Simulizi ya kijasusi: Nafsi zilizotelekezwa

Simulizi ya kijasusi: Nafsi zilizotelekezwa

HADITHI: NAFSI ZILIZO TELEKEZWA
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
WHATSAPP: 0621567672
AGE: 18+
UKURASA WA 48

Mshauri mkuu wa raisi Bacia Ojok alikuwa anasimamia kila kitu hapo lakini hata IGP kwa Uganda Okumu Odinga naye alikuwa amealikwa kwa sababu mara ya kwanza alishiriki kwenye mawasiliano ya mwanzo hivyo kuna taarifa kutoka kwake zingesaidia kwenye huo uchunguzi wao, walikuwa wameungana na maafisa wengine wa usalama wa ngazi za juu za shirika hilo. Mtu ambaye alikuwa amezungukwa alikuwa ni Odong, yeye ndiye ambaye kwa mara ya kwanza kabisa alikutana na mwanaume huyo hivyo alikuwa na taarifa nyingi zaidi ya wote, alikuwa akitetemeka kwa sababu wakubwa zake walikuwa wamemsimamia mbele yake na alijua kabisa kwamba jambo hilo lilikuwa linaweza kumfanya akaishia ndani.
“Unaweza kutuambia kama huyu kijana ambaye alijitambulisha kama Yohani ni mtanzania?”
“Ndiyo”
“Una uhakika gani juu ya hilo?”
“Kwa sababu alinihakikishia wakati tunafanya mazungumzo ya kawaida”
“Vipi kama alikuwa anakudanganya?”
“Hapana, yalikuwa ni mazungumzo ambayo isingekuwa rahisi kunidanganya namna ile kwa sababu alidai kwamba sio kwamba hakuwa na uwezo wa kuwafuata watu ambao alihitaji kuwasiliana nao ndani ya taifa lake bali alikuwa na mipango yake ndani ya taifa hili ndiyo maana aliamua kuja kutumia taifa letu”
“Una uhakika na hili?”
“Ndiyo bosi” alikuwa anamjibu IGP ambaye alikuwa bosi wake, watu hao waliandika kidogo kwenye karatasi mshauri mkuu wa raisi mwanamama Bacia akasogea alipokuwa ameketishwa bwana Odong akiwa anamwangalia kwa macho ambayo yalikuwa na maswali mengi.
“Unahisi kwanini alikuwa tayari kuweza kuleta maafa makubwa namna ile kwenye ule uwanja wa mpira?”
“Nahisi kwa sababu aliamini kwamba tusingemkatalia kile ambacho alikuwa anakitaka yeye”
“Unahisi?”
“Ndiyo kwa sababu sijui alichokuwa anakifikiria kwenye moyo wake ila mimi nimejibu hivyo kwa kutumia uzoefu wangu kwenye hii kazi”
“Tuje kwenye suala la msingi, baadhi ya maofisa wako pale kituoni wanadai kwamba baada ya kumkamata mtu yule kuna video alikuonyesha kwenye laptop yake, baada ya kuiona video hiyo inadaiwa ulishtuka na kuhitaji kufanya naye mazungumzo naye mkiwa wawili tu ambapo inadaiwa kwamba ulichukua muda mrefu kidogo mkiwa wawili pekeyenu, unaweza kuniambia mlichokuwa mkikijadili?” jasho lilianza kumtoka bwana Odong akiwa mwingi wa wasiwasi. Akiwa anajishauri, kuna mwanaume alisogea akiwa na bastola kwenye mkono wake ambapo mwanamama huyo alinyoosha mkono wake akaipokea na kuikoki vizuri akiwa anamwangalia Odong usoni.
“Alikuwa anaitishia familia yangu” aliongea akiwa anatetemeka
“Aitishie familia yako kwa sababu zipi?”
“Kwa sababu ana taarifa zote chafu za viongozi wa juu wa nchi hii zikiwepo na zako” maneno yake yaliwashangaza wote mle ndani.
“Una maana gani?”
“Siwezi kusema hadharani mheshimiwa, naomba uikague ile laptop ukiwa pekeyako nadhani utanielewa” mwanamama yule aliagiza ile laptop ambayo hawakuwa wameikagua ndani yake kujua ina nini, aliletewa na kuhitaji kuingia sehemu ambayo haikuwa na kamera na alitaka kuwa mwenyewe. Alitajiwa namba za kufungulia mafaili hayo akatulia kwa zaidi ya nusu saa akiwa amejifungia ndani ya chumba cha pekeyake, alitoka akiwa amechoka.
“Nani mwingine ambaye ameona haya?”
“Ni mimi pekeyangu”
“Una uhakika?”
“Ndiyo mkuu”
“Unaweza ukaniambia watu wake walijuaje kwamba yeye amepelekwa sehemu ya siri kama ile?” Odong alibaki amekodoa macho akiwa hana jibu la kutoa, ilibidi wamsisitizie kwamba kama angeleta utani kwa ile kesi basi angejikuta akiingia kwenye hatari kubwa ambayo ingempelekea hata kuishia kufungwa hivyo hakuwa na namna zaidi ya kuusema ukweli ambao alikuwa anaujua.
“Alisema kwamba mimi ndiye nitakaye msaidia ila sikujua nitamsaidia vipi mpaka jambo hili lilipo kamilika ndipo nimekuja kuelewa”
‘Unamaanisha nini?”
“Wakati amekuja kituoni pale aliniambia nipige simu nyumbani, baada ya kuipiga ile simu kuna watu ambao walienda pale kunitafuta na mke wangu aliniambia wameondoka. Yohani aliniambia kwamba wale walikuwa ni watu wake hivyo alikuwa anaweza kuua familia yangu muda wowote ule kama nisipo msikiliza ndipo akanionyesha video zangu kama msisitizo kama nisipo fanikisha yeye kuongea na nyie”
“Video zilikuwa zinahusu nini na za wewe na nani?”
“Mimi na mke wangu, maudhui yake ni kama hizo ambazo umeziona humo na aliahidi kwamba anaweza kuzisambaza muda wowote ule akitaka ambazo zinaweza kuleta madhara makubwa kwa taifa hili”
“Baada ya hapo kilifuata nini?”
“Baada ya hapo niliondoka kwenda nyumbani kuhakiki kama familia yangu ilikuwa salama lakini wakati nafaika kule mke wangu aliniwekea kifaa cha mawasiliano kwenye nguo yangu baada ya kutishwa kwamba asingefanya hivyo basi watoto wetu wangeuawa na hakujua kifaa hicho kilikuwa cha kazi gani. Hivyo ndivyo walivyo fanikiwa kujua mahali ambapo tulikuwa tunaelekea kwa sababu walijua moja kwa moja kwamba ni lazima mngeenda na mimi kwa ajili ya ushahidi”
“Na hizo video zako mbona hazipo?”
“Alinipa nafasi ya kuzifuta”
“Kuna kingine cha siri ambacho alikiongea?”
“Hapana” Mwanamama huyo alinyanyuka na kumtaka kiongozi wa eneo hilo ahakikishe anawatuma majasusi wao Tanzania kwa ajili ya uchunguzi na miongoni mwa hao majasusi wao wawili walikuwa ni double agent kutoka Tanzania ambao walikuwa wanakula pande zote. Mtu huyo alitakiwa kupatikana kwa namna yoyote ile ili ijulikane kwamba ni wapi alikuwepo aingie kwenye mikono yao.
Mwanamama huyo alitoka hapo akiwa amefura kwa hasira kwa sababu alichokuwa amekiona mle ndani kilikuwa ni hatari mno kwa usalama wa taifa lao. Aliingia kwenye gari yake na kumtaka dereva aondoe msafara huo haraka lakini alipofika umbali kadhaa kutoka yalipo makao makuu ya ISO alimtaka dereva asimame na kutoka nje ya gari kwani alikuwa na simu ya mhimu alikuwa anaipiga.

Alibonyeza tarakimu kadhaa kutoka kwenye simu ndogo ambayo aliificha ndani ya zipu ndogo kwenye mkoba wake, simu hiyo iliita mara ya kwanza ikakata bila majibu lakini mara ya pili ilipokelewa.
“Ni wewe ulimtuma yule kijana kuja huku Uganda sio?”
“Ndiyo, tatizo liko wapi?”
“Sikutegemea kama ungekuwa mshenzi kiasi hiki, unayakumbuka makubaliano yetu mimi na wewe?”
“Nayakumbuka vizuri sasa sielewi unacho pigia makelele ni kipi!”
“Kwahiyo umeajiri watu ambao wananifuatilia kila sehemu na kunirekodi video nikiwa kwenye faragha zangu? Halafu usivyo na aibu unampa mtu baki tu hizo video unategemea nini zikivuja?”

UKURASA WA 48 unafika mwisho.
 
HADITHI: NAFSI ZILIZO TELEKEZWA
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
WHATSAPP: 0621567672
AGE: 18+
UKURASA WA 49

“Yule sio mtu baki, ni kijana wangu makini kuliko unavyo fikiria wewe. Hizo video ndizo ambazo zimerahisisha zoezi hilo kwenda haraka kabla ya mambo yangu kuharibika kwa huyo kijana ambaye mlikuwa mnamshikilia. Huwa nina namna yangu ya ufanyaji wa mambo yangu hususani kwa watu kama wewe, sijui saa wala dakika ambayo utaamua kunigeuka hivyo hizo video ni ulinzi wako mwenyewe kuhakikisha unanitii na kunisikiliza. Siwezi kuzipeleka popote mpaka siku ambayo utaamua kunisaliti ama kwenda kinyume na vile ambavyo nahitaji iwe Bacia” ilikuwa ni sauti ya kike kutoka upande wa pili. Sauti ambayo ilikuwa inaunguruma kutoka Tanzania.
“Kate umefikia hatua mbaya kunidhalilisha namna hiyo”
“Tuachane na hayo, mmeamua kuchukua hatua gani?”
“Serikali haiwezi kukaa kimya, nimetoa amri watumwe majasusi kupeleleza huko Tanzania”
“Bila shaka wakifika huku wanatakiwa kufa si ndiyo?”
“Ndiyo ila wafe bila kuacha ushahidi wa mwili wala taarifa zozote yaani wasije kupatikana lakini pia wawili miongoni mwao watakuwa ni madouble agent wa Tanzania na Uganda hivyo nina imani hakuna makosa yatafanyika”
“Done” Simu ilikatwa, alikuwa anaongea na Madam Kate ambaye alikuwa nyuma ya huo mpango wa kilicho tokea. Mshauri mkuu wa raisi alikuwa amebanwa kwenye mbavu na mwanamke huyo hakuwa na kauli kwake hivyo alijikuta akiiuza serikali yake kwa mwanamama huyo ili kuendelea kulinda siri zake kwa sababu kama angeenda naye kinyume basi ilikuwa inakula kwake.

