NIMEUMIA SANA
Anaandika Kijana Msomi
Rashid Chilumba
Nimesikia zoezi la uokoaji kwenye ajali ya kivuko Mwanza limesitishwa hadi kesho kutokana na kiza, sasa kesho mtakwenda kuokoa au kuokota Maiti?
Hapo Mwanza kuna kikosi cha Jeshi, boti za doria za polisi, helikopta na vivuko vingine? Hivi kweli vyote hivyo havina taa kubwa za kuwezesha zoezi la uokozi kuendelea usiku kucha? Kama havina tulivinunua vya kazi gani?
Ni aibu kwa viongozi kusema tunaenda kulala eti kuna giza ziwani wakati kuna dazani ya watanzania wenzetu tunaowahudumia wamezama ziwani tena siyo kwa uzembe wao bali kwa ujuba na tabia ya kutokujali maisha ya watu na kutosimamia usalama wao.
Mkuu wa mkoa, RPC, mkuu wa kamandi ya Jeshi la Wananchi, Mkuu wa Bandari Mwanza mnapata wapi ujasiri wa kwenda kulala na kuna watu watoto wao, baba zao, Mama zao wamo majini na hawajui kama watawapata wakiwa hai? Hivi ingelikuwa ni jamaa zenu wa karibu mngepata ujasiri wa kusimamisha zoezi kwa sababu ya kiza?
Katika dunia ya leo seriously kabisa mnasema kiza kinawazuia kuokoa watu? Aiseee.... Kwa hiyo hao waliozama ikiwa kwa bahati bado wapo hai hadi sasa mnategemea Israeli atawangoja ninyi hadi kesho jua litapochomoza? Huu ni uzembe wa hali ya juu mno.
Kweli kabisa mnashindwa kufunga tochi kubwa kama zile za bandari kwenye helikopta moja ya polisi hapo na boti nne tano mkaingia kuwaokoa watanzania wenzetu? Hata ikiwa ni wafu lakini faraja ni kupata japo miili yao hadi kesho samaki, mawimbi ya ziwa nk inaweza kuwa imewapoteza zaidi.
Leo nimeumia sana, makosa yale yake ya Mv Bukoba, Spice Islander, Skagit yamejirudia Mv. Nyerere na watu wanaenda kulala usiku umeingia na vyombo vya habari vinaonesha shilawadu na kutoa dakika kiduchu kwa habari muhimu na msiba mkubwa huo wa taifa.
Na tena mlionywa mara kadhaa kuwa chombo ni kibovu. Mkuu wa bandari ya mwanza bado yupo na wadhifa wake na msimamizi wa Sumatra kanda ya ziwa kesho ataenda pia ofisini.
Mungu awapumzishe waliotangulia na atawalipa waliowasababishia kuzama kwenu kwa uzembe wao.
Cc
Dotto Bulendu
Malisa GJ
Kheri James
Tusaidiane kusema Ndugu zangu. Tunawezaje kwenda kulala na watanzania wenzetu wako majini sasa hivi?