisha nikaagiza visinia viwili kudadeki! Na juisi za kupoza koo kwanza! Tulikuwa tumeshawasiliana na Miryam, nikimtumia anwani na namna ya kufika huku, na yeye akawa ameniambia yuko njiani. Msisimko!

Kwa hiyo zikafata story za hapa na pale, Bi Zawadi na Bi Jamila wakionekana kustareheka, na Mariam akiangalia mazingira ya hapa na kule, kisha ndiyo kisinia namba moja kikawa kimeletwa. We! Msosi kama wote yaani. Masoseji, manyama ya ng'ombe, kuku, pweza, mbuzi, chips yai, matunda yaliyokatwa-katwa, samaki, ubwabwa, michuzi, yaani ujazo! Na matomato na mapilipili pembeni, raa! Bila kusubiri filimbi ipigwe, kandanda ya makamuzi ikaanza.

Tulikula kwa raha zetu yaani, msosi ulikuwa wa maana, mpaka inafika saa kumi na moja na nusu hivi jioni, ndiyo bibie Miryam akawa amefika. Ndugu zake walifurahi kweli, hata Mariam akanyanyuka na kwenda kumkumbatia utadhani alikuwa mama yake mzazi vile. Nilijikuta nikibaki kumtazama tu huyu mwanamke, kwa upendo mwingi sana.

Naona leo alikuwa ameenda kazini kwake akiwa amevalia T-shirt jekundu la mikono mifupi pamoja na suruali nyeusi iliyombana vyema, akionyesha unono wake usiofichika hata kama angekuwa amevaa pana. Nywele zake za kusukwa alikuwa amezibana kisogoni na kuziachia kiasi zimwagikie mgongoni, naye alivaa tabasamu mwanana usoni pia ambalo liliongezea urembo wake urembo maradufu. Hata kama angekuwa na stress za kazini, kweli kuja hapa kungeziondoa.

Kwa hiyo akaketi pamoja nasi, na alikuwa amefika kwenye muda mwafaka ambao kisinia cha pili kikaletwa. Sisi wengine tayari tulikuwa tumeshaanza kushiba, kwa hiyo tukamwambia hilo sinia la pili alipaswa kulimaliza lote. Alifurahia utani mwingi kutoka kwangu, kwa Ankia, na Tesha pia, na aisee kumwangalia huyu mwanamke akitabasamu ama kucheka kulinipa raha ya ndani sana moyoni.

Alipendeza mno kufurahia maisha, basi tu yaani kama ujuavyo maisha hayako kihaki kwa kila mmoja, kwa hiyo changamoto alizokuwa amepitia zilimfanya asiyafurahie kivile na kuwa jinsi alivyokuwa. Nilitamani sana ije siku ambayo mimi ndiyo ningemwondolea mambo yote yaliyokuwa yakimsumbua, hata kama sijui ikiwa kuna mambo yalikuwa yanamsumbua. Nilitaka tu kuwepo kwa ajili yake. Kufanya vitu kama hivi na zaidi ambavyo havingeondoa tabasamu usoni kwake daima. Nilikuwa nimempenda Miryam kweli.

Kisinia cha pili hakikwenda mpaka mwisho, kwa hiyo Tesha na ujanja wake akaona aende kutafuta mfuko ili chochote kile kisibaki. Wakati huo, Miryam pia alikuwa ameshashiba, na Ankia akapendekeza tuanze kupiga picha za pamoja kutunza kumbukumbu nzuri za siku hii. Haikupingwa. Tukasogea sehemu ya nje yenye bustani iliyotunzwa vyema na kuanza kupiga picha kwa pamoja, hadi tukaenda upande uliokuwa na bwawa la kuogelea, na Tesha akawa amerejea na mfuko na kutunza vyakula alivyotaka kwenda kukamulia nyumbani.

Wakati Tesha akiwa amekuja kwetu kupiga picha pia, simu yangu ikaita, mpigaji akiwa ni Bertha, nami nikaona nijitenge kwanza ili nikapokee na kumsikiliza. Ikiwa ni saa kumi na mbili iliyoelekea kulikaribisha giza la saa moja sasa, nikatoka hapo mpaka pale nje usawa wa magari yaliyoegeshwa, pick-up ya Miryam ikionekana kuwepo hapo mbele pia, na hakukuwa na watu huku kwa nje kabisa labda tu walioonekana kwa huko barabarani zaidi.

Ndiyo nikawa nimepokea na nikaongea na madam. Alikuwa tu ameni-miss, na kuniuliza kwa nini sikuwa nimemtafuta leo. Nikamwambia kuna harakati za hapa na pale nilikuwa nikifatilia na nini ndiyo maana, naye akaonyesha uelewa na kuniambia kesho nihakikishe ninaenda kwake nikishatoka kule supermarket, nami nikakubaliana na hilo na kuagana naye haraka baada ya kuona bibie Miryam anakuja upande wangu, ndiyo madam akakata simu. Malkia akawa anakuja kwangu!

Taratibu akaendelea kuja tu mpaka aliponifikia na kusimama pembeni yangu, naye akaachia tabasamu hafifu huku akinitazama kwa macho yake mazuri. "Kwa nini unakata simu kila nikikukuta unaongea na 'baby?'" akauliza hivyo.

Akanifanya nicheke kidogo, naye akacheka pia, kisha nikamwambia, "Miryam unanisoma vibaya bwana."

"Kumbe?"

"Eeeh. Huyo baby unayemsemea hayupo," nikamwambia.

"Mmm... kweli?"

"Kabisa."

"Mbona umekuja huku kote sa' kuongea na simu kama siyo baby?" akauliza kiutani.

"Siyo... ni rafiki tu, siyo baby bwana... ahah..." eti nikahisi haya.

"Mmmm... Jayden, una-blush!" Miryam akasema hivyo kusisitiza zaidi.

Na kweli, nilikuwa nina-"blush" hapa, ila dada wa watu hakujua hiyo ilikuwa kwa sababu yake. Nikabaki kutabasamu tu.

"Gharama ya visinia imetoka ngapi?" akaniuliza.

Nikamwangalia usoni kwa njia ya kuhukumu kiasi.

"Ahah... niambie tu, sitafanya protest yoyote," akasema.

Nikamkazia macho kiasi.

"Kweli. Niambie tu," akasema hivyo.

Nikamwambia, "Laki tatu."

Akapandisha nyusi kama kushangaa kiasi, naye akacheka kidogo kwa pumzi na kuangalia pembeni.

Nikasema, "Okay, nahisi protest inakuja..."

Akasema, "Hamna, wala... hamna shida. Najua umetoa kwa kupenda. Nataka tu kusema asante. Asante sana Jayden. Kwa... kwa kila kitu. Nimefurahia sana kuja hapa, japo nimechelewa lakini... nimefurahia."

Aliongea kwa hisia za shukrani kwelikweli, nami nikamwambia, "Usijali Miryam. Tuko pamoja. Familia yako ni kama yangu pia. Napenda kuwaona wanafurahi."

Akatabasamu kiasi na kusema, "Mara nyingi sana umekuja na familia yako hapa, eti?"

"Ah, siyo mara nyingi... sanasana tu kama dada yangu alikuwa na vi-party na nini, ndiyo tungekuja hapa, au na marafiki... ila sijawahi kuja na mama au mzee hapa..." nikamfahamisha.

"Ahaa... na dada yako, Jasmine, anaonekana mtu wa kupenda party eh?"

"We! Sana! Anapenda sana hayo mambo," nikamwambia.

"Si kama wewe tu? Mtoto wa kishua," akanitania.

"Ahahah... usiniite hivyo bwana..."

"Ahahahah... sawa. Kwa hiyo mna memory nzuri sana hapa eti?" akauliza.

"Eeh. Ahahah... ngoja nikuchekeshe. Kuna rafiki yangu tunamwita Simba, yaani mambo yake, kama Tesha tu..."

Akatabasamu kiasi na kusema, "Enhe..."

"Ilikuwa birthday ya Jasmine. Tukaja hapa. Sasa... alikuwa ameenda uani, amebanwa, kala sanaaa... akawa ameingia kwenye mlango wa choo kilichopigwa marufuku, akashusha haja..."

"Eh!" akasema hivyo kwa sauti ya chini.

"Ahahahah... wasimamizi wakamkuta. Faini ilikuwa elfu hamsini, afu' hakuwa hata na mia. Unajua alichofanya?"

"Akafanyaje?"

"Akaanza kuigiza kwamba ye' kiziwi, hasikii na ni bubu. Akawa anaguna guna tu, anatoa ishara za kuonewa huruma mpaka ikabidi wamwache tu... ahahahah... Miryam, tulicheka! Alikuja kurudi kwetu bado anaendelea kuigiza bubu maana kama wale watu wangemgundua alikuwa amewauza, hela angetoa tu...."

Wakati nikiwa namwelezea bibie hicho kisa, nilikuwa natoa ishara nyingi kwa mikono na mwili kutokana na hisia ya kuchangamka iliyochochewa na kumsikia akicheka kwa furaha sana. Alifurahia sana hicho kisa kiasi kwamba aliendelea kucheka tu, na mimi ndiyo nikaendelea kukielezea kwa njia zilizomfanya afurahie zaidi.

Nikawa nimegeukia upande mwingine nilipokuwa namwonyesha namna ambavyo kipindi hicho huyo Simba aliigiza kutembea kwa njia fulani kama mlemavu ili aonewe huruma zaidi, ndiyo sauti tamu ya Miryam akiwa anacheka ikakoma ghafla. Mimi nikiwa natabasamu, nikageuka kumwangalia usoni na kushtuka kiasi moyoni baada ya kuona jambo fulani ambalo sikuwa nimetarajia kabisa.

"Mambo vipi... JC?"

Swali hilo halikuulizwa na Miryam, bali mtu aliyekuwa amesimama nyuma yake. Tena nikisema nyuma yake, yaani namaanisha alikuwa amegusanisha mwili wake karibu zaidi na mwili wa Miryam kutokea nyuma.