Kamanda wa jeshi la polisi kanda maalumu ya Dar es salaam hakuridhishwa na yale maamuzi ya yeye kupokonywa ile kesi kwenye mazingira ambayo hayakueleweka. Hakuridhika na yale maamuzi ila hakuwa na namna ya kuweza kupinga kwa sababu ilikuwa ni amri kutoka juu na halikuwa ombi, alikumbuka asubuhi ya siku hiyo alikutana na afisa upelelezi wa mkoa kuweza kujadili yale ambayo yalitokea husuani mauaji ya kijana wake Julius Mbandu na baadhi ya maafisa upelelezi wengine.
“Bwana Kono najua kabisa kwamba hukufurahi mimi kuichukua hii kesi kwenye mkono wako ila tulipo fikia kwa sasa sidhani kama kuna haja ya sisi kuendelea kulaumiana kwa yaliyo tokea, nadhani jambo la msingi zaidi ni kuweza kukaa chini pamoja na kujua ni kipi ambacho tunatakiwa kukifanya kwani hiki ambacho kinatokea kwa sasa sio jambo la kawaida”
“Kwahiyo umekuja hapa baada ya kijana wako kupoteza maisha ndipo ukaona ninakufaa?”
“Uko sawa kuwaza hivyo na sikulaumu ila kumbuka hii ni nchi na ina utaratibu wake kwenye kesi kama hizi na wewe sio mgeni na huu utaratibu ambao huwa tunaufuata kila linapo tokea tatizo na ulipewa muda kabisa ukashindwa kuutekeleza”
“Nadhani hata wewe ulipewa muda au wewe umefanikisha hilo?”
“Hapana ndiyo maana nipo hapa kuhitaji msaada wako”
“Msaada wangu wakati kesi imesha enda ngazi za juu?”
“Kumbuka nimempoteza kijana wangu tena ameuliwa kwa kudhalilishwa vibaya akiwa karibu kuupata ushahidi, nahitaji kujua kama kuna jambo lolote uliligundua kipindi ambacho ulikuwa unaifuatilia hii kesi, linaweza kunisaidia na nikajua wapi pa kuanzia”
“Sina kitu ambacho nadhani naweza kusema kwamba kitakusaidia, hakuna jambo la maana mpaka sasa zaidi ya mkanganyiko wa udanganyifu wa binti aliye tekwa na watekaji wenyewe”
“Unajaribu kumaanisha nini kusema hivyo?”
“Yule binti kwa mazingira yanavyo onekana sidhani kama ametekwa”
“Kwahiyo?”
“Nadhani alikuwa anajua anacho kifanya”
“Una maana gani kusema hilo?”
“Yule binti kuna namna ndogo tu aliitengeneza sura yake japo hajaibadilisha ila kuna vitu aliongezea usoni vya kuifanya sura yake isitambulike moja kwa moja, yule ni binti ambaye amewahi kuhudumu kwenye ngazi ya jeshi na mafunzo ya ukomando kule Morogoro”
“Bado sijakuelewa, kwamba komando anaweza kutekwa kirahisi tu namna ile?”
“Ndiyo maana nakwambia hajatekwa yule, alikuwa anajua anacho kifanya. Jambo ambalo linaweza kukusaidia ni jina lake, anaitwa Nicola Aidan Semzaba hivyo nadhani msaada wangu unaweza ukawa umeishia hapo”
“Nashukuru sana kwa hilo lakini nina maswali kadhaa bado na kuna kitu nakihitaji kwako” Raymond Kono hakumjibu zaidi ya kubaki anamwangalia mtu huyo ambaye mara ya kwanza aliichukua kesi kwake kwa dharau ila wakati huo alikuwa analilia msaada wake kwa udi na uvumba.
“Aidan Semzaba unamzungumzia mwanasheria wa zamani?”
“Ndo huyo”
“Asante sana kwa hili ila hiki sicho kilicho nileta hapa, jambo ambalo limenileta hapa ni juu ya kifo cha Julius. Mara ya mwisho alienda kumchukua mzee Kazimoto kwa taarifa ambazo nilizipata na baada ya hapo baadae akanipigia simu kwamba ana masaa mawili tu atamleta mtuhumiwa kwangu akiwa mzima kabisa, sikuhoji kujua kwamba mtuhumiwa huyo alikuwa ni nani hasa lakini kwa bahati mbaya ikapatikana maiti yake na sio mtuhumiwa. Kwahiyo nipo hapa ili unisaidie kama utakuwa unajua jambo lolote lile juu ya kile ambacho kilikuwa kimetokea au kuna uhusiano gani kati ya mzee Kazimoto na kifo cha Julius?”
“Hata mimi kesi hii sikufika mbali kiasi kwamba nipate ushahidi wa kutosha ila ni kwamba nahisi Damasi bado yupo hai”
“Hilo haliwezekani, mwili wake uliagwa kabisa na alisimamia mheshimiwa raisi”
“Wewe ndiye unasema haiwezekani, kwamba raisi akiaga kitu ndiyo sababu ya kusema haiwezekani?”
“Lakini tuliuaga hata mwili wake siku ile na baba yake mzazi alithibitisha hilo?”
“Hii ni dunia ya utandawazi, hakuna jambo linashindikana mbele ya sayansi zaidi ya kushindwa kukwepa kifo tu. Kifo ndicho kitu pekee ambacho teknolojia haiwezi kukizuia ila hivi vingine inawezekana kabisa, sitaki kukuaminisha kwa sababu sina uhakika kamili ila naweza kusema Damasi bado yupo hai na huenda hata kifo cha Julius ni yeye amehusika nacho”
“Kama unacho niambia ni kweli, kuna uhusiano gani kati ya Damasi kuwa hai na kumteka huyu mwanamke ambaye umedai kwamba amewahi kupata mafunzo ya kikomando?”
“Hilo ndilo swali ambalo hata mimi sijui napataje majibu yake na nina imani usinge nipokonya hii kesi kwa kebehi huenda ningekuwa nakaribia kupata majibu yake. Nimekusaidia kadri ya uwezo wangu ulipo ishia hivyo naomba uende kwa sasa nahitaji kubaki mwenyewe” kamanda alijitahidi kumpa ushirikiano mwenzake licha ya yye kumfanyanyia ubabe wakati wa kuichukua kesi hiyo. Afisa upelelezi wa mkoa aliondoka akiwa ana maswali mengi kwenye kichwa chake, mwanga mdogo ambao aliupata haikuwa sababu ya yeye kuamini kwamba ndio ulikuwa ukweli kwani hata kesi ilikuwa haipo chini yake tena hivyo kama ni kuliwasilisha jambo hilo kwa wakubwa, alihitaji kuwa na ushahidi wa kutosha mezani ili asikilizwe bila tatizo lakini alikata tamaa kwani bado asingeipata ile nafasi kabisa ni mambo ambayo yalikuwa nje ya uwezo wake tayari.

Kamanda alikuwa anayakumbuka mambo hayo akiwa kwenye gari yake, alikuwa Tambani Mkuruganga wakati huo. Nafsi yake iligoma kabisa kuamini kwamba Damasi alikuwa mfu kwa matukio ambayo yalikuwa yanatokea hivyo kwake aliamini kwamba kuna kitu mzee Kazimoto alikuwa anakijua na anakificha ndiyo sababu usiku huo aliamua kutembelea yalipo makazi ya mzee huyo ili kuanza uchunguzi wake kimya kimya.

UKURASA WA 49 unafika mwisho.
 
