kwanza niweke hapa taarifa hii rasmi ya ikulu:
taarifa kwa vyombo vya habari
leo, jumatatu, oktoba 7, 2013, zimetungwa habari, zikaingizwa kwenye mitandao ya kijamii na kusambazwa sana zikidai kuwa rais wa jamhuri ya muungano wa tanzania, mheshimiwa jakaya mrisho kikwete ametia saini muswada wa sheria ya marekebisho ya sheria ya mabadiliko ya katiba ambao ulipitishwa na bunge katika kikao chake cha mwezi uliopita.
Kurugenzi ya mawasiliano ya rais, ikulu inapenda kufafanua kama ifuatavyo:
A) kwanza, ofisi ya rais, ikulu haijapokea muswada wa sheria ya marekebisho ya sheria ya mabadiliko ya katiba. Inawezekana muswada huo umekwishakutumwa kutoka bungeni lakini haujamfikia mheshimiwa rais. Hivyo, kama haujamfikia, mhe. Rais hawezi akawa ameutia saini
b) pili, muswada huo ukimfikia mheshimiwa rais,
inatarajiwa kuwa atautia saini kwa sababu muswada huo umepitia katika mchakato sahihi na halali wa kikatiba kwa maana ya kufikishwa bungeni na serikali, kujadiliwa na hatimaye kupitishwa na bunge.
C) tatu, kama yapo marekebisho ambayo yanaonekana yanafaa kufanywa katika sheria hiyo, basi yatafanywa na bunge baada ya mhe. Rais kuwa ametimiza matakwa ya kikatiba ya kutia saini muswada ambao umepitishwa na bunge kwa kufuatia mchakato sahihi na halali wa kikatiba.
D) nne, na wala hii haitakuwa mara ya kwanza kwa sheria kupitishwa na bunge, ikatiwa saini na mhe. Rais na baadaye kufanyiwa marekebisho na bunge baada ya kuonekana umuhimu wa kufanya marekebisho hayo. Mwishoni mwa mwaka 2012, sheria ya marekebisho ya katiba ilipitia njia hiyo.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya mawasiliano ya rais.
Taarifa husika ililenga kukanusha jambo moja tu: Kwamba rais jakaya mrisho kikwete hajasaini muswada wa katiba kama ilivyoripotiwa kwenye mitandao hapa nchini leo hii. Ni taarifa nzuri ili wananchi wasipotoshwe. Kurugenzi hadi hapo ilifanya kazi yake ipasavyo.
Lakini, kurugenzi imevuka mipaka.kwa kanusho hilo tu,hakukuwa na haja ya kuwa na aya zinazoanza na 'pili', 'tatu' na 'nne'. Aya hizi zinarejesha 'chokochoko' zisizo na msingi ambazo rais analenga kuzimaliza. Kwenye aya hizi kuna ubabe usio na tija na ramli ya kuogofya.
Nani kaiambia kurugenzi kuwa rais atausaini muswada husika ukimfikia? Wanamlazimisha rais aendane na mazoea hata katika mambo ya maslahi kwa taifa? Kwanini?
Nazipinga aya hizo kwa nguvu zangu zote. Na msisitizo uliowekwa katika aya inayoanza na 'pili' ni wa kuogofya na kuupuuza. Ni msisitizo usio na tija na wenye nia ya kuvuruga mshikamano wetu juu ya katiba mpya. Kikatiba, rais halazimiki kusaini muswada wowote.
Naiomba kurugenzi ya mawasiliano ikulu iepuke 'makosa ya wazi' kama haya siku nyingine. Aya iliyoanza na 'kwanza' ilikuwa inatosha kabisa. Kurugenzi isivuke mipaka yake. Tafadhali.
mzee tupatupa wa lumumba, dar es salaam