Simulizi: Sasha Mlinzi wa Nafsi - 1

Simulizi: Sasha Mlinzi wa Nafsi - 1

SASHA MLINZI WA NAFSI
Sehemu ya............29
Mtunzi: Saul David
WhatsApp: 0756862047

ILIPOISHIA...
Haukupita muda mara walisikia muungurumo wa helikopta iliyokuwa angani ikiwasili kisiwani hapo.
Naam, walikuwa ni MG Family wakiwasili.

SASA ENDELEA...
Mwisho helikopta hiyo ilitua na kugusa ardhi katika kisiwa cha Magnus. Watu wanne walionekana wakishuka mmoja baada ya mwingi. Wanaume watatu na mwanamke mmoja.
Wanaume hawa walivalia suti nadhifu za bei ghali zenye rangi nyeusi na tai nyekundu. Yule wa kike yeye alivaa baibui la njano hijabu nyekundu na miwani mikubwa ya jua. Walishuka na kuanza kutembea kwa madaha wakiingia ndani ya jumba kuu la Magnus kisiwani hapo. Hawa ndio GM Family wenyewe majina yao waliitwa Kareem, Noel, Yuda na Madam Husnata.

IKO HIVI...
Ni miaka mingi imepita tangu siku Magnus alivyofukuzwa na kutupwa nje ya ISRA. Magnus hakutaka kukubali kushindwa aliendelea kupambana kujipanga upya kuhakikisha anarudi ISRA kwa mara nyingine kuendelea pale alipoishia.
Akiwa nje ya ISRA Magnus aliyaanza upya maisha yake, mambo mengi yanatokea hapa katikati na baada ya kipindi kirefu kupita Magnus anaibuka tena akiwa ni mtu mkubwa anayeishi katika kisiwa kimoja mbali na makazi ya wanadamu. Akiwa huko anaendelea jitihada zake akiamini ipo siku lazima atarudi tena ISRA, wala hakujali kuhusu umri wake ambao tayari ulikuwa umemtupa mkono mno.

Moja kati ya mafanikio makubwa aliyoyapata Magnus katika kipindi chote akiwa nje ya ISRA ni kuunda kundi moja kubwa la kigaidi tena lenye nguvu ambalo alilibatiza jina akaliita MG Family yaani familia ya Magnus, MG ikiwa ni kifupisho cha jina lake.

Kwa msaada mkubwa wa Magnus MG Family ikawa ni mtandao mkubwa na maarufu wa kigaidi Afrika mashariki na hata Afrika kwa ujumla. Ukiacha Boko haram ya Nigeria, Al-Shabab ya Somalia, Ansar-al-sharia ya Tunisia MG Family nayo ikawa ni moja ya kundi tishio la kigaidi nchini likajipatia umaarufu ingawa si kwa ukubwa sana.

Hakuna jambo gumu lililopita kwenye mikono ya MG Family likashindwa kupatiwa ufumbuzi. Walikuwa wamejikamilisha kwa kila idara. si kiuchumi wala si kisiasa kote walikuwa vizuri mno. Tayari walishaingiza mikono yao na kuwashika masikio hadi baadhi ya viongozi wakubwa serikalini. Tofauti na makundi mengine ya kigaidi, MG Family wao walifanya matukio yale tu ambayo yanafaida au ni agizo la kiongozi wao mkubwa yaani Magnus. Mfano wale watu wanaovaa helmet zenye vioo vya rangi nyekundu wanaofanya kazi ya kuwateka watu na kuwapeleka katika kisiwa cha Magnus walikuwa wapo chini ya mtandao huo wa MG Family. Ni mara chache sana MG Family walifanya vitu tofauti, na walifanya kwa siri bila Magnus mwenyewe kujua. Katu hakuwaruhusu kuanza kujihusisha na mambo ya kisiasa kama ilivyo ada kwa makundi mengi ya kigaidi.

