Balozi wa Tanzania nchini Austria, Celestine Joseph Mushy, amefariki dunia kwa ajali ya gari eneo la Mkata, wilayani Handeni mkoani Tanga.
Ajali hiyo imetokea jana usiku wakati akiendesha gari aina ya crown lenye namba za usajili T175 DMF kuelekea Moshi, Kilimanjaro.
===
Balozi wa Tanzania nchini Austria afariki ajalini
Alhamisi, Desemba 15, 2022Balozi wa Tanzania nchini Austria, Celestine Mushy
Muktasari:
Balozi huyo amefariki juzi Jumanne alipokuwa akisafiri kwa kuendesha gari mwenyewe kutoka Dar es Salaam kuelekea mkoani Kilimanjaro.Tanga. Balozi wa Tanzania nchini Austria, Celestine Mushy amefariki dunia katika ajali iliyotokea eneo la Mkata wilayani Handeni mkoa wa hapa.
Mushy aliteuliwa na Rais Samia Suluhu kuwa Balozi wa Tanzania nchini Austria Januari mwaka huu na Mei 5, 2022 akawasilisha Hati za Utambulisho kwa Rais wa Jamhuri ya Austria, Alexander Van der Bellen.
Akizungumza na Mwananchi leo Alhamisi Desemba 15, 2022, Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Siriel Mchembe amesema kuwa balozi huyo ambaye alikuwa peke yake alikuwa akiendesha mwenyewe gari akotokea Dar es Salaam kuelekea Moshi mkoani Kilimanjaro.
Mchembe amesema kuwa ajali hiyo imetokea juzi Jumanne usiku ambapo mwili wa balozi huyo umekutwa ukiwa umeungua.
"Mwili wa balozi tuliuchukua eneo la ajali usiku na tumeuleta Hospitali yetu ya Wilaya. Ndugu zake wapo njiani wakitokea Mbezi Dar es Salaam wanakuja kuuchukua," amesema Mchembe.
Alipoulizwa kuhusu kifo cha balozi huyo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine amesema wizara yake haijapata taarifa rasmi, wakipata watathibitisha hilo.
"Hatujapata taarifa hizo, tuta-comfirm (tutathibitisha), tutakwambia," amesema Balozi Sokoine.
Chanzo: Mwananchi