Mtu huyu alikuwa ni mwanaume mrefu, mweusi, ambaye alikuwa mwenye mwili mkubwa kiasi cha kuwa mnene, akivalia sweta zito jeusi lenye kufunika kichwa chake kuniruhusu kuona tu uso wake wenye ndevu nyingi kutokea kwenye timba uliokuwa makini vibaya mno. Kumtazama kwa umakini usoni kukawa kumenifanya nimtambue. Alikuwa ndiyo yule jamaa aliyenifatilia kule Kariakoo ile Ijumaa kabla ya mimi kufanikiwa kumpiga chenga. Ndiyo huyu aliyekuwa amemshika Miryam sasa.

Kuangalia vizuri jinsi jamaa alivyokuwa amekunjia mkono wake mmoja usawa wa kiuno chake Miryam, ndiyo nikawa nimeona kisu kifupi na kinene kiganjani mwake, ambacho alikigusisha kwenye nyonga ya mwanamke huyo! Ai kudadadadadeki!

Pigo moja zito la rohoni likafanya nihisi kama vile mwili wangu wote unarusha damu huku na huko, kwa sababu niliingiwa na hisi kali sana ya hofu. Miryam alikuwa amesimama kwa kutulia, akiniangalia machoni kwa mkazo ulioonyesha hisia kubwa ya hofu iliyokuwa imemwingia, na huyo mwanaume akaweka kiganja chake kingine usawa wa shingo ya Miryam kwa njia ya kuikaba kiasi kutokea nyuma.

"Naona uko una-enjoy kidogo na watu wako... leo akaunti itakuwa imesoma fresh..."

Mwanaume huyo akasema hivyo. Alikuwa anaongea kwa njia fulani kama vile anataka sana nimwogope, besi nzito, akivuta maneno yake na kuniangalia kikatili eti, nami nikaonyesha kutaka kupiga hatua kumfata....

"Aisee! Tulia hapo hapo!" akaniambia hivyo kwa sauti ya chini.

Nikaganda na kuendelea kumwangalia kwa umakini.

"Kama umecheza na wengi, jua kwamba kwangu hautakuwa na hiyo nafasi. Jaribu kupiga hatua uone nitamfanya nini huyu mwanamke!" akaongea hivyo kwa sauti tulivu.

Aliposema hivyo, niliona akizidi kukikandamizia kisu kwenye nyonga ya Miryam huku akiikandamiza shingo yake kwa nguvu na mkono wake mwingine, naye Miryam akapandwa na woga zaidi na kuniangalia kwa hofu huku akipumua haraka-haraka kiasi.

"E e e e e... bro, tulia. Usifike huko," nikamwambia hivyo kwa sauti ya chini kwa njia ya kumtuliza.

Nilikuwa natamani atokee hata mtu mwingine hapo upesi ili nijaribu kufanya jambo fulani haraka, lakini hakuna nafsi yoyote iliyosogea upande huu. Huyu jamaa akawa ananiangalia kwa utulivu, lakini kikatili. Sijui hata alikuwa ametokea wapi ghafla namna hii!

Nikamuuliza, "We' ni nani? Unataka nini... pesa?"

Akachezesha midomo yake taratibu kama kuonyesha amekerwa, naye akasema, "Nataka tuongee."

Nikakunja uso kimaswali kiasi.

"Unaliona lile gari jeusi?" akaniuliza hivyo.

Nikatazama mpaka upande wa barabarani kule na kuona gari jeusi lenye kung'aa upya kwelikweli, aina ya Toyota Vanguard, nami nikamwangalia jamaa.

"Ndani ya dakika tano uwe umefika na kuingia humo..." akasema hivyo.

Nikawa nimeshagundua mwanaume huyu alikuwa ametumwa na nani, nami nikawa namwangalia kwa mkazo tu.

Akalisogelea shavu la Miryam karibu zaidi na kusema, "La sivyo... huyu mwanamke atakufa... na wote uliokuja nao. Usitake kujua ni jinsi gani... jua tu kwamba hilo ni uhakika."

Miryam alikuwa amefumba macho sasa, akijikaza kutokana na kuhisi maumivu sehemu fulani mwilini mwake.

Nikakaza meno yangu kwa nguvu nikihisi hasira sana, nami nikamwambia jamaa, "Sawa. Nakuja."

Mwanaume huyo akatulia kidogo akinitazama kwa utulivu makini, kisha akamwachia Miryam na kumsukuma kiasi mbele. Miryam akakaribia kuangukia upande niliokuwa nimesimama, nami nikamwahi na kuukumbatia mwili wake ili asidondoke, na nilijua huyo jamaa alikuwa ameshaanza kuondoka kuelekea huko ambako gari lile lilikuwa.

Miryam akawa anapumua kwa presha kiasi kifuani kwangu, nami nikamwachia taratibu ili nimtulize kwa maneno. Lakini nilipomwangalia usoni, nikakuta machozi yakimtoka kabisa huku akipumua haraka-haraka kwa hofu, nami nikaingiwa na simanzi na kumkumbatia tena; nikificha kichwa chake kifuani kwangu. Akawa amenikumbatia kwa nguvu pia huku akivuta nguo yangu mgongoni, nami kiukweli nilihangaishwa sana moyoni na hili tukio. Amani ikawa imevurugika tena!

Nikiwa nimeendelea kumshikilia, nikasema, "Samahani Miryam. Naomba nisamehe kwa... hhh... tafadhali naomba unisamehe..."

Nikashindwa hata kuelezea namna ambavyo nilijihisi vibaya sana, nami nikamwachia tena taratibu na kuanza kumfuta machozi.

"Amekuumiza? Umeumia hapa?" nikamuuliza hivyo huku nikimwangalia usawa wa ubavu wake.

Akatikisa kichwa kukanusha hilo huku akitazama chini.

Nikawa bado nimeishika shingo yake huku nikimwangalia kwa hisia sana, nami nikamwambia, "Nahitaji kwenda."

Akaniangalia usoni.

"Utawaambia wengine... nimepatwa na dharura, tutaonana baadaye... sawa?" nikamsemesha kwa sauti ya chini.

Sikujua angesema nini kwa wengine, ila hapa nilitakiwa kujali muda niliopewa, hivyo sikusubiri anijibu, badala yake nikamwachia taratibu shingoni ili niondoke. Lakini akaushika mkono wangu na kuukaza zaidi kama anaurejesha shingoni kwake, nami nikamtazama machoni kwa umakini.

Akaanza kusema, "Huyo mwanaume ni nani? Kwa nini uende hu... usi... usiende huko Jayden. Tuwapigie mapolisi kama hao ndiyo wale watu... mpigie Ramadh...."

Nikaishika tena shingo yake na kusema, "Hapana Miryam, acha niende... usijali, nitakuwa sawa. Najua jinsi ya kushughulika navyo hivi vitu, wala usiwaze. Ondokeni hapa upesi... kwa uangalifu. Nitahakikisha hamna mtu anawasumbua, sawa?"

"Lakini wakikuumiza je?" akauliza hivyo kwa sauti yake yenye kujali.

"Hawana hiyo jeuri. Nitarudi nikiwa sawa Miryam," nikamwambia hivyo.

Akaukaza mkono wangu na kuuliza, "Promise?"

Nikatulia kidogo nikiyaangalia macho yake mazuri kwa hisia sana, nami nikamwambia, "Promise."

Akabaki akinitazama kwa hisia za wasiwasi mwingi, nami nikamwachia na kutoa simu yangu mfukoni, kisha nikampatia kiganjani. Alinitazama kwa kutoelewa kwa nini nilimpa simu yangu, lakini sikubaki kuelezea maana yangu na kuanza tu kuelekea huko juu.

Sijui dakika tano zilikuwa zimeisha? Sikuona shida yoyote kwa sababu nilikuwa naenda, na nilikuwa nina hasira sana. Ile hasira yaani inayokufanya utamani kuuona utumbo wa mtu unatoka ndani ya mwili wake, ndiyo unaridhika sasa. Huyo bwege alitoa wapi jeuri ya kumshika Miryam namna ile? Kutishia maisha yake mbele yangu? Ah, aisee! Hakujua, yaani alikuwa amenichokonolea sehemu mbaya vibaya mno!

Nikaendelea kulifuata gari hilo mpaka nilipolifikia karibu, na usawa wa milango yake mlango wa nyuma ukawa umefunguliwa kutokea ndani. Nikageuka nyuma na kumtazama Miryam, kukuta mwanamke huyo akiwa amesimama pale nilipokuwa nimemwacha, nami nikampa ishara kwa kidole chinichini kuwa awahi kuwaondoa ndugu zake hapo, naye akatikisa kichwa kukubali kisha akarudi kule tulikowaacha wengine.

Nikaushika mlango huo wa gari na kuingia humo, na niliyekuta amekaa hakuwa mwingine ila mheshimiwa Sudi mwenyewe! Kama nilivyopigia picha, ni huyu pimbi ndiyo alikuwa amemwagiza mbwa wake anifatilie siku ile huko Kariakoo, na pia aje hapa na kutishia maisha ya Miryam ili kuipata "attention" yangu, na kweli akawa ameipata.

Nikatazama na mbele ya gari kumwangalia huyo jamaa aliyekuwa ameagizwa kunifata muda mfupi nyuma, akiwa ndiyo dereva wa gari hili pia, nami nikakaa sitini vizuri na kuufunga mlango kwa nguvu. Sudi akatabasamu kiasi na kuangalia mbele, na gari hilo likaondolewa hapo kuelekea safari ya kwenda nisikokujua.






★★★★★★★★★

ITAENDELEA

★★★★★★★★★


Full Story WhatsApp or inbox

Whatsapp +255 678 017 280
 
MIMI NA MIMI 2

A Story by Elton Tonny

Familia, Urafiki, Mapenzi, Kazi, Siri, Tamaa, Hila, Usaliti, Ukatili, Mauaji, Mambo Yasiyotazamiwa

R-rated 18+

Enjoy!


(NMEI-REPOST HAPA HII SEHEMU MAANA ILIFUTIKA)


★★★★★★★★★★★★★★★★★

SEHEMU YA KUMI NA MBILI

★★★★★★★★★★★★★★★★★


Kwa sababu ya kutaka kufika huko upesi sana, nikaamua kuchukua bodaboda mpaka kufikia Rangi Tatu, kisha kutokea hapo nikapanda nyingine na kuomba nipelekwe moja kwa moja hadi Makumbusho huko kwa nauli aliyoona inatosha. Upesi boda ikaanza kupepea, nikiwa bado najaribu kumpigia Bertha na hata kumtumia ujumbe, lakini sikupata itikio lolote. Sijui nini kilikuwa kikiendelea!

