Simulizi: Nini maana ya mapenzi

Simulizi: Nini maana ya mapenzi

SEHEMU YA 191


Siku hiyo walifika dada zake na wao wakaongea nae kuhusu swala lile lile la baba wa mtoto wake, walikaa chini na kuongea na mdogo wao.
“Erica tulijua baada ya kutenda kile kitendo cha kukutoa mimba ungejifunza mdogo wetu, hivi huyu mtoto ulipanga au ni vipi?”
“Ni bahati mbaya dada”
“Bahati mbaya? Yani tuseme Erica hukujua hata nji za uzazi wa mpango jamani!”
“Nilikuwa najua dada zangu, ila kwa maoni ya watu wengi walisema kuwa ukitumia njia za uzazi wa mpango unaweza usizae maisha yote”
“Yani na wewe msomi unasikia na kuamini hizo stori za wadada wa mitaani?”
“Hapana dada, ila kuna watu kabisa nilikuwa na ushahidi nao ndiomana sikuweza kutumia, walisema ni afadhali uzae kabisa ndio utumie:”
“Sasa utatumia kwasasa wakati ushakosea?”
“Msinikandamize dada zangu, nakubali kuwa nimekosea ana ila msinikandamize kiasi hiko”
“Hatukukandamizi ila unampa mawazo mama ujue, raha ya mtoto ni awe na baba, sasa mtoto wako unabaki kusema tu baba yake yupo yupo, yuko wapi?”
Akadakia Bite na kusema,
“Hatuwezi sema ni Yule kijana wa watu maana mtoto hamfananii hata chembe, tuambie Erica baba wa mtoto ni yupi na una mpango nae upi?”
Yani Erica aliona ndugu zake wakimpa kizunguzungu tu, na usiku ulipofika alijaribu kuwasiliana na Rahim ila msimamo wa Rahim ulikuwa pale pale kuwa Erica abadili dini amuoe, yani swala la kubadili dini kwa Erica lilikuwa kizunguzungu sana kwani hakutaka kumkosa Rahim na muda huo huo hakutaka kumkosea mama yake.
Na kila siku mama yake alimwambia jambo moja kuwa amlete kijana aliyezaa nae amfahamu,
“Hata kama hamna ndoa, basi nimfahamu Erica, mlete huyo kijana nimfahamu”
“Nitamleta mama”
“Yani wewe mtoto hujielewi kabisa, hujielewi Erica, umeharibu maisha yako ukiwa na miaka 23 tu. Ijui unategemea lini huko mbele ya safari”
“Mama jamani”
“Sio mama jamani, umlete huyo mjinga mwenzio ambaye mlishindwa kufikiria hadi mkazaa sijui unataka kumuweka mtoto kwenye kundi gani?”
“Atakuja mama”
Yani kichwa cha Erica kilivurugwa haswaa kwani kila akimuuliza Rahim kuwa anarudi lini alipewa jibu moja tu kuwa nitakuja usiwe na wasiwasi.
 
SEHEMU YA 192

Kadri alivyoulizwa na mama yake kuhusu baba wa mtoto wake ndivyo alivyozidi kupatwa na mawazo mbalimbali hadi kufikia hatua ya kuwa na mawazo yasiyofaa,
“Yani dunia nzima, mkosa ni mimi tu natamani hata kufa kwakweli”
Alichukua simu yake na kuingia kwenye mtandao wa kijamii, wakati anaperuzi tu akakutana na makala yenye kichwa “HAKUNA SABABU YA KUJIUA, MAISHA NI MATAMU SANA. UKIANGUKA INUKA NA USONGE MBELE” alivutiwa na makala ile na kuanza kuisoma, kwakweli iliandikwa vitu vilivyogusa maisha yake, kuna mahali alisoma,
“Unapoamua kujiua, fikiria kwanza unaowaacha, unawaacha vipi? Unaweza kuamua kujiua sababu ya mtu mmoja kakuudhi ila unaacha watu milioni moja wanaokupenda sana na wanapenda uwepo wako. Unaweza kujiua sababu kuna jambo limekukera ila fikiria maisha kuna mambo mangapi mazuri ambayo Mungu ametuzawadia? Jambo moja tu likufanye ukose maisha na mbingu? Ukianguka usiwaze sana ila inuka na usonge mbele, usikubali kilichokuangusha kikuangushe tena. Fikiria watoto unaowaacha, wazazi, marafiki wanaokupenda, ndugu, majiraniwA wanaokupenda. Kwanini ujiue na kuacha wote hawa na simanzi? Ni dhambi kubwa sana kufikiria kujiua, kumbuka Mungu katupa uhai na pumzi bure tu, kwahiyo anatupenda sana na atakusaidia utoke kwenye hiyo hali inayokupa wazo la kujiua”
Erica hii makala ilimuingia akilini sana, akamtazama mtoto wake Angel na kuona kweli ana sababu ya kuendelea kuishi kuyapigania maisha ya Yule mtoto mdogo asiye na hatia.
Leo nyumbani kwao kulifikwa na ugeni, alifika mama Derick ambaye alipoelezwa na Mage kuwa Erica ana mtoto alipenda kwenda kumsalimia, na kwa bahati muda aliofika mama yake Erica hakuwepo alikuwa ameenda kwenye vikoba vyake, Erica alimkaribisha na kumsalimia.
“Kumbe kwetu unapafahamu?”
“Napafahamu ndio, nimewahi kuishi hapa ujue”
“Aaaah karibu sana”
“Asante, niliwasiliana na Mage, akasema una mtoto nikaona ni vyema kuja kukuona”
“Mmmh inamaana na Derick anajua kama nina mtoto?”
“Hapana, unajua Derick alisafiri. Hajui chochote, kwani hutaki Derick ajue?”
Erica alicheka tu ila kiukweli hakutaka Derick ajue kwani alijua kama habari ikifika kwa Derick basi yeyote atakayekutana nae atamueleza kuhusu yeye, kwahiyo alitafuta kauli ya kumdanganyishia mama yake Derick kuwa asimueleza Derick kuwa ana mtoto,
“Basi mama, usimwambie Derick”
“Kwanini?”
“Nataka siku akikutana na mimi ashangae tu, yani iwe ni kitu cha kushangaza kwake. Asijue kwasasa”
Mama Derick aliitikia kisha akamuomba Erica akamlete mtoto ili amsalimie, Erica alienda kumtoa mtoto ndani na kumpa mama Derick, ambaye alimuangalia kwa muda na kusema,
“Umezaa mtoto mzuri sana Erica, hongera kwa hilo. Ila huyu mtoto sio mswahili eeh!”
Erica akacheka na kumuuliza,
“Kwanini unasema hivyo?”
“Namuona ni mtoto wa kipemba”
Erica akacheka, kisha mama Derick akaendelea,
“Baba yake yuko wapi?”
Kiukweli swali la baba wa mtoto lilikuwa linamkera sana Erica na kumkosesha raha kabisa, ila aliamua kuongea kikubwa kwa mama Derick kwani anajua kuwa hata huyu mama ameshawahi kupitia changamoto za mapenzi, kwahiyo alihisi pengine anaweza akampa mawazo mazuri,
“Baba wa mtoto yupo, ila nimetofautiana nae dini na ameniambia nibadili dini ndio anioe”
“Nilihisi tu mtakuwa tofauti dini, ila Erica ngoja nikwambie kitu. Usibadili dini sababu ya mapenzi yani usithubutu kabisa kubadili dini sababu ya mapenzi”
“Kwanini?”
 
SEHEMU YA 193
“Sikia nikwambie, dini ni mambo ya imani halafu ni kitu kikubwa tofauti na sisi tunavyokichukulia. Dini inabadilishwa ikiwa moyo wako umeridhia yani umesikia mafundisho ya dini nyingine, umeyaelewa ndio unabadilisha ila sio kubadilisha sababu ya mapenzi. Ni kazi bure kubadili dini sababu ya mapenzi kwanza ukumbuke hiyo dini utaenda tu ila kiukweli haipo kwako, kwahiyo utakuwa unajidanganya mwenyewe. Badili dini kwa maamuzi yako binafsi ila sio mapenzi”
“Sasa mwanaume anasema nibadili dini ndio anioe”
“Erica kama mwanaume hataki kukuoa huwa wanatafuta sababu nyingi sana, kwamaana hiyo unaweza kubadili dini akakuoa kisha akakufanyia mambo ya ajabu. Mimi nina mifano iliyo dhahiri na pia najiona nilikosea sana. Mimi ni Mwislamu yani nimelelewa katika maadili ya dini tu ila mwanaume wa kwanza kuzaa nae alikuwa Mkristo na aligoma kunioa kwa kigezo cha dini ingawa kwa kipindi hiko nilikuwa tayari kugombana na wazazi wangu ili nibadili dini niolewe na Yule mwanaume, nikaanza kufata mambo yote wakristo wanayoyafanya, nilianza hadi kwenda kanisani mimi, nikabatizwa kisiri bila familia yangu kujua kisha nikamwambia Yule mwanaume nimekuwa mkristo na tuoane ili tulee mtoto pamoja ila mwisho wa siku mwanaume akazingua na kuoa mwanamke mwingine. Niliumia sana na kuona kama dunia imenitenga, nikarudi kwa wazazi na wakanisaidia kumlea Yule mtoto, ndipo nikapata mwanaume wa kuishi nae ambaye pia alihitaji nimzalie mtoto. Nikazaa mtoto, nikamuomba tuoane. Yule mwanaume alikuwa ni Mwislamu kama mimi ila alipodokezewa na watu kuwa mimi nimewahi kubadili dini aliniacha na kusema hawezi kuoana na mwanamke kigeugeu, nikaumia sana na hata hivyo hakumpenda kabisa mwanangu wa kwanza. Ndio kwenda nikampata baba yenu Jose, akaahidi kunioa, nikamuuliza wewe ni mkristo utawezaje kunioa na mimi wakati una mke? Akaniambia nisiwe na shaka kwani kuna wakristo wanaishi na wake wawili, akanitaka nibadili dini, nikabadili tena yani kwa kifupi sikuwa na msimamo ila naye ndio yakanitokea yale yaliyonitokea. Erica, msimamo ni kitu chema sana katika maisha, usipende udhaifu ulikuangusha uendelee kukuangusha, yani ule udhaifu chukulia kama changamoto katika maisha yako. Mimi nilifanya makosa sana sababu sikuwa na msimamo, ukikosa msimamo maisha yanakuwa ni machungu sana. Ushakosea ndio ila sio mwisho wa maisha yako, chagua maisha uyatakayo sasa, usikubali kubadili dini sababu ya mapenzi”
Gafla mama yake Erica akaingia ndani, ila cha ajabu alikuwa akitabasamu sana, kisha alianza kuongea,
“Nilichungulia kwanza na kukuona ni wewe, nilishikwa na gadhabu ya hali ya juu, ila niliposikia ulichokuwa ukimshauri mwanangu kwa hakika kimenigusa sana. Nakushukuru mdogo wangu, umemshauri jambo jema mwanangu”
Kisha mama Derick akainuka na kukumbatiana na mama Erica, huku wakiongea mambo mbalimbali kanakwamba hawajawahi kugombana katika maisha yao yote, mama Erica alizidi kumshukuru mama Derick kisha akamuuliza,
“Ila kwanini umemshauri Erica asibadili dini ikiwa ni dini yako? Huoni kama utaongeza muumini?”
“Sikia dada, dini ni zaidi ya tunavyoitafakari, unatakiwa kuhamia dini nyingine kwa kuamua kutoka moyoni sio sababu ya mapenzi. Kubadili dini sababu ya mapenzi ni kumchezea Mwenyezi Mungu na kukosa msimamo, akija huyu utamfata, akija huyu utabadili tena, dhana ya kusema mwanamke hana dini tuiache. Inasemekana hivyo sababu inajulikana mwanamke hana msimamo, ila tungekuwa na msimamo basi isingesemekana kuwa mwanamke hana dini. Mimi naamini kuwa kama mtu anakupenda kweli basi ndoa mtafunga nae tu, mbona za bomani zipo? Mkiishi ndani na kuiona dini ya mwenzio nzuri, umeielewa vizuri unaweza kuifuata ila sio kufuata sababu ni lazima kufuata yani utajikuta hutendi vile inavyopaswa kutenda. Tufikie hatua ya kubadili dini ikiwa tumeielewa vyema dini tunayoiendea”
“Kwahiyo kwasasa wewe ni dini gani?”
Mama Derick alicheka kisha akasema,
“Nilirudi kwenye dini yangu, niliomba toba basi nikarudi, najua nilikosea sana na ndiomana nasema ili mwingine asikosee kama mimi. Maisha yanataka msimamo, ila ukikosa msimamo tu basi utasumbuliwa sana na maisha, sikuwa na msimamo mimi jamani yani kipindi kile hata mpagani angetokea basi ningemfata yani maisha niliona yamenibadilikia kabisa. Ila saivi nina misimamo yangu yani sitaki kutetereshwa”
“nashukuru kwa ushauri wako kwa binti yangu, Erica umesikia ushauri huo sasa ole wako ubadili dini”
“Dada usimwambie hivyo, unatakiwa tu kumfundisha, unajua unapomwambia ole wako usibadili dini bado hujafanya kitu. Ila mpe mafundisho ya dini yako ilia pate ugumu kwenye nafsi yake mwenyewe akifikiria swala la kubadili sio ole wako usibadili, bado hujafanya kitu hapo. Wanawake sie akili zetu tunazijua wenyewe yani, unatakiwa tu uwe mpole dada yangu”
“Nimekuelewa”
Wakaendelea na maongezi mengine hadi pale mama Derick alipoaga, Erica aliamua kumsindikiza kidogo ambapo huyu mama aliendelea kumshauri,
“Erica kutenda kosa si kosa bali kurudia kosa, usije ukasubiri kurudia makosa, umeshatenda kosa angalia mstakabali wa maisha yako”
“Sasa sitaolewa?”
“Kama huyo mwanaume anakupenda basi atakuoa tu bila kujali dini, na pia usijiwekee kuwa asipokuoa ndio mwisho, huyo ni mmoja tu ila kuna wengi wanaotamani uwe mke kwahiyo usikate tamaa”
“Nashukuru kwa ushauri wako”
Akaagana nae kisha Erica akarudi ndani kwao.
 
