Simulizi: Harakati za Jason Sizya

Simulizi: Harakati za Jason Sizya

ufukweni mombasa.JPG

255

Damu isiyo na hatia…




Saa 6:05 mchana…

MARA tu Leyla alipoondoka akanipa nafasi ya kujiandaa, nilichukua begi langu kisha nikawa katika harakati za kuchagua vitu vichache vya kuondoka navyo. Lakini zoezi la kuchagua kipi nichukue na kipi niache likaonesha kunipa changamoto sana. Ilinichukua takriban dakika tatu nikiwa nimesimama tu nikivitazama vitu vyangu pasipo kuamua kipi niondoke nacho. Wakati huo huo pia nilikuwa najiuliza nikitoka hapo Serena Beach Resort nielekee wapi!

Mara likanijia wazo kwamba nimpigie kwanza Leyla simu ili anishauri ni wapi niende lakini papo hapo nikajikuta nikilifuta wazo hilo, sikujua kwa nini lakini hisia zangu ziliniambia kuwa nilipaswa kujifanyia mambo yangu mwenyewe pasipo kumshirikisha Leyla hata kama alikuwa mtu wangu wa karibu na nilimwamini. Na kama alitakiwa kujua basi ningemfahamisha baada ya kukamilisha mambo yangu na si kabla.

Wakati nikiendelea kutafakari hayo hisia zikanituma nimtafute Merina, yule binti wa mapokezi aliyenipokea siku iliyokuwa imetangulia wakati nafika hapo Serena Beach Resort. Bila kufikiria mara mbili nikachukua simu yangu na kuzipiga namba alizonipa, nilikuwa bado nazikumbuka kichwani, na muda mfupi uliofuata simu ile ilikuwa hewani ikiita.

“Hello, nani mwenzangu?” sauti ya kike upande wa pili iliniuliza kwa wasiwasi baada ya kupokea simu ile. Moja kwa moja niliifahamu sauti ile kuwa ni ya Merina.

“Naitwa Jason Sizya…” nilijitambulisha kwa sauti tulivu. Hata hivyo moyo wangu ulikuwa unanienda mbio, sikujua kwa nini hali ile ilikuwa inanitokea. “Habari za toka jana, Merina?”

“Oh! Jason, mimi ni mzima wa afya. Habari za huko?” Merina alisema kwa furaha baada ya kugundua ni mimi niliyepiga simu.

“Mimi pia sijambo, nilikuwa nabahatisha tu kukupigia nilidhani pengine
umenipa namba za gari!” nilisema kwa utani kisha nikaangua kicheko hafifu.

“Siwezi kufanya hivyo. Kama sikutaka kukupa namba yangu ningekwambia tu badala ya kukufanyia uhuni…” Merina alisema kisha akaongeza, “Vipi uko wapi?”

“Hapa hapa chumbani kwangu namba 204 Serena Beach Resort uliponiacha, lakini ndiyo najiandaa kutoka muda si mrefu. Naweza kukuona?” nilimuuliza Merina huku nikibana pumzi zangu kusubiria jibu lake.

“Hakuna shaka, njoo nipo nyumbani!” Merina alinijibu.

“Namwogopa shemeji,” nilisema huku nikipitisha ulimi wangu kuilamba midomo yangu iliyokauka.

“Sasa… mbona jana ulizungumzia kuhusu kunitembelea nyumbani!” Merina aliuliza kwa mshangao. “Hukujua kama kuna shemeji yako?”

“Lakini… ni wewe uliyeniambia kuna mbwa mkali, au sivyo?” nilimkumbusha. Na hapo nikamsikia akiangua kicheko hafifu. Kisha kikatokea kitambo kifupi cha ukimya.

So?” nilimtupia swali baada ya kuona yuko kimya.

“Kama unaweza njoo na kama una mambo mengine ya kufanya basi karibu siku nyingine kama n’takuwepo nyumbani,” Merina aliniambia.

“Nakuja sasa hivi kwani nahitaji sana kupata mwenyeji wa kwenda kuspendi naye jioni ya leo ili nipate akili mpya,” nilimwambia Merina na hapo nikamsikia akishusha pumzi. “Ulisema nyumbani kwako ni Utange barabara ya Old Malindi karibu na Kanisa la Agape Fellowship Center, sivyo?

“Ndiyo… halafu… hivi nilikwambia Utange?” Merina alisema kwa mshangao kisha akaongeza, “Eneo ninaloishi ni Shanzu si Utange. We chukua teksi mwambie dereva akulete Old Malindi Road, Kanisa la Agape Fellowship Center – Shanzu, na ukifika hapo unijulishe.”

