JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA UJENZI NA UCHUKUZI
TAARIFA YA MTENDAJI MKUU WA WAKALA YA BARABARA (TANROADS) MHA. MOHAMED BESTA WAKATI WA UTIAJI SAINI WA MIKATABA SABA YA UJENZI WA BARABARA KWA KIWANGO CHA LAMI KWA UTARATIBU WA ENGINEERING, PROCUREMENT, CONSTRUCTION PLUS FINANCING (EPC+F)
TAREHE 16 JUNI, 2023
Mtendaji Mkuu wa TANROADS Mohamed Besta
Mhe. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa (MB), Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi;
Mhe. Rosemary Sitaki Senyamule, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Mheshimiwa Mwenyekiti wa Chama wa Mkoa na viongozi wote wa Chama mliopo;
Mhe, Selemani Kakoso; Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Miundombinu;
Waheshimiwa Mawaziri mliopo;
Mhe. Godfrey Kasekenya (Mbunge na naibu waziri wa Ujenzi) na Manaibu Waziri wote mliopo;
Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa mliopo;
Wahe. Wabunge wajumbe wa kamati ya kudumu ya Miundombinu na Wabunge wote mliopo wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Balozi Eng. Aisha Amour Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (sekta ya Ujenzi) na Makatibu wakuu wote mliopo;
Bwana Ludovick Nduhiye, Naibu Katibu Mkuu Ujenzi na Manaibu Katibu wakuu wote mliopo
Bwana Gugu RAS wa Mkoa wa Dodoma na Ma-RAS wote na wawakilishi wa Ma-RAS mliopo;
Mhe. Mkuu wa wilaya ya Dodoma na Wakuu wa wilaya wote mliopo;
Mheshimiwa Meya wa Jiji la Dodoma;
Viongozi wote mliopo wakiwemo wakuu wa Taasisi za umma na binafsi;
Viongozi wa Dini mliopo;
Wafanyakazi wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, TANROADS, na Taasisi zote chini ya Wizara mliopo;
Waandishi wa Habari;
Wageni Waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Nawasalimu kwa jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Mheshimiwa Mgeni Rasmi;
1. Ninaomba kukukaribisha sana katika hafla ya utiaji saini wa Mikataba ya miradi saba ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kwa utaratibu wa EPC+F.
2. Kabla ya kufanya zoezi la utiaji saini, naomba nitoe maelezo mafupi kuhusu miradi ya Ujenzi wa barabara hizi kama ifuatavyo:
Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
3. Miradi hii inayosainiwa leo itatekelezwa kwa utaratibu wa Engineering, Procurement, Construction and Financing (EPC+F) inayohusisha utekelezaji wa Mikataba ya ujenzi (EPC Contract) baina ya Mkandarasi na Taasisi ya Umma.
Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
4. Leo tutashuhudia utiaji saini wa Mikataba saba (7) ya Ujenzi wa Barabara zenye urefu wa jumla ya kilomita 2,035 kwa kiwango cha lami itakayogharimu takribani Shilingi Tirioni 3.7. Barabara hizo ni:
(a) Kidatu - Ifakara - Lupiro - Malinyi - Kilosa Mpepo - Londo - Lumecha/Songea
(b) Arusha – Kibaya – Kongwa
(c) Construction Of Handeni - Kiberashi - Kijingu - Njoro - Olboroti Mrijo Chini - Dalai - Chambalo - Chemba - Kwa Mtoro - Singida
(d) Igawa - Songwe - Tunduma
(e) Masasi - Nachingwea - Liwale
(f) Karatu - Mbulu - Hydom - Sibiti River - Lalago - Maswa
(g) Construction Of Mafinga - Mtwango – Mgololo
Mheshimiwa Mgeni rasmi
1. Kila Mkandarasi anayehusika na mradi mkubwa, atakua na timu nne za ujenzi katika kutekeleza Mradi. Aidha, Mchakato wa zabuni za EPC+F ulifanyika kupitia ushindani wa uwazi, (open competetive tendering). Mchakato ulianza tarehe 27 Juni, 2022. Jumla ya Makandarasi 129 walionesha nia. Mchakato wa zabuni ulipitia hatua mbalimbali na hatimaye baada ya uchambuzi, ilibainika kwamba Makandarasi wanne (4) walikidhi vigezo vilivyowekwa ambao tutasaini nao mikataba leo. Makandasi hao ni:
(a). Kampuni ya China Civil Engineering Construction (CCECC) ikishirikiana na kampuni ya China Railway 19th Bureau Group Corporation Ltd (CR19)
(b). kampuni ya Sinohydro Corporation Ltd.
(c). kampuni ya China Overseas Engineering Group Co, Ltd (COVEC) pamoja na kampuni ya China Railway No. 4 Engineering Group Co. Ltd (CREC4)
(d). Kampuni ya China Railway 15th Bureau Group (CR15G).
Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
5. Kupitia utaratibu wa EPC+F, Makandarasi watawajibika kufanya usanifu wa kina (Design) na kujenga barabara hizi kwa viwango na ubora ulioainishwa kwenye Mikataba. Vihatarishi vyote (risk) vinavyohusu usanifu wa mradi na muda wa ujenzi vitabebwa na Mkandarasi. Hivyo, utaratibu huu utawezesha Makandarasi kusanifu na kujenga barabara kwa Viwango na teknolojia za kisasa.
Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
6. Naomba kuishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuridhia utekelezaji wa Mikataba hii.
7. Wakala ya Barabara (TANROADS) itasimamia ujenzi wa barabara hizi kwa mujibu wa vigezo na masharti yaliyopo kwenye mikataba. Aidha, Makandarasi watakua na timu nne (4) kwa kila mradi mkubwa ili kuharakisha utekelezaji wa Miradi hiyo. Hivyo, sehemu zote zitaanza kutekelezwa sambamba kwa wakati mmoja. Kwa utaratibu huu, kazi zitafanyika kwa umakini na kukamilika mapema.
Mheshimiwa Mgeni Rasmi,
8. Nimalizie kwa kutoa wito kwa Makandarasi kufanya kazi zao kwa weledi wa hali ya juu ili kazi zote zikamilike ndani ya muda uliopangwa kwa viwango na gharama zilizokubalika.
MHE. MGENI RASMI, KWA HESHIMA NA TAADHIMA NAOMBA KUWASILISHA