Simulizi ya Kijasusi: Kiguu Na Njia

Simulizi ya Kijasusi: Kiguu Na Njia

SEHEMU YA 31




SURA YA TATU
Ile Palee, Nchi Wahaya


ulifika nchi ya Wahaya bila kutegemea. Mimi binafsi nilikuwa nimechoka kwa mwendo wa muda mrefu, kulala sehemu za ajabuajabu na
kula chochote kilichoweza kulika, jioni hiyo nilikuwa nikitembea kwa kujivutavuta, kama mzigo. Tulikuwa tukishuka toka juu ya kilima tulichopanda mchana wa jua kali, niliposikia ukelele wa furaha toka kwa mmoja wa watu tuliokuwa nao. Kelele hizo zilipokelewa na watu wengine zikifuatiwa na vicheko vya furaha.
Nilipoinua uso wangu kutazama huko wanakotazama wengine nilipigwa na butwaa. Takriban dunia nzima mbele ya macho yetu iligeuka kuwa uwanda mkubwa, mweupe unaomeremeta hadi upeo wangu kuona. Sikuelewa ninachokitazama hadi pale babu aliponishika bega na kuniambia, “Tumefika!” huku akitabasamu.
Sikumwelewa, “Tumefika wapi? Na kile nini
kinachomeremeta kiasi kile?” nilimuuliza.
“Yale ni maji. Lile ni ziwa Lweru, ambalo siku hizi nasikia linaitwa Victoria. Tumefika salama mwisho wa safari yetu. Ile pale nchi ya Wahaya.”
Ziwa! Ndio kwanza nikaelewa kile ambacho nimekuwa



nikikisikia juu ya maziwa na bahari. Katika safari yetu hiyo ndefu nilipata kuiona mito mingi, mikubwa, na kuivuka kwa mitumbwi. Kamwe sikupata kufikiria kuwa ziwa lingeweza kuwa kubwa na lenye maji mengi kiasi hiki! Niliduwaa kwa muda mrefu, nikiwa nimelitumbulia macho ziwa hilo kwa shahuku. Nilihisi uchovu ulikuwa umeniteka mwili mzima ukitoweka na nguvu mpya na ari mpya kuchukua nafasi yake katika nafasi yangu.
Msafara wetu huo ulioanza kwa upweke mkubwa kati yangu na babu, sasa ulikuwa wa kundi la watu wasiopungua kumi na wawili. Watu hao, Mwarabu mmoja mwenye ndevu nyingi nyeupe na upara kichwani, ambaye baadaye tuliambiwa kuwa anaitwa Sheikh Seif, alitajwa kama mfanyabiashara wa chumvi na pembe za ndovu. Mtu mmoja kati yao, mrefu sana, mweusi sana, tuliambiwa kuwa ni Mnubi toka Uganda na kwamba alikuwa msaidizi wake mkubwa kibiashara. Wengine, mmoja, akiwa Muha aliyelowea Kagera, wawili Wamanyema wa Kongo na waliobaki wakiwa Wanyamwezi wa Tabora walikuwa wapagazi wake, walioajiriwa kwa safari hiyo pekee.
Tulikutana na watu hao katika kijiji kidogo kilichoitwa Kakonko. Siku hiyo babu alishauri tutafute eneo lenye watu ili tuombe msaada wa chakula cha binadamu zaidi, baada ya kukinaishwa na matunda na nyama za kuchomwa ambazo tulizila bila ugali wala chumvi. Mzee mmoja kijijini hapo alitudokeza juu ya kuwepo kwa wageni wengine kama sisi, waliokuwa wakitokea kwenye biashara ya kubadilishana nguo na shanga kwa chumvi za magadi iliyokuwa ikipatikana katika mabwawa ya maji huko Uvinza, Kigoma.
Tulitambulishwa na watu hao na mara moja wale Wahaya wakaanza kumtania babu kwa kumwita ‘mtani’.
 
SEHEMU YA 32

“Msiwe na wasiwasi,” mmoja wao alisema. “Hawa Wamanyema hawawezi kuwala mbele yetu. Tutawafikisha kwetu salama na kuwapatia vibarua kwenye mashamba yetu.”
Babu naye hakuwa mgeni kwa matani, “Nyama yenu chungu hailiki,” aliwajibu. “Wakijaribu tu kuionja watavimbiwa na matumbo yao kufura kama ya tembo. Halafu, huko kwenu hatuendi kutafuta kibarua. Tunakwenda kutafuta vibarua, waje wafanye kazi ya kurina asali katika misitu yetu.”
Wamanyema wale walicheka sana, Wahaya walicheka pia. Hata Mwarabu, ambaye alicheka kwa nadra sana safari hiyo alitabasamu na kuruhusu pengo moja la meno ya juu kuonekana. Mmanyema mmoja, aliyeonekana kuvutiwa zaidi na mimi kuliko babu, alinivuta kando na kuninong’oneza, “Msimchekee sana yule Mwarabu. Mnajua alikuwa akifanya biashara gani zamani? Hata kabla sijamjibu aliongeza, “Biashara ya watumwa. Hapo ulipo bila shaka anakutamani sana. Kwa jinsi ulivyo kijana, mwenye afya nzuri na wajihi wa kupendeza, enzi zake angekuuza kwa faida kubwa sana kuliko babu yako. Tena kwa jinsi alivyokuwa katika enzi hizi, kama angekukamata wewe na babu yako angempiga babu yako rungu la kichwa na kumwacha aliwe na tai, wewe angekupeleka hadi Bagamoyo au Zanzibar ambako angekupeleka mnadani, huku ukiwa umefungwa mnyororo mikononi na miguuni.
Sikujua kama bwana huyo alitaka niichukulie vipi taarifa hiyo, nicheka au nilie? Nilimkodoea macho, jambo alilolitafsiri kuwa ni kuvutiwa na simulizi zake. Hivyo, akaongeza, “Siku hizi amekwisha. Tangu biashara ya utumwa ilipopigwa marufuku amekuwa mtu wa kuuza shanga na chumvi, sio binadamu.
Nilimtazama Mwarabu huyo. Kweli aikuwa akinitazama pia. Lakini macho yake hayakutoa tafsiri yoyote ya ama





kunitamani ama kunipangia bei. Alikuwa bado anatabasamu, tabasamu la kibinadamu!

Tulilala kijijini hapo siku mbili. Kwa kiwango fulani tulilala vizuri na kula vizuri. Hivyo, safari ilipoanza tena nilikuwa mchangamfu, tayari kwa safari.

Wenzetu hao walikuwa na mizigo mikubwa. Walikuwa na pembe nne, kubwa sana, za ndovu, ambazo walizibeba kwa kupokezana. Walikuwa pia na viroba vinne vya chumvi, makapu mawili ya chakula na gudulia la maji. Tuliamua kuwasaidia. Mimi nilikabidhiwa kapu moja la chakula, babu akabeba lile gudulia la maji.

Msafara ukiwa mkubwa kidogo, haukupungukiwa simulizi za uongo na kweli. Utani, michapo na pengine nyimbo za kikabila ziliibuka mara kwa mara kiasi cha kufanya niichukulie safari hiyo kama tukio la kuvinjari tu katika nchi yangu. Tulivuka mito na vijito, tulipenya msitu na misitu, tuliwaona ndege na wanyama wa kila aina. Ndiyo, kuna nyakati tulichoka na kukata tamaa kutokana na njaa, mbu, uchovu na kero nyingine za porini. Lakini, kwa namna moja au nyingine, kero hizi ziliondokea kuwa kama sehemu ya burudani, kwani hakuna raha isiyo na karaha. Hadi tunaliona ziwa likimeremeta mbele yetu, kana kwamba linatulaki kwa vicheko na tabasamu, nilipata hisia kuwa safari yetu ilikuwa ya kheri na mafanikio yalikuwa yakitusubiri.