Bodaboda ilitembea kwa kasi haswa, yaani maeneo mengi tuliyapita upesi sana. Tukiwa bado mwendoni kuelekea maeneo ya Keko, simu yangu ikaanza kuita, na mpigaji hakuwa mwingine ila mzee wangu, Mr. Frank Manyanza. Oh, inaonekana alikuwa amepata kuziona simu zangu na sasa ndiyo akawa ameweza kunitafuta, kwa hiyo nikaamua kupokea haraka ili tuongee japo kwa ufupi.

"Mzee, halloo..." nikasema hivyo simu ikiwa sikioni.

"Eeh, vipi? Za huko?" akasikika.

"Safi. Pole na kazi..."

"Asante. Hizo ni kelele za nini?"

"Aa... niko kwenye boda, kuna sehemu naelekea hapo mbele..."

"Ahaa... sawa. Niambie, nimepata window ndogo ya kuzungumza," akasema hivyo.

"Yeah. Ni kuhusu ile ishu niliyokuja kuzungumza nawe siku ile ofisini. Unaikumbuka?"

"Ee, nakumbuka... vipi?"

"Nasikia sasa hivi mko... mnataka kutaifisha mali za yule dada, ili mrudishe pesa zenu mzee. Ni kweli?" nikamuuliza.

"Kutaifisha? J unakosea ukisema hivyo. Na nilikwambia umlete huyo mwanamke huku ili nizungumze naye, lakini inaonekana haikuwezekana, na sasa kuna vitu vimetokea vikasababisha iamuliwe hizo pesa zirudi..."

"Lakini mwizi wa hizo hela yuko jela mzee, huyo dada hahusiki..."

"Ndiyo, tatizo ni kwamba jamaa alikuwa ametoa rehani ya nyumba yake na ya huyo mwanamke akisema kwa sababu ndiyo mwenye shamba basi inamhusu pia. Hatutachukua mali zingine na..."

"Mzee ngoja kwanza, nyumba ya huyo mwanamke inatunza familia, sawa? Mkiichukua na kuiuza wataenda wapi? Na siyo fair kwanza kuuza nyumba ile kwa milioni 10 tu, kwa nini wafanye hivyo wakati hana... siyo makosa ya...."

"Nisikilize JC, nisikilize. Hiyo ni mechanism ya kumshawishi atuuzie hilo shamba, kwa sababu sawa, tunaelewa imekwenda vibaya sijui kaka yake alifanya nini, lakini na sisi tumekula hasara nyingi, siyo pesa tu. Muda. Tulikuwa na option nyingi za kuchukua plot zingine lakini sasa hivi zimeshakuwa occupied maana muda umepita tukiamini hilo shamba lake ndiyo tutalichukua. Hakuna plot nzuri zilizo available kwa hilo eneo la mkoa wa Morogoro ambako ndiyo tunataka tujenge tawi ietu, na kama tukilikosa kabisa hilo shamba, basi pesa zinatakiwa ziwe zimerudi haraka ili tubebe kingine sehemu tofauti. Unanielewa?"

"Ndiyo nakuelewa, lakini...."

"Elewa kwamba siyo rahisi kwangu pia, JC. Imagine, kampuni imeshahalalisha haki zote za kuchukua hilo shamba ikiwa pesa haitarudi, sawa? Huyo mwanamke amepewa tu option; aidha akubali kutuachia shamba na tumlipe milioni 15 tena kutoka kwenye mauzo ya nyumba ya kaka yake, au atulipe milioni 10 na hiyo case iende mbali. Imeshasimama namna hiyo mwanangu..." akaniambia hivyo.

"Mliuza mali za Joshua kwa milioni 15?" nikamuuliza.

"Ndiyo. Huoni kwamba ni dili zuri tukimpatia huyo mwanamke hizo pesa akaliachia shamba, kuliko akitoa milioni 10 kwa upuuzi alioufanya ndugu yake?"

"Tatizo HAWEZI kukubali kuwaachia hilo shamba, mzee. Ipo... hhh... ipo tight sana yaani, sijui hata nikuelezeeje..."

Akasema, "JC ikiwa ni hivyo, hakutakuwa na jinsi. Mambo yameshapita hayo, akigoma na asiweze kulipa... tutamnyang'anya shamba kwa force... na hata hiyo nyumba yake pia. Hawa jamaa, wana hiyo nguvu na mahakama itakuwa upande wao, so...."

Nikahisi kuchoka kihisia kabisa.

"Kama huyo mwanamke ni rafiki yako, jaribu kumshawishi aliachie hilo shamba, apate milioni 15 ambazo zitamsaidia kwa mambo mengi. Mwambie asiendekeze kiburi," akasema hivyo.

"Hayuko hivyo mzee..." nikamwambia.

"Well, angalau huo ndiyo msaada naoweza kumpatia, maana nimejitahidi kufanya iwe rahisi hata kwa njia hiyo asije kupoteza kila kitu. Rafiki yako asipotaka kuliachia shamba na asipoweza kulipia hiyo milioni 10 kufikia kesho JC... mambo yatakuwa magumu sana kwake," mzee akasema hivyo.

Dah, aisee! Sijui ndiyo ingekuwaje maana najua kumshawishi Miryam aliachie shamba la Mariam ingekuwa ni utata. Na mzee alikuwa na pointi. Hapo pangekuwa pagumu sana kwa huyo mwanamke endapo kama angebebewa kila kitu chake. Familia yake ingeteseka kwa njia nyingine tena. Joshua alikuwa amemharibia sana huyo dada njia nzuri ya maisha, yaani basi tu. Ilikuwa kama amemwachia mzimu wake umsumbue ingawa hakuwa amekufa!

Baada ya maongezi hayo mafupi, mzee akaona aniage nilipomwonyesha kwamba nimeelewa, na kufikia muda huo tayari tulikuwa tumeingia maeneo ya Makumbusho. Nikamuaga pia na kuweka simu mfukoni, nami nikaanza kumwelekeza boda sehemu ya kupita ili tuelekee huko Victoria ya zamani ambapo hapakuwa mbali sana. Ishu ya Miryam na shamba la Mariam ningekuja kuiangalia tena baadaye, wakati huu nilitaka kwenda kumtoa kwanza Bertha ndani ya pango la nyoka waliotaka kummeza, ikiwa ningekuta bado hawajammeza, na kama mimi pia nisingemezwa.

★★

Bwana, bodaboda akawa amefanikiwa kunifikisha kwenye hilo jengo, eneo na pande moja maridadi zaidi jijini lenye majengo makubwa, barabara safi, harakati na watu walioenda shule yaani, nami nikashuka na kumlipa pesa yake. Akaosha. Nikavuka geti la uzio uliozunguka jengo hili mbele yangu lenye ghorofa ndefu kama nne au tano hivi, na kiuhakika zaidi nikawa nimeliona gari la madam Bertha hapo nje; ile Lexus yake mpya.

Hapa palikuwa kama hospitali, lakini zaidi kliniki kubwa ambayo ndiyo ilikuwa ikianza kukua zaidi. Kulikuwa na pande tatu zilizotengana ingawa kwa jengo moja; ya kwanza mkono wa kushoto ambako ndiyo palikuwa pameshakamilishiwa ujenzi wa kliniki za madaktari waliotoa huduma maalumu kwa wagonjwa binafsi sanasana, ya pili katikati ambayo ilikuwa pana sana ikijengewa zaidi vioo iliyobeba kama duka la madawa ya afya na vifaa maalumu vya hospitali kwa ajili ya wagonjwa, na ya tatu mkono wa kulia, ambako bado hapakuwa pametengenezwa kikamili kuanza kutoa huduma.

Ni upande huo wa tatu ndiyo ambao nilielewa kuwa bila shaka Bertha na wengine wangekuwepo, maana ulikuwa na vyumba vilivyo tupu, vikiwa bado tu havijaanza kutumiwa kwa ajili ya kazi. Yaani hakukuwa na watu. Jengo lote lingeungana baada ya kukamilika kama tu hospitali yoyote ile kubwa ya kibinafsi, na hapo nje kulikuwepo na nyumba ndogo ya wazi kwa ajili ya mlinzi, kukiwepo na mlinzi-askari mmoja ambaye aliniangalia kwa utulivu tu.

Kuona gari la madam Bertha likiwa hapo nje bila lingine kuwepo kukanifanya nitambue kwamba Sudi na ushirika wake haukuwa umefika bado, na sikujua huyo Dotto angekuwa amemweka madam katika hali gani kufikia sasa, kwa hiyo nikampungia tu mkono mlinzi kisalamu nikielewa angekuwa ameshalipwa huyo na kuelekea upande huo wa tatu bila presha, nami nikaanza kuangalia mazingira ya vyumba vya hiyo sehemu ya chini na kukosa nafsi hata moja, kisha nikaanza kupanda ngazi taratibu.

Nikafikia ghorofa ya kwanza, nami nikaingia kwenye vyumba vya huko na kupita kimoja baada ya kingine. Kulikuwa na hali ya ugiza, pakionekana kuwa patupu haswa na papana, milango ya vioo ikiwa imeshawekwa, nami nikamaliza vyumba vyote bila kukutana na nafsi nyingine tena. Kulikuwa na msisimko wa hali ya juu maana nilihisi kama vile naangaliwa yaani, ule utupu si unajua kwa sehemu kama hiyo huku ukielewa kuna baya linaweza kutokea, ulizipaisha kiasi hisia zangu. Nilikuwa jasiri sawa, lakini sikuwa John Wick!

Ngazi za kuelekea ghorofa ya pili zikanihusu, taratibu tu, na sikusikia sauti yoyote ile ya watu hadi nilipofikia ujumba wa huko juu na kuanza kupita chumba kimoja baada ya kingine. Ndiyo nikaanza kusikia sasa sauti kama ya kiatu cha kuchuchumia ikigonga sakafu la vigae kutokea chumba fulani cha mbele, na ilikuwa ngumu kujua kipi maana mwangwi ulisafiri haraka kwa njia iliyochanganya, kwa hiyo nikaitoa bastola yangu mguuni na kuanza kuelekea mbele kwa uangalifu zaidi.

