Tukibaki Hai, Tutasimulia

Tukibaki Hai, Tutasimulia

TUKIBAKI HAI, TUTASIMULIA - BONUS


Na Steve B.S.M





Usiku haukuwa umeisha, ndo' kwanza ilikuwa saa nne ya dakika za mapema. Richie alitoka kuoga akiwa anajifutafuta na taulo, amevalia nguo ya ndani rangi ya machungwa, miguu yake myembamba ipo wazi ikipuyanga na vinyweleo.

Alipomaliza kujifuta alitupia taulo kitandani kisha akaenendea mafuta ya ngozi, alichovya kidole lakini kabla hajajipakaa simu ikaita. Hakujua simu ipo wapi, alisahau alipoiweka, akarusha macho yake hapa na pale bahati akaiona, ilikuwa kwenye kona ya kitanda, shida nguo zilikuwa zimetanda sana kana kwamba kitanda kimechapwa na bomu, akainyaka simu hiyo na kuitazama, alah! Alikuwa ni Jamal, akastaajabu ni nini muda huu?

"Hello!" Akasema akiketi kitandani, "... Saa hii? ... Serious? ..." Simu ikakata, akatahamaki kwa sekunde, upesi akajivika suruali na shati, nguo zote hizo aliziokota kwenye kile kifurushi kilichokuwepo kitandani kwake, sijui kama nguo hizi zilikuwa safi au lah, alishuka chini upesi na alipofika nje ya ghorofa hili analokaa aliangaza na kidogo tu akamwona Jamal, mwanaume huyo alikuwa amesimama akiegemea moja ya gari, kwa namna alivyoegema hapo unaweza kudhani huo usafiri ni wake, alipomwona Richie anamjia akasimama.

"Ni nini hiko muda huu?" Aliuliza Richie, Jamal kabla hajaongea akatazama kwanza pembeni yake kana kwamba mtu anayehofia usalama wake kisha akasema,

"Richie, najua hili litakuwa 'too much' kwako lakini naomba unisaidie, tafadhali."

Wakati huo wa mazungumzo yakiwa yanaendelea, kuna mtu fulani alikuwa akiwatazama ndani ya gari.

Mtu huyo alitazama vinywa vya watu hawa na kwa kuutumia mkono wake wa kushoto akawa ananakili jambo kwenye 'notebook' yake, alilifanya zoezi hilo kwa sekunde kadhaa kisha akaifunga notebook na kuiweka kwenye 'dashboard'.

Muda mchache ulofuatia, kama dakika zisizozidi tatu, Jamal akamwona mtu fulani akiwa anaingia ndani ya jengo hili la ghorofa, mtu huyo alikuwa mrefu amevalia 'hood' nyeusi iliyofunika kichwa chake, mikono yake ameizamisha kwenye hood hiyo, mwendo wake wa kasi ya wastani, kichwa amekiinamishia chini.

Jamal hakumjali sana bwana huyo kwani hapa wanaishi watu wengi sana, ni ghorofa yenye 'floors' nyingi na vyumba vingi pia, akamchukulia kama mkazi tu wa eneo hili, akapuuza na kuendelea na maongezi yao kama kawaida, baada ya dakika mbili maongezi yakasimama kwa Richie kusema,

"Ningoje hapa, simu yangu niliiacha ndani."

Bwana huyo akatoka zake kuelekea ndani, alikwea ngazi upesiupesi, akashika korido na kuimaliza haraka, kidogo tu huyu hapa mlangoni mwake, chumba namba 43, akachomoa ufunguo mfukoni mwake na kuuchomeka kwenye kitasa, mara mlango ukafunguka wenyewe! Akahamaki, ina maana sikuufunga mlango kwa funguo? Alisema na nafsi yake, akausukuma mlango na kuingia ndani, akatazamatazama, akajiaminisha kila kitu kipo shwari, akaelekea chumbani kwake kuichukua simu iliyomleta huku.