Muda mfupi baadaye tulifika pwani ya ziwa, katika kijiji cha wavuvi kilichokuwa kando kidogo ya kijiji cha Kashozi. Ilionyesha kuwa Mwarabu huyo na msafara wake walikuwa wenyeji katika kijiji hicho, kwani tulipokelewa juujuu na kuandaliwa chakula murua, ndizi zilizopikwa vizuri kwa samaki wakubwa aina ya sato. Baadaye tulipewa rubisi ambayo mimi
 
SEHEMU YA 33

nilionja kidogo tu, kabla ya kuonyeshwa sehemu ya kulala.
Usingizi ulinipokea juujuu, wengine wanaita usingizi wa kifo, kwani nililala zaidi ya masaa kumi na mawili, bila kushtuka, kuzinduka wala kuota ndoto yoyote ile. Nilipofumbua macho ilikuwa kesho yake, saa mbili au tatu za asubuhi. Wavuvi walikuwa wakitoka ziwani, mitumbwi yao ikiwa imejaa samaki aina ya sato na sangara.
Nilimwona babu akiwa kando ya ziwa, akizungumza na mmoja wa wenyeji wetu, mzee mpole, ambaye baadaye niliambiwa kuwa anaitwa Buberwa, rafiki wa karibu wa ‘Mtume wa karagwe’ mwalimu Ibrahimu Kazigu.

* * *​
Ujio wa kigeni katika mkoa wa Kagera haukuwa lelemama. Kwanza kabisa, Wahaya walikuwa na mungu wao ambaye walimwamini na waliamini kabisa kuwa aliwatatulia matatizo yao. Mungu huyu alijulikana katika majina mbalimbali kama Ruhenga; Mweza wa yote, Mutonzi; Muumba, Nyakubao; Aliyepo, Nyakumerera; Wa milele na kadhalika. Jina kubwa zaidi lililojumisha miungu hio likiwa lile la Mugasha; Mungu wa mvua, Mlinzi wa mito, ziwa, wavuvi na samaki.
Wahaya walikuwa hawatoi zaka wala sadaka. Hali kadhalika, walikuwa hawatoi kafara. Siku zote waliamini kuwa mungu wao alikuwa na kila kitu, kamwe asingehitaji chochote kutoka kwa viumbe wake.
Dini za kigeni zinaweza kuelezewa kuwa ziliingia Kagera kwa kupitia mlango wa nyuma. Mnamo mwaka 1878 mapadri wa kwanza wa kikatoliki walifika Zanzibar wakitokea Algiers, Aljeria. Mapadri hao walitawanyika hadi kufika Uganda kwa Kabaka Mutesa, aliyekuwa mfalme wa himaya ya Buganda,



kumwomba msaada. Mapadri hao walipata upinzani mkubwa sana toka kwa Waislamu ambao walikwishatangulia nchini humo na kumsilimisha Kabaka mwenyewe, pamoja na Wakristu wa madhehebu ya ki-prostetanti ambao pia walikuwa wametangulia. Hata hivyo, Mutesa aliridhia maombi yao na kuwapa mashua iliyowafikisha Bukoba April 1880.
Kumbe Mutesa alikuwa akiwala kisogo. Wakati akijitia kuwasaidia alikuwa pia akitangaza taarifa kwa watemi wa Kagera ambao wengi wao walikuwa wakiwajibika kwake, akiwaagiza kutowapa ushirikiano wamisionari hao. Iliwachukua wamisionari hao miaka kumi na miwili kuweza kuanzisha kazi yao ya kutawanya ‘neno la bwana,’ katika eneo hilo.
Katika eneo hilo la Karagwe watemi Kahigi na Kyobya walikuwa wameshiriki sana kugomea jitihada hizo za kuanzisha kanisa katoliki. Hali kadhalika, upinzani kati ya utawala wa Wadachi waliokuwa madarakani na Waingereza ambao waliwang’oa Wadachi madarakani ulichangia sana katika vita dhidi ya madhehebu ya kikristo. Itakumbukwa kuwa mtemi mmoja wa enzi hizo, aliyejulikana kwa jina la Ntare, alitolewa mhanga katika changamoto hiyo kwa kushtakiwa kwa Wadachi kuwa alikuwa akiwakaribisha Waingereza. Mtemi huyo alihukumiwa kifo na kunyongwa mwaka 1916.
Mwaka huohuo wakati Mwami Ntare ananyongwa mtu mmoja aliyekuja itwa Ibrahimu Kazigu alibatizwa, akiwa na umri wa miaka kumi na mitano. Wana Karagwe wanamwelezea bwana huyu kuwa ni mfano wa mtume Paul, kwani alikubali kuacha kila alichokuwa nacho na kujitolea kulitumikia kanisa. Bwana huyu alitumikia kanisa kwa zaidi ya miaka thelathini na miwili akihubiri, kuanzisha makanisa, kuanzisha shule
 
SEHEMU YA 34

na kubatiza. Mapadri walipokuja kuanzisha misheni eneo hilo, kule Bugere, mwaka 1934 walikuta tayari Karagwe ina waumini wapatao elfu mbili na wanafunzi, wake kwa waume takribani mia nane.
Ni mtu huyu, Kazigu ambaye babu alinikabidhi kwake kupitia kwa mwenyeji wetu Buberwa, ambaye aliondokea kuwa rafiki mkubwa kwa babu. Kitendo cha kuambiwa kuwa tumesafiri safari ndefu, toka nchi ya mbali, kwa ajili ya kuja kufuata ‘neno’ na elimu kilimfanya Ibrahimu Kazigu aliyekuwa hapo Kashozi wiki mbili baadaye kukutana na wamisionari, anipokee kwa mikono miwili. Akanitia mikono kichwani na kunibariki. Jumapili iliyofuata nilibatizwa na kupewa jina la Petro, badala ya langu la zamani la Mtukwao ambalo niliambiwa kuwa ni la kipagani. Kisha nikakabidhiwa katika shule maalumu ambazo zilikuwa zikipokea watoto yatima na wale waliokombolewa kutoka utumwani hasa wakitokea Kongo, Rwanda Uganda.
Babu hakushiriki sherehe za ubatizo wangu. Alitoroka usiku wa kuamkia siku ya ubatizo kwani ‘mtume’ Ibahimu Kazigu alikuwa amemtaka yeye pia kubatizwa kwa maelezo kuwa ‘ameona mwanga, hastahili tena kukaa gizani.’ Lakini babu hakuwa tayari. Alishindwa kumkatalia Ibrahimu kimachomacho kwa ajili ya kuchelea kuharibu jitihada alizofikia juu yangu. Ndipo akaamua kutoroka. Lakini haikuwa kabla ya kuchanjiana damu na rafiki yake Buberwa, hatua ambayo ilihitimisha urafiki wao na kuwafanya ‘ndugu wa damu.’
Tuliagana na babu kwa siri, katika uchochoro wenye kiza, hivyo sikuweza kuyaona macho yake kuona kama anachosema yalikuwa yakitoka mdomoni au moyoni. Alisema maneno machache yaliyojaa pongezi kwa uvumilivu wangu



