Simulizi ya kweli: Niliolewa na Jini bila kutarajia

Simulizi ya kweli: Niliolewa na Jini bila kutarajia

SEHEMU YA 21



Kilio cha mama Suzy kilipasua moyo wangu kwa uoga wa kupewa habari mbaya.
Nikaendelea kumsikiliza mama Suzy huku uoga mwingi umenishika ila mama Suzy hakuweza kuongea zaidi ya kulia kisha ile simu ikakatika.
Nikageuka kumtazama Carlos aliyekuwa amekaa kimya kabisa bila ya kuniuliza chochote nadhani alikuwa anangoja mimi ndio nianze kumuuliza ila alipoona namuangalia tu akaamua kuniuliza kuwa kuna nini, nami nikaamua kumjibu.
"Sijui rafiki yangu Suzy kapatwa na nini maana mama yake analia tu kwenye simu"
"Wewe unafikiriaje?"
"Sijui kwakweli, sijui amekufa"
Nikaanza kutokwa na machozi, kisha Carlos akanivuta karibu yake na kuweka kichwa changu kifuani mwake kama ishara ya kunibembeleza ila nilihisi kuna vitu vinatembea mwilini mwangu na kujitoa kwenye mikono ya Carlos, kisha akaniuliza.
"Kwani wewe unatakaje?"
"Sitaki rafiki yangu afe"
"Kwanini?"
Nikamuangalia Carlos na kumshangaa kuwa ni swali gani lile la kuniuliza, kisha nikamjibu.
"Sababu nampenda sana"
"Unampenda sana kupita Sam?"
Nikamuangalia kwa hasira sasa na kumjibu kwa ukali,
"Swali gani hilo unaloniuliza? Sina muda wa kujibu maswali yako"
Nikaendelea kutokwa na machozi, kisha Carlos akatoa leso na kunikabidhi ili nifutie machozi kisha akaniuliza tena,
"Kweli hutaki Suzy afe?"
Nikamuangalia sana Carlos kwani sikuona umuhimu wa maswali aliyoniuliza na sikuona msaada wake kwahiyo sikumjibu.
Nikachukua simu ili niangalie salio kisha niwapigie ndugu zake Suzy waweze kuniambia vizuri kuhusu Suzy, ila Carlos akanishika mkono na kunikataza kupiga simu na mimi nikamuuliza kuwa anamaana gani kuni kataza,
"Niambie kwanza, je hutaki Suzy afe?"
Ikabidi nimjibu ili aridhike kujibiwa.
"Ndio sitaki afe"
"Basi mimi nitakusaidia"
"Kivipi?"
"Wewe amini ju kuwa nitakusaidia tu"
Nikamuangalia kisha kumuuliza.
"Na mbona umenizuia kupiga simu?"
"Kama unahitaji msaada wangu na huhitaji rafiki yako Suzy afe basi fata ninachokwambia"
"Kwanini?"
"Usiwapigie wakina Suzy simu hadi watakapokupigia wenyewe kama kweli hutaki Suzy afe"
Nikamuangalia tu Carlos kwa mshangao kwani alikuwa ni mtu wa ajabu sana kwangu, kisha akaniaga na kuniambia kuwa atakuja badae kunitembelea tena ila nikamshangaa kwani muda ulienda sana na giza lilishaanza kuingia, nikashangaa kusikia atakuja badae na kujiuliza mwenyewe kuwa hiyo badae ni badae gani, kisha akaniomba nipande kwenye gari yake ili anipeleke karibu zaidi na nyumbani kwa kaka ndio aondoke. Nikapanda kwenye gari yake huku mawazo mengi kichwani yakinitawala, nilipofika karibu nikamwambia anishushe ili wifi asinione nilipotokea.
Kabla ya kushuka Carlos akaniambia tena.
"Usiwapigie simu ndugu wa Suzy hadi watakapo kupigia wenyewe, weka akilini na ukumbuke hilo muda wote"
Kisha nikashuka naye akaondoka, maswali mengi sana nikajiuliza bila ya kupata majibu.
Nikaingia ndani na kumkuta wifi amejilaza kwenye kochi.
"Kheee Sabrina tangia umeondoka ndio unarudi muda huu! Umepata marafiki gani huku?"
Nikamsogelea wifi na kumuuliza polepole.
"Je kaka amesharudi?"
"Bado hajarudi au ulienda kuonana na huyo Sam?"
Nikamuangalia wifi na kutabasamu ili kumpotezea anachoniuliza na kuanza kumwambia mambo mengine kabisa yasiyohusiano.
Tuliongea kidogo na kaka nae akawa amewasili, kisha akamfata mkewe alipo na kumshikashika tumbo lake halafu akasema.
"Atakuja lini huyu? Nina hamu nae"
Wifi akatabasamu kwa furaha na kumjibu.
"Atakuja tu muda wake ukiwadia na utacheza nae hadi uchoke"
Kaka nae akatabasamu kwa furaha, kisha akanigeukia na kuniambia,
"Otea Sabrina, eti atakuwa mtoto gani?"
"Mi nadhani atakuwa wa kiume kaka"
Wifi akainuka na kukaa kisha akajibu,
"Huyu ni wakike nyie sema hamjui tu"
Kaka nae akasema.
"Ni wakiume bhana, Sabrina yupo sahihi. Kwani mke wangu hutaki kuzaa dume?"
"Nataka sana"
"Sasa mbona unadai huyo ni wakike"
"Huyu ni wakike ndio mume wangu, nataka awe ananisaidia kazi hapa nyumbani"
Tukabaki kucheka tu na kaka maana mtoto anapangiwa majukumu akiwa tumboni.
Tukaongea mengi na kula kisha kupumzika na kwenda kulala. Nashukuru maongezi yale yalinisaidia kupotezea mawazo ya kumpigia Suzy.
Nikiwa chumbani kwangu, mawazo juu ya Suzy yakanitembelea kichwani nikatamani kuchukua simu kupiga ila nikasita kufanya hivyo. Mara simu yangu ikaanza kuita, kuangalia mpigaji ni Sam nikapokea kumsikiliza.
"Nasikia Suzy amepatwa na matatizo, hebu niambie kinachoendelea"
"Sijui chochote"
"Ulizia basi kwao tupate taarifa kamili"
"Kwani wewe umeambiwa na nani?"
"Aliyeniambia si wa muhimu kwasasa ndomana nikakuuliza wewe"
"Kama hutaki kuniambia aliyekwambia basi na mimi sitakwambia chochote"
"Sio muda wa marumbano huu Sabrina, nimeambiwa na Lucy tena amenidokezea tu ndomana nauliza ili nijue tatizo"
"Nilijua tu kama umeambiwa na malaya wako, sasa mwambie huyohuyo akueleze vizuri"
"Toka muda ambao Lucy aliniambia hadi sasa hapatikani, acha hasira Sabrina mambo mengine inatakiwa tushirikiane tafadhari"
Nikamsikiliza Sam kisha nikaamua kumpa moyo tu.
"Nikiongea nao nitakupa taarifa"
Kisha nikakata simu ili niweze kulala ila mawazo kuhusu Suzy yalizidi kuugusa moyo wangu na kunifanya nikose raha. Nikapitiwa na usingizi palepale.
Nikajiona nipo kwenye bustani nzuri sana, kisha akaja yule mkaka wa ndotoni na kukaa karibu yangu na kusema.
"Karibia unaingia kwenye himaya yangu Sabrina. Nitakupenda, kukujali na kukutunza"
"Ila mimi sikupendi wewe"
"Utanipenda tu Sabrina, sina sababu ya kukulazimisha bali utakubali mwenyewe kwa hiyari yako na utaolewa na mimi"
Nikashtuka na kusema kwa nguvu.
"Sitaki kuole...."
Kabla sijamaliza hayo maneno kuna kitu kiliziba mdomo wangu kama vile kuna mtu nyuma yangu halafu kaniziba mdomo kwa mkono.
Kisha nikasikia sauti ikipita sikioni mwangu kama vile mtu ananinong'oneza.
"Shiiiii usipige kelele Sabrina, kumbuka tupo ugenini wote watakuona chizi. Kwanini hupendi kunizoea?"