HADITHI: NAFSI ZILIZO TELEKEZWA
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
WHATSAPP: 0621567672
AGE: 18+
UKURASA WA 50

Gari yake aliipaki kwa muda umbali kidogo yalipo makaburi ya familia ya mzee huyo likiwa limezimwa. Kulikuwa na minazi mingi kiasi, alipo ona kiza kimezidi, alishuka na kujongea taratibu kuelekea yalipo yale makaburi akiwa na imani kwamba huenda kuna jambo angeweza kuliona ama kupata kitu chochote ambacho kingemsaidia kwenye uchunguzi wake, kesi hiyo alikuwa akiisimamia yeye mwenyewe kwa mkono wake bila kumshirikisha kijana wake yeyote kwa sababu hakutakiwa kufanya hivyo baada ya kesi kutolewa kwenye mikono yake, kama wakubwa zake wangepata taarifa juu ya hilo basi ingekuwa ni tatizo kubwa ndiyo maana aliichukua kimya kimya na kutaka kupata ukweli kimpango wake.
Alisogea mpaka lilipokuwepo kaburi la Damasi, usiku ulikuwa unazidi kuingia na eneo hilo lilikuwa limetulia huku upepo ukiwa unapiga taratibu kwa mjongeo mdogo wa minazi ambayo ilikuwa imezunguka umbali mdogo kutoka yalipokuwepo makaburi yale. Alikaa kwa zaidi ya saa moja hakuona kitu, alihisi huenda alifanya kosa kuja makaburini na badala yake angeenda kukaa karibu na nyumba ya yule mzee hivyo akaamua kukata shauri la kuondoka eneo lile na kuja siku nyingine lakini wakati anahitaji kugeuka alihisi jambo.
Mchakacho uliyagusa masikio yake ikamfanya awe makini, zilikuwa ni hatua za mtu kuelekea lilipokuwepo lile kaburi. Mtu huyo alikuwa anatembea taratibu bila wasiwasi japo hakuwa anaoneka vizuri kutokana na ambacho kilikuwa kimetawala kwenye eneo hilo. Akiwa anahitaji kuona kile ambacho angekifanya mtu huyo, alishangaa kusikia hatua za mtu mwingine zikiwa zinatoka upande wa pili zikielekea pale pale kwenye lile kaburi la Damasi. Alipigwa na butwaa baada ya kusikia sauti, sauti ya kiume nzito ambayo ilikuwa inaongea na mzazi.
“Shikamoo baba”
“Marahaba mwanangu, siku mbili hizi zimekuwa siku ndefu kwa upande wetu vipi kwema huko utokako?”
“Huko kwema kabisa, hakuna tatizo kwa sababu mtu pekee ambaye alifanikiwa kujua kwamba nipo hai kwa sasa amekufa”
“Ni jambo zuri kwa sababu nilipatwa na mashaka makubwa baada ya kuja hapa na kubomoa hili kaburi akihitaji kwenda kuchukua vipimo vya mifupa na hata baadae alipo niambia kwamba vipimo vyako na mtu aliye zikwa ni tofauti ndipo aliniongezea shaka zaidi ila nimefurahi kama jambo hili limeisha salama”
“Yule bwana mdogo alikuwa anapenda umaarufu kwahiyo ikawa ni vyema kwa sababu hakufanikiwa kumwambia mtu mwingine. Ulifanya kazi kubwa kusimamia ujenzi kwa muda mfupi kwahiyo kwa sasa nadhani siri itabaki mahali salama kabisa ila haitakuwa vyema kama tukiendelea kuonana kwa wakati huu”
“Kwanini unasema hivyo mwanangu?”
“Hii itakuwa hatari kwa upande wenu ninyi hapo, kama tukiendelea kukutana wanaweza kukutumia wewe kama chambo baadae nikapatikana na unajua kabisa siri ikijulikana watu wangu lazima wataua familia nzima ili kupoteza ushahidi. Chukua hili begi lina pesa na nitakutafuta tena kukiwa na ulazima” aliongea Damasi akiwa anamkabidhi baba yake begi ambalo alidai lina pesa ila mpango huo haukukamilika baada ya kusikia sauti ya mamlaka na tochi ikiwashwa kwa nguvu na kufanya eneo hilo kuwa na mwanga mkali.
“Stop Damasi,
! Huwezi kuendelea kulisumbua taifa hili kwa kuigiza kifo chako mshenzi mkubwa wewe. Leo tunaondoka mimi na wewe habari yako inaishia hapa” ilikuwa ni kauli ya mamlaka kutoka kwa Raymond Kono.
“Wewe ni nani ambaye unanifuatilia kiasi hiki?” ilikuwa ni sauti ya dharau kutoka kwa Damasi ambayo haikuwa na wasiwasi, utulivu ilikuwa sehemu ya kujiamini kwake.
“Kamanda wa polisi kanda maalumu ya Dar es salaam”
“Oooh bwana Raymond Kono?”
“Upo chini ya ulinzi Damasi” aliongea akiwa anairushia pingu alipokuwepo Damasi ambaye aliinama kuiokota.
“Najua unayafanya haya kwa sababu ya njaa ya pesa, unatamani upate nafasi zaidi ya hapo hivyo nitakupa nafasi nyingine ya kuishi na kiasi cha pesa na jambo hili liishie kwenye moyo wako”
“Kama unanifahamu basi utakuwa unaelewa kwamba mimi sio mtu wa kula rushwa Damasi, jifunge hizo pingu kabla sijaachia risasi kwenye mwili wako”
“Kwamba utanipiga risasi mtu ambaye natakiwa kukamatwa nikiwa hai na kukupa umaarufu nchini? Hapana”
“Kama ukiwa mbishi nitamuua baba yako”
“Kwamba utampiga risasi raia ambaye hana hatia kwa sababu ya kumkamata mtuhumiwa wako ambaye hata nchi haina taarifa za kuendelea kuishi kwake? Mimi na wewe wote tunajua kwamba huwezi kufanya hivyo kwa sababu utakuwa umeyaharibu maisha yako mwenyewe hivyo hilo huwezi kulifanya kwahiyo ni mimi na wewe hapa japo hata huo ubavu wa kuniua mimi hauna. Acha utoto chukua pesa uondoke zako na usije ukarudi tena kwenye ulimwengu wa namna hii kwa sababu kujua tu kwamba mimi nipo hai basi hautakiwi kuishi tena ila nakupa nafasi”
“Jifunge pingu hiyo acha maneno mj…..” kauli yake ilionyesha kabisa kwamba hakuwa tayari kumuelewa Damasi hivyo kabla hata hajamalizia sentensi yake alirushiwa pingu kwa kasi hali ambayo ilimfanya kupambana kuikwepa hata tochi ilidondokea pembeni ikawa inamulika pale alipo. Wakati anakaa sawa Damasi alimfikia, alimvunja mguu vibaya kwa teke ambalo alitua nalo chini ya goti kisha buti likatua kwenye shingo yake hali iliyo mfanya akibamize kichwa chake kwenye kaburi ambalo lilikuwa pembeni.
Alihitaji kuitumia bastola yake kichwa kikiwa kimechanika vibaya ila mkono wake hakuwa na nguvu za kutosha, alikutana na kisu ambacho kilidondosha kiganja chake chini akabaki analia kama mtoto. Damasi aliiokota bastola na kwenda kukaa pembezoni wa lile kaburi ambapo alikuwepo kamanda wa polisi.
“Watu wengi kinacho waua ni kutafuta umaridadi mbele za watu ambao hawastahili kuwaonyeshea umaridadi huo, maneno haya nimekuwa nikiwaambia watu wengi ila huwa wanayasikiliza wakiwa hawana namna na wapo kwenye hatua za mwisho za maisha yao kama ilivyo kwako hapa saivi na huo ndio ubaya lakini kama ungeamua kubadili mtazamo huo na kunisikiliza tangu mwanzo basi tusinge fikia hapa bwana kamanda” Alitulia na kuendelea;
“Watu ambao wanafanikiwa kufahamu yaliyopo nyuma yangu sio wewe tu, kuna watu kadhaa ambao nimewaua huko nyuma na wote huwa wanakuwa na malengo sawa kutamani kujua ni sababu zipi hasa ambazo zilinifanya nikafikia hatua ya kuigiza kifo changu mwenyewe ila kwa bahati ambayo ni mbaya wote huwa wanayapata majibu wakiwa kwenye nyakati za mwisho kama hivi. Ndugu yangu hata mimi sipendi kuishi kwenye dunia kama hii ya kujificha ficha huku watu wakijua wewe ni mfu, unahisi kwamba labda mimi nafurahia hali kama hii? Hapana sio kweli ila inanilazimu kuwa hivi”
“Hata mimi mara ya kwanza kabisa wakati natafutwa na kupewa mpango huu niligoma ila kugoma kwangu kuliiweka njiapanda familia yangu kwa sababu ilitakiwa waue familia nzima kisha na mimi nife, ni mwanaume gani ambaye unahisi yupo tayari kushuhudia familia yake inakufa mbele yake? Jibu unalo kwenye nafsi yako. Watu ambao ninafanya nao kazi ni watu ambao hutakiwi kuwafuatilia kabisa wala kuwataja kwa sababu ni suala la nusu saa tu kukufanya wewe upoteze kila kitu kwenye maisha yako”
“Who are you working for?” kamanda huyo wa polisi alijilazimisha kuweza kuuliza kuhusu mtu ambaye ndiye alikuwa bosi wake na Damasi huku akiwa anahema kwa shida na maumivu.
“LUNATIC SOCIETY. Siku ya kwanza nafuatwa na hawa watu waliniahidi maisha mazuri lakini pia ilikuwa ni lazima kujiunga nao kwa sababu ukigoma tu basi yanakutokea ambayo niliyaoroshesha huko juu, sasa swali langu likabaki kwamba ni kwanini mimi? Ndipo baadae nikaja kugundua kwamba huwa wanatafuta watu wenye uwezo mkubwa kuanzia kwenye akili na kwenye mapigano kwa ajili ya kutekeleza majukumu yanayo hitaji mabavu na akili. Tangu nijiunge nayo nimefanya matukio mengi ya kutisha, nimeua watu wengi kwa sababu sitakiwi kuuliza huwa naambiwa tu natakiwa kwenda wapi, muda gani na kumuua nani ila sababu za kufanya hayo huwa siambiwi hivyo hata mimi nipo gizani kwenye mambo mengi kama wewe ila nacho kijua ni kwamba mpaka viongozi wakubwa wa kiserikali wapo ndani ya hii mipango ambayo hata mimi sijui mwafaka wake ni upi”

UKURASA WA 50 unafika mwisho.
 