SEHEMU YA 194

Erica akiwa amekaa nyumbani, leo kwa mara ya kwanza aliamua kumpigia simu Bahati maana ni muda mrefu hakuwasiliana nae. Yeye ndio mwenye namba za Bahati ila Bahati hana namba zake sababu alibadilisha, kwakweli Bahati alihisi hata kuchanganyikiwa ile kuzungumza na Erica,
“Kwa hakika ningekuwa Dar, basi leo ningekuja nyumbani kwenu kukusalimia yani nimefurahi sana Erica”
“Uko wapi kwani?”
“Nipo Tanga, kuna mzigo nimeufata ila nikirudi tu Dar nakuja kwenu”
“Sawa, ila ngoja nikuulize jambo. Mimi mkristo na wewe Mwislamu hivi tukitaka kuoana tutaoana kwa ndoa ipi?”
“Erica jamani, hapo si ndoa ya bomani tu. Upo tayari nije nikuoe Erica”
“Hapana, nimekuuliza tu”
“Jamani Erica, unaumiza moyo wangu ila najua ipo siku tu utakubali niwe mume wako”
Basi Erica alikata simu huku akiwaza kuwa endapo Bahati akigundua kuwa ana mtoto itakuwaje? Alijikuta na mawazo pia, ila akaendelea kujipa imani kuwa kuna muda Rahim atafikiria pia kufunga nae ndoa bomani.
Akiwa kule chumbani, alimuona mama yake alifika na kumuita,
“Erica, kuna mgeni wako”
Ikabidi ajiandae na kutoka nje ili kuangalia ni nani huyo mgeni.
Alifika na kushangaa kuwa mgeni mwenyewe ni Babuu,
“Nimeona kimya sana Erica, leo nimeamua kujitoa muhanga na kuja kwenu”
“Karibu”
Muda kidogo mtoto wa Erica akaamka na kuanza kulia, mama yake Erica alifika sebleni na kumwambia Erica,
“Kanyonyeshe mtoto kaamka huko”
Ikabidi Erica aende ndani kumnyonyesha mwanae, Babuu alikuwa akishangaa tu kuwa Erica ana mtoto.
Baada ya muda Erica alirudi na kumtoa Babuu nje kwani hakutaka Babuu amuone mtoto wake,
“Erica umenitoa nje ili nisijue kama una mtoto jamani! Ila mbona nimesikia mama akisema ukamnyonyeshe, Erica unaficha hata mtoto. Kamlete basi nimuone”
“Kalala”
“Haya, si ulisema utazaa ukiolewa, kikowapi sasa? Erica si bora hata mimi ningekuoa kwanza ndio nikuzalishe, huyo mchumba uliyesema unae ndio kakuzalisha kabla ya ndoa? Pole ila atakuoa tu, nilikupenda sana Erica dah na bado nakupenda”
“Sema kilichokuleta uende”
“Jamani Erica usiwe na hasira hivyo, nilipita kukusalimia tu. Leo nilikuja mitaa ya huku kwenu kuna ukumbi wa harusi nilikuja kuuangalia maana ndio tumeshauriwa tutumie ukumbi huo”
“Harusi ya nani? Unaoa?”
“Hapana, mimi kuoa bado. Unakumbuka siku ile uwanja wa ndege ulinikimbia, sasa nilikutana na ndugu yangu Yule niliyekusimulia ndio anaoa”
Erica alihisi kama tumbo la uzazi linamcheza na kuuliza kwa makini,
“Anamuoa nani sasa?”
“Yani wanaume sisi dah! Yule jamaa kachezea mabinti wengi sana, halafu anakuja kuoa msichana mwingine aliyetunziwa. Binti mwenyewe anakaa kwa mama yake, anaitwa Salma”
Yani hapo alihisi kama tumbo la kuendesha limemshika gafla.
 
SEHEMU YA 195

Erica alihisi kama tumbo la uzazi linamcheza na kuuliza kwa makini,
“Anamuoa nani sasa?”
“Yani wanaume sisi dah! Yule jamaa kachezea mabinti wengi sana, halafu anakuja kuoa msichana mwingine aliyetunziwa. Binti mwenyewe anakaa kwa mama yake, anaitwa Salma”
Yani hapo alihisi kama tumbo la kuendesha limemshika gafla.
Badiliko la Erica hata Babuu alilifahamu na kufanya amuulize kwa makini zaidi,
“Erica sikuelewi nini tatizo?”
“Sijisikii vizuri, kwaheri”
Akamuacha Babuu pale nje kisha yeye akaingia ndani kwao, moja kwa moja alienda uwani kwanza maana alihisi tumbo lake si zuri. Na alipotoka aliingia chumbani kwake na kujifungia mlango ambapo alilia sana, yani alilia kupita siku zote alizowahi kulia sababu ya mapenzi,
“Hivi wanaume kwanini mpo hivi jamani? Yani umeniharibia maisha, umenizalisha mtoto halafu leo unaoa msichana mwingine kweli? Kwanini mimi nina kasoro gani? Kwanini wanaume wote hawawi na moyo kama wa Bahati, mbona Bahati ana upendo sana jamani?”
Erica alikosa raha kabisa, na alikuwa analia tu hata anamnyonyesha mwanae huku akilia kiasi kwamba mama yake alihisi kitu na kwenda kumgongea mlango kwani alivyoufungua aligundua kuwa umefungwa.
Erica alifuta machozi na kwenda kumfungulia mama yake,
“Mwanangu, umejifungia mwenyewe chumbani. Ila kujifungia chumbani sio vizuri, hebu njoo na sebleni kidogo na mtoto”
“Sawa nakuja mama”
Kuna jambo mama Erica alilielewa kutokana na ile sauti ya Erica, kisha alimuangalia mwanae kwa simanzi sana na kwenda kumbeba mjukuu wake kisha kumwambia Erica amfate sebleni.
Erica alienda sebleni alipo mama yake, Yule mama alimshika vizuri mtoto wa Erica kwa mtindo wa kumrusha rusha akisema,
“Mjukuu wangu mzuri mwenyewe yani anastahili kuitwa Angel, huyu mtoto ni mzuri mwanangu yani kazuri sana. Hivi Erica umeuona kweli uzuri wa mwanao huyu?”
“Ndio mama, ni mzuri ndio ila naikumbuka kauli yako bado kuwa uzuri wa mtoto haujakamilika kama hana baba”
“Ndio, mtoto anatakiwa kuwa na baba na mama ila mtoto anapokosa baba inaashiria nini? Prngine mama humjui baba wa mtoto au baba kamkana mtoto wake, ila kwa yote ni mtoto kulelewa kwenye maadili yanayofaa ingawa akiwa na baba inapendeza zaidi. Kwani baba yake kasemaje?”
Erica alikuwa kimya tu hakumjibu mama yake, kisha mama yake akaendelea kuongea,
“Erica, inaonyesha ulikuwa unalia. Haya nini kinachokuliza?”
“Hapana mama silii”
“Erica usinifiche nakujua vizuri sana, mwanangu ni kweli umefanya makosa na umenitia aibu sana ila ni wakati sasa wa kuongea na huyo mwenzio ili tujue mstakabali wake kuhusu huyu mtoto. Sasa ukilia Erica inasaidia nini? Hapa tunaangalia maisha ya huyu Angel, kuna leo na kesho mtoto anapaswa kumujua baba yake, usifikirie ninavyokuuliza uliza sikupendi, tena nakupenda sana sana mwanangu hujui tu”
“Nimekuelewa mama”
“Kama unanielewa basi usikazane kulia ila kazana kumwambia huyu mwanaume afike hapa nyumbani, najua mwanangu wewe sio malaya kiasi cha kutokumjua baba wa mtoto wako. Ni dhahiri unamtambua naye pia anajua, basi tumia elimu yako kumfanya aje hapa nyumbani”
“Sawa mama”
Erica aliitikia ila alijua yote anayotasema mama yake hayawezekani maana mwanaume mwenyewe ndio amepata taarifa kuwa anataka kuoa.
 
