Simulizi ya Kijasusi: Bado Ninaishi

Simulizi ya Kijasusi: Bado Ninaishi

HADITHI: BADO NINAISHI (ASHRAFU NDILO JINA LANGU)
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
WHATSAPP: 0621567672
AGE: 18+

SEHEMU YA ISHIRINI NA MOJA
"Kama unaishi vizuri na viongozi wa hapa, umeshindwa nini kuwakamata hao ambao wanakufuatilia?"
"Nikifanya jambo la kijinga binti yangu anakufa, hivyo sitaki kumhusisha mtu yeyote hili jambo kijinga mpaka pale nitakapokuwa na uhakika kwamba mwanangu yupo kwenye mazingira salama" Remy alisimama na kujinyoosha vizuri ambapo mifupa ilikuwa inaitikia kwa nguvu sana. Alikuwa amepata jeuri kwa sababu alijua kupitia mtu huyo maisha yake yangekuwa rahisi kama alivyo hitaji na angetekeleza yale ambayo alikuwa anataka kuyafanya bila kelele yoyote ile.

"Ni njia gani ambayo utaitumia kunitoa mimi sehemu hii?" mwanaume aliuliza akiwa anarudi kuketi chini.
"Una usiku mmoja tu wa kulala hapa, kuna gari ambazo huwa zinaingia humu ndani kuleta walinzi na kutoka nao hilo naona ndilo litakuwa rahisi zaidi wewe kulitumia kutoka hivyo nitakuandaliwa sare kama za watu hao na muda wa kutoka mlinzi mmoja nitampoteza kisha nafasi yake utaingia wewe hivyo utatoka kirahisi sana bila kushtukiwa na mtu na baada ya hapo utaanza kuyatekeleza majukumu yako"
"Mchezo wako ni mzuri sana, na huyo binti yako nitampatia wapi?"
"Wakati unatoka humu kuna maelezo nitakupatia juu ya wapi pa kuanzia ili uweze kufanikiwa kumpata kwa sababu hata mimi sijui mahali alipo mpaka wakati huu"
"Ila itakugharimu pesa nyingi sana kuweza kunifanya niifanye hiyo kazi"
"Shingapi unataka?"
"Bilioni tano pesa za kitanzania"
"Hakikisha haufanyi kosa lolote juu ya binti yangu bwana mdogo"
"Deal, utaniingizia bilioni tatu kabla sijatoka hapa kisha hiyo bilioni mbili utanilipa nikimaliza kazi yako. Jambo la msingi la kulizingatia ni kwamba haitakiwi mtu yeyote kunifuatilia wala kunipangia cha kukifanya kwani kama umeniamini na kuona kwamba naweza kuifanya kazi yako vizuri basi unatakiwa kuniacha niifanye kwa namna yangu mimi ambayo naona itanifaa"

"Deal" wanaume walimaliza mazungumzo yao na kupeana mikono kisha mzee huyo akatoweka humo ndani. Remy alitabasamu na kutamka.
"Umejileta mwenyewe, nitakufanyia jambo ambalo hautalisahau kwenye maisha yako yote. Ni wakati wa kuchukua kila kilicho potea, mwanzo wa kuzitafuta sarafu kumi na tano zilizo potea umefika rasmi" alitamka kwa msisitizo sana mwanaume.

Ndani ya gereza hilo kulikuwa na heka heka nyingi kwa sababu ilikuja taarifa ya ghafla kwamba mheshimiwa raisi alikuwa anelekea ndani ya eneo hilo hivyo mazingira ya kuyaandaa mazingira ya sehemu hiyo yalikuwa yanafanyika kwa nguvu kubwa sana huku wafungwa wasiwe na taarifa yoyote ile juu ya ujio wa kiongozi huyo mkuu wa nchi.

Saa tano usiku ndio wakati ambao msafara wake wa gari kumi na tano ulikuwa unaingia ndani ya sehemu hiyo huku akionekana kuwa na hamu kubwa sana ya kuonana na mfungwa wake ambaye alikuwa humo ndani. Baada ya kupokelewa na mkuu wa gereza walienda moja kwa moja mpaka kwenye ofisi ya Luka Gambino.
"Mheshimiwa karibu sana japo sikujua kama leo ningepata bahati ya kutembelewa na wewe ndani ya eneo hili" Luka Gambilo alijikanyaga kwa hofu ila kiuhalisia taarifa alipewa mapema sana
"Nahitaji kukutana na huyo bwana mdogo haraka sana"
"Sawa mkuu, aletwe au nikupeleke sehemu ambayo tumeiandaa ili mfanyie mazungumzo?"
"Naenda mwenyewe huko huko" hakuwa na namna zaidi ya kumuongoza mheshimiwa raisi kuelekea sehemu ambayo alikuwepo mwanaume huyo.