HADITHI: NAFSI ZILIZO TELEKEZWA
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
WHATSAPP: 0621567672
AGE: 18+
UKURASA WA 51

“Sasa kwa hilo hata nikikuua wewe unahisi unaweza ukanilaumu bwana kamanda? Ni kweli mimi sikufa, mimi nipo hai kabisa ndiyo maana mpaka sasa unaniona hapa mbele yako hivyo kwa mtu yeyote ambaye atatambua uwepo wangu basi ni lazima nimuue kuilinda siri hii”
“Unahisi utaua watu wangapi?”
“Hata mtaa mzima ikibidi kwani ikigundulika siri imevuja basi mimi ndo natakiwa kufa na familia yangu” alihitimisha kauli yake kwa kuzamisha kisu kwenye shingo ya kamanda huyo wa polisi kisha akatoweka naye hayo maeneo baba yake akibakia kusafisha eneo hilo ambalo tukio lilitendeka.
Asubuhi na mapema ulikutwa mwili ndani ya gari, mwili huo ulikuwa umetelekezwa Ubungo mataa karibu na sheli ya mafuta kwenye fly over. Mwili ulikuwa wa kamanda wa polisi kanda maamulu ya Dar es salaam ukiwa umechomwa chomwa vibaya na visu vingi ambavyo viliacha majeraha ya kutosha kwenye mwili huo.
Lilikuwa ni tukio la kushangaza kwa kiongozi mkubwa wa jeshi la polisi kama huyo kukutwa akiwa ameuliwa kwa kudhalilishwa namna hiyo, tukio hilo liliibua na kubeba hisia zingine nyingi kwa wananchi na jeshi la polisi wa ujumla. Matukio yalizidi kila siku, walikuwa wanakufa viongozi wengi wa mamlaka za usalama bila kujulikana chanzo chake hasa kuwa nini hali ambayo iliendelea kuleta taharuki kubwa huku hali hiyo ikizidi kulichanganya shirika la kijasusi la nchi hali ambayo ilipelekea taarifa hizo kuanza kupenya moja kwa moja kwenye masikio ya raisi.

OSTERBAY POLICE STATION
KAPOMBE TYSON, Lilikuwa jina ambalo lilikuwa likisomeka juu ya kibao kigumu ambacho kililazwa juu ya meza moja kubwa na ngumu ya mninga. Karibu na kilipokuwa kibao hicho ilinyooshwa miguu ya mtu ambaye bila shaka alikuwa amechoka kukaa kwa muda mrefu humo ndani kama sio kuwa kwenye dimbwi zito la mawazo.
Ilikuwa ofisi ya mkuu wa kituo hicho cha Osterbay, wakati huo alikuwa amejilaza kwenye kiti chake akionekana kabisa kuzama kwenye usingizi ambao ulizichukua fikra zake kwa wakati huo. Simu ya mezani kwake ilianza kuita kwa fujo na sauti kubwa huenda ni kwa sababu ya utulivu ambao ulikuwepo ndiyo maana sauti ilikuwa kubwa, alishtuka kutoka usingizini na kuhema mara kadhaa huku akijifuta udenda ambao ulikuwa unamwagika wa usingizini kisha akajiweka sawa na kuipokea simu hiyo.
Alishtuka kwa maelekezo ambayo alikuwa anapewa na mtu huyo ambaye hakuwa akimjua ni nani ila yeye alikuwa anamfahamu kiundani. Mtu huyo alimwelekeza kwamba alikuja hapo muda mfupi uliopita na kuacha mzigo wake ambao bila shaka vijana wake walikuwa wamemletea ofisini kwake hivyo alitakiwa kuufanyia kazi haraka na kufuata maagizo ambayo yalikuwepo ndani kisha simu ikakatwa upande wa pili. Alishangazwa na jambo hilo la kupokea simu hiyo, namba ngeni halikuwa jambo geni kwake kwa sababu ni mara nyingi alikuwa akizipokea ila maelekezo ambayo aliyapokea kutoka kwenye namba hiyo ndiyo ambayo alihisi kwamba hakuwa ameyaelewa.
Alitazama saa ya ukutani, muda ulikuwa umeenda. Saa kumi na mbili na nusu ya jioni ndivyo muda ulivyokuwa unasoma kwenye hapo ndipo aligundua kwamba alikuwa amelala kwa masaa matatu kwenye kiti chake hicho hivyo huenda hata vijana wake wakati wanamletea mzigo huo hakuwa macho. Aliyatupa macho yake mle ndani kabla ya kufanya maamuzi ya kumuita katibu muhtasi wake, kwenye meza ndogo ambayo haikuwa mbali na mlango, kulikuwa ana bahasha ya A4 ambayo ilikuwa imeongezeka, akagundua kwamba lazima ndiyo ambayo ilikuwa ikizungumziwa.
Aliisogelea na kuifungua kwa tahadhani huku moyo ukiwa unamuenda mbio, ndani yake kulikuwa vitu viwili; picha na barua ndogo. Aliitazama picha ambayo ilikuwa humo ndani alishangaa kukutana na picha ya mtoto wake wa mwisho wa kike, moyo ulipigwa na ubaridi kwa hofu ambayo ilimuingia moyoni. Aliitoa simu yake mfukoni kupiga nyumbani kwake haraka kujua kama mwanae alikuwepo na mazingira yake kama yalikuwa salama ila kitu cha ajabu nyumbani kwake mtoto alikuwepo na hakuwa na tatizo lolote, hapo akashusha pumzi na kuifungua barua ambayo ilikuwa ndani yake.
Barua hiyo ilikuwa na maneno machache tu ikimtaka jioni hiyo afike Masaki ilipo hoteli ya Sea Cliff kuna maelekezo angepewa huko. Maelezo yalionyesha wazi kwamba akifika huko watu hao wangemuona kitu pekee ambacho yeye angetakiwa kukifanya ni kwenda na gari yake eneo la mbele kidogo kutoka ilipo parking kubwa ya hoteli hiyo eneo ambalo lilikuwa na kanyika kadogo kisha angepata maelekezo ya hatua ambazo alikiwa kufuata baada ya hapo. Ile picha ya mtoto wake ndiyo ilimpa ishara ya hatari kwamba halikuwa ombi bali ilikuwa ni lazima afanye jambo lile kwani huenda asingefanya hivyo basi alikuwa anayaweka maisha ya mtoto wake hatarini huku akiwa hajui ni nani ambaye anadili naye, njia pekee ambayo alikuwa ameamua kuifuata ni kwenda kumsililiza huyo mtu huku moyoni akiwa na jazba.
Hakumuuliza mtu yeyoye wala kumuaga yeyote, alitoka nje na kuingia kwenye gari yake kisha akaondoka eneo hilo kupitia Namanga kwenda Masaki ili akamsikilize huyo mtu ambaye moyoni aliendelea kumtafakari akiwa anashangazwa na jambo hilo kuhitaji kujua kwamba mtu huyo alikuwa anahitaji nini hasa kwake mpaka afikie hatua ya kumtishia mtu kama yeye namna hiyo? Hakupata jibu.
Aliendesha kwa kasi mpaka alipofika kwenye kituo cha Bhakhresa ilipo BAO akasimamisha gari yake na kuingia ndani kupata chakula. Aliona kabisa kwamba alikuwa amewahi na mazungumzo yalionyesha kabisa kwamba gizani yangekuwa vizuri zaidi hivyo aliona sehemu hiyo angeitumia kupoteza muda mpaka wakati ambao angeona unafaa ndipo aondoke. Alitumia dakika arobaini kukaa pale mpaka alipokula ndipo akatoweka na wakati huo kiza kilikuwa kimeanza kulikamata jiji la Dar es salaam. Hakuwa na kasi kubwa kwa sababu palikuwa karibu, aliendesha mpaka alipofika kilipo kituo cha daladala zitokazo Mawasiliano, alisimamisha gari yake karibu na kituo cha polisi cha hapo akiwa anawaza sana maana moyo wake ulizidi kuingia wasiwasi huku akiwaza kama kuna ulazima awataarifu polisi lakini hakuona kama lingekuwa jambo la busara, alitakiwa kulimaliza mwenyewe.
Alikunja mkono wake wa kulia kuanza kuelekea ilipo hoteli hiyo, alitabasamu baada ya kuangaza upande wake wa kulia na kuwaona wazungu kadhaa wakiwa wanacheza tenisi ndani ya jumba moja la mazoezi wengine wakionekana kuwa gym. Ilichukua nusu dakika tu akawa hotelini hapo ambapo aliwaona watu wenye maisha yao wakitoka kwenye gari za kifahari kuingia hotelini kula maisha wengine wakielekea eneo ambalo bila shaka lilikuwa na kasino la hoteli hiyo. Alikunja kulia kuendelea na safari yake akiwa taratibu mpaka alipo fikia eneo ambalo aliambiwa afike hususani baada ya kuipita ile parking.
Palikuwa na utulivu wa kutosha japo upande wa kulia ambako kulikuwa na mijengo kama kawaida watu waliendelea na kujongea na magari yakiwa yanapishana kwenye barabara hiyo ya lami upepo wa bahari ukiendelea kupuliza na kuyafanya mandhari kuendelea kuwa bora kwa watu ambao walikuwa karibu. Alitazama saa yake ilikuwa ni saa mbili kamili usiku, akiwa amezama kwenye mawazo ya kuwaza kile ambacho kilikuwa kinaenda kutokea eneo hilo alihisi mtu yupo kwenye mlango wa nyuma wa gari yake akihitaji kuingia ndani hivyo ikamlazimu kufungua mlango huo na mwanaume huyo akauvuta na kuingia ndani ya gari bila kusubiri ruhusa ya mmiliki.
Alihitaji kugeuka ili amtazame mtu huyo ni nani ila alisita na kuinyoosha shingo yake baada ya kitu cha baridi kugusa kwenye kisogo chake, aligundua kwamba ni bastola na alikuwa akijua hatari ya silaha hiyo ndiyo maana alitii amri bila hata kuambiwa.
“Zima taa kisha zima gari” ilikuwa ni sauti kavu mithili ya mtu ambaye alikuwa amevuta sigara kwa miaka mingi bila kunywa maji ya kulainisha koo lake. Alitii taa zikazimwa na gari ikazimwa ukabaki ukimya wa kutosha.
“Wewe ni nani?”
“Ningetaka kujuana na wewe ningekufuata ofisini tukaja kuongea, umekuja hapa kusikiliza maagizo na sio kutaka kujuana na mimi”
“Una uhakika gani kwamba mimi naweza kukusikiliza?”
“Ungekuwa na hiyo jeuri usingekuja hapa saivi”
“Hivi unajua kwamba unacheza na mkuu wa kituo kikubwa hapa jijini? Hili jambo halitaisha vyema kwa upande wako, niambie wewe ni nani na kwanini umetumia picha ya mwanangu kuhusisha na jambo ambalo limenileta hapa?”
“Kwahiyo mpaka nakuita uje hapa unaona kama mimi sijui kwamba wewe ni mkuu wa kituo? Hiyo nafasi nina uwezo wa kukufanya utolewe kesho asubuhi tu ukarudi kuwa askari wa kawaida. Nimekuita hapa kuna kazi ambayo inabidi uifanye haraka “ Alimeza mate huku akiwa anasikiliza kwa umakini, mzaha wake ungeweza kumdhalilisha kwa mtu ambaye bado hakuwa amemjua ni nani hivyo akaamua kuwa mpole.