SEHEMU YA 196

Usiku ulipofika Erica aliingia kwenye mtandao wa kijamii ili awasiliane na Rahim, aliamua kupiga moyo konde na kumuuliza muhusika, kwani alipenda kufahamu mbichi na mbivu kutoka kwenye kinywa cha muhusika. Kwa kipindi hicho haikuwa kama zamani kwani mawasiliano yake na Rahim yalipungua wakati kuna muda hadi alikuwa akimtafuta kwenye simu ya kawaida ila sio kwa kipindi hiki yani Erica ndio alikuwa akimvizia ili akimuona hewani kwenye facebook basi awasiliane nae, na kwa bahati siku hiyo alimkuta hewani na kumsalimia kisha kuanza kushusha makala yake ya malalamiko,
“Hivi Rahim kipi nilichokutenda kibaya mimi mpaka kunifanyia hivi? Ulishindwa kusema kuwa Erica nipo na wewe tu ila sikuoi? Hivi kweli mimi ni wa kusikia kuwa Rahim unaoa? Tena unamuoa Yule Yule Salma uliyesema umetafutiwa tu hata humtaki? Rahim, hukutaka niwe karibu na mama yako sababu hukutaka nijue ukweli kuhusu mambo unayoyafanya. Rahim wewe wa kunichezea mimi na kuniacha kweli jamani? Liko wapi neno ulilokuwa unasema siku zote kuwa Erica nakupenda sana? Ulisema nibadili dini kama njia tu ya kufanya kuwa imeshindikana kunioa sababu ya dini ila kiukweli ulishapanga yote haya. Umeniumiza Rahim ila Mungu atanilipia”
Alimtumia huo ujumbe huku akisubiri jibu kutoka kwa Rahim, alitegemea atajibiwa makala pia, ila alijibiwa kwa kifupi tu,
“Erica, sikuelewi”
Erica alishikwa na hasira sana na kumuuliza huku akiwa na jazba,
“Hunielewi nini Rahim wakati unaoa?”
“Namuoa nani?”
“Si unamuoa Salma”
“Hizo habari nani amekupa?”
“Unadhani duniani kuna siri? Hakuna siri duniani, mambo yaote yako wazi, najua kama unaoa Rahim ila ulichonifanyia sio sawa”
“Erica, usipende kusikiliza maneno ya watu. Sasa mimi kama naoa nikufiche ili iweje? Kipi naogopa kutoka kwako, usinikere bhana. Kwanza ni usiku sana saa hizi huko hebu lala, unanitesea mwanangu na masimu simu yako”
Erica alisoma huu ujumbe mara mbili mbili na kuona kweli thamani yake imeshuka maana Rahim hata hakujali kuhusu maumivu yake ya moyo zaidi ya kumtaka alale, kiukweli Erica hakuweza kulala kabisa sababu ya mawazo kwani aliwaza sana bila ya kuwa na majibu na alijiona kama kuna kitu kimepunguka katika maisha yake.
Aliendelea kuperuzi facebook ingawa Rahim hakuonekana tena hewani toka muda aliomwambia alale, wakati anaperuzi akakutana na mtu kaandika,
“Yani mimi mwanaume akijifanya anafanya siri eti rafiki zake wasinijue sijui ndugu wasinijue, yani siku nafika mbele yao namuaibisha balaa, na siku hiyo ndio atajua kichaa changu vizuri. Anikatae mbele ya hao asiotaka wanijue”
Akakuta kuna watu wamesapoti wangine wakicheka, wengine wakisema ndio kukomesha wanaume, yani aliona kila mmoja na wazo lake ila mawazo ya wengi yalikuwa yakusapoti kile kilichoandikwa, nay eye alijikuta akipata wazo jipya pale pale,
“Hivi kwanini nisiende hiyo siku ya harusi nikamuaibishe Rahim? Yani naenda na mtoto, hapo ndio watanijua vizuri, kila mmoja kwao atajua kuwa nimezaa na Rahim”
Ila akawaza pia kuwa atajuaje ratiba za ndoa ya Rahim? Aliona ni vyema kama atauliza kwa ujanja ujanja kwa kupitia Babuu ili ajue vizuri. Ila wakati ameafikiana na hilo wazo lake sasa, aliweza kupata moyo wa kulala.
Kulipokucha aliamua kumpigia simu Babuu ili kumuuliza hiyo sherehe ya ndugu yake ni linin a inafanyika ukumbi gani,
“Erica, kwani vipi? Unataka kuhudhuria?”
“Kwani vibaya nikihuduria?”
“Sio vibaya, ila niambie kwanini unataka kuhudhuria?”
“Babuu, mimi napenda sana vyakula vya kwenye sherehe halafu pia napendaga kuona watu wakicheza kwenye sherehe. Sijapata tu nafasi ya kuhudhuria sherehe mbali mbali ila napenda ndiomana nimekuuliza, hutaki nije jamani?”
“Basi hakuna tatizo, nitakuelekeza Erica. Na kama ukifika ukazuiliwa nipigie simu nitakuingiza”
Basi Babuu akamtajia sehemu hiyo sherehe itakuwepo, tarehe na muda, na Erica alimshukuru sana ila tu hakujua kuwa Erica ana mpango gani.
Baada ya hapo, Erica aliona sasa mpango wake wa kumuaibisha Rahim utatimia maana ataenda moja kwa moja kwenye harusi yao.
 
SEHEMU YA 197

Ilikuwa siku ya kumpeleka mwanae kliniki, kiukweli kwa siku zote za kumpeleka Yule mtoto wake kliniki alikodi gari kwani hakutaka mtu yeyote amuone, na alienda hospitali ya mbali na kwao kwani hakutaka hata kukutana na jirani yao na akagundulika kuwa ana mtoto kwani wengi watajiuliza kuwa harusi vipi, na siku hiyo kama kawaida alimpigia simu dereva wa gari za kukodi kisha kujiandaa na kusubiria afike ili ampeleke mtoto wake kliniki.
Wakati anatoka na lile gari, akamuona Tumaini akiwa amebeba pochi na boksi na alionekana kama anaelekea nyumbani kwao, alijiuliza sana
“Yule Tumaini anaenda kwetu kufanya nini? Au ndio zile zawadi alizosema ni Erick amenipa? Mungu wangu jamani, akijua kama nina mtoto itakuwaje? Erica mimi dah!”
Akachukua simu na kumpigia simu mama yake,
“Mama, kuna rafiki yangu nimemuona anakuja hapo nyumbani, nakuomba usimwambie chochote kama nina mtoto. Tafadhali mama yangu”
“Hadi kwa rafiki zako unaficha?”
“Nakuomba mama usimwambie”
“Kwahiyo nimwambie umekwenda wapi?”
“Mwambie nimeenda kwa dada, nitarudi kesho ili aondoke mapema. Akishaondoka unipigie simu nirudi nyumbani”
“Hahaha wewe mtoto loh! Unanifundisha mamako uongo kama wako”
“Nisaidie mama, nakuomba”
“Haya sawa”
Kisha Erica akakata ile simu na kuendelea na safari yao ya kliniki, alifika na kushuka na mwanae kisha Yule dereva kuondoka, yeye akampeleka mtoto kliniki na kumaliza mambo ya vipimo vya mtoto.
Wakati anatoka kliniki akiwa anataka kutafuta usafiri wa kumrudisha nyumbani kwao, akashtuka akishikwa bega, alipogeuka alikuwa ni Rehema rafiki wa dada yake, ambaye amewahi kumpa ushauri pindi anasoma kuwa asiendekeze wanaume,
“Kheee Erica kumbe una mtoto?”
Erica alikuwa kimya tu kwani kama alikumbwa na bumbuwazi na kushindwa hata kumjibu kuwa ana mtoto au la, kwani atakataaje ikiwa mtoto yupo nae mwenyewe, ila aliendelea kumwabia,
“Mtoto wako mzuri sana Erica, hongera mdogo wangu”
“Asante”
“Vipi sherehe za kimya kimya hata hatualikani jamani mdogo wangu?Umeolewan lini? ”
“Hamna dada sijaolewa, nimezaa tu”
Erica aliongea kwa aibu aibu flani hivi, Rehema alielewa na kumwambia,
“Ila usijali mdogo wangu, kuzaa kabla ya ndoa sio mwisho wa maisha na kuolewa kupo tu. Unaniona dada yako, nikikusimulia jinsi nilivyoteseka ni huyu mdudu anayeitwa mapenzi utanihurumia. Nilijua sitakuja kuolewa kamwe, maana nina watoto watatu halafu kila mtoto na baba yake yani kwa kifupi hadi nilishajikatia tamaa. Ila wiki ijayo ni harusi yangu, nitakuja kuwaletea kadi ya mualiko na pale nyumbani”
“Mmmh dada kwanini umeniambia yote hayo?”
“Nimekwambia haya mdogo wangu sababu nimeona sura yako wakati nimekuuliza swali la je umeolewa? Ukainamisha sura chini na kunijibu, hata usijisikie vibaya mdogo wangu, ngoja mambo yangu ya harusi yaishe nitakuja kuzungumza na wewe”
“Sawa dada nashukuru”
“Ila hongera sana mdogo wangu, umepata mtoto mzuri sana, mshikilie huyu yani mfanye kila kitu katika maisha yako na wala hao wanaume hawatakuumiza akili mdogo wangu”
Kisha akaagana nae na kutoka nje ya ile hospitali, akampigia simu mama yake akiulizia kama Yule mgeni ameshaondoka, alipoambiwa kuwa aliondoka alifurahi na kupanda gari kisha kumwambia dereva ampeleke kwao.
 