wa kuweza kuikamilisha safari ile ngumu. Pia alishukuru kwa jinsi jitihada hizo zilivyoweza kuzaa matunda kwa urahisi kuliko alivyotegemea.
“Nakuacha mikononi mwa rafiki yangu wa damu na mtu wa Mungu. Sina shaka kuwa utaishi salama na utapata elimu itakayokupa nafasi katika dunia hii,” babu alisema na kuongeza, “Sina cha kukupa mjukuu wangu. Kitu pekee nitakachokuachia ni hiki.” Alivua hirizi iliyokuwa shingoni mwake na kunivisha. “Hii ni hirizi ya bahati. Ilinde nayo itakulinda maishani mwako. Kamwe usiiweke mbali nawe.”
Nilijikuta nikilengwalengwa na machozi. “Babu hii ni hirizi yako. Imekulinda maisha yako yote. Ukinipa mimi huoni kama maisha yako yatakuwa hatarini?” nilimwambia.
“Hapana mjukuu,” babu alinijibu. “Mie hirizi hii niliirithi kwa baba, ambaye aliirithi kwa baba yake. Ni hirizi ya familia. Wewe unaingia katika safari ndefu ya maisha. Unaihitaji kuliko mimi na baba yako tunavyoihitaji sasa.”
Nikaipokea na kuivaa.
“Halafu uifiche sana,” babu alionya. “Hawa watu wa kanisa kwao kila kitu chetu cha asili kwao ni dhambi. Wakiiona wataipokonya na kuichoma moto. Ifanye siri yako, siri ya moyo wako.”
Baada ya maneno hayo babu alinitemea mate katika paji la uso na kunitakia kheri. Kisha akageuka na kutoweka gizani.
Nilishindwa kujizuia. Machozi yalinitoka.
Laiti ningejua kuwa agano hilo lilikuwa la mwisho, kwamba nisingemwona tena babu yangu, nisingekubali kuachana naye kirahisi kiasi kile.
 
SEHEMU YA 35

“A!”
“Ahaaaaaaaaa!” “E!”
“Eheeeeeee!” “I!”
“Ihiiiiiiiii!” “Oh!”
“Ohoooooo!” “U!”
“Uhuuuuuuuu!”
“a,” inaandikwa kama punje ya harage….’e’ iko kama ndizi iliyovimba juu…. ‘I’ ni kama msumari… ‘o’ ni kama yai…. ‘u’ ni kama shimo. Mnanielewa?”
“Ndiyoooo!”
Mtukwao, bin Karimanzira bin Kionambali nilikuwa nimeanza shule. Hapana! Sikuwa tena Mtukwao, wala Karimanzira. Nilikuwa na jina jipya, Petro Kionambali. Ndivyo nilivyoandikishwa. Ndivyo nilivyokuwa nikiitwa na walimu na wanafunzi wenzangu katika maisha na mazingira hayo mapya.
Tuliishi katika mabweni, tukiwa wavulana wapatao sitini au sabini hivi. Wengi wetu tulikuwa watu wa makabila tofauti, utamaduni tofauti na hata maumbile tofauti. Tulitofautiana pia katika umri. Wakati mimi nilijiona mdogo kwa umri wangu wa miaka kumi na mitatu, walikuwepo kaka zetu wenye umri wa miaka kumi na saba katika darasa hilohilo la kwanza. Wengine walikuwa wadogo kabisa kwa miaka yao kumi hadi minane.
Tulifundishwa kusoma na kuandika. Lakini mkazo mkubwa hata kabla hatujaanza kusoma na kuandika ulikuwa wa mafundisho ya dini. Tulifundishwa upendo, kusali pamoja



na kuimba nyimbo za kumsifu bwana. Tulifundishwa kila kitu juu ya mungu wa Izrael, aliyemtuma mwanawe wa pekee, ili azaliwe kama binadamu katika zizi la kondoo, ateswe, asulubiwe na kufufuka siku ya tatu baada ya kifo chake kwa ajili ya kutukomboa na dhambi zetu. Zaidi, tuliambiwa kuwa tayari siku zote, kwani haikujulikana siku wala saa ambayo angerudi tena duniani na kuwachukua ‘wateule’ wake na wale wasio wake kutupwa jehanamu ambako wangeungua kwa moto mkali wa milele.
Nikijua kuwa nilikuwa nimetembea safari ndefu na ngumu kuifuata fursa hiyo ya kupata elimu nilitilia maanani kila nilichofundishwa na kuzingatia kila fundisho la dini. Jambo hilo lilinifanya baada ya siku chache tu niwe mmoja wa wanafunzi hodari sana shuleni hapo. Walimu walinipenda, wanafunzi walinisikiliza. Hivyo, haikuwa ajabu pale, ulipofika mwisho wa mwaka huo nilipoteuliwa kuwa kiranja wa darasa langu.
Mafunzo ya dini pia niliyazingatia sana. Sikuwa na sababu wala wasaa wa kuiba, sikuwa na haja ya kumtukana mtu wala kumzulia uongo. Kama kuna dhambi pekee, ambayo siku zote ilinisuta moyoni basi ilikuwa ile ya kundelea kuthamini na kuivaa kwa siri hirizi yangu niliyoachiwa na babu. Sikuwa tayari kuitoa kwa shemasi au kasisi ili ichomwe moto. Nilichukulia ile kama kiungo pekee baina yangu na familia yangu, kiungo ambacho kukitoa ingekuwa sawa na kuukata mzizi wa mwisho; kati yangu na asili yangu.
Elimu niliyoipata katika nchi hiyo ya Wahaya haikuwa ile ya darasani wala ya dini pekee. Nilipata elimu ya mitaani ambayo kwa kweli ilinisaidia sana. Kwa mfano, wakati shule hazikufundisha lugha ya Kihaya, huko mitaani nilifundishwa.
 
SEHEMU YA 36

Ndani ya mwaka mmoja tu nilikuwa tayari nikisikia na kuzungumza Kihaya kwa ufasaha kama Muhaya yeyote yule.
Shule hatukufundishwa kuogelea. Lakini mimi katika kipindi hichohicho cha mwaka mmoja tayari nilikuwa hodari wa kucheza na maji kama samaki. Niliweza kuelea juu ya maji kama boya au kupiga mbizi kama sangara. Hali kadhalika, nilijifunza kupiga makasia na kuvuta aina kwa aina za samaki. Kwa kushika maji au kuangalia mwenendo wa mawingu angani nilijua ni wakati gani ziwa lingechafuka kwa upepo mkali, wakati gani limepungua.
Kwa kiasi kikubwa ‘utundu’ wangu ziwani ulichangiwa na mapenzi makubwa niliyokuwa nayo kwa ziwa hilo toka pale nilipoliona kwa mara ya kwanza. Nililichukulia kama hazina ya pekee tuliyojaaliwa na Muumba kwa kuzingatia kuwa nchi nyingine badala ya maji hayo mengi wao wamejaliwa majangwa yaliyojaa mchanga na joto kali. Nililichukulia ziwa hilo kama hazina ndani ya hazina. Wingi wa samaki waliojaa katika ziwa hilo, aina waliokuwa wakiishi ndani au kando mwa ziwa hilo ulikuwa ushahidi tosha wa utajiri huo.
Mtu aliyechangia kunipa elimu na ujuzi mwingi juu ya ziwa hakuwa mwingine zaidi ya mzee Buberwa, baba yangu wa kufikia. Kila nilipopata likizo nilikuwa nikienda kwake ambako nilishirikishwa katika uvuvi na kuweza kujipatia si ujuzi tu bali pamoja na vijisenti vya matumizi kutokana na mchango wangu katika uvuvi. Mtoto wake mkubwa, Muleju, aliondokea kuwa rafiki yangu mkubwa na ndiye aliyenipa darasa la awali la kuogelea. Madarasa yaliyofuata nilijifunza mwenyewe kutokana na ujasiri na jitihada zangu.
Buberwa alikuwa mzee aliyependa sana utani. Hakuchoka kuniambia mara kwa mara, “Mwanangu