Okay!” nilisema na kushusha pumzi. Kisha kabla simu haijakatwa nikakumbuka jambo muhimu sana. Nikamwita, “Merina!”

“Abee!” Merina aliitika.

“Hakikisha hakuna mtu mwingine anayefahamu kama nimeongea na wewe wala kujua kama nakuja kwako,” nilimwambia kwa namna ya kumtahadharisha.

“Ondoa shaka,” Merina aliniambia kisha nikaisikia ile simu ikikatwa upande wa pili hata kabla sijaongeza neno jingine.

Baada ya kuirudisha simu yangu mfukoni nikawa nimepata wazo kwamba nisichukue nguo yoyote bali nichukue vitu muhimu tu kama Ipad, bastola, hati yangu ya kusafiria, kitambulisho na kadi ya benki. Kwa kuwa nilikuwa na fedha za kutosha nilipanga kwenda kununua nguo mbili tatu za kubadili mbele ya safari. Nikiwa nimeridhika na vitu nilivyochukua nikafungua mlango wa chumba changu na kutoka. Nikazifuata ngazi na kushuka haraka haraka.

Nilipofika sehemu ya chini ya hoteli ile nilielekea sehemu ya
mapokezi ambako niliacha ile kadi iliyotumika kufungulia mlango wa chumba changu kwa mhudumu niliyemkuta, kisha nikatoka nje ya hoteli huku nikiwa makini sana kuhakikisha usalama wangu.

Nilisimama pale kwenye varanda ndefu nikiyatembeza macho yangu kuwachunguza watu na hata magari yaliyokuwa yameegeshwa kwenye viunga vya maegesho ya magari pale hotelini, wakati huo nilikuwa najiuliza nitumie usafiri upi kuondoka eneo lile maana kila gari nililoliona limeegeshwa pale sikuwa naliamini. Muda huo huo nikaiona teksi moja ikiingia hapo hotelini na kuwashusha watu wawili ambao kwa mtazamo wa haraka tu nilibaini kuwa walikuwa wanandoa waliotoka kuoana na sasa walikuja hapo kwa ajili ya fungate.

Akili ya haraka ikanituma kuwa ile teksi ingenifaa sana, nikaifuata haraka kabla haijaondoka na kufungua mlango wa nyuma wa ile teksi kisha nikaingia haraka, nikaketi huku nikimtaka dereva anipeleke Benki ya KCB Tawi la Nyali. Dereva wa teksi ile, mwanaume mtu mzima aliyekuwa amepambwa na mvi kadha kwa kadha kichwani kwake, aliiondoa teksi yake pasipo kuhoji kitu.

Niliamua kuchukua tahadhari zote kwa kutotaka kwenda moja kwa moja nyumbani kwa Merina kwani sasa akili yangu ilikuwa imeanza kufanya kazi niliyopaswa kuifanya tangu nijiunge na harakati hizi za kijasusi. Kazi iliyonitaka muda wote niwe macho huku nikiyachunguza magari au watu ninaoongozana nao pale ninapokuwa kwenye safari zangu.

Toka katika kiti kile cha nyuma nilichoketi nilikizungusha kichwa changu taratibu kutazama nyuma ili kuona kama kulikuwa na chochote cha kukitilia shaka, sikuona kitu chochote cha kutishia usalama wangu.

Wakati huo tulikuwa tunaingia katika barabara ya Serena na kuyavuka majengo ya Sonia Hotels & Apartments, Safari Inn Bar & Restaurant, na Kenya Migros Shop. Dereva alikata na kuingia upande wa kushoto na baada ya kitambo kifupi cha safari tukaipita Serena Mini. Teksi hii ilikuwa ikiendeshwa kwa mwendo wa kistaarabu.

Ndani ya gari kulikuwa kimya kabisa. Muda wote nilikuwa natazama nje ya dirisha lililokuwa limezibwa na kioo. Mbali na muungurumo wa gari uliosikika, kingine ambacho ungeweza kusikia ni sauti ya redio. Redio hii ilikuwa inaimba nyimbo za zamani zilizopigwa na bend za Le Mangelepa, Les Wanyika, Super Mazembe na nyimbo nyingine za miaka ya nyuma kipindi ambacho muziki ukiwa muziki. Nyimbo hizi zilikuwa zinaendana na dereva wa teksi.

Dakika ishirini baadaye tukawa tumeingia Barabara ya Malindi na sasa tulikuwa tukiyakaribia majengo ya Shule ya Msingi ya Shimo la Tewa. Na hapo yule dereva wangu, kama walivyo madereva wengi wa teksi ambao huwa na hamu sana ya maongezi, alianza kuongea juu ya kila lililomjia kichwani kama siasa, uchumi, utamaduni, mapenzi, ujambazi na hata yale ambayo hayakunihusu.