"... ndiyo kama tu kwenye hiyo series, pazuri kweli kutoboa kama hivi... hapa, halafu unayapitisha kwa kutumia hiyo pipe, yenyewe si itakaa... itapita hivi? Eeh... yakiteleza mpaka chini wakati wenyewe wanakuja juu, hakuna nafasi wataweza...."

Nikaanza kuisikia sauti ya madam Bertha akisema maneno hayo, na ikitokea karibu zaidi na nilipokuwa nakaribia kufika, nikajibanza ukutani na kuusogelea muimo wa mlango ambao bado haukuwa umejengewa milango na kuchungulia, ndiyo nikaweza kumwona sasa madam. Alikuwa amesimama mbele zaidi kukaribia ukuta ndani ya chumba hiki kipana, akizungumzia jambo fulani pamoja na Dotto, ambaye alisimama kwa kunipa mgongo usawa huu wa mlangoni nilipokuwa.

Nikajitahidi kuingia taratibu kwa kunyata, na Bertha alipotazama huku na kuniona nikiingia huku bastola ikiwa mikononi, akakunja uso kimaswali, jambo ambalo likafanya Dotto anigeukie. Hapo hapo nikamnyooshea jamaa mguu wa kuku kuelekea kifua chake kwa uhakika wa hali ya juu, naye akashtuka na kurudi nyuma huku akinyanyua mikono yake hewani kiasi.

"HB!" Bertha akaniita hivyo kwa sauti ya chini.

Alikuwa amependeza mwenyewe kama kawaida yake; blauzi nyeupe iliyochanika kimtindo sehemu ya juu kifuani, suruali ngumu nyeusi ya leather iliyombana vyema, na mabuti yake ya kike ya kuchuchumia, nami nikaendelea kumwangalia Dotto kwa umakini bila kushusha mkono wangu wenye bastola kumwelekea.

"Hey... unafanya nini?" Bertha akauliza hivyo.

"Pita huku Dotto! Sogea," nikamwambia hivyo jamaa.

Alikuwa akinitazama kwa macho makini, naye akasogea pembeni huku nikianza kuzunguka kuelekea upande wa madam Bertha, na yeye akasimama usawa wa kona moja kutokea upande wa mlango.

"We' JC... nini hiki unafanya? Mabunduki ya nini asubuhi yote hii?" Bertha akauliza hivyo.

"Madam... najua siyo rahisi kuelewa, lakini naomba uniamini. Hapa umeletwa kwenye mtego. Wanapanga kukuua," nikamwambia hivyo bila kuacha kumtazama Dotto.

"Nini? Nani?" Bertha akauliza.

"Sudi, Dotto, Chalii... madam, unatakiwa kuondoka hapa," nikamwambia.

"We' J... hebu tulia. Nani amekwambia hayo yote? Eh? Are you high?" Bertha akaonekana kutoniamini.

"Sikutanii," nikamwambia hivyo.

"Inaonekana ameonja pafu kumi hii asubuhi..." Dotto akasema hivyo.

"Kaa kimya, mjinga wewe! Nitakupasua, usinichezee!" nikamtishia jamaa.

"Hee, wewe, hebu shusha hiyo! JC? Niangalie. Mbona sikuelewi?" Bertha akauliza hivyo.

Nikamwangalia kwa ufupi na kusema, "Ni mpango wao kukuangusha madam... wanataka kukuua. Hii yote, sijui mkutano... kikao... ni fake. Usipoondoka hapa watakuua. Tena mimi na wewe."

"Haya umeyajuaje?" akauliza.

"Nitakuelezea. Hupaswi kumwamini huyu tena madam, atakusababishia kifo... twende tuondoke," nikamsihi.

"Yaani Dotto... apange na Sudi kuniua mimi?" Bertha akauliza.

"Me mwenyewe namshangaa, huyu mtu wako amekuwaje?" Dotto akajitetea.

"Dotto nitakufumua risasi, hujui tu ni jinsi gani unanikera yaani!" nikamwambia hivyo.

"Nimefanya nini? We' una matatizo? Madam mbona simwelewi huyu..." Dotto akaendelea kunipa kero tu.

"JC, hebu nipe hiyo pistol..." Bertha akaniambia.

"Madam, niamini, naomba tuondoke haraka kabla Sudi hajaja, ni mpango wake na Chalii na Dotto waku...."

"Una ushahidi gani me nataka kumuua madam, eh?"

"Si mlijaribu kunishawishi nijiunge na nyie? Halafu now unajikuta mtakatifu sana?"

"Kama ni hivyo mbona ulikuwa hujamwambia madam..."

"Usinigeuzie tairi na kulizungushia kwangu ukifikiri itakupa...."

"Matairi yanatoka wapi tena? We' umeleweshwa na nani bro? Unakuja na pistol halafu unasema me ndo' nataka kumuua madam? Wakati ni wewe!"

"Dotto usinichefue, nitakuzingua kweli! Ni bora ukae kimya kabla...."

Bertha akayakatisha mabishano kwa kusema, "JC, hebu tulia, nimekwambia nipe hiyo pistol... inaweza ikafyatuka bahati mbaya. Ikitoa kelele hapa itakuwa shida... shusha bastola tuongee vizuri..."

Nikamwangalia madam na kusema, "Hatuna muda wa kuongea madam, ninakuomba... please... naomba tuondoke kabla hao watu hawajaja, nitakuambia, nitakuelezea kila...."

Tatizo moja tu kuendelea kumwangalia Bertha likampa mwanya Dotto kufanya kitu fulani ambacho sikutarajia kabisa baada ya yeye kupiga hatua ndefu kunielekea ghafla. Kabla sijaweza kuitikia vizuri, ile tu macho yangu yametua kwake tayari mwanaume akawa ameikwapua bastola kutoka mkononi mwangu na kurudi nyuma tena huku akiielekeza upande wetu! Aaah... makosa!

Nikawa nimebanwa ukutani na madam Bertha sasa. Aloo! Chuma kikiwa kimetazama upande wetu namna hiyo nilihisi damu ikianza kurukaruka zaidi ya ilivyokuwa inafanya shauri ya ule wasiwasi wa kushika tu bastola, sasa ukawa ni wasiwasi wa kushikiwa bastola. Dotto alikuwa mzoefu inaonekana, maana aliweka uso mtulivu tu na kuikoki bastola vizuri, huku mimi na madam Bertha tukimwangalia kwa umakini sana.

"Dotto... shusha hiyo gun. Kwa nini unaielekeza kwangu? Umekuwaje?" Bertha akamuuliza hivyo.

Dotto akaendelea kutuangalia tu kwa utulivu.

"Nimekwambia madam... hayuko upande wako tena," nikasema hivyo.

"Kumbe ni kweli? Unapanga kuniua... na wakina Sudi?" Bertha akamuuliza jamaa.

Kimya.

"Kwa nini? Nimekufanya nini we' na Sudi? Kwa kipi kilichofanya mpaka uamue kunigeuka?" madam akauliza tena.

Dotto akashika sikio lake kwa kiganja kimoja huku akitunyooshea bastola kwa kingine bado, naye akasema, "Niko nao. Ghorofa ya pili. Njooni."

Inaonekana kulikuwa na kifaa kidogo cha mawasiliano ndani ya sikio lake, na hapo ndiyo alikuwa akiwatumia mawimbi wenzake ili waje huku. Kumbe tayari walikuwepo, ni mimi tu ndiyo nilikuwa nasubiriwa!

"Ndiyo unamwita Sudi? Au Charles?" Bertha akamuuliza.

Dotto akaendelea kubunda tu.

"Ahah... D, hebu acha masihara yako. Shusha hiyo chuma u...."

Bertha akajaribu kupiga hatua huku akisema hivyo, lakini Dotto akaielekeza bastola kwake madam moja kwa moja kwa uhakika na kwa nia isiyo ya utani kuonyesha kwamba angefyatua rusasi. Bertha akarudi nyuma kidogo, na mimi kiukweli nilikuwa nahisi kama vile miguu inataka kumwagika, siyo siri.

Nikamwambia, "Dotto... nisikie. Usifanye hivi... haina maana yoyote kumuua... haitakupa furaha kwa lolote..."

"Mbona yeye imempa furaha sana kuwaua wengine? Kwa nini mimi nisifurahie kumuua yeye?" Dotto akasema hivyo.

"Ahah... kwa hiyo kumbe kweli unataka kuniua? Kwa sababu gani? Niliowaua na we' si nilikuhusisha kuwaua? Sudi amekupa shi'ngapi, eh? Sema! Nitai-double," Bertha akamwambia.

"Hii haihusu pesa mama..." Dotto akasema.

"Ila?" Bertha akauliza.

"Utagundua baada ya sekunde..." Dotto akasema.

"Dotto..."

"Kaa kimya, mbuzi nini! Unajiona mjanja hata pistol huwezi kushika, utakufa tu bwege wewe. Ila nikushukuru kwa kuniletea na hiki chuma, umenirahisishia kazi," akaniambia hivyo.

"Sija... Dotto nakuomba, usifanye hivi... Chalii anakufanyia manipulation tu..." nikamwambia hivyo kwa hisia.

"Agh, na maviingereza yako unanikera!" jamaa akasema hivyo.

"Kwa hiyo ndiyo nini, unamlipizia kisasi ndugu yako? Amekaa huko akakudanganya-danganya kwamba mtaweza kuniua mimi, eh?" Bertha akauliza hivyo kwa kujiamini.

Tukaanza kusikia hatua zikikaribia kufikia chumba hiki, na sauti ya Sudi ikasikika ikiuliza, "Kwa nini tushindwe?"

Mimi na Bertha tukaangalia upande wa mlango, lakini Dotto hakuondoa macho yake kutuelekea, na ndiyo hapo mlangoni jamaa akawa ametokea. Sudi ndani ya suti. Jamaa aliingia kama kibosile yaani, taratibu kwa njia ya kuridhika kabisa, na nyuma yake alifuatwa na wanaume wawili; mmoja ikiwa ni Chalii Gonga mwenyewe, pamoja na yule jamaa mzito ambaye alimshika Miryam ile jana na kutishia kumuua.

