LICHA ya kuwapo mchakato wa kuondoa mpasuko wa Muungano unaofukuta, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), imesema suala la mafuta na gesi asilia halikuwepo katika orodha ya mkataba wa Muungano uliosainiwa na viongozi na waasisi wawili wa mataifa mawili Zanzibar na Tanganyika.
Akitoa tamko hilo lililochukua muda wa zaidi ya saa moja mbele ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi jana, Waziri wa Maji, Ujenzi, Nishati na Ardhi, Mansoor Yussuf Himid alisema SMZ inataka kuondolewa kwa suala la mafuta na gesi asilia kwenye orodha ya mambo ya Muungano kwa sababu haliwanufaishi Wazanzibari na pia suala hilo halikuwemo kwenye mkataba wa Muungano mwaka 1964.
Alisema suala la mafuta na gesi asilia kuwemo kwenye mambo ya Muungano ni ukiukwaji mkubwa wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ile ya Zanzibar ambazo zinapaswa kuheshimiwa.
"Mheshimiwa Spika, na waheshimiwa wajumbe wa baraza hili, sheria iliyoanzisha TPDC, na ile ya utafutaji na uchimbaji wa mafuta haikuridhiwa na Baraza la Wawakilishi na hivyo kukosa uhalali wa kuwa suala la Muungano," alisema Waziri Himid.
Akiyataja mambo 11 ya Muungano Himid alisema suala hilo pia halikutajwa hata katika mkataba wa Muungano wenye mambo 11 ambayo aliyataja moja moja mbele ya wajumbe.
Waziri huyo alisema kwamba, TPDC limeundwa kwa mujibu wa amri ya Rais mwaka 1969 na kuundwa tena kwa mujibu wa sheria ya mashirika ya umma 1980, lakini sheria hiyo, haikuridhiwa na Baraza la Wawakilishi na hivyo ni batili linalokosa uhalali wa kuwa chombo cha Muungano.
Waziri Himid alisema Zanzibar na Tanganyika ni nchi mbili ambazo zimeanzisha Muungano wa kisiasa na kila nchi kubaki na utawala wake isipokuwa mambo maalumu yaliyoainishwa katika makubaliano ya mwanzo ya Muungano na ndio maana katiba ya Zanzibar sura ya pili inaeleza malengo na maamuru muhimu ya sera ya SMZ kudhibiti uchumi wa nchi yake, hivyo sio busara kuanza kuingiza suala la mafuta katika orodha ya Muungano.
Hata hivyo, Waziri huyo aliwaambia wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kwamba serikali ilimpa kazi mshauri mwelekezi, lakini ushauri uliotolewa na mshauri mwelekezi huyo umesheheni upotoshaji mkubwa kwani badala ya kutatua tatizo hilo, yeye amejiegemeza kutaka suala hilo kubakia kwenye mambo ya Muungano kinyume na matakwa ya Wazanzibari.
Alisema endapo ushauri alioutoa Mshauri Mwelekezi utatekelezwa, basi Zanzibar itaishia kwenye mgongano wa Kikatiba na kero mama ya Muungano kuendelea kuwaumiza Wazanzibari na kusisitiza ni muhimu kuondolewa na kusimamiwa na SMZ suala hilo.
Waziri huyo alitaja mapendekezo matatu ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa Baraza la Wawakilishi kuwa, Ardhi na bahari ya ndani ya Zanzibar, maeneo ambayo kwa mujibu wa katiba ya Zanzibar sura ya kwanza 2 (1) ni milki ya Zanzibar, katika maeneo hayo usimamizi, udhibiti na uendeshaji wa shughuli zote za utafiti na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia uwe wa Zanzibar pekee na sio sehemu nyingine kwa kuwa hata Tanzania Bara wana mali asili zake kama vile almasi, dhahabu na mambo mengine ambayo Zanzibar hainufaiki navyo.
Pendekezo la pili ni kuwa, sasa wakati umefika kwa Zanzibar kuwa na chombo chake cha kusimamia mambo yote yanayohusiana na utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia na mengineyo yanayoendana na hayo , chombo hicho kitakuwa sawa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC).
