Dar es Salaam. Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) kwa kushirikiana na kikosi cha wanamaji wamewakamata watu saba wakiwa na dawa za kulevya aina ya heroin zaidi ya tani moja wakizisafirisha kwa kutumia jahazi katika Bahari ya Hindi eneo la Kilwa Masoko mkoani Lindi.
Waliokamatwa ambao wote si raia wa Tanzania ni nahodha wa jahazi hilo, Jan Mohammad Miranira, Amir Hussein, Yusuph Bin Hamad, Salim Bin Mohammad, Ikbal Pakir Mohammad, Jawid Nuhan Nur Mohammad na Mustaphar Nowani Kadirbaksh..
Akizungumza na Mwananchi Digital kamishna wa DCEA, Gerald Kusaya amesema raia hao wamekamatwa usiku wa kuamkia leo Jumamosi Aprili 24, 2021 eneo la Kilwa Masoko wakisafirisha dawa hizo.
Amebainisha watu hao bado wapo safarini kuletwa nchi kavu na watakapofika watahojiwa kuhusu dawa hizo, walikuwa wanakwenda wapi.