UKURASA WA 51 unafika mwisho.
 
HADITHI: NAFSI ZILIZO TELEKEZWA
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
WHATSAPP: 0621567672
AGE: 18+
UKURASA WA 52

“Wilson Ndamaru anatakiwa kufa kwa mkono wako na baada ya kukamilisha zoezi hilo hakikisha unapiga picha” jina ambalo alilisikia wakati huo lilimshutua kiasi kwamba alianza kuhema kwa shida. Mtu ambaye alitajiwa jina lake alikuwa ni bondia namba moja ndani ya taifa la Tanzania, bondia ambaye alipendwa na watu kwa sababu alikuwa mtu wa watu lakini alikuwa akisaidia watu wengi. Mbali na hilo mwanaume huyo alikuwa anajua kuitumia vizuri sanaa ya mikono yake ambayo iliwapa burudani machoni watanzania kila apandapo ulingoni ndani na nje ya nchi, halafu leo anaambiwa kwamba alitakiwa kumuua mwanaume huyo! Kivipi na kwanini? Hakujua.
“Hilo ni jambo ambalo haliwezekani”
“Una masaa arobaini na manane ya kufanya hivyo. Ni mwanao au Wilson utachagua wewe” Alibaki amehamaki akiwa hajui afanye nini, uchaguzi ulikuwa ni wake, amuue mwanaume huyo bondia ama mtoto wake auawe. Alikuja kushtuka wakati amebaki mwenyewe humo ndani, aliangaza kila sehemu hakumuona mtu ambaye alikuwa anaongea naye, hali hiyo ilimfanya ashuke kwenye gari na kuanza kuita kwa sauti akimtafuta mwanaume huyo kama mtu ambaye alikuwa amechanganyikiwa kwani alikuwa na maswali mengi ya kumuuliza ila kwa bahati mbaya hakupewa nafasi hiyo. Mwanaume huyo alikuwa ametoweka kwenye mazingira ya kutatanisha huku barabarani akiwa anamuona mtu mmoja mmoja ambapo kila mtu alikuwa ameshika yake kama ilivyo kawaida ya jiji hili kubwa.
Bwana Tyson alirudi nyumbani kwake akiwa mwingi wa mawazo kichwani, hakujua wale watu walikuwa ni akina nani hasa na sababu ya msingi ya kuhitaji bondia yule ambaye alikuwa kipenzi cha watu auawe. Alikuwa amepewa nafasi ya kuchagua kati ya kumlinda mtu huyo na kuiteketeza familia yake yeye jambo ambalo kiuhalisia lisingewezekana kwa sababu asinge ruhusu mtoto wake aweze kuuawa kwa kumlinda mtu mwingine hivyo maamuzi yake kichwani ilikuwa ni lazima alitekeleze zoezi hilo, kivipi?
Aliiangalia saa yake na kugundua kwamba ilikuwa mapema bado, saa nne usiku ndipo mshale wake wa saa ulipokuwa umegotea. Aliitafuta simu yake na kuingia kwenye mitandao ya kijamii, aliingia kwenye akaunti ya bondia huyo mkubwa kuweza kujua mpangilio wa ratiba yake ulikuwaje. Alikutana na taarifa ambayo ilipostiwa ndani ya nusu saa bondia huyo akidai kwamba angekuwa kwenye gym yake usiku huo kwa ajili ya kujiandaa na pambano lake na bondia kutoka Urusi ambalo lilikuwa linatarajiwa kutokea ndani ya wiki mbili zilizokuwa zinafuata.
Kulingana na maisha ambayo alikuwa nayo bondia huyo, hiyo ilikuwa ndiyo nafasi ya pekee kabisa ya kuweza kulitekeleza jambo hilo. Hakutaka kulaza damu, aliamka haraka na kuweza kujiandaa kwa kuvaa nguo za kawaida za mtaani na kofia kichwani mwake. Alihakikisha bastola ipo mahali pake kisha akatoka ndani kwake akihitaji kuelekea huko ambako alihisi kwamba angekutana na mtu huyo. Kwenye mikono yake alikuwa amevaa gloves nguvu, gloves ambazo alikuwa amepachika sindano mbili ndani yake, zilikuwa na kazi yake maalumu ya kutekeleza jambo lake kirahisi.
Alitumia dakika arobaini mpaka kufika ilipokuwa gym ya bwana huyo maeneo ya Masaki Dar es salaam. Palikuwa kimya mno huku walinzi kadhaa wakiwa wanaranda randa eneo hilo, walihitaji kumzuia kuingia ila alipowapa kitambulisho chake kuonyesha kwamba alikuwa ni askari basi walimruhusu aweze kuingia bila tatizo. Alimkuta bondia huyo akiwa anamalizia mazoezi yake ili aweze kuondoka na hilo jambo hakutakiwa kuliruhusu kabisa hivyo alicho kifanya ni kuomba mechi ya mazoezi na bondia huyo
Kwake ilikuwa kama heshima kuzichana na mkuu huyo wa kituo ambaye kila mtu alikuwa akimjua vyema jijini, hakupinga wakaingia ulingoni. Wakati wanavaa zile gloves za kupigania Kapombe alizivutia zile sindano zake kwa juu eneo ambalo alifunga plasta nyeupe, walianza kuzichapa wanaume huku wakiendelea kupiga stori mbili tatu mpaka pale ambapo bondia huyo alipigwa ngumi ya shingo na kuyumba kidogo. Alisimama vizuri ili kumkabili askari huyo lakini kwa mara ya pili tena alipigwa eneo lile lile na mara hiyo ya pili alihisi kama kuna vitu vimemchoma.
Kapombe alimuomba wamalize pambano hilo na kumsifu bondia huyo kwa ubora ambao alikuwa nao hivyo haikuwa vyema yeye kupoteza nguvu zake. Aliondoka ndani ya eneo hilo akiwa amemaliza kazi ambayo ilikuwa imempeleka kuifanya. Asubuhi ya kesho yake zilisambaa habari mbalimbali, habari ambayo ilikuwa mbaya baada ya bondia pendwa nchini kuzidiwa ghafla usiku wa manane.
Kuzidiwa kwake ndio ukawa mwanza wa taarifa mbaya ambapo saa mbili ya asubuhi kilitangazwa kifo chake ambacho kilikuwa cha ghafla huku madai ya kifo chake ikidaiwa kuwa ni sumu ambayo alichomwa. Walishindwa kupata ushahidi wa moja kwa moja kwani bondia huyo alikuwa akilindwa na alikuwa makini kwenye kila nyendo ambayo alikuwa anaipiga sasa hiyo sumu alichomwa wapi na nani? Hakuna kiashiria chochote ambacho kilionekana kuhusishwa na jambo hilo wakielezea tu kwamba jana yake usiku alifanya mazoezi ya kawaida na kucheza mechi ya majaribio ambayo haikuwa na madhara yoyote kwani mtu ambaye alicheza naye hiyo mechi alikuwa ni mtu wa kuaminika japo jina lake halikuwekwa wazi.
Mheshimiwa alikuwa kwenye ofisi yake wakati taarifa hiyo inatolewa kwenye vyombo vya habari, alikuwa anaendelea kushushia kahawa taratibu akiwa makini kusikiliza ili kujua kama kuna kosa lolote la kijinga alilifanya. Ilimuuma kuyakatisha maisha ya mtu huyo ila hakuwa na namna kwa sababu ya kuisaidia familia yake ndiyo maana alijikuta anafikia hatua hiyo. Akiwa kwenye dimbwi la mawazo simu yake ilianza kuita kwa fujo, aliipokea;
“Umefanya kazi nzuri japo umekosea masharti, nilikwambia unatakiwa kuupiga picha mwili wake ndipo tungemalizana hivyo tegemea nitakutafuta wakati mwingine nikikuhitaji” Alishikwa na ghadhabu, alitamani kumtukana mtu huyo wa upande wa pili wa simu lakini hakuwa na huo uwezo kwa sababu simu ilikuwa imekatwa tayari. Alilaani jambo hilo.