Inaendelea...
 
ufukweni mombasa.JPG

256

Sikumtia moyo sana kwa jinsi ambavyo sikujiingiza katika maongezi hayo kikamilifu kama alivyotaka. Nilichofanya ilikuwa kutia kicheko au neno moja moja ili aendelee kupiga soga. Kimawazo nilikuwa mbali sana. Nilikuwa nafikiria ni vipi ningekabiliana na adui zangu katika nchi ile ya ugeni. Ni vipi ningemwingia Miriam na kumfanya afunguke kuhusu alichokuwa akikijua. Si rahisi kumwendea jasusi kama yule, ambaye alikuwa akishirikiana kwa karibu sana na magaidi kwa kulipwa mamilioni ya fedha ili avujishe siri za kiusalama.

Yaani kumkabili Miriam pasipo kujipanga kisawa sawa isingetofautiana sana na kutia kichwa changu katika domo la mamba mwenye njaa. Hata hivyo, kwa kuwa haikuwepo njia nyingine, kazi yangu ilikuwa kumfanya azungumze. Hilo ndilo lililonifanya nimtafute kwanza Merina ambaye niliamini angenisaidia kupata maficho yasiyoweza kushtukiwa kwa urahisi, kama ambavyo roho yangu ilinituma.

Nilikuwa na uhakika kuwa kumkabili Miriam ambaye kwa vyovyote alishachukua tahadhari zote ingekuwa rahisi kama kwenda kumwona Mchungaji wangu lakini baada ya hapo nini kingetokea? Hilo ni jambo lililonisumbua.

Gari liliendelea kukata mitaa, likiyavuka majengo ya White Cliff Villa na baada ya mwendo wa dakika kadhaa tukaanza kuyavuka majengo ya makazi ya watu, ofisi na migahawa mbalimbali na kisha Kanisa la AIC. Na hapo nikakumbuka tena wajibu wangu na kuzungusha kichwa changu taratibu kutazama nyuma bila kumshtua dereva na hapo mwili wangu ukajikuta ukiingiwa na ubaridi wa ghafla. Nililiona gari aina ya Jeep jeusi lenye vioo vyeusi visivyomwonesha aliyemo ndani likiwa nyuma yetu kiasi cha umbali wa mita therathini hivi.

Muda huo tulikuwa tukiyapita majengo ya City Mall na CTM Mombasa, Nakumatt Nyali Shopping Center na Naivas Supermarket. Nilikumbuka kuliona lile gari aina ya Jeep likiwa limeegeshwa kwenye maegesho ya magari pale Serena Beach Resort wakati tukiondoka, na sasa lilikuwa nyuma yetu. Niligeuka kumtazama dereva wangu kwa udadisi na kugundua kuwa alikuwa hafahamu chochote kilichokuwa kikiendelea. Dereva aliendelea kupiga stori. Nikageuka tena kutazama kule nyuma.

Moyo wangu ulikuwa kama uliosimama ghafla kabla ya kurudia mapigo yake na kuanza kwenda mbio huku jasho jepesi likianza kunitoka mwilini. Hata hivyo nilijiweka sawa kwa mapambano. Kilichonitia hofu ni kuwa wale watu sasa walionekana wazi kuwa walikuwa wamedhamiria kunifuatilia pasipo uficho wowote.

Niliupeleka mkono wangu kiunoni nikaigusa bastola yangu ndogo aina ya Glock 19M ambayo hutumiwa na wapelelezi wa Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI), mwili ukanisisimka. Na kabla sijajua nifanye nini dereva wangu akakatiza ghafla stori yake na kunifanya nigeuze shingo yangu kumtazama. Na hapo nikakiona kilichomfanya asite.

Mita chache mbele yetu, gari kubwa la mizigo aina ya Tata Daewoo lilikuwa likitujia kwa mwendo mkali likiwa upande wetu. Lilikuwa tukio la ghafla mno na haikuwepo nafasi hata ya kufikiria. Sikuwa na muda, bila kujiuliza mara mbili niliivuta kabali ya mlango na kuusukuma kwa nje, ukafunguka na bila kuchelewa nikajirusha nje ya gari huku nikiviringika kuelekea pembeni kabisa ya barabara.

Dakika hiyo hiyo mlio wa kutisha ukasikika wakati magari hayo yalipogongana uso kwa uso. Toka nilipoangukia niliinuka haraka huku nikiyatupa macho yangu kuyatazama magari yale yaliyogongana uso kwa uso na kuambulia kumwona dereva wa gari la mizigo aina ya Tata Daewoo lililotugonga akisaidiwa na dereva wa gari lililokuwa likitufuata nyuma aina ya Jeep ambalo lilisimama ghafla katika eneo hilo.