tumekupeleka shule kuchukua elimu. Hatukukupeleka pale kujifunza utawa na upadri. Chukua elimu yako, usichukue upadri wao. Nataka ukimaliza shule nikupe msichana mrembo wa Kihaya, umuoe na kurudi naye kwenu. Watu wa huko wajue Mungu alivyopendelea nchi ya Wahaya si kwa samaki na maji pekee, bali pamoja na wajihi murua wa wakazi wake.” Kuoa! Nililichukulia kama jambo ambalo lingenitokea baada ya karne nyingine zijazo. Sikupata kumjibu kwa hilo. Naye nadhani hakutegemea jibu langu. Ilikuwa kama mtu anayenikumbusha jambo fulani, mara kwa mara, ili lisije
likanitoka akilini.
Nimezungumza mengi juu ya raha za ziwani, raha za kula samaki watamu, raha za kuelea juu ya maji, raha ya kupata fedha kutokana na mauzo hayo. Pengine haitakuwa haki kama sitataja chochote pia juu ya karaha zake pia.
Wanasema, wavuvi wengi kwamba ukiwa ziwani ujue kuwa unatembea na ‘kifo mkononi.’ Madai ambayo niliyadhibitisha kwa vitendo kwa uhai wangu wa ziwani hapo.
Tukio la kwanza lilikuwa lile la kupotea ziwani. Siku hiyo tulikwenda kuvua samaki usiku. Ghafla, ulizuka upepo mkubwa ulioambatana na mvua nzito ambayo ilifanya karabai tulilokuwa tukilitumia kwa ajili ya mwanga lizimike. Upepo huo ulisababisha mawimbi makubwa yaliyofanya mara kwa mara maji yaingie ndani ya mtumbwi. Huku nikitetemeka nilipewa kazi ya kuondoa maji hayo yaliyoingia huku wenzangu wawili waliobakia wakijitahidi kupiga makasia kurudi ufukweni. Zilikuwa jitihada zisizo na matunda. Kwanza, kutokana na kiza kilichotanda hakuna aliyefahamu nyumbani ni upande upi. Pia, kasi ya maji kuingia katika mtumbwi ilikuwa kubwa kuliko ile ya kuyaondoa. Muda mfupi baadaye wenzangu walikata
 
SEHEMU YA 37

tamaa ya kupiga makasia bila kujua kama wanakwenda mbele au wanarudi nyuma. Wakajiunga nami katika jukumu la kuondoa maji katika mtumbwi. Haikusaidia. Muda mfupi baadaye mtumbwi wetu ulizama na kupinduka. Tukaogelea na kupanda juu ya mgongo wake huku tukipiga kelele kuomba msaada.
Katika purukushani hizo mwenzetu mmoja alipotea. Nadhani alichoka kuendelea kuung’ang’ania mgongo wa mtumbwi ambao ulikuwa ukiyumba na kutupwa huku na kule kwa mawimbi hayo. Mimi na Muleju tuliendelea kung’ang’ania hadi alfajiri, upepo huo ulipopoa.
Tulishinda ziwani humo, juu ya mgongo wa mtumbwi huo tukiwa hatuna la kufanya. Makasia yetu yalikuwa yamechukuliwa na mawimbi na uwezo wa kuufunua mtumbwi huo hatukuwa nao.
Siku ya kwanza na usiku wake ukapita. Siku ya pili, jioni sana, tukiwa tayari taabani kwa njaa na uchovu, tuliona mtumbwi wa wavuvi ukitujia. Hawa walituzoa na kutupakia kwenye mtumbwi wao kisha wakajitahidi kuubinua mtumbwi wetu na kuondoa maji yaliyokuwemo. Wawili kati yao waliingia katika mtumbwi huo na kuupiga makasia kuelekea ufukoni. Ufukwe huo uliondokea kuwa kisiwa kidogo cha Bumbire, mbali sana kutoka Kashozi tulikoanzia safari.
Tulipumzika kisiwani humo kwa siku tatu zaidi, kabla ya kurejea nyumbani ambako walikwishakaa matanga wakiamini kuwa nilikwishakufa. Tuliopona tulifanyiwa sherehe ndogo, mwenzetu aliyepotea aliombolezwa kwa taratibu za kimila.
Nikiwa na hakika kuwa kilichoniokoa katika mkasa ule ilikuwa ile hirizi yangu niliyopewa na babu, ambayo muda wote ilikuwa kifuani mwangu, niliibusu na kuikumbatia kwa



furaha, “Nitakulinda daima, ili nawe unilinde,” niliinong’oneza. Katika hali ya kawaida, tukio hilo lingetosha kabisa niliogope ziwa hilo kama simba mla watu. Lakini, kwa jinsi ziwa lilivyokwishaniingia akilini niliichukulia tukio zima kama jambo la kawaida tu, katika pilikapilka za maisha. Nikaendelea
na shughuli zangu bila hofu wala wasiwasi wowote.
Tukio lililofuata, ambalo pia sikulitegemea kiasi lilikuwa kama la kuchekesha. Nilikuwa nikiogelea kando ya ziwa, baada ya kazi ya kutwa nzima za mchana huo. Nadhani nilikuwa nimeogelea kwa muda mrefu kiasi, kwani nilijihisi uchovu mwingi. Mara nikaona kitu kama gogo likielea juu ya maji mbele yangu. Nikalifuata na kuparamia juu yake ili nipumzike kidogo. Nilishangaa kuona gogo hilo likizama ghafla na kisha likiibuka hatua chache mbele yangu na kufunua domo lake kubwa ama kupiga mwayo ama kunifokea.
Mamba!
Nilikuwa nimeparamia mgongo wa mamba. Kwa kujua kuwa mamba hana uwezo wa kumnasa mtu katika maji mengi niliogelea harakaharaka kupanda ziwani. Zilipogeuka nilimwona mamba yule akiogelea kurudi ufukoni. Ama alikuwa ameshiba sana, ama alishtuka mie kukimbia.
Hilo na lile la kukoswakoswa na kiboko mmoja aliyefanikiwa kupindua mtumbwi wetu ni miongoni mwa matukio mengi, ya kutisha yaliyoambatana na maisha yangu katika ziwa hilo.
Kwa kupona hatari baada ya hatari, huku nikiendelea kupata mafanikio kimaisha na kitaaluma niliamini kabisa kuwa hirizi yangu ilikuwa ikitimiza wajibu wake. Mara kwa mara niliibusu na kuinong’oneza, “Nitakulinda daima ili nawe unilinde.”
 
SEHEMU YA 38


SURA YA NNE
Hirizi yazua jambo.


ana mkasa iliyosababisha safari yangu kielimu ikome baada ya miaka mitano tu.
Wakati huo nilikwishashuhudia watu wote waliovuka miaka kumi na minane akihesabiwa katika kile kilichoitwa sensa ya kwanza nchini Tanganyika. Tukio hilo lililofanyika Julai mosi, mwaka 1931. Mimi sikuhesabiwa kwa ajili ya umri na hata kama ningekuwa na umri nisingehesabiwa, kwani Makarani wa kazi hiyo walikuwa wakihesabu wakuu wa kaya pekee na kisha kwenda kutengeneza hesabu zao. Jambo hilo lilileta manung’uniko kuwa kazi hiyo haikufanyika kwa ufanisi.
Pia, wakati huo nilikuwa nikidonoadonoa maneno kadhaa yaliyoandikwa katika gazeti la Kiingereza lililoitwa Tanganyika Standard, ambalo lilikuwa limeanzishwa huko Dar es Salaam mwaka uleule wa hesabu ya watu.
Ni kupitia gazeti hilo nilipofahamu kuwa Gavana wa nchi wakati huo aliitwa H.A MacMichael akiwa amemrithi
G.S Symes ambaye naye alimrithi D.C Cameron. Wote hao walikuwa wamemfuatia Gavana wa kwanza wa Uingereza nchini aliyeitwa H.A Byatt, aliyepewa wadhifa huo mara baada ya Wajerumani kupokonywa nchi ya Tanganyika mwaka 1920.