JACK THE LAWYER

Baada ya kutoka kukutana na Nicola alirudi nyumbani kwake, kichwa chake kilikuwa na mambo mengi ya kuyawaza, jambo kubwa ambalo lilikuwa linamsumbua ni kumsubiria mtu ambaye hakujua kwamba angekuja kumtafuta lini kwenye maisha yake na mambo yalikuwa yameanza kuharibika. Yeye kuanza kujulikana kwamba ndiye yule komando ambaye alipona Somalia ilikuwa ni hatari kwa sababu habari hizo zingekuja kujulikana kwa wananchi, kusambaa kwa habari hizo kungemharibia jina lake lakini pia lingekuwa suala la muda mchache yeye kuweza kuuawa kitu ambacho ndio ulikuwa mpango wake mkubwa.
Alikuwa anaendesha gari kichwa chake kikiwa kina mawazo mengi, aliongeza kasi ya gari ili kidogo kutuliza kichwa chake na kwa vile usiku huo barabara ilikuwa nyeupe basi kwake ilikuwa rahisi kutembea atakavyo. Alipofika nyumbani kwake geti lilikuwa wazi, alipigwa na butwaa kwa sababu nyumba yake ilikuwa inalindwa na walinzi wake wanne hivyo wasingefanya kosa la kijinga namna hiyo eti usiku wa manane wasahau nyumba ikiwa ipo wazi hivyo akahisi kabisa mazingira hayakuwa salama.
Alishuka akiwa makini bila kuingiza gari yake ndani, aliichomoa bastola yake mkononi na kuingia ndani ambapo hakuona dalili ya uwepo wa mtu. Jumba lake lilikuwa limetulia huku taa zikizidi kulipamba na kulifanya liendelee kumeta meta, aliangalia chini ya sakafu ndipo akashtuka baada ya kuona michirizi ya damu ikiwa inaelekea upande lilipokuwepo bwawa la kuogelea. Aliifuata damu hiyo mpaka karibu na hilo bwawa ndipo mbele yake alipoona wale walinzi wake wakiwa wamefungwa kwenye viti wakiwa wamechapika vibaya.
Aliangaza sehemu zote bila kuona mtu hapo ndipo akakumbuka kwamba kuna upande hakuwa ameuangalia ambao alikuwa anatumia kuhifadhia gari yake nyingine ya kifahari hivyo akageuka haraka upande ule ndipo alipo kiona kile ambacho alikuwa amekikusudia. Kuna mtu alikuwa ameketi kwenye kiti uso wake ukiwa umefunikwa na kofia, kwenye mkono wake kulikuwa na damu kiasi huku chini karibu na buti lake pakiwa na bastola mbili na katikati kukiwa na kisu ambacho kilikuwa kinang’aa kwa makali yake.

UKURASA WA 52 unafika mwisho.
 
HADITHI: NAFSI ZILIZO TELEKEZWA
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
WHATSAPP: 0621567672
AGE: 18+
UKURASA WA 53

Alimkadiria mwanaume yule huku akijiuliza kama alikuwa amepitiwa na usingizi au alimuweka yeye kwenye mtego.
“Umechelewa kurudi, ilibakia kidogo niweze kuwaua hao vijana wako kisha niondoke” sauti yale ilipenya vizuri kwenye masikio yake, ilikuwa ni sauti yenye ujazo wa kutosha na ni wakati huo ambao mwanaume huyo aliuinua uso wake. Yes, alikuwa ni yule ambaye alimsubiri kwa muda mrefu bila mafanikio ya kuweza kutokea mbele yake. Edison!
Hakuongea jambo zaidi ya kumwangalia kwa umakini, Edison aliinamana na kuokota silaha zake ambapo bastola alizihifadhi kwenye kiuno chake huku kisu akikifuta vizuri na kukipachika pembezoni mwa buti lake sehemu ambayo ilikuwa na sehemu ndogo kama ala ya kuhifadhia. Alizitupa hatua zake kuelekea kule ambako alikuwepo mwanasheria Jack bila hofu ila alisimama baada ya kuona mwenzake akiwa siriasi isivyokuwa kawaida, haikuwa sawa kama ambavyo alikuwa anatarajia yeye.
Alirudi nyuma hatua kadhaa baada ya kuona mwenzake anamsogelea kwa kasi akiwa na silaha mkononi, alikoswa kwenye shingo kukitwa na kitako cha bastola hali iliyo mfanya kuyumba mpaka kwenye kingo za lile bwawa la kuogelea na kumfanya ainame mithili ya mtu ambaye alikuwa anataka kudondokea ndani lakini alisimama vyema. Ngumi moja ilipenya kwenye tumbo lake ambalo alilikaza vilivyo hivyo haikumletea madhara, alikuwa bado amesimama eneo lile lile kuweza kukabiliana na mwenyeji wake.
Ilifika zamu yake kurusha ngumi, alirusha ngumi kumi mfululizo ambazo zilionekana kuwa mzigo kwa Jack, licha ya kujaribu kuzipangua hakufanikiwa, alipigwa kwenye mbavu ngumi nne ambazo zilimfanya kuhema kwa maumivu ambayo yalizama mpaka ndani ya mwili. Edison hakumsubirisha, sasa alikuwa anamfuata yeye, alitishia kama anajigeuza kwa mateke yake ye hewani ila hakufanya hivyo bali alijigeuza kwa mtama mkali ambao ulimpata vyema Jack ambaye alibaki anaelea hewani lakini hakuruhusu kufanya kosa la pili tena hivyo alijirusha kwa sarakasi na kutua chini.
Jack aliipachika bastola yake kiunoni na kuupanga mkono wake, alijitelezesha kwa kutumia mguu wake wa mbele ambao aliutumia kudanganyishia kisha akajirusha sarakasi ya mbele ambayo ilikita kwenye bega la Edison aliyekuwa amekomaa isivyo kawaida, nafasi ile ilimfanya Jack kuitumia vyema kwa kukita ngumi eneo la mbavu ambalo lilionekana kuwa na udhaifu kwa Edison kwani aliuma meno yake bila shaka lilikuwa ni jeraha la muda lakini kujiona kwake ameshinda alipigwa ngumi nyingi kifuani Jack kiasi kwamba alibaki anahema kama kuku mwenye kideli. Alijaribu kujikusanya ili arudi kwa bahati mbaya alipigwa na ngumi nzito mithili ya nyundo na kumfanya arudi nyuma hatua kadhaa akiwa anayasikilizia maumivu yake makali.
Hakukubali kupigwa, alihesabu hatua kadhaa akiwa anajiviringisha kama tairi kuja kwa kasi, alipiga mbele yake ambapo Edison alikuwepo, alijikuta amepiga hewa mpaka yeye mwenyewe akashangaa, mwenzake alikuwa pembeni yake ambapo wakati anageuka ili kumshambulia tena alipigwa na viganja viwili vikali kwenye masikio yake akahisi dunia inampigia kelele. Alipandwa na hasira akihitaji kujikakamua hivyo hivyo, alirusha mguu ambao ulipanguliwa na mguu mmoja wa Ed kisha mguu mwingine ukatua kwenye kifua chake na kumfanya adumbukie kwenye bwawa lake. Alizama wakati anajiinua alikuwa anatazamana na jicho la bastola.
“Sijaja hapa kupoteza muda wala kukuua, ningetaka kufanya hivyo mpaka sasa ungekuwa umekufa muda mrefu tu. Nimekuja hapa kupata majibu” Edison aliongea akiwa anampa mkono mwanaume huyo aweze kutoka humo ili wafanye kile ambacho kilimleta hapo. Jack alisimama na kuitoa ile sura ambayo ilikuwa kwenye uso wake, sura ambayo ilibakia ilikuwa ni ya Edison, kama mtu yeyote angefanikiwa kuwaona basi hakuna ambaye angeweza kuwatofautisha hata mama mzazi asingekuwa na huo uwezo, walifanana kwa kila jambo kiasi kwamba mpaka Ed mwenyewe akabaki ameduwa akimshangaa bwana huyo ambaye alimsoma vyema kwenye kitabu alichokuwa ameachiwa na Edward Pande.
Jambo hilo lilionekana kuwa la ajabu kwake yeye pekee, kwa mwenzake halikuwa geni wala halikuwa na shida yoyote ile, alisogea na kuwafungulia vijana wake kisha akamtaka pacha wake huyo amfuate ndani kwani walikuwa na mengi ya kuyafanya kwa pamoja usiku huo. Waliingia ndani ya jumba hilo la kifahari ambapo walishuka ngazi kuelekea chini, walikutana na lango kubwa la shaba, Jack alisogeza jicho lake na lango hilo likafunguka wakaingia huko ndani. Chini huko kulikuwa na chumba kikubwa ambacho kilikuwa na kila kitu, pembeni kulikuwa na vyumba vidogo vidogo ambavyo baadhi vilikuwa kwa ajili ya kufanyia matibabu na vingine vilijaa vitabu vya kutosha.
“Unataka tuanzie wapi?” Jack aliuliza akiwa anamkabidhi Edison matunda kwenye sahani naye akaketi pembeni yake.
“Haya yote umeyafanya kwa moyo wako au ulilazimishwa?”
“Mpaka umekuja hapa umekisoma kitabu na kama umekisoma basi unajua kabisa kwamba nimeyafanya haya yote kwa sababu ya mapenzi yangu binafsi na sio kulazimishwa na mtu”
“Kwanini?”
“Kwa sababu mimi nilikufa siku ile nilipo jitupa chini ya lile daraja”
“Lakini upo hai, umepata maisha mapya, kwanini usiitumie hii nafasi ukayatengeneza maisha yako badala ya kuigiza na kujitesa kunilinda mimi?”
“Jambo pekee ambalo namshukuru Mungu mpaka leo ni kwamba naenda kufa huku maisha yangu yakiwa yamekuwa na umuhimu wa kugusa maisha ya watu wengine, nimesimamia zaidi ya kesi hamsini na mbili na sijawahi kushindwa kesi hata moja. Sijawahi kusimama mahakamani kutetea wahalifu hata siku moja bali huwa nahakikisha haki inapatikana, hilo ndilo jambo kubwa kwangu zaidi hata ya kuhitaji kuwa hai na kuyaishi maisha ambayo hata sijawahi kuyapenda kamwe hivyo kile ambacho unakijua na sababu za mimi kuhitaji kufa ndilo jambo pekee ambalo nimelisubiri kwa hamu kwenye maisha yangu yote niweze kupumzika”
“Una mtoto?”
“Hapana”
“Ni muda gani utanichukua kuweza kurejesha kumbukumbu zangu zote?”
“Ni masaa kadhaa tu”
“Una mpango gani kwa sasa?”
“Kwa sababu umekuja basi nitakapo malizana na wewe nitaandaa mkutano wa vyombo vya habari ambapo nitajitambulisha kama mimi ni wewe na kuvumbua ule ushenzi wote ambao serikali imeufanya na watu ambao nawajua na baada ya hapo watanikamata na huku kuna watu watatumwa kuniua kwa sababu watajua kwamba mimi ni hatari kwao na hiyo ni nafasi ya dhahabu kwako kwani wataamini kwamba umekufa hivyo unaweza ukayafanya mambo yako kwa utulivu kwa sababu hawatakuwa na uhakika na uwepo wako japo unatakuwa kuwa makini mno kwenye hatua zako zote ambazo utakuwa unazipiga”

