WAKALA WA SIRI SEASONAL 2.
Mtunzi; Robert Heriel
0693322300
ILIPOISHIA
Ndani kulikuwa na vumbi licha ya kuwa jumba lilikuwa limefungwa kwa vioo. Harufu ya uvundo kwa mbali ilizichezea pua yake, upesi akaenda kufungua mapazia na madirisha kuruhusu hewa iingie. Akaingia ndani kabisa kulipo na maktaba ya ile nyumba, akachukua kijarida kimoja chenye picha ya mtu aliyeshika ndoo ya maji pamoja na brashi. Akatoa simu akabinya binya kisha akaweka namba sikioni.
“ Hallo! Mr. Zaburi hapa, naomba mje hapa Mbezi Magari Saba kunifanyia usafi, msichelewe. Nashukuru” Sajenti akaongea na simu kisha akakata. Baada ya dakika thelasini, kampuni ya usafi ya TCS Iliwasili ikiwa na vijana wawili na mabinti wawili.Sajneti aliwapa maelekezo kisha akatoka kwenda kula kwani tayari ilikuwa imefika saa sita mchana, njaa ilikuwa imembana kwani tangu jana alikuwa hajatia kitu mdomoni..
SEASON 2 >>> EPISODE 01
“Hii simu ya Meja Venance Kagoda lazima iwe na mambo makubwa ya siri, inaweza ikawa msaada mkubwa kwangu. Lakini kwa nini Meja Venance auawe, kama hiyo haitoshi familia yake mpaka sasa haijulikani mahali ilipo, hakuna anayejua wako hai au wamekufa. Waliomuua ni kina nani; Baada ya mwili wake kuchukuliwa kwa ajili ya uchunguzi na kupelekwa katika maabara ya Boreti ukaibiwa, Who did this?” Fernanda akawaza huku akitoka katika nyumba za Meja Venance akiwa ameibeba ile simu janja aliyoikuta sirini, chumbani kwa Meja Venance. Akapanda ukutani kama mjusi, akatoa kichwa akachungulia nje kukagua usalama wa eneo la nje. Hali ilikuwa ni tulivu, giza na mwanga hafifu wa taa za nyumba za eneo lile zilimfanya Fernanda awe macho, hakuyaamini kabisa mazingira yale. Upande wa kulia aliliona gari lake alilokuwa ameliegesha, akatazama kwa kitambo akiwa bado amening’inia juu ya ukuta; akaona hali ni shwari. Akaruka kwa nje. Akasonga kulifuata gari akiwa mkononi kaishika bastola vizuri. Kila alipopiga hatua tano aligeuka huku na huku kuangalia usalama mpaka alipolikaribia gari lake. Akasimama, akaangalia alipotoka kisha akaangalia saa yake ya mkononi iliyomuonyesha ilikuwa saa saba za usiku. Fernanda hakutaka kupoteza muda akabonyeza rimoti ya gari, mlango ukafunguka akatoma ndani. Akaitoa ile simu janja, kisha akajaribu kuiwasha lakini ikagoma kuwaka,
“ Itakuwa haina chaji, nikifika nyumbani, nitaichaji kisha niikague, mbona akili yangu inanituma kuwa ndani ya simu hii kuna mambo mazito ya siri. Nafikiri itakuwa hivyo, maana hata ilipofichwa lazima itakuwa na jambo zito la siri.” Fernanda akajiwazia huku akiirudisha simu mfukoni. Alafu akawasha gari lakini kabla hajaweka gia alishtushwa na kitu kigumu kikigusa kisogo chake, na kabla akili yake haijampa cha kufanya, sauti nzito isiyomzaha ikasema;
“ Tulia hivyo hivyo, usijitingishe wala kufanya jambo lolote, nisije nikapasua bichwa lako” Yule mtu akaongea kisha akameza mate alafu akaendelea;
“Weka mikono yako juu…..”
“ Wewe ni nani, unashida gani na mimi??” Fernanda akamkatisha huku akiweka mikono yake juu.
“ Kaa kimya! Ukithubutu kufungua mdomo wako nitakichangua kichwa chako. Fuata maelekezo” Yule mtu akasema, sauti yake ilikuwa ikitokea nyuma ya kisogo cha Fernanda, ilikuwa sauti iliyomfanya Fernanda achore picha ya mwanaume jeuri mwenye sura ya kikatili, ilikuwa sauti nzito na mbaya. Fernanda akakaa kimya akisubiri maelekezo, kitambo kidogo kilipita pakiwa kimya hali iliyomfanya Fernanda atake kugeuka nyuma ili amuangalie mtu Yule. Alipogeuka bahati haikuwa yake, akakutana na kitu kizito kilichompiga usoni, Fernanda akaanguka na kupoteza Fahamu.