SEHEMU YA 198

Alifika nyumbani kwao na kumkuta mama yake, akamsalimia ila kabla hajauliza kuhusu mgeni aliyefika mama yake akamwambia,
“Mgeni wako kakuachia huu mzigo wako, amesema nikupatie halafu anasema mbona hupatikani hewani? Eti kakukumbuka sana”
“Aaah asante”
Erica akachukua lile boksi na kuingia nalo chumbani kwake huku akishikwa na kimuhemuhe kujua kuna nini kwenye lile boksi, kwavile mwanae alikuwa amelala akamlaza halafu akafunga mlango wa chumbani kwake na kuanza kufungua lile boksi.
Alipofungua, juu kabisa alikutana na kadi halafu na karatasi ndogo yenye maandishi, akaichukua na kuisoma,
“Kwako Erica, nimetumia njia ya zamani kidogo sababu najua kama tungeanza mapenzi yetu kipindi kile basi tungetumia njia hii pindi tungesoma shule za mbali mbali, ila Erica ulikubali maneno ya watu yatenganishe mapenzi yetu. Nakiri kukupenda toka siku ya kwanza kukuona darasani, wewe ni msichana wa kwanza kwangu kumpenda nab ado nakupenda toka kipindi kile. Ni mengi nimeambiwa na dada yangu kuhusu wewe, na picha nimetumiwa ila nikawaza sana kuwa kwanini maneno yaendelee kuharibu mahusiano yetu? Moyo wangu unaniambia kuwa wewe ndiye mama wa watoto wangu, inawezekana umepata habari kuwa nilikuwa na wasichana wengi sana na wengi walitamani kuzaa na mimi ila kwavile nimeshaipanga akili yangu kuwa nahitaji kuzaa na wewe basi siwezi kuzaa na yeyote Yule labda ukatae. Nikawa na msichana huku ila sina furaha maana wewe ndio umebeba furaha yangu, Erica nakupenda sana na pia najua kuwa unanipenda sana. Watu wengi husema ni vigumu wapendanao kuwishia pamoja ila najua kwetu itawezekana ikiwa tu tutaamua kuishi bila kusikiliza maneno ya watu. Upatapo ujumbe huu Erica tafadhali nitafute hewani, usiponitafuta najua ujumbe wangu hujaupata na kama nimeambiwa umeupata na hujanitafuta nitajua moyo wako haupo tena kwangu. Tunapendana Erica, naomba tuwe pamoja. Zawadi niliyokuwekea ni kitu ambacho ulionekana kuvutiwa nacho sana siku ile kwenye picha hotelini, hukujua ila kuna picha moja ulivutiwa nayo sana na ilikaa akilini mwangu na leo nimeweka zawadi hiyo kwenye boksi hili. Nakupenda Erica, ni mimi kipenzi chako Erick”
Chozi lilimtoka Erica kwani alijiona ni msichana mpumbavu kuliko wote maana alichoandikiwa na Erick ndio kitu alichokuwa anakitamani maisha yote ila atafanyaje sasa na ana mtoto na mwanaume mwingine? Je Erick atamuelewa kweli? Alihisi kama kuchanganyikiwa vile, kwani ukweli upo wazi anampenda sana Erick na alitamani siku moja aambiwe maneno aliyoambiwa na Erick kwenye barua, sasa bahati hiyo imemjia ila ana mtoto tayari, akisoma barua ya Erick anaona ni jinsi gani mwanaume huyo kajiuzuia asiwape wasichana mimba sababu anataka mtoto azae na Erica, vipi yeye aliyejiachia na kupata mimba na kusahau kabisa kama kuna Erick wakati anampenda sana? Alihisi kupagawa hata akashindwa kumtafuta Erick hewani na wala hakuendelea kulifungua lile boksi kwani alijua ni atajiumiza zaidi kwani anampenda sana Erick. Akainuka na kulibeba lile boksi kisha kuliweka kwenye kabati lake na kulifungia, alirudi kitandani na kuinama huku akilia kwani moyo wake uliumia kila alipofikiria kuhusu Erick maana ndiye mwanaume ampendaye ila Rahim ndiye baba wa Angel yani hapo alihisi akili yake inakengeuka.

Kesho yake alitumiwa ujumbe na Babuu,
“Ile shughuli ni leo”
Erica alishtuka sana na kisha kujiandaa ili awahi ukumbini maana aliambiwa saa tisa mpaka saa kumi itakuwa imeanza. Basi ilipofika saa kumi akamvalisha mwanae na kuita gari ili iwapeleke, wakati anataka kutoka tu mama yake akamuwahi,
“Haya haya, kiguu na njia. Miguu imeanza kukuwasha eeh! Unaenda wapi na mjukuu wangu?”
Kwavile hakujiandaa kusema chochote alijikuta akijiuma uma tu,
“Naenda kumsalimia Johari”
“Usinichekeshe mie, si wewe mwenyewe ulisema kuwa hutaki watu wajue kama una mtoto! Iweje utake kwenda kwa Johari na mtoto?”
“Aaah mama, sikuona mtu wa kumuachia hapa nyumbani, halafu Johari kaomba niende”
“Haya mlete”
Erica alimkabidhi mtoto mama yake, kisha mama yake akamwambia,
“Nenda mwenyewe huko unapotaka kwenda, mjukuu wangu niachie”
Kwakweli pozi lilimuisha gafla Erica maana hakuelewa kabisa, ila kwavile alishaita na gari ilibidi atoke tu ili aende.
Wakati anatoka getini ili apande gari, alimkuta Bahati nje ya geti ndio anataka kugonga.
 
SEHEMU YA 199

Erica alimkabidhi mtoto mama yake, kisha mama yake akamwambia,
“Nenda mwenyewe huko unapotaka kwenda, mjukuu wangu niachie”
Kwakweli pozi lilimuisha gafla Erica maana hakuelew kabisa, ila kwavile alishaita na gari ilibidi atoke tu ili aende.
Wakati anatoka getini ili apande gari, alimkuta Bahati nje ya geti ndio anataka kugonga.
Bahati alimsogelea Erica na kumkumbatia, ila gari nalo lilikuwa nje likimsubiri Erica, alimuangalia Bahati hakujua kwa muda huo amwambie kitu gani, Bahati alimuuliza Erica,
“Vipi mbona uko hivyo?”
“Kuna mahali natakiwa kuwahi”
“Basi twende wote”
“Aaah wewe nisubiri tu hapa”
Erica akasogelea lile gari na kufungua mlango ili aingie, ila Bahati akamshika mkono na kusema,
“Erica, nimeacha kazi zangu zote na nimekuja kwa lengo la kukuona wewe. Kumbuka hata ningekupigia simu yangu usingepokea, ila unataka kuondoka na kuniacha una maana gani? Nimekwambia twende wote hutaki”
“Bahati, nielewe yani kuwa muelewa pale mtu anaposema jamno. Niache niende, kuna mahali nawahi”
“Kwahiyo mimi sio wa muhimu?”
“Sijui kama unanielewa”
Ila kabla Bahati hajamuachia mkono, mara alitoka mama Erica pale nje na kumwambia Erica,
“Eeeeh afadhali bado hujaondoka, mtoto kacharuka mwenzangu”
Yani Erica ndio aliona hapo pamechanganywa maji na mafuta maana mama yake nae kaja kuvuruga tu kama kawaida. Ikabidi ampe Yule dereva pesa ya usumbufu, halafu aingie ndani ambapo Bahati nae alimfata nyuma huku akijiuliza maswali kuhusu mtoto aliyecharuka.

Erica aliingia ndani na kumchukua mtoto kwa mama yake kisha kwenda nae chumbani kumnyonyesha, kwahiyo sebleni alibaki mama Erica na Bahati. Ambapo Bahati alimsalimia vizuri sasa huyu mama, kisha huyu mama alianza kwa kumuomba msamaha,
“Nisamehe mwanangu kwa yaliyopita, yani sikujua nilijua ndio unaniharibia mwanangu hadi tukakupeleka polisi. Nisamehe sana”
“Usijali mama”
“Yani kijana una moyo wewe, nilijua toka siku ile hutokuja tena nyumbani kwangu, ila umekuja jamani una moyo sana. Haya mwenzio huyo ana mtoto”
“Ana mtoto?”
“Ndio, kumbe hujui?”
“Sijui mama”
“Mtoto angekuwa wa Kiswahili tungekuhisi ni wewe ila mtoto ni wa kiarabu sijui kipemba na baba yake hajulikani”
Kiukweli Bahati alijihisi vibaya sana ila hakuweza kujionyesha pale kuwa kajihisi vibaya na hakuweza kumjibu zaidi huyu mama kwani maneno yale yaliujeruwi moyo wake, huku akitamani sana kusikia kutoka kwenye kinywa cha Erica maana bado hakuamini amini kama Erica ana mtoto.
Baada ya kimya kuzidi mama Erica alimuuliza tena Bahati,
“Utakunywa kinywaji gani?”
“Aaah usihangaike mama”
“Hapana sio nisihangaike, hujawahi kunywa chochote hapa nyumbani kwangu, leo nahitaji utie baraka kwa kunywa kitu kwenye nyumba yangu”
“Basi maji mama”
Basi mama Erica alienda kuleta maji na kumpa Bahati ambapo bahati alikunywa maji yale na kuyamaliza kwa muda mfupi tu kwani alihisi kama kuna kitu kimekaa kooni halafu Erica hakutoka chumbani wala nini, ikabidi wakati mama yake anarudisha kikombe aende na kumuita Erica.
Alimkuta kalala pembeni ya mwanaye,
“Yani Erica umeingia kumnyonyesha mtoto na kulala hapo hapo wakati kuna mtu anakusubiri kweli!”
Erica akashtuka na kukumbuka ni kweli Bahati alikuwa akimsubiria ila usingizi ulimpitia alivyokwenda kumyonyesha mtoto kitandani na kuwa na mawazo mengi kuhusu harusi aliyoambiwa ni ya Rahim. Akainuka ili akamsikilize Bahati, alipotoka mama yao alitoka nje na kuwaacha waendelee na maongezi.
Erica hakuongea chochote ila Bahati ndio alianza kuongea,
“Erica kumbe una mtoto? Mbona hukuniambia?”
Erica alikuwa kimya tu, na Bahati aliendelea kuongea
“Ungeniambia mapema Erica, unajua ni jinsi gani nakupenda na sipo tayari kuona ukiaibika. Mamako kaniambia kuwa baba wa mtoto hajulikani ila ungeniambia mapema ingekuwa rahisi kuliweka sawa swala hili. Naweza kuwa baba wa mtoto, haijalishi mtoto huyo anaonekanaje, mama kasema sijui ni mwarabu au mpemba, ninachojua mimi ni kuwa kitanda hakizai haramu, naweza kuwa baba wa mtoto Erica sio sawa kuwa na mawazo kiasi hiko. Yani unapatwa na tatizo unashindwa hata kunishirikisha jamani Erica? Ulihisi nitakataa au?”
Erica alikaa kimya tu ila alikuwa akijiuliza kuwa Bahati ana upendo wa aina gani maana alikuwa ni tofauti na wanaume wote ulimwenguni, alishangaa sana kwani hakujua kama kuna wanaume wenye moyo kama wa Bahati, kwakweli alimshangaa sana na kubaki akimuangalia tu bila ya kumjibu. Bahati aliendelea kuongea,
“Sema neno lolote nielewe Erica, mimi nipo kwaajili yako”
“Nashukuru sana kusikia kuwa bado upo kwaajili yangu, ila kuhusu mtoto haikuwa nafasi nzuri kwa leo kuliongelea hilo swala. Nilitaka nikutafute kwa muda wangu nikueleze ila kwavile umejua sina budi kukwambia, ni kweli nina mtoto na kuhusu swala la baba wa mtoto bado ni kitendawili kwangu. Ila bado nina msimamo wangu ule ule wa tafuta pesa kwa bidii Bahati ili leo na kesho mkeo na watoto wako wafurahie uwepo wako”
“Mke wangu ni wewe na mtoto wangu wa kwanza ni huyo uliyemzaa wewe Erica, nitafanya kazi kwa bidii kweli ili mimi,wewe na mtoto wetu tuishi vizuri. Na kwa hakika kabisa Erica huwezi amini ambayo Mungu katutendea, najua ulishakosea ila hujakosea bado maana hujanikosa mimi. Biashara yetu imekuwa kubwa sana, yani huwezi amini samaki wamekuwa na soko kubwa ambalo sikulitegemea, pia nilikuanzishia biashara ambayo nilisema utaifanya ukimaliza chuo ila sababu unalea acha niendelee tu kuifanya”
“Ni biashara gani?”
“Erica, siwezi kutoka nje ya ufugaji kwahiyo biashara ambayo nilianzisha ni ya kuku wa kienjyeji. Uwiii natamani uone jinsi biashara hiyo ilivyo na neema yani Erica jamani biashara imekuwa kubwa naogopa, na juzi nilikuwa mkoani kuchukua kuku wengine niliagizwa. Na leo nilikuwa nabahatisha tu, ila kwasasa nitakuletea kuku na samaki uwe unakunywa na supu kwaajili ya afya yako na mtoto”
Mara mtoto wa Erica alianza kulia, na Erica akainuka ili akamchukue, Bahati akamwambia,
“Naomba uniletee mwanetu nimuone Erica”
Basi Erica alipotoka ndani alitoka na mtoto, ambapo Bahati alimshika mtoto Yule na alionekana kumfurahia balaa kama mwanae vile.
Bahati hakuondoka mapema kwakina Erica na kuzidi kufanya Erica kukosa muda kabisa hata wa kwenda tena ukumbini kama alivyopanga, basi kwenye mida ya saa mbili na nusu usiku ndipo Bahati alipoaga kuwa anaenda, alimwambia Erica amuitie mama yake ili amuage ambapo Erica alifanya hivyo, wakati mama yake anatoka Erica alienda kumlaza mtoto ndani, kwahiyo mama Erica alivyofika sebleni alimkuta Bahati akijiandaa kuondoka, Bahati akampa mkono wa kwaheri mama Erica ambapo alimwachia na pesa,
“Asante mama, kwaheri. Tutaonana tena”
Mama yake Erica alitabasamu sana na kuendelea kumkaribisha hadi Erica alipotoka na kumsindikiza hadi getini na kumuaga.
Erica alirudi ndani na kumkuta mama yake akiwa ameshika hela mkononi,
“Kheee mama, hela za nini unaenda wapi?”
“Naenda wapi? Nimepewa hela na baba Angel”
“Baba Angel! Sikuelewi mama”
“Si Yule kijana kanipa hela, yani sikujua kama Yule kijana ana moyo wa upendo kiasi hiki”
“Kakupa shilingi ngapi? Mama bhana, sasa Yule kijana kawa baba Angel toka lini?”
“Yule ndio baba Angel mwanangu, ona alivyokaa kumbembeleza mtoto hapa. Yale ile ndio aina ya wanaume wanaotakiwa ulimwenguni. Kanipa elfu hamsini ya pole ya kulea mzazi, nimefurahi sana hata kama mtoto mwarabu ila Yule ndio baba yake”
Erica alimuangalia mama yake ambaye alienda chumbani nay eye akaenda chumbani pia.
 
