Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa akizungumza na Wafanyabiashara wa Soko Kuu la Kariakoo, leo Mei 17, 2023.
Wafanyabiashara hao wametoa malalamiko mbele ya Waziri Mkuu ambapo wameilaimu TRA kwa kutokufuata taratibu sahihi za utozaji kodi wakishirikiana na Jeshi la Polisi.
Mfanyabiashara mmoja akitoa malalamiko yake amesema kampuni yake imewahi kusumbuliwa na Askari wa Kituo cha Kamata akidaiwa kutokuwa na risiti halali za mizigo yake, jambo ambalo sio la kweli. Pia, amemtaja kwa jina moja Askari anayehusika na kashfa nyingi za hapo kuwa ni "Mpemba"
Aidha, mfanyabiashara mmoja aliyesimama kwa niaba ya wafanyabiashara wa Vitenge amemhoji Waziri Mkuu kama Serikali haitaki wanawake nchini wapendeze maana wamekuwa wanachukuliwa kama wanauza madawa ya kulevya.
Wamewalamumu pia watu wanaohusika na uzoaji wa taka kuwa wanadai pesa zisizotakiwa, kwani huenda hadi kwenye stoo zao. Pia, watu wa TRA wamekuwa wanawafata hadi majumbani wakitaka pesa. Mama huyo amehoji, "Kwa hiyo tukadange?, hapa sio mahali sahihi kwa kuongea, nitahatarisha maisha yangu. Nipe namba nije chemba tuzungumze"
Kuhusu sababu ya kufunga maduka, mfanyabiashara mmoja amesema walifanya hivyo kutokana na;
- Uwepo wa utitiri wa kodi usioendana na uhalisia
- Kuhamia kwa maduka barabarani kwa jina maarufu la machinga, watu ambao wamekuwa wanatumiwa na wafanyabiashara wakubwa hivyo kubana biashara zao (wafanyabiashara waliosajiliwa). Duniani kote hakuna machinga kwenye vituo halisi vya kibiashara
- Adhabu za makosa ya kutolipa kodi zisizolipika sababu ya ukali wake hivyo kuweka mianya ya rushwa