****************************************************************
Taa zilikuwa zikiwaka katika ghorofa ya nane katika jengo hili. Lilikuwa jengo refu la ghorofa zisizopungua kumi na tano. Pamoja na kuwa ilikuwa usiku wa manane lakini ndani ya jengo hili kulikuwa na kikao kizito kilichokuwa kinaendelea. Watu kumi walikuwa wamekaa kwenye meza yenye muundo wa Herufi U “U-Shape Style” Wote walikuwa wamevaa suti maridadi zilizokuwa zimewakaa vyema. Kiongozi wa kikao hiki cha siri alikuwa amekaa amevaa suti ya kijani uso wake ukiwa nyumba ya miwani ya macho.
“ Mipango yetu imesimama, kila mmoja wetu anafahamu sababu ya kusimama kwake, inaweza kuwa ni uzembe wa baadhi yetu humu, kama sivyo, leo hii tungekuwa tumeshafika mbali. Inashangaza kuona mpaka muda huu tumedorora, tupo katika mdororo, tangu kiungo wetu muhimu auawe na hasimu wetu mambo yetu yamesimama kama sio kurudi nyuma, tulifanikiwa kuiba mwili wake katika maabara ile, najaribu kufikiria kama tusingemuwekea IN-BODY GPS iliyotusaidia kutoa taarifa ya mwili wa Meja Venance Kagoda ulipo, tungepata kazi ngumu na yaziada kujua ulipo mwili wa ndugu yetu. Kazi hii aliifanya Adele kwa weledi mkubwa kabisa” Yule mtu akasema kisha akameza funda la mate, akamgeukia mwanadada mmoja aliyevalia suti ya kijibu iliyomkaa vyema.
“ Adele! Nichukue nafasi hii kukupongeza kwa kazi nzuri uliyoifanya kwa weledi wa hali ya juu. Hakika tunajivunia kuwa na wewe, nafikiri wote tuliiona video iliyoletwa na Dr. Binamungu iliyoonyesha kazi kubwa aliyoifanya Adele, ilikuwa ni kazi nzuri sana. Dr. Binamungu kama mtakumbuka siku ile alituambia kuwa siku waliyokaa kikao kujadili tukio la kuibiwa mwili wa Meja Venance, karibu watu wote waliokuwa kwenye hicho kikao walisema kuwa aliyefanya tukio hili alikuwa mwanaume….” Yule mtu alikatishwa na vicheko vya wanakikao wengine, naye akaungana nao kucheka. Kisha akaendelea.
“These people are so stupid, I can't understand their ignorance is endless or what it is, kumuita Adele ni mwanaume wakati ni mwanamke mrembo kuna maana mbili ambazo ni; mosi, hawana elimu ya ujasusi katika utambuzi wa miondoko na utendaji wa wahusika katika matukio ya uhalifu; pili, walikuwa wamejawa na hofu au kuchanganyikiwa kwa kile kilichotokea” Yule mtu akameza mateka kisha akaendelea;
“ Natoa zawadi ya Milioni hamsini kwa Adele, kisha kila mtu humu atapatiwa milioni ishirini kama sehemu ya kujipongeza kwa kuuokoa mwili wa kiungo wetu, Meja Venance” Yule mtu akasema kisha sauti za makofi yakikijaza chumba kile.
“Naomba tutulia tafadhali, hatuna muda wa kutosha” Yule mtu akasema akijaribu kuwatuliza wanakikao.
“ Nimewaiteni hapa kuwajulisha kuwa kikao chetu kilikuwa na agenda kuu mbili ambayo ya kwanza nimeshawaeleza, kuhusu mdororo unaoendelea katika mpango wetu, lakini jambo la pili ni kueleza kuhusu hali inavyoendelea katika utafutaji wa chipu ambayo kwa taarifa za kiungo wetu anasema chipu hiyo ipo mikononi mwa kijana mmoja aitwaye Sajenti Jacob Warioba…..” Yule Mtu akasema lakini akakatishwa na Adele.
“ Sajenti Warioba?” Adele akabwatuka kwa sauti jambo lililowafanya wanakikao wamtazame kwa mshangao.