Nikawa nafurukuta tu pale kitandani kwani aliniziba mdomo kwa nguvu.
Nilipofanikiwa kugeuka sikuona mtu yeyote na ile mikono iliyoniziba mdomo sikuhisi tena, nikainuka haraka na kuwasha taa huku nikitetemeka sana, nikatamani niwaite wifi na kaka lakini nilisita.
Nikafungua mlango ili nitoke sebleni, nikamshangaa wifi akiwa pale sebleni akipiga maombi. Nakasimama na kumuangalia, alipomaliza akaniangalia na kusema.
"Unajisikiaje Sabrina?"
"Nipo salama tu"
"Njoo karibu yangu"
Nikamsogelea wifi ili nijue anachotaka kuniambia.
"Nilipokua chumbani kuna kitu kimeniambia kuwa kuna mapambano kwako, ndiomana nikatoka kuja kuomba hapa. Unaendeleaje lakini kwasasa?"
"Naendelea vizuri wifi"
"Kuwa makini sana mdogo wangu, nenda kalale sasa"
Nikarudi ndani na kulala hadi kulipokucha, sikupatwa na njozi yoyote ile iliyombaya nikashukuru maombi ya wifi yamenisaidia kwani maruweruwe yalitaka kunianza tena kama ilivyokuwa nyumbani.
Mchana wa siku hiyo nikiwa nimetulia pale nyumbani na wifi, mara simu yangu ikaita kuangalia mpigaji ni mama Suzy.
Nikapokea ile simu huku hofu kubwa imenitawala nikahisi kama sio habari mbaya basi nitape wa lawama tu, nikaweka simu sikioni ili kusikiliza.
"Asante sana Sabrina mwanangu, Mungu akubariki sana umetusaidi sana mwanangu"
Nikashangaa kuwa ile asante ya nini kitu kilichofanya niongee kwa kigugumizi sasa.
"Aah kwani kwani ni..."
"Umetusaidia mwanangu, yule kijana uliyemtuma jana ametusaidia sana. Kwasasa Suzy anaendelea vizuri na yupo hospitali kwaajili ya matibabu mengine."
"Sawa mama nashukuru kwa taarifa"
"Umwambie yule kijana tunashukuru sana"
Kisha akakata simu, maswali mengi nikajiuliza huyo kijana ni kijana gani niliyemtuma mimi na je amewasaidiaje wakina Suzy bado sikupata jibu, na je Suzy alipatwa na nini haswaa bado sikupata jibu. Nikabaki kujiinamia tu ila nikapata wazo la kumpi gia simu Lucy ili anipe taarifa kamili, ingawa sikutaka kuongea na Lucy ila ilinibidi ili kuijua hali ya Suzy.
"Niambie Lucy, kwani Suzy amefanyaje?"
"Mmh leo umenipigia simu! Kweli Mungu ashukuriwe"
"Niambie bhana Lucy, mambo mengine achana nayo"
"Nitakwambia kwa kifupi tu, kwakweli hali ya Suzy ilikuwa mbaya sana kuna watu walimpiga na kumtegeshea nyoka. Bila Carlos tungeongea mengine sasa, kwakweli Carlos ametusaidia sana hadi Suzy anapumua sasa na kuendelea vizuri kwa msaada wa Carlos"
"Sasa Carlos alimsaidiaje?"
"Tukionana nitakwambia vizuri Sabrina."
Bado akaniacha na maswali mengi tu bila ya majibu yoyote, ikabidi nimngoje Carlos akiwasili ili anijibu maswali yangu kwani yeye ndio atakuwa na majibu ya maswali yangu yote.Nikarudi kukaa na kuzungumza na wifi mambo mbalimbali kisha akaniomba nimsindikize kwenye kwaya kama kawaida.
Wakati tunaenda, tukampitia na yule mwalimu wa kwaya ili twende wote.
Wakati namsubiria wifi amalize mazoezi yake, ukaingia ujumbe kwenye simu yangu kutoka kwa Carlos akiniomba kuwa nikutane nae nilipokutana nae jana yake.
Nikainuka na kwenda kumuaga wifi kuwa kuna mahali naenda mara moja.
"Ila usichelewe kama jana"
"Nakuahidi wifi leo sichelewi"
Nikaondoka na kumuacha wifi akiendelea na mazoezi yake ya kwaya.
Kufika alipo Carlos nikamkuta akiwa makini kabisa kuningoja, jambo la kwanza ni kumuuliza kuhusu Suzy.
"Eeh niambie, ulitoa msaada gani kwakina Suzy jana?"
"Achana na habari hizo Sabrina hebu tuongee mambo ya maana sasa. Haya wifi yako umemuacha wapi?"
"Kwenye kwaya"
Carlos akacheka sana tena sana.
"Je, unataka nikwambie siri aliyonayo wifi ya ko kuhusu ule ujauzito wake?"
"Ndio niambie"
"Wifi yako ananichukia kwasababu kubwa moja tu, mi ni mtu wa kawaida tofauti na yeye anavyosema. Ngoja nikupe siri yake sasa."
Nikamuangalia Carlos kwa makini kisha nikamwambia.
"Niambie sasa, mbona husemi hiyo siri?"
"Ile mimba aliyonayo wifi yako si ya kaka yako"
Nikabaki kumshangaa Carlos kwani sikumuelewa, moja kwa moja nikajiuliza, kama mimba si ya kaka je ni ya nani? Na huyu Carlos amejuaje!
Itaendelea
 
SEHEMU YA 22





Moja kwa moja nikajiuliza, kama mimba si ya kaka je ni ya nani? Na huyu Carlos amejuaje!
Nikamuangalia vizuri ili kumdadisi maneno yake, Carlos nae alikuwa akiniangalia kwa makini kabisa nadhani alikuwa akicheza na akili yangu. Mara akasema,
"Najua unajiuliza maswali mengi Sabrina juu ya hili swala ila ukinisikiliza kwa makini utaelewa kila kitu"
"Ndio nahitaji kujua, je kaka anajua kama ile mimba si yake?"
"Kakako hajui chochote na ndomana nimekwambia kuwa ni siri, wifi yako ameitunza kwa muda mrefu sasa na hafikirii kama kuna mtu wa kuijua siri hii"
"Wewe umejuaje sasa?"
"Nina upeo mpana tofauti na unavyofikiri Sabrina, nilirithishwa na babu yangu. Niliposalimiana na wifi yako ndipo nikaijua siri hii na nikamwambia kisiri ila yeye akapiga makelele kama mtu aliyewehuka na kuongea maneno mengi ili wewe usiniamini mimi na unione ni mtu wa ajabu ila ninachokwambia mimi ni kitu cha kweli tena ni ukweli mtupu, kama huamini kamuulize wifi yako na kama akikataa mlete kwangu nimuumbue kwani ukweli wote naujua"
Maneno ya Carlos yakafanya nifikirie sana kwani nilikuwa siamini ingawa Carlos amekuwa akiniambia mambo mengi ya kweli.
"Ila je ile mimba ni ya nani?"
"Unataka kumjua Sabrina? Na ukimjua je utachukua hatua gani?"
"Kwakweli sijui, tena sijui kabisa hatua ya kuchukua ila lazima wifi nimuulize kuhusu hilo jambo"
"Muulize tu halafu upime maneno yangu, huwa siongopi mimi hata siku moja"
Nikamuangalia sana Carlos jinsi alivyoongea kwa kujiamini kabisa tena akionekana ni mtu mwenye uhakika wa kitu anachosema.
"Basi niambie kabisa kuwa ile mimba ni ya nani?"
"Nenda ukamuulize kwanza wifi yako, akikataa ndio nikutajie mwenyewe ile mimba kuwa ni ya nani"
"Tutaonana lini sasa tena?"
"Kesho, nitakuja tena hapahapa"
Nikakubaliana na Carlos kisha kuagana na kuondoka.
Nikaamua kurudi kule kwenye kwaya ili niungane na wifi kurudi nyumbani ila sikumkuta ikabidi nifanye safari ya kwenda nyumbani nako nikakuta mlango umefungwa kwa maana kwamba wifi alikuwa bado hajarudi, ikabidi nimngoje pale nje.