Jambo ambalo liliendelea kuwa siri na hakuna aliyejua ni kuhusu kiongozi mkuu wa kundi hilo la kigaidi yaani Magnus mwenyewe.
Hawakujua Magnus ni nani anaishi wapi anafanya nini. Siku zote watu waliokuwa chini ya mtandao wa MG Family waliamini viongozi wakubwa ni watu wanne waliokuwa wakiratibu kila kinachoendelea yaani Kareem, Noel, Yuda na Madam Husnata. Hawa walikuwa ni viongozi wakubwa waliowekwa na Magnus, lakini wengi waliamini hawa ndio wamiliki wakuu wa mtandao wa kigaidi MG Family.
[emoji294][emoji294][emoji294]

Baada ya helikopta kutuwa Kareem, Noel, Yuda na Madam Husnata walishuka na kuanza kutembea kwa madaha kuingia ndani ya jumba kuu la Magnus kisiwani hapo.

Walimkuta Magnus amekaa kwenye kiti chake cha heshima akiwasubiri kwa hamu.
Walisimama mbele yake na kuinamisha vichwa vyao kwa heshima kubwa. Magnus aliwatazama kwa zamu mmoja baada ya mwingine kisha akaongea.

"Nafikiri kila mmoja anataarifa ya kile kinachoendelea wakati huu, nataka kujua wakati mwanangu anaingia kwenye vitabu vya polisi wapelelezi na kuanza kutafutwa ninyi mlikuwa wapi?" Hili lilikuwa swali la kwanza kutoka kwa Magnus.

Kimya kilitawala kila mmoja akimtegea mwenzake ajibu, walimuogopa mno Magnus.

"Mkuu, ukweli hatukujua lolote na hata watu wetu hawamfahamu Felix kama...." Noel alijitoa muhanga na kujibu

"Hamkujua lolote?" Magnus alifoka na kusimama. Kareem, Yuda, Noel na Husnata wote wakapiga magoti na kuinamisha vichwa vyao chini, hawakutakiwa kusimama pindi ambapo mkubwa wao Magnus amesimama.

Magnus aliwatazama tena kwa zamu akionekana kuwa na hasira sana.

"Niangalieni" alitoa amri. Wote wakatii na kuinua nyuso zao.

"Mwanangu anafika Tanzania kesho asubuhi, sitaki aguswe hata unywele wake. Sitaki awe na kesi ya aina yoyote, aachwe huru na asifuatiliwe tena"

"Sawa mkuuu.." Waliitikia kwa pamoja.

"Sitovumilia uzembe wa aina yoyote utakao jitokeza" Magnus alisisitiza.
[emoji294][emoji294][emoji294]

Dakika tano baadae vigogo wa MG Family walitoka nje ya jumba la Magnus, kila mmoja akionekana kuwa bize na simu yake, tayari taratibu za kutimiza jukumu walilopewa zilianza papo hapo.
Mwisho waliingia ndani ya helikopta na baadae helikopta hiyo ikaacha ardhi na kupaa angani.
[emoji294][emoji294][emoji294]

David, Zungu na Dayana wakiwa bondeni waliisindikiza helikopta hiyo kwa macho hadi pale ilipopotelea juu mawinguni.

"Next time hii helikopta ndiyo itakayotubeba na kututoa hapa" Aliongea David. Dayana na Zungu wakageuka kwa pamoja kumtazama.

"Unaota au?" Aliuliza Dayana.

"Nimepata wazo" Alisema David

"Kabla hujatuambia hilo wazo lako kuna kitu nataka kuwaeleza" Zungu alidakia.

"Nini?" David na Dayana wakauliza kwa pamoja.

"Nimepata njia ya kutoka hapa moja kwa moja hadi ufukweni mwa bahari"

"Nini? Acha masihara Zungu" Alisema Dayana

"Unamaanisha kweli jamaangu?" David naye kaongeza swali. Zungu alitikisa kichwa akiashiria kumaanisha kile alichokisema kisha kaongea...

"Wakati mvua imeanza kunyesha mimi nilitoka hapa, kawaida kukiwa na mvua walinzi huwa wanatoka na kukaa kwenye vibanda vyao hivyo niliweza kupenya vikwazo vyao vyote kwa urahisi, kwa bahati nzuri leo nimefanikiwa kuona njia ya pango linalopita chini kwa chini na kutokea kwenye ile barabara iliyopita mlimani chini ya ardhi"

"Unamaanishe ile barabara tuliyopita wakati tunaletwa hapa"

"Ndiyo David" Zungu aliitika.