SEHEMU YA 200


Erica alimfikiria sana mama yake na kumkosea jibu kabisa,
“Mama yangu anashangaza sana, siku zote anasema mwanaume mwenye hela ndio mwanaume halafu mimi kuzaa lawama zote kanipa haya leo kapewa hela na Bahati kaanza kumsifia kuwa ndio mwanaume. Dah jamani mama yangu ni balaa”
Kisha akainuka na kwenda kuoga, halafu kula na kurudi na mawazo yake ila kiukweli swala la Bahati lilimchanganya sana yani alishindwa kuelewa kuwa Bahati ni mwanaume wa aina gani ambaye huwa haoni maovu kwake,
“Yani yeye kila kitu kwangu ni sawa, jamani kwanini wanaume wengine wasiwe kama Bahati? Laiti Erick angekuwa na moyo wa Bahati ningefurahi sana, lakini akijua nina mtoto najua upendo wake kwangu utaishia hapohapo. Au anaweza kuwa na moyo kama Bahati! Jamani Bahati mbona yupo tofauti sana na wanaume wengine?”
Hakupata jibu ila aliingia kwenye mtandao ilia one kama Rahim yupo amuulize maswali yake ila cha kushangaza siku hiyo hakumkuta kabisa Rahim hewani na kumfanya aamini kuwa ni kweli alikuwa ameoa, roho ilimuuma sana na kumfanya ashindwe hata kupata usingizi tena kwa mawazo. Mwanae alipokuwa akiamka alikuwa akiongea nae kama mtoto anayesikia,
“Angel mwanangu, wanawake tuna mitihani mingi sana ila nisingependa ukikua uwe kama mimi. Napenda uwe ni mtoto wa kusikiliza ushauri na kuupima, ona mama yako nilimuamini baba yako ila kaniacha na kwenda kuoa mwanamke mwingine. Baba yako katuacha Angel, haoni thamani yetu”
Machozi nayo yalikuwa yakimtoka na kumkosesha raha kabisa yani siku hiyo hakulala kabisa na alikuwa akigalagala tu kitandani, akainuka na kwenda kuchukua lile boksi alilotumiwa na Erick na kutoa ile barua ya Erick akaisoma tena na kulia haswaaa kwani muda huu ni kama alikuwa akitonesha kidonda chake kwani hawezi kupingana na ukweli kuwa Erick ndiye mwanaume anayempenda sana ila tu maisha ndio yaliyomtenganisha naye. Bado hakuwa na ujasiri wa kufungua zawadi alizoletewa na Erick, alirudisha lile boksi kabatini ila safari hii hakulifunga kabati. Alirudi kitandani na ile barua aliyoandikiwa na Erick, alikuwa akiibusu huku akilia sana kisha akafungua mkoba wake na kuiweka kwani alitaka kila muda akiitaka aichukue tu na kuisoma imchome moyo wake, kwani alijiona kuwa anastahili kuchomwa moyo.
Siku hiyo alijikuta yuko macho hadi alfajiri kabisa kwahiyo ile asubuhi ndio akalala, tena alilala sana ule usingizi wa hoi kabisa.

Ilikuwa kwenye mida ya saa tano na nusu asubuhi ambapo Erica aliamshwa na dada yake Bite,
“Loh! Yani wewe unalala kama mzigo? Ndio kusema mtoto kakusumbua sana usiku au? Mama kamchukua mtoto kamuogesha hadi mtoto kalala tena ila wewe bado umelala”
Erica aliinuka ila macho yalikuwa mazito sana ni kweli mamake wakati anamchukua mtoto kumuogesha alimsikia ila alishindwa kumjibu sababu ya usingizi, na hakukumbuka chochote zaidi ya kulala, basi akaamka pale na kumsalimia dada yake ambapo dada yake alimwambia akaoge ilia pate nguvu kwahiyo Erica aliinuka na kwenda kuoga ili kupata nguvu na kuondoa uchovu wa usiku.
Erica alipotoka kuoga alimshangaa dada yake akiwa kitandani na lile boksi yani kashalipekua lote na alikuwa ameshika vitu vya kwenye lile boksi, Erica alimshangaa dada yake,
“Kheee dada!”
“Unashangaa nini Erica? Kwani ni dhambi mimi kuona zawadi ulizoletewa na baba Angel?”
“Nani kakuonyesha hilo boksi dada?”
“Nilikuwa natafuta mtandio ndio nikafungua kabati lako na kukutana na hili boksi, oooh kumbe baba Angel anakupenda kiasi hiki!”
Ilibidi tu Erica awe mpole maana kama boksi dada yake alishalisaula na kila kitu kilikuwa juu kwahiyo hata kama hakupenda kuviangalia ilibidi aangalie tu, na kumuuliza dada yake,
“Kwanini unasema ananipenda?”
“Unajua ukiona mwanaume anakuletea zawadi hadi ya nguo ya ndani ujue anakupenda sana, anakujali yani huyo mwanaume usimuache”
Kisha dada yake alizishika zile nguo za ndani na kuzitathmini vizuri huku akisema,
“Ooooh ni nzuri hizo, mdogo wangu una bahati sana. Nimeishi na James kwa miaka mingi, hadi tumepata mtoto, amekuwa na kuchangamka sasa, anaita hata baba ila James hajawahi kuniletea zawadi ya nguo ya ndani hata ndotoni. Siku zote nimekuwa nikijisifia kuwa James ananipenda sababu ananipa pesa lakini pesa sio kila kitu katika maisha. Kuna vitu vingi zaidi ya pesa, kama mtu kukujali na kukuthamini. Baba Angel simfahamu ila kwa zawadi hizi kwa hakika anakupenda”
“Dada jamani, yani kwa zawadi tu ndio kusema mwanaume ana upendo jamani!”
“Ndio, hebu angalia huu mkoba aliokuletea yani dah mtamu huo unavutia hata kuuangalia, mwanaume anajua kuchagua jamani, sijapata kuona.”
Erica alimuangalia dada yake alivyokuwa akisifia vitu vilivyoletwa na Erick akijua ni baba yake Angel kumbe ni mtu mwingine kabisa maana baba Angel yupo mahali akila raha zake.
“Ngoja nikuulize dada, mapenzi ni nini?”
“Mapenzi ni kupendana, yani ukipendana na mume wako utajiona kama upo dunia nyingine sababu unaishi na mtu anayekupenda na wewe unampenda. Ila kuishi na mtu unayempenda halafu yeye hakupendi ni mzigo na kuishi na mtu anayekupenda halafu wewe humpendi ni mzigo. Ubaya wa mapenzi upo sehemu moja, kuna watu ni waigizaji nalaa, yani anaweza kukuigizia anakupenda kufa na kupona hadi ukaweka moyo wako kwa mtu wa aina hiyo na mwisho wa siku unaumia na kujiuliza kuwa huyu mtu si alikuwa ananipenda! Imekuwaje tena! Kumbe alikuwa anakuigizia, yani kupenda bhana kupo automatic kuna viashiria Fulani ukiviangalia kwa mtu unaelewa kuwa huyu ananipenda haswaa na ukiangalia kwa mwingine unaona kuwa huyu hakuna lolote ila na stress zake tu ndio anakuja kumalizia kwangu kwa kujifanya kuwa ananipenda.”
“Wewe na shemeji mpo kwenye kundi gani? Mnapendana?”
“Jamani mambo ya mimi na James aache tu, mwanaume ni muigizaji Yule sijapata kuona. Niliamini napendwa balaa, nikajitoa kwa moyo wangu wote na kumpenda pia, jamani hadi nimezaa huyu mtoto ndio nimekuja kujua James hakuwa na mapenzi na mimi kama nilivyofikiria ila navumilia nitafanyaje sasa. Nahitaji mwanangu apate malezi ya baba na mama, halafu siwezi kumkimbia James niache nafasi kwa lile janamke lisilokuwa na akili kurudi pale kwangu. Erica mdogo wangu, mapenzi yanaumiza kichwa sana, mshikilie huyu baba Angel, anaonyesha anakupenda sana na inaonyesha na wewe mnampenda. Utaishi nae vizuri mlee mtoto wenu”
“Haya dada asante”
Erica aliamua kuitikia ilia amridhishe dada yake ila kiukweli alikuwa anaumizwa sana, alianza kuvaa kisha dada yake akamwambia kuwa alimfata sababu alikuwa na shida nae amsindikize mahali,kisha dada yake alitangulia sebleni ambapo Erica alijiandaa halafu akabeba zile zawadi ambazo dada yake amezisasambua pale kitandani na kuzirudisha kwenye boksi kisha kuweka kabatini kwake ila alikuwa na mawazo sana kiasi kwamba hakujua mume yupi ni sahihi kwake, alitoka sebleni ikambidi akamue maziwa ya kumuachia mtoto wake halafu wakamuacha na mama yao na wenyewe kuondoka.