Baada ya muda wifi alirudi akiwa amesindikizwa na yule mwalimu wa kwaya na kunikuta pale nje moja kwa moja wifi alianza kuongea.
"Yani Sabrina umeniudhi leo balaa, kwanini hukuniambia mapema kama utachelewa kiasi hiki? Umefanya nikungoje muda wote kuwa utarejea, kwanini lakini?"
Nikamuangalia wifi bila ya kusema chochote.
Alikuwa akiongea huku akifungua mlango, kisha tukaingia ndani na yule mwalimu akaaga na kuondoka.
Wifi hakuacha kunisema hata tulipokuwa ndani akidai kuwa nimempotezea muda wake akiningoja kule kwenye kwaya.
"Nadhani itakuwa vyema nikimwambia kaka yako kuhusu hili, umenikera sana. Au nimwambie tu kakako?"
Mara kaka alikuwa amewasili na kusikia vile ambavyo wifi alikuwa akifoka,
"Kuniambia nini tena? Kwani tatizo ni nini?"
Wifi akagelesha kwa hilo na kusema.
"Hapana bhana, nilikuwa naongea na Sabrina kuwa mtoto atakayezaliwa kama akiwa wakike basi tumuite Sabrina, yeye akawa anaogopa kuwa wewe hutokubali ndio nikamwambia kuwa au nikwambie wewe"
Maneno ya wifi yaliweza kumlainisha kaka na akakubali kuwa ndio ilivyokuwa.
"Usiogope Sabrina, wifi yako amekupenda sana ndomana anachagua jina lako"
Nikatabasamu tu ili kisieleweke chochote kwani wifi aliniokoa kwa lile maana kaka angejua kuwa kuna mahali nilienda ingekuwa shida.
Tukapika na kula ila sikuweza kumuuliza chochote wifi kwani niliogopa pa kuanzia ukizingatia kaka yupo.
Muda wa kulala nikaenda zangu chumbani na kulala.
Nilipokuwa kitandani maswali mengi sana nilijiuliza na kusema kuwa lazima nimuulize wifi kuhusu kitu nilichoambiwa na Carlos.
Mara Sam akanipigia simu, nami nikapokea na kuongea nae.
"Nasikia ulimuagiza Carlos aende kwa wakina Suzy kuwasaidia. Naomba nikuulize kitu Sabrina"
"Uliza"
"Je, huwa unaonana na Carlos huko?"
"Ndio, kwani kunatatizo?"
"Hamna tatizo nimeuliza tu, Carlos ulimpigia simu muda gani kumwambia kuwa wakina Suzy wapo khatarini?"
"Muda nilipopewa taarifa kwani nilikuwa naongea nae muda huo huo"
"Kuwa mwangalifu Sabrina sababu Carlos sio kama unavyomuona. Simjui Carlos ila namuona kama kikwazo kwenye maisha yetu"
"Kwani Carlos rafiki yako au rafiki yangu?"
"Ni rafiki yako wewe Sabrina ila mimi kama mpenzi wako nina haki ya kukwambia rafiki bora na mbaya"
"Hayo mapenzi mimi na wewe yalishaisha Sam nenda tu ukaendelee na Lucy wako"
"Ilimradi najua na kutambua kuwa hakuna chochote kinachoendelea kati yangu na Lucy basi sitaacha kukufatilia wewe Sabrina hadi mwisho wangu"
"Unajisumbua tu kwa sasa"
"Na sitaacha kujisumbua kwa mtu nimpendaye, najua umevurugwa tu kwasasa"
"Nani kavurugwa?"
"Wewe hapo umevurugwa Sabrina"
"Umevurugwa mwenyewe"
Nikakata simu kwani alikuwa akinizidishia hasira tu, ila nikatafakari sana na kuona kweli Sam ananipenda. Nikachukua simu yangu na kumtumia Sam ujumbe mfupi wa maneno.
"Asante kwa kunipenda Sam, nitakupenda daima"
Kisha nilala baada ya kutuma ujumbe huo, kwenye ndoto nikamuona Sam na Lucy wakiwa pamoja na kufurahi sana, mimi nilikuwa pembeni kuangalia jinsi wanavyofurahia mapenzi yao huku roho ikiniuma sana kutokana na wivu, kisha nikawaona ndugu wa Sam na ndugu wa Lucy wakiwa pamoja kama vile watu wanaojuana sana halafu nikamuona Sam akimvisha pete Lucy, hapo nikashtuka na kusema kwa nguvu.
"Noooooo...."
Nikaamka na kugundua kuwa ni ndoto tu, nikachukua simu yangu ili nimpigie Sam kumwambia nilivyoota.
Nikakuta ujumbe kwenye simu yangu kutoka kwa Sam umeandikwa,
"Usijali mpenzi nakupenda sana Lucy wangu"
Hapo mapigo ya moyo yakaanza kunienda kwa kasi na machozi kunidondoka. Nikajiuliza nitaumia hadi lini kwaajili ya Sam? Kwanini anitese kiasi hiki halafu bado anadai kunipenda? Roho iliniuma sana, nikaghairi kumpigia tena Sam na usingizi sikupata sababu ya mawazo na machozi yaliyonitoka mfululizo hadi kunakucha sikuwa na raha yoyote.
Siku ya leo sikuwa na raha kabisa kwani nilijihisi mpweke na uchovu mwaingi huku nikitamani kumuuliza wifi kuhusu mimba yake ila sikujua ni wapi pa kuanzia kumuuliza. Nikabaki kumtazama tu kwa yote aliyokuwa akiyafanya.
Muda ulipotulia nilikaa na wifi huku tukitaniana akaanza tena kuniambia kuhusu jina la mtoo atakayezaliwa.
"Yani huyu mwanangu lazima nitamuita Sabrina"
"Hata kama wa kiume?"
"Wakike huyu, mbona unapenda kung'ang'ania jambo moja? Mimi ndio mama wa huyu mtoto na nimekwambia kuwea ni wa kiume"
"Sawa wifi, kuna swali nataka kukuuliza"
"Uliza tu, kuwa huru Sabrina"
Nikasita kidogo kwani swali langu lilikuwa na utata na sikujua wifi angelipokeaje swali lile.
"Mbona huulizi? Nipo makini hapa kukusikiliza ujue!"
Nikapumua kidogo kabla ya kuuliza swali langu. Nikaamua kutafuta njia ya kuuliza kwa urahisi nitakacho kujua.
"Wifi unadhani mtoto atakayezaliwa atafanana na nani?"
"Mmmh! Asipofanana na wewe basi atafanana na kaka yako"
"Kwanini wifi?"
"Kwanini tena?? Si kwasababu ni damu yenu"
Hapo ndipo nikabadilika na kumwambia kuwa wifi ni muongo.
"Muongo wifi"
"Mimi muongo? Uongo wangu uko wapi?"
Sasa nikapata ujasiri wa kumwambia na wifi akachukizwa sana.
"Hiyo sio damu yetu maana hiyo mimba sio ya kaka"
"Unasemaje Sabrina? Kama mimba hii sio ya kaka yako ni ya nani sasa? Wewe mtoto vipi umetumwa nini nyumba imekushinda hii eeh! Kukupenda kote Sabrina bado unanizulia maneno! Kweli binadamu wabaya"
Wifi aliongea maneno mengi bila hata ya kupumzika na akanichukia gafla.
"Sema sas, kama hii mimba si ya kaka yako ni ya nani?'
Nikabaki kutoa mimacho kwavile sikujua mimba ni ya nani.
Tangia hapo wifi hakutaka tena kuongea na mimi hata kwenye kwaya leo alienda peke yake nami nikabaki nyumbani.
Nikiwa mwenyewe nyumbani nikapigiwa simu na Carlos ambaye alihitaji kuonana na mimi, na kwa vile mimi nilitaka kuonana na yeye kwa sana nikamwambia aje pale nyumbani kwa kaka kwani wote hawapo na pia nahitaji kuzungumza nae.
Hakuchukua muda sana alikuwa ameshawasili pale kwa kaka, nikamkaribisha na kuzungumza nae.
"Wifi yangu amekataa kabisa na kunichukia"
"Nilijua hilo kabla ndiomana leo nimekuja"
"Sasa utanisaidiaje kwa hilo?"
