Simulizi ya kipelelezi: Idaiwe maiti yangu

Simulizi ya kipelelezi: Idaiwe maiti yangu

STORY: IDAIWE MAITI YANGU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
SEHEMU YA SITINI NA TANO
SONGA NAYO................


Hakuna kitu ambacho kiliundwa na intaneti au mtandao kingempiga chenga, alikuwa miongoni mwa magwiji wa IT wakati anasoma. Kama ilivyokuwa kawaida kwa taifa la Tanzania, haikujalisha mtu ana uwezo gani lakini kama hakuwa na marefa wa kumbeba basi uwezo wake ungefia ndani kwake bila kuufaidisha ulimwengu wala taifa. Kijana huyo alikuwa mmoja wao, kijana mwenye uwezo mkubwa lakini hakuwa na ajira ila hakujali kwa sababu uwezo wake ulikuwa unampa nafasi ya kufanya lolote na popote bila kuacha alama mahali popote pale. Kwa Ethan kijana huyo alionekana kama dini la dhahabu ambalo lilitupwa juu ya jalala halafu kila mtu akawa analidharau.

“Ethan mshikaji wangu, nakujua sana, hunaga muda kabisa wa kuja kunisalimia au kunijulia hali rafiki yako. Mara nyingi ukija hapa unahitaji ni msaada, kwa leo nikwambie mapema kabisa kwamba siwezi kukusaidia” kijana huyo aliongea akiwa anamwangalia mwanamke mwenye maumbile makubwa ambaye alitoka dukani kwake wakati huo. Ethan aliishia kucheka, rafiki yake alikuwa kiwembe sana linapokuja suala la kupenda ngono.
“Hili tatizo ambalo ninalo mimi haliwezi kulala Ethan ndiyo maana nipo hapa”
“Oioooooh shiit Ethan!”
“Mimi ndiye ndugu yako ambaye tutazikana hivyo najua huwezi kunitupa Brian”
“Ni kuhusu kazi yako?”
“Ndiyo”
“No, kwa leo siwezi kukusaidia kwanza nipo busy sana na kazi hapa”
“Funga duka Brian, tunaondoka muda huu kwenda kwako”
“Ethan mimi na wewe tumesha malizana”
“Kuna kiongozi mkubwa ameuawa muda mfupi uliopita?”
“Are you serious?”
“Unapoteza muda mwingi kufanya ngono, unapenda mno kukata viuno kwa wanawake vinginevyo hizi taarifa mpaka muda huu ulitakiwa kuwa nazo kwa sababu zimesambaa kila sehemu”
“Sio mbaya hawa wanasiasa nao wawe wanauawa hivi ili waone maumivu ambayo raia huwa wanayapitia wanapo wapoteza wapendwa wao kwa uzembe wa hawa wanasiasa ambao wamejaa propaganda mdomoni”
“Hii kesi nataka kuifuatilia off books Brian”
“Hilo ni jambo la hatari kama ukikutwa, sikushauri”
“Hakuna kitu unaweza kuongea kikanishawishi mimi kuachana na hili”
“Una uhakika?”
“Ndiyo Brian kwa sababu hii kesi ilikuwa kwenye mkono wangu ila mamlaka za juu wameibeba hivyo nataka kuwathibitishia kwamba naweza kuitatua kesi kwa ukubwa na kwa namna bora kuliko wao huenda kuna siku watakuja kuona umuhimu wangu ndani ya hili taifa”
“Bado unahitaji kupanda madaraja kazini kwako?”
“Ndiyo ndoto yetu Brian” kijana huyo alimsikitikia mwenzake kwa sababu alikuwa anajiingiza kwenye hatari ya waziwazi ila hakuonekana kabisa kujali juu ya jambo hilo.
“Haya mambo yatakuja kuwa na mwisho mbaya sana kwa upande wako. Huenda mambo ambayo unataka kuyagusa yanaenda kuharibu maslahi ya wengi hivyo ungeshukuru watu hawa kukutoa huenda wanakuokoa na mengi” Brian aliongea akiwa anafunga sehemu ya duka lake na kuongoza kwenye gari yake ndogo. Ethan hakujibu kitu zaidi ya kutabasamu tu maana alimjua jamaa yake huyo kwa kupenda kutoa toa ushauri ambao haukuwa na umuhimu wake kwa muda huo.

Taarifa ambazo zilikuwa zinahitajika zilikuwa ni taarifa za Othman chunga lakini pia taarifa za siri za waziri wa mambo ya ndani. Kijana huyo alihakikisha amefunga kila kitu kwenye nyumba yake, alikuwa na chumba cha siri ambacho kwenye kuta zake kulikuwa kunafunikwa kompyuta kubwa zenye uwezo mkubwa sana.
“Hivi vitu vyote huwa unavitoa wapi Brian?”
“Hahahaha Ethan ili uweze kuishi kuna muda maisha yanatufundisha mambo mengi sana. Siku ikitokea umeingia kwenye hii kazi yangu utaelewa namna ambavyo vinapatikana ila kwa sasa huwezi kuelewa kwa sababu hauna kazi navyo”
“Mhhhhhh” Ethan aliishia kuguna tu kwa sababu kwa wakati huo hakuwa na jambo la kuweza kuongezea hapo.

