369
“Mimi ni Jason Sizya, linapokuja suala la teknolojia mimi ndo kiboko yao, hii ndiyo kitu iliyofanya niaminiwe kupewa kazi tata na Idara ya Ujasusi,” nilisema katika namna ya kujigamba.
“
All the best,” Daniella alisema na kukaa kimya. Hakutaka kuongeza neno lingine.
Kwa kuwa nilikuwa nimefanya kazi kwenye taasisi ya SPACE ambayo ilikuwa taasisi maalumu ya Usalama wa Taifa ya kushughulika na masuala yote ya kiteknolojia kama sehemu ya ulinzi wa kimtandao dhidi ya nchi, hivyo nilijiamini kuwa ningeweza kuifungua mitambo ile na kuyabaini mawasiliano yote.
Kabla ya yote niliwasha kwanza kiyoyozi na hapo hewa safi ya ubaridi ikaanza kuingia mle chumbani, kisha nikaanza kubofya hapa na pale na sikuchukua muda nikagundua kuwa ili kufungua mitambo ile na kupata mawasiliano ilihitajika kwanza kufungua
codes fulani kwani mitambo ile ilikuwa imefungwa kwa namba maalumu ambazo mpaka ujue mjumuiko wake ndiyo uweze kupata mawasiliano.
Sikutaka kushindwa hasa kwa kuzingatia kuwa nilikuwa nimemtambia Daniella hivyo endapo ningeshindwa ingekuwa kichekesho cha mwaka. Pia nilitambua kuwa ni sisi wawili tu tuliokuwa tunategemewa na nchi kumkomboa Rais, japokuwa polisi na wapelelezi wao nao walikuwa wanafanya upelelezi juu ya tukio lile tata la kutekwa kwa Rais.
Kadiri nilivyocheza na zile codes niligundua kuwa zilikuwa ngumu sana kiasi cha kuanza kunitoa jasho. Daniella aliendelea kunitazama pasipo kusema neno. Kwa kweli ilikuwa kazi ngumu sana, kama vile kutafuta miguu ya nyoka.
Lakini baada ya kucheza na codes zile mara kadhaa hatimaye nilifanikiwa kuzifungua, hata hivyo hadi muda huo sikuwa nimegundua kulikuwa na chaneli ngapi zilizounganishwa kupeleka au kuleta mawasiliano pale kwenye kile chumba.
“Sasa hapa ninachotaka kufanya ni kutafuta kujua mitambo hii inatoa wapi mawasiliano na kupeleka wapi, na nani anayapokea…” nilimwambia Daniella kisha nikaongeza nikielezea kitaalamu, “hapa nitaiunganisha halafu nijaribu kuona codes zake zinavyooana, hapo tutajua upande gani unatuma taarifa kuja hapa na upande upi unapokea taarifa kutokea hapa, hii itakuwa rahisi sana kuwapata watu wetu.”
Daniella aliendelea kubaki kimya akinikodolea macho kwa mshangao maana kwenye masuala yale ya teknolojia alikuwa mtupu kabisa.
Niliziunganisha zile codes na kuiwasha ile mitambo, na hapo runinga kubwa iliyokuwa ukutani ikawaka na ramani ya Tanzania ikatokea huku yakionekana mawimbi fulani madogo madogo na mengine mawili makubwa, ambayo kwa haraka nilibaini kuwa yale mawimbi madogo zilikuwa chaneli za mawasiliano zilizokuwa zikileta taarifa pale kwenye kile chumba na yale mawimbi makubwa vilikuwa ni vituo vilivyokuwa vikipokea mawasiliano kutoka pale kwenye kile chumba.
Kama ramani ile ilivyojionesha, zile chaneli ndogo zilizokuwa zinaleta mawasiliano pale kwenye kile chumba zilikuwa zimetapakaa sehemu mbalimbali katika maeneo ya Dar es Salaam, Dodoma na pale Mtwara, na hii ilidhihirisha kuwa walikuwa wametega vinasa sauti kwenye ofisi kadhaa nyeti za taasisi za ulinzi na usalama, na hivyo taarifa zote za kutoka ndani ya ofisi hizo zilifika pale kwenye kile chumba bila chenga.