Naikumbuka vizuri sana siku ya balaa. Ilikuwa tarehe
4 Novemba, 1934. Kule Dar es Salaam kulikuwa na kikao muhimu cha watawala kilichoitwa Kamati ya Ushauri wa Elimu kwa Mwafrika. Kamati hiyo ilipinga wazo la wanafunzi wa Kiafrika kuchangia mitaala na madarasa ya Wazungu au Waasia kwa madai kuwa uwezo wa watoto wa Kiafrika kuelewa wanachofundishwa ulikuwa duni sana ukilinganishwa na Wazungu na Wahindi. Hata hivyo, mjumbe mmoja, aliyeitwa Martin Kayamba, alipinga vikali madai hayo. Alisema, “Huwezo wa mtoto wa Kiafrika haukuwa na tofauti yoyote na ule wa Wazungu au Wahindi bali tatizo pekee lililosababisha hisia hizo zijitokeze ni watoto hao kutopewa nafasi sawa na wengine.”
Habari ambazo shuleni hapo, miongoni mwa walimu na wanafunzi, zilikuwa kubwa sana. Kayamba alisifiwa na kupongezwa sana kwa kitendo chake cha kuwapa wakoloni ukweli.
Kwa utoto wetu tuliamini kauli yake ingekuwa mwisho wa kutengwa na mwanzo wa kuruhusiwa kusoma pamoja na watoto wa Wazungu na Wahindi ambao walikuwa na shule bora mara kadhaa zaidi yetu. Tulikuwa katika vijikundi vidogovidogo tukijadiliana juu ya hilo baada ya masomo ya kutwa nzima tulipozinduliwa na kelele za baadhi yetu ambao walikuwa tayari wakikimbilia nyuma ya shule wakibeba mifuko na mabakuli.
“Senene!” mmoja wetu alitamka. Mara alikurupuka na kupiga mbio kuwafuata wengine.
Ulikuwa msimu wa senene. Mara nyingi msimu huo uliambatana na ule wa kumbikumbi ambao ni jamii ya mchwa ambao huota mbawa na kuruka kwa makundi makubwa angani kwa muda mfupi. Baadaye kuishiwa uwezo wa kuruka
 
SEHEMU YA 39

na kudondoka ardhini huku mbawa zao zikinyofoka.
Wakishapoteza uwezo wa kuruka kumbikumbi huzagaa ardhini wakitafuta namna ya kurudi katika vichuguu vyao. Wengi huishia kuwa kitoweo cha binadamu na ndege. Kati ya wachache ambao hubaatika kunusurika mmoja wao hugeuka Malkia ambaye hutaga maelfu kwa maelfu ya mayai hivyo kuanzisha upya kizazi chao. Hao ni kumbikumbi.
Senene, ambao ni jamii ya panzi, ni maarufu zaidi kwa wakazi wa eneo hilo jirani. Wao wana tabia ya nzige, ingawa hawana madhara makubwa kama ndugu zao hao ambao wanaweza kugeuza pori kuwa jangwa kwa muda mfupi sana.
Senene, ni chakula maarufu zaidi, na kwangu mimi walivutia zaidi. Hivyo, kama wenzangu wote sikuweza kujizuia. Nilikimbia huko na huko na kuwakamata wengi tu ambao niliwajaza katika mfuko ili kesho niweze kuwaanika na kisha kuwahifadhi kwa matumizi ya baadaye.
Na baada ya pilikapilika hizo, wakati tukiwa katika sala ya mwisho kabla ya kulala nilipohisi upungufu fulani katika mwili wangu. Nimepoteza nini? Nilijiuliza huku nikijipapasa. Haikunichukua muda kubaini kuwa hirizi yangu, ambayo tunapokuwa darasani nilikuwa na tabia ya kuhifadhi mfukoni, ilikuwa imetoweka! Bila shaka ilidondoka katika zile purukushani za kunasa senene.
Hirizi yangu! Niliwaza kwa uchungu, nikihisi nguvu zote zikiniisha mwilini. Ibada iliyokuwa ikiendelea haikuniingia akilini. Nilitamani kutoka nikaitafute lakini tayari ulikuwa usiku mwingi, kwanza nisingeiona, pili nisingeruhusiwa kutoka.
Usiku huo usingizi ulinikata kabisa. Alfajiri sana, kabla ya mtu yeyote kuamka mimi tayari nilikuwa nje nikijaribu



kupita kila mahala nilipohisi kuwa ningeweza kuidondosha. Sikuipata.
 
SEHEMU YA 40

“Unatafuta nini?” nilisikia sauti ya mtu ikizungumza nyuma yangu. Nilipogeuka nilimwona Byabato, mwanafunzi mfupi, mnene, ambaye kwa kweli hakupata kuwa rafiki yangu.
“Natafuta kalamu yangu,” nilidanganya.
“Kalamu! Utaiona kweli saa hizi? Kwa nini usingoje jua lichomoze?”
“Siyo kazi yako!” nilimwambia
Byabato alinitazama kwa mshangao. Mara nikamwona yeye pia anaanza kutafuta kitu huko na huko kama mimi. Ilikuwa zamu yangu kushangaa.
“Unatafuta nini?” nikamuuliza.
Naye akanipa jibu lilelile ambalo mimi nilimpa dakika mbili zilizopita, “Siyo kazi yako!”
Kihoro kilinipanda. Kwa jinsi nilivyomfahamu Byabato nilijua kuwa kama angeipata hirizi ile asingesita kubaini kuwa ndiyo nilikuwa naitafuta. Na kwa tabia yake asingekuwa mtu wa kuniwekea siri. Ingemchukua dakika chache sana kuitangazia shule na dunia nzima kuwa nilikuwa na hirizi. Sikuwa na namna ya kumzuia. Nilichofanya nilijaribu kumpoteza kwa kutafuta sehemu ambayo nilikuwa na hakika kuwa sikuifikia. Lakini, kwa mshangao wangu yeye alielekea upande wa pili, ambako ndiko hasa nilikopita katika nyendo zangu.
Nilishukuru pale kengele ya kujiandaa kuingia madarasani ilipolia kabla sijaipata wala kumwona Byabato akiiokota. Nikaondoka kinyonge na kurejea bwenini kujiandaa.
Nilikuja kuiona tena hirizi hiyo saa nane za mchana. Kuiona, siyo kuipata rafiki yangu! Kwani ilikuwa mikononi mwa Padri Backhove aliyekuwa ametembelea eneo hilo ili



kukagua maendeleo ya shule na maendeleo ya wanafunzi na waumini wengine kiimani.
 