Sura za watu hao ziliingizwa kwenye mtambo maalumu, jambo la kushangaza ni kwamba taarifa na wasifu wa waziri ulikuja kirahisi sana lakini kwa upande wa Othman ilikuwa ni tofauti kabisa, kilikuja kivuli tu hakukuwa na taarifa ya namna yoyote ile.
“He is a ghost” kijana huyo aliongea akiwa anamgeukia Ethan
“Comon Brian, wote tunajua unaweza kuzipata taarifa zake”
“Kama ikitokea nikafanya hivyo itanilazimu kuingia kwenye taarifa za siri zaidi ambazo ili kuingia huko natakiwa kulipia na ni jambo la hatari mno kwa sababu naweza kujulikana na mhusika kwamba namtafuta na sijui ni mtu wa namna gani Ethan. Unayajua kabisa maisha yangu ni ya siri hivyo naweza kuishia kuuawa kama kuna watu watajua ninacho kifanya”
“Please Brian, hii itakuwa mara yangu ya mwisho kuuhitaji msaada wako na hiyo pesa mimi nitailipia” kijana huyo alisikitika kwa sababu alikuwa anafanya jambo la hatari mno hususani kuingia kwenye mtandao ambao kisheria haukuwa unaruhusiwa, ulikuwa unatumiwa na watu zaidi wa Dark Web nao walikuwa ni wa kuhesabika na ulikuw wa gharama kuweza kupata taarifa yoyote ile. Ni mtandao ambao ulikuwa una nguvu ya kumpata yeyote na mahali popote hata kama anaishi kwa siri vipi, kikubwa kama kungekuwa na kiunganishi chake chochote kama picha au jina.

Ilimlazimu Brian kuzima mitambo yote na kuitoa laptop yake moja ambayo ilikuwa kwenye safe, alijifikiria sana kabla ya kufanya maamuzi ya kuweza kuiwasha ili afanye kazi ambayo rafiki yake alimuomba waweze kuifanya.
“Ethan hili jambo naenda kulifanya kwa sababu wewe ni rafiki yangu wa muda mrefu ila kitu unachotakiwa kukijua ni kwamba jambo kama hili mwisho wake huwa ni damu. Tunaweza kufa wote ama mmoja wetu kufa, kwamba tutaishi wote sina uhakika kabisa juu ya hili. Nimewahi kuona baadhi ya kesi za namna hii na mwisho wake haujawahi kuwa mzuri hata siku moja. Nakuuliza tena, una uhakika na hili jambo?”
“Ndiyo Brian” kijana huyo alionyesha kuwa na wasiwasi mkubwa ndani yake ila hakuwa na namna. Yalitumika masaa matano wakiwa mbele ya laptop hiyo kuweza kutafuta taarifa hata chache tu za mtu huyo aliyejulikana kwa jina la Othman chunga. Baada ya muda mrefu kuweza kupita ikiwa wanaelekea kukata tamaa ndipo lilitokea jambo ambalo hata wao hawakuweza kulitegemea kama lingeweza kuja hapo.

Ilikuja picha ambayo ilionekana kuwa na mfanano na picha hiyo, haikuwa picha ambayo kwa mfanano ni kweli ilikuwa inaendana na Othman ila kwa taarifa za huo mtandao wa siri zilikuwa na mfanano kwa maana hiyo kulikuwa na nafasi kubwa kwamba watu hao walikuwa ni ndugu, sasa kama ni ndugu ni undugu upi huo? Bila shaka ulikuwa wa baba na mtoto. Jina lililokuja hapo ilionekana picha ya mwanaume mmoja ambaye alikuwa kwenye vazi la polisi mwenye nyota mbili begani.

Dato Pazu, ndilo jina ambalo lilikuja hapo na taarifa chache, mwanaume huyo alikufa kwa kukutwa ameuawa miaka kadhaa iliyokuwa imepita baada ya kujihusisha na kesi moja ambayo alikuwa anamshitaki mwanasiasa Slyvester Mboneka wakati huo akiwa mbunge. Ni jambo ambalo liliwashangaza pakubwa, kwamba ilikuwa bahati mbaya jambo hilo kutokea? Wote walikuwa na uhakika kwamba haiwezi kuwa bahati mbaya, sasa ni nini kilikuwa kinaendelea? Ikawalazimu kusoma taarifa zaidi ndipo wakagundua kwamba bwana huyo alikuwa na mtoto mmoja wa kiume. Kanaan ndilo lilikuwa jina lake.

65 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: IDAIWE MAITI YANGU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
SEHEMU YA SITINI NA SITA
SONGA NAYO................