Zilikuwa ni habari njema mno kwa wote watatu, mwisho walikaa na kukubaliana usiku watoke kwa mara nyingine kwenda kuhakiki njia hiyo.
Taratibu matumaini ya kutoka kwenye mateso hayo yalianza kujionyesha japo si kwa asilimia kubwa sana.
[emoji294][emoji294][emoji294]

Upande wa pili...
Dakika 17 pekee baada ya kutoka hospitali zilitosha kabisa kufika nyumbani kwa Mama David. Nyumba ilikuwa imejitenga peke yake maeneo ya uswahilini hatua kama 50 kutoka barabarani. Ilikuwa ni nyumba ya kawaida yenye bati lililochakaa.

"Asante mwanangu, tutashuka tu hapa hapa haina shida..." Alisema Mama David huku akimuomba Tesha amsaidie kufungua mlango wa gari.

Kwa sababu Tesha naye alikuwa na haraka hakutaka kubishana na Mama David aliona ni heri ashukie hapo ili yeye na dereva wake warudi haraka mjini aendelee kufuatilia habari za Ndege aliyopanda mpenzi wake Felix kutoka Marekani.

"Usijali mama, muhimu nimepajua nyumbani nitakuwa nakuja mara kwa mara kukutembelea. Naomba usisahau maelezo ya daktari mama yangu, punguza mawazo, kula chakula kwa wakati na usiache kutumia dawa pia"

"Nashukuru sana mwanangu. Kwa hiyo David atarudi lini?" Aliuliza Mama David mara baada ya kushuka garini pamoja na mwanae tatu.

"David mmm! Nafikiri baada ya siku nne hivi atakuwa amekamilisha kazi yake, ila tutawasiliana kama kukiwa na mabadiliko nitakwambia" Tesha alidanganya mwisho wakaagana na mama David. Lakini kabla Dereva hajaondosha gari Tesha alitupa macho kwa mara nyingine kutazama nyumbani kwa mama David akaona gari tatu za kifahari aina ya Benz-Mercedes zikiwa zimepaki nje ya nyumba hiyo tena zote zilikuwa nyeusi zinafanana.
Hali hii ilimshangaza sana Tesha lakini kwa kuwa alikuwa na haraka hakutaka kulizingatia sana hilo, akamtaka Dereva aondoshe gari, wakaondoka.

Si kwamba hali hiyo ilimshangaza Tesha pekee, hata Mama David naye alibaki kinywa wazi mara baada ya kuziona gari hizo nyumbani kwake. Haikuwa kawaida na vilevile haikuwahi kutokea tangu ahamie kwenye nyumba. Alijipa moyo akawa anapiga hatua kusogea, mkono wake wa kulia alishika mkoba wake mkubwa na mkono wa kushoto alimshika mwanae tatu.
Akiwa amebakiza hatua kama kumi kufika nyumbani kwake mara ghafula mlango wa gari moja ulifunguliwa akashuka mwanaume wa miraba minne aliyepigilia suti nadhifu nyeusi. Mwanaume huyo alisogea nyuma akafungua mlango wa gari kwa heshima kubwa mara akashuka mwanamke mmoja maji ya kunde, mrefu na mnene kiasi. Alivaa baibui la njano hijabu nyekundu na miwani mikubwa ya jua.
Huyu alikuwa ni Madam Husnata kigogo mmoja wapo kutoka kundi la MG Family linalomilikiwa na Magnus.
Ndiyo ni Madam Husnata yule yule ambaye muda mfupi uliopita alikuwa katika kisiwa cha Magnus akiwa na wenzake Kareem Noel na Yuda.

Kwa nini mwanamke huyu yupo nyumbani kwa mama David? Kuna mahusiano gani? Kafuata nini? Kivipi?

Haya ni maswali ambayo hata mimi mtunzi wako yananiacha kinywa wazi.

Usijali majibu ya maswali haya utayapata kwenye mfululizo wa episode zinazofuata KAA MKAO.