Walifika kilipokuwepo chumba hicho huku nje kukiwa na ulinzi mkali isivyokuwa kawaida. Ni kama Remy hakujiandaa kabisa kuweza kumpokea mheshimiwa raisi ndani ya hilo eneo hivyo kiasi fulani alishtuka japo hakuhitaji kuonyesha mshtuko wake waziwazi. Wakati huo ndio alielewa kwamba ni kwa nini jioni ya siku hiyo alipelekwa ndani ya chumba kisafi sana namna hiyo ambacho kilikuwa na kila kitu.

Mkuu wa gereza aliingia ndani ya chumba hicho na kubonyeza rimoti yake ambapo sehemu ya ukuta ilijifungua. Chumba hicho kilikuwa kikubwa sana kiasi kwamba kikawa kinagawanywa katikati na ukuta huo mzito ila baada ya kufunguliwa mbele yake kulikuwa na sehemu ambayo ilikuwa ina kila kitu ambacho kinatakiwa kuwa ndani na hata hali yake ya hewa ilikuwa nzuri sana kwa sababu kulikuwa na viyoyozi. Wanaume waliokuwa na silaha nzito walimpa ishara Remy kuongoza hiyo sehemu ambayo alitakiwa kufanyia mazungumzo na mheshimiwa raisi lakini raisi aliwazuia watu hao kwa sababu alihitaji kufanya mazungumzo yeye tu na huyo mtu wake.

"Mheshimiwa hauwezi kufanya mazungumzo ukiwa mwenyewe kwa ajili ya usalama wako mbele ya huyu mtu ambaye ni hatari sana inatakiwa uwe na walinzi kwa karibu sana"
"Huwa sipendi kuongea mara mbili mbili, nahitaji kufanya mazungumzo yangu binafsi na huyu mtu nikiwa pekeyangu" mheshimiwa aliongea akiwa anampiga jicho kali sana mkuu wa gereza ambaye hakuwa na namna zaidi ya kuwatoa vijana wake hiyo sehemu na hata walinzi wa raisi walikuwa wapo nje kabisa ya hicho chumba.

"Una miaka mingapi bwana mdogo?" raisi aliuliza swali huku akiwa anafungua friji dogo na kutoa wine ambayo ilikuwa humo ndani na kuimimina kwenye bilauri mbili ambazo zilikuwa zimeandaliwa mezani.
"Thelathini na sita"
"Miaka hiyo mpaka leo hujui namna ya kumheshimu mkuu wako wa nchi?"
"Nimesikia kwamba huku hatuishi wanadamu wa kawaida, tunaishi watu ambao dunia imetusahau kabisa na hatuna maana yoyote tena hivyo kama wewe haujali kuhusu watu wako, unahisi watu wako wanteuheshimu uwepo wako nchini?"

"Ni mtu pekee ambaye ana uhakika sana na usalama wake ndiye anaweza kumjibu raisi wake jibu la kipumbavu kama hilo"
"Sina cha kupoteza nasubiria kufa tu hivyo sioni tofauti yoyote ile kufanya jambo lolote lile kwa ajili ya kukufurahisha wewe hapo"
"Una uhakika? nilidhani unaweza ukawa unaniomba msamaha au kuomba msaada wangu nione kama naweza kukutoa hapa bado unaniletea kiburi?"

"Najua haujaja hapa kwa ajili ya kunitoa mheshimiwa na hauwezi kuja kumuona mtu ambaye ametelekezwa kwenye hili gereza bila kuwa na sababu ya msingi hivyo ni vyema kama ukaniambia ni kipi unakihitaji kwangu"
"Nimevutiwa sana na ujasiri wako bwana mdogo japo unaweza ukakuponza sana. Unajua mimi kufika hapa nilipo imetumika gharama kubwa sana ambayo huenda kwa mwanadamu mwenye uwezo wa kawaida asingekubali kabisa kuitoa lakini kwa sababu nilikuwa najua kitu ambacho nakifanya na ni kitu ambacho nilikuwa nakiishi nilipambana mpaka kila mtu akaanza kuliheshimu jina langu ndani ya taifa hili"

"Sasa inapotokea mtu anakuja na kuanza kucheza na hili jina langu huwa najisikia vibaya sana. Kazi yangu kubwa pale Ikulu ni kuhakikisha kila mtu yupo sawa kwenye hili taifa hivyo kama sipo sawa maana yake ni kwamba naweza kujikuta nafanya maamuzi ya hovyo ambayo yanaweza kulifanya taifa likaingia kwenye hatari kubwa sana kitu ambacho sitaki kitokee"
21 inafika mwisho.