Chalii na huyo jamaa walivalia masweta meusi yenye vikofia ambavyo havikufunika vichwa vyao, na Sudi pamoja na Chalii ndiyo waliosogea mbele zaidi kumpita Dotto, na yule jamaa akasimama pembeni mkono wangu wa kushoto huku akishikilia bastola mkononi iliyowekewa kifinya sauti (silencer). Ikawa ni 'four against two,' watu wanne dhidi yetu wawili, na Bertha alionekana kuwaangalia kwa njia isiyo na hofu bali hasira, huku mimi hapa nikihofia usalama wetu kwa pamoja.

"M(....)mmoja wewe!" Bertha akamwambia hivyo Sudi kwa sauti ya chini.

Sudi akatabasamu kidogo kwa kiburi, naye akasema, "In the flesh. Happy to see me?"

"F(...) you!" Bertha akamwambia hivyo kwa sauti tulivu.

"Mke wako ameamkia upande wa chaga iliyovunjika leo," Sudi akamwambia Chalii Gonga hivyo.

Chalii akatabasamu kiasi kwa kiburi, naye Dotto akafanya kuiachanisha bastola yangu aliyoshika na kitunzio chake cha risasi, kisha akavitupa pembeni, halafu akavuta bastola nyingine nyeusi kutoka nyuma ya kiuno chake na kuanza kuifungia silencer taratibu, tayari kwa ajili ya mauaji. Aisee! Nilihisi kufa!

Bertha akamtazama mume wake na kusema, "Kwa hiyo ridhaa ya kufanya haya ni ya moyo wako wote kabisa Charles?"

"Kwa asilimia mia. Ulitegemea nini? Kwamba uendelee kunitendea kama mbwa wako kwa maisha yangu yote halafu nitulie tu?" Chalii akamsemesha hivyo.

"Kama mbwa? Ulistahili zaidi ya yale niliyokutendea mshenzi wewe! Wewe ndiyo sababu mwanangu aliuawa!" Bertha akasema hivyo.

"Oh, unaekti kama vile haungeweza kuzaa tena, hujui kifo kipo tu mama? Unashikilia jambo moja tu kunifanya mdoli wa ku-torture utafikiri kuzaa ni mara moja? Ungesema tu kama hukuwa na uwezo wa kuzaa tena, ingeeleweka," Chalii akamwambia hivyo.

"Ulinipima ukaona huo uwezo sina?" Bertha akamuuliza hivyo.

Nikamtazama Chalii kwa mkazo na kumuuliza, "Kwa hiyo kumbe ulikuwa unanidanganya uliponiambia kuhusu jinsi mtoto wenu alivyokufa?"

"Wewe kama nani unaniuliza mimi hivyo?" Chalii akaniuliza.

Bertha akaniangalia na kuuliza, "Unamaanisha nini?"

Nikamtazama na kusema, "Chalii aliniambia wewe ndo' ulisababisha mtoto wenu akafa... ulimpa sumu Giselle... yaani ukiwa unataka kumuua mwanamke wake Chalii."

Bertha akamwangalia Chalii na kusema, "We' ni Shetani Chaz!"

"Ahah, zaidi yako? Hiyo ilikuwa business mpenzi. Tulikuwa tunajaribu kumleta jamaa upande wetu, lakini ni wazi ameona hawezi kutoka kwako maana una (....) tamu mno eti... najua, inapumbaza mno wapumbavu kama yeye... siyo mimi," Chalii akaongea kwa dharau.

Wenzake wakacheka kidogo, naye Bertha akasema, "Hujisikii vibaya hata kidogo kwamba mwanao alikufa kwa sababu ya upuuzi wako... upuuzi ambao mimi ndiyo nikalipia? Halafu tena unanisingizia?"

"Ooh acha kujifanya victim sana mama G, si ulipata faida lakini? Kunitesa huko kote, kunilisha nyama mbichi, kuniwekea watu wa kunichunga kama ng'ombe... tena hukuchoka, yaani ulitaka tu niendelee kuwa kama mdoli wako...."

"Basi, inatosha," Sudi akamkatisha jamaa.

Mimi na Bertha tukamwangalia Sudi usoni, huku Chalii Gonga akipumua kwa hasira kiasi.

Sudi, akiwa ameweka mikono yake mfukoni, akasema, "Mambo ya familia hayajalishi tena. Tumetoka mbali Bertha, najua... lakini sometimes mwisho wa safari huwa ni lazima ufike, you know that..."

"Safari gani? Me nimeshawahi kufanya venture yoyote na wewe hata mara moja? Kwa nini unaniogopa sana?" Bertha akamuuliza hivyo kwa ujasiri.

"Mimi nikuogope wewe?"

"Kinachofanya utake kuniua ni nini kama siyo woga? Kwamba... unitolee mfano, ili na wakina Farao, Tito, wote wakuogope eh? Umesahau kuhusu Festus? Hujui atakufanya nini akigundua kuhusu...."

"Atagunduaje?" Sudi akamkatisha.

Tukabaki kumwangalia kwa umakini.

"Hawezi kujua, na yeye ana lake linalokuja muda si mrefu..." Sudi akasema.

"Mmm?" Bertha akafanya hivyo kikejeli.

"Eeeh. Kwa hiyo... sitaki tupotezeane muda Bertha. Unajua kinachoenda kutokea now, kinachotakiwa ni uwe tayari kukubaliana nacho. Basi," Sudi akasema hivyo.

"Na baada ya hapo?" Bertha akamuuliza.

"Oh well, yatakayofata hayana faida kwako maana tayari utakuwa six feet underground. Hata kama ukiweza kuyaona wakati upo kuzimu, basi haitakuwa mbaya pia. Lakini hapa sijisumbui kukupa hadithi utamu kolea," Sudi akasema hivyo.

Chalii Gonga akacheka kidogo.

"Unachezea moto Sudi. Wewe na hawa malaya zako," Bertha akasema hivyo.

Yule jamaa mwingine wa Sudi akainyoosha bastola yake kumwelekea madam, nami nikamkinga Bertha kwa mbele.

"Bro... tafadhali, weka chuma pembeni, taf... Sudi... hii siyo fresh aisee, haipasw...." nikajaribu kutuliza hali.

Sudi akacheka na kusema, "Yaani unawaita wanaume wangu wa kazi malaya, wakati malaya wako namba moja huyu hapa! Wewe JC... nilikupa masaa 12 ya kutumia vizuri kabisa lakini ukaamua kuchagua..."

"Sudi tafadhali..."

"... kusimama mbele ya huyu mwanamke, sawa. Nimeelewa. Utakipata kinachokuja kwake pia maana ndiyo umekiomba..." Sudi akamalizia maneno yake.

"Basi sawa, Sudi... nita... nitakufanyia kazi, sawa? Nitakutengenezea madawa... coke nzuri zaidi hata ya nayompa madam, alright? Just please... usimuue... nitakuja upande wako, mwache tu, haina...."

Bertha akaja usawa wangu zaidi na kusema, "Acha kuwa kama (....), JC! Unaogopa nini?"

Nikamwangalia na kusema, "Sitaki uumie Bertha! Ya nini? Eh? Mwachieni aende... nitawafanyia kazi.... nawaomba..." nikaelekeza maneno hayo kwa maadui.

"Aww... mpaka inagusa sana!" Chalii akaongea kwa dharau.

"Sana! Anampigania mke wako mpaka mwisho, yale ya Kantala na Odemba eh?" Sudi akasema hivyo.

"Odama," yule jambazi wake akamsahihisha.

"Eeeh, Odama. Hahah... lakini huyu mwanamke Shetani hafanani hata kidogo na Odama. Odama alikuwa malaika, yeye Bertha ni roho mchafu sana... pepo yaani... na ni lazima kuwaondoa roho na mapepo wachafu kwa kumwaga damu zao ikiwa maombi yatashindikana," Sudi akasema hivyo.

Chalii akacheka kwa sifa, naye Sudi akatoa ishara kwa upande wa Dotto, na jamaa akawa amenyanyua bastola yake kutuelekea sisi. Niliingiwa na hofu! Yaani kifo hiki hapa nilikuwa nakitazama, bastola mbili zikielekea vichwa vyetu na sijui, yaani sijui ningetokaje!

"Pole JC... umechelewa sana. Masaa 12 yameenda, muda umekwisha," Sudi akaniambia hivyo.

Akarudi nyuma kidogo, nami nikaingiwa na wasiwasi hata zaidi kwa kuwa bastola ndiyo zilikuwa zikielekezwa kwetu zaidi, ikibaki tu amri kwa wanaume waliozishika wavipasue vichwa vyetu, na Bertha alikuwa akiwatazama kwa umakini sana. Kisha, ghafla tu mwanamke huyu akaanza kucheka. Sana. Alicheka kicheko cha kutoka moyoni yaani, kama mtu aliyekuwa amefurahishwa na utani wa hali ya juu, mpaka mimi nikamwangalia kwa mshangao kiasi.

"Aaaa... classic madam Bertha," Sudi akasema hivyo kikejeli.

Bertha akaendelea kucheka zaidi, ikiwa wazi wakati huu kwa sifa.

"Unacheka nini?" Chalii akamuuliza hivyo.

"Oh, mwache. Ni defense mechanism. Kicheko chake cha mwisho lazima kiwe kizuri," Sudi akasema hivyo.

Bertha akamalizia kucheka na kusema, "Haaahh... what drama! Hii imenifurahisha kwa kweli."

"Sehemu ipi zaidi? Kwamba unakufa, ama haufanani na Odama?" Sudi akamuuliza hivyo.

Bertha akasema, "Hivi kwa nini huwa mnajivuta hivyo? Kama kuniua si mgekuwa mmeniua tu tayari? Mnaongeea, mwishowe msababishe mmoja wenu adondoke tu ghafla out of nowhere..."

Ile kamaliza kusema hivyo, damu zikaruka ghafla kutokea upande wangu wa kushoto, nami nikashtuka kiasi na kutazama hapo baada ya mguno usio mzito sana kumponyoka yule jamaa mwingine aliyekuwa ametuelekezea bastola. Kumwangalia, alikuwa amepigiza mwili wake kwa kishindo kikubwa ukutani kisha ukadondoka chini kwa nguvu, na hapo ndiyo nikaona tundu moja la risasi likiwa limetoboa upande mmoja wa kichwa chake, na damu nyingi zikivuja!