SEHEMU YA 40 & 41

Ilikuwa baada ya mlo wa mchana, ambao mimi niliula kidogo sana, kengele ya dharura ilipigwa na wote tukakusanyika katika ukumbi wa ibada. Padri alianza kwa kutoa nasaha au somo refu juu ya raha inayotusubiri huko mbinguni na mateso makali ya moto wa milele unaowasubiri huko jehanamu wote ambao watakwenda kinyume na amri kumi za Mungu. “Mungu wetu ni mwenye wivu,” aliongeza Padri. “Moja ya amri zake kumi, alizozileta kwa mkono wa mtumishi wake Musa pale kwenye mlima Sinai inasema waziwazi, ‘Usiitumikie miungu mingine ila mimi’ Sawa?”
“Sawa,” wote tuliitikia.
“Mungu wetu ni msafi,” Padri Backhove aliendelea, “Anapenda wote tuwe wasafi wa miili na mioyo yetu. Sawa?”
“Sawa.”
“Kumfuata bwana maana yake ni kukana dhambi. Kukana mila na desturi zetu zote potofu na kuanza maisha mapya ndani ya Kristo. Maisha safi kimwili na kiroho. Mkristo wa kweli hatakiwi kuamini uchawi. Hatakiwi kuabudu sanamu… Hatakiwi kuvaa hirizi… sawa?”
Mara lilipotajwa neno ‘hirizi’ nilijua wapi mahubiri hayo yanaelekea. Nilihisi miguu yangu ikiishiwa nguvu na mwili wangu ukitetemeka. Sikuwa na uwezo wa kusikia tena chochote ambacho padri aliendelea kusema hadi pale nilipomwona akiwa ameishika hirizi yangu na kuining’iniza mbele yetu, huku akisema, “… Nauliza kwa mara ya pili nani kati yenu aliyeidondosha hii?”
Wote tulitazamana. Macho yangu yalikutana na yale ya Byabato ambayo yalinitazama kwa namna ya kunisuta



na kunidhihaki. Macho yaliyokuwa yakisema, “Unajua kuwa najua kuwa ni yako!”
“Nitauliza kwa mara ya tatu,” Padri aliendelea. “Nani kati yenu aliyedondosha hirizi hii jana?”
Macho ya Byabato yalikuwa yameganda juu ya macho yangu, yakinicheka. Sikuweza kustahimili zaidi. Niliinua mkono wangu juu na kisha kusimama huku nikijibu taratibu, “Ni yangu, Padri.”
Si Padri wala wanafunzi wenzangu walioamini masikio yao. Kwa darasa langu, kwa shule nzima na hata jamii nzima ya eneo hilo mimi nilikuwa mfano bora zaidi kimasomo na kikanisa. Nilikuwa hata nikiwasaidia mashemasi katika huduma ndogo ndogo za kanisa.
“Ni yako?” Padri aliniuliza tena, kana kwamba alitaka nibadili kauli na kuikana hirizi yangu. Sikuwa tayari kwa hilo. “Unajua kuwa mwili wako ni hekalu la Mungu? Aliniuliza​

Padri.

“Najua!”
“Kwa nini basi unavaa uchafu? Kwa nini unahifadhi

dhambi na kuishi nayo? Hutaki kuingia katika ufalme wa Mungu?”
Sikumjibu.
“Sio neno,” Padri aliendelea. “Leo Bwana amefanya muujiza kwa ajili yako. Ameifichua hirizi hii chafu, ambayo umeivaa kwa muda mrefu, ili ujitakase upya. Tutawasha moto hapo nje, utaichoma hirizi hii kwa mkono wako mwenyewe. Kisha tutakuombea na kukubariki kwa kitendo hicho cha kuachana na upagani milele.”
Tulitolewa nje. Zikaletwa kuni, moto ukawashwa.
Huku wenzangu wakiimba pambio mbalimbali, mimi na Padri



Backhove tulisimama mbele ya kadamnasi hiyo, mikononi mwake akiwa na Biblia na hirizi yangu.
“Wakati nikianza kusali, ichukue hirizi hii uitupe ndani ya moto ukitamka maneno yafuatayo ‘Shetani nakuteketeza sasa na milele, kwa jina la Yesu’ Umeelewa?”
Niliitikia kwa kichwa.
Nyimbo zilipamba moto. Sauti ya Padri akisoma sala ilisikika waziwazi. Lakini mkono wangu uliokuwa na hirizi uliishiwa nguvu huku nikitetemeka mwili mzima. Niliishikilia kwa zaidi ya dakika mbili, nikiining’iniza juu ya miale murua ya moto huo lakini vidole vyangu vilielekea kunigomea. Hisia zangu zilikwenda mbali sana toka hapo. Zilisafiri hadi usiku ule tulipoagana na babu uchochoroni. Masikio yangu yalisafiri pia. Yalikuwa pamoja nami huko uchochoroni, gizani, yakimsikia babu akisema; Hii ni hirizi ya bahati. Ilinde nayo itakulinda maishani mwako. Sauti hiyo ilikuwa wazi wazi kabisa masikioni mwangu.
“Ichome!” Padri alikatiza sala na kuniambia kwa ukali. “Siwezi!” Nilimjibu.
“Huwezi nini?” aliniuliza kwa mshangao. “Tupa uchafu huo ndani ya moto!” nilishindwa kabisa kuviamini vidole vyangu kufanya hivyo. Mara nikageuka na kuanza kuondoka. Padri hakuyaamini macho yake. Akanifuata na kujaribu kunishika. Nikamsukuma.
Padri Backhove alikuwa mtu mnene na mzito sana. Lakini hakuwa na nguvu nyingi. Nilimsukuma kidogo tu, lakini akaanguka chali, kama gunia. Sehemu ya kanzu yake ndefu, iliyofika miguuni iliangukia ndani ya moto huo na kuanza kuungua.
“Nakufa!” Padri alipiga kelele akijiviringisha huku na
 
SEHEMU YA 42 & 43



kule katika jitihada za kujizoa ainuke toka mavumbini hapo.
Nilishikwa na hofu kubwa. Wakati wenzangu wakihangaika kuzima moto katika mwili wa padri, wengine wakijaribu kuinua mwili wake wenye zaidi ya kilo mia na sitini mimi nilianza kukimbia kwa nguvu zangu zote huku nikihisi sauti za watu wanaonifuata wakizomea nyuma yangu. Sikugeuka wala kusimama hadi nilipofika vichakani, mbali sana, ambako niliamini mtu yeyote asiye na uwezo wa kukimbia kama mimi na ujuzi wa mambo ya porini kama mimi, asingeweza kunipata.

* * *​
Nilijipumzisha kwa muda chini ya kivuli cha mti aina ya mvule, ulioonekana kupevuka sana. Nikaketi na kuegemea shina lake huku nikiitumia akili yangu kutafakari mustakabali wa maisha yangu baada ya tukio lile. Moyo wangu ulijaa kiza, hofu kubwa ikiwa imetanda katika nafsi yangu kwa kufikiria tu uzito wa mkasa ule.
Sikuwa na hakika kama padre Backhove alikuwa hai au la kwa moto na mweleka ule. Hata hivyo, hakika niliyokuwa nayo ni kwamba alikuwa ameathirika sana kimwili na kisaikolojia. Kwa vyovyote vile kama angenitia mkononi adhabu ambayo ningeipata isingekuwa kifani. Wazo ambalo lilinifanya nisahau kabisa ndoto ya kurudi shuleni pale na kuomba msamaha.
Zaidi ya hayo, hata kama ningerudi na kusamehewa ningeishi maisha gani shuleni pale bila kuwa kituko na kichekesho kwa kila mtu kwa miaka nenda miaka rudi? Sikuwa radhi kwa hilo.
Halafu, hata kama ungetokea muujiza nirejee shule na yote mengine yasahauliwe, jambo moja tu lisingeweza kusahauliwa kamwe. Hirizi. Kwa vyovyote vile msamaha wangu