Yule dereva wa Tata Daewoo alikuwa amevaa suruali nyeusi ya dengrizi, sweta jekundu jepesi lililoungana na kofia na juu yake alivaa kofia pana nyeusi aina ya pama, miwani myeusi mikubwa ya jua iliyoyaficha macho yake na glavu maalumu mikononi mwake. Nilichoshuhudia ni kuona akipandishwa ndani ya gari hilo la aina ya Jeep. Na kabla sijafahamu kinachotendeka nikaliona gari lile aina ya Jeep likiondoka kwa mwendo wa risasi. Sikupata hata muda wa kusoma namba za gari hilo.

Sikutaka kuzubaa eneo lile kwani watu walishaanza kusogea, nikaokota haraka vitu vyangu kisha nikamwendea yule dereva wa teksi na kumtazama. Kichwa chake kilikuwa kimepondeka na kifua chake kilikuwa kimefumuliwa na usukani wa gari lake. Alikuwa hatazamiki, alikuwa kama nyama na mifupa iliyosagwa. Wakati watu wakijaa eneo lile na wengine kuanza kusimulia walivyoshuhudia lile tata Daewoo likiigonga teksi, mimi nilipata nafasi, nikageuka na kuondoka haraka eneo lile.

Hisia zangu ziliniambia kuwa kutoka pale ilipotokea ajali nilikuwa karibu na barabara ya Old Malindi eneo la Shanzu na hivyo nikaanza kutembea haraka kando ya ile barabara ya Malindi na kujichanganya na watu wengine, nikaelekea kule nilikodhani ndiko iliko barabara ya Old Malindi. Wakati natembea nilikuwa makini sana kumchunguza kila mtu niliyepishana naye au aliyekuwa akija nyuma yangu na wakati huo huo nikiomba kuwa nisikutane na shambulizi lingine mbele ya safari.

Mawazo mengi yalianza kupita kichwani mwangu huku nikijaribu kuunganisha nukta za mlolongo wa matukio yote yaliyojiri tangu nilipoanza safari yangu ya kumfuatilia Rahma wa Singida Jijini Dar es Salaam nchini Tanzania. Mawazo yangu hatimaye yakahamia kwa Merina huku nikijiuliza kama angekuwa mtu sahihi wa kunisaidia, na kama angeweza kuufunga mdomo wake, maana upo msemo wa Kiingereza unasema “If you want a thing broadcast tell a woman, otherwise make your mouth shut!” yaani ukitaka jambo lake lisambae basi mweleze mwanamke vinginevyo funga mdomo wako!

_____

Teksi niliyoikodi karibu na makutano ya barabara za Malindi na ile ya Old Malindi ilinishushia kwenye makutaano ya barabara za Old Malindi jirani na jengo la Fezeti Enterprises kabla ya Kanisa la Agape Fellowship Center – Shanzu. Akili yangu ilikuwa imechoka sana kutokana na misukosuko ya siku hiyo.

Nilimlipa dereva wa teksi fedha yake na kushuka kisha nikasimama kidogo kando ya ile barabara nikiyatembeza macho yangu kwa makini kuyapeleleza mandhari ya eneo lile na niliporidhika na tathmini yangu nikaanza kutembea taratibu nikirudi nyuma huku mkono wangu mmoja ukiwa ndani ya mfuko wa suruali yangu umeikamata bastola.

Muda huo ile teksi ilikuwa imeshika hamsini zake na kutokomea mbali na eneo lile. Niliinua mkono wangu kutazama majira kwenye saa yangu ya mkononi. Mara moja nikagundua kuwa ilikuwa inaelekea kutimia saa nane na nusu mchana. Nikashangaa kuona Merina hakuwa amenitafuta kwenye simu kuniuliza nilikuwa wapi kwani hadi muda huo hatukuwa tumewasiliana au kumjulisha kama bado nilikuwa na mpango wa kwenda nyumbani kwake au la. Nilipoitazama simu yangu ya mkononi nikagundua kuwa ilikuwa imejizima. Nikaiwasha huku nikiendelea kutembea taratibu.

Mara nikasikia mlio kwenye simu yangu ulioashiria kuwa ujumbe mfupi wa maandishi ulikuwa umeingia, nilipoutazama nikakuta ulikuwa unatoka kwa Merina ambaye alikuwa akilalamika kuwa kama sikuwa na mpango wa kwenda kwake ningemweleza badala ya kutotokea na kuzima simu. Muda huo huo nikaamua kumpigia simu na alipopokea nikamjulisha kuwa simu ilikuwa imejizima pasipo mimi kufahamu halafu nikamwambia kuwa nilikuwa nimefika pale kanisani.