“Mimi ninaweza kuyafanya haya bila wewe kujitoa sadaka, tunaweza kuishi wote kwa pamoja na haya mambo yakaisha”
“Hiki ni kiapo ambacho nilikula kwa mzee kabla hajafa, ni ahadi ambayo kuitimiza kwangu ni zaidi ya kuwa hai hivyo utanisamehe kwa sababu siwezi kukitengua kiapo changu Edison”
“Sasa mpango unaanzia wapi?”
“Kwanza kabla sijakwambia mambo mengi, jambo la mhimu ambalo unatakiwa kulijua ni kwamba mama yako mzazi yupo hai na anaishi bado na hili nina uhakika nalo asilimua mia?”
“Mhhhhhh!!”
“Mama yako mzazi bado yupo hai na anaishi”
“Hilo ni jambo ambali haliwezekani, kama mama yangu yupo hai nina uhakika angekuwa amenitafuta kwa miaka yote hii!”

UKURASA WA 53 unafika mwisho.
 
HADITHI: NAFSI ZILIZO TELEKEZWA
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
WHATSAPP: 0621567672
AGE: 18+
UKURASA WA 54

“Mama yako inasemekana kwamba ni moja kati ya watu wenye nafasi za juu ndani ya jamii ya LUNATIC SOCIETY kwa miaka mingi kwa sababu ameifanya kazi yao kwa uaminifu mkubwa. Huyu mwanamke alitengenezwa akiwa chuo na umoja huo ili adili na baba yako mzazi tu hivyo alilengeshwa kwa baba yako ili aingie kwenye mtego wao na kweli baba yako mzazi alikuja kumpenda sana mwanamke huyo mpaka akafikia hatua ya kumuoa ila kwa taarifa zilizopo ni kwamba mama yako hakuwahi kuwapenda wewe na baba yako mzazi ila kwake ilikuwa ni kazi kama kazi zingine Edison” mwanaume alikuwa anauma meno yake huku akiwa anatetemeka, hiyo kauli ilimfanya ajisikie vibaya kwenye moyo wake yaani mwanamke ambaye alimbeba tumboni miezi tisa alikuwa hampendi? Kivipi? Kwanza alishangazwa sana na taarifa hizo za kuthibitisha kwamba alikuwa hai bado.
“Ni kwa muda gani unajua kuhusu hili jambo?”
“Ni kwa miaka kadhaa”
“Na mzee alikuwa anajua tangu mwanzo na alikuwa na uhakika?”
“Ndiyo”
“Kwanini hakuwahi kuniambia kwa kinywa chake habari hizi?”
“Alitamani uweze kuja kuujua ukweli wewe mwenyewe na ufanye maamuzi wewe mwenyewe juu ya nini cha kukifanya. Alihofia anaweza kukupa ushauri halafu baadae ukafanya maamuzi magumu ukamlaumu yeye hivyo mpaka sasa una uhakika kama mama yako yupo hai, ni jukumu lako kuamua kama utamtafuta na umhoji au kama hautahitaji kumfahamu basi huenda ipo siku unaweza ukamuua kwa mkono wako mwenyewe bila kujua”
“Hili jambo umeanza kulifanya kwa muda gani?”
“Tangu siku ya kwanza kuanza kuishika kalamu yangu kusimamia kesi kama mwanasheria, ndiyo siku ambayo nilianza kuchimba juu ya uwepo wa hawa watu”
“Kuhusu mke wangu?”
“Hilo jambo siwezi kuliongelea, utalikumbuka mwenyewe nitakapo kurejeshea kumbukumbu zako”
“Natakiwa kuanzia wapi?”
“Kwenye kumtafuta mama yako?”
“Ndiyo”
“Kwenye karakana ya taifa pale ya kutengenezea treni kuna mtu anaitwa Kanaani, mtafute huyo mtu umhoji kwa nguvu huenda anaweza akakupa mwongozo na njia ya safari ya kuweza kumtafuta mama yako mzazi japo aliwahi kufanya kazi na mzee atakuwa anajua baadhi ya mambo japo haitakuwa rahisi kuongea ndiyo maana itahitajika nutumia nguvu ikibidi”
“Tuhamie kwa baba yangu, unahisi yupo hai?”
“Sina uhakika ila naweza kusema baba yako ameshakufa muda mrefu tu ila ni jambo ambalo lipo kwenye vichwa vya watu wachache”
“Kuna lolote ambalo silijui kuhusu yeye?”
“Umeelezwa mambo yote kumhusu lakini jambo moja ni kwamba ile sumu ambayo yeye aliitengeneza daktari ambaye aliitumia kumuua raisi alikuwa hai mpaka usiku wa leo”
“Uma maana gani?”
“Nimeenda kwake kutaka kumhoji kwa sababu ni mtu ambaye amejificha kwa miaka mingi, nilipo pata taarifa za uwepo wake nilikwenda kumhoji kwa sababu angekuwa ndiyo njia rahisi ya kufikia nilipokuwa naelekea kutafuta ushahidi wa kuishtaki serikali lakini kwa bahati mbaya wakati nafika pale kuna mtu aliniwahi kama dakika kumi mbele na kumuua”
“Huyo mtu unamfahamu?”

“Hapana, sura yake sio ngeni kwangu ila sina taarifa zake. Inasemekana ni miongoni mwa watu ambao huwa wanafanya kazi za mauaji ya kulipwa kwa sababu historia yake ina utata kiasi chake kwani naye anaishi kwenye sura ya mtu mwingine kama mimi. Sura yake halisi haitambuliki na hiyo ambayo anaitumia ni ya mtu ambaye alishakufa miaka mingi ambayo imepita” aliongea huku akiwa anamuonyesha Edison picha ya Yohani Mawenge.
“Jina lake?”
“Yohani Mawenge anaitwa, juzi hapa ametoka huko Uganda ambako alijikamatisha mwenyewe”
“Kwanini afanye hivyo?”
“Kuna mtu alihitaji kumuua hivyo njia pekee ya kumfikia ilikuwa ni kujifanya yeye ni gaidi ndani ya nchi hiyo?”
“Alifanikiwa?”
“Ndiyo, shirika la kijasusi la Uganda limejaribu kuifanya siri habari hiyo lakini alifanikiwa kwenda huko na kumuua mtu wake ambaye alimfuata”
“Kwanini ajitoe sadaka namna hiyo kwenda kumuua mtu mmoja tu?”
“Baada ya kuona hili jambo limeanza kuwa wazi hususani kwa presha ambayo naipa serikali, wana wasiwasi kwamba siri zao zinaweza kuanza kuvuja hivyo kuna watu watakuwa wanakufa kipindi hiki hususani wale ambao walihusika kwa namna moja ama nyingine kwenye ufichwaji wa siri hizo”
“Na unajua hatua yao ambayo inaweza kufuata?”
“Ndiyo”
“Ipi”
“Nicola Aidan Semzaba ndiye binti ambaye nina wasiwasi kwamba siku sio nyingi anaweza kuuawa”
“Nililisikia jina lake, nadhani yupo upande wao sasa watamuuaje?”
“Huyu alidanganywa na watu hao akaamini kwamba wewe ndiye muuaji wa kaka yake lakini kwa sasa atakuwa njiapanda juu ya hilo hali ambayo itamfanya asiwe na umuhimu kwao tena”
“Bado sijakuelewa”
“Huyo binti amenitafuta muda huu baada ya mimi kuvujisha habari zile kwamba ndiye Edison mwenyewe, alitaka kuhakiki kwamba mimi ndiye nilimuua kaka yake kisha aniue pia na kisasi chake yeye kingeishia hapo lakini nimempa onyo juu ya watu wake na kumhakikishia kwamba mimi sikuhusika na hayo mauaji huku nikimuonyesha na sura hii kama ndiyo sura yangu. Nimemwambia kwamba watu hao wamepika taarifa za uongo kumhadaa yeye afanye mambo bila akili kuwasaidia kukamilisha kazi yao na yeye bila kujiuliza anaingia kichwa kichwa tu hivyo anatakiwa kujitathmini”
“Baada ya hapo akakuacha ukaondoka?”
“Hapana, asingeniacha hivyo nimemzimisha nikatoweka. Nina uhakika maneno ambayo nimemwambia yataanza kujirudia kwenye akili yake na baada ya hapo ataanza kuwachunguza wao wenyewe ili aweze kuupata ukweli na hapo sasa ndipo hatari kubwa kwake inapo zaliwa kwani wakisha gundua kwamba anawachunguza lazima watamuua kwa namna yoyote ile. Huyu binti kama akifa basi ujue wewe ndiye umemuua kwa sababu anaamini wewe ndiye muuaji wa kaka yake hivyo kuhangaika kote huko ni kwa ajili yako, moja kati ya majukumu yako ya kwanza kabisa ni kumlinda huyu binti kwa gharama yoyote ile”
“Namlinda vipi mtu ambaye hata hanifahamu, mtu ambaye sijui anaishi wapi?”
“Ili kumlinda basi inakulazimu uwe naye karibu”
“Unamaanisha?”
“Lazime uhakikishe anakupenda”
“Umelewa?”
“Ujivuni wa maisha ulinifanya nikayapoteza maisha ya watu kwa sababu kama zako, yule binti ni jukumu lako wewe, unatakiwa kuhakikisha anakuwa karibu yako na kukuamini kwa namna yoyote ile. Utajisikiaje labda kuyapoteza maisha ya mtu ambaye anaamini wewe ndiye muuaji wa kaka yake? Huoni kama utakuwa na hatia ya mauaji ya watu wawili wa familia moja kwenye moyo wako?”
“Yupo chini ya nani kwa sasa?”