Taarifa za mkewe zilikuwa fupi kwamba alikufa miaka mingi akiwa anajifungua mtoto wake wa pili ambapo mama na mtoto walikufa, sasa kama mtu huyo aliuawa huyo mtoto wake Kanaan alikuwa wapi? Taarifa zilidai ni UNKNOWN.
“Hii sio bahati mbaya, Othman ndiye Kanaan”
“Kwamba ndiye mtoto wa huyo askari ambaye tumemsoma hapa”
“Kwahiyo ni yeye amemuua waziri wa mambo ya ndani kwa sababu alimuua baba yake?”
“Kuna ukweli mkubwa kwenye hilo lakini kuna kitu bado hakiji hapa” Brian aliongea akiwa anaendelea kutafuta taarifa zaidi ya hizo ambazo walikuwa nazo.
“Kipi?”
“Kama ni mtoto wa askari kivipi taarifa zake zilipotea ghafla? Lazima taarifa zake zingekuwepo”
“Huenda baba yake hakutaka kumuweka hadharani mwanae kwa sababu alikuwa anajua kazi ambayo anaifanya” Ethan aliongea akiwa anatazama taarifa hizo mara mbili mbili.
“Hapana, Ethan kuna kitu hakipo sawa kabisa”
“Kivipi?”
“Kwanza kama ni yeye amefanya haya kwa hiyo video ilivyo ni wazi kwamba amefundishwa na mtu mwenye uwezo mkubwa sana lakini pili kuishi kama mzimu kwa muda mrefu kwenye dunia hii ya teknolojia kubwa inatakiwa uwe na rasilimali fedha nyingi sana. Ukiacha hilo huyu waziri kwa taarifa za ndani ni kwamba alikuwa anajihusisha na kuwa na ukaribu na wafanya biashara kadhaa akiwemo mmoja wa huko Zanzibar ambaye mtoto wake anadaiwa amekutwa amekufa”
“Ndiyo namfahamu, anaitwa Ismail Mhammed, kafanyaje?”
“Waza vizuri, kuna muunganiko wa haya matukio, haiwezi kuwa bahati mbaya, sasa kama huyu alimuua baba yake sawa, tuseme kwamba alikuwa na kisasi binafsi na mtu huyu. Vipi na huyo tajiri wa Zanzibar?”
“Hapo sasa Ezra alishtuka na kulikumbuka jina ambalo limekutwa huko Gavin Luca” alikuwa kama amepigwa na butwaa.
“Unamfahamu vizuri huyo mtu?”
“Hakuna anaye mjua vizuri lakini jina lake lilivuma sana kipindi cha miaka ya huko nyuma kwenye kesi moja ya muuzaji wa madawa ya kulevya. Huyu alidaiwa kuwa mtoto wa huyo bwana lakini aliuawa ila baadae akaja mtu mwingine na kuanza kutumia jina lake ambaye amekuwa akiisumbua serikali kwa muda mrefu sana wakiwa hawajui mtu husika ni nani. Mara ya kwanza walihisi kwamba ni mtu ambaye anatafuta kiki za mitandao ila kwa sasa na haya mauaji anaanza kuonekana kuwa mtu tishio zaidi kwa taifa” Ezra alielezea zaidi kwa undani kumpa mchanganuo mzuri rafiki yake.
“Kwa maana hiyo hawa wapo nyuma ya mtu mmoja”
“Wapo?”
“Kama ni hivyo maana yake huenda ni kundi la watu ambao wamejikusanya kuhitaji kulipa visasi. Huenda ni mtu mmoja aliamua kuwakusanya wote ambao wazazi au ndugu zao walionewa na watu fulani hivyo kila ambaye alihusika lazima alipe kwa dhambi zake. na inaonekana kwamba kila mhusika anamuua mtuhumiwa wake kwa mkono wake mwenyewe” Brian hakuwa na hizo taarifa kiundani zaidi ila alikuwa anajaribu kuunganisha matukio kutokana na taarifa ambazo alikuwa nazo hapo.
“Ooooh shiiit, maana yake wapo wengi hivyo ni watu wengi wataendelea kufa. Hii sio bahati mbaya maana yake ni mpango wa kulipa visasi” sasa alianza kupata muunganiko sahihi wa hayo matukio.
“Natakiwa kumjua kiundani zaidi huyu askari na maisha ya huyo mwanae kabla ya kuja kuwa muuaji namna hii”
“Kwa hili vazi ambalo amelivaa unatakiwa kukutana na The Future” Brian aliongea akiwa anaandika kitu kwenye karatasi.
“Ndiye nani?”
“Huyo ni jamaa mmoja ambaye anapatikana SKY PARK, anapenda sana wanawake ila ni mtu hatari mno, huyu atakupeleka kwa mzee mmoja ambaye alikuwa ni askari wa miaka hiyo hivyo anaweza kuwa na taarifa nyingi za huyu mtu na zitakuongoza moja kwa moja kupata kitu unakihitaji” walikaa jumla kwa masaa saba mpaka kuzipata hizo taarifa. Zilikuwa ni taarifa za ndani sana ambazo nazo zilikuwa zinaungwa ungwa ila zilimpa mwanga juu ya ile kesi yake.

Mpaka wakati huo alikuwa na uhakika kwamba Othman alikuwa analipa kisasi kwa waziri, je ungekuwa mwisho wa watu kuuawa na yeye na baada ya hapo angekuwa anafanya nini? Alikosa jibu sahihi. Alitamani kuyajua maisha ya kijana huyo yalikuwaje mpaka kuja kuwa hatari namna hiyo hivyo kwa maelezo ambayo alipewa na rafiki yake aliamini kwake angefanikiwa kupajua mahali kijana huyo alikulia hivyo ingekuwa rahisi kwake kuanza kuunganisha matukio ambayo kwa mwanzo wake tu ulivyokuwa hakuona mwisho mwema wa mambo hayo.

Alimshukuru sana rafiki yake na kuondoka hilo eneo, kuanzia ule mchana mpaka anatoka ulikuwa ni usiku tayari hivyo alihitaji kuonana na mwanaume aliye ambiwa kwamba angeweza kumsaidia kumwelekeza kwa mzee ambaye alikuwa na taarifa za maaskari wa zamani hiyo kwa kuangalia mavazi ambayo walikuwa nayo kwenye miili yao. Hakutaka kulala kabisa Ezra, alikuwa na njaa kubwa mno na hiyo kesi na alitaka kuitumia kesi hiyo kuweza kupata umaarufu, aliamini kesi hiyo ingempa jina kubwa na kumfanya wakubwa wamtambue vyema kama sio kumpa cheo kikubwa.

Lakini pia kuna maneno yalikuwa yanajirudia kwenye kichwa chake kutoka kwa Brian kwamba jambo hilo lilikuwa la hatari mno na huenda lingepita na maisha yao wote wawili ama mmoja. Walikuwa wameingia eneo baya lakini hakuwa tayari kabisa kuweza kuyapotezea maamuzi yake, aliamini kabisa kwamba hatua ambayo alikuwa anaifanya ilikuwa nzuri na mwelekeo wake ulikuwa wa ushindi. Tamaa ya umaarufu ikawa inakitafuna kichwa chake kiasi kwamba akawa hawezi kusikia kuhusu jambo lolote lingine tena.


