Waisrael wanapozungumzia Historia ya utaifa wao, huanzia kwenye ufalme wa Daudi (David) ambaye ndiye muasisi wa Ufalme wa Israel uliojulikana kama United Monarch mnamo mwaka 1004- 960BC. Baada ya kifo cha Daudi, mwanaye Suleiman (Solomon) alishika hatamu ya uongozi kuanzia mwaka 961-922BC. Baada ya kifo cha mfalme Suleiman mwaka 922BC Makabila kumi ya upande wa Kaskazini yalikataa kuwa chini ya Utawala wa mfalme Rehoboam ambaye alikuwa ni mtoto wa Mfalme Suleiman, hivyo makabila haya yalifanya uasi na kuanzisha ufalme wao walioupa jina la Ufalme wa Israel-Samaria, mji mkuu wa Ufalme huu uliitwa Samaria, baadae walihamishia makao makuu kwenda mji wa Wacaanan wa Sichem ambao kwa sasa unajulikana kama Nablus. Ufalme huu ulisambaratika baada ya kuangukia mikononi mwa dola ya Assyria ( Assyrian Empire) mnamo mwaka 720BC.
Hali hii ilipelekea kuwepo kwa falme mbili za Kiebrania za upande wa Kaskazini na upande wa kusini ambayo hii ya upande wa kusini ilibaki kuwa chini ya Mfalme Rehoboam ilijulikana kama nchi ya Yuda (Judah), makao yake Makuu yalibaki katika mji wa Jerusalem na baadae yalihamishiwa katika mji wa Hebron. Ufalme huu ulisambaratika baada ya kushindwa vita na kuangukia mikononi mwa mfalme Nebuchadnezzar wa Babeli mnamo mwaka 587BC.
Mwaka 63BC nchi ya Yuda iliwekwa chini ya uangalizi wa dola ya Kirumi na mwaka wa 6CE iliunganishwa na kuwa jimbo la Warumi. Mnamo kwaka 135CE Wayahudi waliasi na kupelekea vita baina yao na Warumi ambapo walishindwa vibaya, walipoteza uhuru wao na mji wa Jerusalem uligeuzwa kuwa mji wa
kipagani.Wayahudi walipigwa marufuku kuishi Jerusalem na Warumi waliibadili jina nchi ya Yuda na kuiita Syria Palestina.
Kusambaratika kwa falme hizi mbili za kiyahudi na kutawaliwa na madola makubwa kuanza Assyria empire, Babylonian empire, Persian Empire (Iran), Greek empire, Roman Empire, Rashidun Caliphate, Ummayad Caliphate, Ayyubid Dynasty, Mamluk Sultanate, Ottoman Empire na British Empire (United Kingdom) kulipelekea Wayahudi kutawanyika katika maeneo mbali mbali Duniani. Kutawanyika huku kuliwagawa Wayahudi kwa majina kutegemea na maeneo waliyotawanyikia. Makundi haya ya Wayahudi ni Ashkenazi (Ashkenazi Jews) kundi hili ni lile lililohamia katikati na Mashariki ya bara la Ulaya. Sephard (Sephardic Jews ) ni kundi lililohamia maeneo ya kusini ya bara la Ulaya na Kaskazini ya Afrika na Mizrahi (Mizrahi Jews) ambao walibaki mashariki ya kati, Asia ya Kusini na Asia ya kati.