Aliufungua mlango akayatupia macho yake kitandani, akaiona simu, lakini nyuma ya mlango kulikuwapo na mtu amesimama hapo na yeye hakuwa anafahamu jambo, akaichukua simu yake na kuiweka mfukoni, kugeuka, kabla hajaondoka hapa, akashuku kitu mlangoni.

Aliutazama mlango kwa sekunde tano, kuna kivuli kilikuwapo hapo, kivuli kisichoeleweka, moyo ukaguta, haraka akili yake ikamkumbusha yale ya mlango kuwa wazi, hofu ikamvaa, alihisi mwili mwake umepitwa na baridi fulani jepesi ambalo halieleweki, akaupiga moyo konde, mimi ni mwanaume, alisema na nafsi yake, akausogelea mlango taratibu, alipoufikia, katika kiza cha kivuli kile, akaona kiatu cha mtu, buti kubwa jeusi, moyo ukaita pah!


....


Jamal alitazama saa yake ya mkononi, muda ulikuwa umeenda, toka Richie amemuaga kwenda kuchukua simu sasa yapata nusu saa, akajiuliza bwana huyo anafanya nini muda wote huo? Alingoja kidogo, mwishowe akakata shauri kwenda kumwona.

Aliingia ndani akashika ngazi, alizikwea haraka akiziruka mbilimbili, muda si mrefu akawa ameishika korido ya kumpeleka kwa Richie, alipopiga hatua nne akamwona bwana yule aliyevalia hood nyeusi, bwana huyo alikuwa anamjia, uso wake, kama kawaida, ulikuwa unatazama chini, mikono yake ipo ndani ya nguo yake hiyo.

Jamal alimzingatia bwana huyu lakini hakuambulia kitu, hakumwona uso wala hakujua ngozi yake, alichoambulia ni harufu tu wakati akipishana naye, alimsindikiza kwa macho mpaka alipokata kona na kutokomea zake.

Alipofika kwenye mlango wa makazi ya Richie akagonga, kimya, akagonga tena lakini mara hii mlango ukafunguka wenyewe, akashangaa, akausukuma mlango huo na kuingia ndani, akaangaza, hamna kitu, akaita lakini napo kimya, akarudia kuita mara tatu, bado kimya, akaanza kuingiwa na hofu, kutazama mlango wa chumbani upo wazi, taratibu akaujongea na kuusukuma, lah! Akamwona Richie akiwa amelala chini!

"Richie!" Aliita lakini bwana huyo hakuonyesha dalili ya uhai, alikuwa ametulia tuli kana kwamba maiti ndani ya jeneza, upesi akamsogelea na kumtikisa, akampima mapigo yake ya moyo kwa masikio, akabaini bwana huyo alikuwa hai ila ni ufahamu amepoteza, basi upesi akatoa simu yake mfukoni na kupiga 911 kwaajili ya kuomba msaada wa dharura.


......


"Hallo!" Redio ndogo ilitamka ndani ya gari, "kuna mtu amezirai hapa, na mapigo yake ya moyo yako chini sana!" Redio iliendelea kutamka, na bwana aliyevalia hood alikuwa akiskiza kila jambo, ametulia kwenye kiti cha dereva alichokilaza chini kiasi.

Maongezi yaliendelea kidogo katika redio kisha kukawa kimya, baada ya dakika chache sana sauti ya king'ora ikaita kwa mbali, sauti hiyo ikawa inaongezeka kadiri na muda unavyozidi kwenda, kidogo tu eneo hili likaanza kuwakawaka kwa rangi nyekundu na bluu, mara 'ambulance' hii hapa, watu wawili wakashuka upesi na kwenda ndani ya ghorofa hili.

Wakati haya yanatokea, bwana yule mwenye hood alikuwa anatazama kila kitu. Muda si mrefu wale watu waliongia ndani wakatoka na mwili katika 'machela' yao, nyuma wakifuatwa na Jamal. Ilipofikia hapo, bwana huyu ndani ya hood akawasha gari yake na kuondoka zake, akiwa anaenda, Jamal akalikodolea gari hilo ambalo lilikatiza kwa ukaribu kwa kasi yake ya wastani lakini hakuambulia kitu, gari lilikuwa na vioo vyeusi ti, alichobaini ni gari hilo halikuwa na namba zozote za usajili.


