MKWASA AMTAKA MOLINGA ATULIE
Kaimu Kocha Mkuu wa Yanga Charles Mkwasa amemtaka mshambuliaji wa timu hiyo David Molinga kutulia inapotokea anafanyiwa mabadiliko
Molinga ni mchezaji asiyependa kutolewa uwanjani na mara nyingi anapofanyiwa mabadiliko huonyesha hasira zake waziwazi
Ni tabia ambayo hakuianza wakati huu wa Mkwasa, hata wakati Yanga ikinolewa na Mwinyi Zahera alifanya hivyo
Mkwasa amesema mabadiliko yanayofanyika mara nyingi yanakuwa na lengo la kuiweka timu sawa baada ya kubaini mapungufu ya mchezaji au mbinu za mchezo "Sio jambo jema kuonyesha utovu wa nidhamu pale mchezaji anapofanyiwa mabadiliko. Benchi la ufundi ndilo linafahamu mahitaji ya mchezo hivyo suala la mabadiliko halifanywi tu kwa utashi wa kocha, kunakuwa na sababu," alisema Mkwasa "Molinga atulie, tuna mechi nyingi sana.. lakini pia kutolewa haimaanishi kuwa mchezaji amefanya vibaya, wakati mwingine ni mabadiliko ya mbinu tu"
Mkwasa alimtoa Molinga kwenye dakika ya 67 ya mchezo dhidi ya JKT Tanzania na nafasi yake kuchukuliwa na Abdulaziz Makame 'Bui'
Mkwasa aliondoa mshambuliaji na kuongeza kiungo katika jitihada za kuimarisha safu ya kiungo ambayo ilikuwa imetawaliwa na JKT Tanzania katika kipindi cha pili
Mabadiliko hayo yaliisaidia Yanga kulinda ushindi wa mabao 3-2 waliokuwa wameupata kwenye kipindi cha KWANZA.