Sudi, Chalii, mimi, tulishangazwa sana na hilo, isieleweke imekuwaje, na ile nimeangalia pembeni, nikakuta Dotto akiwa ameelekeza bastola yake yenye kizuio cha sauti kuwaelekea Sudi na Chalii Gonga, moja kwa moja ikionyesha kwamba ni yeye ndiyo alikuwa amemtungua yule jamaa mwingine!

Nini? Nilishindwa kuelewa, kuamini, na kutathmini kilichokuwa kimetokea. Sudi na Chalii Gonga wakamwangalia Dotto kwa taharuki, huku mwili wa jamaa pale chini ukitulia tuli na damu kutokea kwenye tobo la risasi zikiruka kwa kushtua-shtua. Nilichoka!

Uzito wa namna ambavyo hali hiyo ilichanganya ulizidi kupanda tu, nami nikamwangalia madam Bertha pembeni kukuta anaangalia vidole vyake vya mkononi kwa kugeuza-geuza kiganja kama vile hajaona na hajali kilichokuwa kimetokea yaani.

"Madam Bertha will kill you, hiyaa hiyaa oooh..."

Bertha akaimba hivyo kwa sauti ya chini, kisha akaniangalia machoni na kutabasamu. Nikarudi nyuma kidogo huku nikimtazama kwa kutoelewa kabisa kilichokuwa kinaendelea, naye akawaangalia wahasimu wake.

Sudi na Chalii, bado wakiwa wametikiswa pia na jambo alilofanya Dotto, walionekana kuchanganyiwa haswa, naye Chalii akataka kupiga hatua kuelekea mlangoni lakini Dotto akafyatua risasi sakafuni iliyofanya patoboke na kigae kupasuka-pasuka. Jamaa akarudi nyuma kwa hofu.

"Dotto! Unafanya utumbo gani huu?" Sudi akamuuliza hivyo.

Dotto akaendelea kumnyooshea bastola kwa utulivu tu.

"Labda umuulize mmiliki, siyo mmilikiwa," Bertha akasema hivyo.

Sudi na Chalii Gonga wakamwangalia, hata mimi pia nikamtazama huyu mwanamke.

Bertha akasema, "Oooh, the twissst! Imewabamba eh?"

Sote tukabaki kumwangalia kwa umakini.

"Sudi kama uliiangalia hiyo filamu vizuri, utakumbuka kwamba Odama na Kantala waliibuka washindi mwishoni kwa sababu hawakuchoka kupambana. Tena, ni Kantala ndiyo alimpigania Odama na kuwashinda maadui, kama tu JC wangu hapa. Right? Kwa nini tusiibuke washindi?" Bertha akamwambia hivyo.

Nikiwa bado sijaelewa mambo vizuri, nikamuuliza,"Madam, nini kinaendelea?"

Akanishika usoni na kusema, "Usijali, HB wangu. Nilikuwa najua kila kitu. Hii ndiyo intermission."

Nikamwangalia Dotto kwa umakini. Kumbe huu muda wote alikuwa akiigiza? Ai, kudadeki!

Chalii Gonga akamwambia Dotto, "We' mjinga kumbe ulikuwa unatuchezea huu muda wote? Yaani... uko tayari kuendelea kuwa mbwa wa huyu mwanamke badala ya kusimama na mimi kaka yako?"

"Charles, nimeshakwambia tokea muda mrefu sana, huniwezi mimi. Yaani elewa kwamba sikuzote ukifikiri unaijua kesho, Bertha tayari ameiona kama jana. Ulifikiri kweli kabisa mimi... mimi madam Bertha ungeweza kunipangia kifo? Tena yaani unilete tu hapa na kuniua yaani... kihivyo tu? Chaz umesoma kweli wewe?" Bertha akamuuliza hivyo.

Chalii Gonga akaendelea tu kumwangalia usoni.

Bertha akamtazama Sudi na kusema, "Na wewe. Usifikiri nilikuwa sijakuona ukija. Nimekuangalia kwa muda mrefu sana. Una... unatamani kuwa kama mimi, lakini umeshindwa, na unalazimisha kunizidi lakini umeshindwa pia, ndiyo maana ego yako ikakudanganya kufikiri ungeweza kuniondoa kirahisi tu..."

Sudi akawa akimtazama kwa njia ya hasira.

"Ahah... hata katika nyakati hizi unapaswa ujue kuna vitu vikubwa zaidi ya ego, rafiki yangu. Kimoja? Loyalty. Mtu akijitoa kwako kwa moyo mkunjufu Sudi, haijalishi atapewa nini, yaani hawezi kuacha kuendelea kushikamana nawe mpaka mwisho. Move mbaya kwako zaidi kufanya ilikuwa kum-enlist Dotto. Ulifikiri ingekuwa rahisi kumnunua kwa sababu una kaka yake upande wako, lakini huyo hapo. Amekuonyesha nini maana ya loyalty. Loyalty siyo damu tu. Ni RESPECT. Ungekuwa loyal kwa muungano wetu hata kama hunipendi, usingefanya huu upuuzi Sudi. Hata mimi sikupendi, lakini sikukaa kufikiria kukufanyia kitu cha namna hii. Umeharibu palipokuwa pametulia mdogo wangu, na hakuna namna nyingine iliyobaki ila wewe kupatengeneza tena," Bertha akamwambia hivyo kwa sauti tulivu.

"Nani unamwita mdogo wako, malaya wewe?" Sudi akamsemesha hivyo.

Bertha akatabasamu kiasi huku akimtazama kwa hisia kali. Kisha, akarudisha mkono wake mmoja nyuma ya kiuno chake na kuchomoa bastola nyeusi pia, ikiwa ndefu shauri ya kuwekewa silencer, naye akaishikilia kiganjani kwake huku akimtazama Sudi kwa njia ya kawaida. Aisee, huyu mwanamke! Alikuwa anajua kuigiza! Yaani kumbe huu muda wote mchezo ulikuwa ni wake kabisa!

Sudi akatusogelea kidogo bila woga na kusema, "Kwa hiyo unajiona umeshinda? Kwamba una akili sana, unajua yote? Hata kama umeweza haka kamchezo sasa hivi, kumbuka zamu yako itakuja tu..."

"Zamu yangu ya nini? Kufanya upuuzi wa ki(.....) kama wako ni kitu ambacho siwezi... never, kukifanya. We' ndiyo malaya kwangu kutotambua kwamba me mwanaume wako nilikuwa hatua mbili mbele zaidi yako, na sasa hivi nitahakikisha nayapanua zaidi matundu yote saba ya mwili wako ukiwa kama malaya aliye wewe!" Bertha akamwambia hivyo kwa mkazo.

Dah! Tusi moja baya kinoma lililosemwa kwa ufasaha wa hali ya juu! Unaachaje kumpenda Bertha? Sudi akabaki kimya tu na kuendelea kumwangalia usoni kwa hasira.

Chalii akasema, "Kwa hiyo utatuua? Dotto? Utaniua mimi? Kweli mimi kaka yako? Hm?"

Dotto akamtazama madam.

Bertha akasema, "Unaogopa sana kufa Chaz, eh? Umekuja hapa unajiamiiini, eti '(....) yako inapumbaza wapumbavu kama yeye, siyo mimi,' kumbe we' ndo' umejaza ma(....)-uoga tu mishipani mwako. Ilihitajika kibao kukugeukia ili ujionyeshe jinsi ulivyokuwa pussy... na yeah, Dotto atakuua mpumbavu wewe!"

Nikamwambia Bertha, "Madam... haina haja ya kufika huko. Tunaweza tu ku...."

"Nini? Oooh... naelewa JC. Unataka wewe ndo' uvute chuma?" Bertha akaniuliza hivyo.

Nikaweka uso makini na kusema, "Hapana, sijamaanisha..."

"Ahahah... chukua JC. Nataka uutungue ubongo wa huyu mpumbavu hapa hapa," Bertha akaniambia hivyo.

Loh!

Nikaitazama bastola yake, ambayo aliinyanyua kunielekezea ili niichukue, lakini nikashindwa kuipokea. Nikabaki nikimtazama machoni tu kama vile sijaelewa somo, na katika hali hiyo ya kusubiriwa, Chalii Gonga akaona kwamba amepata nafasi ya kujaribu kufanya kitendo fulani cha kibishi kwa kuanza kukimbilia mlangoni, lakini hapo hapo Bertha akaielekeza bastola yake huko na kufyatua risasi mbili zilizomtoboa jamaa mgongoni vibaya mno!

Nilishtuka. Chalii Gonga akaanguka pale pale kwa kishindo kikubwa na kuanza kutoa sauti ya kilio cha chini cha maumivu, nami nilipomwangalia Bertha, nikaona akimtazama Dotto na kutikisa kichwa mara moja kwa uharaka, na ndiyo Dotto akaielekeza bastola yake hapo Chalii alipolala na kufyatua risasi moja kichwani kwa jamaa iliyomfanya akate uhai!

Ilikuwa kama nimeshindwa kuamini jambo hilo kabisa, yaani sikuwa yule mtu wa kuonyesha mshangao sana, lakini nilishangaa yaani. Nilimwangalia Chalii Gonga pale chini kwa njia ambayo mtu angefikiri nilikuwa nimetulia tu, lakini moyo ulikuwa ukifanya riadha ya ajabu ndani yangu. Sikuwahi kufikiri ningeshuhudia kihalisi jambo kama hilo kwa ukaribu tofauti na kuona tu lilivyokuwa likiigizwa kwenye filamu nilizowahi kuona, na kiukweli nilikosa amani sana. Ikiwa mambo yangekuwa yameenda vise versa, mimi ndiyo ningekuwa kwenye hiyo sakafu hapo chini.