Febiani Babuya.
 
HADITHI: BADO NINAISHI (ASHRAFU NDILO JINA LANGU)
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
WHATSAPP: 0621567672
AGE: 18+

SEHEMU YA ISHIRINI NA MBILI
"Mheshimiwa unazunguka sana, nini unakitaka?"
"Napenda sana ujasiri wako kwa sababu unaonekana haupendi sana kona kona, sasa nahitaji uniambie huyu ni nani?" mheshimiwa alitamka kauli hiyo akiwa anatoa gazeti na kulirushia mezani kwa Remy. Ikamlazimu mwanaume kulinyanyua gazeti hilo ili kuweza kuisoma habari hiyo ambayo alitumia dakika mbili tu akalirudisha gazeti hilo chini uso wake ukiwa mkavu mno.
"Kwahiyo unahisi mimi ndiye nimefanya hiki?"
"Hapana, tukio hili limetokea wewe ukiwa ndani tayari ila najua kabisa lazima utakuwa na uhusiano mkubwa na mtu ambaye amelifanya hili"
"Nadhani hiyo ni kazi ambayo unaweza ukawahusisha watu wako wa ulinzi wakaifanya, sijaelewa mimi unanihusishaje kwenye jambo kama hilo"

"Habari hiyo imeanzia hapo ambapo wewe umekamatwa hivyo kukamatwa kwako ndiko kumezalisha hiyo taarifa kwenye hilo gazeti nadhani umeona vizuri. Halafu baada ya hapo limeunganishwa tukio la kukamatwa kwako na maisha ya Dominic Sawa sawa hivyo nahitaji kujua pia wewe una uhusiano gani na huyo mtu mpaka imefikia hatua nakosewa heshima na mwananchi wa kawaida akinihitaji mimi nikaombe msamaha tena kwa kupiga magoti hadharani?" Remy alisimama na kuzunguka kidogo kisha akarudi kukaa.

"Mheshimiwa kwani kuna kitu gani hasa kilitokea hiyo miaka ishirini ambayo imezungumziwa hapo kabla ya mimi kukujibu swali lako kadri nilivyo lielewa?"
"Mhhhhhh haya ni mambo ya ndani sana ya serikali ila kiufupi ni kwamba huyo mtu alifanya mambo ya ajabu sana kwenye taifa hili mpaka ikafikia hatua hili gereza likaja kuitwa jina lake ikiwa ni kama kumbukumbu kwa wale wote ambao wanafanya hayo mambo wakiliona jina hilo basi walikumbuke hili gereza na mateso yake makali ambayo yapo ili wasije wakafanya makosa kama ambayo aliyafanya mtu huyo"

"Nadhani jambo la mhimu hapo kama kweli taarifa inadai kwamba mwanae bado anaishi, hapo mtakuwa na kazi mbili. Kwanza ni kumtafuta ambaye ameitoa habari hii lakini pili ni kumtafuta huyo mtoto ambaye anadaiwa kwamba bado anaishi kwa sababu mimi sijui lolote kuhusu mtu huyo na sihusiki kwa lolote na habari hiyo. Huenda nimewahi kufanya mambo mabaya sana kwenye maisha yangu ila sijawahi kumiliki gazeti wala kuwa na mtu ambaye anaweza akanisemea mimi kupitia gazeti, sababu kubwa ni kwamba hata ndugu mimi sina"

"Kama ni hivyo Remy, kwanini unafanya haya yote?" Remy alimwangalia sana mheshimiwa raisi ambaye alionekana kuwa na hamu kubwa sana ya kumsikia mwanaume huyo akitoa jibu la kwanini aliamua kuyaishi maisha ya namna hiyo. Alikifungua kinywa chake;
"Kuna wakati unaihitaji dunia na kila kitu chake ikukubali wewe kwa jinsi ulivyo, lakini wakati unawahitaji wanadamu wakupokee na kuishi na wewe kwa wema kwenye hiyo hiyo dunia, unakuta kila mtu anakupa mgongo na kukukataa basi unakuwa hauna chaguo zaidi ya kuishi maisha ambayo upande wa dunia na hao wanadamu wanakuchagulia uyaishi. Maisha yametuachia chaguo moja tu la maisha ili tuweze kuishi na kuyamudu maisha hivyo naishi kwenye machaguo ambayo dunia na walimwengu wamenipatia"