na kutakasika kwangu kungeendana na kuiteketeza hirizi ile hadharani, hirizi ambayo ni urithi wangu pekee! Kiungo cha mwisho kati yangu na familia yangu!
Mara nikaikumbuka hirizi hiyo! Iko wapi? Nilijiuliza nikitia mkono wangu mfukoni kuitafuta. Haikuwemo. Nilikagua mifuko yangu yote na kujipapasa mwili mzima, wapi. Hirizi yangu ilikuwa imepotea, bila shaka katika zile purukushani za kukimbia!
Nilihisi nikiishiwa nguvu. Kwa muda nilipoteza mapigo kadhaa ya moyo, huku macho yakiingia kiza. Hirizi yangu ambayo ilikuwa kila kitu maishani mwangu. Hirizi ambayo ilisababisha nipoteze kila kitu maishani mwangu! Imepotea!
Wanasema binadamu katika uhai wake, anaweza kufa kidogo! Kama madai hayo ni ya kweli basi mimi Petro Kionambali, siku hiyo, chini ya mti ule wa mvule nilikufa kidogo.
Na hata pale uhai uliponirejea sikuwa mtu yuleyule tena. Sikuwa na pa kwenda. Nisingeweza kurudi Kashozi kwa mzee Buberwa na kumsimulia kuwa nimeshindwa shule wa ajili ya hirizi. Kadhalika, nisingeweza kurudi kwetu Buha na kumwambia babu na wazazi wangu kuwa nimeacha shule kwa ajili ya hirizi ambayo haipo tena. Shule nako kusingeendeka. Iko wapi hirizi tuichome? Ningeulizwa kabla ya mengine yote. Imepotea! Lingekuwa jibu langu. Nani ambaye angeniamini? Zaidi nani ambaye angenithamini? Haikuwepo namna.
Ghafla nikajiona yatima. Hapana, nilikuwa mwana
mpotevu, asiye na mbele wala nyuma.
Nikainuka na kujitazama. Tayari nilikuwa kijana mrefu kuliko watu wote katika familia yangu. Nilikuwa mwembamba lakini mkakamavu. Mikono yangu ilikuwa na nguvu, miguu



yangu ikiwa na uwezo. Zaidi ya kaptula, shati na viatu nilivyovaa sikuwa na chochote mkononi wala mfukoni mwangu. Nilikuwa masikini. Lakini nilijiamini. Afya yangu, elimu yangu na ari yangu vilifanya niamue jambo moja; sirudi kwetu wala sirudi shule. Nitapiga mguu, kutafuta maisha upya. Hata kama nitafika mwisho wa dunia!

* * *​
Nilipiga mguu kuelekea Kanazi. Nilifika usiku sana. Kwa kuhofia kuwa habari zangu zilishafika hapo nililala porini, juu ya mti. Alfajiri nilianza tena safari. Kiguu na njia hadi Muhutwe. Hapo niliomba hifadhi kwa wavuvi waliokuwa wamejenga vibanda vyao pwani. Hawakuwa na hiyana, ingawa mavazi ya shule niliyoyavaa yalifanya wanishuku kuwa nimetoroka shule. Sikukosa uwongo wa kuwaambia hata mashaka juu yangu yakaisha.
Katika elimu yangu fupi shuleni nilikuwa nimepata ufahamu wa kutosha wa Jiografia. Baada ya kughairi kurudi kwetu au kwenda kwa mzee Buberwa niliamua kwenda nchi ya Wasukuma. Mengi yalikuwa yakizungumzwa juu ya nchi hiyo ambayo nilitamani kuyaona kwa macho.
Zilikuwepo hadithi za Msukuma aliyeitwa Ng’wanamalundi ambaye alisemekana kuwa mganga aliyewashinda wachawi wote kwa kutumia ngoma zake. Mtu huyo wa miujiza alisemekana pia kuwa alikuwa na macho yenye nguvu za ajabu, ambayo yaliweza kukausha miti na hata binadamu aliowakazia macho, jambo lililopelekea awe akitembea huku akiwa amejifunga kitambaa usoni kufunika macho yake. Mtu huyo alidaiwa kuwa katika moja ya hafla zake alipata kukausha msitu mkubwa na mamia ya watu waliokuwa mbele
 
SEHEMU YA 44 & 45

yake. Jambo hilo liliifanya serikali ya mkoloni imkamate na kumhukumu kunyongwa. Lakini hakuna aliyethubutu, kwani kabla ya hukumu hiyo kutekelezwa alifungwa katika kimojawapo cha visiwa vidogovidogo vilivyo baharini katika pwani ya Bahari ya Hindi, huko Dar es Salaam. Hata hivyo, ilielezwa kuwa Ng’wanamalundi huyo kila jioni alionekana katika vilabu vya pombe Dar es Salaam akiwa amevuka bahari kwa kutembea juu ya maji. Wakoloni wakalazimika kumwachia.
Sifa nyingine ya nchi ya Wasukuma ni zile hadithi kuwa kulikuwa na milima ya mawe, ama majini ama nchi kavu. Baadhi ya milima hiyo ilielezewa kuwa ilikuwa katika maumbile ya binadamu, ikiwa imesimama miaka nenda rudi kama inayosubiri mwujiza fulani utokee, ili ipate uhai na kuanza kutembea kama binadamu wengine.
Nchi hiyo pia ilikuwa ikisifiwa sana kwa ukubwa wa ardhi na wingi wa rutuba yake. Kilimo cha mazao ya chakula na yale ya biashara kama pamba na katani kilielezewa kuwa hakikupata kumtupa mtu. Kwa bahati mbaya, mimi sikupata kuwa mkulima wa haja. Wala sikuona kama ningeweza kuwa na ustahimilivu wa kulima leo kusubiri mavuno miezi au miaka kadhaa baadaye. Mimi nilikuwa mtu wa maji. Mtu wa kutupa nyavu na kuzitupa huku tayari zimejaa samaki! Hivyo, sababu kubwa iliyonipa msukumo wa kutamani kufika huko hasa lilikuwa ziwa. Jiografia yangu ilionyesha kuwa Wahaya na Wasukuma walichangia ziwa hili. Wakati Wahaya wakiwa Magharibi wakilitumia kwa shughuli zilezile.
Kwa kuzingatia hali yangu ya kutokuwa na kazi wala ujuzi wowote wa kuweza kupata ajira nyingine nililichukulia ziwa hili kuwa mkombozi wangu pekee. Nilitegemea ziwa



liniajiri, linilee, kwani taaluma ya uvuvi niliyoipata katika likizo zangu ilitosha kabisa kunipatia ajira hiyo.
Ni kwa mtazamo huo ndipo nilipojikuta nikijiunga na vikundi mbalimbali vya uvuvi kwa lengo la kujipatia fedha. Siku zote za uvuvi wangu nilifuata ziwa kuelekea upande wa kushoto kwangu badala ya upande wa kulia. Kama ningeelekea kushoto, ningelazimika kufika Uganda na baadaye Kenya, kabla ya kuingia Tarime, Musoma, Bunda hadi kufika Mwanza. Ingekuwa safari ndefu isiyo na sababu yoyote.
Mimi nilielekea kulia. Nilivua katika pwani na visiwa mbalimbali kama Bambire, Iroba, Rubondo na Nyamiende. Ilikuwa safari ndefu na ngumu sana. Takribani mwaka mzima uliishia njiani. Ama nilikwamishwa na ukosefu wa majahazi yanayoelekea huko nilikokuwa nikielekea, ama upepo mkali wa siku kadhaa ziwani ulifunga kabisa njia. Msimu wa masika ulioambatana na mvua kubwa za radi na mingurumo ya kutisha ni miongoni mwa sababu nyingine iliyonichelewesha njiani. Nililazimika kusubiri kwa zaidi ya miezi minne katika kijiji fulani huko Biharamulo.
Urefu huo wa safari ulikuwa na faida moja. Kwanza, ulinipa fursa ya kupata ukomavu na uvumilivu mkubwa katika pilikapilika za ziwani na nchi kavu. Ningeweza kuvumilia mvua ya siku mbili au tatu ikinipiga mwilini, niliweza kustahimili jua kali linalochoma kama mkaa wa moto. Niliweza pia kuipuuza njaa kwa muda mrefu. Zaidi, mwili wangu ulijenga uwezo mkubwa wa kuyashinda maradhi madogomadogo kama homa au tumbo bila haja ya kutumia dawa za madukani au mitishamba tele niliyopata kuelekezwa na babu.
Faida nyingine kubwa niliyoipata kutokana na urefu wa safari hiyo ilikuwa udugu. Nilikutana na watu mbalimbali,