Akawa amebaki Sudi na suti yake, tukiwa tumemweka kati, na hakuonekana kama mtu anayeogopa sana ingawa ilikuwa wazi kwamba alishtushwa na kilichompata mwenzake wa pili. Akatuangalia mimi na madam Bertha kwa umakini sana, na mimi pia nikamtazama madam kukuta akitabasamu kwa kiburi huku macho yake yakielekea kwa jamaa. Ilikuwa ile kwamba 'umebaki wewe,' Sudi alilijua hilo, na naelewa alikuwa akijihukumu sana kutengeneza mtego namna hii halafu ukamnasa yeye mwenyewe.

Lakini akajikaza kiume na kumwambia Bertha, "Unasubiri nini? Go ahead."

"Ooh, haraka ya nini Sudi? Hauna maneno ya mwisho unataka tumtumie baby mama wako huko aliko? Na watoto?" Bertha akamuuliza hivyo.

Sudi akaweka uso ulioonyesha wasiwasi.

Bertha akacheka na kusema, "Niambie. Nitawafikishia, personally."

"Mimi ndiyo mbaya wako Bertha, kama kuniua niue, nimeshakubaliana na hilo. Ila familia yangu usiiguse. Hawajui lolote kuhusu haya," Sudi akasema hivyo.

Eti sasa hivi alikuwa anaongea kwa njia fulani kama vile kuonyesha yeye ndiyo mwathirika yaani, kama vile anaonewa hivi, na sijui kwa nini ila nikajikuta nashindwa kujizuia kumwonea huruma kiasi. Bertha asingemwachia, najua, ila kama angeenda kuiharibu na familia ya jamaa, hiyo ingekuwa imekwenda mbali mno. Lakini yalikuwa makosa ya nani?

Mwanamke huyu akiwa anamcheka Sudi kwa furaha baada ya jamaa kuonyesha hofu juu ya familia yake, tukaanza kusikia hatua zikikaribia kufikia chumba hiki kwa mara nyingine tena, naye Dotto akasogea usawa wa mlangoni na kuangalia huko nje. Kisha, akaonekana kutulia tu na kurudi ndani tena, akimtikisia madam Bertha kichwa kama kumpa ishara.

"Finally," Bertha akasema hivyo.

Ikaeleweka kwamba kuna mtu wa upande wake aliyekuwa akija, nami nikaangalia hapo mlangoni mpaka mtu huyo alipofika na kusimama kwanza, akiangalia mazingira ya hapo ndani.

"The (....)?"

Ilikuwa ni Festo. Mwamba akawa ameuliza hivyo baada tu ya kufika na kukuta miili miwili ikiwa imelala chini, damu ikitapakaa hapo mithili ya rangi iliyomwagika, naye akatutazama sisi wote kwa umakini. Alikuwa amevalia kwa njia ya kawaida tu; T-shirt la mikono mifupi lenye rangi mbalimbali alilochomekea kwenye suruali ya kardet pamoja na kiatu rasmi cheusi, huku akishikilia kalamu nzuri kiganjani na funguo nyingi zikiwa zinaning'inia kutokea kwenye mkanda wa suruali yake.

"Festus. Pole nimeanzisha party kabla hujafika, ila bado haijaisha," Bertha akamwambia hivyo huku akitabasamu.

Festo akamwangalia Sudi na kusema, "Kinachofanyika hapa ni nini?"

Sudi akabaki kimya tu huku akiangalia pembeni kwa njia fulani ya jeuri.

Bertha akamwambia Festo, "Njoo nikupe ubuyu."

Festo akaupita mwili wa Chalii Gonga hapo chini na kuja mpaka nilipokuwa nimesimama na madam, naye Bertha akaanza kumwelezea. Akasema namna ambavyo alijua toka mwanzo kuhusu mipango ya wakina Sudi kutaka kunigeuza dhidi yake na kumuua, na aliona aendelee kuigiza kwamba hajui ili aone kama ningemsaliti pia mpaka siku ambayo wote tungejikoroga ili atuondoe.

Lakini alifurahia jinsi nilivyothibitisha kuwa upande wake leo, kwamba upendo wangu kwake ulikuwa halisi, na hapo sasa kilichokuwa kimebaki ni hukumu ya msaliti Sudi, na ndiyo maana alikuwa amemwita Festo mapema ili aje kuhalalisha hukumu hiyo kwa kitendo cha jamaa ambacho kilionyesha hakuwa mmoja wao kwa ajili ya faida yao wote, bali alitaka tu faida za kibinafsi zaidi.

Festo akamwangalia Sudi na kusema, "Sudi haya yote ni kweli? Yaani... ulikuwa unataka kumuua madam kwa sababu tu amekuzidi kimapato? Hujui sokoni ni competition? Kwa nini usingetafuta na wewe mtu mwingine wa kukufanya uwe competitive badala ya kujaribu kufanya cut ya kishenzi namna hii kwa mwenzako? Umechanganyikiwa wewe..."

"Ndiyo nimechanganyikiwa!" Sudi akamwambia hivyo Festo kwa ujasiri.

Festo akamkazia macho kwa umakini.

"Unafikiri sisi wote hatuoni jinsi unavyompendelea huyu? Umempa territory kubwa zaidi yetu sisi wote, hata tukijaribu kuomba utuongezee unatupiga chini tu, eti kuna risk. Mbona kwa Bertha hauoni risk? Kwa sababu yeye ni mwanamke?" Sudi akamuuliza hivyo.

"Ikiwa hauridhishwi na jinsi mtandao unavyofanya kazi, ungejitoa. Suala la territory siyo sababu tosha ya wewe kuchukua maamuzi ya kutaka kumuua mwenzio, nina sababu zangu kugawa nachogawa ninavyokigawa, ukiwa na tatizo na hilo, ondoka," Festo akamwambia.

"Katika maana gani? Mniue? Ahah... me siyo mjinga Festus. Hakuna mtu anaweza akatoka tu mkamwachia hivi hivi, mnaogopa kusnichiwa, kwa hiyo kuondoka unamaanisha nife. Nisingefanya hilo, hakuna choice. Biashara zetu zinaporomoka kwa sababu ya huyu mwanamke, na wewe...."

Bertha akamkatisha jamaa na kusema, "Kwani nimekufunga mikono? Unashindwa kutafuta njia ya kuinua biashara kwa upande wako unakaa kuendekeza upumbavu, eti 'nimuue Bertha, nichukue biashara zake?' Tena hadi alikuwa na mpango wa kukumaliza na wewe Festus, si ndiyo Dotto?"

Dotto akatikisa kichwa kukubali.

"Umeona alivyo mshenzi? Kaja hapa anatamba nakwambia, mpaka movie ya Odama kanisomeshea! Hizo swaga zooote, kiko wapi Sudi? Yaani unapata kingi vizuri tu, lakini ukiona mwanamke karefusha ngazi zake kupanda juu zaidi, hutaki. Eti nakuporomoshea, nimekuporomoshea nini mimi?" Bertha akamuuliza hivyo kwa hasira.

"Unaiba mpaka wateja walio kwenye territory yangu Bertha, usifikiri mimi ni mpumbavu, sioni..."

"Sijakuibia lolote mimi! Una wazimu? Me nikuibie nini, una nini kwanza cha kuibiwa wewe? Hao unaowasema wanakuja kwangu wao wenyewe, sijafunga mtu yeyote kamba shingoni kumburu...."

"Jitetee utakavyo we' mwanamke, lakini nakujua vizu...."

"Ulikuwa unataka kuniua na mimi?" Festo akakatisha hizo kelele kwa kumuuliza Sudi hivyo.

Sudi akatulia na kumwangalia, vilevile na mimi pia, ambaye nilikuwepo hapo kama vile sikuwepo yaani.

"Mwambie. Jitetee," Bertha akamwambia hivyo Sudi.

Kwa ujasiri, Sudi akasema, "Ndiyo. Na wewe ningekuondoa."

Bertha akacheka na kunishika begani, huku mimi na Festo tukimwangalia Sudi kwa umakini. Jamaa alikuwa anajua ameisha, ila alitaka kuonyesha kwamba anaisha kibabe.

Bertha akamwambia Sudi, "Yaani mateso nayotaka upitie wewe kinyang'anyiro wewe! Utajitafuna mwenyewe mpaka ufe!"

"Unaelewa unachokisema, Sudi?" Festo akamuuliza hivyo kwa sauti yake kuu.

Akamwambia Festo, "Vizuri sana. Nyie wote hamna utofauti. Mnajifanya mko upande mmoja sasa hivi, lakini haitachukua muda mrefu kwenu nyote kugeukana. Na unajua sababu itakuwa ni nini? Huyu. Mwanamke. Sisi wote hapa wanaume tunajua vizuri jinsi wanawake wanavyoweza kuvuruga mambo mengi mazuri ndani ya kipindi kifupi, na Festo nakwambia, sasa hivi si una kifua kipana sana na nguvu ulizonazo? Chote kitamomonyoka kwa sababu tu ya mwanamke..."

"Huwa una shida gani na wanawake? Hm? Mama yako hakukupenda sana wakati wa utoto, au... au ndo' na we' walikukuta kwenye shimo la choo? Alikutupa?" Bertha akamuuliza hivyo kwa dharau.

Sudi akaendelea kumtazama Festo na kusema, "Huo ugumu ulionao wote moyoni mwako Festus, uliofanya sisi sote tukuogope, hautaendelea kuwepo tena kwa sababu unajiruhusu kufanya mwanamke awe udhaifu wako. Ahah... tena unajua nini, yaani... sasa hivi hata sikuogopi. Kiukweli mwanangu, yaani nakuona mdogo sana kwa sababu umeshamalizwa na upuuzi wa kufatilia wanawake tu ambao hawakupi faida yoyote, mambo kwenye mtandao yanaharibika, mpaka kufikia hivi... huna habari, wakati mwanzo ulikuwa unajua kila kitu... ni shauri tu ya huyo mwanamke..."

Aliposema hivyo, hakuonekana kama alikuwa akimwongelea Bertha, naye Festo akavuta pumzi ya juu kuonyesha hasira imempanda na kuishusha taratibu huku akimtazama kwa mkazo. Nilielewa kwamba alikuwa akimzungumzia Miryam, na kiukweli sikujua alilitambua jinsi gani suala hilo la Festo kumtaka Miryam. Ila hapo akawa amegusa pabaya.