"Wifi yako anadhani unakisia tu na huujui ukweli ndomana anakufanyia ukali ili usitambue kabisa kinachoendelea, sasa mimi nakutajia mtu aliyempa ujauzito wifi yako. Ukipata muda wa kumwambia mwambie tu halafu utaona kitakachoendelea"
"Niambie basi ile mimba ni ya nani?"
"Ile mimba ni ya kijana flani anaitwa James, mwambie wifi yako hivyo ataelewa halafu akigoma kukwambia ukweli nijulishe mimi nitakwambia kila kitu ilivyokuwa"
Kwakweli hakuna mtu aliyekuwa akinishangaza kama huyu Carlos kwani aliongea mambo mengi kwa kujiamini kisha akaniaga na kuondoka.
Nilitulia ndani nikimngoja wifi arudi huku hamu yangu ikiwa moja tu nayo ni kuujua ukweli wa mambo.
Kama kawaida wifi alirudishwa pale nyumbani na mwalimu wa kwaya kisha mwalimu huyo akaondoka,. Nilikaa na wifi ila hakunichangamkia tena halafu alionekana kuwa na hasira sana ila sikutaka kuacha kumwambia ukweli.
Nikamsogelea wifi na kumwambia,
"Hiyo mimba si ya kaka, ni mimba ya James"
Mara wifi akaanguka chini na kuanza kutapatapa kama mtu mwenye kifafa.
Itaendelea
 
SEHEMU YA 23


Mara wifi akaanguka chini na kuanza kutapatapa kama mtu mwenye kifafa.
Hofu ikatawala ndani yangu, nikaogopa sana kwani sikujua cha kufanya kwa wakati huo na sikujua ni kitu gani kimempata wifi yangu.
Wakati nahangaika pale chini na wifi huku nikimuamsha kwa kumtaja jina, kaka alikuwa amewasili na kukimbilia pale chini nilipokuwa na wifi.
"Vipi tena Sabrina, wifi yako kafanyaje?"
"Hata mi sijui, ameanguka gafla tu na kuanza kutapatapa"
Nikaogopa kumweleza kaka jambo lolote huku nikihofia kuwa kaka ataniona mimi mbaya.
Kaka akamnyanyua wifi na kwenda kumpakiza kwenye gari yake ili kumpeleka hospitali, bora kaka yangu ni mwenye nguvu maana mi mwenyewe nisingeweza kumbeba wifi na ile mimba.
Kisha nami nikapanda kwenye gari kwa lengo la kumpeleka wifi hospitali.
Kufika hospitali, wifi alikimbizwa moja kwa moja kwa daktari. Nilitulia kusikilizia kinachoendelea mara kaka akanifata na kuniambia kuwa nirudi nyumbani ili niandae vitu vya wifi kama khanga na vitenge na nguo, akanikodia gari.
Nami nikaondoka na kurudi nyumbani nikajua tu kuwa wifi atakuwa anataka kujifungua ndiomana wanahitaji hivyo vitu.
Nilifika na kuandaa kila kitu, nikaona karatasi iliyokunjwa vizuri kwenye kabati la kaka ila kabla sijafungua kaka alikuwa amewasili ikabidi nimkabidhi zile nguo na kumuuliza.
"Kwani wifi anaendeleaje?"
"Anaendelea vizuri ila ni kifafa cha uzazi kinamsumbua, tumuombe tu Mungu ili ajifungue salama maana kifafa kibaya sana"
"Basi unipe taarifa za huko kaka, uwe unanipigia simu"
"Hakuna tatizo, nimeshamtaarifu na mama kwahiyo atakuja hospitali. Wewe baki tu mdogo wangu kila kitu kitakuwa sawa, Mungu atasaidia"
Basi kaka akaondoka na kuniacha pale nyumbani, hamu ya kujua kilichoandikwa kwenye kile kikaratasi ilinijaa, nilitamani kujua maneno yaliyomo.
Nikaenda na kukichukua, kiliandikwa hivi:
"Nampenda sana mke wangu Joy, namuamini kuliko chochote duniani eeh Mungu nashukuru kwa kunipa mke muaminifu kama Joy"
Nikakisoma mara mbili mbili na kujiuliza, je ni kweli Joy ni mwaminifu? Kama ni mwaminifu mbona akabeba mimba ya mtu mwingine? Je uaminifu wake umepimwa kwa yapi?
Yote hayo ni mapenzi yao na sikutakiwa kuyaingilia ila je nitakaa kimya bila ya kusema ukweli? Maswali mengi nilijiuliza bila majibu, nikaamua kurudi chumbani kwangu huku nikiendelea na mawazo yangu hadi muda wa kulala ulipofika.
Nilipokuwa nimelala nilimuona wifi akijifungua mtoto mzuri sana wa kiume.
Nikashtuka na kutabasamu na kujisemea kuwa kumbe mawazo yangu yalikuwa kweli kuwa wifi atajifungua mtoto wa kiume, ila kuangalia vizuri ilikuwa ni ndoto sema siku hizi nimeanza kuziamini ndoto zangu, nikawa nangoja kukuche ili nipate uthibitisho wa ndoto yangu.
Asubuhi na mapema kaka aliwasili sababu alilala hukohuko hospitali kwaajili ya mke wake.
"Wifi anaendeleaje kaka?"
"Anaendelea vizuri sana, amejifungua mtoto wa kiume saa kumi na mbili asubuhi"
Nikafurahi sana,
"Ndio umuandaliage uji na kila kitu naenda kumchukua hivyo, nitarudi hapa na mama"
"Yupo hospitali na yeye?"
"Ndio yupo, nitarudi nae hapa"
Nikawa nangoja kwa hamu hata yale mawazo mengine kuhusu wifi yakapotea.
Nikaandaa uji kama nilivyozoea kuandaa kwani sikuzoea uji wa mzazi unatiwa nini.
Wakati naandaa uji, simu yangu ikaita na mpigaji alikuwa Carlos.
"Nini tatizo Carlos?"
"Nakusalimia tu, utampa jina gani mtoto wa wifi yako?"
"Mmh! Sijui, kwani umejua kama kajifungua?"
"Ndio najua, tena mtoto wa kiume"
Nikaishia kuguna kuwa huyu Carlos licha ya kuwa na upeo mkubwa basi atakuwa na upeo tofauti na wengine.
Nikakata ile simu ila akanitumia ujumbe mfupi wa maneno.
"Fikiria jina la kumpa mtoto wa wifi yako kwamaana wewe ndiye umeteuliwa kutoa jina"
Nikaanza kujifikiria sasa kuwa mwanzoni kabla wifi hajajifungua nilimwambia kuwa kama akijifungua mtoto wa kiume basi tutamuita "James" ila kwa sasa jina hilto lilinipa utata na nikashindwa kufikiria zaidi kwani ndio jina la kweli la baba wa mtoto.
Baada ya muda waliwasili nyumbani wifi, mama na kaka.
Mtoto alikuwa mzuri sana tena alichangamka na alipendeza kumuangalia, mama alienda kumuweka vizuri wifi, mimi na kaka tulibaki na mtoto.
Muda wote kaka alitabasamu huku akisema.
"Dah dume langu hilo"
Nilimwangalia tu kaka bila ya kusema chochote kwani nilihofia kwamba nitaanzia wapi kusema ukweli.
Mchana wa siku hiyo mambo yakawa shwari kabisa, wifi alitulia huku akimnyonyesha mtoto wake, mama nae alitulia pembeni na kaka yani kila mmoja alikuwa na hamu ya kumbeba mtoto ukizingatia mtoto mdogo anavutia sana.
Kaka akamuuliza mama,
"Mama eti tumuite nani?"
"Mi sijui, wazazi ndio muamue"
"Basi mdogo wangu Sabrina achague jina la kumpa mtoto"
"Mmh kaka mchagulie mwenyewe tu"
"Mi ningempa jina la mtu wangu wa karibu ila kwavile toka mwanzo wifi yako alitaka mtoto aitwe jina lako kama akiwa wakike basi ni wakiume na utatakiwa wewe utaje jina la kumpa"
"Kuna jina nilichagua kabla labda mmuulize wifi kama litafaa maana mimi nimelisahau"
Ikabidi kaka amuulize wifi
kuhusu hilo jina.