***


Uwanja wa Kimataifa wa New York, saa tano asubuhi.


Taksi yenye rangi nyeupe iliingia katika eneo la uwanja wa ndeges ehemu mahususi kwaajili ya kupakulia wateja. Taksi hiyo ilisimama akashuka mwanamke fulani aliyevalia mithili ya walimbwende, nywele zake ni ndefu na ni nyeupe pe, miwani yake ya jua iliziba karibia robo ya uso wake, 'lips' zake zilikuwa zinang'aa na zimelowana, hakika alivutia.

Mwanamke huyu ambaye mwonekano wake ni mpya kabisa machoni petu alikuwa na mwendo mithili ya twiga mwenye kufuata maji ya mtoni, alitembea pasipo papara, kila hatua akiihesabu, kila alipokatiza kati ya watu alionekana wa tofauti kwa namna alivyonawiri, na yeye ni kama vile alilitambua hilo, akaringa.

Mkoba wake wa thamani uliokuwapo begani ulitetemeka, akaufungua na kutoa simu yake, akaitazama kwa kusimama, akatazama nyuma na pembeni yake kisha akapokea simu hiyo,

"Naam," alisema kisha akaendelea na mwendo, mwendo wa madaha kama kawaida, alizungumza na simu hiyo kwa hatua kama tano hivi kisha akasimama, akauliza,

"Umetuma saa ngapi?"

"Tazama kwenye barua pepe yako, utaona," sauti ilimjibu upande wa pili kisha simu ikakata, kabla hajapiga hatua nyingine akafungua 'inbox' ya barua pepe yake, huko akakutana na 'links' mbili za mtandao, akapiga simu.

"Nimeona," alisema kisha akakata simu yake na kuirejesha kwenye mkoba alafu akaendelea na safari yake, baada ya mlolongo mfupi wa abiria akawa sehemu ya ukaguzi, hapo alikuwapo mwanamke mmoja wa makamo ya miaka arobaini, amevalia miwani ambayo ameishusha chini ya pua, macho yake ni kuyarembua lakini kayakaza kuwatazama abiria, ukimtazama vibaya waweza sema anatazama kwa madharau.

Aliipokea 'passport' ya mwanamke huyu kisha akaikagua kwa macho yake, alipomaliza akamtazama mwanamke huyu na kumwamrisha avue miwani yake, mwanamke akatii, akaivua na kumtazama, alikuwa na macho ya kijani, sawa sawia na picha ilokuwepo kwenye 'passport' yake, basi mkaguzi alipojiridhisha akamruhusu aende zake, mwanamke huyo akatabasamu akirudishia miwani yake usoni kisha akasema,

"Tchao!"

Akaenda zake kwa mwendo wake wa madaha, mkononi mwake alikuwa amebebelea tiketi ya ndege kubwa ya Uchina, ndege zao la Boeing yenye uwezo wa kubeba abiria lukuki, humo alijikalia katika kiti cha dirishani na safari ikaanza si muda, ndege ilipong'oa nanga kuidaka anga mwanamke huyu alishusha pumzi ndefu, hatimaye aliiacha ardhi ya Marekani.

Baada ya masaa na masaa ya kudumu angani, hatimaye ndege hii kubwa ilitua salama ndani ya Taiwan katika uwanja wa kimataifa wa Taoyuan, kutokana na utofauti wa ukanda wa muda ulokuwepo baina ya pande hizi mbili, yaani New York na Taipei, Taiwan, ndege hii ilifika katika muda salama kabisa, jua linaangaza vya kutosha, mwanamke huyu akapokelewa na mwanaume aliyekuwa anamngoja muda wote huo, mwanaume huyo alikuwa ameegamia gari kubwa nyeusi, modeli ya Alphard, alipomwona mwanamke huyu alimtambua upesi akampungia mkono, mwanamke akamjia.