Mtunzi: Saul David
WhatsApp: 0756862047
 
SASHA MLINZI WA NAFSI
Sehemu ya............30
Mtunzi: Saul David
WhatsApp: 0756862047

ILIPOISHIA...
Huyu alikuwa ni Madam Husnata kigogo mmoja wapo kutoka kundi la MG Family linalomilikiwa na Magnus.
Ndiyo ni Madam Husnata yule yule ambaye muda mfupi uliopita alikuwa katika kisiwa cha Magnus akiwa na wenzake Kareem Noel na Yuda.

SASA ENDELEA...
[emoji294][emoji294][emoji294]
Ni ndani ya mgahawa mmoja maarufu kama SUTRA HOTEL, Inspekta Brandina na Inspekta Masoud walionekana wamekaa meza moja ndani ya mgahawa huo wakipata kinywaji baada ya mizunguuko mingi na migumu siku hiyo. Tayari walishakamilisha taratibu zote muhimu za kumkamata Felix na sasa walichokuwa wakisubiri ni muda ambao Ndege aina ya BOENG 707 AIRWAY itawasili ikitokea nchini Marekani.

"Unajua nini Masoud"

"Nambie Brandina"

"Moyo wangu bado unakosa amani kabisaa"

"Kwa nini tena?"

"Hili suala naona linaweza kuwa kubwa tofauti na tunavyolichukulia unajua kwa nini nasema hivyo..?"

"Eeh! Kwa nini Brandina...?"

"Hili zoezi la utekaji ni la muda sana najua unafahamu, ila mpaka sasa hatujui hawa jamaa ni wapi huwa wanawapeleka mateka, ni nani yupo nyuma yao kuwapa nguvu. Nikikumbuka pia namna huwa wanajipanga, silaha na gari wanazotumia, mambo ya kutisha ambayo huwa tunakutana nayo tunapojaribu kuwafuatilia zaidi naona kabisa kuna haja ya kuongeza nguvu kesho asubuhi wakati wa kumkamata Felix"

"Mmh! Brandina ujue maneno yako ni kweli tupu, kama wameweza kusumbua kwa miaka yote hii si ajabu kesho wakapata upenyo wa kuchomoka na Felix kama tutafanya mzaha"

"Kabisa, ingawa tunaamini hata kuwa na mahali kwa kukimbilia lakini kinga ni bora kuliko tiba, Masoud tuongeze nguvu tena airport iwe na ulinzi wa kutosha kuanzia mda huu" Alisema Brandina ni kama vile alijua kwani kile anachokisema kiliakisi uhalisia wa mambo yaliyokuwa yakiendelea chini kwa chini yakifanywa na mtandao hatari wa kigaidi MG Family wakitaka kuhakikisha Felix anakuwa salama.

"Natamani hata nilale airport leo" Brandina aliongeza wazo.

"Aah! Hapana bana yaani kama tunaenda kumkamata Osama vile, wazo la kuongeza nguvu liko sahihi ila sio kulala uwanja wa ndege" Masoud aliongea na mwisho wakakubaliana kuongeza ulinzi mara dufu eneo la uwanja wa ndege wa kimataifa wa mwalimu Julius Nyerere.
[emoji294][emoji294][emoji294]

Muda ulizidi kwenda masaa nayo yakazidi kusogea na hatimae ikatimia saa kumi na mbili kasoro.
Zilikuwa zimesalia dakika 5 pekee kuufika muda ambao watu kazi yaani MG Family walipanga kukutana mara baada ya kila mmoja kutimiza majukumu waliyopeana.

Nje kabisa ya mji katika uwanja mmoja mpana uliojaa michanga mithiri ya jangwa Yuda alikuwa ni wa kwanza kufika eneo hilo akiwa ndani gari kali la kifahari aina ya Bugatti. Alishuka garini na kabla hajafanya kitu mara alisikia muungurumo wa gari aina ya Harrier ambalo lilifika na kufunga breki kali mbele ya gari lake, akashuka Noel akiwa amevalia suti kali yenye rangi ya kijivu. Kabla hata hawajasalimiana yaani ni kufumba na kufumbua vumbi kubwa lilitanda angani gari aina ya Toyota crown ilikuwa imesimama mbele yao. Akashuka Madam Husnata wakati huu akiwa amevalia kijigauni kifupi kilichoubana na kuuchoro mwili wake kama ulivyo. Hustana akapiga hatua na kusogea pale walipo wenzake. Na wa mwisho kabisa alikuwa ni Careem ambaye yeye alifika akiwa kwenye pikipiki ya bei ghali NCR, alivaa pensi ya kadeti, shati jepesi na vesti nyeupe huku shingo yake ikiwa imepambwa kwa cheni za dhahabu na almasi. Alisogea na kusimama pale waliposimama wenzake.
Sasa MG Family wakawa wamekamilika wote wanne, mwisho kila mmoja alitazama saa yake ya mkononi. Ilikuwa ni saa 12 kamili jioni.