"Unamaanisha nini kusema hivyo?"
"Ni ngumu sana kunielewa mheshimiwa kwa sababu unaishi maisha safi ambayo huelewi watu wanapitia nini huku nje ya box, upo ndani ya uwanja hivyo ila ladha ya mpira wewe unaijua ni tofauti na mtu ambaye yupo nje ya uwanja yeye kazi yake ni kupiga kelele tu za kushabikia"
"Who are you Remy?"
"Remy Claude ndilo jina langu la kuzaliwa, mengine siyakumbuki kwa sababu wakati naanza kujielewa nilikuwa mtaani tu hivyo kuhusu maisha yangu ya nyuma huwa siyakumbuki tena"
"Hiyo ndiyo sababu unaua watu?"
"Hapana huenda naua watu ambao wanataka kuniua mimi kwanza, kisheria nadhani mnaita kujilinda"
"Unacheza na akili yangu bwana mdogo sio?"
"Hakuna mtu kwenye hili taifa ambaye anaweza kucheza na akili yako kwa sababu wewe ndiye mwamuzi wa mwisho wa kila kitu"
"Unataka kuniambia hiyo ndiyo sababu pia ambayo ilikufanya wewe uue maaskari na wafungwa wenzako ili uje kwenye hili gereza?"
"Ndiyo mheshimiwa"
"Niliwahi kuambiwa kwamba ndege mjanja huwa ananasa kwenye tundu bovu sana, sio muumini sana wa misemo ya zamani ila nakupa muda wa masaa sabini na mawili ujitafakari na kunipa majibu sahihi ya nilicho kuuliza, usinilazimishe nije kukuuliza kwa lazima nikaonekana mtu mbaya sana kwako"
"Sawa mheshimiwa" raisi alimwangalia sana kijana huyo, alinyanyuka na kutembea hatua kadhaa mbele kisha akageuka tena maana hakuwa akiamini namna kijana huyo alivyokuwa anajiamini sana.
"Unafanana sana na mtu mmoja wa miaka mingi iliyopita huko nyuma, ni wazi usipofanya maamuzi sahihi unaweza ukamfuata muda sio mrefu huko aliko" kauli ya raisi ilimfanya Remy macho yaanze kubadilika lakini alitabasamu na kutamka;
"Wakati utaamua mheshimiwa" mazungumzo yao yaliishia hapo raisi akawa anaondoka sehemu hiyo, hakujibiwa kile ambacho alikuwa anakihitaji lakini alipata mwanzo wa kile ambacho alikuwa anakihitaji kwa sababu lengo lake kubwa lilikuwa ni kuunganisha doti tu ya mambo ambayo yalikuwa yanatokea na kufanyika ndani ya nchi yake.

Kila kitu ambacho kilikuwa kinafanyika kuna mfungwa alikuwa makini sana kukifuatilia ila alishtuka sana baada ya kumuona mheshimiwa raisi akiwa anatoka ndani ya hiyo sehemu maana ni wazi hakurajia kabisa kukutana kumuona raisi huyo.


Wakati huo wa usiku ambao raisi alikuwa ameenda kukutana na Remy ndio muda ambao Robert alikuwa amemteka mwanaume mmoja na kumfungia kwenye chumba ambacho walikuwa yeye na Hezroni. Mwanaume huyo alikuwa ni mmoja kati ya walinzi ambao walikuwa wanalinda ndani ya gereza la Dominic na kupatikana kwake ilikuwa ni kazi nzuri ya Hezroni.

Mwanaume huyo aliteswa sana mpaka akalazimika kuweza kusema ukweli juu ya utaratibu wote na ulinzi wa sehemu hiyo na namna walivyokuwa wakibadilishana shifti kwa siri kubwa sana. Alikuwa ametoka hivyo asubuhi wakati kunakaribia kukucha kuna gari ya jeshi ambayo ilikuwa inatakiwa kuwapeleka huko kisha ingetoka na wanaume wengine ambao walikuwa wamemaliza shifti zao na huo ulikuwa ni utaratibu ambao ulikuwa unafanyika mara nyingi sana japo sio wote ambao walikuwa wanaweza kutoka na kuingia hiyo ilikuwa ni kwa wale ambao walikuwa wapo ndani ya gereza hilo kwa muda mrefu sana na kuitengeneza imani kubwa.

Hakukuwa na jambo lingine zaidi ya kuyafanyia kazi maelezo yake ambapo Robert aliyavaa mavazi ya mwanaume huyo na kuelekea sehemu ambayo gari ingemchukua usiku huo. Kwa sababu ya kiza kinene ambacho kilikuwepo hakuna mtu ambaye alikuwa na muda wa kuweza kuwakagua sana huku kwenye mfuko wake akiwa na kitambulisho cha mwanajeshi huyo, kofia ikisaidia kwa ukubwa sana kuilinda sura yake.