"Muda mrefu hatujaonana!" Mwanaume huyo alimpokea mgeni wake kwa kumkumbatia, hapa kwa karibu ndo' akaonekana vema, alikuwa ni Taiwan, mwanamke alipoingia ndani ya gari akavua wigi lake na kunyofoa sura bandia alokuwa amebandika, hapo akawa mtu mpya kabisa! Usingeweza sema ni mwanamke yule tuliyemwona kule New York, walikuwa watu wawili tofauti, wa kule ni mwanamke mgeni machoni petu ila huyu wa sasa ni mwanamke tunayemfahamu, mwanamke tuliyemwona si mara moja ama mbili, alikuwa ni Mitchelle!

Aliuliza,

"Kila kitu kipo sawa?"

Taiwan akamjibu, "sawa sawia."

Mitchelle akasema,

"Nataka kuwaona Truce na Kiellin. Tunyookee huko saa hii."

Taiwan akakaa kimya.

"Umenisikia?" Mitchelle akauliza.


***
Tuko bega kwa bega[emoji123]
 
TUKIBAKI HAI, TUTASIMULIA - 31


Na Steve B.S.M




SUV nyeusi iliposimama, mwanaume aliyevalia suti na tai nyeusi alishuka upesi akafuata mlango wa nyuma na kuufungua, akatoka bwana mkubwa. Kidogo mlango mwingine ukafunguka akatoka mwanaume maridadi ndani ya suti, alikuwa ni Babyface, na yule bwana mkubwa aliyefunguliwa hapo mwanzo alikuwa ni mkubwa wake wa kazi, mkubwa ambaye huwa anakuwa naye mara kwa mara, bwana huyo kwa sifa ni mtulivu na asiyeongea maneno mengi, pengine hekima za uzee zilimzidia, hutanguliza akili kuliko mdomo, hamna anayejua.

Bwana Babyface pamoja na bwana huyo waliingia ndani ya jengo ambalo kwa nje walipokelewa na maafisa wengine wa usalama, kwa haraka kama watano hivi, walikuwa wako 'alerted, wanatazama huku na kule kutazama na kuhakikisha usalama wa jengo hili, na hawakuwa wenyewe, kwa mbali pia walikuwapo wengine ambao ukiwatazama tu kwa jicho la umakini utabaini ni wana usalama, wanarandaranda huku na kule.

Babyface alipanda lifti ya jengo hili pamoja na mkuu wake, walikuwa wawili tu ndani ya lifti na huu ukawa wasaa wao mzuri wa kuzungumza baadhi ya mambo.

"Nategemea kila kitu kitaenda sawa," Mkuu akasema akivutavuta koti lake kwa kulitengenezea, "Kama jambo hili likikoma, basi nitastaafu kwa heshima, nikilishindwa itabaki kuwa fedheha maishani mwangu."

Aliposema hayo akamtazama Babyface na kumuuliza,

"Unadhani nitafanikiwa?"

Babyface hakujibu kwa kinywa, badala yake akainamisha kichwa chini, Mkuu akashusha pumzi ndefu na mara mlango wa lifti ukafunguka, wakatoka, wakaongozana mpaka kwenye chumba maalum, chumba kikubwa cha kufanyia mkutano, humo wakakuta kuna watu wawili waliovalia kombati za kiofisa wa jeshi, muda si mrefu baada ya kufika hapa, chumba hicho kikajawa na watu kadha wa kadha wenye wadhifu mkubwa katika mambo ya usalama, watu hao walikuwa wamekaa kuizingira meza kubwa lakini kiti cha mkubwa wa kikao hiki bado kilikuwa wazi.