itaendelea
 
SEHEMU YA 201


Wakiwa kwenye gari ya Bite, Erica alimuuliza dada yake,
“Ni wapi huko tunaenda dada?”
“Sikutaka tu kusema nyumbani ili mama asijue, nimemdanganya kuwa kuna mkopo nataka kuchukua inabidi Erica akanisainie. Ila kiukweli mdogo wangu, dada yako hapa nimechanganyikiwa kabisa, yani mapenzi yananichanganya haswaaa.”
“Kivipi dada?”
“Si Yule msichana mjinga nae ana mtoto, nasikia James kampangishia nyumba mahali na anamuhudumia. Tatizo sio kumuhudumia, tatizo ni kuwa James anashinda huko jamani yani James asikii wala haoni, huwezi kuamini siku hizi hadi nyumbani harudi yani akili yangu imegoma kufanya kazi kabisa.”
“Kheee makubwa, sasa tunaenda wapi dada?”
“Tunaenda huko anapoishi huyo mwanamke, tukifika nataka wewe uingie ndani kwanza halafu mimi nitakuwa nje.”
“Sasa mimi nitaingia kufanya nini dada?”
“Nataka James ajue kama familia yote tumejua upuuzi anaoufanya, unajua sijamwambia dada Mage wala mama maana haya mambo ya aibu jamani yani dah! Huyu mwanaume siamini mwenzenu, sina raha kabisa yani. Sijui nitakuwaje nikihakikisha kuwa ni kweli James anakuwaga kwenye nyumba hiyo, nataka uingie ndani wewe kwanza, nitakuwepo nje nikisikilizia kama ni yeye au la kisha nitaingia na mimi”
Erica aliweza kumuona dada yake alivyoonyesha kuumizwa na swala hilo la shemeji yake, kwahiyo alikubali kwenda kumfumania shemeji yake.
Walifika na dada yake kwenda kupaki gari mahali, kisha wakashuka na kuanza kuelekea kwenye nyumba ambayo James alimpangia mwanamke wake, ila kwa bahati Yule mwanamke hakuwepo hapo ndani kwa muda huo alikuwa ameenda dukani.
Bite alikaa nje na kumtaka mdogo wake aingie ndani, Erica alifungua mlango na kuingia alimkuta James akiwa amekaa tu tena hana habari, Erica alimwambia kwa mshangao,
“Shemeji!”
“Kheee Erica! Umekuja kufanya nini?”
“Nikuulize wewe unafanya nini?”
“Jamani Erica kipenzi changu, yani anaacha kuwa na wivu dadako unakuwa na wivu wewe. Kweli tunapendana”
Bite alichukia sana kusikia maneno hayo.



 
SEHEMU YA 202

Bite alikaa nje na kumtaka mdogo wake aingie ndani, Erica alifungua mlango na kuingia alimkuta James akiwa amekaa tu tena hana habari, Erica alimwambia kwa mshangao,
“Shemeji!”
“Kheee Erica! Umekuja kufanya nini?”
“Nikuulize wewe unafanya nini?”
“Jamani Erica kipenzi changu, yani anaacha kuwa na wivu dadako unakuwa na wivu wewe. Kweli tunapendana”
Bite alichukia sana kusikia maneno hayo.
Kwakweli Bite hakuweza kuvumilia zaidi yay eye kuingia ndani pia, alimuangalia mumewe kwa gadhabu sana,
“James, hivi ni dharau kiasi gani unanionyesha? Umeona kuzaa na msichana wa kazi haitoshi, ukaamua kumpangishia nyumba na wewe kuzamia hukuhuku. Halafu bila haya unamuita mdogo wangu kipenzi chako eti mnapendana sana, hivi James una nini lakini?”
Bite alikuwa na hasira sana hata maneno hayo alikuwa akiongea huku machozi yakimtoka, James alikuwa kama amepigwa na butwaa vile maana hakufikiria kama Erica amefika na mkewe, kitendo cha James kukaa kimya kilimchukiza zaidi Bite na hasira zake alienda kumalizia kwenye vyombo vya nyumba ile,
“Unaniacha nyumbani, unaniambia siku hizi hela ngumu kumbe unakuja kutumbua kwa malaya wako huku”
Bite akaifata Tv na kuibeba juu kisha akaibwaga chini, James akashtuka akasema,
“Bite hebu acha uchizi huo”
Muda huo Bite alienda katika kabati la vyombo na kubwaga vyombo vyote vilivyokuwa kwenye lile kabati,
“Wewe Bite, kuwa na heshima basi. Nyumbani kwa watu hapa”
“Nyumbani kwa watu? Kwani mimi nyani? Yani mwanaume una roho mbaya wewe hata shetani anakuogopa, hivi ni wa kunifanyia vitendo vya ajabu kiasi hiki wewe? Hata humfikirii mtoto? Nimevunja ndio, wewe si tajiri, na ununue vingine”
Muda huo alikuwa anaelekea kwenye friji, ilibidi James atake kumfata, ila Bite aliwahi kisu mikononi mwake,
“Ukinifata tu wewe kenge nakuchoma, yani leo napelekwa jela na wewe unakufa halafu sijui mtoto atalelewa na nani”
James akamuangalia Erica na kumwambia,
“Erica nakuomba mtulize dada yako”
Kisha James aliruka nje na kutoka maana aliona pale ni balaa tupu kumbe hata mwanamke wake alikuwa amerudi ila baada ya kuona lile balaa alikimbia.
Erica alimuangalia tu dada yake, ni kweli aliona anachofanya dada yake si sawa ila alitambua kuwa dada yake anafanya yale kwa hasira tu na si vinginevyo. Sema alipaswa kumzuia kwani dada yake mwenyewe alionyesha kutokwa na damu kwamaana hiyo vile vyombo alivyopasua vingine vilimchoma, Erica alimuangalia dada yake,
“Dada, hasira haijengi. Hebu mfikirie Junior, hivi wewe ukienda jela na shemeji akifa halafu Junior akawa yatima kwa wazazi kujitakia hasara ya nani? Twende mahali dada yangu ukatulize hasira zako, achana na huyu mwanaume.”
“Erica, niache. Huyu mwanaume si hela inamuwasha, atanunua vingine”
“Ndio dada, ila ufanyacho sio suluhisho dada yangu, tuondoke”
Erica alijitahidi kumwambia dada yake maneno ya kumsihi hadi akakubali kuondoka, waliondoka na kwenda moja kwa moja walipoacha gari. Yani walipoingia tu Bite alianza kulia kamavile kafiwa kama sio aliyekuwa anaongea akitabasamu mwanzoni, hapo Erica akatambua kuwa mwanzoni dada yake alikuwa na hisia tu sababu kashaambiwa kila kitu sasa pale kathibitisha na macho yake kuwa kweli mumewe ana nyumba ndogo ndiomana imemuuma sana. Alilia sana kisha kuanza kuongea mwenyewe,
“Wanaume ni mbwa kabisa, yani wanaume hawafai. Lijitu unalipenda, unajitunza kwaajili yake jamani, kwani hakukuwa na vijana wengine walionitaka zaidi ya james? Ni vijana wengi walinitongoza mimi nab ado wengine wananitongoza ila nilijitunza kwaajili ya mume wangu, siku zote nilisema nampenda mume wangu, ndio chaguo langu nimepewa na Mungu na nilijua hata yeye ananipenda pia. Hata baada ya kuzaa na msichana wa kazi nikahisi kuwa ni bahati mbaya sababu sikuwa nyumbani, kumbe janaume lenyewe ni mbwa tena mbwa koko uuuwiii jamani mimi huyu mwanaume huyu”
Bite alikuwa akilia kama mtoto, mdogo wake alikuwa akimbembeleza na kumsihi kuwa waondoke mahali pale, ilibidi Erica ndio aendeshe gari, kwa bahati alikuwa amejifunza kuendesha gari maana bila ya hivyo wangebaki kubembelezana tu bila mwisho.



 
SEHEMU YA 203

Wakiwa kwenye gari, Erica aliona ni vyema waende nyumbani kwanza ila dada yake alimkataza na kumuomba ampeleke nyumbani kwake,
“Twende kwanza nyumbani kwangu nikamchukue Junior wangu”
Basi walienda hadi nyumbani kwa Bite na kumchukua mtoto tu, kisha akampa hela Yule mdada wa kazi na kumwambia aende kwao na atamwambia akimuhitaji tena, Yule msichana alishangaa ila ikabidi ajiandae na kuondoka kisha Bite akafuna milango na kupanda kwenye gari akiwa yeye, mtoto na Erica. Ila bado aliongea kwa uchungu sana,
“Nimejikuta nikimchukia na huyu mdada wa kazi wakati huyu hajanifanyia lolote baya, hivi kumbe mdada wa kazi anaweza kukuchukulia mume kabisa kabisa ukabaki umebung’aa tu. Ila uliniambia mdogo wangu, sema sikusikia mimi, nilijiamini napendwa, nilijiona nimepata kumbe nimepatikana.”
Alikuwa akitoa machozi tu hadi wanafika nyumbani kwao, aliingia ndani na hata mama yao akawashangaa kuwa tatizo ni nini,
“Bite, nini tatizo mwanangu imekuwaje tena? Si mlisema mnaenda kusaini mkopo? Imekuwaje tena”
“Mama, subiri nikueleze”
Bite hakuweza kumficha mama yake kwani hakuweza kukaa na lile jambo moyoni, alihisi moyo kulipuka tu muda wowote. Akamueleza mama yake kila kitu na hadi alivyoenda na Erica, jinsi alivyomsikia James akisema na Erica,
“Yani anathubutu hata kumuita mdogo wangu ni kipenzi cahake? Imeniuma sana”
“Yani kumbe Erica alituambia ukweli ila tuylimpuuzia”
“Alisema nini mama?”
“Alisema kuwa James alitaka kumbaka”
Yani hapo Bite ndio akashtuka zaidi baada ya kusikia kuwa mumewe alishawahi kutaka hata kumbaka mdogo wake, alimuita Erica ili amsikie Erica mwenyewe, na Erica hakuacha neno alimueleza kila kitu dada yake toka ile siku ya kwanza alivyotaka kumbaka,
“Jamani mdogo wangu, mbona hukuniambia?”
“Sikutaka kuvunja ndoa yenu dada”
“Hukutaka ila imevunjika sasa, mama simtaki tena James simtaki”
“Tulia mwanangu, ni hasira tu hizo. Tuliza hasira, Yule ni mumeo”
“Sitaki mama, James sio mume wangu kuanzia sasa”
Mama yao alijua tu ni hasira na hakuweza kumshauri kwa chochote kwa muda huo. Badala yake alimuacha na kumwambia aende chumbani akapumzike,
“Bite mwanangu hapa ni nyumbani kwenu, jisikie huru kabisa wala usibabaishwe na mambo ha mumeo ila ndio wanaume walivyo. Usijali mwanangu yatakwisha tu”
Alimwambia akapumzike huku Erica nae akienda chumbani kwake na mwanae.