UKURASA WA 54 unafika mwisho.
 
HADITHI: NAFSI ZILIZO TELEKEZWA
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
WHATSAPP: 0621567672
AGE: 18+
UKURASA WA 55

“Bado sijajua ila kuna taarifa nyingine kubwa ukiachana na hiyo”
“Ipi?”
“Novack Nyangasa inadaiwa mahali alipo panajulikana ila sasa kumpata mtu wa kukupeleka huko ndipo sijui anaweza kuwa nani”
“Unamaanisha yule ambaye alimuua kaka yake na kumuoa Irina?”
“Ndiyo”
“Hivyo huyo akipatikana anaweza kuwa na taarifa ya wapi alipo Irina Espanovich?”
“Haswaaa kwa sababu inasemekana kwamba walibahatika kupata watoto wawili ambao nao bila shaka mpaka sasa watakuwa watu wazima”
“Na kuhusu vifo vya wanajeshi walio enda Kongo?”
“Kuna frash ambayo uliipata kwa Issa bila shaka, ukiiangalia kuna taarifa za mhimu utazipata juu ya hao watu na unaweza kuwa mwanzo wako mzuri wa kupata hayo majibu ya maswali kama hayo”
“Kuna komando yeyote mwingine alipona Somalia?”
“Hapana”
“Mzee aliwaandaa watu kama wewe wangapi?”
“Tulikuwa wawili tu”
“Unamaanisha hata Issa amekufa kwa sababu yangu?”
“Ndiyo, kama ungewahi kukutana naye mpaka sasa angekuwa hai ila kwa vile ulienda kwa kuchelewa basi maisha yake yakapotea kwa sababu ya kulinda siri ambazo watu hao hawakutaka zitoke kwenye mikono yao na lengo kuu la Issa baada ya kupokea taarifa za mzee kuuawa siku ile kanisani aliamua kutaka kutoweka jijini ndipo kwa bahati mbaya akaweza kuuawa”
“Kwahiyo kwa sasa natakiwa kufanya nini na natakiwa kuanzia wapi kulitekeleza jambo hili?”
“Kwa sasa unatakiwa uishi kama haupo kwa sababu mimi naenda kufa hivyo taifa zima litaamini wewe haupo. Wakati ambao utakuwa unafanya hivyo unatakiwa umtafute Nicola kwani atakuwa kwenye hatari kubwa, hilo litaenda sambamba na wewe kukitafuta kikosi cha siri kutoka ndani ya shirika la kijasusi (IBA) kiitwacho RIGHT HAND ambacho ndicho kimekabidhiwa hii kesi kuisimamia. Jana kiongozi wao amekuja ofisini kwangu na kwa maelezo yake ni wazi kuna mengi hata wao hawayajui hivyo huenda viongozi wao wanahitaji kuupindisha ukweli kwa kigezo cha kuzuia vurugu. Kama hawa wakikuelewa basi wanaweza kuwa msaada mkubwa kwako kwa hapo baadae kwani unashindana na watu wa hatari na sio mtu mmoja bali ni mfumo mzima”
“Una taarifa za huyo kiongozi wao?”
“Anaitwa Aaliyah Beka”
“Mbona kama wa kike?”
“Ni wa kike ndiyo ila ni binti hatari isivyo kawaida, anawaongoza wanaume wengine wa shoka watatu na ndio watu ambao wapo karibu na mkurugenzi wao”
“Hilo nitalifanyia kazi, nahitaji taarifa za tukio ambalo lilitokea uwanja wa ndege juzi”
“Aliye tekwa siku ile ndiye huyo Nicola wakati anafanya mpango wa kukutana na watu hao ili aungane nao kwa ajili ya kukuua wewe lakini mmoja wa watu ambao alikuwa pale ni mwanajeshi ambaye alikufa miaka miwili iliyopita”
“Kama alikufa, ameonekanaje?”
“Aliigiza kifo chake”
“Kivipi na kwanini?”
“Alikuwa amekwenda na wenzake huko Somalia kwa oparesheni ya kijeshi lakini kwa bahati akawa ameonekana kuwa wa mhimu kwa muda mrefu na jamii ya LS hivyo walikuwa wanatafuta namna nzuri ya kumfanya kuwa wao bila kuacha ushahidi kwa upande wa serikali na ndipo walipotengeneza kifo feki cha mtu huyo na kuwaua wenzake, aliuawa mtu mwingine ndiye akatengenezewa sura bandia hivyo nchi iliamini kwamba amekufa ila ni mzima kabisa yupo hai. Jina lake anaitwa Damasi Kazimoto, ni mzaliwa wa Tambani Mkuranga na familia yake ipo huko yote, sijawahi kutenga muda wa kumtafuta ila ni mtu mhimu mno kwenye safari ya kazi yako hivyo ukitaka kumpata unatakiwa kumteka baba yake mzazi, atakuja popote pale ambapo utahitaji aweze kufika”
“Unahisi anaweza kuwa msaada kwangu au natakiwa kumuua?”
“Kwa ushauri wangu, kuna muda inabidi ucheze nje ya box sio kila mtu unatakiwa kumuua, unatakiwa umpate mtu hata mmoja ambaye ni wa maana kwako anayefanya nao kazi huyo anaweza kukufikisha kule ambako unataka kufika kirahisi kwa sababu yeye ana uwezo wa kufanya nao mawasiliano muda wowote ule”
“Unahisi anaweza kukubali kuwasaliti watu ambao wanaweza kuua familia yake muda wowote?”
“Sasa hapo atachagua yeye kama aendelee kufanya kazi kwa umakini na kuilinda familia yake au wewe uiteketeze familia yake muda huu”
“Basi huyu anaweza akanifaa, natakiwa kumuacha akiwa hai” Wanaume hao wawili walitumia masaa sita kuweza kuzungumza kwa kina. Jack alimwambia mambo mengi Edison ambayo alikuwa hayajui hususani wakati ambao alikuwa kwenye kizuizi kizito cha kumbukumbu zake. Alipewa taarifa nyingi za mhimu ambazo zilikuwa zinakwenda kuwa msaada mkubwa wa kipindi ambacho angebaki mwenyewe kwani Jack alikuwa ni kama star wa huo mchezo lakini kuanzia siku hiyo alikuwa na muda mchache wa kuweza kuwa hai hivyo Edison alitakiwa kujiandaa kwa kila kitu kimpango wake mwenyewe bila kuwaza kuhusu msaada wa Jack tena.
Vitu vyote hususani miliki za mali zote ambazo aliziacha marehemu babu yake sasa zilikuwa chini yake na kila kitu ambacho kilikuwa chini ya Edward Pande na JACK THE LAWYER vilikuwa vipo chini yake kwani viliandaliwa kwa muda mrefu kwa ajili yake yeye. Baada ya mazungumzo ambayo yalichukua muda mrefu kukamilika, zoezi ambalo lilifuatia kwa wakati huo lilikuwa ni kuweza kumrejeshea kumbukumbu zake kwa njia ya upasuaji ambao ulichukua masaa mengine kumi na matano mpaka kukamilika kwa kila kitu.
Baada ya muda huo kupita, kichwa chake kilikuwa kizito alipo amka kwa sababu vitu ambavyo vilipunguzwa vilikuwa vimerejeshwa, alikuwa amekumbuka kila kitu ambacho kiliwahi kumtokea kwenye maisha yake. Alielewa sababu ya msingi ya Edward Pande kuweza kuzitoa kumbukumbu hizo kwa sababu zilianza kumtesa, nyuma yake zilikuwa na maumivu makali ambayo mengine hakutamani hata kuendelea kuyakumbuka ila hakuwa na namna zaidi ya kuukubali ukweli huo na kujua namna ya kuweza kuushinda.
Jack alikuwa amemuacha pekayeke ndani ya chumba kikubwa ambacho kilizungukwa na vioo kila kona, lengo la kumuacha pekeyake ni kumpa muda wa kuweza kukumbuka kila ambacho kilitokea na kupata muda wa kuyatafakari maisha yake. Ile picha ya mwanamke mrembo ambayo kwa mara ya mwisho alikuwa akiishangaa na kujiuliza kwanini ilikuwa mfukoni mwake kwa miaka mingi, ilikuwa ni picha ya mkewe kipenzi ambaye wakati anasafiri kwenda Somalia alimuacha akiwa mjamzito tena chini ya ulinzi wa Edward Pande lakini mrembo huyo hakuwa hai tena, alikuwa amekufa na sio kufa tu bali alikufa na mtoto tumboni. Hiyo haikutosha mashababi wakaamua kumbaka mkewe bila huruma kisha wakayachukua maisha yake.
Alijiona mjinga kwa kushindwa kuilinda familia yake mwenyewe, mkewe na mtoto huenda wangekuwa hai mpaka wakati huo na yeye angeitwa baba. Umri ulikuwa unaendelea kumsaliti asijue hili wala lile lakini muda ulimpa kumbukumbu sahihi za maisha. Alipiga ngumi nyingi ukutani kwa hasira, hakujali wakati vioo vilipokuwa vinamchubua mikono yake, aliona huenda damu kumtoka ingekuwa ni njia sahihi zaidi ya kuweza kutuliza hasira zake huenda maumivu yangepoa kwani alihisi ndani yake kuna mtu anauvuruga moyo wake na pasi ya umeme. Hakika aliapa kwa kila ambaye aligusisha mkono wake kwenye jambo hilo, asilani! Asingeweza kuishi yeye akiwa bado anahema.

UKURASA WA 55 unafika mwisho.
 
Back
Top Bottom