"Mmh hata mimi nimelisahau"
"Basi hilo jina litakuwa ni zuri, ukilikumbuka Sabrina ututajie tena"
Yani kaka alikuwa na furaha iliyopitiliza kwa yeye kupata mtoto tena mtoto wakiume.
Watu mbalimbali walianza kufika na kumuangalia mtoto huku wakimsifia kuwa mtoto ni mzuri sana na kumpa hongera wifi na kaka.
Moyo ulikuwa waniuma kila nikimsikia wifi akisifia kuwa mtoto kafanana na baba yake kwani sikuelewa anamaanisha kaka yangu au huyo James.
"Yani huyu mtoto mtundu kama baba yake, ona na macho yake ni baba yake mtupu"
Nilikuwa nikimuangalia tu na kukosa cha kufanya, kaka alikuwa akifurahia muda wote hata hakwenda mahali popote leo akimshuhudia mtoto aliyejua kuwa ni mwanae.
Ilipita wiki nzima bila ya mimi kutaja jina la kumpa mtoto, ikabidi kaka ampe jina lingine.
"Napendekeza huyu mtoto aitwe James"
Wifi akashtuka sana na kuropoka
"Kwanini asiitwe Deo?"
Kaka akacheka,
"Aitwe Deo kivipi? Itakuwaje mtoto Deo na baba Deo? Kwahiyo atakuwa Deo Deo! Mmh hata haipendezi"
Kisha kaka akanigeukia mimi na kuniuliza.
"Eti Sabrina hebu ona eti Deo Deo ndio nini? Itapendeza kweli!"
Nikaishia kucheka tu, kisha kaka akaendelea
"James Deo ndio itapendeza sio Deo Deo bhana"
Nikaguna na kujisemea moyoni je James James inakuwaje? Nikaishia na swali langu moyoni.
Wifi alikuwa kimya kabisa akitusikiliza kisa na yeye akaamua kumuuliza kaka.
"Kwanini umechagua jina hilo mume wangu?"
"Kwanza ni zuri, pili nina jamaa yangu anaitwa James dah ana roho nzuri sana. Ni mpole na mcheshi"
Nami nikachangia mada hapohapo.
"Hata mimi nilichagua jina hilohilo kaka"
"Kumbe mawazo yetu yanafanana, vizuri sana mdogo wangu"
Wifi alipokea jina lile kishingo upande, ni mimi tu niliyejua kwanini amenyong'onyea kwa kusikia hilo jina.
Wanakwaya wenzie walikuja kumuona mtoto wa wifi na kama kawaida watu hupenda kuanza na jina la mtoto ila wifi hakuwatajia huku akisema mtoto bado hajapewa jina.
Jioni yake nikapigiwa simu na Carlos,
"Badae nitakuja kwenu Sabrina"
"Utakuja kivipi mbona muda umeisha?"
"Nilisahau kama muda umeisha, basi nitakuja kesho"
Nikamaliza kuongea na Carlos na kuendelea kufanya mambo yangu mpaka muda wa kulala ulipowadia nikaenda kulala.
Nilipokuwa nimelala, nilihisi kuna mtu amelala pembeni yangu, uoga ukanijaa kwani niliogopa hata kugeuka huku nikihisi kuona mtu kweli nyuma yangu.
Nikahisi yule mtu akinipapasa mgongoni, hapo uoga ukawa zaidi ya mwanzo na nikatamani kupiga makelele ila sauti iliishia njiani, nikasikia kama mtu akiniambia.
"Acha uoga Sabrina, kwanini unakuwa muoga hivyo?"
Hofu ikazidi na kujibu nikashindwa, nikajikuta nikifumba macho kwa nguvu ili ile hali ipotee lakini haikupotea kwani nilihisi uwepo wa mtu kweli mgongoni mwangu.
Mara gafla mlango wa chumba changu ukafunguliwa na uwepo wa yule mtu ukapotea, hapo nilishtuka na kujifunika na shuka zaidi kwa uoga huku nikiwa nimejikunja.
Aliyeingia alikuja moja kwa moja na kunitingisha mgongoni kama kuniamsha.
"Sabrina, Sabrina"
Nilipoisikilizia ilikuwa ni sauti ya wifi Joy, hapo nikainuka na kumkumbatia.
"Una nini Sabrina?"
"Hamna kitu wifi"
"Mbona unaonyesha uoga halafu ulikuwa unaongea na nini?"
"Hakuna mtu wifi"
Akanishika mkono na kunivutia sebleni, kisha tukashikana mikono na kuniambia kuwa tuombe.
Kwakweli sikuwa muombaji mzuri kwahiyo ni wifi mwenyewe aliomba.
Baada ya maombi wifi alianza kunieleza.
"Unajua nilipokuwa nimelala chumbani, mtoto alikuwa anashtuka mara kwa mara nikajua kuna kitu tu. Unajua hawa watoto ni malaika huwa wanaona mambo mengi na vitu vingi ambavyo wakubwa hatuvioni, ndomana nikaja kukuamsha ili tusali"
"Asante wifi"
"Nenda ukalale kwa amani sasa"
Nilienda chumbani kwangu na kulala hadi kunakucha ila swala la wifi lilizidi kunichanganya kwani nilishindwa kujielewa kuwa ilikuwaje wifi hadi akamsaliti kaka, nilijiuliza sana bila ya majibu.
Siku ya leo niliamua kuvunja ukimya na kwenda kumuuliza tena wifi ili kupata ukweli ulio kamili.
Nilivizia muda ambao tulibaki wawili tu tena wakati mtoto amelala.
"Wifi niambie ukweli au unataka niseme kwa kaka?"
"Usifanye hivyo Sabrina, nihurumie wewe ni mwanamke mwenzangu"
"Hata kama mi ni mwanamke mwenzako, kumbuka mumeo ni kaka yangu wifi! Ilikuwaje hadi ukamsaliti na kwanini ulimsaliti? Hivi unajua ni kiasi gani unapendwa na kaka yangu? Yupo tayari kwa lolote kwaajili yako halafu unamsaliti kwa vazi la ulokole, mlokole gani wewe msaliti?"
"Usinitusi Sabrina, hujui nini kilitokea ni shetani tu huyu anataka kuharibu imani yangu"
Akainama akifuta machozi,
"Acha kumsingizia shetani, kwani huyo shetani hajakupeleka wewe huko kwenye mambo ya ajabu"
"Ndiomana nakwambia hujui kilichotokea mdogo wangu hujui, sikupanga wala kutaka kumsaliti kaka yako ila shetani anapitia kuvuruga watu wa Mungu"
"Nimekwambia acha kumsingizia shetani wifi unajua viapo vya ndoa wewe? Mi sijaolewa ila ninajua, hakuna mahali panaporuhusu kusalitiana."
"Mi sijamsaliti kaka yako wifi"
"Kama hujamsaliti ilikuwaje ubebe mimba ya mtu mwingine? Huo ni usaliti wifi, tena usaliti uliowazi kabisa tena huku ukiendelea kumuongopea kaka kuwa mtoto ni wake"
"Sabrina nielewe tafadhari, yaliyonipata mimi yanaweza kukupata hata wewe nihurumie wifi yangu"
"Huruma yangu kwako ni kumwambia ukweli kaka"
"Tafadhari nihurumie Sabrina, nitaenda wapi mimi? Nani atanihudumia jamani!"
"Akuhudumie huyo James, kwani anashindwa nini?"
"James hawezi kunihudumia Sabrina hawezi, nisaidie mwanamke mwenzio nateseka mimi"
Huruma ilianza kuingia moyoni mwangu ila nikamkazia.
"Msaada wangu kwako ni huo tu, kumwambia ukweli kaka Deo"
Wifi akainuka na kupiga magoti mbele yangu huku akilia. Huruma ikanijaa
"Nihurumie wifi nihurumie"
Mara kaka akarudi na kutukuta katika hali ile.
Itaendelea
 
SEHEMU YA 24


Mara kaka akarudi na kutukuta katika hali ile.
Moja kwa moja aliuliza swali.
"Kuna nini hapa?"