 
SEHEMU YA 204


Kuna muda Erica aliwaza sana kuhusu mambo ya wanaume na kukosa jibu,
“Mfano ningejitunza, kwahiyo George angenioa sababu angenikuta bikra? Je angenipenda kweli au angekuwa kanipenda sababu ya bikra? Na je George ni mwanaume wa kuishi vizuri na mwanamke, ikiwa tu mimi aliniwekea kisasi cha kunibaka kwa kosa ambalo sio langu? Ningeolewa na aina hiyo ya mwanaume, si ndio yangekuwa haya haya ya dada Bite. Ila wanaume hawa wanawafikiria na kuwakosea jibu kabisa, hivi wote wangekuwa kama Bahati, hivi kuna mwanamke ulimwenguni hapa angelia jamani? Kwanini hawana moyo wa Bahati, hivi Bahati anaweza kumtenda mwanamke kweli? Hapana jamani”
Alijikuta akiwaza sana, na kujaribu kutmtafuta Rahim hata kwa muda huo ila bado hakumkuta hewani, na kumfanya ajipe asilimia mia moja kuwa Rahim ameoa kweli.
Alipoona dada yake amepumzika vya kutosha, akaona akamuulize maswali kadhaa ya kuhusu mapenzi maana alihisi lazima atakuwa na majibu maana tayari ameshaumia,
“Dada samahani, hivi katika maisha yako, mwanaume wako wa kwanza kumpenda ni shemeji?:”
“Sikia mdogo wangu, katika maisha yangu niliamini kuwa mwanaume asipokukuta bikra ndio anakusaliti na niliamini wanawake wote wanaosalitiwa ni kwavile hawakukutwa bikra, nilijua wanaume wengi wanapenda wanawake mabikira ni kweli wanapenda ila wanapenda kwavile anajisikia raha kusema wanawake kadhaa nimewatoa bikira zao ila sio kwa mapenzi. Nilijitunza mdogo wangu, nilijitunza sana, kuna mkaka mmoja nakumbuka vizuri, alikuwa anaitwa Deus, alinipenda sana na kuja kuja kunipa habari za kunitongoza mara kwa mara, nilijikuta nikianza kuvutiwa nae ila nikaona nitatenda dhambi bure, nikaamua kuwa nae mbali kabisa. Nilfata mafundisho ya mama, ni heri nikae kanisani kuliko kuwaza wanaume. Ilinisaidia sana kwani mawazo ya wanaume hayakuchukua nafasi katika akili yangu, ndipo akaja James, na tena huwezi amini ila James alikuja kanisani sababu yangu na kujifanya kaokoka pia, kwakweli niliona napendwa yani mwanaume anaacha vitu vyote vya anasa sababu tako, nikamkubali na akatangaza ndoa. Tulioana na kukaa kwenye ndoa kwa mwezi mmoja tu ndipo James akasafiri na kwenda nje, nilikuwa na furaha moyoni kwa kupata mwanaume mwenye upendo wa dhati, na zaidi ya yote ni mcha Mungu. Hiyo ilikuwa furaha yangu, ila kumbe sikumjua James vizuri, kipindi amerudi nchini ndio nimemjua James jamani, mwanaume kumbe ni mlevi balaa ila aliniigizia mimi tu kipindi cha uchumba kujifanya hanywi pombe ili niamini ni mlokole kweli. Sasa bora hata angekuwa ni mlevi tupu, kumbe ni mzinzi pia jamani, si kuleteana maradhi huku eeeh! Mi bora niishi mwenyewe tu”
“Pole dada, ila mapenzi yanaumiza sana. Hivi inakuwaje mtu upo hivi ila unapata mwanaume yuko hivi yani haendani na wewe. Na kwanini kwenye ndoa wengi wanalia? Yani wengine tunatamani kuolewa halafu wengine mmechoka kwanini?”
“Wewe tamani tu kuolewa, baba Angel anakupenda sana. Sio mimi niliyependwa kwa kupewa pesa tu na kununuliwa kile kigari ila sina furaha ya ndoa”
Erica alitamani amueleze dada yake kuhusu mikasa yake ya mapenzi ila aliona aibu na pia hakujua dada yake angemchukuliaje, kwahiyo alijikuta akiitikia tu kuwa kweli baba Angel ana upendo sana.
Wakaongea vitu mbali mbali na kushauriana mambo mbalimbali, ilikuwa ni jioni ambapo mama yao alienda kuwaita,
“Haya, mabosi wenye mawazo njooni mnywe supu mtulize mawazo yenu”
Walitoka na kwenda sebleni ambapo mama yao aliwawekea supu ya kuku, Bite alimuuliza mama yake,
“Kheee supu ya kuku! Umeenda kununua muda gani mama au wakati sie hatupo?”
“Hata sijanunua, kaja baba Angel kaleta kuku wane na misamaki kibao nimeweka kwenye friji. Mwaka huu hadi mtu fidenge amalize kunyonyesha na mimi nitakuwa nimefutuka”
Erica alielewa kuwa mama yake anamuongelea Bahati ila Bite hakuelewa bado alijua ni baba Angel aliyeleta zile zawadi ndio kaleta na hizo kuku na samaki,
“Kheee baba Angel ana upendo jamani. Mungu ambariki”
Akamgeukia mdogo wake na kumwambia,
“Mshikilie baba Angel mdogo wangu, huyu ndio mwanaume”
Erica alitabasamu tu na alipomaliza kunywa ile supu aliingia chumbani kwake na kumpigia simu Bahati,
“Kumbe ulikuja kwetu?”
“Ndio, ila sikukukuta nikaamua kumuachia mama mzigo”
“Ndio una kuku wengi sana nini hadi umeleta wane!”
“Erica, afya yako ni bora kuliko kitu chochote kile. Kuku wapo mama, wewe jilie tu na kama na kesho mtahitaji utaniambia”
“Hapana bhana, labda wiki ijayo, usilete tena”
“Basi nitakuja kumsalimia mtoto”
“Usije hadi nikwambie, sawa”
“Ila Erica usinifanyie hivyo. Unajua kama ndugu zangu wote nimewaambia kuwa nimezaa na wewe”
Kwakweli Erica alimshangaa Bahati kuwa akili yake ikoje hadi afikie hatua ya kuwaambia ndugu zake kuhusu mtoto ambaye anajua fika si wa kwake, alimshangaa sana. Aliongea nae na kukata simu.
Erica aliendelea na shughuli zingine ila barua ya Erick ilimkaa sana kichwani mwake, alitamani hata kumtafuta ila kilichomzuia ni swala la mtoto kuwa Erick akigundua ana mtoto itakuwaje?
“Ila nisipomtafuta pia atahisi simpendi tena. Ni kweli Bahati ananipenda sana na yupo tayari kuishi na mimi kwa hali yoyote ile lakini simpendi na hilo limekuwa tatizo kwangu, najitahidi balaa ila upendo kwake haupo hata kidogo. Nikiangalia upande wa Rahim, ni baba wa mwanangu pia nimejitolea kuishi nae ila inaonyesha hanipendi na alikuwa akinitumia tu. Maana halisi ya mapenzi kutokana na maneno ya dada nadhani nikiwa na Erick ndio nitakuwa nimekamilisha neno mapenzi kwangu, ila nawezaje kuwa na Erick wakati nishazaa na mwanaume mwingine? Oooh Erica mimi jamani yani sijielewi kabisa.”
Ni kweli hakujielewa, na alikuwa akijishughulisha na kazi za hapa na pale ili tu kupisha siku.


 
SEHEMU YA 205

Kesho yake alifika dada yao Mage maana alipata ile habari kwa mama yao kuhusu James, kwahiyo alifika ili azungumze na mdogo wake.
Muda ambao Mage alikaa kuzungumza na Bite ilikuwa ni chumbani kwa Erica kwahiyo Erica naye alikuwepo ndani. Mage alisema ili wote wajifunze, ila bado ilikuwa ngumu kwa Bite kukubaliana na jambo alilolisema mage,
“Dada sijui kama kuna jambo utasema nikaelewa, dada sirudi tena kwa James bora niishi mwenyewe tu”
“Bite, elewa jambo moja. Una mtoto sasa na mtoto anahitaji malezi ya baba na mama, unajua kila ndoa zinachangamoto nyingi. Najua utasema ya kwako imezidi ila ukisikia za wengine utaona ndio balaa, angalia maisha ya Junior kwasasa sio unajali tu furaha yako, jail na furaha ya mtoto”
“Dada sikuelewi, kwahiyo unanishauri nirudi tena kwa James!”
“Sikushauri kwa ubaya ila ndoa inahitaji uvumilivu wa hali ya juu na wala haiitahi usikilize maneno ya watu, najua si maneno ya kuambiwa ila ni kitu cha kushuhudia ila ni wewe unayeweza kuitetea ndoa yako na kuifanya isimame tena. Kuikimbia ndoa sio suluhisho katika ndoa yako”
“Ila suluhisho ni kuendelea kuishi mahali ambako unajua fika utapata ukimwi!”
“Bite, ukimwi si kuna kupima jamani? Mimi nakupa ushauri kwaajili ya mtoto wako, hakuna malezi bora kama ya baba na mama yani mtoto bora ni Yule anayelelewa na wazazi wawili. Kama mzazi mmoja amekufa basin a ijulikane amekufa sio yupo hai halafu haiwezekani kuishi nae au haiwezekani kuwa karibu na mtoto, jamani kumuweka mtoto mbali na baba yake ni kumsononesha mtoto”
Erica alikuwa ameinamia chini tu kwani kwa kiasi Fulani nae yale maneno yalimgusa, kisha dada yake Mage akamwambia,
“Na wewe, hakuna kitu chema kama mtoto kuwa na wazazi. Sasa wewe toka umlete huyu mpemba kwenye familia hii mbona baba yake hatumuoni? Tatizo nini?”
“Sasa dada nifanyeje?”
“Ufanyeje nini? Akuoe sasa”
“Kama hanitaki?”
“Hivi ulianzaje kuzaa na mtu asiyekutaka, yani Erica kuna muda unaongea kama sio msomi vile. Wewe umesoma, napenda kukwambia heshima ya mwanamke sio elimu yake tu bali kuwa kwenye ndoa sio kutangatanga na kuzaa hovyo”
Erica alikuwa kimya maana walipewa darasa ambalo hata hakujua kwa yeye atalichukuliaje hilo darasa maana kwa vitu vinavyoendelea kwake, alihisi kuchanganyikiwa tu na hilo darasa.
Mage aliwafundisha pale, na badaye kuongea zaidi na mdogo wake huku akimsihi kuwa amsamehe James na wakaishi walee mtoto wao, ila bado msimamo wa Bite ulikuwa palepale kuwa hawezi kumsamehe James.



 
SEHEMU YA 206

Siku hiyo Erica alihisi kila akifikiria kichwa chake kinavurugika tu, kwani tangu habari za ndoa ya Rahim, zilipita kama wiki mbili na Rahim hakupatikana hewani kabisa, kitu hicho kiliumiza sana moyo wa Erica kwani kila akikumbuka maneno ya dada yake kuwa mtoto anahitaji malezi ya baba na mama aliumia sana, kwani bado aliona itakuwa ngumu sana kumkubalia Bahati kuwa mtoto awe mtoto wake.
Akapata wazo moja kuwa aende nyumbani kwakina Rahim na akaongee na mama yake, akaona vyema akienda na mtoto kwani atakuwa na uthibitisho kwa mama yake Rahim kuwa amezaa na Rahim.
Akajiandaa kila kitu na kutaka kutoka ila kama kawaida mama yake alimzuia kutoka na mtoto,
“Jamani mama, sasa kama naenda nae kliniki!”
“Erica, sio mjinga mimi eeh! Tarehe zote za kliniki nazijua. Huwa machale yananicheza kuwa una mipango yako isiyopendeza ndiomana nataka uende mwenyewe na mjukuu wangu niachie”
Erica akaona isiwe shida, na kumuacha mwanae nyumbani kisha yeye kuondoka zake.
Alifika kwa Mrs.Peter na kugonga geti, alifunguliwa na Salma yani msichana Yule Yule aliyeambiwa kuwa kaolewa na Rahim.
Erica alijikuta akishikwa na hasira za hali ya juu hata kutamani kumparamia Yule dada, kwa hasira alizokuwa nazo alijikuta akimsukuma na kuingia ndani. Yule dada alikuwa na mshangao kuwa huyu ana maana gani, akamsogelea na kumuuliza
“Kwanini umenisukuma?”
Kabla Erica hajaeleza gadhabu aliyokuwa nayo, alimuona kijana anayemfahamu akitoka kwenye nyumba ya kina Rahim na kumfanya abaki na mshangao.