Inaendelea...
 
ufukweni mombasa.JPG

257

Wakati nikiwa nakaribia kufika pale kanisani nikaanza kujilaumu kwa kuwa mwepesi wa kumwamini Merina kutokana na kubabaishwa na uzuri wake. Sasa nikajikuta nikiwa njia panda katika kuamua uelekeo. Upande mmoja wa nafsi yangu ulinisukuma niondoke haraka eneo lile kabla Merina hajatokea na niende sehemu nyingine kabisa na upande mwingine wa nafsi yangu ukinisukuma kuwa nimsubiri pale kanisani huku nikiwa tayari kukabiliana na kitu chochote cha hatari ambacho kingetokea.

Hata hivyo wakati nikiwa katikati ya hali ile nikashtuka kumwona msichana mrembo akinijia huku uso wake ukipambwa na tabasamu maridhawa. Macho yangu yakatia nanga kwenye umbo zuri la msichana huyo ambaye alisimama mbele yangu akinitazama kwa utulivu huku akiendelea kutabasamu. Loh! Sikutegemea kama Merina angekuwa mzuri namna ile. Kwa sekunde kadhaa nilisimama nikimtazama Merina huku macho yangu yakishindwa kuamini kama kweli msichana yule mzuri alikuwa ni yeye.

Huyu hakuwa Merina yule niliyeonana naye kule Serena Beach Resort jioni ya siku iliyokuwa imetangulia akiwa katika sare zake za kazi kwani siku hii uzuri wake ulikuwa umeongezeka maradufu na kufanikiwa kuzigaragaza hisia zangu.

Alikuwa amevaa sketi fupi nyeusi yenye miraba myeupe iliyoishia juu kidogo ya magoti yake na kuzuiwa na kiuno chake chembamba kiasi, blauzi ya pinki ya kitambaa chepesi ya mikono mirefu iliyoyahifadhi matiti yake imara madogo, na viatu vyenye vikanyagio virefu vya mchuchumio. Mkononi alikuwa amevaa bangili nyingi za pembe na alijipulizia mafuta mazuri.

Nyusi zake zilikuwa zimetindwa vizuri na kupakwa wanja, kope zake zilirembwa vizuri na kuyafanya macho yake malegevu yaonekane vizuri na kupendeza, midomo yake ilikolea rangi ya pinki na shingoni alikuwa amevaa kidani kilichopotelea kwenye uchochoro wa matiti yake mazuri.

Macho yangu yakaanza kufanya ziara kifuani kwake na hapo kupitia kivazi chake chepesi nikaziona chuchu zake laini zilivyosimama kwa utulivu juu ya vilima viwili visiyojua adha yoyote ya volkano. Wakati nikiwa katika hali ile ya mduwao Merina akavunja ukimya baada ya kuitazama saa yake ya mkononi.

“Ulipitia wapi mbona umechelewa?” Merina aliniuliza kwa utulivu huku akinitazama usoni.

“Nisamehe bure, kuna dharura ilijitokeza,” nilisema kwa sauti ya chini iliyokaribia kuwa ya kunong’ona.

“Haya, twende nyumbani,” Merina aliniambia kisha akageuka kuanza kuondoka. Nikamfuata taratibu kama kondoo aliyekuwa anapelekwa machinjioni huku ule upande mmoja wa nafsi yangu ukiendelea kunisisitiza niwe makini sana na nisimwamini mtu yeyote, hata hivyo kwa Merina nilijihisi kama mbwa mwoga mbele ya chatu mwenye njaa kali.

Tulivuka Zaituni Shop na kisha Presitige Guest House kisha tukakunja kushoto na kutokea Kwa Antie Shop, kutokea hapo hatukwenda mbali tukawa tumefika nyumbani kwa Merina, kwenye nyumba ya vyumba viwili, sebule, jiko, eneo la kulia chakula na chumba cha maliwato, akanikaribisha sebuleni.

Tulipoingia niliketi kwenye sofa huku nikiyatembeza macho yangu kuitazama ile sebule. Ilikuwa sebule nzuri iliyopambwa na seti moja ya makochi ya sofa ya kifahari yaliyopangwa katika mtindo wa kuizunguka ile sebule. Sakafuni kulikuwa na zulia maridadi la manyoya la rangi za kupendeza na katikati ya sebule ile kukiwa na meza fupi nyeusi ya kioo yenye umbo la yai.

Upande wa kushoto wa ile sebule kulikuwa na runinga pana aina ya LG iliyofungwa ukutani na chini yake kulikuwa na meza fupi nyeusi yenye sistimu ya muziki, deki ya Dvd, kisimbuzi cha DStv na vinyago viwili vilivyopangwa kwa ustadi wa hali ya juu. Pia kulikuwa na jokofu aina ya Boss kwenye kona moja jirani na eneo la kulia chakula. Kando ya ukumbi ule mdogo wa chakula kulikuwa na kishoroba ambacho bila shaka kilielekea vyumbani.