22 naweka nukta hapa.
 
HADITHI: BADO NINAISHI (ASHRAFU NDILO JINA LANGU)
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
WHATSAPP: 0621567672
AGE: 18+

SEHEMU YA ISHIRINI NA TATU
Mida ya saa tisa usiku walikuwa wanaingia sehemu hiyo huku kila mtu akiwa na kitambulisho chake mkononi na baada ya ukaguzi huo wote waliruhusiwa kuingia ndani bila shaka. Gari ilisimamishwa wakashuka na wakati huo wanajeshi wengine wakawa wanapanda hapo ili kuweza kutoka kwani waliokuwa wanaingia walikuwa wanazichukua nafasi zao lakini akiwa anatembea alihisi kama kuna mtu alimfananisha hivi, aligeuka haraka sana kuangalia vizuri ila kwa bahati mbaya mwanaume huyo alikuwa amempa mgongo akiwa ameinamia chini huku akiiweka kofia yake vizuri. Alitamani kumfuata mwanaume huyo ambaye aliishia kuingia kwenye gari la jeshi ambalo muda huo huo lilianza kuondoka ila hakuwa na hiyo nafasi kwani ni wakati ambao walitakiwa kuingia na kutoka kwake huko ilikuwa ni changamoto sana.

Masaa mawili yalipita tangu gari ya jeshi iweze kutoka na walinzi ambao walikuwa wanaondoka eneo hilo, ilisikika filimbi ya hatari hali ambayo ilifanya wanaume na silaha zao kupita kweye kila selo kukagua baada ya kugundulika kwamba mfungwa mmoja alikuwa anakosekana. Mkuu wa gereza alishtuka sana kwa taarifa hizo ambazo alikuwa amezipokea hivyo akakimbilia moja kwa moja kwenye chumba ambacho walikuwa wamemhifadhi Remy, baada ya kufika ndani ya chumba hicho alianza kucheka kwa sauti kubwa, ungehisi kwamba alikuwa na furaha sana lakini alikuwa anatoa kicheko cha hasira na ghadhabu kubwa sana.

Alitoa amri upite msako mkali sana kwenye kila kona ya gereza hilo. Licha ya msako mkali ambao ulifanyika kwa saa zima hakuna kitu ambacho walikipata wala kupata alama ya uwepo wa mtu huyo ndani ya hilo eneo. Mzee huyo alihisi kuchanganyikiwa kwa sababu hakuwa na jibu la kuwaambia wakubwa wake wa kazi kwani ni masaa machache tu tangu raisi aingie ndani ya eneo hilo hivyo kutoroka kwa mtu huyo ingekuwa ni ishara kwamba alikuwa mzembe sana na huenda angesababisha madhara hata kwa mheshimiwa raisi, alijua wazi nafasi yake ilikuwa mashakani sana.

Alishangaa sehemu yenye ulinzi mkali kama hiyo mtu mmoja kafanikiwaje kutoroka? Hapo ndipo jibu likamjia kichwani kwamba lazima mtu huyo ametoka kama moja ya mlinzi humo ndani. Ulipita msako wa kutafuta ni nani ambaye hakuwepo wakati huo ndipo walikuja kuukuta mwili wa mlinzi mmoja ndani ya maji kwenye tenki akiwa amekufa.

Mkuu wa gereza alijihisi kuchanganyikiwa asiamini alichokuwa anakiona mbele ya macho yake. Aliwaita makamanda wote ambao alikuwa anawaamini sana wakiwemo wale wanaume wa kazi ambao mmoja wao alimshushia kipondo Remy. Watu hao walipewa kazi ya kuingia kimya kimya mtaani kwenda kumtafuta mtu huyo kabla taarifa hazijawafikia wakubwa maana ilikuwa inaenda kuwa hatari sana kwake.

Wakati huo Robert akiwa amefika humo ndani ndipo aligundua kwamba mhusika ambaye yeye alimfuata humo ndiye huyo aliyekuwa anatafutwa hivyo hakuwa na cha kusubiri maana yake kama mambo yangetulia basi asingeweza kutoka tena hivyo wakati ambao wanachaguliwa watu wa kuweza kuingia mtaani kumtafuta mwanaume huyo naye alijipenyeza na kutoka nao. Sio yeye tu ambaye alitoka wakati huo lakini pia mwanaume ambaye alikuwa anamfuatiliwa Remy kwa umakini sana naye alipotea muda huo huo kwa kuitumia nafasi hiyo kuondoka ndani ya hilo eneo. Msala ulikuwa unabaki kwa Luka Gambino akiwa haelewi nini kilifanyika lakini kupaniki kwake kulitoa mwanya wa watu wenye akili zao kuweza kuingia na kutoka kwa namna walivyotaka wao. Remy Claude waweza kumuita The Menace, alikuwa mtaani tayari kwa ajili ya kwenda kumkomboa mtoto wa mzee ambaye alikutana naye ndani ya gereza akamuahidi kuwa huru na kiasi kikubwa sana cha pesa huku watu wengi sana pia wakitumwa mtaani kwenda kumtafuta kwa sababu alitakiwa kurudishwa mapema sana gerezani kabla taarifa hazijasambaa juu ya kupotea kwake wala kuleta madhara kwa raia wasiokuwa na hatia.