Alifika kwa Mrs.Peter na kugonga geti, alifunguliwa na Salma yani msichana Yule Yule aliyeambiwa kuwa kaolewa na Rahim.
Erica alijikuta akishikwa na hasira za hali ya juu hata kutamani kumparamia Yule dada, kwa hasira alizokuwa nazo alijikuta akimsukuma na kuingia ndani. Yule dada alikuwa na mshangao kuwa huyu ana maana gani, akamsogelea na kumuuliza
“Kwanini umenisukuma?”
Kabla Erica hajaeleza gadhabu aliyokuwa nayo, alimuona kijana anayemfahamu akitoka kwenye nyumba ya kina Rahim na kumfanya abaki na mshangao.
Yani alibakinkama dakika tano hivi akishangaa kiasi hata Yule Salma alibaki akimuangalia, mara akatoka Mrs.Peter, na kama kawaida ya huyu mama akimuonaga Erica anavyomfurahia kwahiyo alimfurahia kama siku zote na kumuita kwa nguvu,
“Wao Erica binti yangu jamani”
Alimsogelea na kumkumbatia huku akimkaribisha pale ndani kwake ila Erica alibaki nje tu akimuangalia Yule kijana ambapo Mrs.Peter alianza kwa utambulisho,
“Erica, si nilikwambia kuwa nina watoto wawili. Basi wa pili ndio huyu anaitwa John”
Kisha akamgeukia Yule mwanae na kumwambia,
“John, huyu ni binti yangu pia anaitwa Erica”
John akamuuliza mama yake kwa mshangao,
“Binti yako?”
“Ndio, ni msichana niliyezoea kumuita binti yangu maana nilitokea kumpenda”
John alimsogelea Erica na kumkumbatia kwa furaha kisha akamwambia,
“Yani leo siamini kama huyu Erica nimemuona tena jamani”
Mama yake alimuuliza kwa mshangao,
“Kwani mnafahamiana John?”
Muda huu Erica alikuwa kimya kabia maana hata yale makeke aliyoenda nayo kwenye nyumba ile hakuwa nayo tena, John aliongea kwa tabasamu zito,
“Mama, huyu ndiye msichana niliyekueleza kuwa nilimpenda sana. Nilimtafuta sana bila mafanikio na siku ile kama angekuwepo yeye basi ni yeye ndiye ningemvalisha pete ya uchumba kwani katika maisha yangu nilishasema ya kwamba sitokuja kuchezea hisia za msichana kamwe na nikimpenda msichana nitampenda kweli na wala maneno yangu hayatakuwa ya uongo kwake maana nitahakikisha kumuoa”
“Kheee kumbe Erica nisingemfahamu kwa njia ile ya kukutana nae njiani basi ningemfahamu kwa njia ya kuolewa na mwanangu! Ila mimi nampendaga tu huyu binti, hata mwanaume aliyempata pia ni mpole kama wewe John mwanangu”
Erica alikuwa kimya kabisa kwani aliona kama anagongelewa msumari wa mto, ndoto yake kwa muda huo ni ndoa halafu anasikia kuhusu John kutaka kuoa kwakweli alijikuta akikosa raha sana, kile kitendo cha kutokujibu kilimfanya Mrs.Peter kuendelea kuongea,
“Nisamehe Erica kwa kutokukualika kwenye shughuli ya mwanangu, ni kwavile simu yako haipatikani na sijui nini tatizo, ila ningekualika ungeona jinsi ilivyofana”
Erica alimuangalia John ambaye bado alionyesha ana furaha sana ya kuonana nae, kisha John akamvuta Erica kwa pembeni kuzungumza nae kwani alimuona Erica kama kapigwa na bumbuwazi Fulani hivi ambalo binafsi hakulielewa.
“Erica, una tatizo gani mbona kama sikuelewi au umechukia niliposema kuwa kuna msichana nimemvalisha pete ya uchumba!”
“Hapana”
“Sasa mbona unaonekana huna raha”
“Basi tu”
“Kweli Erica, niliposema nakupenda nilikuwa namaanisha kuwa nakupenda na ndiomana nikakupa simu ili tuwasiliane. Cha kushangaza gafla sikukupata hewani, kwa muda nikahisi kwavile umerudi shuleni, nilihamishiwa kimsaomo nje ya nchi ila baada ya miaka miwili nilirudi na lengo langu lilikuwa kukutafuta wewe. Nilihisi kuna siku ningekupata klwenye ile namba ila sikuweza kukupata hadi mwaka juzi naipiga ile namba naambiwa tafadhali ichunguze namba ya mteja unayepiga na upige tena, niliumia sana maana kila nilipokuangalia Erica sikukupata. Ndipo nilipoamua kutafuta msichana mwingine wa kutimiza ndoto zangu za kumaliza masomo na kuoa, na hivi ninavyokwambia ni baada ya miezi miwili ndoa”
Erica alihisi kama akiumia kuendelea kusikiliza yale maneno na kujikuta akimuga John,
“Naomba niende, nitakuja siku nyingine”
“Ila Erica, yani wewe ndio ulikuwa msichana wa ndoto zangu maana nilitamani uwe ni mama wa watoto wangu, sijui ni kitu gani kiliingilia kati hadi hukutaka tena kunitafuta Erica, nilijiuliza maswali mengi sana, pengine hukunipenda ndiomana ikawa vile ila mimi nilikupenda sana Erica”
“Sawa, nitakuja siku nyingine ila kwasasa naomba niende tu”
Erica alianza kuongoza kwa kutoka nje hata John alimshangaa kuwa Erica amekumbwa na kitu gani maana alionekana kama yupo tofauti sana, alimfata tena na kumwambia,
“Usichukie Erica, kwani unanipenda na wewe?”
Erica alikaa kimya tu na kuendelea kutoka, na alipofika nje alisimamisha bodaboda ili impeleke stendi ingawa stendi haikuwa mbali ila alifanya hivyo ili tu kumuepuka John.


 
SEHEMU YA 207


Alifika stendi na kuingia kwenye daladala, kwa hakika alikuwa na mawazo mengi sana kiasi cha kumkosesha raha kabisa kabisa.
Wakati anashuka kwenye daladala ili aingie kwenye daladala lingine alishikwa bega, alipogeuka nyuma alishangaa kuona aliyemshika bega ni Dora yani Yule rafiki yake wa kitambo chuoni, halafu Dora alionyesha furaha sana kukutana na Erica maana alimkumbatia kwa furaha, na kuanza kumsalimia ila Erica hakuwa na furaha kabisa kwanza alikuwa na mawazo yake halafu pia hakufurahishwa na kumuona Dora, rafiki msaliti kwake.
“Jamani Erica, bado tu unanichukia hadi leo jamani!”
“Hapana sikuchukii”
“Yani ungejua nilivyofurahi kuonana na wewe jamani!”
“Kilichokufurahisha?”
“Kwanza nimefurahi kukutana na rafiki yangu wa muda mrefu, pia nimefurahi maana tatizo langu wewe unaweza kunisaidia”
“Tatizo gani?”
“Erica, naomba tuweke tofauti zetu pembeni kwa muda. Twende pale tuongee kidogo, nina shida rafiki yangu”
Erica alimuangalia Dora, ila kwa jinsi alivyokuwa akiongea ilionyesha kweli alikuwa na shida, ikabidi asogee nae mahali chini ya mti kwenye kivuli ili amsikilize alikuwa na shida gani,
“Erica, nilikuwa mkoani mwenzio nikapata mchumba na ananipenda ile ile yani yule mkaka ananipenda haswaaa. Sasa nikaja Dar, kwa bahati mbaya nikakutana na mpenzi wangu wa zamani, kwa hakika nilishindwa kumkataa na kujikuta nikibeba mimba maana ilikuwa ni siku za hatari halafu nilimshauri atumie kinga akasema atamwaga nje ila matokeo yake kanisababishia matatizo”
“Sasa kubeba mimba ni tatizo Dora? Si uzae tu”
“Erica, najua unatambua vizuri kuwa kuzaa kunataka malengo. Siku zote huwa natumia uzazi wa mpango maana nilivyotoaga zile mimba tatu sikutaka tena ujinga nikawa natumia uzazi wa mpango ila tangu nilipopata Yule mchumba wa mkoani niliacha sababu Yule mkaka alionyesha ana lengo na mimi na kashanitambulisha kwa ndugu zake wote kule mkoani, ila yani mimba nazo kama zinatumwa jamani yani nimeacha kunasa kwa Yule kaka nimekuja kunasa kwa huyu mjinga. Na kumbambikia Yule kaka haitawezekana maana Yule mjinga alivyo mtoto ataniumbua tu. Nataka kutoa shoga yangu, yani nitoe tu hii mimba”
“Sasa dora jamani, kutoa mimba ni siri ya mtu ndio unanieleza kweli!”
“Erica, mimi najua kila kitu kuwa hata wewe ulishawahi kutoa mimba, shida yangu nielekeze hospitali uliyoendaga kutolea maana nimeenda pale pa siku zote dokta kanizingua eti anasema nizae tu na mimi sipo tayari kuzaa na Yule mwanaume jamani. Naomba nielekeze Erica”
“Yani Dora naona unanichanganya tu kwakweli na wala sielewi kitu chochote unachonieleza, habari za kutoa mimba mimi sina na nikuambiavyo nina mtoto kwasasa”
“Khee hongera Erica jamani, umeamua kuzaa, hongera sana. Ila mimi sitaki kuzaa kabla ya ndoa na Yule mchumba wangu kaniambia anakuja Dar kunitambulisha kwa ndugu zake wengine halafu tuanze harakati za ndoa. Erica sitaki kuikosa ndoa sababu ya uzembe wa mimba, nahitaji kuitoa hii mimba”
“Sawa, ila mimi sijui madokta wa kutoa mimba”
“Poa, Erica nibanie ila hii mimba nitatoa na kwenye harusi yangu nitakualika. Nipe namba zako”
“Sina haja ya kuja kwenye harusi yako, kwaheri”
Erica aliondoka zake na kwenda kupanda daladala ya kwenda kwao sasa, akiwa ndani ya daladala alijikuta akiwaza mambo mengi sana,
“Au Dora ndio mchumba wa John? Mungu wangu jamani, yani Dora na uuhuni wake lakini ndio anapata bahati ya kuolewa jamani! Kweli kuolewa sio kutulia loh!”
Aliwaza sana bila ya kupata jibu la aina yoyote, alikuwa akiondoka kwao huku ana mawazo mengi sana na hakuwa na raha kabisa.



 
Back
Top Bottom