Katika kuta safi nyeupe za sebuleni kulikuwa na picha moja kubwa iliyomwonesha Merina akiwa ufukweni na kalenda kubwa. Kupitia vile vitu nilivyoviona pale sebuleni nikatambua kuwa Merina alijitahidi kuishi maisha ya daraja la kati kwa kadiri alivyoweza ingawa kwa kazi yake niliamini kuwa kipato chake kilikuwa cha chini.

“Karibu sana, Jason, hapa ndiyo nyumbani kwangu,” Merina aliniambia huku akinitazama kwa makini.

“Nashukuru kupafahamu,” nilijibu huku nikiendelea kuzungusha macho yangu kuyatazama mandhari ya kupendeza ya ile sebule. Merina alishusha pumzi za ndani kwa ndani.

“Humu ndani mnaishi watu wangapi?” nilimuuliza Merina huku macho yangu yakiwa makini kumtazama.

“Kwa nini?” Merina aliniuliza kwa mshangao huku akinikodolea macho kutokana na swali langu, kisha akajibu, “Naishi peke yangu.”

“Peke yako!” nilishangaa huku nikiendelea kupepesa macho yangu mle ndani, sauti yangu ilibeba mshangao kidogo.

“Huamini?” Merina aliniuliza huku akiachia tabasamu pana.

“Hawakuoni au ni wewe huwataki?” nilimtupia swali lingine.

“Wananiona sana ila bado sijampata yule ambaye naweza kusema ameziteka fikra zangu kiasi cha kumkabidhi moyo wangu,” Merina alisema kisha kama aliyeshtuka akaniuliza, “Kwa nini unaniuliza hivyo?”

“Usijali… ila samahani kwa kuuliza maswali kama vile nafanya sensa,” nilisema na kucheka kidogo kisha nikajiweka sawa juu ya sofa.

“Bila samahani, we uliza tu maana aulizaye ataka kujua,” Merina alinijibu.

“Basi kama bado hujampata wa kumkabidhi moyo wako itabidi umwombe sana Mungu akupatie mume mwema,” nilimwambia Merina.

“Amina!” Merina alijibu kisha akanitaka radhi na kuinuka huku akinitazama usoni, “Sijui nikuletee kinywaji gani? Ila humu ndani kuna maji, juisi ya embe na pasheni tu. Ukitaka tofauti na hapo itabidi nikanunue hapo dukani.”

“Nipatie ya embe,” nilimjibu.

Hakuongeza neno, alielekea kwenye jokofu, akafungua na kutoa jagi lililokuwa na sharubati ya embe, kisha akaliendea kabati la vyombo na kutoa bilauri moja ndefu, boksi lenye mirija na sinia dogo. Akaviweka vitu juu ya lile sinia dogo na kuja nilipokuwa nimeketi. Akaliweka lile sinia dogo juu ya meza ya kioo na kuisogeza mbele yangu. Halafu akamimina sharubati kwenye bilauri na kutoa mrija, akauweka ndani ya bilauri hiyo na kunitazama kwa tabasamu. “Karibu, mheshimiwa.”

“Nashukuru, mrembo,” nilijibu huku nami nikiachia tabasamu kabambe.

“Samahani Jason, naomba univumilie kidogo,” Merina alisema na kuondoka haraka akaelekea jikoni na baada ya takriban dakika ishirini nikamwona akiandaa meza kubwa kwa mapochopocho. Alipomaliza akanialika mezani. Tulikuwa wawili tu mezani.

Alikuwa ameandaa wali wa nazi, mchuzi mzito wa samaki ulioungwa kwa nazi pia, bakuli la mboga za majani pembeni, na vipande vya matunda aina ya nanasi, ndizi, embe, na tikiti maji lililokoza wekundu kwenye sinia. Kando yake jagi la maji baridi na bilauri mbili.

“Karibu. Jisikie uko nyumbani,” Merina aliniambia na kunikabidhi kijiko cha kupakulia.

Sikuwa na sababu ya kujivunga kwa kuwa niliamini hicho kiliandaliwa kwa ajili yangu. Nikajipakulia mlima wa sahani kisha nikakumbuka kusali kimoyomoyo nikikibariki chakula. Tukaanza kula kimya kimya kila mmoja akitafakari lake.

Inaendelea...
 
ufukweni mombasa.JPG

258

Pamoja na mawazo kuniandama lakini chakula kilishuka vilivyo kutokana na ustadi wa mapishi. Muda mwingi Merina alionekana kunitazama lakini nilikuwa mbali kimawazo. Nilikuwa namfikiria dereva wa teksi iliyonibeba kutoka Serena Beach Resort.