Wifi alishtuka na kutetemeka, sikujua ni kitu gani cha kusema wakati huo.
Wifi akajifuta machozi na kujibu kwa haraka.
"Tulikuwa tunaigiza mume wangu"
Huku akijichekelesha, kaka akabaki kushangaa na kuuliza.
"Kuigiza! Kuigiza kivipi na kuigiza gani huko mpaka machozi. Eti Sabrina?"
Kaka alinikazia macho huku wifi nae akiniangalia na kunikonyeza ili tu nikubali kuwa ni kweli.
"Ndio, tulikuwa tunaigiza kaka"
Kaka akakaa chini sasa na kuendelea kudadisi,
"Kwanza huko kuigiza mmeanza lini? Na ndio mniambie sasa hayo maigizo ni maigizo gani ya wewe Joy kumpigia magoti Sabrina tena huku ukitoa machozi na kumwambia akuhurumie"
Nadhani akili ya wifi ilifanyakazi kwa haraka sana na kupata cha kuelezea.
"Tulikuwa tunabishana hapa na Sabrina, alikuwa anasema kuwa mimi siwezi kuigiza kulia kama waigizaji wafanyavyo ndio tukawa tunajaribu hapo kuigiza kulia"
"Kwahiyo sasa umeweza?"
"Ndio hadi Sabrina kanikubali mwenyewe"
Huku akiendelea kujichekelesha kwa kujifanyisha, mara mtoto akaanza kulia.
"Nenda kamchukue mwanangu analia huko Joy, acheni ujinga wenu hapa"
Wifi akainuka na kaka akamfata, nikabaki mwenyewe nikitafakari bila ya kupata jibu la maana wala lililo kamili.
Nikiwa pale sebleni, kaka alikuja kukaa huku amemshika mtoto mikononi kisha akaongea nami.
"Unamuonaje James Sabrina, nimefanana nae eeh!"
Ikabidi niitikie tu na kumkubalia.
"Ndio unafanana nae haswaa rangi"
"Dume langu hili, dume la mbegu. Huyu ndio mwanamke bhana yani first born kaniletea dume, nimefurahi sana"
"Kwani angekuletea wa kike usingefurahi?"
"Ningefurahi ila furaha yange isingezidi niliyonayo
sasa. Kwakweli nimefurahi sasa kwasasa. Mtu unapata kipenda roho bhana"
Nikatabasamu tu huku nikitamani kumwambia kaka kuwa yule sio mtoto wake ila mdomo wangu ukasita na kujisemea kimoyomoyo kuwa kitanda hakizai haramu.
Tuliongea na kaka pale hadi muda wa kula, siku hizi alikuwa anawahi sana kurudi nyumbani tofauti na hapo mwanzoni.
Tulipomaliza kula nilienda chumbani kulala nikapigiwa simu na Sam.
"Hivi wewe mwanaume utaniacha lini mwenzio niweze kuishi kwa amani?"
"Siwezi kukuacha Sabrina sababu nakupenda, hujui tu jinsi gani unamaanisha kwenye maisha yangu"
"Porojo sitaki Sam, mtu gani wewe hadi massage za Lucy unanitumia mimi! Sikutaki Sam ingawa bado nakupenda"
Nikakata simu, muda huo huo simu ya Carlos ikaingia.
"Vipi Sabrina, naona namba busy ulikuwa unaongea na Sam"
"Ndio kwani vipi?"
"Ngoja, kesho nitakuja kukuonyesha kitu"
"Kitu gani Carlos?"
"Nitakuonyesha kesho hata usiwe na haraka"
Nikamuaga na kukata simu huku nikitafakari mambo ambayo Carlos anataka kunionyesha.
Siku ya leo nililala vizuri sana kwani hapakuwa na tatizo lolote.
Kesho yake baada ya kaka kwenda kazini nilikaa na wifi na kuzungumza nae haswaa kuhusu swala lake la kuzaa na mwanaume mwingine zaidi ya kaka.
"Ninachotaka toka kwako wifi ni unieleze ilivyokuwa hadi kufikia hatua ya kumsaliti kaka yangu"
"Kwanza kabisa naomba unielewe wifi yangu, kitu hiki sikukitarajia hata mara moja kuwa kuna siku nitamsaliti mume wangu"
"Ndio umeshamsaliti sasa, niambie tu ilikuwaje na kwanini. Pengine maneno yako yanaweza kunisaidia mimi kuificha siri hii"
"Nitakwambia kila kitu wifi yangu, na utaelewa kwanini nasema kuwa ni mipango ya shetani."
"Nakusikiliza wifi, nipo makini kuyasikia maelezo yako yote utakayoyatoa"
Wifi akatulia kwanza na kujifuta machozi yaliyokuwa yakimtoka, kisha akaanza kunielezea.
"Mimi ni mwimbaji mzuri sana wa kwaya na pia nina moyo wa huruma, huruma hiyo ndiyo iliyoniponza hadi imekuwa hivi.
Siku moja mwalimu wetu wa kwaya hakufika mazoezini halafu akatupigia simu kuwa anaumwa sana. Niliwaomba wanakwaya wenzangu kuwa twende tukamuone ila waligoma kwavile James alinipigia mimi kunitaarifu na sio wao halafu wakidai kuwa James ni mvivu wa kutembelea wenzie wakiwa wagonjwa.
Walivyogoma iliniuma sana, ingawa niliwasihi kuwa wasilipize ubaya kwa ubaya bali walipize ubaya kwa wema ila hawakunisikiliza wala kukubali na kusema labda wataenda siku nyingine.
Nikaamua kwenda mwenyewe nyumbani kwa James kuona hali yake ukizingatia anapoishi ni njiani na ninapoishi mimi.
Kufika kwa James nilimkuta amelala hoi kitandani hajiwezi kabisa akafurahi kuniona na kuniomba nikamtafutie chakula kwani hata kula alikuwa hajala, nilitoka na kwenda kumtafutia chakula na kumletea.
James alikula chakula kile hadi kukimaliza na mara gafla alichangamka sana na kuanza kuongea maneno mengi kamavile ugonjwa uliomsumbua ni njaa.
Ni hapo nilipomuuliza kuwa anatatizo gani akaniambia ni upweke unamsumbua tena huku akitoa machozi na kudai kuwa hawezi kuwa na mwanamke amtakaye sababu hana uwezo, nilimsikiliza na kumtia moyo kuwa aendelee kumwomba Mungu tu ipo siku atampatia amtakaye.
Kimya kikatawala nami nikaaga kuondoka, kabla sijainuka James alikuja na kusimama mbele yangu huku akinizuia kuwa nisiondoke.
Nikaanza kupambana nae ila James alikuwa na nguvu za ajabu na akatumia nguvu hizo kuniingilia kimwili kwa nguvu kwahiyo alinibaka. (wifi akainama na kujifuta tena machozi yaliyomtoka kama maji)
Nililia sana tena sana ila ndio hivyo nilikuwa nimeshabakwa.
Kaka yako hakuwepo kipindi hicho kwani alisafiri kikazi, nilirudi nyumbani na kulia sana huku nikitubu kwani sijui ni kwanini mimi nipitie haya yote.
Sikwenda kwenye kwaya wiki mbili kwani bado nilikuwa na uchungu wa kuonana na James ila nae alikuja kuniomba msamaha na kusema hakutarajia ila shetani alimpitia.
Baada ya muda nilijihisi mjamzito, kwenda kupima nikajikuta ni mjamzito kweli, kaka yako aliporudi tulikaa kama mwezi nikamfahamisha kuwa nina mimba yake na sikutaka aujue ukweli kwani angeniacha.
Kuhusu siri ya ujauzito huu ni mimi pekee nijuae hata James mwenyewe hajua sababu sijawahi kumwambia, huwa anadhani hii mimba ni ya mume wangu.
Kutoa nilishindwa wifi ndiomana nikaendelea kufanya siri hata sijui wewe umejuaje jamani ila naomba unisaidie Sabrina, mwanamke mwenzio mimi"
"Nimekuelewa wifi yangu, pole sana ila kama James alikufanyia vibaya hivyo mbona unapatana nae sana?"