Kidogo king'ora kikalia, gari lilimleta mtu, ndani ya muda mfupi mtu huyo akawa amefika, alikuwa ndo' mkubwa wa kikao hiki, waziri wa ulinzi wa taifa hili, bwana Logan Diff, mwanaume mrefu shupavu, nywele zake mchanganyiko wa rangi nyeupe na nyeusi, mwili wake mkakamavu na umenyooka kimazoezi, hatua zake ni kamilifu akitembea kuonyesha amepitia mafunzo ya jeshi, kisigino ndo' kinaanza kugusa chini kisha mguu mzima, amevalia shati la bluu bahari, amelikunja mikono yake.

Bwana huyo alipoingia katika ukumbi huu, wote wakasimama, ni mpaka alipoketi yeye ndipo na wengine wakaketi kisha kikao kikaanza, muhtasari wa kikao ulitajwa na mada iliyowakutanisha hapo.

Bwana Logan Diff alikabidhiwa faili lenye nyaraka za siri, faili lenye jalada la jeusi huku likiwa na chapa nyekundu ya neno CONFIDENTIAL, akalipitia faili hilo kwa umakini, uso mkavu, kwa dakika mbili, kisha akaliweka faili hilo pembeni na kumtazama bwana yule aliyekuja akiongozana na Babyface, kwenye meza yake kulikuwa na kijibao kilichoandikwa jina lake, na ilikuwa hivyo kwa kila mtu aliyeketi hapa, mbele yake kilisimama kibao kinachomtambulisha jina kamili, kwa mkuu wa kazi wa Babyface kibao chake kilisoma Brendan Garret, afisa mwandamizi wa taasisi ya CIA.

"Garret," Logan aliita kisha taratibu akaanza kuaeleza mambo yahusuyo oparesheni ambayo ilipatiwa jina la oparesheni BALTIKA.

"Bwana Garret, kwa sahihi yako mwenyewe mnamo mwaka 2005, ulihitaji serikali iidhinishe mkakati wako wa kuwatengeneza binadamu bora zaidi kwaajili ya mapambano ya nje ya nchi, kwa maelezo uliyoyatoa, watu hao watatumika kama mbadala wa taifa letu kupoteza wanajeshi lukuki katika uwanja wa mapambano, mkakati kabambe kabisa, serikali ikaidhinisha na kuupitisha mkakati huo baada ya mapitio, mabilioni ya dola yakatolewa kwaajili ya kuufadhili, lakini baada ya vita tano kubwa, huko Iraq, Afghanistan, Syria, Sudan na Somalia mkakati wako ukashindwa kuonyesha matunda baada ya watu wako kubadilika, haukuweza kuwamudu tena kama hapo mwanzo, ikabidi wateketezwe, sio?"

Garret akatikisa kichwa kukubali maelezo hayo yote, Waziri Logan akaendelea kutoa taarifa kwa kutumia kumbukumbu ya kichwa chake,

"Jambo hili ni la siri, Garret, lazima kila kitu kisafishwe huku chini, laiti nisingefanya hisani ya kiubinadamu basi unajua mambo yangekuwa magumu zaidi lakini shida ni kwamba unanifanya niwe katika wakati mgumu, wa kujutia hisani yangu ...."

Alipofikia hapo akaweka kituo kikubwa, akanyanyua glasi ya maji iliyokuwapo pembeni yake na kunywa mafundo mawili makubwa kutibu koo lake kavu, alipofanya hivyo akaendeleza maneno yake kwa utaratibu kabla ya kwenda kwenye hukumu,

"Katika vita ya mwisho, kwa maelezo ambayo taasisi yako iliyatoa, Bwana Garret, hao watu waliuawawa wote, hakuna aliyebaki, chanzo kikiwa milipuko mikubwa ya mabomu, lakini ...."

Akavuta faili jingine na kutazama, faili hilo lilikuwa limetokea upande wa kitengo cha Polisi, akafungua moja kwa moja ukurasa nambari sitini na mbili, hapo kulikuwa na picha kadhaa pamoja pia na maelezo, hakuyasoma, yalishakuwa kichwani, alishajua kilichopo hapo, akalisogeza faili hilo kwa Garret kisha akaendeleza maneno Garret akiwa anatazama faili alilosogezewa karibu,

"Sidhani kama maelezo yako yalikuwa sawa, Garret, kwa mujibu wa picha hiyo katika faili za polisi, mwanamke huyo yuko hai na yuko mtaani, nadhani unamfahamu sivyo?"