Halafu niligundua kuwa yale mawimbi makubwa mawili yaliyopewa utambulisho wa
‘the first wave’ na
‘the second wavei, vilikuwa vituo vikubwa vilivyopokea mawasiliano kutoka pale kwenye kile chumba. The first wave ilikuwa jijini Dar es Salaam na the second wave ilikuwa jijini Dodoma.
Hilo lilikuwa wazi kabisa, ila kazi kubwa ilikuwa kubaini vituo hivyo vilikuwa vipo kwenye majengo gani na nani walipokea mawasiliano hayo! Ningeweza kubaini endapo ningekuwa na muda kwani kazi hii haikuwa ya lelemama, ilihitaji muda wa kutosha wa kucheza na mitambo ile ili kubaini.
Tulipiga picha kila kitu ndani ya kile chumba kwa kutumia simu zetu zilizokuwa na kamera zenye uwezo mkubwa, kisha tukafanya upekuzi ndani ya chumba kile lakini hatukuweza kupata kingine chochote cha kutusaidia. Wakati tukianza kutoka nikaona kitu fulani ukutani kilichovuta umakini wangu.
Kilikuwa pembezoni mwa mlango ambapo kulikuwa kuna kitu kidogo chenye umbo la pembe nne, nikaanza kutafuta swichi fulani na kuiona kando ya ile mitambo ikiwa imefichwa, nilipoibonyeza sehemu fulani ya ukuta ikasogea.
Kiukweli nyumba ile kama ungeitazama kwa nje ungeichukulia kuwa ya kawaida sana na usingeweza kuipa uzito anaostahili. Kwenye macho ya kawaida ya binadamu ilikuwa ya kawaida lakini kiuhalisia ilikuwa kubwa sana kutokana na mambo kadha wa kadha yaliyowekwa katika muundo wa siri.
Baada ya ile sehemu ya ukuta kusogea likaonekana kabati moja lililokuwa limehifadhi nyaraka na makabrasha muhimu. Kulikuwa na mafaili mawili mekundu yaliyoonekana kuwa muhimu sana yakiwa na maandishi;
Top Secret.
Niliyachukua nikampatia Daniella ayashike kisha nikaangaza hapa na pale lakini sikuona kitu kingine, tukaanza kutoka nje. Mara nikahisi kusikia sauti fulani, sauti kama karatasi. Nikampa ishara Daniella, halafu tukajigawa, yeye akielekea upande wa kushoto na mimi nikaelekea upande wa kulia.
Wakati nikizunguka upande ule wa kulia nikasikia tena sauti ya kitu kama karatasi nyuma yangu. Haraka nikageuza shingo kutazama. Sikumwona mtu! Nikaendelea mbele huku nikizungusha macho yangu kutazama huku na kule. Sikuona mtu.
Sasa nilikuwa karibu na banda tulilomficha yule mlinzi wa ile nyumba, takriban hatua nne hivi kulifikia lile banda, nikahisi tena sauti ile ya mwanzoni. Haraka nikageuka huku nikinyoosha bastola yangu kuielekeza huko. Sikuona mtu! Niliporejesha tu uso wangu mbele, nikakutana na mwanamume mmoja mrefu akiwa amesimama.
Akili yangu ilifanya kazi haraka sana, lakini yule mtu alionekana kuwa mwepesi zaidi yangu katika kufanya maamuzi, kufumba na kufumbua nikamwona akiwa juu, nikapigwa teke lenye kilo nyingi lililonitupa chini kama peto la pamba!
Nilinyanyuka upesi kwa kujifyatua na mikono yangu. Yule mtu alionekana kutonipa mwanya hata kidogo, akachumpa na kujilaza hewani akijizungusha kama tairi na kuchanua miguu yake, kisha akaachia teke lingine.