SKY PARK LOUNGE.
Ilikuwa ni Lounge maarufu ya kisasa ambayo ilikuwa ikipatikana mjini, umaarufu wake ulizingatiwa zaidi na aina ya huduma ambazo zilikuwa zinapatikana ndani ya eneo hilo ikawa sababu kubwa ya umashuhuri wake. Walikuwa wanajazana watu wengi ambao walikuwa na ukwasi wa kutosha, kwa wanyonge haikuwa sehemu sahihi kwao kwa sababu vitu vilikuwa vinapatikana kwa bei ghali mno.
Ughali wake ukafanya sehemu hiyo kupokea wageni wengi hususani wachina ambao mara nyingi huwa wanapendelea kuwepo maeneo kama hayo kwa ajili ya kufanya starehe na kupumzisha miili yao. Hilo ndilo eneo ambalo Ezra Ethana (Double E) alielekezwa kwenda kumtafuta The Future.
Alifika ndani ya hilo eneo muda ukiwa umeenda kidogo lakini kwa sehemu kama hiyo ndiyo kwanza kulikuwa kunakucha, watu walikuwa wakimwaga radhi, pesa ilikuwa inaongea. Walijaa wanawake warembo wa kila aina, kila taifa ambalo ungelihitaji basi ni wewe tu na ukubwa wa mfuko wako ndiyo ilikuwa tiba ya kwenda kukonga mioyo na wanawake waliokuwa wanavutia kama yale maua ya uwaridi mbele ya macho ya mtu aliyezama hubani.

Ezra hakutaka kabisa kuipoteza nafasi yake ya dhahabu hiyo eneo hilo, alifika kwenye kiti kimoja safi akaketi na kuagiza champagne. Mdada ambaye alimletea alianza kumzoea zoea sana mwanaume akakubali kuwa naye kwa wakati huo, mwanamke huyo hakuwa tu anashoboka bali alikuwa anajieleza, alikuwa moja ya wanawake maridhawa ambao Ezra aliwahi kuwaona kwenye maisha yake.
“Unaitwa nani?”
“Rola”
“Nina bahati ya kuweza kuliona tunda bora kama wewe mbele yangu”
“Bila shaka usiku wa leo utakuwa mwanaume mwenye bahati kuweza kupanda juu ya kiuno changu”
66 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: IDAIWE MAITI YANGU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
SEHEMU YA SITINI NA SABA
SONGA NAYO................

“Natamani iwe hivyo, lakini nahitaji baadhi ya taarifa ambazo naweza kuzinunua kwako bei sawa na ambayo ningekuvua nguo”
“Huwa sifanyii mazungumzo eneo kama hili” Ezra alielewa kwamba mwanamke huyo kugoma kufanyia mazungumzo eneo hilo alikuwa anahitaji ni eneo ambalo limetulia ili waweze kufanya biashara, kama wangeondoka hapo maana yake pesa yake ingekuwa kubwa. Alilielewa hilo hivyo hakuhangaika naye kabisa, akakubali.

Bidada alimshika mkono na chupa yao akawa anamvutia bwana huyo kwenye chumba cha pembeni ambacho kilikuwa kimejitenga mbali na vyumba vingine. Ile kugusana gusana kulizalisha hali ya tofauti kwa Ezra, mwanamke yule alikuwa na joto kali mno kwenye mwili wake kiasi kwamba mnara wake ukaanza kusoma kwa kasi kubwa mpaka akashindwa kujizuia.
Alishtuka baada ya kufika juu ya kilele cha mlima ndipo akakurupuka baada ya kugundua kwamba sicho ambacho kilimpeleka ndani ya eneo hilo.
“Ni shilingi ngapi mrembo?”
“Nahitaji laki mbili”
“Mhhhhh kwa dakika tano tu hizi? Nakupatia laki moja na nusu ila naweza kukupatia laki tano kama utaniuzia taarifa”
“Zipi?”
“Namhitaji The Future”
“Ni hilo tu?”
“Ndiyo”
“Nipe pesa nikupeleke alipo” ilikuwa biashara ya muda mfupi, Ezra alifurahia baada ya kuona mambo yake yanamuendea kama anavyo hitaji yeye.

Baada ya dakika kumi alikuwa amekaa kwenye kiti kimoja sehemu ambayo mwanga ulikuwa hafifu akimwangalia mwanaume mmoja ambaye alikuwa amejisahau kwa kujirusha na mtoto wa kike kwenye kochi. Bwana huyo baada ya kama dakika thelathini alinyanyuka akaacha pesa na kuanza kutoka hilo eneo, Ezra alihisi huenda mtu huyo alikuwa anaondoka hivyo akawa naye sambamba akimfuata nyuma kujua hatima yake ilikuwa ni ipi.

Mwanaume huyo alitoka kabisa mpaka nje sehemu ambayo ilikuwa inatumika kama parking, eneo hilo lilikuwa limetulia, hapakuwa na mtu yeyote kama ilivyokuwa ndani. Aliona lilikuwa eneo zuri la kuweza kukutana naye, alimkimbilia mwanaume huyo ambaye alikuwa amepanda kwenye pikipiki lake kubwa, aliona mtu anakuja upande wake akashuka kwa sababu ilikuwa ni ghafla. Hakuuliza maswali kwa namna mtu huyo alivyo mjia, Ethan alipishana na kisu ambacho kilikita kwenye nguzo iliyokuwa pembeni kidogo na sehemu ambayo alikuwa amefika.

Alitamani kujitambulisha ila muda haukuwa unatosha kwa sababu mtu wake alikuwa amefika tayari, aliikwepa ngumi iliyokuwa inakuja usoni. Aliinama, alitaka kuuinua uso wake aligundua kwamba nyakati hazikuwa rafiki kwake, akiwa anaendelea kujitafakari zaidi ndipo alikutanishwa na ngumi ya uso ilikuwa kama imemzindua kutoka usingizini. Ezra hakuwa mgeni wa hiyo michezo na alitarajia kabisa kwamba jambo kama hilo lingeweza kumtokea hivyo haikumpa presha kubwa, alisogea kwa mahesabu makali mpaka alipokuwepo The Future akiwa anamhesabia.