Sudi akaendelea kusema, "Kuniua mtaniua tu, najua. Lakini hata na nyie mtakufa. Unajitahidi sana kuishi kama... spy mwenye maisha included mno, unafikiri hauna vulnerability kwa sababu hutaki tuzione, lakini najua unazo, na tena kwa huyo mwanamke ndiyo umemalizwa kabisa Festus. Hata sisi usiotaka tujue, tunajua, baba... umekwisha. Hauna lolote tena zaidi ya jina, siyo mimi, wala Farao, wala Tito, na hata huyu Bertha... hakuna yeyote kati yetu atakayeendelea kuogopa pimbi kama wewe kwa sababu tumeshaona madhaifu yako kwa wanawake... na I swear, huyo mwanamke cheupe cheupe huyo unayemfatilia saaana, huyo huyo ndiyo atakuja...."

Kabla Sudi hajamaliza kuongea, Festo akaikwapua bastola ya Bertha na kufyatua risasi tatu moja kwa moja juu ya paji la uso wake Sudi!Ilikuwa ghafla sana, na hapo hapo jamaa akadondoka chini na kupoteza maisha yake!

Nilifumba macho, nikikaza meno, na kuinamisha uso wangu, nikijihisi vibaya sana moyoni. Kifo cha tatu ndani ya chumba kimoja, na kiukweli, najua Sudi alikuwa amefanya maku-Sudi kuongea maneno hayo kumwelekea Festo kwa kujua angekasirika sana, kwa hiyo alionyesha kutaka auliwe upesi badala ya mateso ambayo hawa watu wangempa kwa sababu ya matendo yake. Akawa amekipata.

Nilianza kuhisi tumbo likinivuruga ghafla yaani, siyo labda kinyaa sijui, hapana, maana mimi kama ni damu, nyama, viungo vya mwili vikiwa vimeachanishwa, na mengine ni mambo niliyokuwa nimeshazoea kuyaona mara nyingi mno na ilikuwa kawaida, lakini kuwa hapa kama mhusika wa haya mauaji ilikuwa ishu nyingine kabisa. Sikujiona kuwahi kuja kufika huku, lakini ndiyo nikawa nimefika sasa.

Bertha akasema, "Aww, Festus! Umemuua haraka mno, tulipaswa tumpe vyake vya taratibu kwanza aelewe maumivu ni nini!"

Festo akamrudishia mwanamke huyu bastola yake na kusema, "He wasn't worth it."

Kwamba Sudi hakuwa na umuhimu wowote wa kuanza sijui kumteeesa, yaani hawa watu!

Bertha akamuuliza, "Alikuwa anaongea kuhusu cheupe gani huyu mjinga?"

Festo akamwangalia Dotto na kusema, "Hey, harakisha. Fanya mpango hii sehemu isafishwe."

Dotto akatikisa kichwa kukubali, naye akachomoa simu kutoka mfukoni na kumpigia mtu fulani. Najua Festo aliliepuka swali la Bertha kwa makusudi, na kwa sababu nzuri pia.

Bertha akasema, "This was so fun! Imeuma tu HB wangu hujapata nafasi ya kutia tobo mtu, nilikuwa nina hamu ya kuona unapiga action leo."

Nikamwangalia usoni tu nikiwa nimeishiwa raha.

Akanishika shingoni na kusema, "Aww, mpenzi, mbona hivyo? Haujafurahi maadui zetu wameenda?"

Nikaacha tu kumwangalia na kutazama pembeni.

"Ahahah... najua bado hujawahi. Usijali. Utapata nafasi nyingine real soon," Bertha akaniambia.

Yaani walikuwa wanaona kuua ni jambo la kawaida sana, aisee!

Festo akasema, "Kutakuwa na mabadiliko ya management baada ya huu upumbavu. Jioni tukutane Red Room. Spread the word."

"Sawa. Nitafurahi ukinipa na territory ya huyu mjinga, nguvu yetu itakua," Bertha akamwambia hivyo.

"Yako unamaanisha," Festo akamwambia hivyo.

"Yetu... Festus. Come on, unanijua," Bertha akamsemesha kwa njia fulani ya kumbembeleza.

Nikamwangalia na kukuta amemshika Festo shingoni, na jamaa akaniangalia pia.

Bertha akanigeukia na kusema, "Twende JC. Nasikia njaa."

Nikatikisa kichwa kukubali.

"Ulikuwa umetokea mbali?" Bertha akamuuliza hivyo Festo.

"Nilikuwa hapo Goba. Nyie nendeni, tutaonana baadaye," Festo akasema hivyo.

Jamaa alionekana kuudhika sana, na alijua naelewa kwa nini aliudhika mno mpaka akamuua Sudi mbele ya macho yangu. Hata jinsi tu alivyokuwa akinitazama ilionyesha wazi namna ambavyo alielewa najua uzito wa maneno ya Sudi ulielekea kwenye suala la Miryam, kitu ambacho kilimtia hasira kugundua kuwa baadhi ya watu wake wengine walitambua hatua zake za kumfatilia yule mwanamke, na walimwona kuwa mdhaifu kwa sababu hiyo. Kwa hiyo alikuwa amekasirika haswa.

Inaonekana Dotto alikuwa amewaita watu fulani waje kusaidiana naye kusafisha hii sehemu kabla haijazua gumzo, watu walio makini, naye akamwambia Festo kwamba wangefika hapo na vifaa baada ya dakika chache. Bertha akanishika mkono na kumwambia Dotto aibebe bastola yangu aliyokuwa ameitupa pembeni muda ule kisha angeileta baadaye huko hotelini, halafu akaanza kunivuta kuelekea mlangoni ili tuondoke.

Ile tumefikia mlangoni hapo, Festo akaniita, nami nikasimama na kumgeukia, huku Bertha akiningoja pia. Jamaa akiwa ananitazama kwa umakini machoni, akaniambia, "Be careful."

Mh!

Sikuelewa maana halisi ya maneno hayo na kuchukulia kwamba alikuwa akinitahadharisha kuhusiana na ishu yake na Miryam. Alikuwa akinitaka niendelee kuwa kimya, nisiseme lolote lile juu ya huyo mwanamke hata kwa Bertha, na jinsi alivyoyawasilisha hayo maneno kwangu yaani hadi ilitisha mzee. Alitoka kunionyesha roho yake ya kikatili inavyokuwa akikasirishwa sana, na kuniangalia kwake kuliionyesha hiyo roho pro max.

Aisee, hii siku ilikuwa imegeuka kuwa mbaya mno zaidi ya siku zingine zilizokuwa mbaya sana maishani mwangu. Nilipata somo kubwa zaidi juu ya Festo wakati huu. Huyu mwamba alikuwa ni hatari sana, sikupaswa kuwa mzembe hata kidogo. Inawezekana labda hata alichukulia suala la Sudi kujua kuhusu nyendo zake kwa Miryam lilisababishwa na mimi, kwa hiyo kweli, nilihitaji kuwa "careful," maana asingechelewa kuniharibu. Alikuwa amekwishaniambia hivyo, kwa hiyo mimi ndiyo ningetakiwa kufanikiwa kumharibu yeye kwanza.






★★★★★★★★★

ITAENDELEA

★★★★★★★★★


Pata Full Story WhatsApp au inbox

Whatsapp +255 678 017 280

Karibuni sana
 
Sijui tu ,, yani sielewi kwanini hisia zangu zinaniambia hivi ...

Elton Tonny - huyu ndiyo Jc mwenyewe lakini pia

Elkey ndiyo Miryam mwenyewe tunaye msoma humu ndani kwenye story hii ...

Sasa basi pengine mpaka muda huu niandikapo watu hawa ni wapenzi au ni mume na mke ,, hivyo kwa upande mmoja J.C atuelezeapo juu ya simulizi yake tukafurahi na kuenjoy.

Upande wa pili ,,, unamuelezea ana msimulia mpenzi wake Elkey ( humu kwenye story tumemfahamu kama miryamu ).. juu ya mambo au misukosuko mbali mbali aliyompata kabla na hata baada ya kuwa naye kwenye mahusiano ..

Hivyo jambo hili linamfanya miryamu (Elkey ) afurahi sana maana anapata wasaa wa kukumbuka mengi yaliyotokea katika safari ya ujenzi wa penzi lao uliofanywa na J.C na huku sisi wasomaji tukipata burudani safiii kabisaa .. yani Mwamba anapiga ndege wawili kwa jiwe moja..

Wote tumeona au kujua ni jinsi gani mwanaume huyu J.C(Elton tonny) alivyo dhaifu kwa bibie miryamu ( Elkey ) na ndiyo maana mwanadada Elkey akumuita tu "Eltoniii" jamaa huyo fasta anashusha story ... Mimi ukweli nimeshawashtukia hawa..
 
Sijui tu ,, yani sielewi kwanini hisia zangu zinaniambia hivi ...

Elton Tonny - huyu ndiyo Jc mwenyewe lakini pia

Elkey ndiyo Miryam mwenyewe tunaye msoma humu ndani kwenye story hii ...

Sasa basi pengine mpaka muda huu niandikapo watu hawa ni wapenzi au ni mume na mke ,, hivyo kwa upande mmoja J.C atuelezeapo juu ya simulizi yake tukafurahi na kuenjoy.

Upande wa pili ,,, unamuelezea ana msimulia mpenzi wake Elkey ( humu kwenye story tumemfahamu kama miryamu ).. juu ya mambo au misukosuko mbali mbali aliyompata kabla na hata baada ya kuwa naye kwenye mahusiano ..

Hivyo jambo hili linamfanya miryamu (Elkey ) afurahi sana maana anapata wasaa wa kukumbuka mengi yaliyotokea katika safari ya ujenzi wa penzi lao uliofanywa na J.C na huku sisi wasomaji tukipata burudani safiii kabisaa .. yani Mwamba anapiga ndege wawili kwa jiwe moja..

Wote tumeona au kujua ni jinsi gani mwanaume huyu J.C(Elton tonny) alivyo dhaifu kwa bibie miryamu ( Elkey ) na ndiyo maana mwanadada Elkey akumuita tu "Eltoniii" jamaa huyo fasta anashusha story ... Mimi ukweli nimeshawashtukia hawa..
Bro, you trippin hard 🤣🤣
 
Back
Top Bottom