“ Unamfahamu?” Yule mtu akauliza.
“ Sajenti….! Kama ni yeye basi tuna kazi ya kufanya” Adele akasema wenzake wakimtazama. Kisha akaendelea.
“ Sajenti ndiye alinifanya nifungwe kwa miaka miwili kabla hamjaja kunitoa, kijana huyu ni hatari, nimeshtuka kusikia jina lake mahali hapa” Adele akasema akiwa amehamanika.
“ Unataka kuniambia ndiye Yule aliyefanya uchunguzi wa kifo cha Ramla na walioharibu harusi ya Ismaiya na Robert?” Yule Mtu akauliza.
“ Sina uhakika kama ndiye, lakini majina yake ni hayohayo”
“ Huyu si ndiye aliyepambana na kundi letu la Ambagon kule Mogadishu, Somalia? Si ndiye huyuhuyu aliyeleta fujo katika meli yetu ya ambagoni na kuua watu wetu? Kama ndiye naapa he must pay, he will regret getting into the crocodile's mouth” Yule mtu akasema huku sauti yake ikiwa imebadilika kwa kiasi kikubwa, ilikuwa sio ile sauti ya mwanzo, aliongea kwa hasira midomo ikitetemeka.
“ Huyu mbwa wakati huu hatanikimbia, alinikatili katika mipango yangu ya kumuua Ismaiya wakati ule, akasababisha nikafungwa na kusota jela nikila maharage na kuishi maisha kama panya buku. Sajenti I swear by the name of the world, I will teach you. Nitakapokukamata nitakuua kifo kibaya ambacho tangu dunia iwepo hakuna aliyeonja uchungu wake” Adele alikuwa akiwaza.
“ Taarifa tulizonazo ni kuwa, Sajenti kwa sasa hana makazi maalumu na haifahamiki anaishi wapi, hiyo haitatuzuia kumtia mikononi mwetu. Tunakila nyenzo zitakazotusaidia kumkamata mtu huyu. Hana uwezo wa kutukimbia, wengi waliofanya kama yeye walijileta wenyewe pasipo kujua” Yule mtu akasema kisha akamtazama Adele;
“ Adele tupo pamoja? Maana naona upo mbali kimawazo”
“ Ndio Mkuu tupo Pamoja” Adele akasema wakati huu akiwa makini kumsikiliza Yule Mtu.
“ Tutamkamata Sajenti kwa sababu kuu mbili; yakwanza ni kuhusu suala la chipu, hili ndilo la muhimu kwa sasa, alafu lapili ni kulipa kisasi cha aliyotufanyia, kwa kweli hatuwezi kumsamehe kwa aliyotufanyia huyu Panya. Niwaombe jambo moja, hakikisheni Sajenti anakamatwa mzima mzima akiwa hai, sitaki aletwe hapa akiwa amekufa, kwani kwa akiwa hai ndio itakuwa nafasi yetu ya muhimu kutimiza mipango yetu” Yule Mtu akiwa anaongea mara simu yake iliyokuwa mezani ikaita, jambo lililowafanya wote waitazame na kimya kidogo kitawale. Yule mtu akaichukua simu yake akapokea na kuiweka sikioni.
“ Hallo! Kweli! Upo wapi! Sawa nakuja sasa hivi” Yule mtu akasema akiongea na mtu wa upande wa pili simuni, kisha simu ikakatika.
“ Samahani nimepata dharura hapa, simu hii imetoka kwa moja ya viungo wetu waliopo maeneo mbalimbali hapa jijini, mambo yanazidi kunyooka, nafikiri niwaache muendelee na kikao mimi nikakutane na kiungo wetu huyu ili mambo haya yasilale. Mr. Gombe utaendelea kuendesha kikao hiki alafu utanipa maazimio” Yule mtu akasema kisha akatoka akiwaacha wenzake wakitamani kujua anaenda wapi.
ITAENDELEA.
Kitabu hiki kinamahusiano makubwa na Kitabu cha " MLIO WA RISASI HARUSINI" ambacho tayari kipo sokoni.
Jipatie Hardcopy kwa bei ya Ofa Tsh 10,000/= Ikatayodumu mpaka tar 14/10/2021
OFA hii isikupite!
MLIO WA RISASI HARUSINI
Kitauzwa Kwa Tsh 10,000 badala ya Tsh 15,000.
Mwisho WA OFA ni tarehe 14/10/2021
TUMA PESA KWA NAMBA
0693322300
Airtelmoney
Robert Heriel