Alitishia na mguu wake mwanaume yule akayumba kidogo, ilimpa nafasi kupitisha mguu wake ambao ulizama kwenye mbavu za yule bwana, akarudi nyuma kidogo. Ezra hakumpa nafasi ya kutulia, alimkimbilia na kujigeuza kwa miguu yake yote miwili ambayo iliishia kwenye mikono, aliuzamisha mmoja mpaka kifuani kabisa kwa mwanaume yule, naye hakuwa kinyonge, aliunyoosha mkono wake ambao ulitua kwenye mwili wa Ezra akayumba mpaka nyuma.
The Future alichomoa kisu kingine na kuhitaji kumrushia mwanaume huyo kwa mara nyingine tena lakini wakati huo Ezra alikuwa ameitoa bastola yake na kumnyooshea huyo bwana hivyo kisu hakikufua dafu kabisa mbele yake.
“Wewe ni nani?”
“Ni ofisa wa polisi”
“Mbona unanivamia kama jambazi ambaye ninatafutwa kwa kesi ya mauaji! Kuna nini ofisa?”
“Niligundua kwamba huwezi kunisikiliza ndiyo maana nikatumia hii njia” aliongea akiwa anaonyesha kitambulisho chake, jambo hilo lilimpa amani kidogo bwana huyo akashusha kisu chake.
“Kipi unakihitaji kwa mtu kama mimi?”
“Nimeagizwa kwako na Brian”
“Ndo wewe unaitwa Double E?”
“Bila shaka”
“Amenitumia taarifa zako na aina ya msaada wa kukupa ila naweza kukushauri kwanza?”
“Milango iko wazi”
“Kwenye hili jambo ambalo unataka kulifuatilia, ni kitu gani haswa ambacho unafaidika nacho kikubwa?”
“Haki”
“Ni haki tu basi ndiyo inakuingiza huku? Nakuona wewe bado ni kijana ambaye una nafasi ya maisha mengine zaidi ya haya”
“Unamaanisha kwamba haki kwako sio kitu cha msingi?”
“Usikimbilie kutonielewa, taarifa ambazo unaonekana unazitafuta ni hatari sana kwa upande wako kwa sababu zinaweza kwenda na maisha yako”
“Umejuaje kama ni hatari na hujui ni kitu kipi naenda kukifanya?”
“Nina uzoefu mkubwa kwenye hii dunia bwana mkubwa, zoezi lolote ambalo huwa linawahusisha wanasiasa basi damu huwa haikwepeki. Haitakuwa mara ya kwanza kwako wala haitakuwa mara ya mwisho kukutwa na matatizo pale ambapo unajivika ugwiji wa kuingilia habari za hawa wapuuzi. Naichukia sana siasa”
“Nashukuru kwa kujali kwako ila niamini mimi najua ninacho kifanya hivyo nitashukuru kama utanipa taarifa”
“Anitwa mzee Miraji, mara nyingi huwa anakuwepo kwenye jumba la sinema majira ya usiku. Anapenda kukaa pale mwenyewe baada ya kumpoteza mtoto wake wa pekee, alikuwa akipenda kwenda naye kwenye jumba hilo la sinema hivyo huwa anaenda pale ili kuweza kulinda kumbukumbu zake na mwanae”
“Natakiwa kwenda saivi?”
“Hapana, muda umekwenda sana, jitahidi uende kesho usiku”
“Asante kwa taarifa, nitaukumbuka msaada wako”
“Kama hautaingia kwenye mchanga litakuwa jambo bora zaidi kwako” mwanaume huyo aliongea akiwa anakifuata kisu kingine kisha akapanda kwenye pikipiki yake ili aweze kuondoka.
“Nina imani tutaonana kwa wakati mwingine”
“Jitahidi usimuingize Brian kwenye haya matatizo kwa sababu mpaka sasa umenunua nusu kesi na yeye yupo kwenye hii kesi”
“Usijali hakuna kitu kitamkuta Brina, nitamlinda kama italazimu kufanya hivyo”
“Wewe mwenyewe huna huo uwezo wa kujilinda halafu unaweka ahadi ya kuwalinda watu wengine? Nikutakie kazi njema” alimaliza na kuondoka The Future, jukumu lake lilikuwa dogo tu eneo hilo kumwelekeza kwa mzee ambaye alidaiwa kuwepo ndani ya jeshi la polisi miaka hiyo, mzee huyo alifanya kazi kwenye maeneo mengi hivyo alikuwa akiwajua watu wengi na mambo mengi, huyo huenda angempa muunganiko mzuri a kesi ya Othman na baba yake dhidi ya mauaji ya waziri wa mambo ya ndani na mambo ambayo yalitokea nyuma hususani ile kesi ambayo iliishia kwa waziri wa mambo ya ndani kudaiwa kumuua baba yake.

67 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: IDAIWE MAITI YANGU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
SEHEMU YA SITINI NA NANE
SONGA NAYO................


Masaa hayasimami, muda unazidi kujongea, kesho yake ilifika Ezra hakuwa na utani kabisa juu ya hiyo ari yake mpya ya kuhitaji kufanikisha alichokuwa anakihitaji. Aliwahi mapema kwenye jumba la sinema ambalo alikuwa ameelekezwa, lengo lake alihitaji kuonana na mzee huyo ambaye alikuwa anaitwa Miraji. Watu walikuwa ni wengi ndani ya eneo hilo lakini haikumpa shida kumtambua mtu wake kwa sababu alitakiwa kusubiri mpaka watu wote waishe ndipo angeweza kuonana naye moja kwa moja.
Muda ulivyozidi kwenda ndivyo watu walianza kupungua hususani baada ya ile tamthiliya ambayo iliwapeleka pale kuisha. Baada ya watu kutawanyika alibakia mzee mmoja ambaye alikaa katikati kabisa ya ukumbi. Taa zote zilizimwa ikabaki moja tu ambayo ilikuwa imefifia lakini kutokana na kiza kikali ambacho kilikuwepo, taa hiyo ilisaidia kuweza kuangaza na kufanya amuone alipokuwa. Ethan alijua kabisa yule ndiye alikuwa mtu wake haswa ambaye alikuwa akimhitaji, alitembea taratibu mpaka mstari wa nyuma kutoka pale alipokuwepo mzee yule.

