Timothy Peter Thomas, nitakujibu japo kwa ufupi kwani naamini kama umeufuatilia huu mjadala toka mwanzo wake, majibu mengi ya maswali yako yapo humu humu. Hata hivyo kwa kukusaidia;
Field Marshal John Okello ndiye aliyeyaongoza mapinduzi ule usiku wa tarehe 12 January 1963, mapinduzi yaliyomfungasha virago Sultani Sayyid Jamshid bin Abdullah Al Said, kiongozi mkuu wa serikali ya Zanzibar. Okello ndiye alikuwa mwenyekiti wa kwanza wa Baraza la Mpinduzi na hata baada ya kumtangaza Karume kama Raisi kupitia chama cha ASP, alibaki kama msemaji mkuu wa serikali. Baada ya wiki moja tu vitendo vya Okello vilianza kumfadhaisha sana Karume pamoja na viongozi wengine wa serikali lakini ikawawia vigumu kuchukua hatua kwani Okello alikuwa na wafuasi waliokuwa tayari kumlinda kwa gharama yoyote ile. Kujaribu kumweka kando akiwa bado kwenye ardhi ya Zanzibar kungeweza kusababisha machafuko makubwa ambayo pengine yangeuangusha serikali ya Karume.
Mpango ulisukwa na kuna wakati Karume alitaka hata msaada wa Jomo Kenyatta, Raisi wa Kenya, amkamate Okello alipozuru Kenya katikati ya mwezi wa pili lakini mpango huu haukufanikiwa. Baadaye Okello na Karume walisafiri pamoja kuja Dar es Salaam kwa mwaliko wa Mwalimu Julius Nyerere ambaye pia wakati huo hakuwa anafurahishwa na vitendo vya kikatili alivyoendesha Okello. Bila kujua Okello alikubali huo mwaliko lakini baada ya kufika Dar es Salaam alizuiliwa na hakuweza kurejea Zanzibar. Kilichofuata ni namna ya kuwatuliza wafuasi wake ambao walianza kuonesha wasi wasi kwa yaliyompata hivyo ilibidi mbinu isukwe jinsi ya kupooza mambo.
Kazi ya propaganda ya kufuta nyayo za Okello zilianzia hapo na kazi hiyo alikabidhiwa Abdulrahman Babu ambaye tarehe 23 Machi 1964, alianza rasmi kazi hiyo. Babu alidai redioni kuwa Field Marshal John Okello siyo tu hakuongoza mapinduzi ya Zanzibar bali alikuwa ni moja tu katika watu waliofanikisha mapinduzi. Hizi zilikuwa ni jitihada katika kupambana na umaarufu wa Okello kama kiongozi mkuu wa mapinduzi na kuwashawishi wafuasi wake kwa kuwaahidi waliokuwa wapiganaji wake ajira ndani jeshi la wananchi lililokuwa linaundwa. Walifanya jitihada sana kufanikisha hili lakini hawakuweza kufuta vielelezo vyote kama picha zake na sauti yake, hizi zipo mpaka leo.