Taarifa za kupotea kwa mfungwa gerezani zilifika kwa mheshimiwa Henry Mawenzi kupitia kijana wake ambaye alikuwa amempenyeza ndani ya gereza la Dominic. Taarifa hizo zilikuja wakati mbaya na zilikuwa za kushangaza sana kwa sababu kwa namna yoyote ile haikudhaniwa kama mfungwa huyo anaweza kutoroka ndani ya gereza na wakati ambao taarifa hizo zinafika, ziliambatana na taarifa za kuelezea kwamba kila kitu kuhusu mtu huyo kilikuwa ni cha uongo kabisa kwenye maisha yake. Pia uwepo wa mtu huyo gerezani uliambatana na kukutana na mtu mwingine ambaye alikuwa humo humo ndani na baada ya kukutana na mtu huyo ndipo kupotea kwake kulitokea, hivyo huenda mtu huyo alikuwa na taarifa za kutosha kuhusu kupotea kwa mwanaume huyo, ilitakiwa afuatiliwe kwa ukaribu sana maana angeweza kuwa mtu sahihi kusaidia kupatikana kwake kabla madhara makubwa hayajaweza kujitokeza.

Mwanaume huyo alimsisitiza pia bosi wake kwamba mtu huyo kila kitu kumhusu kilikuwa ni cha uongo hivyo walikuwa na kazi kubwa mbele yao ya kuweza kuujua ukweli kuhusu yeye ili waweze kujua ni wapi walitakiwa kuanzia na lengo hasa la mtu huyo kufanya mambo yote hayo lilikuwa ni lipi. Mr Henry hata hakushtuka sana kuletewa taarifa za mtu huyo maana ni yeye ambaye tangu mwanzo alikuwa na wasiwasi naye sana na hakuamini kama mtu huyo alikamatwa kwa bahati mbaya bali ulikuwa mpango wake ila taarifa za kupotea kwake gerezani hizo zilimshtua sana maana ilikuwa ni hatari ya wazi ambayo ilikuwa mbele yao.

Baada ya kuzipokea taarifa hizo aliona ni sahihi kama akimhusisha moja kwa moja mkubwa wake hivyo akapiga simu ili waweze kuonana.
"Bosi"
"Nakusikiliza Henry"
"Nina habari mbaya sana, naomba tuweze kuonana wakati huu"
"Kuna nini Henry?"
"Hautazipenda hivyo tukutane ana kwa ana"
"Tukutane Kariakoo"

"Sawa bosi" simu ilikatwa kisha mwanaume huyo akaongoza moja kwa moja sehemu ambayo bosi wake huyo alimuita ili waweze kuzungumza. Kariakoo mtaa wa Kongo, ndipo mahali ambapo walitakiwa kukutania kwenye duka moja kubwa sana la nguo ambalo lilikuwa linamilikiwa na mama huyo na watu wengi ambao walikuwa wanamfahamu mtaani hapo mama huyo walijua kwamba ni mfanya biashara mkubwa sana wa nguo, hakuna mtu hata mmoja ambaye aliwahi kuhisi kwamba mama huyo alikuwa ndiye mkuu wa usalama wa nchi. Ndani ya duka hilo ambalo alilimiliki kwa muda mrefu sana kulikuwa na ofisi ya siri ambayo alikuwa anaitumia kufanyia majukumu yake hata akiwa humo ndani. Mr Henry aliingia hapo kama mnunuzi wa nguo lakini baada ya kufanya manunuzi kadhaa alihitaji kuzungumza na bosi wa duka na hapo akapata nafasi ya kuongea na bosi wake ikiwa ni mchana kweupe.