"Hii ni njia pekee ya kuondosha migongano ya madaraka na masilahi na pia ni njia pekee ya kuhakikisha haki za Zanzibar na watu wake zinalindwa kwa sasa na baadaye kwani Zanzibar haina cha zaidi ya rasilimali zake," alisema Himid.
Pendekezo la tatu ni kwamba kwa upande wa bahari kuu (EEZ), Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, inashauri kukubali ushirikiano na Serikali ya Jamhuri ya Muungano kwa eneo hilo pekee kwa makubaliano maalumu na sio muundo wa sasa wa Taasisi na sheria kwamba Zanzibar itakuwa ni mshiriki sawa.
Katika ripoti yake, Mshauri Mwelekezi anapendekeza kuundwa kwa wizara itakayoshughulikia mafuta chini ya Jamhuri ya Muungano, kuundwa upya kwa TPDC ili iwe yenye sura ya Muungano na kusisitiza vyombo hivyo kuwa ndiyo viwe vyenye mamlaka ya kusajili makampuni yote jambo ambalo halikuridhiwa na SMZ.
Waziri Himid alisema suala la kuundwa kwa Taasisi hizo mbili likikubalika, Zanzibar itakosa mapato yote yatokanayo na usajili wa makampuni hayo na uchimbaji wa mafuta, pia SMZ itakosa mapato ya leseni pamoja na Renewal ya leseni hizo kila mwaka kama ilivyo hivi sasa.
Waziri huyo alisema licha ya gesi kuchimbwa na kuuzwa, lakini SMZ haijapata mapato ya aina yoyote licha ya kuwa kwa sasa ni jambo la Muungano,"rasilimali ya mafuta na gesi asilia inatokana na ardhi, kinachoshangaza ni kuona Tanzania Bara ina mali asili nyingi zinazotokana na ardhi ambazo hazijaingizwa katika orodha ya Muungano.
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ilitafuta Mshauri Mwelekezi kwa ajili ya kupata mgawanyo mzuri wa rasilimali za mafuta na gesi asilia itakayozalishwa nchini.
Kampuni ya AUPEC ya Uingereza ndiyo iliyoshinda zabuni na kupewa kazi hiyo chini ya Mtaalamu wake, David Reading kutoka Scotland ambaye katika ripoti yake alishauri mafuta na gesi asilia kuendelea kubaki kwenye orodha ya Muungano ripoti ambayo iliyobezwa na kutiwa kasoro nyingi na SMZ.
Ripoti ya Mshauri Mwelekezi huyo iliwasilishwa mbele ya Baraza la Mawaziri (Baraza la Mapinduzi) na kujadiliwa na hatimaye kutolewa mapendekezo ambayo ndio yaliyowasilishwa mbele ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na kutolewa maamuzi.
Kwa mara ya mwisho wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wa pande mbili kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Wananchi (CUF), waliungana na kutoa tamko la kuishauri serikali kutokubali suala la mafuta na gesi kuwemo katika orodha ya Muungano kwa kuwa hati halisi ya mambo 11 ya Muungano suala hilo halikuwemo.
Awali, Mshauri Mwelekezi alisema kwamba mafuta yaliyopo katika visiwa vya Zanzibar ni kidogo na huenda yakawa sio ya kibiashara kama inavyotarajiwa na wajumbe hao lakini kauli hiyo ya Mshauri ilionekana kuwapandisha hasira wajumbe hao na kusema hata kama mafuta yatakayoonekana yatakuwa sawa na kichupa cha pombe 'kinibu' basi yabaki kama ni rasilimali ya Wazanzibari na vizazi vyao hata kama ni ya kujipaka, lakini yasiingizwe katika orodha ya Muungano.
Awali, akitoa tahadhari, Waziri Kiongozi, Shamsi Vuai Nahodha kabla ya kuwasilishwa kwa tamko hilo la serikali aliwakumbusha wajumbe wa baraza hilo kutoa maoni yao kwa uwazi na bila ya kutumia jazba za kisiasa ili maoni hayo yaweze kuwanufaisha Wazanzibari wote juu ya rasilimali zake.
From mwananchi 4/4/2009