"Natumaini mko poa wote, vipi kila mtu amekamilisha majukumu yake?" Careem alianzisha mazungumzo.
Wakatazamana huku kila mmoja akitikisa kichwa chake kuonyesha mambo yamekwenda vizuri kwa upande wake.

"Vizuri, sehemu ngumu ilikuwa kwa upande wa Madam Husnata na Noel" Alisema Careem huku akiwatazama aliowataja majina kwa zamu, ni kama alihitaji angalau maelezo mafupi kutoka kwao.

Noel aliingiza mkono kwenye mfuko wa koti lake, akatoa CD mbili zinazofanana zikiwa zimehifadhiwa vizuri kwenye makasha yake, Careem alielewa akatikisa kichwa kukubaliana na kazi kubwa aliyoifanya Noel kisha akageuka na kumtazama Madam Husnata ambaye kama utakumbuka kwa mara ya mwisho alikuwa nyumbani kwa Mama David.

"Mambo yako vizuri kila kitu kilienda kama tulivyopanga" Alisema Husnata maneno machache lakini wote walielewa.

"Good, basi sasa tuingie kwenye mpango kamili. Nitamtumia maelezo Mkuu wetu kumueleza jinsi tulivyousuka huu mchezo, kama atakubaliana na sisi basi nitawataarifu na mapema tunaingia mzigoni. Kila la heri" Aliongea Careem mwisho kila mmoja akageuka na kuingia kwenye chombo chake cha usafiri alichokujanacho.

Sekunde chache baada kilichoonekana ni vumbi kubwa likiwa limetanda hewani na lilipokuja kutoweka, hakukuwa na mtu eneo hilo. Walishaondoka.
[emoji294][emoji294][emoji294]

Majira hayo ya saa mbili usiku Magnus alikuwa njiani kuelekea kwenye darasa lake la usiku kama ilivyo kawaida yake. Aliongozana na wale wanawake wanne walioshika visahani vinavyotoa moshi. Akiwa bado hajaingia darasani mara msaidizi wake wa karibu alionekana anakuja huku akikimbia.

Magnus alimuona, akasimama kumsubiri.

"Mkuu hii ni taarifa kutoka kwa MG Family wanaomba uipitie kisha utoe ruksa kama waendelee au laa..." Alisema yule msaidizi mara baada ya kumfikia, akatoa karatasi fulani na kumkabidhi Magnus.

"Ni taarifa kuhusu nini?"

"Ni kuhusu mpango mzima wa kumtoa Felix kwenye lile tatizo kama ulivyoagiza"

Baada ya kusema hivyo Magnus alilipokea lile karatasi akalisoma haraka haraka kwa dakika tatu, mwisho kabisa akatabasamu.

"Hawa ndio MG Family ninao wajua mimi, wambie waendelee na kazi. Nasubiri matokeo" Alisema Magnus kisha akairudisha karatasi kwa msaidizi wake na kuingia zake darasani.

"MAPINDUZI YAFANYIKEEEE....."

"KWA AJILI YA MAISHA BORA YA ISRA NA WATU WAKEEE....."

"Leo ninazo habari ambazo ni njema kutoka ISRA" Magnus alianza darasa lake kwa mazungumzo hayo. Kila mmoja akatega sikio kwa makini kusikiliza ni habari gani hizo njema kutoka ISRA. Magnus akaendelea kuongea akisema...