"Remy ametoroka gerezani" mwanamama Cleopatra Gambo alibaki ameduwaa akihisi kwamba masikio yake hayakuwa yakisikia vyema kile ambacho kilikuwa kinaongelewa.
"Umejuaje?"
"Nadhani mapema siku ile nilikwambia nitalifanyia uchunguzi jambo hili kuhusu uongo wa huyu mtu kudanganya kila kitu kwenye maisha yake. Hali hiyo ilinifanya nimtume kijana wangu kule kufanya uchunguzi, akiwa anaendelea na kazi hiyo kwanza amegundua kwamba tulikuwa sahihi Remy ana ajenda zake za kwenda kule jela lakini akiwa kule kuna mtu mmoja ambaye inadaiwa kwamba amekutana naye na baada ya kukutana na mtu huyo, baadae akakutana na mheshimiwa raisi ambapo hajamaliza hata masaa sita akawa amepotea"

"Ni nani huyo ambaye amekutana naye kabla ya kukutana na raisi?"
"Bruno Josephat"
23 naweka nukta.
 
HADITHI: BADO NINAISHI (ASHRAFU NDILO JINA LANGU)
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
WHATSAPP: 0621567672
AGE: 18+

SEHEMU YA ISHIRINI NA NNE
"Unamaanisha yule tajiri mfanya biashara?"
"Ndiyo bosi"
"Why?"

"Kimekuwa kitendawili kizito sana ambacho tunatakiwa kukipatia jibu lake"
"Bruno Josephat ameingiaje ndani ya lile gereza?"
"Bado sijajua juu ya hilo bosi"
"Kwahiyo wanatuchezea mchezo hawa wajinga si ndio? Unaweza ukaniambia mtu mmoja amefanikiwa vipi kutoroka kweye gereza kama lile?"
"Kwa hesabu za haraka haraka inaonekana kwamba ametoka wakati walinzi wanatoka alfajiri"
"Taarifa za ulinzi ni siri kubwa sasa inawezekana vipi yeye ajue akiwa na siku chache tu gerezani?"
"Ni wazi kwamba kuna watu waliuza taarifa"
"Natakiwa kukutana na vijana haraka sana huyu mtu atafutwe kwa namna yoyote ile, mimi naenda gerezani huko wakati huu"
"Tunaenda wote bosi" madam alimwangalia msaidizi wake, hakuwa na namna ikamlazimu kukubali kufanya jambo hilo wakati huo walikuwa wametoka nje wakijifanya kama wana maongezi ya biashara kisha wakapanda kwenye gari kuanza kuelekea hiyo sehemu.

Kila hatua chache walizokuwa wanazipiga, kuna gari ilikuwa inaunga msafara wao, hao walikuwa ni walinzi wa mkuu wa usalama ambao walitakiwa kuhakikisha mheshimiwa yupo salama wakati wote mpaka wanaishika njia ya kuelekea huko msafara ulikuwa umekamilika gari sita zikiwa kwenye mwendo mkali sana. Cleopatra Gambo aliitoa simu yake mfukoni na kumpigia mwanadada Anelia Baton;
"Uko wapi?"
"Mheshimiwa raisi amenipigia simu nakutana naye muda huu"
"Baada ya hapo jiandae, tuna tatizo limejitokeza"
"Lipi hilo?"
"Remy ametoroka gerezani"
"Whaaaat?"
"Haya mambo tutayaongea nikirudi, hakikisha raisi haipati habari hii kwanza na kama kuipata basi mimi ndiye natakiwa kumfikishia mwenyewe"
"Sawa bosi"

Wakati huo ambao simu hiyo ilikuwa inamfikia Anelia, ni wakati ambao alikuwa anaingia kwenye mlango wa Ikulu kwenda kukutana na raisi kama mheshimiwa huyo alivyokuwa ameahidi. Alijitambulisha na kukaguliwa kila kitu baada ya kuonekana yupo salama walimruhusu kuingia na kwenda kukutana moja kwa moja na raisi wake.

Mheshimiwa huyo alikuwa amekaa bustanini sehemu ambayo ilikuwa na upepo safi hususani ule ambao ulikuwa unatokea baharini, hiyo ndiyo sehemu ambayo alikuwa anahitaji kufanyia mazungumzo na mwanamke huyo. Hakuwahi kabisa kumuona mrembo huyo hadharani zaidi ya kuzisikia sifa zake nyingi za uchapakazi kutoka kwa mkurugenzi wake, siku hiyo tena mchana kabisa kukiwa hakuna hali ya jua alibahatika kuona sura adimu sana kwenye taifa lake, sura ambayo huenda haikumfanya aamini kwamba kwenye nchi yake kulikuwa na malaika wazuri namna hiyo. Alijikuta anamkadiria mrembo huyo tangu akiwa mbali mpaka alipo mkaribia pale alipokuwepo, Anelia alifika hapo akiwa kwenye vazi bora sana la kike mpaka mheshimiwa alisahau hata kumkaribisha kitu ambacho kilimfanya mlinzi wake kumkumbusha kwamba mwanamke huyo alikuwa amefika tayari na hapo ndipo mheshimiwa alijikohoza na kumkaribisha kiti mwanamke huyo na kumtaka mlinzi wake awapishe.
"Karibu sana, Anelia nani vile?"
"Baton" ni kama kuna kitu kilimfanya ashtuke baada ya kulisikia jina hilo ila alijifanya kwamba hakuna lolote.

