Mohamed Said
JF-Expert Member
- Nov 2, 2008
- 21,967
- 32,074
View: https://www.youtube.com/watch?v=_PCe60hMfms
Mimi unanikumbusha redio ya cassette ya panasonic mida ya menu mchana RTD nikiwa na mama na marehemu babangu.
Kweli muda unakimbia sana.
Mshana Jr
Def ...
Huu mwimbo umepigwa na Egyptian na mwimbaji ni Nuru bint Sudi.
Nakuwekea hapo chini historia fupi ya Nuru bint Sudi kama nilivyoiandika katika kitabu cha Abdul Sykes:
Ilikuwa katika taarab iliyoandaliwa kusheherekea kufunguliwa kwa tawi la TANU Dar es Salaam ya Kaskazini katika mtaa wa Mvita, nyumba namba 10, tarehe 10 Agosti, 1957, ulimi wa Sheikh Takadir ukateleza, akamuita Nyerere ‘’Mtume.’’
Tawi la TANU Dar es Salaam ya Kaskazini lilikuja kuwa lenye nguvu sana kuliko yote na tawi likawa na mafanikio labda kupita matawi yote katika Tanganyika.
Mwenyekiti wake alikuwa Mtoro Kibwana na mweka hazina Haidar Mwinyimvua, ambae baadae aliingia Kamati Kuu ya TANU ya taifa.
Kwenye hafla ile, katika kumtambulisha Nyerere na kummiminia sifa, Sheikh Takadir bila kufikiri aliwaambia wasikilizaji wake kuwa ‘’Nyerere ni mtume wa Afrika.’’
Kama kauli ile ingetolewa siku nyingine yoyote ile, huenda tamko hilo lisingezua kishindo, na huenda lingepita bila kuwa na taathira yeyote mbaya.
Lakini ufunguzi wa tawi la TANU la Mvita katika siku hiyo tarehe 10 Agosti, 1957 ilikuwa siku maalum kwa wakazi wa Dar es Salaam.
Kwanza, Dar es Salaam ilijitokeza shuhudia kuhama kwa mwimbaji stadi, Nuru binti Sudi, kutoka Al-Watan na kujiunga na wapinzani wao Egyptian.
Hivi vilikuwa vikundi viwili vya taarab vikishindana mjini Dar es Salaam.
Siku hiyo Nuru alikuwa anaimba pamoja na kikundi chake kipya Egyptian kwa mara ya kwanza na mashabiki wake walikuwa wamekuja kumwona bingwa wao akiimba katika hafla ya TANU.
Halikadhalika mashabiki wa Egyptian walikuwa wamekuja vile vile kushagilia na kuwazomea washindani wao kwa kumchukua bingwa wao.
Kulikuwa na sababu nyingine kwa watu kushangilia.
Katika kuhama huko kutoka Al-Watan na kuingia Egyptian, Nuru alikuwa ameweka msimamo wa kisiasa.
Nuru alikuwa na damu mchanganyiko. Baba yake alikuwa Mwarabu na mama yake alikuwa Mwafrika.
Kabla ya kutoka Al-Watan na kuingia Egyptian, Nuru bint Sudi alikuwa mwanachama wa Coronation ambacho kilikuwa chama cha akina-mama wenye asili ya Kiarabu.
Kwa hiyo ilichukuliwa kwamba, maadam Egyptian ilihusiana na Waafrika, kwa kitendo kile cha kuhama Al-Watan, Nuru alikuwa ameasi na kurudi kwa ndugu zake, yaani Waafrika.
Amerudi kwenye asili yake, kwenye tumbo la mama yake aliyemzaa. Hivi ndivyo mambo yalivyokuwa siku zile, kila jambo lilipewa tafsiri ya kisiasa.
Wakati huo UTP ilikuwa tayari imeshanzishwa na Egyptian ilikuwa imetunga nyimbo maalum kwa ajili ya hafla hiyo ambayo Nuru aliimba kuidhihaki UTP.
Sehemu ya mashairi yake yalikuwa yanasema hivi: ‘’Ma-UTP wana majambo, TANU wanaichukia.’’
Pili, ili kuadhimisha kufunguliwa kwa tawi la TANU Mvita, TANU iliwaalika wajumbe wa Baraza la Kutunga Sheria, wengi wao machifu, ili kushuhudia sherehe hiyo.
Miongoni mwao walikuwa Chifu Kidaha Makwaia, Humbi Ziota, Msabila Lugusha, Mwami Theresa Ntare na wengine wengi.
Vilevile walikuwepo watu wengine mashuhuri kama Hamis Mfaranyaki ambae ndiye alikuwa kiongozi wa Wangoni mjini Dares Salaam,
Paul Bomani, Sheikh Said Chaurembo, Sheikh Abdallah Chaurembo na wengine wengi.
Pamoja na watu wote hawa mashuhuri kuhudhuria, huu ulikuwa usiku adhimu kwa TANU.
Hapakuwa na shaka yoyote kuwa chochote kitakachosemwa katika hafla kama hiyo kitakuwa na athari kwa watu.
Ilikuwa katika hafla hii ndipo siku ulimi wa Sheikh ukateleza.
Akamwita Julius Nyerere, ''Mtume wa Afrika.''
Aliyesimama ni Sheikh Suleiman Takadir na juu ya meza ni bakora yake kulia ni John Rupia na
anaefuatia ni Julius Nyerere.