“Bila shaka unapata kumbukumbu bora ambazo mwisho wake haukuwahi kuwa mwema mzee wangu” ilisikika sauti nyuma yake ambayo ilimfanya mzee huyo kugeuza shingo yake kutazama nyuma kumwangalia mtu ambaye alikuwa anamwongelesha kwa sababu hakumsikia wakati anafika eneo hilo.
“Ni muda gani tangu umekaa hapo nyuma yangu?”
“Nina sekunde kadhaa tu”
“Bila shaka umekuja kwa ajili yangu hapa?”
“Ndiyo mzee”
“Tunafahamiana kabla?”
“Hapana”
“Sasa nakusaidiaje kijana?”
“Kwanza pole kwa kukukatisha kwenye kumbukumbu za kumkumbuka kijana wako ila nimefanya jitihada kubwa mno mpaka kufanikiwa kufika hapa ili kuweza kuonana na wewe, nina imani utanisikiliza kwa hili”
“Bado haujaongea shida yako”
“Ninahitaji taarifa za bwana mmoja ambaye alipata kuitwa Dato Pazu” jina halikuwa geni kwa mzee huyo ila mtu ambaye alilitamka ndiye alikuwa mgeni, alilazimika kusimama na kugeuka ili amwangalie kijana huyo vizuri usoni, alimwangalia kwa dakika nzima akiwa anausoma uso wake kisha akarudi tena kuketi chini.
“Wewe ni nani?”
“Ukweli ni kwamba mimi ni ofisa wa polisi ambaye napeleleza kesi ya kifo cha waziri wa mambo ya ndani kwa siri kwa sababu hakuna anayejali kuhusu kazi yangu”
“Kwahiyo unataka kuwadhihirishia kwamba una uwezo?”
“Hapana nafanya kwa sababu nahisi kabisa ni jukumu langu kufanya hii kazi”
“Simjui huyo mtu kijana hivyo hakuna msaada ambao naweza kukupatia” mzee huyo hakuonekana kuvutiwa na hiyo maada, aliongea huku akinyanyuka na kuanza kuondoka hilo eneo.
“Fikiria kama angekuwa mwanao, bado ungemjibu hivyo? Najua umempoteza mwanao wa pekee na eneo hili huwa unalitumia kwa ajili ya kumbukumbu bora ambazo alikuachia akiwa hai, msaidie kijana mwenzie basi kukamilisha kumbukumbu yake, nina imani hata huko aliko atajivunia wewe kuwa baba yake” alipewa maneno ya familia ambayo yalimgusa kwa ukubwa, maneno ambayo yalimuingia vilivyo alirudi kukaa tena kwenye kiti.
“Unataka kujua kuhusu nini kwenye hilo jambo?”
“Nataka kuyajua maisha ya Othman chunga, nina uhakika uliiona video ya mauaji ya waziri hivyo lazima unamjua mhusika ambaye namuulizia hapa”
“Una miaka mingapi kijana?”
“Thelathini”
“Wewe bado ni kijana mdogo ambaye bila shaka una ndoto nyingi za kuweza kuzitimiza. Una uhakika unataka kuivaa hii kesi ambayo unaiulizia muda huu?”
“Mpaka nafika kwako basi ujue kabisa kwamba nimefanya maamuzi mzee wangu, natamani hata siku nikifa angalau niwe nimefanya jambo lolote la mhimu kwenye taifa langu”
“Huyo mtoto jina lake anaitwa Kanaan Dato Pazu ila hilo jina ambalo analitumia sasa nadhani alipewa ama ni yeye amejipatia. Baba yake mimi namfahamu sana kwa sababu nimefanya naye kazi kwa muda mrefu kabla ya kustaafu na amewahi kuwa bosi wangu pia hivyo namjua vyema hata huyo mtoto wake japo kuna wakati alikuja kutoweka
Baba yake udadisi ndio ambao ulimponza, udadisi wa kutaka kujua mambo ya wanasiasa. Slyvester Mboneka alikuwa ni miongoni mwa wanasiasa washenzi ambao walikuwepo kwenye taifa hili, bwana huyo alikuwa akijihusisha na biashara haramu. Kuna kipindi kesi yake ilifika kwenye mikono ya Dato ambaye hakuichekea, licha ya kila mtu kumkanya na kuikataa hiyo kesi yeye alidai kwamba alitaka kuitumia kama mfano ili wanasiasa waweze kupata somo kuhusu kuheshimu sheria za nchi hivyo akaipandisha mahakamani akiwa na ushahidi wa kutosha.
Kesi ile haikuwa na mwisho mwema kwake kwa sababu iliyabeba maisha yake muda mfupi tu baadae na kesi yenyewe ikaishia hewani tu kwahiyo haikuwahi kuendelea tena. Lakini enzi za uhai wake alikuwa na mtoto huyo wa kiume ambaye hakuwa akimuweka hadharani ila ni watu kadhaa ambao tulikuwa tunamjua, hii ni kwa sababu aliamini kwamba kupenda kwake haki kungemfanya kuwa na maadui wengi hivyo angekuja kumletea matatizo mtoto wake ndiyo sababu ya msingi ikamfanya amuondoe kwenye mfumo wa utambulisho wake kabisa. Kijana huyo tangu baba yake afe hakuwahi kabisa kuonekana tena, alipotea jumla mpaka baada ya miaka kadhaa ndipo alikuja kuonekana nyumbani kwangu, alikuwa kabadilika mno na wakati amekuja kwa sababu alijua mimi nilikuwa miongoni mwa watu wa karibu zaidi na baba yake alinipa machache kuhusu maisha yake.
Walikuwa wapo chini ya mtu mmoja ambaye anaitwa Gavin Luca, bwana huyo inadaiwa kwamba aliwakusanya wote ambao waliwahi kuonewa na hao wanasiasa wakubwa kisha akawataka vijana hao walipe hayo madeni yao kama wangetaka yeye angewasaidia, uliwahi kusikia mtu amjue mdeni wake, akapewa nafasi ya kumfanya amlipe halafu akamuacha? Hawezi kufanya hivyo kwahiyo vijana hao walikubali kulifanya jambo hilo lakini huyo mtu ambaye alidaiwa kwamba ndiye aliwakusanya na kuwapa tumaini jipya la maisha ukizingatia karibia wote walikuwa na maisha magumu, anadaiwa kuwa mtu hatari sana na mimi nimekuja kumfahamu vizuri siku kadhaa hizi ambazo zilipita ndipo nikaikumbuka ile simulizi ya yule muuza madawa maarufu hapa Tanzania kwamba huyo bwana aliye wakusanya ndiye bosi wake.
Kwahiyo huyo ndiye ambaye aliwapa mafunzo mwenyewe, ndiye kawatengeneza hawa vijana kwa mkono wake na ndio hawa ambao wanayafanya haya mambo ambayo yamekuleta wewe hapa.
“Amewapa? Kwamba ni wengi?”
“Inaonekana sio mmoja kwa sababu hata yeye wakati ananiambia habari hizi alikuwa anatumia wingi”
“Naweza kumpatia wapi Kanaan mzee wangu”
“Kijana unatarajia kabisa kwamba nimuuze mtoto wa rafiki yangu kirahisi namna hii?”
“Hilo nalitambua lakini mimi nataka nikutane naye nimhoji, wala hili jambo halitafika popote kwa sababu hata mabosi zangu hawajui kama nafanya haya, hii kesi nimepokonywa”
“Nihakikishie kwamba hakuna kibaya kitamkuta Kanaan”
“Siwezi kufanya kibaya kwake mzee, kama kutakuwa na ulazima basi naweza kuwa msaada mkubwa kwake” mzee huyo alimwangalia sana kijana huyo, alimtaka ampe kalamu ya wino na karatasi, aliandika mahali ambapo angeweza kumpata kijana huyo.
“Baada ya hapa sitegemei kutafutana tena, najua kama nisingekupa taarifa hizi ungenitisha kwamba unenda kuniripoti kwa sababu nilishuhudia baadhi ya matukio ya huko nyuma ila baada ya hapa ni matumaini yangu kwamba mimi na wewe hakutakuwa na ulazima wa kuweza kuonana kwa mara nyingine”
“Roger that, sir!” Ezra moyo wake ulikuwa unafurahi, alikuwa anapiga hatua kubwa ya mwendo wake ambao alikuwa ameuanza, hakukuwa na kitu cha kuweza kumzuia kufanya alichokuwa amekusudia wakati huo, kila kitu kilikuwa upande wake, alianza kuuona mwanga taratibu wa kesi yake.

