Mohamed,
Hii dhana kwamba kanisa Katoliki lilikuwa linatisha wafuasi wake wasijiunge na harakati za kupigania uhuru unahitaji kuifanyia utafiti zaidi. Kwa nini nasema hivyo? Katika vitabu vyote nilivyosoma kuhusu harakati za uhuru Tanzania ni wewe peke yako unayedai kuwa Wakatoliki walikatazwa kujiunga na harakati za kupigania uhuru. Pili, kama hiyo ingekuwa ni kweli, Sivalon asingekuja na kitabu chake kuonyesha jinsi kanisa katoliki lilivyokuwa karibu na harakati za kupigania uhuru pamoja na ukaribu wake na Julius Nyerere. Kanisa ambalo ningekubali kuwa lilikataza wafuasi wake kujiunga na harakati za uhuru nadhani ni Anglican, kwa sababu hili ni dhehebu la Kiingereza. Kaka yangu mkubwa (marehemu) pamoja na Oscar Kambona na John Malecela walifukuzwa shule, kaka yangu akiwa mwanafunzi na Malecela na Kambona waalimu, pale Alliance Secondary School Dodoma mwaka 1954 baada ya wao kuhudhuria mkutano wa TANU. Mwaka 1974 nilisafiri pamoja na Samora Machel kwenye ndege ndogo ya serikali kwenda Musoma. Ilikuwa ni safari ya saa tatu. Mimi nilikaaa kiti cha nyuma na Machel alipoingia akakaa nyuma, mbele kuna Butiku na Braganza (huyu alikuwa Mreno akimshauri Machel, na walikufa pamoja kwenye ile ndege iliyotunguliwa na Afrika kusini.) Anyway, katika mazungumzo yetu nilibaini kuwa yeye pia alikuwa mkatoliki, lakini non practicing. Akaniambia hapa Tanzania, kanisa la Katoliki limejiweka upande wa wananchi wakati Msumbiji, kanisa katoliki lilikuwa bega kwa bega na Wareno kuwakandamiza waafrika. Kwa hiyo haiingii akilini kwamba kanisa ambalo liliwazuia wafuasi wake wasishiriki katika juhudi za uhuru hilo hilo litoe mchango kwa Nyerere kwenda UN 1955, mwaka mmoja tu baada ya kuundwa kwa TANU.