Beki katili Nathan Fasika Idumba kwenye rada za Simba
View attachment 2251820
INAELEZWA kuwa, Rais wa Heshima wa Simba, ambaye pia ni mwekezaji wa klabu hiyo, Mohamed Dewji ‘Mo’, ameingilia usajili wa beki wa kati wa Cape Town City ya Afrika Kusini, Nathan Fasika Idumba.
Idumba raia wa DR Congo mwenye umri wa miaka 23, alijiunga na Cape Town City FC Julai 16, 2021, akitokea FC Saint Eloi ya kwao DR Congo.
Beki huyo anatajwa kuja kuwa pacha wa Henock Inonga Baka katika eneo la ulinzi la Simba msimu ujao ambapo tayari wachezaji hao wameshawahi kucheza pamoja.
Chanzo chetu kutoka ndani ya Bodi ya Wakurugenzi ya Simba, kimeweka bayana kwamba: “Ukisikia msimu ujao tumejipanga kufanya usajili wa kutisha basi ni vema tukaelewana hivyo, maana tayari Mo, kashika usukani wa usajili na hapa ninapoongea tayari ameiita menejimenti ya mchezaji wa Cape Town City, Nathan Fasika Idumba ili kukamilisha dili.
“Kimsingi Mo ameamua kufanya mazungumzo na uongozi wa Bro Soccer Management, ambao unamsimamia Idumba, hii ni baada ya kukamilisha mazungumzo ya awali na uongozi wa Cape Town City.
“Bodi yetu imeweka mkazo zaidi kwa Idumba kwa kuwa ni moja ya mabeki bora kwa sasa, kama akitua hatakuwa na kazi kubwa ya kuzoeana na Inonga ambaye tayari alishawahi kucheza naye, wanajuana vizuri,” kilisema chanzo hicho
Chanzo : Globalpublishers