Mama Samia ana dhambi kubwa mbele za Mungu kwa kuutweza utu wake.
Binadamu wote tumeumbwa kwa mfano na sura ya Mungu. Anayemtweza binadamu mwenzake, anajitweza mwenyewe, na anamtweza Mungu Muumba wetu aliyetufanya tuwe tofauti na chochote, na akatushirikisha katika ukuu wake.
Ameutweza utu wa baadhi ya watu, kwa kuruhusu watu wabambikiwe kesi za uwongo. Aliishia tu kuwalaumu polisi bila ya kuchukua hatua. Ameutweza utu wa watu wengi, vijana kwa wazee, watu wa kawaida mpaka maaskofu na mashekhe, akaruhusu wawekwe mahabusu kwa sababu tu walikuwa wamejiandaa kuhudhuria kongamano la katiba. Watu hao hawakuwa na hatia yoyote.
Ukipewa mamlaka yanayokupa haki ya kuzuia watu kuonewa, lakini ukakaa kimya kwa kusingizio kuwa siyo wewe, ilihali umepewa wajibu, ni sawa na kuyabariki na kuyakubali matendo yale maovu.
Ukiwa kiongozi una wajibu ulio mkubwa kuliko watu wengine. Na wajibu huo usipoutimiza kikamilifu, huwi tofauti na mhalifu.
Kama unataka utu wako uheshimiwe, anza na kuheshimu utu wa watu wengine, hata kama dhamira yako haifurahiwi na yale wasemayo au watendayo, alimradi hawavunji sheria.
Viongozi wote watambue kuwa wana wajibu kwa wanaowaongoza. Na wajibu huo, maadamu umeyakubali mamlaka ya kuwa kiongozi, hauwi tena ni takwa la hiari, bali ni wajibu wa lazima.
Lazima Rais Samia atambue ana wajibu:
1) kuhakikisha watanzania wote wanatendewa haki. Polisi hawawabambikii watu kesi. Wateule wake hawawapori watu mali zao wala kuwatendea watu isivyostahili. Hao wote, iwe polisi, TIS, magereza, maDC, maRC, mawaziri, wakitenda maovu, ni sawa ametenda yeye. Au la awachukulie hatua madhubuti hasa ambazo zinapeleka ujumbe kwa watu kuwa hawa wayatendayo, siyo niliyowaagiza. Polisi wakiwabambikia watu kesi, Rais akawa kimya, maana yake watu hao wamebambikiziwa kesi na Rais. Watu hawakuwachagua Polisi, walimchagua Rais. Yeye ndiye aliyewaajiri Polisi.
2) kuhakikisha Watanzania wanapata huduma zao muhimu, pamoja na matibabu, umeme, maji, n.k. Kutokuhakikisha hayo, na kuridhika, ni kutotimiza wajibu.
3) kuhakikisha wananchi wanatengenezewa mazingira ya haki ya kuongoza nchi na jamii zao kwa haki, uhuru na usawa. Asipohakikisha hayo, kwa nafasi yake, anakuwa ametenda uovu.
4) kuhakikisha haki na uhuru wa watu unalindwa, alimradi uhuru huo haukiuki sheria. Asipofanya hivyo hastahili kuwa kiongozi. Na watu wakinyimwa haki na uhuru wao na chombo chochote, yeye ndiye anakuwa mwovu mkuu maana hao wote ni wateule wake. Anaposhindwa kuchukua hatua dhidi yao maana yake ameridhia na kubariki uovu ule.
Wananchi, wakati wote tusipotendewa haki, mtu wa kumbana ni Rais. Huyo ndiye zao la matakwa ya wananchi, hata kama tunafahamu uchaguzi wa 2020 ulivurugwa. Sisi hatukumchagua waziri, IGP, Mkuu wa Magereza wala majaji. Wakivurunda majaji, polisi, mawaziri, maRC, maDC, wakurugenzi, aliye halali yetu, kwa lawama zetu zote na hatua nyingine zozote, ni Rais.
Hao wengine atajuana nao yeye. Uovu wa polisi, ni uovu wa Rais. Uovu wa majaji ni uovu wa Rais, uovu wa mawaziri, ni uovu wa Rais, uovu wa maDC na maRC, ni uovu wa Rais. Tuliye na haki naye kumwajibisha ni yule tuliyempa mamlaka, na siyo mtu mwingine. Polisi wakiwabambikizia kesi Raia na majaji wakala njama za kutengeneza mashahidi bandia, lawama zetu ni kwa Rais maana ndiye anayeteua makamanda na majaji wote.
Mkitaka kupambana na anayewaonea, msitawanye mishale.