68 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: IDAIWE MAITI YANGU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
SEHEMU YA SITINI NA TISA
SONGA NAYO................


Kesho yake mchana Ezra alikuwa ndani ya gari, wenye vyao hawaiti gari wanaita usafiri kwa sababu ni kama kulidhalilisha neno gari. Alikuwa kwenye daladala za kutokea Gongo la Mboto kwenda Mbezi Mwisho ambazo huwa zinapita Tabata Segerea, aliamua kubeba usafiri huo ili hata likitokea tatizo huko iwe ni rahisi kupotea. Kwenda na usafiri wake ingekuwa tatizo kwa namna fulani na hakutaka kushtukiwa na mtu hata mmoja.
Eneo ambalo alielekezwa ilikuwa ni nyumbani kwa akina Kanaan, mahali ambako hata baba yake alizikwa, kijana huyo alidaiwa kwamba mara kadhaa alikuwa akitembelea ndani ya eneo hilo kwa siri kubwa kwenda kulitazama na kulienzi kaburi la baba yake. Angeenda huko angeweza kumpata, lile tukio ambalo alilifanya Kariakoo mchana halikuwa la bahati mbaya, ilikuwa ni kawaida yake ratiba yake kwenda mchana kwa sababu baba yake alizikwa mchana baada ya kuuawa. Matukio yake mengi alikuwa anayafanya mchana ili kumuenzi baba yake.

Hiyo ndiyo ilikuwa sababu kubwa nyuma ya Othman kuyafanya matukio yake wakati wa mchana wa jua kali. Ezra alikuwa kwenye usafiri wa umma akiwa pembezoni mwa siti ya dirishani kabisa, akili yake ilikuwa ikiwaza mambo mengi isivyokuwa kawaida. Hakujua hatima ya mambo hayo huko mbele yangekuwaje ukizingatia aliirukia kesi bila ruhusa kutoka kwa wakubwa wake. Ulikuwa muda mrefu umepita bila yeye kuwa kwenye usafiri wa namna hiyo hivyo alibaki ameduwaa tu na namna watu walivyokuwa wamejaa kwenye huo usafiri wa umma.

Kwenye mdomo wake alikuwa akitafuna banzoka mawazo yakiwa mbali, mwili ulikuwa hapo ila yeye alikuwa anawaza mbali sana kiasi kwamba hakuwa akielewa kilichokuwa kikiendelea kwenye gari. Alimaliza kuitafuna banzoka yake mpaka alipohisi kwamba ladha imetoka, aliitoa mdomoni na kuitupa dirishani lakini jambo hilo lilikuwa kosa mchana wa siku hiyo kwa sababu ilienda kutua kwa mtu.

Banzoka ilimkuta mwanaume mmoja ambaye alikuwa anatembea pembezoni mwa barabara hiyo ya lami, hakuwa amemzingatia wala hakumuona kusema kwamba alifanya makusudi hivyo alimtaka dereva aendelee na safari yake kwani alijua jambo hilo lingeleta mushkeli hususani kama mhusika angeamua kulichukulia jambo hilo kwa usiriasi mkubwa. Lakini mambo yalienda tofauti na vile alivyokuwa anahitaji yeye kwa sababu dereva wa gari hiyo hakuwa anahitaji kutengenezewa kesi kama ingetokea gari yake ikaweza kuripotiwa.