"Ndio."

Logan akaongezea, "huyo ni 00/89/31/12 CKM. Imekuaje bado yuko hai?"

"Tulibaini hili jambo si muda mrefu," Garret aliteta, "tulistaajabu yupo mtaani na ..."

"Na akawa tayari ameshaua!" Logan akamkatisha. "Si ndivyo?"

Garret hakujibu, alinyamaza akitazama meza.

"Alafu mnaleta hapa maelezo ambayo hayajitoshelezi kabisa, Garret, unafahamu wazi kuwa watu hawa ni hatari, kama mlishindwa kuwamudu, raia wa kawaida huko mitaani wataweza? Haya maafa tutambebesha nani lawama? Nani anayejua kitakachofuatia baada ya hiki? Na nani anayejua kama kuna wengine zaidi ya mwanamke huyu huko mtaani?"

Logan alifungua faili jingine toka polisi, akalipitia kwa ufupi kisha akampatia bwana Garret kwa kulitupia mezani, faili hilo lilijawa na picha nyingi sana, picha za mauaji kadha wa kadha, picha ya maiti ya Ronelle, Travis, pamoja pia na picha ya ajali mbaya iliyommaliza Mpelelezi huko San Fransisco, hapo Logan Diff akasema,

"Mpelelezi huyo alikuwa anafuatilia mauaji yaliyotokea The DL, mauaji aliyoyafanya 00/89/31/12 CKM. Huyo mwanamke Ronelle alikuwa katika orodha yake ya upelelezi, akaishia kufa, huyo Travis kwa mujibu wa maelezo yake ya mwisho ya simu, aliongea na Mpelelezi, bila shaka ni kuhusu kesi hiyo ya The DL, naye akafa, na mwisho wa siku Mpelelezi mwenyewe akapata ajali, hit and run, una lolote la kutuambia kuhusu haya? Huu ni mkakati wenu wa kuzuia taarifa zenu kwenda kwa umma? Kwahiyo watu wenu wanaua na nyie pia mnaua?"

Garret aliipotaka kufungua mdomo wake kujitetea Logan alibamiza meza kwanguvu kumkatiza kisha akamkodolea macho ya ukali na kusema, "ulifanya kazi kubwa sana, Garret, hamna asiyefahamu hilo katika nchi hii, lakini kwa hili, unaenda kufuta 'legacy' yako yote uliyoijenga kwa damu na jasho!"

Baada ya kitambo kidogo ya kikao kumalizika, Bwana Garret alikuwa kwenye gari lake akiwa amezama ndani ya fikra, kichwa chake alikiegamiza kwenye dirisha macho yake yakitazama nje, pembeni yake Babyface aliketi akimtazama, alifahamu muda ule haukuwa sahihi kumwongelesha mkuu wake wa kazi ijapokuwa alitamani sana, basi akaishia kujihifadhi kifuani.

Gari lilienda kwa mwendo wa kilomita chache, liliposimama kupisha taa nyekundu ya barabarani, bwana Garret akaongea akiwa bado amelaza kichwa chake kwenye dirisha,

"Unafahamu chochote kuhusu mauaji ya wale watu?"

Garret aliuliza akilenga vifo vya Travis, Ronelle pamoja na Mpelelezi, kuna jambo alikuwa analipambanua kichwani mwake, jambo ambalo bado lilikuwa na kiza kinene, kabla Babyface hajajibu swali hilo akanyanyuka upesi na kumtazama kwa kuyakaza macho, akaongezea swali,

"Ulishiriki kwenye hayo mauaji?"

Babyface akajikuta anayakodoa macho yake kwa mshangao, hakutarajia swali hilo ghafla kiasi hiko.


***


Metropolitan Hospital, New York, asubuhi ya saa nne.


