Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu
WATANZANIA wametakiwa kuongeza umakina katika kujilinda na virusi vya corona (COVID-19), kwa kuwa siku chache zijazo, nchi itaingia katika hatua ya kuambukizana wenyewe kwa wenyewe.
Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam …(endelea).
Na kwamba, katika hatua hiyo, mtua anaweza kupata maambukizi na asijue amepata kutoka wapi.
“Tumetoka kwenye maambukizi yanayoletwa kutoka nje ya nchi (imported transmission), tuko kwenye local transmission (maambukizi ya ndani).
Hivi sasa, takwimu za kesi za jana na juzi, zinaonesha tumeanza kuambukizana wenyewe kwa wenyewe, hili lazima tuweke wazi. Hakuna maambukizi ya nje,” amesema Waziri Ummy na kuongeza:
“Tumeanza kwenye ‘local transmission’ na siku chache tutaingia kwenye ‘community transmission,’ maana yake tutapata mgonjwa hatutajua ameupata wapi huo ugonjwa, ndio maana tunafanya ufuatiliaji.
“Na ndani ya siku chache tutaingia katika hatua hiyo, lazima niwaambie ukweli viongozi wa dini, nisiwafiche kwamba soon tutaingia kwenye community transmission.”
Hata hivyo, Waziri Ummy amesema Tanzania imevuka kihunzi cha Shirika la Afya la Kimataifa (WHO), cha kuwa na wagonjwa 1,000 wa COVID-19 ifikapo katikati ya mwezi Aprili mwaka huu.
“Tunamshukuru Mungu, hadi sasa anatutendea maajabu, tumevuka kihunzi WHO, walisema mwezi Aprili tutapata wagonjwa 1,000 na kati kati ya mwezi Mei tutapata wagonjwa 10,000 lakini kila mtu akichukua nafasi yake, tunaweza kuvuka hicho walichotutabiria,” amesema Waziri Ummy.