Hali hiyo ilifanya gari kusimamishwa bwana huyo ambaye hawakujua kama ni afisa wa polisi akasukumiwa nje ili aweze kumalizana na mtu wake, baada ya yeye kutua chini gari hiyo ilitoweka hapo kwa spidi kubwa kiasi kwamba ungehisi dereva yule alikuwa amemgonga mtu nyuma na watu wakawa wanamfukuza. Ezra hakuwa na namna zaidi ya kumsogelea mtu wake ili waweze kuongea kiume kwani hakuwa na namna nyingine angeweza kufanya ili kuweza kulimaliza jambo hilo zaidi ya kwenda kuomba msamaha.

Lakini jambo la kushangaza ni kwamba mtu wake hakuwa na muda naye kabisa, mtu huyo aliendelea na safari yake na hakufanikiwa kumuona kwa sababu hakumpa umakini mara ya kwanza. Alitaka kuachana naye lakini aligundua kwamba ndiye alikuwa sababu kubwa ya yeye kushushwa kwenye gari hivyo asingeweza kumuacha akaenda zake bila kuongea naye hivyo alianza kukimbia kuelekea alikokuwa huyo bwana.

Alimuita kwa sauti ya mamlaka bwana huyo akageuka, mwilini mwake alivaa jeans ambayo ilikuwa na oili, chini yake alikuwa amevaa buti la tanesco, kwenye kifua alivaa tshrit kubwa ambayo ilikuwa na picha ya msanii wa marekani Tupac. Kichwani alijifunga kitambaa ambacho kilizingira kwenye rasta zake ambazo zilikuwa zinaonekana kwa mbali huenda ni kwa sababu ya kubanwa. Usoni alikuwa na mabaka mabaka ambayo yalisababishwa na oili iliyokuwa usoni kwake huku kwenye mkono wake akiwa ameishika spana moja.

Kwa kumtazama tu bwana huyo hakuhitaji maelezo mengi kujua kwamba alikuwa ametoka gereji kwa ajili ya kurekebisha kati ya gari ama pikipiki lakini upekenyufu wa ofisa huyo wa polisi ndio ambao ulimfanye aendelee kuwa mdadisi kwenye mwili wa mwanaume huyo ambaye mkono wake ulikomaa sana, hakuonekana kuwa fundi gereji tu, mkono wake ulikuwa umejigawa kwa mishipa mingi ilikuwa imepasuka mno, mtu wa gereji angekuwa na ukomavu ndiyo lakini usingekuwa kama huo.

Hapo ndipo alishtuka baada ya moyo wake kupige kite!
“Othman” alijikuta anatamka kwa sauti ya chini ila yenye mshtuko mkubwa, bado hakuwa anayaamini macho yake kwamba anamuona mwanaume ambaye ndiye alikuwa na hamu kubwa mno ya kuweza kuonana naye na hata wakati huo alikuwa anaenda kubahatisha eneo ambalo alielekezwa na mzee Miraj kuona kama anaweza kumpata huko. Moyo wake ulishtuka na kugubikwa na furaha kwa wakati mmoja, Ezra aliona ndoto yake inaenda kutimia kwa wakati mmoja huo huo alijiona kuwa anaenda kuwa shujaa mkubwa kwa kumkamata mtu ambaye hata mamlaka zilishindwa kumpata kirahisi.

Nani hapendi kupata maujiko? Alisahau kama alimpa ahadi mzee Miraji kwamba asingemkamatisha kijana huyo bali angetumika kama msaada kwake hususani baada ya kujua alikuwa analipa ni kisasi baada ya baba yake kuuliwa na waziri yule wa mambo ya ndani lakini kwenye jambo hilo alijua kabisa kwamba waziri hakuwa mwenyewe bali lilikuwa ni kundi la watu ambao walishiriki kwenye kutekeleza jambo hilo.
“Ezra unaonekana kabisa umeshangazwa na uwepo wangu eneo hili, kwanini unanitafuta namna hiyo? Unataka kunikamata au unataka kupata umaarufu kupitia mimi?” mwanaume huyo aliuliza swali ambalo hata Ezra mwenyewe lilimshangaza, kwanza alistaajabu baada ya kugundua kwamba bwana huyo alikuwa akimjua mpaka jina lake.
“Kwa kumbukumbu zangu mimi na wewe hatujawahi kuonana hapo kabla Kanaan, umefanikiwa vipi kunifahamu?”
“Mhhhhh hilo swali la msingi sana kwa sababu ninaweza kupata taarifa za kila kona za hili taifa kwa muda fupi tu. Najua umekutana na mzee Miraji ila sijajua hamu ya wewe kutaka kuonana na mimi ilikuwa ni ipi?”
“Kwahiyo yule mzee alikupa taarifa kwamba nakuhitaji?”
“Sina huo muda wa kumuuliza yeye hizo habari, nilitaka kujua nani amekutuma wewe uwe na hamu kubwa ya kuonana na mimi?”
“Bila shaka hili sio bahati mbaya bali ulijua kabisa kwamba nitakuwepo hapa muda huu hivyo umepita makusudi si ndiyo?”
“Nani amekutuma uje kunitafuta Ezra? Hii ni nafasi ambayo inatokea mara moja tu kwenye haya maisha na nina uhakika hauji kuipata tena lakini jambo lingine nahitaji kujua kwamba unataka nini mpaka unaamua kuyatoa maisha yako sadaka namna hii?” Ezra hata hakuwa anayasikiliza maswali hayo, alikuwa anawaza namna nzuri ya kuweza kumpata bwana huyo asiweze kuondoka siku hiyo kwenye mikono yake na alijua kabisa njia ya amani isingefaa hivyo yalitakiwa kutumika mabavu. Ndiyo, alielewa ndiyo ilikuwa njia pekee ya wao kuweza kuelewana vizuri hapo.
“Upo chini ya ulinzi na hauwezi kuondoka Othman, mimi nahitaji kumpata Gavin Luca” hiyo ndiyo sehemu ambayo alifanya kosa kubwa, kulitaja hilo jina alikuwa anakitafuta kifo mchana kweupe.

69 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
Back
Top Bottom