Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch limesema kwamba hakuna ushahidi wowote unaothibitisha madai ya jeshi la Israel kwamba makao makuu ya Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (Hamas) yako chini ya Hospitali ya Al-Shifa.
Taarifa hiyo ya Human Rights Watch imetolewa huku ndege za kivita za Israel zikiendelea kulenga hospitali kadhaa katika Ukanda wa Gaza.
Shirika hilo la kutetea haki za binadamu lenye makao yake makuu New York nchini Marekani, limetahadharisha kuwa, kuendelea kwa mashambulizi karibu na Hospitali ya Al-Shifa "kunazua wasiwasi mkubwa kuhusu usalama wa maelfu ya raia waliokimbilia hifadhi kwenye hospitali hiyo."
Human Rights Watch imeongeza kuwa, viongozi wa dunia wanapaswa kuitaka Israel iwalinde raia na miundombinu ya kiraia na sio kufanya mashambulizi kinyume cha sheria.
Taarifa ya Shirika hilo la kimataifa la kutetea haki za binadamu imetolewa kukadhibisha madai ya jeshi la Israel ambalo liliituhumu Hamas kwamba imeweka makao yake makuu ya uongozi chini ya Hospitali ya Al Shifa, ambayo ndiyo hospitali kubwa zaidi katika Ukanda wa Gaza.
Harakati ya Hamas ilikadhibisha shutuma hizo za Israel na kusema kwamba, ni kisingizio kinachotumiwa na utawala huo haramu kuhalalisha "mauaji mapya ya kimbari."
Ofisi ya vyombo vya habari vya serikali katika Ukanda wa Gaza pia ilisema kuwa walikuwa tayari kupokea kamati ya Umoja wa Mataifa ili kukagua hali ya hospitali hiyo.