"Sikuweza kuendelea kuwa na kinyongo nae, wakati nina mimba uwepo wake kwangu ulinivutia sana na sikuweza kumkwepa wala kumtenga Sabrina"
"Huoni kama itakuwa tatizo kama kaka akigundua jambo hili?"
"Ndiomana nakwambia nitunzie siri hii Sabrina, sina pakwenda mie. James hawezi kunihudumia"
"Ila ana haki ya kutambua uwepo wa mtoto wake"
"Tafadhari Sabrina, nisaidie mie. Deo ndio mwanaume anayeweza kunitunza na kunihudumia, James hawezi jamani nisaidie mimi"
"Ila wifi, ukweli humuweka mtu huru"
"Si ukweli kama huu Sabrina, ukweli huu utaniangamiza mimi jamani"
Kilio cha wifi kilinipa moyo wa huruma ila bado ni ngumu kwangu kuitunza siri hii tena kwa kaka yangu wa damu.
Jioni ya leo nilitulia kabisa huku nikitafakari yanayotokea na maana yake katika maisha yangu, bado sikuelewa.
"Kwanini siri hii niijue mimi na si mwingine?"
Nilikosa jibu kabisa, wakati natafakari nikapigiwa simu na Carlos na kunitaka tukutane.
Nikajiandaa na kumuaga wifi kisha nikaondoka.
Kama kawaida nilimkuta Carlos ameshawasili eneo lile akiwa na tabasamu kubwa sana. Nikasalimiana nae pale, kisha kuanza kuzungumza yaliyohitajika pale.
Kabla ya kuanza kuzungumza nikaona gari ya kaka ikipita pale karibu, nikashtuka sana kuwa kaka ataniona mara akanipigia
simu.
"Kuna mahali nakuona hapa Sabrina, ni wewe au sio?"
Nikapata kigugumizi cha kujibu na kumuangalia Carlos aliyeniambia niseme kuwa si mimi. Nikamjibu kaka kuwa si mimi ila inaonyesha kaka hakuamini maneno yangu, nikamuona akishuka kwenye gari yangu na kuja eneo nilipo kuhakikisha.
Nilikuwa natetemeka, Carlos akaniambia.
"Tulia hivyo hivyo Sabrina, hawezi kukujua huyo"
Nilizidi kutetemeka tu kadri kaka alivyosogea hata sikuelewa itakuwaje pale agundue ni mimi, nilihisi kupigwa vibao leo ila sikuweza kukimbia kwani hata nikikimbia ameshaniona.
Nilimuangalia kaka akizidi kusogea mahali nilipo na mimi nikizidi kutetemeka.
Kaka alifika hadi mbele ya mimi na Carlos akatuangalia kisha akaondoka, alipofika karibu na gari yake akanipigia tena simu.
"Kumbe nimekufananisha mdogo wangu, yani hadi sikuamini nikaenda kushuhudia mwenyewe mmh kufika pale sio wewe kabisa ni watu wengine"
"Usijali kaka"
"Uko wapi lakini muda huu"
Carlos akasema nijibu kuwa nipo nyumbani, nami nikamjibu hivyo hivyo.
"Sawa basi tutaonana badae"
"Hakuna tatizo kaka"
Nikakata simu na kupumua kidogo kisha nikamuuliza Carlos.
"Je akienda nyumbani bila kunikuta itakuwaje?"
"Kaka yako haendi nyumbani saa hizi"
"Umejuaje?"
"Nimejua tu kama haendi"
Nikaguna na kumuuliza,
"Na mbona hapa hajanitambua kama ni mimi?"
"Unajua mahali popote ukibambwa, wewe jikaushe tu yule mtu akikusogelea usionyeshe wasiwasi basi atajua tu amekufananisha"
Maneno ya Carlos niliyaamini nusu nusu.
"Haya sasa nionyeshe vitu unavyotaka kunionyesha"
Carlos akatabasamu na kuniangalia kwa makini sana kisha akaniuliza.
"Kweli unataka kuviona?"
"Ndio, nionyeshe"
"Utaweza kustahimili?"
"Nitaweza Carlos kwanini nisiweze?"
"Basi kaa tayari kuona utakacho"
Nikatulia kumsikilizia Carlos na kitu anachotaka kunionyesha, kisha akaniambia.
"Fumba macho Sabrina, usifumbue hadi nitakapokwambia ufumbue"
Nikafumba macho ila uoga ukanishika ukizingatia maneno ya watu wanaoniambia kuwa Carlos sio mtu wa kawaida.
Nikajikuta nafumbua macho kabla ya Carlos kusema nifumbue.
Ile kufumbua tu, nikayaona macho ya Carlos yakiwaka moto.
Itaendelea
 
SEHEMU YA 25


Ile kufumba tu nikayaona macho ya Carlos yakiwaka moto.
Nikashtuka sana na kujifunika usoni mwangu kwa kiganja cha mkono huku nikitaka kukimbia, Carlos alinishika mkono kwa kunizuia. Muda wote nilikuwa natetemeka.
"Acha uoga Sabrina"
"Uoga gani wakati macho yako yanawaka moto"
"Yanawaka moto! Acha uoga bhana, hebu toa mkono na ufumbue macho uone kama kweli macho yangu yanawaka moto"
Nikiwa naogopa sana na kutoa mkono usoni kwa uoga huku nikifumbua macho kwa uoga na kuogopa kumtazama Carlos huku nikihofia kuona mengine makubwa zaidi.
"Fumbua Sabrina usiogope"
Nikafumbua na kuyaona macho ya Carlos yakiwa kawaida kabisa kama ya wengine.
"Haya niambie, wapi yanawaka moto?"
Nikatikisa kichwa tu kuwa hakuna.
"Niangalie vizuri Sabrina, mimi ni mwanadamu wa kawaida kama wewe, maneno ya watu yanafanya uniogope na kufikiria mambo mengine ambayo mimi sihusiki nayo"
Nikawa namtazama tu Carlos na maneno yake.
"Najua kwanini umefikia kuwa hivyo"
"Kwanini?"
"Kwanza ulikuwa unafikiria maneno ya watu wanayokwambia kuhusu mimi pia hukufumbua macho bali mawazoni mwako uliwaza kuwa umefumbua na kuniona hivyo. Siku zote unapomuwazia mtu mabaya unajikuta ukiwa na wasiwasi nae muda wote. Kama ningekuwa mtu mbaya ningekudhuru muda mrefu tu Sabrina ila mimi ni mtu mwema na pia nina nia nzuri maishani mwako, huwezi kujutia kuwa na rafiki kama mimi. Niamini Sabrina kuwa mimi ni binadamu wa kawaida"
"Sawa nimekuelewa Carlos"
Mazungumzo yetu yakaendelea ila katika hali ya tahadhari sana, kisha Carlos akanikabidhi bahasha na kuniambia kuwa nikaifungulie nyumbani, halafu tukaagana.
Nikapanda kwenye gari yake hadi mitaa ya karibu, na kushuka kisha kwenda nyumbani.
Nilipofika ndani jambo la kwanza ni kumuuliza wifi
"Kaka amerudi?"
"Hata bado hajarudi, amechelewa kweli leo"
Nikaenda chumbani kwangu na kuweka ile bahasha kisha kwenda kumsaidia wifi kazi mbalimbali, muda huo huo kaka nae akawasili akiwa na mizigo.
"Nilipitia kumnunulia mwanangu vitu vya kuchezea"
Wifi alionyesha furaha sana, tukavipokea vile vitu vilikuwa vingi sana na nguo nzuri pamoja na viatu vya mtoto.
Wifi akauliza kwa utani.
"Mmmh hata mama mtu nasahaulika zawadi jamani"
"Muda wa mwanangu kujidai huu, wewe mama mtu tulia"
Wote tukacheka na kuendelea kupanga mizigo, kwakweli kaka alimpenda sana mtoto James hata nikawaza kama itawezekana kumwambia kaka ukweli kuhusu mtoto huyo.
Tuliongea mengi hadi muda wa kula na kulala ulipofika.
Kama kawaida nilienda zangu chumbani kwangu mapema kabisa.
Nilipokuwa chumbani nikaikumbuka ile bahasha niliyopewa na Carlos, nikaichukua na kuangalia kilichomo ndani yake.