"Mtoto wa mwisho wa Gu Gamilo yaani Sasha ametenda kosa kubwa ndani ya ISRA, kosa lililompelekea apewa adhabu nzito ya kunyang'anywa nguvu zake na kufukuzwa nje ya ISRA. Hivi ninavyoongea tayari Sasha hayupo ISRA, lakini nawaahidi nitahakikisha namtafuta na kumpata kisha atakuja hapa kuungana na sisi, hivyo ndivyo namna tunavyokwenda kuijenga ISRA mpya. Dhambi walizozitenda kwangu zinaendelea kuwatafuna hadi kwenye familia zao"

Hii ilikuwa ni taarifa ya kushtua mno iliyomshangaza kila mmoja hasa kwa Zucc na Femi ambao wao walikuwa ni miongoni mwa walinzi wa Sasha wakiongozwa na Handan.
[emoji294][emoji294][emoji294]
SAA NNE USIKU...
Usiku huu ulikuwa ni mgumu mno kwa mwanadada mrembo Tesha. Hakuwa amekula chochote tangu asubuhi ya siku hiyo. Mfuatano wa matukio ya kushtua na kustaajabisha pia yalimnyima mwanamke huyo amani. Tangu tukio la kutekwa kwa David siku ya jana, leo tena anapata habari kuwa mpenzi wake aliyemuacha na kumtelekeza yupo njiani anarudi Tanzania akitokea nchini Marekani. Haya yote yalikuwa ni matukio yaliyoichanganya mno akili ya Tesha.
Hadi dakika hii tayari Tesha alikuwa amepeleleza na kujua ni Ndege gani aliyopanda mpenzi wake Felix, akajua hadi saa na dakika Ndege hiyo itakapowasili Tanzania. Akawa amejipanga kuwahi asubuhi na mapema siku inayofuata katika Uwanja wa Ndege wa kimataifa wa mwalimu Julius Nyerere bila kujua sakata kubwa lililokuwepo kati ya MG Family na maafisa wa jeshi la polisi.

Kuna wakati mawazo yake yalizama ndani zaidi akajikuta anamuwaza sana mwanaume wake Felix bila kumpatia majibu. Hakujua ni kwanini alimuacha ghafula na kutoweka, baadae akasikia mwanaume huyo yupo nchini Marekani. Ilikuwa ni ngumu sana kwa Tesha kuamini kama Felix anaweza kumfanyia kitu kama hicho kwani mwanaume huyo alikuwa akionyesha mapenzi ya dhati kwake.
Lakini ajabu kuna muda pia Tesha alijikuta anamuwaza sana kijana David, alishamzoea kwa muda mfupi akawa anatamani uwepo wake. Sasa akili yake ikawa imetawaliwa na wanaume wawili tofauti kwa wakati mmoja yaani David na Felix.

Majira hayo hayo ya saa nne usiku Zungu, Dayana na David walitoka wakiwa na lengo la kuelekea kwenye ile njia ya pango aliyoivumbua Zungu mchana wa siku hiyo. Kila mmoja nafsi yake ilionekana kuwa na shauku kubwa ya kutembea hadi nje ya bonde hilo. Walidhamiria kutoka nje kabisa, wafike hadi ufukweni mwa bahari kama Zungu alivyoeleza.

"Dayana mbona kama hauko sawa" David aliuliza wakati wakipiga hatua kusonga mbele lilipo pango hilo.

"Huwezi kuamini David moyo wangu hauna amani kabisa, napata hisia mbaya sana. Sidhani kama huku tunakokwenda ni salama" Alisema Dayana.

Je, watafanikiwa?
Ni kitu gani Madam Husnata amekifanya nyumbani kwa Mama David?
Ni mpango gani umesukwa na MG Family kuhakikisha Felix anakuwa salama?
Nini kitatokea Uwanja wa Ndege kesho asubuhi?
Vipi kuhusu Sasha?

Simulizi ni shillingi 1,000/= lipia kwa mpesa namba 0756862047 jina saul au Airtel money namba 0788967317 jina saul kisha njoo WhatsApp inbox namba hizo hizo

ITAENDELEA...
 
Shikrani mkuu ngoja tuende nayo sawa, nilikiwa nimekomaa na stori ya Madam Presidaaa....nishahitimisha kuisoma
Karibu sana
Mkeka wa siimulizi yangu nyingine ya KIJASUSI + LOVE STORY huu hapa [emoji116]
 
Back
Top Bottom