Niliamini kuwa kifo chake ulikuwa ni mwanzo tu wa mlolongo wa matukio ya damu kumwagika kwa ajili yangu. Kama ningekuwa naandika kitabu basi damu ya yule dereva wa teksi ingekuwa ni dibaji. Na hivyo ilikuwa lazima damu hii ilipizwe. Bei ya damu ni damu, na yeyote aliyesababisha kumwagika kwa damu hiyo nilimhitaji kwa udi na uvumba na nisingejisamehe kumwacha mtu huyo aendelee kusheherekea hewa safi ya dunia baada ya kumwaga damu ya dereva asiye na hatia.

Ni watu wangapi wangeendelea kupoteza maisha yao katika sakata hilo kabla sijaupata ukweli? Je, ningeendelea kuwa mtu wa kujificha na kuketi kizembezembe hadi lini nikiwatazama watu wanavyouawa kinyama kwa ajili yangu? Lini ningejibu shambulio?

Ukweli kifo cha yule dereva wa teksi kilinitia uchungu mkali moyoni, na mara nikajikuta nikiwaza kile ambacho sikupenda kukiwaza, kwamba kama nisingeruka na mimi muda huo ningekuwa maiti! Halafu…? Likanijia wazo jingine kuwa pengine yule mwuaji alikusudia kunitisha, kwa nini asitumie risasi kunimaliza pale chini nilipoanguka baada ya kunusurika? Nini kilimfanya aondoke haraka eneo lile? Maswali hayo yalizidi kuniongezea kiu ya kutaka kufahamu nini kilikuwa nyuma ya pazia.

Tulimaliza kula kisha tukashushia na matunda halafu maji baridi. Tukarudi kwenye sofa huku kila mmoja akiwa na kimbaka mdomoni kuondoa masalio ya chakula kwenye meno. Sikuacha kumsifia Merina kwa mapishi. Tukiwa pale kwenye sofa nikakumbuka wajibu wangu na kuanza kumsaili Merina.

“Hivi, Merina, una muda gani pale Serena Beach Resort?” nilimuuliza kwa sauti tulivu.

“Miaka miwili,” Merina alijibu.

“Unapaonaje?” nilimsaili tena huku nikimtazama kwa tuo usoni.

“Kupaonaje kivipi?” Merina aliniuliza huku akishindwa kuuficha mshangao wake.

“Panalipa, au unafanya tu kazi kwa sababu huna mahali pengine pa kwenda kufanya kazi?” niliendelea kumuuliza.

“Panalipa,” Merina alisema kwa kifupi na kushusha pumzi.

“Wanalipa vizuri?” nilimuuliza tena na hapo nikamwona akiangua kicheko hafifu.

“Vipi kwani, unataka kuniondoa hapo uniajiri nini?” Merina alisema huku akicheka.

“Yote yanawezekana,” nilisema huku nami nikicheka kidogo.

“Si mbaya, mshahara wao unanisaidia kwa namna fulani lakini uwepo wangu pale unanipa connection zinazonisaidia kama hivi unavyoona!” Merina alisema huku akinionesha pale sebuleni.

Connection kama zipi?” nilimuuliza na hapo nikamwona akisita kidogo kisha akanitazama usoni kwa umakini zaidi. Nikabadili swali, “Nani mmiliki wa hoteli hiyo?”

“Mmiliki simfahamu ila najua asilimia 45 inamilikiwa na Aga Khan Fund for Economic Development,” Merina alisema.

“Samahani lakini… kuna wageni wawili jana nimewakuta hapo hotelini, mmoja mwanamume wa Kisomali anaitwa Abshir na mwingine mdada wa Kiarabu anaitwa Rahma, unaweza kuwa unawafahamu?”

“Ab-shi-r… Ra-h-ma…” alisema kama aliyejaribu kukumbuka jambo halafu akatingisha kichwa chache kukataa huku uso wake ukionesha shaka fulani. “Hapana, siwafahamu na wala sikumbuki kusikia majina kama hayo pale hotelini.”

“Yule Msomali mrefu ambaye jana tulipishana pale orofa ya pili wakati unanionesha chumba… unamkumbuka?” nilimuuliza tena huku nikimkazia macho.

“Mh! pale kuna Wasomali wengi kwa hiyo sikumbuki yupi unayemkusudia!” Merina alijibu huku akinitazama kwa tuo usoni.

Anyway, labda niulize hivi… kuna wale waliopanga katika chumba nambari 201 jirani na chumba changu wamejiandikisha kwa majina gani?” nilimtupia swali lingine na kumwona akinitazama kwa namna ya mshangao.