Zilikuwa ni picha, nikazitoa kuziangalia.
Picha zilionyesha Sam na Lucy wakiwa ufukweni moyo wangu ukapasuka kwa wivu, kwakweli nakiri wazi kuwa siwezi kuacha kumpenda Sam.
Roho iliniuma sana kwani nilihisi kuanza kumsahau Sam ukizingatia toka nije kwa kaka sijaonana nae tena na wala sitegemei kuonana nae kwa kipindi hiki ila kwanini nizione picha za kuumiza moyo wangu kiasi hiki? Lucy na Sam walionekana ni wenye furaha sana kwenye picha huku wakifurahia mapenzi yao.
Zile picha zilionyesha tarehe mwezi mwaka na muda ambao zilipigwa ilikuwa ni juzi, kwakweli sikuamini nikachukua simu yangu na kumpigia Sam ili kujua juzi alikuwa wapi.
"Ulikuwa wapi juzi jioni?"
"Nilienda beach kwani vipi Sabrina?"
"Ulienda na nani?"
"Marafiki zangu tu"
"Hawana majina?"
"Jamani Sabrina kwani ugomvi?"
Nikakata simu na kuamini moja kwa moja kuwa Sam alikuwa na Lucy siku hiyo moyo ukaniuma sana, nikajikuta natokwa na machozi na kujiuliza kuwa ni lini nitajifunza kumsahau Sam, mbona ananitesa sana!
Nilijililia tu, wakati naendelea kuangalia zile picha nikaona karatasi lenye maandishi kwenye zile picha limeandikwa;
"Mtoto mzuri kama wewe hutakiwi kulia lia hovyo, mimi nipo kuyafuta machozi yako yote na kukufanya binti mwenye furaha siku zote. Usilie Sabrina, tambua kwamba Carlos yupo kwaajili yako"
Nikakisoma mara mbili mbili na kujiuliza, inamaana Carlos ananitaka au? Itakuwa ananitaka tu ndiomana yupo karibu sana na mimi. Na kama kweli ananitaka je nimkubalie kweli? Ila anaweza akanisaidia mengi maana ana upeo mpana.
Nikajikuta nikiwaza hivyo kuhusu Carlos na mambo yake yote kwangu.
Ingawa picha ziliniumiza sana ila maneno ya Carlos kwenye kile kikaratasi yalinifariji moyo wangu.
Ili kujiridhisha zaidi na zile picha nikampigia Lucy simu kumuuliza.
"Samahani, unaweza kuniambia juzi jioni ulikuwa wapi?"
"Kwani unanidai? Nilikuwa beach"
"Na nani?"
"Swali gani hilo sasa? Nilikuwa na mpenzi wangu"
Nikakata simu na kuamini zaidi kuwa ni kweli walikuwa wote na moyo kuzidi kuniuma.
Nilikaa kitandani huku ninalia ila badae nilihisi kuna mtu ananibembeleza hadi kujikuta nimelala hadi asubuhi kulipokucha.
Nilitoka chumbani na kwenda kufanya kazi za usafi kwa ile asubuhi.
Wakati nadeki nikaona maandishi mekundu juu ya zile marumaru nyeupe pale sebleni, yameandikwa jina tu "JAMES" Nikashtuka sana na kumuita wifi, alipokuja yale maandishi hayakuwepo.
"Kwani ni kitu gani Sabrina?"
Nikakataa kuwa hamna kitu kwakuwa yale maandishi hayakuwepo tena kwahiyo nikaona kuwa wifi atanishangaa tu.
"Ila wewe Sabrina una matatizo ingawa hupendi kuyaweka wazi"
Nikamuangalia tu wifi bila ya kusema chochote.
"Badae tuongee kama utakuwa tayari kuniambia basi nijue jinsi gani ya kukusaidia"
Nikamuitikia wifi kuwa badae nitazungumza nae.
Nikaendelea na kazi zangu kama kawaida mpaka kuzimaliza.
Nilipokuwa nimepumzika sasa wifi akaona kuwa ni muda muafka wa mimi kuzungumza na yeye kuhusu matatizo yangu.
"Niambie Sabrina, usinifiche kitu tafadhari. Niko tayari kukusaidia kwa lolote lile"
"Ni kweli wifi nina matatizo, pia swala lako la kuniambia kuwa nikutunzie siri linanisumbua sana"
"Jamani wifi yangu, hayo si yalishakwisha jamani! Yani bado unayo tu!"
"Lazima niwe nayo wifi ukizingatia yanamuhusu kaka yangu wa damu"
"Nakuelewa mdogo wangu, tuachane na hayo kwanza niambie kinachokusumbua zaidi. Au ni kuhusu yule mpenzi wako?"
Nikainuka na kwenda chumbani kwangu na kumchukulia zile picha wifi yangu ili nae akazione.
"Hapo kuna mpenzi wangu na huyo rafiki yangu"
Wifi akaangalia zile picha huku akiguna na kusema.
"Ila siku hizi kuna picha za kutengeneza wifi yangu"
"Sio kama hizi wifi"
Mara wifi akazitupa zile picha pembeni huku akishtuka sana.
"Mbona hivyo wifi kuna nini?"
"Naomba uzitoe hizo picha mbele yangu wifi sitaki kuziona"
"Zina nini kwani?"
"Zitoe kwanza nitakwambia"
Nikazibeba zile picha na kuzirudisha chumbani, kisha nikarudi tena sebleni kumuuliza wifi.
"Kwani zina nini wifi?"
"Subiri kwanza"
Wifi alikuwa kama mtu aliyechanganyikiwa, akainuka na kwenda chumbani kwake.
Nikabaki pale sebleni huku nikijiuliza maswali mengi mengi bila majibu yoyote.
Baada ya muda wifi alirudi tena pale sebleni.
"Niambie basi wifi, zile picha zina nini?"
"Tuachane na habari ya zile picha, tufanye mengine mdogo wangu"
Nikamshangaa sana wifi kwani sikumuelewa kabisa kuwa kwanini amebadilika kiasi kile.
Ikabidi tuendelee na mambo mengine tu.
Jioni yake kama kawaida nilifanya kazi za ndani na kumaliza ila bado wifi hakuwa na raha kabisa siku ya leo tangu muda ule nilipomuonyesha zile picha.
Akaniita tena kuzungumza na mimi.
"Sabrina, hebu niambie ukweli kabisa kuhusu matatizo yako."
"Mmh wifi mbona unakuwa hivyo?"
"Nahitaji kujua Sabrina, au niambie aliyekupa zile picha ni nani?"
Maswali ya wifi yangu yalikuwa yananichanganya tu, ila nikasikia mlio wa simu chumbani kwangu na kwenda kupokea.
Mpigaji alikuwa ni Suzy nikashangaa kuona napigiwa simu na Suzy leo.
"Asante Sabrina, nasikia wewe ndiye ulinisaidia"
"Pole sana rafiki yangu, kwani tatizo lilikuwa ni nini?"
"Yote anayafanya Carlos"
"Kivipi?"
"Siku tukionana nitakwambia rafiki yangu ila kuwa makini sana na Carlos"
"Kwanini?"
"Amenisababishia matatizo makubwa sana, siruhusiwi kumweleza mtu yeyote ila nitakwambia wewe tukionana rafiki yangu"
"Mmh! Ila unaendeleaje kwa sasa?"
"Naendelea vizuri, asante sana rafiki yangu umeokoa maisha yangu ila..."
"Ila nini Suzy?"
"Nitakwambia tu tukionana, usijali Sabrina"
Suzy akakata ile simu na kuniacha na maswali mengi bila majibu ukizingatia siku za nyuma niliambiwa ni Carlos aliyewasaidia, sasa iweje Suzy aniambie kuwa Carlos ndiye aliyemsababishia matatizo yale.
Bado sikupata jibu na kurudi sebleni pale alipo wifi ili niendelee kuzungumza nae.
Wakati tunaongea tukasikia mtu akigonga mlango, nikamsikia wifi.
"Aliyekupa picha huyo"
Nikashangaa na kwenda kufungua.
Nikamkuta Carlos amesimama huku akitabasamu.
Itaendelea muda si mrefu..!!
 
Back
Top Bottom