"Unaweza kumwona hivi sasa, amesharuhusiwa," mhudumu aliposema hivyo Hilda akashika zake njia lakini kabla hajafika popote akamwona Richie akiwa anakuja, mwanaume huyo alikuwa amekunja sura yake kana kwamba ametoka kulamba ndimu kali, mwendo wake pia ulikuwa wa taratibu akijikongoja, basi Hilda akamfuata na kumshika mkono ili apate kumsaidia, Richie akamshukuru kwa kuja kumjulia hali, wakaongozana mpaka nje ya hospitali ambapo walisimamisha taksi kwaajili ya safari, walipokwea na kuondoka, Hilda alimtazama Richie kwa macho ya huruma akauliza,

"Richie, kwani nini kilitokea?"

Kabla Richie hajajibu, Hilda akaongeza, "Jamal alinipigia simu amekukuta umezidiwa, nini kilikukumba, Richie? Mbona imekuwa ghafla hivyo?"

Richie akatikisa kichwa, akahisi maumivu makali, haraka akatuliza kichwa chake akisonya mithili ya mtu anayeita paka, alafu akasema,

"Nikikwambia sijui unaweza kuniamini?"

"Hujui nini?"

"Sijui kilichotokea."

"Hujui kilichotokea?"

"Sikumbuki kitu chochote kile, nastaajabu sana, naweza kukumbuka vitu vya juzi ama juma lililopita lakini sikumbuki kitu chochote kuhusu jana usiku, kitu pekee ninachokumbuka ni kukutana na Jamal."

"Serious?"

"Serious, nakwambia kweli, lakini nahisi maumivu ya kichwa kweli, kadiri niongeavyo nahisi kuyatibua."

Baada ya hapo Hilda akajiepusha kumuuliza maswali bwana huyu kwa kuhofia kumsababishia maumivu, walipofika nyumbani wakamkuta Jamal akiwa hapo anawangoja, wakasaidizana kumpeleka Richie chumbani kwake kwaajili ya mapumziko kisha wakasogea kando kwaajili ya mazungumzo mafupi.

"Anasema hakumbuki kitu?"

"Ndio, nimemuuliza anasema hamna anachokumbuka, lakini wewe ulikuwa naye hapa jana, uliona nini?"

"Alikuwa vizuri kabisa, nilifanya naye mazungumzo kabla hajaniaga kwenda kuichukua simu yake, ajabu nilipomfuata baada ya kuona anakawia ndo' nikamkuta amelala chini, hana fahamu!"

"Hakuona dalili yoyote?"

"Hapana ... lakini kuna mtu fulani nilimwona, hisia zangu zinapata kumshuku sana kuwa si mtu mwema, huenda akawa alimfanyia kitu Richie."

"Nani huyo?"

"Simjui, alivalia nguo za kujificha hata gari lake halikuwa na namba za usajili!"

"Atakuwa anataka nini kwa Richie? Kuna kipi cha kumfanya awindwe na mtu?"

"Sijajua ... lakini nilikuja hapa kumwona Richie sababu ya matatizo yangu binafsi, kwasababu yupo katika hali ya kutokumbuka si mbaya nikakushirikisha wewe, pengine unaweza kunisaidia."

"Nini hiko?"

Jamal akaleza kinachomsibu, wakati huo wakiwa hawana hili wala lile, palikuwa na mtu aliyekuwa anawatazama kwa umakini akiwa ndani ya gari, mtu huyo alikuwa ameshikilia kalamu mkono wake wa kushoto na alikuwa anaandika kila alichokitambua kwa kupitia kusoma 'lips' za wahusika. Bwana huyu alikuwapo hapa kwa muda, na hakuwa mwingine bali yuleyule aliyekuwapo hapa jana yake na kumvamia Richie.


***
 
Yani wewe nilikutafutaga Sana Kumbe umewekeza huku siku hizi eeh ,.. malkia wa gosheni bado nangoja S3 [emoji23][emoji23]
 
Back
Top Bottom