nikashirikiana nao kwa hili na lile na kujikuta nimepata ndugu na marafiki tele, ambao kila nilipoondoka kuendelea na safari yangu walisikitika sana, lakini haikuwa kabla ya kunitakia kheri na baraka za safari.
Nilikosa raha kiasi pale tulipofika kisiwa cha Kome tukikaribia kabisa Mwanza. Rafiki zangu hao walishauri tubadili mwelekeo na kwenda kwanza Ukerewe. Tulifika Nansio. Tukafanya shughuli zetu za uvuvi hapa na pale, katika kijiji hiki na kile hadi tukajikuta tumeingia katika kisiwa kingine kidogo kiitwacho Ukara.
Ulipata kuona au kusikia juu ya mawe yanayocheza muziki? Kama hujapata hata kusikia mwenzio niliyaona kwa macho yangu katika kisiwa hicho cha Ukara. Kisiwa hicho kina mawe yaliyokaa kiajabu ajabu. Mtu anaweza kufikiria kuwa yalipangwa na binadamu, kwani baadhi yako juu ya mengine, yakiwa yamegusana kwa sehemu ndogo sana lakini hayadondoki si kwa mawimbi wala dhoruba la ziwani. Nilikuwa nikiyakodolea macho mara kwa mara mawe yale hadi mwenzangu mmoja aliposema, “Unashangaa kuyaona yalivyokaa, jee ukiyaona yanacheza?”
Nilidhani ni mzaha. Tulipobishana jamaa hawa walinipeleka katika kijiji cha Kome, ambako tulipata mwenyeji aliyetupelekeka eneo la Kululibha yalipo mawe haya ya ajabu. Mwenyeji wetu alitoa amri kwa lugha yake ya Kikara. Mara mawe hayo yakaanza kucheza kama watoto mapacha moja juu ya jingine. Hadi leo sijui ni kitu gani kinachotokea hadi mawe hayo yamtii binadamu.
Lakini huo si muujiza pekee wa Ukara. Pale kijijini kuna kisu chenye makali pande mbili. Unapotokea uhalifu wa aina yoyote watuhumiwa hupelekwa kwa mtaalamu na kuamriwa

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 16

“Kwahiyo walinigeuza biashara. Zile safari nyingi za hapa na pale, toka nchi hadi nchi, kumbe zilikuwa za kunifanyia maonyesho. Watu walitoa pesa nyingi ili wamwone ‘nyani mweusi’ anayekula kwa uma na kuzungumza Kiingereza. Kuna wakati niliombwa kuimba, au kualikwa kucheza muziki na wasichana wa Kizungu. Picha nyingi zilipigwa na kuuzwa kwenye vyombo vya habari.”
“Nikiwa nchini Sweden, katika mji mmoja uitwao Jonkoping niliajiriwa na familia moja ya watu ambao walikuwa wakiendesha shamba la wanyama. Wengi kati ya wanyama hao walikuwa wa porini ambao walikamatwa wangali wadogo na kufundishwa ama kuishi na binadamu. Wale wakali kama simba, chui na vifaru walifungiwa katika maeneo maalumu.”
“Ajira yangu kama nilivyoambiwa awali ilikuwa kusaidia kuwatunza wanyama hao. Niliingizwa katika mikataba ambayo sikuielewa na kushawishiwa kuweka dole gumba kwenye karatasi zao kama sahihi. Niliiona kazi rahisi na kuziona mia tatu kila wiki nilizokuwa nikilipwa kama za bure. Lakini nilishangaa pale nilipoanza kuvalishwa mavazi yaliyoandaliwa kitaalamu na kuonekana kama nyani dume. Hayo yalianza pale nyani aliyekuwa shambani humo alipofariki kwa uzee, wamiliki wakaifanya habari hiyo siri kwa hofu ya kupoteza wateja wao waliokuwa wakimiminika kila siku kumtazama nyani huyo anavyoruka toka tawi hadi tawi la miti iliyooteshwa shambani humo.”
“Nikaelekezwa kujifanya nyani yule. Kwa kuwa nilikuwa hodari sana wa kupanda miti, kuachia tawi moja na kudaka jingine halikuwa jambo geni kwangu. Niliwafurahisha sana watazamaji, hasa watoto. Nadhani niliwafurahisha zaidi kwa kuwa nilikuwa binadamu nikisoma hisia zao na hivyo kufanya



mengi ambayo hawakuyatarajia.”
“Waajiri wangu walifurahi sana. Muda wote walikuwa na kamera za video ambazo walizitumia kunukuu kila kitendo changu. Baadaye wateja walipoondoka waliendelea kunipiga picha hata wakati navua mavazi yale ya kinyani na kuvaa ya kibinadamu. Mara kwa mara walinihoji vilevile, kwa lugha zote nilizoweza kuzungumza na kunukuu maongezi yangu kwa vinasa sauti.”
“Ikaja siku ya balaa. Wakati nikiruka toka tawi hadi tawi la mti uliokuwa juu ya zizi la simba dume ilitokea bahati mbaya nikateleza na kudondokea ndani ya zizi hilo kando kidogo ya simba yule. Nadhani nilipiga ukelele wa hofu, kwani nilijua nimefika mwisho wa maisha yangu. Nilitetemeka zaidi pale simba huyo alipoanza kuninyatia taratibu akinguruma. Wakati nikijiandaa kwa vita ya kuipigania roho yangu nilishangaa kuona simba huyo akiweka kinywa chake kando ya sikio langu na kuninong’oneza, “Usiogope, mimi ni binadamu kama wewe!”
“Kweli? Wewe mtu wa wapi?” nilinong’ona vilevile. “Mimi ni Mmarekani. Nipo hapa mwaka wa tatu.” Alisema.
“Nilipigwa na butwaa. Lakini walioduwaa zaidi ni watazamaji ambao kwao kitendo cha simba kuteta na nyani kilikuwa muujiza wa pekee. Walitegemea kuona nikiliwa hadharani, badala yake nanong’ona na simba!”
“Toka siku hiyo shamba hilo likawa linafurika wateja. Walitoka miji ya mbali na hata nchi za jirani kuja kushuhudia maajabu ya ‘nyani’ na ‘simba’ waliojenga urafiki.”
Lakini kwangu hiyo ilikuwa siku ambayo niliamua kuacha kazi hiyo. Pamoja na kulipwa fedha nyingi, nilikichukulia kitendo hicho kama udhalilishaji mkubwa.
R
Basi fuatilia, Simulizi ya Kijasusi: Mikononi Mwa Nunda inakaribia kuisha
hii ya kiguu na njia ni ndefu mno

Basi fuatilia, Simulizi ya Kijasusi: Mikononi Mwa Nunda inakaribia kuisha
hii ya kiguu na njia ni ndefu mno
Unanikatisha tamaa eroo inamaana utaishia njiani?
 
Back
Top Bottom