“Sikumbuki, kwani vipi?” Merina aliniuliza huku akiniangalia kwa udadisi zaidi machoni. “Naomba uniambie ukweli, Jason… wewe ni nani hasa! Are you a cop?”

“Kwa nini umeuliza hivyo?” nikamtupia swali huku sauti yangu ikiwa bado tulivu na ya kirafiki.

“Nataka tu kufahamu, maana maswali yako ni ya kipolisi polisi,” Merina alisema huku akitabasamu. “Kama kuna jambo baya linaendelea pale hotelini unaweza kuniambia, we are friends.”

Kwanza niliachia tabasamu lililozaa kicheko hafifu huku nikiyaondosha macho yangu toka usoni kwa Merina, “Hapana, mimi si polisi.”

You can trust me… kama kuna lolote unahitaji kufahamu we funguka tu, ila kama huniamini pia hakuna shida,” Merina alisema huku akitabasamu. “I can understand…”

“Wala si hivyo…” nilisema na kuachia tabasamu pana.

Muda huo akili yangu ilikuwa inasumbuka iwapo nimweleze ukweli au nisimweleze hasa nilipokumbuka kazi ngumu iliyokuwa mbele yangu, sikuona sababu ya kumficha lakini nilichagua kipi cha kumwambia na kipi nikiache.

“Sina hakika lakini kuna uwezekano mkubwa kuwa hao watu waliopanga chumba nambari 201 si watu wazuri kabisa. Usiniulize nimeona nini lakini elewa hivyo tu,” nilimwambia Merina kisha nikaongeza, “Naomba uwe makini saana lakini usimwambie mtu, sawa?”

Merina alibetua kichwa chake kukubali huku uso wake ukianza kupambwa na wasiwasi, na hapo hapo nikabadili mada, “Hivi eneo hili kuna gym kweli?”

“Ipo pale jirani na Bridge International Academy,” Merina aliniambia huku akielekeza kidole chake upande wa Magharibi.

“Basi nitaomba baadaye unipeleke,” nilimwambia kisha nikaongeza, “Pia n’tahitaji kununua nguo maana nimeona duka fulani la nguo kule barabarani.”

* * *



Saa 12:15 jioni…

Jioni ya siku hiyo ilinikuta nikiwa katika gym moja eneo lile la Shanzu barabara ya Old Malindi nikifanya mazoezi. Niliamua kufanya mazoezi makali mpaka watu wengine waliokuwemo ndani ya ukumbi huo wa mazoezi wakawa wananishangaa lakini sikujali bali niliendelea na mazoezi yangu na kuhakikisha mwili umetona jasho la kutosha.

Muda wote wakati nafanya mazoezi Merina alikuwa amesimama kando akinitazama kwa namna ya kunishangaa, hakujua kile kilichokuwa kikipita akilini kwangu muda huo. Huenda yeye pia alikuwa na maswali mengi kichwani kwake hasa baada ya mazungumzo yetu pale sebuleni.

Baada ya mazoezi yale makali nilichukua taulo langu dogo nililolinunua kwenye duka la nguo eneo lile na kujifuta jasho taratibu, kisha tukaondoka kurudi nyumbani kwa Merina.

Ilipofika saa moja na nusu Merina alikuwa tayari amekwisha maliza kujiandaa na alipotoka chumbani alinikuta nikiwa namsubiri sebuleni nikiwa tayari nimejiandaa. Nilivaa suti nzuri ya rangi ya kijivu na shati jeusi ambavyo nilikuwa nimevinunua kwenye duka la nguo pale pale Old Malindi Road, Shanzu. Kichwani nilivaa kofia ya kijivu aina ya pama iliyoendana na ile suti.

Merina yeye alivaa vazi la jioni, gauni fupi laini jekundu la kumetameta lililoishia juu ya magoti yake na kuufichua vilivyo ubora wa umbile lake. Miguuni alivaa viatu vyekundu visivyo na visigino, kisha akakamilisha urembo wake kwa kubeba mkoba mzuri mwekundu.

Usiku ule hali ya hewa ya jiji la Mombasa ilikuwa imepoa zaidi tofauti na hali ya joto iliyozoeleka, kulikuwa na manyunyu hafifu ya mvua yaliyoanguka kutoka angani kulikotanda wingu jepesi la mvua. Tulipotoka nje tuliikuta teksi ikiwa inatusubiri, dereva wa teksi ile alikuwa kijana wa makamo aliyefahamiana vyema na Merina kwa kuwa alikuwa ni mteja wake wa kuaminika. Alipotuona akaachia tabasamu.

Inaendelea...
 
Back
Top Bottom