"Asante sana mheshimiwa, najihisi mwenye bahati sana kuweza kupata nafasi ya kukaribishwa na wewe sehemu bora zaidi kama hii ambayo kila mtu ana ndoto ya kuja kufika japo mara moja tu kwenye maisha yake yote"
"Usijali kabisa, wewe ni moja kati ya watu mhimu sana kwenye taifa hili hivyo unastahili kabisa kufika ndani ya sehemu kama hii kwa makubwa ambayo unaifanyia nchi hii. Nimepata taarifa zako na sifa zako nyingi sana juu ya kazi nyingi ambazo umezifanya ndani na nje ya nchi hususani hili la kutusaidia kumkamata huyu gaidi ambaye nasikia alikuwa na magenge mengi sana ya kihalifu. Hii inakufanya wewe kuwa mtu sahihi kabisa kupata sifa zangu na kupata zawadi zangu ambazo nitazitoa kwa ajili yako" mheshimiwa alionekana kabisa amemtamani kama sio kumpenda mwanamke huyo maana alianza kubabaika sana akiwa anamuangalia kuanzia chini na Anelia aliligundua hilo hivyo akawa anajiachia sana.

"Anaonekana anapenda sana chini huyu, ngoja nifanye kila ambacho anakitaka ili kama akiingia kwenye anga zangu basi nitamtumia kulipiza kisasi changu na kuutafuta ukweli juu ya kifo cha wazazi wangu ambacho nahisi kuna mikono ya watu fulani lazima ilihusika" Anelia alijiongelea mwenyewe kwenye moyo wake baada ya kuona tamaa za kifisi mbele ya macho ya raisi kisha akamjibu;

"Najisikia fahari sana kupata sifa kwa bosi wa nchi, naahidi nitafanya kila kitu kwa ajili yako na taifa hili mheshimiwa"
"Una uhakika kwamba upo tayari kufanya lolote kwa ajili ya raisi wako?"
"Ndiyo mheshimiwa"
"Safi sana, kwenye maisha yako wewe unahitaji nini labda Anelia?"
"Napenda nchi yangu iwe na amani kwanza kisha ifuate amani ya moyo wangu"
"Moyo wako nafikiri ni jambo la kumtafita mtu wa kuufanya uwe na amani tu"
"Lakini kazi yangu hainiruhusu hilo mheshimiwa"
"Hahahaha inawezekana ni wewe tu kuamua"
"Hii kazi inakufanya usiwe na chaguo"
"Sio kweli, siku zote lazima uwe na chaguo"

"Mimi silioni kwa sababu kila kitu nakifanya kwa kuiweka nchi mbele kwanza kabla hata ya uhai wangu"
"Ni jambo kubwa kufanya hivyo kwa sababu kama taifa tunawahitaji watu wazalendo kama wewe lakini sio sababu ya kukufanya wewe ukose chaguo"
"Huenda upo sahihi mheshimiwa"
"Unahitaji nini kwa kazi nzuri ambayo unaifanya?"
"Sihitaji chochote kile, kwangu kunitambua tu kwamba nafanya kazi nzuri ni jambo kubwa ambalo linanifanya nijivunie sana"
"Unaonaje leo baadae tukikutana kwenye moja ya nyumba zangu zilizopo baharini huko?"
"Kutakuwa na kazi nyingine mheshimiwa?"
24 inafika mwisho.
 
Ukitaka kumalizia episodes 76 zilizo bakia kwa mkupuo ni 3000 tu.

WhatsApp 0621567672
 
Ndio Anelia kutakuwa na kazi tena kazi tamu hhhhahahhah. Thank you Babuya
 
Matajiriiii hope mko poa.

Been a minute, nilikuwa online kwa cm nyingine ila cm ya kazi nilipasua kioo bahati mbaya nikiwa mezani kuandaa simulizi mpya hivyo ikabidi nikapigwe za kichwa kariakoo ili cm ipone.

So kwa sasa ipo sawa hivyo leo baadae narudi hapa kuweka, nitaweka episode tano kufidia.

So far naona kununua mmegoma kabisa [emoji28]


NB
Kwa ambaye anataka kumalizia yote mpaka 100 analipia 2500 tu.

Wasalaam,

Febiani Babuya
 
Back
Top Bottom