Mara hii nililiona, nikainama kidogo kulikwepa, na yule mtu alipotua tu chini, kabla sijakaa sawa, mkono wangu wenye bastola ukapigwa teke lingine, bastola ikarukia mbali. Nikatabasamu nikiamini kuwa sasa nilikuwa nimempata kiboko yangu.
Nilikiri kimoyomoyo kuwa nilikuwa nimekutana na mtu makini mwenye kila aina ya mbinu na ujuzi katika sanaa ya mapigano. Lakini hii haikuniogopesha na badala yake ilinifanya kuwa makini zaidi.
Baada ya kugundua kuwa aina ya upiganaji wa yule mtu ulifanana sana kimtindo na ule niliokuwa nikipenda kuutumia nikajua mchuano ungekuwa mgumu, na hivyo niliamua kuingiza mafunzo kadhaa ya kijeshi niliyoyapata toka kwa makomando kule nchini Misri. Nikatanua miguu yangu na kumwita yule mwanamume kwa ishara.
Kama nilikuwa nimemchukulia poa sasa niliamini kuwa nilikuwa napambana na mtu wa kazi na hivyo kama ningejilegeza Daniella angenicheka. Kwa hesabu za haraka haraka tu niliamini kuwa nilikuwa nammudu yule, kama ni matemebezi basi alikuwa ameingia peku peku kwenye shamba lenye mbigiri na hivyo alipaswa kuvumilia miiba.
Yule mtu alinisogelea kwa kasi huku akikunja ngumi, akarusha mateke mazito ambayo niliyaona na kuyaepa, mateke hayo yakapita kando ya kichwa changu. Akarusha ngumi, akarusha teke, akapiga viwiko, vyote hivyo niliviona, nikavinyima mwelekeo.
Jamaa akashangaa kidogo, na hapo nikawa nimeamsha kichaa chake maana yule mtu alianza kutuma ngumi zake nzito kwa spidi ya ajabu. Vuuuup! Vuuuup! Lakini niliweza kuziepa, zote zikapita! Yule mwanamume akatuma ngumi nyingine na nyingine, na nyingine… nikazikwepa zote kama niliyekuwa kwenye mchezo wa rede.
Jambo lile likamshangaza sana, na baada ya dakika moja na nusu hivi nikawa nimeshamsoma adui yangu, sasa nikaanza kujibu mashambulizi. Nilimwona Daniella akiwa amesimama kando ya ukuta akitutazama kwa umakini. Alikuwa ametuachia ukumbi sisi wawili tuoneshane umwamba.
Sikukutaka kupoteza nguvu, niliamua kupiga maeneo dhoofu kwenye mwili wa yule jamaa. Ncha za ngumi zangu zilitafuta kingo za kwapa za yule jamaa, nikamtia ganzi mikono yake. Halafu nilimpiga pia chini kidogo, katikati ya shingo, penye kashimo kanakotenganisha shingo na kifua, na kisha kummalizia juu ya kitovu.
Ilifikia hatua yule mtu akaonekana kuchoka kwani alikuwa ametumia nguvu nyingi kurusha ngumi zilizokuwa zinaenda patupu. Pia ukijumlisha na ngumi zangu zilizokuwa zinatua maeneo dhoofu basi alishindwa kufua dafu. Alikuwa hoi.
Ni wazi alikuwa ameshindwa kuhimili mapigo yangu na hakutaka kuingia kwenye mikono yangu, hivyo basi alijikakamua kisha akafanya kama aliyetaka kunirukia, nikaepa kidogo na hapo hapo nikamwona akijirusha kwenye ukuta uliokuwa ukiizunguka nyumba ile kwa namna ambayo ilinishangaza kidogo, akadanda juu.
Daniella alipoinua bastola yake kumlenga akawa amechelewa kwani yule mtu alijirusha kwa nje na kukimbia.
* * *
Usichoke, endelea kufuatilia hadi mwisho wa mkasa huu wenye utata...