Joe Biden ashinda uchaguzi wa Marekani na kuwa rais mteule wa Marekani baada ya kumshinda Donald Trump.
Bw. Biden ameshinda katika jimbo muhimu la Pennsylvania, akijizolea kura zaidi ya 270 zilizohitajika ili kunyakua kiti cha White House.
Kampeni ya Trump imeonesha mgombea wao hana mpango wa kukubali matokeo ya uchaguzi huo.
Matokeo hayo yanamfanya Trump kuwa rais wa kwanza kutumikia awamu moja madarakani tangu miaka ya 1990.
Uchaguzi huu umeshuhudia watu wengi wakijitokeza kupiga kura tangu miaka ya 1900. Bwana Biden ameshinda zaidi ya kura milioni 73 mpaka sasa, idadi ya juu kuwahi kutokea kwa mgombea yoyote yule Marekani. Trump akipata kura zaidi ya milioni 70 akishika nafasi ya pili kwa idadi kubwa katika historia ya Marekani.
Rais Trump alijitangaza mshindi wa uchaguzi wakati kura zikiendelea kuhesabiwa. Wakati wote amedai kuwa zoezi la kuhesabu kura limekuwa na dosari, lakini hajawasilisha ushahidi wowote kuhusu madai yake.
Kampeni yake imefungua kesi katika majimbo mbalimbali mapema Ijumaa, wakati Biden alipokuwa akikaribia kunyakua ushindi, alisema : ''uchaguzi huu haujakwisha.''
Mchuano ulikuwa ukiendelea huku idadi ya maambukizi ya virusi vya corona na vifo vikiongezeka, huku Rais Trump akisema kuwa kwa Biden madarakani kutasababisha watu kubaki majumbani hali itakayosababisha uchumi kudorora.
Biden amemshutumu Trump kushindwa kuchukua hatua madhubuti kudhibiti kuenea kwa ugonjwa wa Covid-19.
Joe Biden sasa anajiandaa kurejea Ikulu ya White House, ambako alipatumikia kwa miaka minane akiwa makamu wa rais, msaidizi wa Barack Obama. Akiwa na miaka 78, atakuwa rais mwenye umri mkuba kuwahi kutokea katika historia ya Marekani, rekodi ambayo awali ilikuwa ikishikiliwa na Trump ambaye ana miaka 74.